Tulifika
hospitalini lakini muda wa kuingia watu kuwaona wagonjwa ulikuwa bado, na hata
hao akina mama walipojaribu kutumia wadhifa wa waume wao ili wapate nafasi za
upendeleo waligomewa , ikabidi sasa wajishushe na kuanza kubembeleza.
‘Hatuwezi
kuwaruhusu kiukweli,kutokana na hali za wagonjwa, muda huu wanaonana na
madakitari wao, wengine wanapata huduma mbali mbali, mkiingia mtasababisha kazi
zingine zisifanyike, na wakati mwingine ni kwa afya zenu pia,kwani mlitaka
kumuona nani..?’ akauliza mhusika wa wodi hiyo.
Wale
akina mama hapo wakgeukiana, kwani wote walikuwa hawajui jina la mgonjwa
wanayetaka kumuona,….
‘Unajua
huyo mgonjwa ndio leo tumapigiwa simu, ni ndugu wa mfanyakazi wetu wa ndani, na
yupo kule nje, sasa muda unatubana, tumajiiba mara moja kuja kumuona kuna
maswala muhimu ya kufuatilia, nasikia anahijika dawa, na dawa hizo ni gharama
sana, tunahitajika kuchangishana, sasa tusipokutana naye akatuambia vyema ni
dawa gani tunashindwa kulifanyia kazi, tunataka tuongee na mgonjwa mwenyewe
tusikie kauli yake,…’akasema
‘Nimewaelewa,
ina maana nyie mnachotaka ni kuhakikisha kama kweli anahitajia hizo dawa, maana
hawa wafanyakazi wa nyumbani wengine ni waongo ni kama watoto wadogo au sio…’akasema
na ashukuru wakati anaongea hayo nilikuwa nje.
‘Ndio
hivyo…’akasema mama mmojawapo
‘Oh,
sasa kwa unyeti wa jambo lenyewe, mimi siwezi kuwaruhusu wote kuingia huko
ndani, kwani lolote likitokea mtaniweka mimi kwenye wakati mgumu…’akasema.
‘Lolote
kwa vipi,….sisi lengo letu nikupata huop uhakika, na kauli ya mgonjwa,
tunakuhakikishia hakuna baya litatokea, kama mume wangu angelikuwepo hapa
..yeye ni askari basi angekuhakikishia hilo…’akasema mama .
‘Sio
swala la uaskari au ubosi, ni utaratibu mama yangu, haya ingieni lakini
nawaomba, msije mkafanya jambo la kunifukuzisha kazi tafadhali…’akasema na
hapo, ndio wakapata mwanya wa kuingia kwa kujiiba, na sisi kwa haraka tukakimbia
na kujiunga nao, msimamizi huyo alikuwa kaangalia kwingine kwahiyo hakutuona
sisi tukiingia wodini.
Ilikuwa wodi ya wagonjwa wa namna hiyo,
ukianzia mlangoni, utaanza kuhisi huruma kama binadamu, kuna magonjwa
yanawatesa watu, mtu wa kwanza mguu umekuwa kama umeoza, uso umeshakata tamaa
ya kupona, wa pili yeye mguu wake mmoja umeshakatwa,…ukiendelea mbele, ni kila
mmoja humo yupo kwenye mtihani mnzito wa maradhi haya ambayo, yanatishia amani
za watu. Wakina mama hao japokuwa walikuja kwa jaziba, lakini kutokana na hiyo
hali, nafsi, zikanywea.
Tulitembea
hadi kitanda alicholazwa huyo mtu wetu tunayemfuatilia, nilijaribu kuwaza jinsi
gani wataweza kumuongelesha hapo maana chumba kina wagonjwa,..na wapo macho,
watasikia,…tukasogea hadi kwenye kile kitanda, tulimkuta jamaa kakaa kitandani
akiwa kainamisha kichwa chini, hakutarajia ugeni labda maana alipotuona
alishtuka, na kutukazia macho, na alipogundua ugeni huo ni wa watu gani, akainamisha
kichwa chini.
‘Kumbe
ndio wewe…’akasema yule mama mwenye nyumba kwa mdada.
‘Ndio
mimi, karibuni wapendwa, karibuni sana, mimi sijambo kiasi, ndio nasubiria
vipimo, ila mengine nimeshaambiwa, kuna dawa zinahitajika, ni aghalai kweli,
kwahiyo kufika kwenu, nahisi tatizo litakwisha…’akasema.
‘Pole
sana, naona umetukumbuka….’akasema huyo mama.
‘Ndio
nimewakumbuka sana, siku ile, nilikuja
pale nyumbani kwako, kuonana na mdada…’ akasema.
‘Sio
siku ile tu, umekuwa ukitutembelea mara kadha wa kadha, unatuona sisi tukiwa
tumelala, si ndio hivyo, kwahiyo huwezi kutusahau…’akasema mama mfadhili wangu
wa kwanza.
‘Kuwatembelea….mmh,
hapana mimi nimelazwa hapa, tokea wiki sasa, ningekujaje nyumbani kwako…nafikiri
umehisi vibaya…..’akajitetea akionyesha uso wa mashaka.
‘Kama
kabla ya matatizo hayo, uliweza kutokea huko kwenu mikoani, hadi hapa Dar, na
kuingia ndani kwenye majumba ya watu usiku ushindwe kuja kwangu ukiwa hapa dar…au
tunaongea kwenye watu wengi usingelipenda watu wakakufahamu ..’akaambiwa na
hapo akakaa kimia.
‘Tuambie,
sasa lengo lako ni nini, na unapata faida gani kwa ushenzi huo…’akaulizwa na kwanza
akazungusha kichwa kuangalia watu, wagonjwa walikuwa wamejilalia, wakiugulia
maumivu, kwahiyo hakuona mtu mwenye dalili y akuwasikiliza, akasema;
‘Jamani
mbona siwaelewi,….’akasema
‘Huwezi
kujibu maswali yetu, …au unataka ukayajibie polisi..’akaambiwa
‘Jamani
sikilizeni, hapa siwezi kuongea kitu, kama ingeliwezekana, nilitaka tuwe na
nafasi nyingine sio hapa, nieleweni kidogo, kama kweli mna nia ya kusaidiana
kwa matatizo yenu…’akajitetea
‘Kwanini
unaogopa kuongelea hapa, wewe si unajiamini, huko kijijini unatamba kabisa wewe
ni nani, au ?’ akaulizwa
‘Mambo
mengine ni ya siri, siwezi kuyaongea hapa, na hayo uliyoyasikia kutoka huko
kijijini ni uwongo na fitina za watu, tuyaache hayo tuongelee jambo la msingi,
au mnataka nini kwangu…?’akasema na kuuliza.
‘La
msingi kama lipi, haya tunayokuuliza kwetu ni ya msingi sana, maana yanatutesa,
hatuna amani, sasa tuambie wewe ulitaka tuongelee nini kwanza..?’ akaulizwa.
Akageuka
huku na kule , mara uso wake ukatua kwa mdada, ambaye ndiye chanzo cha haya
yote, akakunja uso, na hakumuangalia sana, akainamisha kichwa chini na kusema.
‘Mhh,
yaani, hata wewe, ….nilikuamini, nika….Ina maana, hebu jamani niambieni, shida
yenu ni nini hasa….?’ Akauliza.
‘Ndio
ujue kuwa mwisho wa mambo yako umefikia kikomo, si nilikuonya,…nilikuambia huko
ulipokwenda utakuja kujuta, wewe tucheze sisi wanyonge lakini ipo siku
utakutana na wasioingilika, uliniambia nini kuwa hujali, hata nilipolia,
nakumuomba mungu akuangamize, ulisema nini, rudia yale maneno yako wayasikie
hawa watu…’akasema.
‘Jamani
wandugu ni hivi,…huyu ni mmoja wa watu wanaonijengea majungu na fitina, alikuja
kwangu na kuanza kunilalamikia kuwa mimi ndio nimemfanya hiki na kile…nikamsaidia,
nikamuambia akafanye kadha wa kadha, atapona, muulizeni hakupona huyu, sasa na
nyie kama mna matatizo yenu, nitawasaidia, lakini kwanza kwa hali niliyo nayo
na mimi nahitajia kusaidiwa…’akasema.
‘Utatusaidia
nini, ni nani kasema anahitajia msaada wako kati yetu sisi hapa, wewe ndio wa
kutusaidi sisi, au unafikiri vitisho vyako vya uchawi vinaweza kututisha sisi,
watishe watu wa huko kijijini, lakini sio sisi, unasikia..’akaambiwa
‘Sasa
mumefuata nini hapa..?’ akauliza sasa akionyesha jeuri yake, akawaangalia akiwa
kawakazia macho.
‘Sisi
kwanza tunataka kuwaita waandishi wa habari wazichukue taarifa zako zote tuna
ushahidi wote kuwa wewe ni mchawi..wewe ndiye wale watu wanaowatishia watu huko
kijijini, kwa imani za kishirikina, nyie ndio watu mnaotafutwa na polisi, mnaua
wazee, mnaua watoto, mnawakata kata viongo vyao,..kwa imani za kishirikina,
..kweli si kweli…’mama akasema kwa nguvu na kuwafanya wagonjwa waliopo humo
ndani kugeuka kuona ni nani huyo anaongelewa
‘Jamani
hayo yanakujaje, una ushahidi gani na kauli yako hiyo,…kama ningelikuwa mchawi
si ningelijiganga mimi mwenyewe, mbona na mimi nipo hapa hospitalini nahitajia
matibabu, hizo kauli ni uzushi kabisa…’akasema sasa akiwa kainama tena.
‘Kuumwa
kwako huko, ni kuwa umehangaika ukashindwa, wewe hujui ni kwanini huponi, hiyo nio
adhabu ya uchawi wako, maapizo ya watu yanakurudia….’akaambiwa.
‘Ina
maana wote wanaoumwa humu ndani ni wachawi…au umeniona mimi tu..?’ akauliza
alipoona watu sasa wanaangalia wao.
‘Wao,
sio wachawi , usitake kukwepesha mada, wewe ndio mchawi, wengine wanaumwa
maradhi kama mitihani tu, mungu atawajalia watapona, hiyo ni mitihani ya mungu
kwao, lakini wewe kuumwa kwako ni tofauti na wao, wewe umekuwa ukiwatesa watu,
ukiwatembelea usiku ukiwanga.., kweli si kweli…muda umefika sasa tubu dhambi
zako ili upone…vinginevyo utaoza mwili mzima huku unajiona…’akaambiwa.
‘Mumeharibu
ndugu zanguni,..hapo mlipofikia, nawaambia wazi mumeharibu, hatuendi hivyo…
nilitaka kuwasaidia lakini kwa njia hii hamtaweza kupata msaada wangu tena, na
mtakuja kuniambia, mnasikia, hamnijui tu mimi ni mtu mwema sana, kwa wanataka
wema wangu, lakini ukinichefua, huwezi kuamini, na ndio maana watu wananiogopa..’akasema.
‘Na
sisi tukuambie hivi, hapa tumekuja rasmi, tumejiandaa kwa hilo, ulisikia mdada
alivyokuambia, ulizoea kuwasumbua watu wa huko kwenu, sasa umejaribu kusipojaribiwa,
umeingia choo cha kike, na utajuta kwa hilo, hatukutishi bali tunakuambia,….sasa
tuambie, wewe kwanza unataka kutibiwa si ndio hivyo, sasa utatibiwaje, wakati
unategemea pesa kutoka kwetu..?’ akaulizwa.
‘Nitazipata
tu, hilo halina shaka,…nyie subirini muone, nina namna nyingi ya kuzipata hizo
pesa, ila kwa vile mimi niliona nyie ni watu wema, mnaishi na binti wa huko
kwetu na mpo kwenye matatizo, basi tusaidiane, ndio lengo langu hilo…’akasema
na mara docta akaingia.
*************
‘Mbona
naona kama kuna kelele hapa, kuna nini..?’ akauliza huyo docta na mmoja wa
akina mama wale akamchukua huyo docta na kwenda kuongea naye pembeni waliongea
kwa muda halafu yule docta akarejea na kusema;
‘Mgonjwa
samahani, kwa vile nyie mna mazunguzmo nyeti, kama nilivyoambiwa, hatuna
kawaida hiyo, ila kwa dharura tunafanya hivyo, ili kutokuwasumbua wagonjwa
wengine, tutakuombe muende nje, au chumba …nitawaonyesha muingie huko muongee
kwa uhuru, naukimaliza, utarudi hapa, sawa, upo tayari..?’ akaulizwa na yeye
akabakia kimia kwa muda, halafu akasema;
‘Sawa
ilimradi unihakikishie usalama wangu…’akasema huyo jamaa.
‘Usalama
wako kwa vipi tena, unaogopa nini, kwani hawa sio jamaa zako?’ akaulizwa.
‘Ni
jamaa zangu ndio, lakini wamekuja kwa hasira, hatuelewani ..lakini hamna shida,
nitaongea nao tu, ukiwa na shdia, huna ujanja…’akasema.
‘Lakini
kauli yako inanipa mashaka, kwanini unasema hivyo,…?’ akauliza docta.
‘Ndivyo
alivyo huyu, tokea aanze kuumwa anakuwa hivyo anahisi kila mtu ni mbaya wake,
hata kwa yale mambo ya kumsaidia, …’akasema mama mmojawapo, na docta akatikisa
kichwa kuonyesha kuwa kaelewa.
‘Ndio
hivyo ni kweli, haya magonjwa wengu hufikia hivyo, lakini watapona tu, ila
jamani msije mkabishana hadi kuleta vurugu, kauli yake hiyo kwangu nimeipokea
vingine kabisa, mnasikia….’akasema docta.
‘Kama
nilivyokuambia docta kuna mambo nyeti, tunatakiwa tuongee naye, tukiwa peke
yetu, hilo la usalama wake usiwe na wasiwasi, yeye ana kawaida ya kuongea hivi,
kutokana na kuchanganyikiwa kwake, maradhi etna hayo docta….’akasema huyo mama.
‘Sawa
mimi nawaruhusu lakini nataka uhakika wenu wa kuwa hamtafanya lolote baya..kama
anavyodai yeye…’akasema docta.
‘Tunakuhakikishia
hilo docta, atarudi salama..’akasema mama yule aliyenipeleka mimi hospitalini,
na docta akaondoka, akisema;
‘Njooni
huku na mgonjwa…’akasema
Mgonjwa
kwanza akawa anasita kuondoka, ndipo mdada akajitokeza na kusema
‘Wewe
ni mwanaume unatishwa na wanawake hahaha, na kujifanya kwako mchawi, nguvu za
gizani kwenye mwanga unaogopa au sio, kama kweli unataka msaada wa kipesa ,
jitokeze uwashawishi hawa akina mama, vinginevyo, utaoza, na utazikwa kwa aibu..’kauli
ile ilimfanya jamaa ajitutumie na kuinuka kitandani, akaanza kutembea kulekea
huko kwenye chumba cha maongozi, kiukweli alishaanza kuwa kwenye hali mbaya
hata kutemba ilikuwa ni shida.
Mama
mmojawapo akawa anapiga simu kuwasiliana na watu wake na mwishoni akasema
‘Tayari..kakubali,
mleteni, na kila kitu…’akasema
Mimi
nilikuwa nyuma nyuma nikimuangalia huyu mtu kwa mbali, jinsi alivyo,
anavyotembea, kiukweli japokuwa anaumwa na huruma za kibinadamu mtu kama huyo
inabidi umuonee huruma, lakini nikiwazia yaliyonipata nilihisi vibaya, nikahisi
kama kutapika!
Sikuweza
kuvumilia…nikaruka kumvaa huyu jamaa..
NB: Sehemu
hii iishie hapa, lakini shemu nyingine ipo tayari, kama watu watasoma kwa
haraka, nitaweka sehemu nyingine jioni..Mungu akipenda..
WAZO LA LEO: Unaweza ukawa mtenda madhambi,
mdhulumaji, watu wakawa wanakuhisi na hata kukuonya,lakini ukajifanya
hujulikani, ukakana madhambi yako, huku unaendelea kuyatenda madhambi…, swali
je unamdanganya nani, ..ukumbuke vyovyote ufayavyo, chochote ukifanyacho
mwenyezimungu anakuona, na uovu wake unazidi…kwa vile umeonywa na wtu ukakaidi.
Jamani tumuoge mola, dunia hii ni ya kupita, huyajui ya kesho.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment