Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, July 24, 2017

DUWA LA KUKU.....18



‘Mimi naona,…tukakutane na huyo mchawi huko huko hospitalini, kwanini anatutishia amano...'alisema huyo mama mwenye nyumba

'Sawa mimi naona iwe hivyo, kwa maana kwanza kama ni kweli yeye aliingia nyumbani kwangu akafanya hayo aliyoyafanya..akaharibu familia yangu na kutia fitina,..mimi mwenyewe , nahitajia kuonana naye...'akasema mama mfadhili wangu wa kwanza.

'Hilo jambo jema,, tuhakikishe tumelimaliza hili ili tuishe kwenye familia zetu kwa amani, maana leo kwako kesho kwangu, kama huyu binti kaja kwangu na mzigo, na huenda huo mzigo ni wake, si lazima atakuja kunisumbua na mimi,...huyu na mwenzake tuwakabidhishe kwake, na huyo mtu, apate kipigo, ajifunze...'akasema yule mama aliyenipeleka hospitalini.

Kiukweli sikuwa na amani, nikajua sasa maisha yangu yanakwenda kuharibiwa kabisa, bado nina mzigo, na simjui baba yake ni nani, na....haya yanayokwenda kutokea huko sijui yatatufikisha wapi, kama akina mama hawa wataamua kufany hayo yaliyopo kwenye nfasi zao

Tuendelee na kisa chetu...

****************

Wale akina mama watatu wakakubaliana hivyo ikawa ni muda wa kusubiria simu ambayo ilikuwa inapigwa kwa mume wa mmojawapo hapo, na wengine wakaamua na wao watumie muda huo kuwasiliana na waume zao, ili wajulikane wapi  walipo na wanataka kwenda kufanya nini huko.
Kiukweli waume walikubaliana na maamuzi yao, ila waliwatahadharisha kutokuchukua maamuzi ya haraka na kuchukua hatua mikononi mwao, muhimu wafike huko wamuulize wasikie huyo mtu atasema nini, kwasababu mambo ya kichawi, mara nyingi huwa hayana ushahidi wa moja kwa moja.

Baada ya kauli hiyo, wale akina mama wakashauriana kidogo, na baadae tukaanza safari ya kuelekea huko hospitalini, ocean road. Sisi tulipotoka tukawa tunajiuliza tuingie kwenye gari gani, na bahati nzuri, mimi nikajikuta nipo kwenye gari la mfadhili wangu wa awali,…pamoja na yote hayo, mfadhili huyu , kwangu mimi sikumuona na roho mbaya kama hao wengine.

Wakati tumeshaingia njia kuu, mara mama huyu akanigeukia mara moja na kunitupia jicho, alinikuta natoa machozi, akaangalia mbele na kuendelea kuendesha gari lake akiwa kimia, baadae akasema;

'Mimi sipendi kuongea nikiwa naendesha gari, napendelea kuwa kimia, labda iwe ni kitu muhimu cha kuongea, sasa ni hivi, nataka kukuuliza maswali, unijibu , na nataka ukweli, usiwe mtu wa kuzunguka zunguka, huu ni muda wa kusema ukweli la sivyo, yatakayotokea usije kumlaumu mtu..’akasema.

'Niulize tu madam..'nikajikuta nimemuita madam, tofauti na nilivyozoea kumuita `mama’ na hapo akanitupia jicho, hakusema kitu kwa mara moja, akawa kimia kwa muda hivi huku akiendesha gari lake yeye alikuwa nyuma ya wenzake wote.., halafu akasema;

 'Mimi sijakuamini kuwa mume wangu hakuwahi kukufanyia jambo …au hata kukutongoza, au kukushika kwa nguvu, pia sijakubaliana na wewe kuwa hukuwahi kumuona akiingia chumbani kwako, sasa nataka kwa mara ya mwisho uniambie ukweli…’akasema na mimi kwanza nilikaa kimia, halafu nikasema;

 'Kiukweli mama, mengine yote ni hisia, na hisia huwezi kusema ni ukweli, unaweza ukahisi kitu kumbe sio kweli, ila jibu langu ni lile lile, kuwa mume wako, hajaweza kunifanyia kitu kama hicho, nikiwa namuona, kwa macho yangu, mimi siwezi kumsingizia mtu ubaya wakati sijamuona…ndio hivyo mama…’nikasema.

'Kwahiyo hata siku ile nillipokukuta umelala sakafuni, yeye yupo juu yako, hukumuona au wakati unafagia chumbani kwangu hajawahi kukugusa..?’ akaniuliza na hapo nikajaribu kukumbuka yale matukio, na jibu likanijia hivi…

'Sikuwahi kumuona…naogopa kusema hivyo,…macho ndio ushahidi unaoutaka, na macho yangu hayakuwahi kumuona, huo ndio ukweli…mungu anajua zaidi…’nikasema hivyo.

'Na haijawahi kutokea jambp la kuweza kumuhisi vibaya,…?’ akaniuliza.

'Hapana, hajawahi…kwa maana mimi huwa siwachunguzi watu, kwahiyo inakuwa vigumu kwangu kumuhisi vibaya, yeye kama wanaume wengine najitahidi sana kuwa mbali nao…’nikasema na nilisubiria aniulize kuhusu mtoto wake, hapo majibu huenda yangelikuwa tofauti.

'Kwahiyo huwezi kumshuku kwa hiyo mimba, kuwa huenda kutokana na maelezo ya huyo rafiki yako, inaweza ikawa ni yake…?’ akaniuliza nashangaa hakugusia kuhusu mtoto wake.

'Nitamshukuje sasa, mama hebu jaribu kunielewa, mimi naogopa kutenda dhambi, kumshuku mtu bola ushahidi ni dhambi, au nakosea mama…’akasema hivyo.

'Mfano kama aliyoyasema huyo mdada ni kweli, na ikatokea kuwa mtoto ni wake, labda baada ya kujifungu avikachukuliwa vipimo, au huyo mchawi akalithibitisha hilo, kuwa mume wangu anahusika, je wewe utachukua hatua gani..?’ akauliza na mimi nikakaa kimia.

'Mimi kwa hilo sijui, ninachoweza kusema, hayo yote ni mungu mwenyewe kapanga hivyo, nay eye ndiye atanipa njia, maana mimi kama mimi nitasemaje, je nilikubaliana na hilo, kama ningekuwa nimshikiriki kwenye makubaliano, au nilithibitisha, ningelisema ningefanyaje, …ndio maana nachanganyikiwa..’akasema.

'Sawa mimi nimekuelewa, pamoja na yote,…ila kwa hali ilivyo mimi siwezi kukusaidia zaidi ya hapo, na pia siwezi kubeba huo mzigo, ni wewe mwenyewe ujipange, na uhangaike, kutafuta jinsi gani ya kufanya, au unataka mimi nikusaidieje kwa hilo..?’ akaniuliza

'Ndio hapo, naona nabebeshwa mizigo ambayo mimi sijui imetokea wapi, na sijui nitaenda wapi, labda natakiwa nimfuate mama yangu..kila nikiwaza naona iwe hivyo, namuomba mungu , kama yawezekana iwe hivyo, maana mimi siwezi jamani, siwezi hata kufikiria nifanyeje, kwa umri huu, na mambo kama haya ni mageni kwangu..basi tu, nitazidi kuomba, japokuwa duwa la kuku halimpati mwewe…’nikasema huku machozi yanaendelea kunitoka.

 'Kwahiyo wewe unataka kusema nini, kuwa ni heri ufe,..hahaha, kwa mtihani huo, ujue dunia hii imejaa mitihani mingi, huo ni mwanzo tu, ..sikusemei mabaya, lakini umri utakavyokwenda, ujue utaingie kwenye matatizo, wewe usione mimi nipo hivi, nab ado tuna uwezo, nimetokea kwenye familia yenye uwezo, lakini matatizo, na mitihani ni mingi ajabu….’akasema.

'Sio kwamba mimi nataka nife, ila nionavyo, ndivyo watu wanataka iwe hivyo, najiuliza sana , ten asana kwanini wanatufanyia sisi hivi, tuna nini cha kuwapa, tuna nini ambacho ni zaidi ya wengine, ..nashindwa kuelewa, ..mungu mwenyewe ndiye anajua..’nikasema.

'Sikiliza binti..wewe nimekuchukua kama binti yangu, na nilitarajia kwa vile mimi ndiye nimekutoa nyumbani unekuwa karibu na mimi ikanieleza matatizo yako…katika maisha haya vyovyote uwavyo, usikubali kuwa mnyonge kiasi hicho..pambana na maisha na anzia hapa kuidai haki yako, mimi siwezi kukuambia fanya hivi, maana mengine yanaweza kuja kuniathiri mimi, na ikifikia kwenye kupambana kudai haki yangu ukiwa mbele yangu, tutapambana na wewe pambana kivyako…’akasema.

 'Sasa mama nikuulize kitu…nachukulia kama mfano, hivi itokee kuwa mimba ni ya mume wako, mimi sijui lakini nakuuliza wewe tu, labda alivyosema mdada ikawa ni kweli, utachukua hatua gani kwa mume wako, au kwa ki-…’hapo sikumalizia maana alinitupia jicho kuniangalia.

'Nichukue hatua gani hahaha…unajua nimeliwazia sana hilo, nilitaka kuchukua hatua kama tulivyoongea kwenye kikao, kwa hasira, lakini sasa…navuta subira, maana mambo kama haya, yana mwisho wake, za mwizi ni arubaini, na mimi kama binadamu nina hatua zangu za uvumilivu,..kwa hivi sasa sina haja ya kuchukua hatua yoyote, zaidi ya wewe kuondoka, wewe swali hili nikugeuzie wewe..ingawaje umenijibu awali,…’akasema.

'Mimi kiukweli jibu langu lipo pale pale… sijui, maana nitashindanaje na tajiri, na akiwa labda kadhamiria, au kama ndio hivyo sio kwa utashi wake, na alishakataa kata kata, na ni kweli kama ni kweli alivyoongea huyo mdada, sasa mimi nitfanyaje hapo…’nikasema.

'Kwahiyo utakaa kimia, je huyo mtoto utamleaje na hali kama hii, na usitarajia kwa hali kama hiyo mimi nitatia mguu wangu hapo, dunia itaniona wa ajabu ni kama vile tulipanga mimi na mume wangu,..ndio huruma ninayo, lakini …hapana, hilo kama ni hivyo utajua wewe mwenyewe utakavyo mshawishi mume wangu, …ndio hivyo…’akahema kama vile katua mzigo mnzito.

'Mungu anajua zaidi mama, nashukuru wewe umekuwa mkweli wangu…na kama mungu kanibebesha mtihani huu kwa maana maalumu, basi nitafanyaje, nitaubeba tu..na nitajitahidi kumuambia huyo mtoto nitakaye mzaa, kuwa hana baba,…na mimi nina imani kuwa mungu kama kanipa mtihani huu, bado nitamuomba anipe njia ya kuishi, njia ya kumlea huyo mtoto…sitamtupa…’nikasema nivuta pumzi ya mtu anayelia.

'Wewe ni mtu wa ajabu kweli, sijawahi kumuona, sijawahi kumsikia mtu anakubali kirahisi hivyo, imani yako ni ya ajabu…mmh, wote tungelikuwa hivyo, dunia ingelikuwa nyingine, lakini hayo si ya dunia hii nikuambie ukweli,…..’akasema.

'Sasa wewe kama mama yangu ungenishaurije..nifanyaje kwa hatua kama hii…?’ nikamuuliza.

'Mimi siwezi kukushauri kitu zaidi ya hivyo nilivyokushauri, kuwa upiganie haki yako, usikubali kuwa mnyonge, maana haki wakati mwingine inabidi uipiganie, ili mungu akuone kweli una nia hiyo, unanielewa hapo….’akasema.

'Nimekuelewa kama sikukuelewa,…mungu anisaidie tu, unajua mama yangu aliniasa sana alijua dunia itanielemea, lakini alinishauri sana ten asana, nisije kusema uwongo, na kitu kama sina uhakika nacho ni bora nikae kimia tu…ndio maana najitahidi kuwa hivyo…’nikasema

'Sawa, ila kama huyo mchawi atakiri kuwa huenda mimba ni yake, sisi tutakukabidhi kwake, mtajuana wewe nay eye ni nini cha kufanya hayo ndiyo maamuzi yetu, na kama atasema ni ya mume wangu halikadhalika, sisi tutakubadihidha kwa mume wangu mtajua namna gani ya kufanya,..hilo nakugusia tu…’akasema

'Siwezi kukubali, kwa mamaumizi hayo,… hata kama mimba ni yake, mimi siwezi kushirikiana na mshikirikia matu anayempinga mwenyezimungu kiuwazi, mchai hapana, ni bora nibakia na mtoto wangu nihangaike kivyangu…’nikasema

'Tunasemea kama yeye atakiri hivyo…maana yeye kama hivyo ni kweli, ndiye anayefahamu ukweli wote….’akasema
'Mungu anajua zaidi, siwezi kujua yajayo, kadara zake zitatenda, mimi kwa ufupi namuachia yeye aliyeyakadria haya, sina zaidi mama…’nikasema.

‘Mmmh, kweli tembea uone, sikubahatika kukutana na mtu kama wewe kabla, nikuambie kitu, dunia hii haipo, kama wewe unavyofikiria hivyo, na imani ya kweli si hivyo tu, bado inatakiwa juhudu za kimakusudi, maana kama ingekuwa imani ni hivyo watu tusingelifanya kazi, mungu si atatupa riziki zetu, unahisi ni kwanini ado tunahangaika…’akasema.

‘Hata mimi nahangaika, sikuwahi kukaa tu,…mama alinishauri nisiwe mvivu, sasa ndio nimekuja kufanya kazi kwenu yametokea hayo, ningelifanya nini,…mfano kama ningechukulai hisia zangu tu nikasema kutokana na hisia zangu tu huoni kuwa ningelivunja ndoa yenu, na sasa hapo kama je sio kweli….mungu ataniadhibu sana, ndio maana nimeamua kusema niliyoyasema.’nikasema.

'Haya sawa, ila nikupe tu kama angalizo, mume wangu hawezi kukuoa, na hata kama mtoto atakuwa ni wake, sio kwasababu ananipenda mimi, hapana, ni kwa vile lengo lake ni mali, anajua akiniacha mimi atakosa kila kitu, akija kwako utampa nn, eeh,..utampa mwili, eeh, mvuto wa ujana, lakini yeye pia anaangalia na maisha huko mbele yatakuwaje,…au wewe mfano akikuchukua utamsaidia nini ili maisha yasonge mbele..nikuonavyo wewe utakuwa unamwambia, msubirie mungu atawashuhia riziki….’akasema.

 'Mimi sijasema namtaka mume wako, naomba hilo unielewe mama, mimi  sina wazo hilo kabisa, yeye namuona ni sawa na baba yangu, hata kama mtoto ni wake, kamwe sitaweza kufanya hivyo..yeye afanye ajuavyo, lakini sio kunichukua mimi, na asitarajie kuwa mimi atakuja kuniomba….nimkubalie nikiwa na akili zangu hivi, hilo asahau..kama ni yeye alinifanya hivi basi ashukuru sikuwa na akili zangu timamu…’nikasema na yeye akanitupia jicho mara moja.

'Sawa, labda eeh, najua yeye hajui lolote, mfano napo ingelitokea ni kwa kijana wangu, maana hapo unasema hutamkubalia mume wangu kwa vile ni mzee, ni mkubwa wako, mfano sasa ikatokea kuwa kijana wangu anahusika, kama alivyosema huyo mdada rafiki yako…?’ akaniuliza.

‘Nikuulize na wewe hilo swali , kama ikitokea hivyo, wewe utamkubalia mtoto wako anioe mimi…?’ nikamuuliza na yeye akakaa kimia kwa muda, mpaka nikajua hataongea tena, lakini baaadae akasema;

‘Siwezi kukubali kamwe,..hilo sahau…’akasema.

'Kwasababu gan, kwa vile mimi ni masikini au kuna sababu gani nyingine na hata kama mtoto wako kanipenda mimi..?’ nikamuuliza.

'Hebu wewe jiweke kwenye nafasi yangu, naona wewe una hekima sana, basi jaribu kujiweka wewe ndio mimi, je ungelikubali hilo litendeke…?’ akaniuliza.

'Kama ingelikuwa mimi ndio wewe, kwa kutoka moyoni mwangu, na uelewa wangu mdogo, mimi ningelikubali tu, kwasaabbu gani, ili masikini waweze kusaidiwa, matajiri wawaoe masikini na waolewe na masikini ili kusaidia kuwawezeshana, ili jamii ya kimasikini ipungue..na kuwe na usawa, kusiwe na kudharauliana…’nikasema na hapo akatulia kwa muda tena, halafu akasema;

'Kwahiyo hilo ndilo lengo lako…?’ akaniuliza na mimi kwanza nikabakia kimia nikiwaza kwanini nimesema hivyo, sikujua yeye atalichukulia hivyo, na sikusema hivyo nikimaanisha hivyo, baadae nikasema;

'Hapana mimi hilo sio lengo langu kabisa, tumeongea kama ingelikuwa hivyo, na sizani kama ndio hivyo, na hata kama itakuwa hivyo bado mimi sitakubali kwa maana kuwa nitakuwa nimejirahisisha kwasababu ya mali, na matokea yake nitakuwa mtumwa wa watu wengine…’nikasema

‘Haa..haya ngoja tuone maana tunakaribia hospitalini, mimi hapa nilipo hasira zinanizidi kiasi jinsi gani nikikutana na huyo mtu nitakavyofanya, sijui…huyo mtu kaniharibia maisha yangu na familia yangu…huyo mtu kaniweka kwenye wakati mgumu…na kama kweli aliwahi kuingia ndani kwangu na kufanya hivyo…nina ushahidi, lakini hauna mshiko,…’akasema

‘Una ushahidi gani, kama unao kwanini usiende polisi…?’ nikauliza

‘Ushahidi una utata, utaniumiza badala ya kusaidia, ..ngoja tukutane na huyo mtu, nitajua la kufanya huko tukifiika, ..nikipata mwanya tu, nitakachokifanya watu hawataamini…’akasema

‘Upo kama mimi madamu…’nikasema na tukawa tumeshafika

*************

Huku kwa upande mwingine mdada alipanda gari la madamu wake, na waliendelea kukaa hivyo hivyo kimia hadi walipokaribia kufika, na madam akasema;

‘Unajua tangia ulipofika kwangu nilikuwa nahisi mwili ukinisisimuka, unajua wewe uliletwa kwangu bila hata ya mimi kupata muda wa kukuchunguza, na hasa ulipofika na kuanza kuongea mambo ya kishirikina, nilianza kukuhisi vibaya…’akasema.

‘Lakini mimi sio mshirikina…’akasema mdada.

‘Unajua maana ushirikina,..ni kuamini mambo bila kupitia kwa mola wako, unakwenda kwa mwanadamu mwenzako ati akupigie ramli, unaamini mambo yatatokea hivi kwa sababu hii, badala ya kuamini kuwa mambo yanayotokea ni kwa matakwa ya mungu…’akasema.

‘Kwahiyo hata ukiibiwa,eeh, hata…au ndio hata mume wako akifanya mambo usiyoyataka, au kama ilivyotokea huko kwa huyo mwenzangu, kwani hajui kabisa kilichotokea, hayo tuamini tu kuwa ni mungu kapenda, tusihangaike …si ndio hivyo..tatizo sis hatujasoma, na ..ndio hivyo madamu…’akasema.

‘Ndio hivyo nini…sikiliza kusoma au kutokusoma hakukuruhusu wewe kujiingiza kwenye mambo ya nguvu za giza, unajua ramli, au kuamini mambo ya uchawi ukayafuta, ukayaamini, ni ushirikina, hata bila kusoma utaelewa hivyo tu..’akasema

‘Mimi niliamua kwenda hivyo baada ya kukutwa na matatizo, nikahangaika hospitalini bila mafanikio, naota ndoto mbaya..nahisi kuna watu wana…nikaba, wananidhalilisha, sasa kwa hilo kama hiyo ukiongea hospitalini watakusaidia nini…ndio maana nikapata ushauri niende kuhangaika, na ndio nikamgundua mbaya wangu…’akasema

‘Huyo mchawi ndio mbaya wako, kwahiyo ulimgundua kwa kupitia kwa hao waganga wa kienyeji au..?’ akauliza

‘Yule sio …ni mtaalamu, anakuangalai hivi tu, anaanza kukuambia matatizo yako..na anakuambia mambo mengo ambayo ni kweli yapo , yamekutokea, ..sijaona akipiga ramli,…’akasema

‘Ulikwenda huko lini..?’ akauliza na mdada akajua ni swali la mtego akasema;

‘Kabla sijaja kwako…’akasema

‘Na hujawahi kwenda huko tena..?’ akauliza

‘Sijawahi, maana sina pesa za kumlipa hata deni la kwanza sijamaliza…’akasema

‘Mfano sasa tukifika kwa huyo mtu wako utafanyaje, maana ndio hivyo kasema usipomsaidia pesa za matibabu hataondoa, nini vile kitu gani..zandi…..’akashindwa kutaja

‘Mazindiko…’akamalizia mdada

‘Ehh, hayo wanayawekaje..?’ akauliza

‘Mimi sijui ..wanawekaje…’akasema

‘Kwahiyo anakuona kila unachokifanya..?’ akauliza

‘Ni kitu kama hicho…’akasema

‘Nitamuua huyo mtu, ina maana atakuwa anatuona hata tukiwa uchi..?’ akauliza

‘Kama anaweza kufika usiku bila yaw ewe kukuona akakuchukua, akakufanya atakavyo, unahisi hawezi kukuona kwa kila ukifanyacho…’akasema mdada

‘Weee, anaweza kufanya hivyo, sio kweli, na wala siamini, unasikia hayo mambo ni uwongo, na kama yapo labda uwekwe vifaa vya kitaalamu, huyo kakudanganya, sikiliza mume wangu ni askari, ana cheo kikubwa tu, atamtesa mpaak atasema kila kitu..hata hivyo sizani kama nitasubira mume wangu aje, …nitajua cha kumfanya, watu kama hao hawastahiki kuishi, unasikia,…yaani umenifanya nihisi vibaya sana. Maana anaweza kuwafanya vibaya watoto wangu, na juzi niliota ndoto mbaya sana,…nilimuona,..na wewe, …’akasema akimuangalia mdada kwa macho makali

‘Na mimi..” akauliza

‘Ok tumefika…ila kiukweli naanza kuhisi kuna ukweli fulani, ngoja nifike nimuone kama ndio yeye, atanitambua…mtanieleza mlichokuwa mkikifanya…’akasema sasa kwa sauti yenye hisia za chuki.

‘Uliniona na mimi, mungu wangu, uliota, anakufanya nini, na mimi nafanya nini…?’akauliza mdada kwa shauku, lakini akionyesha wasiwasi, lakini huyo mama hakujibu na gari likawa limefika hospitalini.

NB: Naishia hapa kwa leo..


WAZO LA LEO:  Hakika dhana mbaya ni madhambi katika madhambi makubwa, dhana mbaya humsukuma mtu kujenga chuki na kuleta uadui kwa wenzake, sio vizuri kushutumu, kusakama, au kuchukua hatua kwa kutegemea dhana tu, kwani  hebu jiulize hapo, kama hiyo dhana sio kweli, kiasi gani huyo mtu au kundi la watu waliodhaniwa hivyo walivyumia, je hayo maumivi unaweza kuyalipa. 

Dunia sasa hivi imegubikwa na tabia hiyo, watu kudhaniana ubaya, kwa malengo ya kujenga fitina, watu wanakosana, mataifa yanapigana, damu zinamwagika, wasio na hatia wanapata taabu, je hi dhuluma hatuioni ilivyo mbaya. Tumuombe mola wetu atuongeze kwenye njia sahihi, na ubaya uwe dhahiri ili watu wasiingie kwenye dhana mbaya, na ikiwezekana ubaya huo upotee, na wenye kutenda hayo watubu, na kukiri,na kujirudi… ili dunia iwe salama na haki.

Ni mimi: emu-three

No comments :