Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, July 13, 2017

DUWA LA KUKU....11


‘Najua mumekusanyika hapa kuhusu yanayotokea humu ndani, najua nyote mtakuwa mumeninyoshea kidole mimi, kutokana na tuhuma za huyo mtoto wenu kuwa mimi ni …mchawi au namini ushirikina, najua kuna mengo mnataka kusikia kutoka kwangu…’akaanza kuongea huyo binti.

‘Tunachokitaka kutoka kwako ni ukweli, je hayo yanayosemwa ni kweli…?’ akaulizwa

‘Yapi hayo....kuwa mimi ni mshirikina, kuwa labda nimemfanyia kitu mtu humu ndani, au si ndio hivyo,..?’ akauliza.

‘Hapana sisi hatuna maana hiyo, labda utulie tukuulize maswali utujibu kwa ukweli unavyoujua wewe…’akaambiwa.

‘Mimi nimekuja kuusema ukweli... ili niwahi kazini kwangu, najua labda itakuwa ni hatari kwangu, lakini sina jinsi, kutokana na wema niliotendewa na hawa watu,...na.. labda nikiri kuwa kweli haya yanayotokea humu chanzo ni mimi…’akasema na watu wakamkodolea macho.

‘Tuelezee kwa vipi?

‘Ehee….ngoja nianze tokea awali ili mnielewe vyema japokuwa naogopa nitachelewa huko kwa mabosi zangu….’akasema.

‘Sawa endelea, kwa haraka kidogo, ili usichelewe….’akaambiwa.

‘Mimi nilifika kwenye nyumba hii, nikitokea mitaani,..' akaanza hivyo.

'Huyu baba, ndiye alinikuta siku moja nikiwa na hali mbaya sana, nina njaa, naumwa, akanionea huruma, bada ya kunihoji hoji, …akaninunulia chakula na kunipeleka hospitalini. Huko nikalazwa,…nililazwa wiki hivi, na yeye alikuwa akija kunijilia hali na hata kuniletea chahakula…kiukweli niingiwa na faraja, na badala ya kufurahi nikawa nalia…’akatulia kidogo.

‘Kwanini sasa ulie..wakati mtu kajitolea kukusaidia…?’ akaulizwa.

‘Unajua huwezi kuelewa haya mpaka yakukute, nililia kwasababu nilijiuliza hivi sisi tulikosa nini, …ina maana na mimi nilitakiwa niwe na baba kama huyu, je yupo wapi huyo baba yangu, haya mama alifariki, lakini …..aah, sitaki nikumbuke, nililia kwakweli, na…namshukuru mungu…japokuwa sikuelelewa kwenye mazingira ya dini, lakini najua mungu yupo….’akatulia.

‘Ehe ikawaje…?’ akaulizwa.

‘Baada ya wiki hivi nikaambiwa nimepona, hapo nilitamani niwadanganye pale hospitalini kuwa sijapona ili niendelee kubakia hapo, ili niweze kupata chakula cha kupikwa sio cha kuokota majalalani…ili nilale kitandani, sio kulala kwenye maboksi, huku mbu ndio marafiki zako…ili..jamani msiombee maisha haya, nyie mliojaliwa kuwa na wazazi, mshukuru sana….’hapo akageuka kuangalia huku na kule kama anamtafuta mtu, na watu walibakia kimia.

‘Je utakwenda wapi ukitoka hapa..?’ akaniuliza huyu mfadhili wangu, alipofika na kusikia kuwa natakiwa kuruhusiwa nimeshapona.

‘Mimi sijui pa kwenda, sina wazazi, sina ndugu, …nyumbani kwangu ni mitaani tu…’nikasema na huyu mfadhili akaniangalia kwa jicho la huruma akasema;

‘Oh,… basi ngoja nitaongea na mke wangu tutaona jinsi gani ya kukusaidia…’akasema na aliondoka siku hiyo, akijua nitaruhusiwa, lakini nahisi alishindwa kunichukua moja kwa moja mpaka akaongee na mke wake…mimi nilibakia pale nikisubiria taratibu za hospitalini, ili niweze kuondoka na kurejea mitaani, na haikupita muda docta akaja akaniambia nipo huru kuondoka.

‘Nikiwa nimekata tamaa,…nikijua sasa ndio maisha yangu tena yameanza, mara nikaona gari likija, muda huo nimeshatoka nipo nje, napiga plani za wapi nianzie maana maisha yetu ilikuwa kuomba omba, …kutukunwa, na usiku ku…zalilishwa, tulishazoea hivyo.

Gari likasimama, kumbe ni huyu baba wa watu, sasa alikuwa kaja na mke wake, wakaniuliza nimeambiwaje, nikawaambia, wao wakaenda kuongea na docta, kuona kuwa kila kitu kipo sawa, kama kuna dawa, au gharama yoyote, walipomalizana huko, wakaniambia niingie kwenye gari.

Basi ndio wakanichukua kwenye gari lao hadi nyumbani kwao, ndio nikanza maisha ya kuishi kwenye nyumba, sisi makazi yetu yalikuwa mitaani, vichochoroni,…..mara ya kwanza naingia kwenye nyumba nzuri, bila kutukunwa, kwa kukaribishwa na kuulizwa nitakula nini..kwanini machozi yasinitoke, nililia sana..nililia mpaka wenyeji wangu wakashangaa, wakaniuliza nalilia nini tena.., na mimi niliwajibu tu;

‘Nyie acheni tu…nalia, nimemkumbuka mama yangu, ….’nilisema hivyo, wakajua ni hivyo, lakini sikuwa nalia kwasababu hiyo tu, nilikuwa nalia, nikijiuliza maswali mengi,…na sikuamini kuwa hata siku moja nitakuja kupata fadhila kama hizo, mungu awazidishie watu kama hawa wenye moyo wa upendo….’akasema na aliyeitikia amina alikuwa kiongozi wa dini.

‘Kiukweli nilifika kwa watu hawa nikiwa sina mbele wala nyuma, nilifika hapa mchafu sijui hata kuoga, nikaambiwa nikaoge, nikapewa nguo za kubadilisha,..nikafundishwa mambo mengi tu ya maisha,…japokuwa kiukweli mimi sio mvivu, kazi za ndani, kuosha vyombo kufagia, nilifundishwa na mama yangu, navijua sana, lakini yale maisha ya watu wenye uwezo, umeme…na vitu vya kisasa, nilikuwa sijui kuvitumia.

Kwa haraka sana nikazoea maisha hayo mazuri, na unajua tena, ukitoka kwenye shida ukapata raha, mwili hubadilika kwa haraka sana…nikawa binti mrembo, watu , hasa wanaume wakawa wakiniangalia kwa macho ya tamaa,…sisemi haya nia mbaya, lakini ndivyo ilivyokuwa, hata wafadhili wangu waliniambia hivyo, kuwa mimi ni binti mrembo sana…mimi sijui…’akatulia.

Kuna kipindi niliona mabadiliko kwa wafadhili wangu hasa kijana..hahaha, hivi yupo wapi, samahani kwa hilo, ila inabidi niseme tu, nilivyoona mimi, labda nimekosea lakini ndivyo ilivyokuwa, sio kama ilivyokuwa awali, nikaona macho ya aina yake, kwangu mimi niligundua ni macho ya namna gani,…maana mitaani, na maisha niliyoishi nilijifunza mambo mengi bado nikiwa na umri mdogo….’akatulia.

‘Ningelipenda huyu kijana wa humu ndani awepo ili nisije kuonekana mimi ni muongo maana mengi anayafahamu na aje kuyathibitisha haya nitakayoyasema, na ili baadae litakolotokea, maana ndicho kilichonisukuma hadi kuja hapa,…ili nisije kulaumiwa…’akasema.

 ‘Ehee, hebu muiteni huyo kijana…una maana huyu kijana wa humu ndani…?’ akaulizwa.

‘Ndio namuita kijana japokuwa kwa umri tupo sawa, tulizoea kumuita hivyo …’akasema huyo binti, na Kijana akaitwa, na huyo kijana alipoingia tu na kumuona huyo binti, akashikwa na mshtuko kidogo, halafu akasema.

‘Huyu mdada msimuamini kabisa, huyu mshikirina huyu…atawadanganya na kubadili badili maneno, mimi simuamini kamwe…’akasema huyo kijana.

‘Ndio maana nimekuja unionyeshe huo ushirikina wangu, hiyo kauli yako mimi siipendi, nakuambia kabisa……na nitaongea ukweli wote leo, …uukane sasa, hata yale uliyosema nisiseme nitasema yote,….mimi sio mshirikina kama unavyohisi wewe…,na kama unadai kuwa mimi ni mshirikina nataka unionyeshe huo ushirikina wangu la sivyo tutafikisha kubaya….’akasema huyo binti.

‘Aaah, wewe tulia, hayo hayana nafasi hapa endelea kuelezea historia yako ya kuishi humu ndani, ilitokea nini, unasema ulipoanza kupendeza kijana akaanza kukutamani, kwani humu ndani alikuwepo kijana peke yake wa kukutamani,  hebu tuambie hapo una maana gani…?’ akaulizwa.

‘Ni kweli, kwasababu kijana ndiye tulikuwa naye wakati mwingi, wengine walikuwa wakija na kuondoka, na hata baba alikuwa anaonekana usiku tu na siku za wikiendi, kwahiyo mtu niliyekuwa naye karibu alikuwa huyu kijana…kwani nadanganya, aseme yeye mwenyewe, huyu kijana maana yeye ndiye aliyenianza kunitongoza, nikamkatalia, akaanza kunifanyia vitimbwi, aseme ukweli…’akasema

Kijana akawa kimia tu, hakusemi neno hapo, ila mama yake aliniangalia kwa macho ya hasira, akitaka kusema neno, lakini mdada huyo hakumpa nafasi akaendelea kuongea.
.
‘Kijana huyu akaanza kunisemea kwa wazazi wake kuwa mimi usiku natoka kwenda kufanya uhawara, au huo ushirikina anaousema,..wakati hata siku moja sijawahi kufanya hivyo, kisa nimemkatalia.., …kwanini niende nje wakati wanaume wapo humu ndani,…eti, tena wenye pesa, lakini nikavumilia, na siku moja kijana akaanza visa vyake, muulizeni alinifanyia nini…’akasema.

‘Wewe elezea, alikufanyia nini…?’ akaulizwa

‘Alitaka kunibaka, nikapiga ukelele…’akasema

‘Mwongo huyu, …ananisingizia, hata siku moja sijawahi kufanya hivyo, yeye usiku alikuwa akifanya madawa yake, nikamfuma, akiwa nje uchi…si umetaka niseme ….na…siku anayosema nilitaka kumbaka alikuwa akipiga kelele, nikawa namshika, maana alikwua akigonga gonga,…’akasema kijana.

‘Hahaha…eti nikiwa nje uchi, wakati ni mambo yenu humu ndani,…. ndio yalinifanya nitoke nje, nikiwa sijitambui,…nimejikuta niko nje uchi,….na kama ningeliendelea kubakia humu , bila ya kwenda kuhangaikiwa sijui ingelikuwaje,…labda ningekuwa kichaa...kuna kitu kilikuwa kikiniingia kichwani nakuwa kama nimechanganyikiwa, navutwa kufanya mambo nisiyoweza kuyafanya nikiwa na akili zangu, nilikuwa sio mimi…’akasema.

‘Oh, kwahiyo…sio huyu kijana ni kitu kingine kilitokea kwako, ?’ akaulizwa.

‘Huyu kijana ana yake, lakini kiukweli mimi niliambiwa matatizo hayo yametoka huko kwetu, kuna watu wananitaka nirudi nyumbani…nikaolewe huko, kuna mjamaa mmoja anaogopewa sana huko, eti aliniona akanipenda, kipindi fulani nilikwenda huko, …wakati nimeshapendeza, nilipata ruhusa , na kwenda kuona asili yetu, nikiwa na rafiki yangu mmoja wa kutokea huko kijijini walipotokea wazazi wangu...’akatulia.

‘Akamuambia huyu rafiki yangu aniambie kuwa yeye anataka kunioa, mimi nikamkatalia, kwanza nilikuwa mdogo, japokuwa umbo langu, lipo hivi, naonekana mkubwa lakini sio sawa na umri wangu…’hapoa akatulia kwa muda kidogo.

‘Sasa ikawaje, ?’ akaulizwa.

‘Nilimkataa, na ndipo akasema atanikomoa…na huyo rafiki yangu alinisihi nikubali, kwani nispokubali, huyo mtu anaweza kunifanyia vituko…mimi nikamwambia sitaki, na huko sitarudi tena, bai huyo jamaa akamwambia huyo rafiki yangu, atanifanyia mambo mpaka nitakubali, na huko ninapoishi wote watakoma ubishi, mpaka wanifukuze.

‘Mimi …nilikuja nikawaambia humu ndani, ndio wakaanza kuniita mimi mshirikina, hasa huyu kijana, mama aliniambia kama nina tabia hiyo ya kishirikina niache kabisa, lakini ujumbe niliufikisha…’akasema.

‘Kwahiyo ulimwambia mama kuhusu huyu mzee….?’ akaulizwa.

‘Kwanza nilimuambia huyu kijana maana ndiye nilikuwa karibu naye…’akasema

‘Kwanini ulikuwa karibu naye..?’ akaulizwa.

‘Nilianza kusema awali, kuwa nilianza kupendeza, na huyu kijana akawa aknitongoza, kila siku, kiukweli kama …isingelikuwa ni tofauti za hali, ningelisema nikubali, si nitaolewa kwenye nyumba ya watu wanaojiweza, lakini nafsi ilinisuta, nikamkatalai kata kata…sasa nilipopata taarifa hiyo ya huyo mzee, nikamwambia kijana.

‘Umenikataa mimi, sasa nenda kaolewa na wazee wa kijijini….’akaniambia.

‘Mimi siwezi kuolewa huko, na wala sitaki kuolewa,…’nikamwambia.

‘Ila kuna kitu nataka umwambie mama, huyo jamaa kasema nisipokubali kuolewa na yeye atanifanyaia kitu kibaya, na hata nyumba hii mtafanyiwa hivyo hivyo…’nilimuambia hivyo, na yeye akasema, huyo mzee hawezi, hayo ni mambo ya kishirikina, na neno hilo lilianzia hapo.

‘Na haikupita muda, huyo jamaa akanitembea usiku, nikiwa usingizini sijijui…’akasema.

‘Una maana gani hapo, kukutembea usiku, kwa vipi..?’ akaulizwa.

‘Kutokana na nilivyoambiwa, huyu jamaa ni mchawi, huko kijijini wanamfahamu sana, na akitaka jambo lake ni lazima alipate, kwahiyo alivyonitaka mimi na kukataa, ndio akawa anakuja usiku, humu ndani…’akatulia.

‘Unamuona..?’ akaulizwa.

‘Siku ya kwanza nilimuona, …lakini ni kama njozi, na akaniambia ..sasa nimekuja, wewe si hunitaki, sasa nitakufanyia mambo mabaya, mpaka ujute kuzaliwa….nikawa sijui nifanyeje, na akasema, yeye, nia yake ni kunioa, ila kwa vile sitaki, basi atawatumia watu wa humu ndani kunizalilisha….’akatulia.

‘Watu gani…?’ akaulizwa.

‘Baba na kijana…’akasema na watu hapo wakahema.

‘Ni kweli alifanya hivyo…?’ akaulizwa.

‘Hahaha, hivi hamuamini hayo…muulizeni mama aliona nini, aliniambia alimuona baba akija chumbani kwangu, mimi nilimkatalia kwasababu yaliyokuja kutokea baadae, mimi nilikuwa sioni, nakuwa kama nipo kwenye njozi,…siwezi kufanya lolote zaidi ya ufanyiwa hayo anayoyataka huyo mzee….’akasema.

‘Lakini uliambiwa, hujawahi kuona kwa macho yako…?’ akaulizwa.

‘Kiukweli hivyo vitendo, nafanyiwa, ila wanaonifanyia siwaoni, maana ninakuwa usingizini…’akasema.

‘Na sikuyajua hayo, mpaka nilipokuja kuambiwa…ila siku ya kwanza huyo mzee nilimuona kwenye njozi zangu, akiniambia kuwa atakuwa anakuja kila siku kunifanyia vitendo vibaya, na atawatumia watu wa humu ndani, kunizalilisha, huku yeye akiniangalia, na kunikaba….’akasema.

‘Kwahiyo ni kweli kuwa baba mwenye nyumba na kijana huwa wanakuja usiku na kukufanyia hivyo, bila hata yaw ewe kujua, …kuwaona..kujua unajua kwa vile uliambiwa, sio ila wanapokuja huwaoni kwa sura si ndio hivyo..?’ akaulizwa.

‘Ndio wanakuja, muulizeni hata mama aliwahi kwuafuatilia akawaona, anasema ana ushahidi wa kuonyesha hayo, mimi kiukweli sijawahi kuwaona ila nakabwa, ..na kuhisi nazalilishwa, na watu nikiwa kwenye ndoto..ni kama ndoto…’akasema

 ‘Unasema nini wewe…?’ aliyeuliza sasa ni baba mwenye nyumba.

‘Nasema nilivyoambiwa, na yanayonikuta,…huyo jamaa lengo lake ni kunikomoa, unielewe hapa, ndio maana nimesema sasa nataka kuufichua ukweli, sasa iwe ni kazi kwenu…kama mtahangaika sawa, kama mtakaa kimia sawa, ila kama msipohangaika ndoa yenu itakuwa matatani, ndivyo alivyoahidi kwani alitaka kunioa na nyie mlinishauri nikatae…’akasema.

‘Kwani wewe ulimwambi ahivyo, kuwa umeshauriwa na wafadhili wako usikubali....?' akaulizwa

'Hata, sijaongea naye, unajua yeye mara nyingi alikuwa akiongea na huyo rafiki yangu sio mimi, sasa sijui alifahamuje hivyo...siwezi kujua,...'akasema

'Kwahiyo kwa kifupi, haya yote yanayotokea humu ndani kumbe kisa ni wewe?’ akulizwa.

‘Kisa ni mimi ndio, kama nilivyoambiwa,….ndio maana nimekuja kuwaambia, ili isje kujulikana baadae mkaniona mimi ni mbaya, au kama anavyoniita huyo kijana kuwa mimi ni mshirikina,…na nilimuambia mama, yeye hakuniamini, na wakafanya mbinu niondoke humu, wakijua nikiondoka huenda mambo hayo yataisha,… lakini huyu mtu alishasema atawakomoa na nyie mlionishauri nisiolewe na yeye…’akasema.

‘Sasa hebu tueleze inakuwaje, yaani huyu jamaa si anaishi huko kwenu mbali kabisa anawezaje kufika huku usiku, na anawezaje kumchukua huyu baba mwenye nyumba atoke naye waingie kwako na kuanza kukusumbua, si ndio hivyo, yeye anasafiri na nini hadi huku..?’ akaulizwa.

‘Ina maana hamuamini hayo mambo, mimi pia nilikuwa siamini, lakini anakuja kweli, ananifanyia hayo wanayofanya, na je kweli mama hajawahi kumuona baba akiingia chumbani kwangu susiku….?’ Akauliza akimuangalia mama.

‘Wewe ndio utuambie…’akaambiwa.

‘Huyu jamaa ana njia zake za kusafiri , niliambiwa anasafiri kwa njia za kichawi, usiku, na kila mara anafika hapa,…sasa anasafirije mimi sijui,….’akatulia.

‘Na eti wewe mdada, haya mambo hayayajakutokea na wewe…maana alisema na yoyote atakayeingia humu naye atakumbana na matatizo hayo, na hasa baada ya mimi kutibiwa nasikia alisema keshapata badili yangu, ..lakini hao watu waliosababisha yote hayo, ataendelea kuwasumbua mpaka wakome ubishi…’akasema.

‘Haya hebu tuambie ukweli, katika siku zote ina maana hukuwahi kumuona baba mwenye nyumba akiingia chumbani kwako usiku,..?’ akaulizwa.

‘Tatizo ni kuwa huyo jamaa, anapokuja nyumbani kwako, wewe mlengwa huwezi kumuona labda uwe umezindikwa,..au una imani safi ya dini, wapo wenye imani za dini mungu anawalinda, hawezi kufanyiwa mambo hayo, lakini wengi wetu imani zetu ni haba, kama mimi sikuwahi kufundishwa dini, nikamjua mungu, nikajua kujilinda kwa kupita kwa mwenyezimungu….’akasema.

‘Sasa akija anaingia ndani, sote tumelala, hakuna anayweza kumuona, na wanafanya mambo yao, unachohisi ni kama kukabwa, maana wanakuzuia usije kuzindukana,..na wakimaliza kazi yao wanaondoka huku nyuma ukizindukana usingizi unahisi athari hizo,…alinifanyia hivyo, lakini kwa kupitia kwa baba mwenye nyumba na kijana wake…’akasema.

‘Hatujakuelewa hapo…’akaambiwa.

‘Ni hivi nia yake ni kunikomoa mimi…, kwahiyo anachofanya akija, anawavuta wawili hao wakiwa usingizini, wanakuja kwangu, wananizalilisha, huku yeye akiniangalia na kunikebehi,…’akasema.

‘Sasa akifanya hivyo, wewe huoni, na wala hujui, huwaoni hao wanaokufanyia hivyo, sasa yeye anapata  faida gani..?

‘Si ndio hivyo,…mimi silali kwa raha, nahsi nakabwa, ni yeye ananikaba,…huku hao wawili wananizalilisha, yeye anafurahia hivyo,…mimi naona kama hamuniamini, sasa ni hivi mkitaka muamini kama hamtaki shauri lenu, mimi naondoka…’akasema.

‘Ngoja kwanza..’akasema kiongozi wa dini pale huyo msichana alipotaka kuondoka.

‘Ningoje nini tena hapa,  huo ndio ukweli wenyewe hangaikeni …’akasema.

‘Nasikia wewe uliwahi kupata mimba, ni kweli si kweli..?’ akaulizwa.

‘Ndio nina mimba mpaka sasa, ila yeye alinifanya nisiione hiyo mimba, nikaenda kuangaikiwa, nikapona na huyo mzee akasalimu amri baada ya mimi kuhangaikiwa, na akaja kuniachia, sasa yupo kwa wengine sio mimi tena, labda kwa huyu mdada hapa, kama haamini basi,…ila mimba nilikuwa nayo ikapotea, ….’akasema.

‘Kwa vipi? Akaulizwa.

‘Nilitaka kuitoa, kwasababu nilimbiwa nitazaa kioja sio mtoto kamili anaweza akawa shetani, huyo mzee kaniwekezea shetani tumboni…, ndio nikaona niwaambie hapa wanisaidie tuitoe, tukaitoa, kumbe yote ilikuwa kiini macho tu, ikaonekana nimeharibu hata kizazi, kumbe ni huyo mzee ananichezea, hata hospitalini waliona kizazi kimeharibika, lakini wiki iliyopita baada ya kutibiwa, nimeenda kupimwa , tatizo hilo halipo tena,…’akatulia.

‘Kwahiyo bado una mimba?’ akaulizwa.

‘Ndivyo walivyosema hospitalini kuwa bado nina mimba, haikutoka…’akasema.

‘Sasa mimba hiyo mimba ni ya nani..?’ akaulizwa.

‘Hapo mimi sijui…’akasema.

‘Kwa vipi, maana kama ni hiyo ya awali ilitoka sasa hiyo uliyo nayo, utakuwa umeipatia wapi..?’
‘Nasema mimi sijui tusubirie nizae, kiumbe kikitoka tutakipima na ukweli utajulikana ni mimba ya nani…na safari hii siitoi, …sitaki kuja kuharibu kizazi changu….’akasema.

‘Hebu kwanza naona unataka kuharibu ukweli, nataka unijibu kwa uwazi,..je mume wangu aliwahi kuingia ndani kwako mkafanya uchafu wenu..?’ aliyeuliza hivyo ni mama mwenye nyumba.

‘Mimi sikuwahi kumuona, unielewe hapo, nilikuja kuambiwa kuwa wawili hao, wanakuja kwangu, kwa kuongozwa na huyo mzee, wakiwa hawajijui, na kunifanya wanachoamrishwa kukifanya, sasa kama waliingia , hawakuingia, mimi sijui, niliambiwa hivyo, kama huamini shauri lako….’akasema.

‘Usitake kunitania wewe,  sema ukweli wako, kwanza umeanza kusema mume wangu na kijana walianza kukutamani, hiyo kauli inaashiria kuwa wewe ulikuwa na njama nao, sasa nataka useme ukweli la sivyo, nitakuitia polisi kuwa wewe unakuja kwenye majumba ya watu na kuharibu ndoa za watu..’aliyesema hivyo ni mama mwenye nyumba.

‘Waite hapo polisi,..nenda kawaita na mimi nitawaambi ahuo ukweli wote,… kama wataweza kukusaidia haya,….hivi mimi kuamua kuwaambia huu ukweli ndio nimekuwa mbaya, sawa, waite nikafungwe, nyie si mna pesa zenu, ila nazidi kuwatahadharisha, humu ndani hakuna usalama, huyo mzee keshafanya humu ndani ndio makao yake …hangaikeni …’akasema sasa akitaka kuondoka.

‘Kijana wewe unasema ulimuona huyu mdada akifanya mambo ya kishirikina akiwa uchi, sawa si sawa ?’ akaulizwa kijana.

‘Ni kweli nilimuona usiku akiwa uchi,…na sio mara moja, aliniambia kuhusu huyu mjamaa huko kijijini, mimi sikuamini, na hilo la kuwa tunakwenda usiku kwake, niliona ni mambo ya kishirikina, ila, yalinipa mawazo sana, sikupenda kuwasumbua wazazi wangu…’akasema.

‘Ulipomuona ulifanya nini..?’ akaulizwa.

‘Nilishindwa kufanya lolote, nilitaka kupiga kelele au kumuendea lakini sikuweza kabisa, ilikuwa kama nimenatishwa,…’akasema.

‘Je wewe ulishawahi kuingia chumbani kwake usiku ?’ akaulizwa.

‘Ndio, nilitaka kuhakikisha kuwa kweli huyo mtu ni mshirikina au la…na siku zote nilipoingia nilimkuta ndani kalala…’akasema.

‘Ila uliwahi kumuona nje, akiwa uchi..?’ akaulizwa.

‘Ndio..?’

‘Alikuwa akifanya nini..?’akaulizwa.

‘Kasimama tu, au kachuchumaa, au anatembea tembea, ni kama anasubiria kitu…lakini sikuweza kufanya lolote, maana nilikwua kama nimegandishwa….’akasema.

‘Oh…sasa hili ni tatizo…’akasema mzee mmojawapo.

‘Wazee, huyu binti ni muongo, nahisi kuna kitu anatuficha….’akasema mama mwenye nyumba.

‘Kama ni muongo, au ni mkweli, sisi tutakuja kumjua tu,….watu kama hawa hawawezi kushindana na mungu, sisi hatutakwenda huko kwa waganga wa kienyeji, sis tunafanya yetu kwa kumtegemea mungu, na yote haya yatakwisha…ila tunachotaka ni nyie wawili mkubaliane, muwe kitu kimoja, maana shetani lengo lake ni kuharibu ndoa za watu, na ndio matokea yake haya, niliwaambi awali kuna kitu nimegundua, sasa kimejitokeza, na haya yataisha kama mtaungana na kuelekeza nguvu zenu kwenye imani ya kweli…’akasema kiongozi wa dini.

‘Sasa mimi nakwenda…’akasema huyo binti.

‘Sawa unaweza kuondoka, ila tutakihitajia tena,…’akaambiwa.

‘Hahaha, kama hamjaamini, subirini mtakachokiona huyo mzee akijua mumemfahamu atakuja kuwafanyia baya zaidi ya hilo…’akasema.

‘Atafanya nini acha kutisha watu hapa…’akasema kiongozi wa dini.

‘Sawa mimi nawatisha,..lakini jiulizeni mangapi yamefanyika humu ndani na hamkuweza kuyazuia…jamaa huyo alikuwa anakuja kwangu usiku, wewe mama uliweza kumzuia…hujaweza kumzuia,…na nani anapata shida, ndio mimi nimepata shida, lakini hata nyie, …..mimi nimejitolea kuja kuusema ukweli kwa vile mumenisaidia sana…’akasema.

‘Ila tunakuonya kama wewe upo nyuma ya haya mambo utakuja kupata shida …’akaambiwa na hao wazee.

‘Wazee wangu, ..ndio maana nimekuja, nimeona nateseka kwa kuiweka hii siri moyoni mwangu, hawa watu walinipokea wakanilea, wakanihifadhi, na haya yanatokea kwasababu yangu mimi, ..kwanini nikae kimia, hapana, ..mungu mwenyewe anajua ila nimetimiza wajibu wangu, sasa iliyobakia ipo mikononi mwenu kwaherini…..’akaaga, na alipofika mlangoni, akageuka na kusema

‘Na wewe binti mdada mwenzangu, uwe makini, kwani yaliyonipata mimi , huenda ndio hayo yanayokupata na wewe, siku ile nilikuona unalia, huenda hayo yameanza kwako, …sasa ni juu yako kuhangaika au kukaa kimia na kusema,..’mimi sijui….’haya endelea kutokujua, …kwaherini…’binti akasema na kuondoka.

NB Tuendee…. hapana tusubirie sehemu ijayo.


WAZO ZA LEO: Mwenyezimungu alitujua sisi wanadamu tulivyo, kuwa kuna wengine nafsini mwao ni zaidi ya mnyama, roho mbaya, na wengine wanyonge, ndio maana akatuambia vyovyote iwavyo, yeye yupo karibu nasi kuliko mshipa wa damu uliopo mwilini wetu, tumuombe yeye, tumtegemee yeye, lakini ukweli wa kumuamini, na sio kwa kinafiki au kwa kumshirikisha. Tumuombe mola wety atupe imani thabiti ya kumuamini yeye, na kumtegemea yeye..Aamin.
Ni mimi: emu-three

No comments :