‘Haya, sasa jiandae uje kuna maongezi, nataka uje uelezee
kila kitu, ukinificha, basi shauri lako, ..yatakayokutokea usije
kunilaumu..mimi nawafahamu sana hawa wanaume, ..unanisikia, mimi nataka
nikusaidie wewe haya yasije kutokea tena…unanielewa…, kwahiyo sema kila kitu
kinachotokea humu ndani, na kama uliwahi kufanyiwa jambo lolote na mume wangu, uliongee,
huu ndio wakati wako…’
Hiyo ilikuwa kauli ya mama mwenye nyumba
.Unasikia,….uwe makini na kauli zako, mama ni
mjanja sana, anatafuta njia ya kumuona baba ana makosa, nina uhakika kuwa baba
hana makosa mimi namfahamu sana baba yangu, na ikithibiti kuwa kuna kitu
kinahusiana na baba, na mama akasikia kutoka kwako,…utavuruga ndoa yao,…na hapo
hutapata mtetezi tena, baba ndiye mtetezi wako, na alipanga mambo mengi ya
kukusaidia....'alinionya huyo kijana
Niliwazia hayo...na kunifanya niwe njia panda...
Tuendelee na kisa chetu...
****************
Nilifika kwenye hicho
kikao nilichoitiwa, nilijua labda ni hao wanandoa wawili na mimi mwenyewe,
lakini humo nikawakuta wazee wawili,….niliambiwa mmoja ni mzazi wa baba na
mwingine ni baba mkubwa wa mama, wenye nyumba.
Baadae yule kijana
alikuja…kama nilivyosema huyu alikuwa na umri karibu sawa na mimi,kama kanizidi
mimi ni kidogo tu…huyo kijana alipoingia, kwanza aliwatupia macho hao wazee,
halafu akanigeukia mimi na kuniangalia kwa mashaka, kama ananionya kuhusu jambo
fulani, mimi sikumjali, dhamira yangu ilikuwa kusema ukweli tu, sikutaka
kudanganya tena, ila kwa mbali akilini nikawa nakumbuka onyo la huyu kijana..
‘….na uwe makini na
kauli zako, mama ni mjanja sana, anatafuta njia ya kumuona baba ana makosa,
nina uhakika kuwa baba hana makosa mimi namfahamu sana baba yangu, na
ikithibiti kuwa kuna kitu kinahusiana na baba, na mama akasikia kutoka
kwako,…utavuruga ndoa yao,…na hapo hutapata mtetezi tena, baba ndiye mtetezi
wako, na alipanga mambo mengi ya kukusaidia…’
Nilijiuliza kwanini huyo mama anatafuta makosa ya mumewe,
ili ndoa ivunjike…au sikumuelewa vyema huyo kijana, ….na kwanini ukweli wangu
uje uvunje hiyo ndoa, sasa nifanyeje, niseme ukweli au nikae kimia, na je
ikijulikana kuwa mimi nasema uwongo,….hapana, mimi nitafuta ushauri wa mama
yangu, mama yangu wakati wote aliniusia kuwa mkweli…hata kama ukweli huo
utaniumiza.
Nilisalimia kwa adabu halafu nikaambiwa nikae , nilikaa
sehemu ambayo naangaliana uso kwa uso na huyo kijana, nilimuona akinitupia
jicho la aina yake, na mara nyingi alikuwa kainamisha kichwa chini.
' Haya tuambieni mlichotuitia…’alianza mzee mmojawapo., na
baba mwenye nyumba ndiye akaanza kuongea;
'Wazee wangu, samahani sana, imebidi niwaite,..nilishawaita
kabla lakini tukaweza kuyamaliza wenyewe, ila hili la sasa
limeshindikana…nikaona ni bora, niwasumbue…lakini hata hivyo, nyie ni wazazi
wangu, mara nyingi matatizo ya kifamilia yakifikia hatua mbaya, ni lazima
tuyafikishe kwenu kuliko kukimbilia mahakamani kwanza….ili muweze kutusaidia…’akaanza
kuongea na wale wazee wakatikisa kichwa kukubaliana, lakini hawakusema neno.
‘Wazee wangu ndoo yangu imeingiliwa na matatizo….’akasema na
kumtupia mkewe jicho, mkewe alikuwa kaangalia pembeni.
'Sawa, kuna tatizo
gani…tuambie…’akasema mzee.
' Mke wangu
haniamini, kafikia kunishuku ugoni, na hata kunitaka tuachane, kwasababu za
kunishuku tu, hana ushahidi, maana sio kweli kwa hayo anayonishuku nayo….’akasema.
'Hilo tu…?’ mzee
akauliza na baba mwenye nyumba akamuangalia huyo mzee kwa macho ya kushangaa,
na kutahayari, akasema;
' Wazee, hilo
mwaliona ni dogo, ..jamani, mpka nimeamua kwuaita mjue kuwa mimi nimeshindwa
kumshawsihi mke wangu, kang’ang’ania kuwa tuachane….na kuachana huko anataka
mimi niondoke kwenye hii nyumba…’akasema.
'Mimi nimeuliza kama kuna nyongeza ya hilo,nikitaka
ufafanuzi zaidi, sina maana ya kuliona hilo jambo kama jambo dogo, udogo wake
na ukubwa wake, unategemeana na maelezo yenu, maana hata sisi tumepitia huko…’akasema
mzee.
'Mengine ya ziada ni kiwa mke wangu kwa hivi sasa haniheshimu
kama mume wake, amekuwa akitafuta mwanya wa kunichafulia heshima yangu….na
kunidharau, sawa, mimi..labda kwa vile hii nyumba tumepewa na wazazi wake,
..lakini tulikubaliana na wazee wakaridha kuwa hii ni nyumba yetu sote,
sikulipinga hilo nikijua haya ni maisha yetu ya mume na mke…’akasema.
'Labda tuanza kulidodosa hili jambo, maana naona utakimbilia
kutoa maelezo mengine ambayo hayayaweza kuleta suluhu, nikuulize kisa hasa nini
nini..ndio huko kukushuku, kwanini akushuku, kuna tukio lilitokea, au …?’
akauliza.
'Labda tumuulize yeye
ambaye ananishuku mimi….’akasema baba mwenye nyumba, na mzee akasema;.
'Kabla ya kumuuliza yeye…sisi
kwanza tunataka tukukabili wewe baba mwenye nyumba, na kwa vile wewe ndiye
umefikia kutuita sisi, yeye, atakuja kuulizwa, lakini kwanza tunataka kusikia
kutoka kwako wewe, kichwa cha familia..swali je ni kweli, kuhusu shutuma hizo…?’ akaulizwa.
'Sio kweli wazee wangu, ndio maana nikaziita shutuma, ni
hisia tu, na sijui kwanini anafikia kunishuku hivyo….’akasema.
'Je mke wako kwa
bahati mbaya, aliwahi kukufumania ukiwa na mwanamke mwingine…?’ akaulizwa na
akamuangalia huyo mzee kwa uso wa kujiuliza ni kama vile anahisi mzee
anamkandamiza, lakini huyo ni baba yake mwenyewe.
'Hapana,..hiyo
haijawahi kutokea,…ndio maana nashindwa kumuelewa…’akasema.
'Sasa ilitokeaje mpaka
akafikia kukushuku…maana yeye sio mtoto mdogo, kuna sababu kakuambia, au
hamjawahi kuliongelea hilo…nakuuliza hili nikiwa na maana mpaka, wanandoa
wanafikia hatua ya kuwaita wazee, ni lazima wameliongea, wakazozana, wakawa
hawaweze kuafikiana, na katika kuzozana huko ni lazima mwenzako atakuwa
kakuambia …na hata kukutokea ushahidi wake, au sio mzee mwenzangu…?’ akasema
huyo mzee.
Mzee mwenzake, akatikisa kichwa kukubaliana na maneno hayo.
'Kuna matukio
yalitokea, yeye akanihisi vibaya, lakini kiukweli sivyo hivyo kama
ilivyoonekana…’akasema.
'Ilikuwaje..tuambie, maana kama mumetuita, basi tunahitajia
ukweli wote…’akasema huyo mzee.
'Kwa tukio la hivi karibuni ambalo limevuka mpaka,…mimi
nilirudi nyumbani na kumkuta mdada wa kazi akiwa kapoteza fahamu….’akasema na
sasa aliyeuliza ni huyu mzee mwingine.
'Kapoteza fahamu…!!, kwa vipi…hebu tuelezee hapo…’akasema
huyo mzee mwingine.
'Nilimkuta kalala sakafuni akiwa hajitambui, …akiwa kapoteza
fahamu….’akasema.
'Oh, kwanini awe hivyo, labda mnajua sababu yake, na je hiyo
ni ara ya kwanza kwa tukio kama hilo..?’ akaulizwa.
'Mhh, kuna kipindi
ilitokea hivyo, na aliyekuwepo, na kumuona ni mke wangu, na wakawahi kumpeleka
hospitalini….’akasema.
'Kwani huyo bint ana
tatizo gani hasa…?’ akauliza.
'Hicho kipindi
alipodondoka, na kupelekwa hospitalini walimpima na wakagundua kuwa aalikuwa na
malaria,ana malaria hiyo ilikuwa imepanda kichwani….’akasema.
‘Kwahiyo wewe ulipomkuta kapoteza fahamu hukutaka kumpeleka
hospitalini au…?’ akaulizwa
'Kwanza ukimkuta mtu
kapoteza fahamu si unatakiwa umkague, na kumpa huduma ya kwanza, si ndio hivyo
wazee wangu…’akasema.
‘Kwahiyo wewe uliamua kumkagua kwanza kama ulivyosema awali….na
ulipomkagua ukaona haina haja ya kumpeleka hospitalini au ulifanyaje..?’
akaulizwa.
'Nilimkagua ndio
nikahakikisha kuwa kapoteza fahamu…na ndio nikaanza kumpatia huduma ya kwanza…’akasema.
'Ulifanyaje…?’
akaulizwa, wazee hawa ni wasomi, kwahiyo maswali yao yalikuwa ya ujanja ujanja,
jamaa wakati mwingine aliona kama wazee hawa na wao wanamshuku vibaya, hata
hivyo aliendelea kuwajibu bila kukasirika.
‘Kwanza nilimlegeza khanga aliyokuwa kajitanda mwilini….’akasema.
‘Kwanga, kwanza alivaaje, maana ukisema khanga, …..ok,
alivaaje,…?’ akaulizwa.
'Mhh,… alikuwa
kafunga khanga moja, ile unafungwa shingoni, na kufunika mwili mnzima.
'Kwanini akawa kavaa hivyo, ina maana alivaa khanga moja tu,
…bila kitu kingine, ndio kawaida yake au…?’ akauliza huyo mzee kwa mashaka.
'Hilo la kwanini,
mimi siwezi kujua, labda atajieleza yeye mwenyewe….’akasema akimtupia mke wake
macho, hakumuangalia huyo binti.
'Kwahiyo wewe
ulifanyaje….ulipomkuta huyo binti kapoteza fahamu baada ya kumkagua…?’ akauliza
mzee.
‘Ina maana mnataka niongee kila kitu, mengine naona kama
hayana umuhimu ….’akalalamika
‘Kijana, mwaneti, sisi ni wazee wako, tuna maana kubwa ya
kukuuliza haya, fununu za hayo yanaytokea humu ndani tumeyasikia sana
tukayapuuzia, sasa tunataka uyajibu maswali yetu, …kwani kuna ubaya ukituelezea…?’
akaulizwa.
'Kwasababu alikuwa kapoteza
fahamu, muhimu nijuavyo mimi ukimkuta mtu wa namna hiyo cha kwanza ni kumlegeza
nguo alizovaa, kama zinambana, kabla ya kumfanyia huduma ya kwanza….’akasema.
'Umesema huyo binti
alikuwa kavaa khanga moja, na khanga tujuavyo sisi ni nguo nyepesi sana, je
ilikuwa inambana, …..?’ akaulizwa.
'Ndio kwasababu, ile
kanga alikuwa kaifunga shingoni, huoni itakuwa imekaza mishipa ya damu shingoni..’akasema.
'Haya,bwana, halafu..ukaifungua
shingoni, na kumuacha uchi au…?’ akauliza na hapo akacheka ile yakuonyesha
anakerwa na hayo maswali.
‘Hakubalia uchi, ililegea kwenye ule mkunjoa wa kufungwa
shingoni,…..’akasema
‘Kwahiyo ukamaliza au ulifanya nini tena…?’ akaulizwa
'Nikamminya kifuani, mara
moja, …mbili….na tatu…ili kurudisha mapigo yake ya moyo…’akasema
'Ok, huo ni utaalamu, unajua wewe,….hebu tukuulize tu, huo
utaalamu wewe ulijifunza wapi..?’ akaulizwa
'Huduma ya kwanza,
nilijifunza chuoni…tunafundishwa, hata vitabuni ipo, kwenye mitandao ipo, ni
kitu cha kawaida tu….’akasema.
'Kifuani kulikuwa
wazi…maana mfano khanga ikifningwa hivi, ukaifungua huku singoni, si inaacha
kifua wazi, na kwa vile alikuwa hajavaa nguo nyingine ni …..atabakiwa huku
wazi, au sio…?’ akauliza mzee.
'Mzee hakubakia wazi,
alikuwa kavaa khanga..kanga ilimfunika….’akasema.
'Khanga tu, hakuvaa
sidiria…hata sidiria….’akasema mzee.
'Wazee, mbona mnauliza maswali hayo…mimi sioni kama
yatasaidia….’akalalamika.
'Mwanetu, sisi sio
watoto wadogo, tunakudodosa tujue ukweli ulivyo, huyo ni mdada, mwili wake wote
unatia hamasa kwa mwanaume, katika maelezo yako hatukusikia neno, kuogopa
kumgusa, nay eye kuna maelezo
alimuelezea mama yake,…je hukumguza zaidi ya kumminya kifuani mara tatu, maana
labda tutasema aliota…’akasema huyo mzee, na jamaa akamtupia mkewe jicho, lenye
kuonyesha chuki fulani.
'Mzee, huyu ni sawa
na bint yangu, namuona kama mtoto wangu, na kwa hali niliyomkuta nayo,
nisingeliweza kuwa na mawazo kama hayo mabaya…sijui kawaambia nini, au mke
wangu kawaambia nini,…lakini mimi nilifanya kile kilichokuwa ni sahihi….’akasema
sasa kwa ukali kidogo.
'Je ungemkuta yupo
kwenye hali tofauti, ungefanyaje..labda kavaa kahanga moja kama hivyo, kama
hujawahi, maana kama alivaa hivyo, yaonyesha ni kawaida,…au sio, …?’ akaulizwa.
'Mimi kama mzazi, ningelimkemea kuwa haifai kuvaa hivyo, na
mimi sijawahi kumuona akiwa kavaa hivyo kabla….’akasema.
'Je ni mara ya ngapi
umemkuta,akiwa katika hali kama hiyo…..?’ akaulizwa
'Una maana gani mzee,
unajua wazee, mimi huwa natoka asubuh, narudi usiku, huwa nipo nyumbani siku za
wikiendi tu na mara nyingi, siku kama hizo, mke wangu yupo….’akasema.
‘ Ni mara ngapi...hivi umeelewa swali..?’ akaulizwa.
'Sikuweza kujua hilo,
kifupi, sijawahi kumuona akiwa katika hali hiyo kabla…, hiyo ni mara ya kwanza
kwangu akasema na mkewe alionekana kutikisa kichwa kama kusikitika kuashiria
kuwa mumewe anadanganya..
'Una uhakika na hilo,
je ukitolewa ushahidi kuwa hiyo sio mara ya kwanza kumuona hivyo utasemaje..?’
akaulizwa
'Mzee…..’akataka
kulalamika na mzee hakumpa nafasi, akamuuliza.
'Hilo tuliache, nikuulize, japokuwa hili ni swali la nyie
wote wawili, ni kwanini ulimkuta huyo binti huko chumbani kwenu…?’ akaulizwa,
na kwanza akamtupia mkewe jicho, kama kutaka kumlaumu lakini akaona mkewe
hamuangalii, akasema;
'Labda alikuwa
anafanya usafi…’akasema
‘Labda, huna uhakika…kwahiyo yeye huwa anafanya usafi hadi
chumbani kwenu, anatandikia, ana…panga nguo zenu,..si ndio hivyo…?’ akaulizwa.
'Mzee kwani hapo kuna
ubaya gani, huyo ni kama binti yangu tu, yupo makamo sawa na huyu kijana
hapa..kwahiyo hata akiingia akafanya usafi, kwangu mimi sioni kuwa ni tatizo…..’akasema.
'Hahaha,…mwanetu…. eti unasema nini,…kuwa hilo sio taizo,
labda niseme kwangu mimi na uzee wangu huu, na kwa mila na desturi, na…hata ukiangalia,
kiuhalisia, na kiubinadamu , hilo kwangu ni tatizo, huwezi kumruhusa mfanyakazi
wa ndani, kufanya usafi hadi chumbani kwenu, huko ni sehemu ya siri kati yenu
wawili, hamjafundishwa hilo jamani, mtasema mnaishi kidhungu au sio…mwanetu,
hilo ni kosa, …sisubirii kulisema huko mwishoni..hilo ni kosa..na adhabu yake
ndio hiyo…’akasema.
'Mzee..adhabu gani…?’
akauliza.
'Msijitetee, mambo mengine mnajitakia nyie wenyewe..mimi
hilo naliwekea alama ya kuuliza, nyie wananda mna matatizo, kama mumeiga,, kama
mlifanya hivyo, kwa vile mnamuona huyo ni sawa na binti yenu,…lakini sio binti
yenu huyo ndio maana hayo mengine yalitokea,….’akasema mzee
‘Mengine yapi mzee…?’ akauliza sasa akionyesha mashaka.
‘Mzee mwenzangu unasemaje kuhusu, wewe unona ni kawaida
kumruhusu binti wa ndani afanye usafi ndani, chumbani, atandike,…na kuvaa
kwenyewe ndio huko…hivi kweli mna akili nyie…’mzee akasema kwa hasira.
'Mhh, hata mimi najiuliza,
labda ndio usasa huo…na madhara yake ndio hayo, na watu hawataki kujifunza,
wanaiga tu,….kiukweli sio sahihi, …’akasema mzee mwenzake.
'Haya ulipomshika
kifuani, ukakandamiza , mara tatu, halafu ikawaje…?’ akauliza huyo mzee sasa
akicheka.
'Mzee naona mnielewe, kama hili mwalichukulia mzaha, mimi ….’akasema
‘Mwanetu, hatukuja kupoteza muda hapa, sisi tunataka
kuwaonyesha madhaifu yenu, ili mjifunze, msione sisi wazee tulikuwa tunafanya
hivyo, tunayajua hayo sana, binadamu ni mdhaifu, nafsi ni kitu kingine,..msiige
tu bila kujua madahara yake…..’akasema huyo
‘Haya atujibu Sali letu, hapa sasa mpo mahakamani, mnatakiwa
mjibu maswali kama yanavyoulizwa, sisi ni wazazi, hata kama mumezaa mna watoto
wakubwa, lakini mkiwa mbele yetu, nyie ni watoto tu…’akasema huyo mzee.
‘Hakuzindukana…’akasema sasa akiwa katahayari.
'Ukafanyaje ulipoona
hakuzindukana…?’ akaulizwa.
'Mzee, kuna huduma ya kumpuliza mdomoni..kama hiyo ya
kifuani haikufanya kazi….’akasema
'Ehee..haya makubwa hayo, ya mdomoni...!!..’akasema huyo
mzee, wazee hawa wawili wakaangaliana.
'Ndio mzee, kwahiyo hayo si yanajulikana jamani….’akasema
'Kwahiyo ukaifanya hiyo, au sio…?’ akaulizwa.
'Hapana mzee..sikufanikiwa kuifanya….wakati najiandaa
kuifanya hiyo, ndio mke wangu akatokea,…..’akasema kwa sauti ya kunywea kidogo.
‘Ukaacha kuifanya hiyo huduma, kwanini sasa….?’ Akaulizwa
'Ndio nikaacha kwasababu….’hakumalizia.
'Kwanini uliacha na wewe ulikuwa ukimuhudumia mgonjwa, hebu
nikuulize docta akamuhudumia mgonjwa, je akitokea docta mwenzake ataicha hiyo
kazi, kwa vile mwenzake katokea…?’ akaulizwa.
'Nilisita,kwa jinsi
mke wangu alivyoniangalia, macho yake yalionyesha kuhisi vibaya, yalimtoka kama
vile kani..’akasita kumalizia.
'Malizia..hilo neno ni muhimu sana tukalisikia…’akaambiwa.
'Ni kama kaona kitu cha kutisha vile….na mimi nikashikwa na
mshangao, kwanini ananiangalia hivyo….’akasema
"Ni kama vile kakufumania au sio...?" akasema huyo
mzee
'Nahisi hivyo..lakini sio kweli….’akasema
'Kwanini akuhisi hivyo, kwani alikukutaje, ulikuwaje, wakati
unafanya hayo…?’ akaulizwa
'Mimi Sijui kwanini
alionekana kuniangalia hivyo, na hakunipa nafasi ya kujieleza…’akasema
'Hebu nikuulize wakati unamfanyia huyo mdada huyo huduma
ulikuwa umekaaje…?’ akaulizwa
'Mzee kwa vyovyote
nitakuwa nimepiga magoti, nimemuinamia….ningafanyaje ..?’ akaulizwa
‘Kwanini ulivua shati, …?’ akaulizwa na hapo akashtuka.
‘Mzee hapo ni chumbani kwangu,….nilipofika nilivua shati,
nilihisi joto, na nilitaka nibadili nichukue jingine nilivua hilo hata kabla
sijajua kuwa kuna mtu humo ndani…..’akasema.
‘Una uhakika kuwa ulimshika kufuani, tu ukambinya mara tatu
tu….maana ukumbuke hilo tendo, hukulifanya ukiwa peke yako, kuna watu
walikuona, na mtendewa mwenyewe …unajua..mwanetu, humu ndani kuna tatizo,….mna
mataizo makubwa, mpaka sisi tunakubali kufika hapa, mjue kuna tatizo, na sio
wajinga sisi kukuuliza maswali kama hayo….sasa kabla hatujaanza kumuhoji mkeo,
..kabla hatujaanza kumuuliza binti, na kabla hatujawaleta mashahidi kuwa..hapa
ndani kuna tatizo, nakupa nafasi ya mwisho.
‘Mzee, unataka kusema nini, kuwa mimi …’
‘Mimi ni baba yako, nimekuzaa mwenyewe, na haya yaliyotokea humu
ndani yalilifika hadi kwangu, awali nilikutetea sana maana sivyo nilivyokulea
hivyo , na sikuamini nilipoambiwa hayo, nikataka kutafuta ushahidi,
na..nimekuhoji maswali hayo nikiwa na maana…kijana, mimi ni baba yako
nimemuangukia mzee mwenzangu ili haya yaishe,..lakini yataishaje kama
hujauangama…ukakiri kosa yakaisha…
‘Baba….’akawa kakasirika sasa.
‘Nataka wewe ukiri ukweli, useme ukweli haya yaishe,
mwenzako kasema ukikiri ukweli, yupo tayati kukusamehe, lakini kama utaendelea
kuwa mkaidi, na wakati unajua ulitenda kosa, na yaliyashatendeka awali
akakusamehe, …sasa ni mara ya pili…mimi nitanawa mikono, nimekudhamini kuwa
wewe utasema ukweli na kukiri kosa, sasa nakupatia nafsi hiyo ya mwisho kabla
hatujamuuliza bint ambaye ndiye mtendewa, najua ataelezea yote yaliyowahi
kumtokea, na hilo, ulipojifanya unamfanyia huduma ya kwanza,..na kuna mashahidi
wengine…..’akasema huyo mzee.
‘Mwanetu, hebu fikiria hivi, wewe haupo duniani, una binti kama
huyu, anafika kwenye nyumba za watu wanamfanyiwa mambo kama hayo..utajisikiaje…,
hebu liweke akilini hivyo. Maana usiseme kwako haiwezi kutokea, mungu ni wajabu
sana, wangapi walikuwa wanahali nzuri sana, lakini sasa wapo mitaani, wangapi
walikuwa na hali nzuri, walipofariki, wakawaacha nyuma wanafamilia, wakaja
kufirikisika hadi kufikia kuwa omba omba..hawa waliomba..hapana,…hii inaweza
kumtokea yoyote, …liwazie sana hilo mwanangu…’akasema mzee
‘Kama unaona sio kweli, tutaanza kuitisha mashahidi…na hapo
sijui utasemaje,…maana nimesikia mengi,..kuna binti alikuwa hapa awali,
ilitokeaje,…utasema ni uzushi….ee , na huo ni uzushi…nakuuliza wewe….? mwanangu ndivyo nilivyokulea hivyo, kuna
tatizo gani….sasa ni muda wa kuniambia ukweli, kama umeniita hapa kuja kuikoa
ndoa yako, sasa nahitajia ukweli, na…huyu binti wa watu apate haki yake,
sipendi watu kama hawa wateseke, eti kwa vile masikini….je upo tayari kuusema
ukweli…na …’akatulia.
Baba mwenye nyumba akageuka kumuangalia kijana wake, halafu
binti, kwa mara ya kwanza akamuangalia huyo binti,…sasa akiwa kakunja uso kwa
hasira, baadae akainamisha kichwa chini, na alipoinua machozi yakawa yanamtoka…huku
uso umejaa hasira.
NB: Imebidi niliweke hili hivi…ili kufunua ukweli wa maisha
katika familia.
WAZO LA LEO: Ili
uishi kwa amani,…jitahidi kuepuka,..kuweka visasi moyoni, kupenda kulalamika-lalamika,
kulaumu wengine…, kufanya mambo kwa vile umefanyiwa, wewe fanya mema vile
itakiwavyo bila kujali kuwa na wewe umefanyiwa au la…maana kufanya hivyo, kuna
neema yake, kuliko kutokufanya, na ukifanya kwa vile umefanyiwa hiyo ni ria, na
ria ni shrike ndogo,…wewe fanya ukijua ni wajibu wako, na Mola atakuzidishia
baraka kwa kujitolea kwako kwa mema unayoyafanya.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment