Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, July 19, 2017

DUWA LA KUKU---15



‘Sasa hapo utaamua moja, mimi niondoke au huyo hawara wenu aondoke, kama ikigundulikana kama ninavyofikiria mimi, basi utachagua moja kati ya hayo mawili... unasikia, mzee wewe,...'ilikuwa kauli ya mama mwenyeji akimuambi mume wake kabla hatujafika hopsitalini.

 Tuendelee na kisa chetu..

                                                           ***********

Waliongea wenyewe huko bila kujua ni nini kimekubaliwa, ila subuhi ndio nikaambiwa nijiandae kwasababu nitakiwa kuepekwa hospitalini,…’nikaambiwa.

‘Na kule kwa wafadhili wako wa awali, wamepiga simu na kusema kuwa bado mambo hayajakaa sawa, kwahiyo wameomba niendelee kukaa na wewe hapa hadi muafaka utakapopatikana…’akasema mzee wa hapo

‘Lakini mimi siumwi kwasasa najisikia nafuu kwa sasa..na kwa vile zile dawa nilizopewa awali bado zipo, naona ni bora niendelee kuzitumia,, sioni ni kwanini twende huko hospitalini nikapewe madawa mengine zaidi…’nikasema.

‘Hapana inabidi tukupeleke ukachunguzwe vizuri afya yako, huenda kuna tatizo jingine limejificha, huko kuanguka-anguka sio kuzuri, unajua kizungu zungu, kinaweza kuwa ni sababu ya matatizo mengi, sasa ni tatizo gani, hatuwezi kulijua mpaka ukapimwe, …na vipimo ndio vitasema,…’akasema mzee.

‘Sawa, lakini mimi sikuona sababu ya kwenda huko, na mara nyingi mimi nikiumwa natumia dawa za miti shamba na zinanisaidia, hazi dawa za hospitalini zinaniongezea matatizo tu…mimi najua dawa zangu, kama tukienda kwa wauza madawa ya kienyeji nitawaonyesha…’nikasema

‘Hapana hayo matatizo, kama malaria, huenda una upungufu wa damu, au shinikizo la moyo, halihitajii madawa ya kienyeji, usiwe kama wazee, wao walifanya hivyo kwa vile hakukuwa na hospitali, au hospitali zipo mbali, hapa hospitali zipo….’akaambiwa

‘Sawa mimi nawasikiliza nyie, kama siwatii hasara, basi, mimi nipo tayari twendeni…’nikakubali tu kwa shingo upande.

Tuliondoka hapo nyumbani mimi na baba na mke wake,…namuita hivyo baba kama wenzangu walivyozoea kumuita,…na hatukuchelewa tukafika hospitalini, wao wakongea na docta na nikachukuliwa vipimo vya damu , choo na mkojo, na tukaambiwa tusubiria nje, na tulipokuwa tunasubiria mama akamuona rafiki yake mmojwa, wakawa wanaongea, na baadae wakasema wao wanakwenda kumuona mgonjwa aliyelazwa hapo, kama nikiitwa kabla hajarudi tuende mimi na baba, basi mimi nikabakia na huyo mzee tukisubiria majibu ya vipimo.

‘Usiwe na wasiwasi kabisa…, kama ulivyoniambia ni kweli, basi hakuna jambo la kuhofia…au sio, kama ni kweli lakini, nilikuambia awali, usinifiche kitu, nichukulie mimi kama baba yako,…unasikia,..na kuja kwtu hapa ni utaratbu wa kawaida tu wa kujirizisha, ni muhimu ukaijua afya yako, sawa, kwahiyo usiwe na mawazo na wasiwasi…’akasema.

‘Kwani mnataka kujua ni nini zaidi baba..kuwa labda nina..tatizo gani..?’ nikauliza

‘Hapana, sio kwamba tunahisi kuna tatizo kubwa,lakini ni vyema upimwe, hakitaharibika kitu ukipimwa, …’akasema

‘Sawa baba, basi Itakuwa vizuri, ili mjirizishe nafsi zenu, maana naona mna wasiwasi sana na mimi, na kiukweli hata mimi naona iwe hivyo, maana sijawahi kujisikia hivi kabla, ..’nikasema.

‘Umeona eeh, sasa vipimo ndivyo vitasema ukweli, …nikuulize tena,..umesema hujawahi kuwa na rafiki yoyote wa kiume, niambie ukweli, hili ni mimi na wewe, kama yupo wewe usiwe na wasiwasi na mimi nitajua jinsi gani ya kukulinda..?’ akaniuliza.

‘Sijawahi kuwa na rafiki yoyote wa kiume mzee wangu, niamini kweli kabisa, kama angelikuwepo ningelikuambia wewe nakuamini sasa kama baba yangu,…mimi sina tabia hiyo,  mama alinikataza kabisa alipokuwa hai, na siwezi kuvunja ahadi ya mama yangu..’nikajitetea.

‘Basi kama ni hivyo itakuwa vizuri sana, mimi nimemuambia mke wangu haina haja ya kuwa na wasiwasi, wewe ni binti mwema kabisa,nimechukua dhamana kwako, ..na nikuulize kitu kingine labda kuhusu zile ndoto, si ulisema hujaota tena, tangia uje hapa kwangu, au sio… je kule ulipokuwepo, una uhakika ilikuwa ni ndoto tu, maana hapa unatakiwa useme ukweli wote, docta takuuliza yote hayo, kama kutatokea tatizo lolote, japokuwa kama ulivyoniambia ni kweli hakuna tatizo,....’akasema huyo mzee.

‘Kweli kwa vipi baba…, ilikuwa ni ndoto tu, kama kuna jingine mimi sijui, na kwa vipi, kwani ndoto inaweza kuwa kweli baba, maana haya sasa yananitia mashaka..?’ nikauliza.

‘Unajua bint  nyie wanawake mna mitihani mingi, …sasa ukiwa msiri sana, unaweza ukaficha tatizo likaja kuwa kubwa,…mkiumwa maradhi kama hayo,…, kuna mambo mengi sisi kama wazazi tunayafikiria, lakini usijali, kipimo kitasema ukweli, nia ni kuondoa mashaka , hasa kwa mama yako, mimi nina imani hauna tatizo lolote jingine…’akasema.

‘Tatizo kama lipi, analonifikiria yeye, naona kanihoji maswala mengi akinihisi labda mimi ni wanaume, baba mimi sina tabia hiyo kabisa, na wala siyajui mambo hayo, sijui anataka kujua nini..?’ akaniuliza na mara tukaitwa, kuwa vipimo vipo tayari na mama mwenyenyumba alikuwa hajarudi,ikabidi tuingie na huyo mzee, na docta alipotuona tupo wawili , akamuuliza mzee.

‘Huyu ni nani wako?’ akauliza

‘Mimi ni baba yake mlezi….’akasema, sijui kwanini hakusema babu, lakini ndio hivyo, hata mimi nimezoea kumita baba
.
‘Je huyu binti ameolewa..?’ akauliza docta, hapo nikahisi mwili ukinisisimuka, maana haya maswali ya kuolewa, mchumba, mbona yanazidi kuwa mengi.

‘Bado hajaolewa, na wala hana hata mchumba, kwani kuna nini umegundua docta…?’akasema na kuuliza.

‘Je ana rafiki yoyote wa kiume…anayetambulikana..?’ akauliza na hapo mzee nikamuona sura ikimbadilika, na haraka akasema;

‘Hapana, hana, nimekuambia huyu binti hana rafiki wala mchumba, hana tabia hiyo kabisa…kama vipimo vyenu vinasema kweli hamtagundua jambo lolote la mahusiano…’akasema mzee na docta akaniangalia usoni, halafu akamgeukia mzee, na kusema;

‘Kwasababu hiyo mzee, mimi nakuomba utupe nafasi kidogo, nataka kuongea na huyu binti peke yake, tafadhali ….’akasema docta.

‘Lakini mimi ndio mlezi wake, nilitaka kufahamu ana tatizo gani, yeye kasema hana tatizo, …..ndio maana nikajitolea kumleta mimi na mke wangu, sasa ukisema unataka kuongea na yeye tu , basi tungelimuambia aje peke yake..’akasema mzee.

‘Sawa naelewa hilo…, lakini kuna mambo ya kitaalamu zaidi nataka kuongea na huyu binti akiwa peke yake, kuna maswali naweza kumuuliza akashindwa kuyajibu kwa vile wewe upo hapa….’akasema na mzee  akaelewa na kusimama ili atoke nje, nikamuona kama anasita sita, halafu akasema;

‘Basi ngoja nimuite mama yake aje… kama ni mambo ya akina mama zaidi…’akasema mzee akiharakisha kutoka nje.

‘Usijali mzee, haina haja kumita yeye,…, nitawaita wote nikimalizana na binti, ni bora niongee na yeye tu kwanza, sio tatizo kubwa..ni jambo jema tu, usiwe na wasiwasi mzee.’akasema na mzee akaondoka, na mlango ukafungwa.

***********
 .
Docta akasimama na kusindika mlango vizuri, mimi pale nikawa na wasiwasi, kukaa chumba na mwanaume halafu ndio kafunga mlango kabisa, moyo ukaanza kunienda mbio, najiuliza huyu mtu anataka kunifanya nini, nilishajipanga kupiga ukelele, kama lolote litatokea,…docta akahisi nina wasiwasi. Kwanza akarudi kwenye kiti chake na kukaa, halafu akaichukua ile karatasi ya vipimo, akawa kama anaisoma, halafu akasema;

‘Afya yako haina matatizo, huna maambukizi yoyote, ni uchafu kidogo tu kwenye mkojo, itabidi uendelee na hizo dawa ulizopewa awali, si bado unaendelea kuzitumia hizo..?’ akaniuliza, akiongea kwa lugha nyepesi kuniweka sawa.

‘Ndio bado naendelea kuzitumia, niliwaambia haina haja ya mimi kuja huku, lakini sijui wana wasiwasi gani…’nikasema.

‘Lakini hawajafanya vibaya, unajua ukipatwa na tatizo, hata kama huna tatizo ni vyema ukajenga tabia ya kuchunguza afya yako, yaonekana wazazi wako ni watu wema sana….’akasema

‘Nashukuru sana kwa kupata walezi kama hao….’nikasema

‘Mhh…unajua umri , ukienda, mwili nao unabadilika, na tabia ilivyo, kuna mambo yanakuja kujitokeza kwa kadri tunavyokuwa, hiyo ni kawaida,  kuna maswali machache nataka kukuuliza ili usije kupata matatizo kama hayo tena,…’akasema

‘Sawa niulize tu….’nikasema.

‘Mimi ni docta, na madocta ni wasiri wakubwa , kwa wagonjwa wao, usipomuamini docta basi wewe hutaki afya yako iwe njema, …nataka uniamini sawa, …’akasema

‘Sawa mimi nakuamini docta….’nikasema.

‘Niambie ukweli, unajua nilipokuwa shule, nilikuwa na rafiki wa siri, watu walikuwa hawalijui hilo, na wengi wanakuwa hivyo, na wakati mwingine kuna ule mchezo wa baba na mwana, tunajificha..na hata tunajikuta tunaanya mambo bila kutegemea…’akasema.

‘Mhh, mimi hata siku moja sijawahi kucheza hiyo michezo ya baba na mama…, docta maisha yangu na mama ni ya shida, sisi tulikuwa wakuhangaika barabarani kuomba, hatuna shamba, ni kibanda kidogo tu,hatuna jamaa , tulizaraulika....basi ni shdia, namshukuru mungu kuwa nimepata hawa wafadhili, na niliposikia kuwa mama kafariki, nilijua basi hata mimi nitakuja kumfuta tu…’nikasema.

‘Hapana wewe ni kijana na maisha yapo mbele yako, kamwe usikubali kushindwa, na matatizo iwe ni sehemu ya changamoto ya kupiga hatua mbele…, inatakiwa ufike mahali ujipange upate kitu cha kufanya ambacho kitakuingizia kipato, kama hivyo upo na walezi kama hao, wanakujali.. watumie, ujifunze jambo, ufundi, au kazi yoyote ya kuzalisha, ambayo itakufanya usimame kwa miguu yako mwenyewe, usikate tamaa kabisa…’akasema docta.

‘Sawa nitafuata ushauri wako docta…’nikasema.

‘Na kama nilivyokuambia, uniamini, kuna jambo nataka unifunulie kidogo, sio bay asana…, nataka uniambie kitu, kwasababu sote tumepitia huko, nata uniambie ni nani huyo rafiki yako wa siri..usiseme huna rafiki, kila mtu anaye…, hata awe siri,… unajua kuna jambo hapa, linatakiwa wewe nay eye mtibiwe pamoja, tunaweza kupanga mimi na wewe jinsi gani ya kumuita, hata watu wengine wasijue…najua unaye rafiki wa kiume, kwahiyo nilipenda tusaidiane kwa hilo, unasemaje…? Akasema.

‘Mhh docta, ina maana huaniamini, mimi sina rafiki hata mmoja wa kiume, na ..kwanini tena.., si umesema sina tatizo…au?’ nikauliza.

‘Ni kweli huna tatizo kabisa..umesema huna rafiki wa kiume, au mchumba, lakin inaweza kutokea, ujana una mambo mengi mimi naelewa, labda, nikuulize hujawahi kukutana na mwanaume, au kwa kulazimishwa au kwa namna yoyote ukakutana naye kimwili,..inaweza ikawa ni kwa bahati mbaya.?’ Akaniuliza.

‘Kukutana na mwanaume kwa vipi..hapana haijawahi kutokea, hapana wee, mama akijua hilo, yaani sio kwa ajili ya mama tu, mimi mwenyewe nimeahidi sitaki mwanaume, hadi hapo mungu atakaponiongoza, sitaki na sijawahi kuwa na rafiki mwanaume,..na hakuna, ..hata kushikwa kwa nguvu. Haijawahi kutokea kabisa, mimi sijawahi kukutana  na mwanume, sijawahi niamini docta..kwani kuna nini mbona kama kuna tatizo, niambie kama kuna tatizo?’ nikauliza.

‘Huwa inatokea kwa umri wenu, wenu, na ni vyema ukasema ukweli , maana ni vizuri sana hili swala likajulikana na wazazi wakajua, ndio maana nikata tuongee uniambie ukweli, ukificha, itakuwa vigumu kwako kusaidiwa, na mtu wa kukusaidia ni mimi, unajua sisi madocta kisheria tunatambulikana sana, pia mimi nipo kitendo cha kuwasaidia wanawake walio kwenye mazingira magumu, lakini siwezi kumsaidia mtu kama hasemi ukweli..’akasema

‘Docta unataka ukweli gani…?’ nikamuuliza

‘Unajua ukinificha, haitasaidia kitu, maana mimi naweza kukupima kuona kama kweli hujawahi kukutana na mwanaume, na itabidi nifanye hivyo kama utaendelea kunificha, bora useme ukweli ili tuanze sura nyingine, na ukificha, nitawaachia wazee wafanye kazi yao…’akasema.

‘Docta niambie ukweli, kwani mimi  nina tatizo gani, usinizungushe zungushe…’nikasema.

‘Una mimba…na kwa maelezo yako na vipimo, una mimba ya miezi miwili na kitu hivi hongera sana, lakini unanistajaabisha ukisema hujakutana na mwanaume unaona hapo, unajidanganya mwenyewe, sasa iambie ukweli ili niweze kukusaidia…’akasema.

‘Hongera, docta, unanitania, mimi mimba nitaipataje..’nikasema kwa hasira
‘Binti, usifiche, hili swala sasa sio la kuficha, unanielewe, inabidi umtambulishe huyo mwenzako ili muona jinsi gani ya kuliweka sawa, ukiendelea kuficha, wazee watakuelewa vibaya, kwa ushauri wangu umsema mapema, mimi nitakusaidi kuliweka sawa nikiongea na wazee wako…’akasema

*************

Docta aliponiambia hivyo, kwanza sikuamini, lkn jambo lililonijia akilini ni kuhakikisha kuwa wafadhili wangu hao hawaipati hiyo taarifa, na hata wakiipta niwe mbali kabisa na wao, wasije kuniona tena..

'Tafadhal docta, nakuomba nipo chini ya miguu, unisitir na hii aibu…kama ni kweli..maana mpaka sasa mimi siamini….’nikasema.

'Kwann unasema hivyo, kwani huna mume, huna mchumba, mimba hii umeipataje…haiwezekani, sema ukweli tu…’akasema.

'Docta mimi sijui nakuambi aukweli mimi sijui… na ndio maana siamini, mimi sijawahi kukutana na mwanaume yoyote, nitapataje mimba, kwani mimba unaweza kuipata hata kwa kupitia kwenye ndoto..sio kweli docta…’nikasema

'Docta kwanza akasita, halafu akauliza;

'Unasema wewe hujawahi kukutana na mwanaume ila uliwahi kuota kuwa umekutana na mwanaume, na ukawa na dalili hizo za kukutana na mwanaume au sio niambie ukweli..?’ docta akauliza akionyesha uso wa kushangaa na kutokuamini maneno ya huyo binti.

'Ndio docta,…huwaga naota hivyo, lakini sio hapo kwa sasa,  tena zilikuwa ni  ndoto za majinamiz hata sura ya huyo mtu sikuwahi kuiona, ni ndoto tu na sio kweli, mtu ananikaba, halafu nazalilishwa, ni ndoto na sio kweli…’nikasema.

'Mhh, hili la ajabu eeh,… kwani awali ulikuwa unaishi wapi, na ulikuwa ukiishi na nani..?’ akaniuliza docta

 "Ni hadith ndefu docta , ukitaka kuifuatilia historia ya maisha yangu utachoka....muhim, usiwaambie hao jamaa zangu, nakuomba tafadhali sana docta, nipo chini ya miguu yako, nitaumbuka mimi, na wala sina kosa, sijui ni nini hiki jamani, hivi mimi nina tatizo gani, jamani..mungu wangu nisaidie na mitihani hii…’nikasema nikiashiria kuomba kwa kuweka mikono kifuani na docta akawa ananiangalia kwa uso wa kushangaa kidogo.
'Kwani hao jamaa zako ni nani kwako hasa….?’  Docta sasa akawa ana mashaka na mimi.

'Ni wafadhili wangu tu, mimi sina baba wala mama, sina hata ndugu wa karibu, wao wamejitolea kunifadhili, na…awali sikuwa na wao, na baya zaidi ni kuwa hawa wafadhili wangu wakilifahamu hili, watanifukuza kama mbwa….nisaidia sana docta…’nikasema.

 'Sasa mimi sielewi, wewe ulitaka niwaambie unaumwa nini, maana kukusaidia kwangu ni kuwaambia hao jamaa zao jinsi gani ya kuhakikisha afya yako inakuwa salam, hadi muda wa kujifungua ukifika, sasa ukisema nisiwaambie, nitakuwa nafanya vibaya …’akasema docta.

'Uwaambie ugonjwa mwingine wowote lakini sio kwamba mimi nina mimba, kwasababu hata mimi simini kuwa nina mimba, ni mimba ya nani wakati mimi sijawahi kukutana na mwanaume..’nikasema.

 Docta, akatikisa kichwa kutokukubalina na mimi lakin baadae akasema;

‘Sikiliza wewe nenda nje, waite hao jamaa zako waingine na mimi nitajua jinsi gani y akuongea na wao, na wala usiwe na wasiwasi, hakuna baya litatokea dhidi yako, niamini mimi..’akasema docta, na mimi nikawa sina la kufanya,nikatoka, na wakati natoka, nikagundua kuwa mama mwenye nyumba alikuwa hapo mlangoni, nahisi alikuwa akijaribu kuona kama atasikia ni nini tulikuwa tunaongea huko ndani.

'Ehe tuambie ukweli, kulikoni masaa yote hayo…?’ akauliza mama mwenye nyumba
'Amesema muende, atawaambia mwenyewe tatizo ni langu ni nini….’nikasema sasa nikikwepa hata kuwaangalia usoni.

'Kwahiyo kumbe una tatizo, mbona baba yako kasema huna tatizo, ni mazungumzo ya kawaida ya kimalezi tu, kwa vile umekuwa, ..ooh, nilijua tu, una kitu wewe…’akasema baba mwenye nyumba.

‘Hakuna kitu mama, yote ni mitihani ya mungu tu..’nikasema kwa sauti ya kutaka kulia, nilijitahidi sana nislie nisje kuharibu , na baba mwenye nyumba, alikuwa mbali,akawa anakuja ili waungane na mkewe kuingia kwa docta, akanitupia jicho, lakini mimi sikuweza kumuangalia usoni.

‘Kwahiyo docta kasema twende ndani, mumemalizana kuongea…najua hakuna tatizo au sio, mama yako ana wasiwasi bure tu…’akasema baba mwenye nyumba.

‘Hahaha, eti hakuna tatizo, wewe unajidanganya bure, kuna tatizo, humuoni huyo binti alivyo….huyo ana tatizo, na ole wake, nigundue kuwa ni hivyo ninavyofikiria mimi, sizani kama kutakalika, sizani kama nitaweza kuishi naye tena, unasikia wewe mwanaume, huyo utamtafutia makazi ambapo mtaenda kukutana wawili sio nyumbani kwangu…’akasema huyo mama

‘Mke wangu kwani umesikia nini..mbona unanitia aibu…’akasema mume wake

‘Mimi nakutia aibu au nyie ndio mnatutia aibu sisi, familia yetu haina doa, tunahitajia kuijenga familaia yetu kwenye maadili safi, sasa wewe unataka kuleta doa, kwa kuleta watu wenye tabia mbaya..huyo bint ana mimba asitudanganey hapa…’akasema mke wake.

‘Eti nini, hapana hili sio kweli na haliwezekani, umasikia wapi hayo, kakuambia huyu binti…?’ baba mtu akauliza kwa mshangao, na jicho likamtoka kama kasikia jambo la kutisha

‘Unajifanya hujuiee,..wewe a utu uzima wako wote huwezi kuliona hili, mimi nilitaka tuje huku, il uhakikishiwe kitaalamu,wewe si unapenda hivyo, haya  twende huko ndani ukasikie mwenyewe, kwa octa, mtaalamu unayemuamini….’akasema na kufungua mlango.
Baba mtu akawa kasimama, kaduwaa, hakuniangalia, akakatikisa kichwa, halafu akamfuata mke wangu huko ndani kwa docta. Na mimi nikatulia kidogo, halafu nikasimama, nikaanza kutembea kwa haraka kuelekea kitu cha boda boda, akili hapo ilikuwa sio yangu,..

NB: Mdada anazidi kuingia kwenye mitihani, tuone jinsi gani watu wanavyoteseka,…
WAZO LA LEO: Ukiona kwako kuna fuka moshi ujue kuna kwingine kunawaka moto.. Ukiona wewe una shida, una matatizo yanakuandama kila kukicha,…, ujue kuna mwingine shida hizo na matatizo ni zaidi maradufu ya matatizo uliyo nayo wewe. Wapo wengine hawaijui raha duniani, wapo wengine hawajui watakula nini,..wapo wengine kila siku ya mungu wanalia kwa mauimivu ya mwili na akili, ….

Je hayo matatizo uliyo nayo ndio unafikia kukata tamaa…


Ndugu yangu…usikate tamaa ya maisha ilimradi unapumua,.., mkabidhi mola wako matatizo yako, huku ukitafuta njia rahisi ya kufanikisha mambo yako, lakini iwe ni njia ya halali…tatizo wengine wanatafuta njia za haramu, ukitumia njia hizo, utakuwa unajipalia makaa..hutafanikiwa na ukifanikiwa itakuwa ni kwa muda tu. Tukumbuke wakati wote kuwa Mungu hamtupi mja wake, na kila mja ana riziki yake, ni namna tu ya kuitafuta riziki hiyo ,lakini iwe sababu ya halali. Tumuombe mola wetu atufanikishie malengo yetu halali na atujalie tuipate riziki ya halali, bila kuingie kwenye dhuluma..Aamin.
Ni mimi: emu-three

No comments :