‘Wewe binti uliwahi kuniona nikiingia chumbani kwako
usiku…?’
‘Hapana….’ akasema
Binti wa nyumbani akaulizwa na kuambiwa aseme ukweli, yeye
akasema hakuwahi kumuona baba mwenye nyumba akiingia ndani , maana yeye huwa anakuwa
na usingizi mnzito, japokuwa anakabwa na majinamizi….
Ushahidi huo ukaonekana hauna mshiko…na baba mwenye nyumba
akapendekeza yule binti mwingine aitwe, ili atoe ushahidi, mimi niliona ni
ajabu , kwanini baba mwenye nyumba awe anajiamini hivyo, inawezekana kweli
hahusiki na hizo shutuma, lakini mama mwenye nyumba anadai ana video
inayoonyesha tukio zima.
Tuendelee na kisa chetu….
***************
‘Huyu binti mwingine kakataa kuja, lakini sio kitu, tunaweza
kuangalia shahidi mwingine, eti mke wangu.. tumuulize nani tena…au, labda
kijana wetu , kama na yeye anaweza kuwa shahidi wako…’akasema baba mwenye nyumba,
‘Hapana, ….’akasema mama mwenye nyumba, na kuwafanya watu
pale kushikwa na mshangao.
‘Kwanini hutaji kijana wako akahojiwa, yeye aliwahi kuingia
ndani, au sio, yeye alikuwa karibu na huyu binti, na huyo aliyekuwepo hapa
kabla, basi huenda kuna jambo analifahamu ,…’akasema kiongozi wa dini.
‘Sitaki kumuingiza mtoto wangu kwenye maswala haya ya
kikubwa, nina uhakika hahusiki ni ujanja ujanja wa baba yake tu….’akasema mama
mwenye nyumba.
‘Basi ngoja nihakiki jambo kwa huyu binti wa sasa kwanza,
nataka nikuulize maswali tena machache…’akasema kiongozi wa dini akimuangalia
huyo binti….na baadae akaanza kumuhoji…
.
'Mama amesema kuna siku alikukuta umepoteza faham chumbani
kwake, ulikuwa ukifanya usafi au sio…?’ akaulizwa,
'Ndio…nilikuwa nfanya usafi nikagundua barua, nilipoisoma
ndio nikapoteza fahamu…’akasema.
'Baba mwenye nyumba anasema alikufanyia huduma ya kwanza,
ambayo ndio ilimfanya mama mwenye nyumba amuhisi mumewe vibaya…kwa maelezo
niliyopewa, je kwa muda wote wakati baba mwenye nyumba anakufanyia huduma ya
kwanza ulikuwa huelewi hicho anachokufanyia..?’ akaulizwa.
'Ndio, nilikuwa sielewi kabisa..…wala sijui alinifanyia
nini,….’akasema.
'Sasa kwanini ulipozindukana ukakimbia…?’ akaulizwa
'Nilihisi anataka kunizalilisha..kwa vile …hata sijui,
unajua mwanaume awe amekukalia juu hivi.., …inatisha, ndio maana
nikakimbia….’akasema.
'Alikukalia juu kwa vipi…?’ akaulizwa
‘Alikuwa kapiga magoti, na kuniinamia, uso wake ulikuwa
karibu na uso wangu, …ndivyo nilivyoona hivyo, na sikuelewa anataka kufanya
nini, ..wazo lililonijia haraka ni labda alikuwa anataka kunifanyia kitu
kibaya….’akasema.
‘Sasa kwanini uhisi hivyo, wakati huyo ni baba yako, ni sawa
na baba yako…?’ akaulizwa.
'Kwa jinsi alivyokuwa kaniinamia…siweza kuwazia jambo
jingine zaidi ya hilo, hata sijui kwanini niliwazia hivyo….’akasema.
'Yaonyesha humuamini baba yako, ..au kuna kitu kiliwahi
kukutokea mpaka ukaogopa au?’ akaulizwa.
'Wanaume wote mimi siwaamini, mama aliniusia hivyo..anasema
nisipende kuwa karibu nao kihivyo, maana ibilisi ni mkali ukiwa nao karibu na
wao hawawezi kujizuia, kuingiwa na ushawishi mbaya…’akasema.
'Sio kwasababu ya hayo yaliyotokea humo ndani, au kuna jambo
liliwahi kukutokea, la kukutia mashaka..?’ akaulizwa.
'Zaidi ni hayo majinamizi tu ..mmh, hakuna jambo lilinitokea,…mmmh,
mimi sikumbuki zaidi….., ni hisia zilinijia tu hivyo…’akasema.
'Unahisi labda kuna mtu humu ndani anaweza kuhusika na hayo
majinamizi au unaamini ni ndoto tu, au kuna mashetani…?’ akaulizwa.
'Hapana, sitakiwi kumuhisi mtu vibaya, na sijui nini,
mashetani, hapan, mimi siyajui hayo, …kiukweli mimi sijawahi kutokea na vitu
kama hivyo, nasikiaga kuna ndoto za majinamizi ,na dalili zake ni kama hizo,
..hivyo tu…’akasema.
'Chumba chako kipo karibu na kijana, na kijana anasema, mara
nyingi amekusikia ukipiga kelele, je na yeye hujawahi kumuona akiingia chumbani
kwako usiku ukiwa umelala..?’ akaulizwa.
'Mhh, hapana, ..awali nilipofika kwenye nyumba hii, ndio
yeye alikuwa akinielekeza mambo mengi ya humu ndani, kazi nk…ndio aliwahi
kufika siku usiku siku za awali nilipoanza kazi… , nilipofungua macho,
nikamuuliza nini kimetokea, amefuata nini ….akasema kanisikia nikipiga kelele,
lakini haijatokea tena mimi kumuona akiingia ndani usiku…’akasema.
'Huhisi kuwa anaweza kuwa ndio yeye anayekufanyia hivyo
usiku…?’ akauliza.
'Siwezi kumuhisi mtu yoyote vibaya, kama hajanifanyia, na
kuhakikisha kuwa ndio yeye, kwangu mimi hayo yote nayaona kama ilikuwa ni ndoto
tu…’akasema.
'Sasa ikitokea baya mfano umepata mimba utasemaje..nasema
hili kwa vile umesikia mwenzako aliyekuwa hapa awali ilimtokea kama hivyo,
akajikuta ana mimba…?’ akaulizwa.
'Mimba!... nitapataje hiyo mimba, hapana kwani ndoto inaweza kumpatisha mtu mimba!, mmhh, mimi
hata sijui...mimba mungu wangu! , iingiaje hiyo mimba....hata sijui…’nikasema
sasa nikionyesha mashaka.
'Ndio hivyo,
usiposema ukweli, usije kumlaumu mtu , utafukuzwa humu ndani, na hakuna wa
kukusaidia tena….’akaambiwa
'Sasa mlitaka mimi niseme nini zaidi, maana hivyo
nilivyosema ndivyo nijuavyo, kama kuna zaidi mimi namuachia mungu.
***************
‘Ngoja nimjaribu tena huyu binti mwingine labda aliogopa
kupokea simu kwa vile yupo na mabosi wake….’akasema baba mwenye nyumba na
kuanza kupiga simu tena, na safari hii binti akapokea na wakaanza kuongea na
baba mwenye nyumba. Baba mwenye nyumba akaweka spika ya nje ili kila mtu asikie
anachoongea na huyo binti, hakutaka ionekane kampanga huyo binti aje kuongea
atakavyo yeye.
‘Samahani unaweza kufika hapa nyumbani mara moja…?’ akasema.
‘Nije kufanya nini, mizigo yangu nimeshaichukua, mimi siwezi
kufika hapo nyumbani kwenu tena…’akasema.
‘Kwanini, ..hakuna
tatizo lolote baya, muhimu kuna kitu
tunataka kukuuliza, tunakuomba tafadhali…’akasema na huyo binti hakujibu kitu
akakata simu.
‘Siwezi kuja,….kwanza bosi wangu hataki niwe ninatoka toka
ovyo, …’akasema
‘Basi tuongee hapa kwenye simu , tukuulize maswali mawili
matatu utusadie….’akaambiwa
‘Hapana hata hivyo nimetoka nje kidogo simu ilipoita…,
nasubiriwa ndani kuna kazi nafanya, kwaheri….’akakata simu.
‘Huyu bint naona hatuwezi kumpata kwa hivi sasa, nilitaka na
yeye aje hapa ili aweze kuthibitisha hili, kwa kauli yake, ili tuyamalize haya
mambo kwa amani, nitafurahi turejee maisha yetu ya kawaida, …’akasema baba
mwenye nyumba.
‘Kwa hali kama hii sizani kama hilo litawezekana
tena….’akasema mama mwenye nyumba.
‘Kwanini mke wangu, mbona hujaamini hilo, niamini mke wangu…unajua
wewe ni hisia zako tu, lakini kiukweli sivyo hivyo kabisa, je uliwahi kuingia
ndani ukaniona nikifanya lolote baya,..hujawahi, na mengine yote ni hisia zako
tu….’akasema.
‘Tatizo lako, unajifanya mjanja sana, unaniona mimi sina
akili, mimi sijui hawa mbinti umewapa nini,…hata sijui…na huyu binti angelisema
ukweli, lakini nahisi kuna kitu umewafanyia, mpaka wanaogopa kusema ukweli,na
huo usiku kuna kitu unawafanyia mpaka wanashindwa kuamuka,…’akasema mkewe.
‘Sasa huko nikunisingiziana uchawi, mimi nifawafanyie nini,
na kwa ajili gani, kuna raha gani hapo…mke wangu, hivi na umri huu ninaweza
kuanya kitu kama hicho…’akasema.
‘Sio uchawi, sio lazima uchawi, ila kuna jambo uliwafanyia
hawa mabinti, haiwezekani itokee siku zote washindwe kuzindukana, na mimi
mwenyewe nilikuona ukiingia huko chumbani kwao, …’akasema mama mwenye nyumba na
kiongozi wao wa dini, akasema;
‘In maana uliwahi kumfuatilia, akienda huko chumbani kwa hao
mabinti, hebu hapo kidogo, tuelezee ulivyomfuatilia na kumuona akiingia huko
chumbani kwao na je ilitokea hivyo kwa mabinti wote wawili..?’ akaulizwa.
‘Siku ya kwanza, nilipoanza kumshuku, …’akasema huku
akimuangalia mume wake.
************
‘Ilikuwa ni usiku, ghafla nikashtuka kutoka usingizi,
nikajiona nipo peke yangu, nikajua mwenzangu labda kaenda kujisaidia,
nikasubiria kama nusu saa sikumuona mwenzangu akitokea, nikaamuka na kuanza
kumtafuta chooni, alikuwa hayupo, hapo nikaingiwa na mshaka, huyu mtu kaenda
wapi..sikuwa na wazo jingine zaidi ya kuwa, labda katoka nje kuna tatizo.
‘Nikataka kuelekea nje, lakini wazo likanijia huenda kuna tatizo
chumbani kwa huyo binti, maana tatizo hilo nilishalisikia kutoka kwa mtoto wangu,
kuwa huyo binti huwa anapiga kelele usiku,…wazo hilo liliponijia nikaelekea
huko chumbani kwa huyo binti….’akatulia
‘Wakati natoka sasa kuelekea huko, nikamuona mume wangu akitokea
chumbani kwa huyo binti, na mimi kwa haraka nikajificha na kumuacha apite,..hakuniona,
aknipita na aliponipita tu mimi
nikamfuata kwa nyuma hadi chumbani, yeye akapanda kitandani kulala, na kuanza
kukoroma, kama vile hakujatokea kitu…’akasema.
‘Hukumuuliza kwa muda huo..?’ akaulizwa.
‘Hapana, sikumuuliza usiku huo, nilimuuliza asubuhi yake, na
nikashangaa, akikataa kuwa hakutenda hivyo, nikaona ajabu sana, kwanini akatae,
nilipombana sana, akasema, huenda alisikia sauti, maana huyo binti wakati
mwingine huwa anapiga makelele, na aliposikia sauti za ukelele,ndio akaenda huko,
kuangalia kuna nini,,….’akasema.
‘Sasa kwanini nimekuuliza mara ya kwanza ukakataa kuwa
hukufanya hivyo…?’ nikamuuliza.
‘Aaah, unajua kichwa changu kina mambo mengi, nikiamuaka asubuhi
huwa nawazia mambo ya kazini, nisamehe tu mke wangu….’akaniambia hivyo.
Kiongozi wa dini, akauliza swali jingine;
‘Na huyo binti ulipomuuliza na yeye alisema nini..?’ akaulizwa.
‘Alisema hajui…maana alikuwa amelala, ila ni kweli yeye aliendelea
kuota kukabwa,….na hajui zaidi…basi kwa vile sikuwa na mashaka sana siki hiyo, sikutaka kudadisi zaidi, na hiyo ilikuwa siku
ya kwanza kugundua hayo mambo kutoka kwa mume wangu, kuwa huwa usiku ana tabia
ya kuelekea huko kwenye chumba cha mabinti…’akasema.
‘Je kuna siku nyingine ilitokea hivyo, na ilitokeaje, maana
umesema hukuwa na wasiwasi na tukio hilo…?’ akaulizwa.
‘Kiukweli japokuwa sikuwa na wasi wasi na tukio hilo ,
lakini siku zilizofuatia niliamua kulala kwa kuvizia ili kama nitamuona mume
wangu akitoka nimfuatie, au nikisikia kelele kwa huyo binti, mimi sasa ndio niende
huko badala ya mume wangu…, lakini hutaamini, nikawa nashikwa na usingizi
mnzito, najikuta nazindukana kukiwa ni asubuhi….’akasema.
‘Kwahiyo hukuwahi kumfuatilia na kumfumania mumeo wako, kama
ni hivyo kumbe hisia zako ni za kuhisi tu, sio kweli kuwa uliwahi kumfamania
mume wako..?’ akaulizwa.
‘Ipo siku moja, nilizindukana kama hivyo hivyo tena,…na
nikakuta mume wangu hayupo kitandani, nikasema sasa nitaweza kuhakiki jambo
hilo , kama sijachelewa…akilini sio kwamba nilikuwa simuamini mume angu, lakini
kutokana na kisa cha mfanyakazi wa awali na yaliyotokea kwake, na tukio hilo
lililotokea humo ndani kipindi hiki, nikawa naanza kujenga hisia hizo,…’akatulia.
‘Basi kwa haraka nikaamuka na kuelekea huko chumbani kwa
binti, ni kweli kumbe alikuwa keshaingia huko ndani, ..nilipofika mlangoni,
nikasikia kelele za kulalamika….’akatulia.
‘Sauti ya nani anayelalamika….?’ Akaulizwa
‘Nahisi ilikuwa ni ya binti,..sikuwa na uhakika sana… ni
kama mtu anayeongea akiwa usingizi, ..’sitaki, mimi sitaki…niach, sitaki,…’.vitu
kama hivyo…niliposikia sauti kama hiyo nguvu zikaniishia,…nikataka kufungua
mlango,…nithibitishe huo ukweli, maana hapo akili ilikuwa kama sio yangu tena,..kwanini
asema sitaki, niache, …ina maana kuna mtu kweli anataka kufanya kitu kibaya kwa
huyo binti,na ni nani zaidi ya mume wangu…kwa haraka kwa hasira nikataka
kufungua mlango, na ile nashika kitasa,
cha mlango, mlango ukafunguliwa kwa haraka…akatokea mtu…’akatulia .
‘Ni nani…mume wako…?’ akauliza.
‘Hapana alikuwa ni kijana wangu…!’akasema, na watu
wakaonyesha uso wa mshangao.
‘Oh, kijana wako tena….?’ Akaulizwa na huyo kiongozi.
‘Ndio, kijana wangu, na aliponiona akanishika mkono na
kuvuta pembeni, akaniambia…’
‘Huyo binti anapiga ukelele, na baba yupo ndani, anajaribu
kumsaidia….’akasema.
‘Oh, mimi nikataka kwenda huko, ili nikasaidie, lakini kwa
mshangao kijana wangu akanizuia na
kusema;
‘Hapana mama usiende huko, baba aliwahi kuniambia awali,
kuwa mtu akiota ndoto kama hizo haitakiwi kumshtua, na akizindukana akiona watu
ni wengi wamemjalia, mtu kam huyo anaweza kushikwa na presha, ..basi mimi
nilipomuona baba yupo huko ndani, sikutaka kuwasumbua hata baba hajui kuwa
nimefika huko na kuwaona, ….’akasema.
‘Umewaonaje..?’ nikamuuliza hivyo tu.
‘Baba alikuwa akijaribu kumtikisa kidogo huyo binti ili
aweze kuamuke, lakini huyo binti alikuwa bado anaendelea kupiga kelele, anagala
gala tu,…’akasema.
‘Kelele gani..?’ nikamuuliza
‘Kama anakabwa, anasema sitaki, niachie,…lakini sauti
haitoki vizuri, ..kama yakujiuma uma …’akasema, na wakati tunaongea mara mume
wangu akatokea huko ndani, na kuelekea chumbani, mimi nikamfuatilia hadi
chumbani, na kumkuta ameshalala fofo…, ..kiukweli siku hiyo sikuwa na amani,
kwasababu kumbe hata kijana wangu analijua hilo.
‘Ulipomuuliza kesho yake alisemaje?
‘Kama kawaida yake alidai kama ni kweli basi alikwenda huko,
aliposikia kelele, na madhumuni ni kuangalia kuna nini kinachomfanya huyo binti
apige makelele,…’akasema.
‘Alitamka hivyo….’kama
ni kweli,…’ kwanini asema hivyo, kama ni kweli….?’ Akaulizwa.
‘Ndio alitamka hivyo…, hata mimi nikajiuliza kwanini anasema
hivyo, kama ni kweli, ina maana hakumbuki, ina maana gani, nikawa najiuliza
sana, ndio nikajiwa na wazo hilo la kuweka video ya kurekodi matukio huko
chumbani, nione ni nini kinachotokea maana kufuatilia usiku ilishindikana,kwasababu
ya usingizi,..huwa mara zote nilizopanga nifuatilie, najikuta nimelala usingizi
mnzito…’akasema.
‘Ukafanikiwa kufanya hivyo….?’ Akaulizwa.
‘Ndio..nilifanikiwa video ilichukua picha vizuri sana…japokuwa,
..kuna …mapungufu fulani, lakini nilichotaka kukiona nilikiona, kwa uwazi zaidi
hawezi kukataa akiiona hii video….’akasema.
‘Muongo, …hiyo kanda ya video, itakuwa imetengezwa huko
mitaani, sio kweli kabisa, je ilionyesha nini, kuwa mimi ndiye ninayewakaba hao
mabint…?’ akauliza.
‘Ni zaidi ya kuwakaba,……ulikuwa unawazalilisha hao mabinti,
kwa ushahid huu hapa…’akasema mama mwenye nyumba,a kionyesha hiyo kanda ya
video alioyokuwa nayo.
‘Sikubaliani na hilo kabisa, na kwasabau hiyo itabidi
uionyeshe hiyo kanda ya video, tuhakikishe, …siwezi kufanya lolote zaidi ya
kuwakagua na kumtikisa tikisa ili azindukane….’akasema.
‘Sio kweli..nimeona kwa macho yangu ulichokifanya kwa huyo
binti…, ni aibu mume wangu, sikupenda kulisema hili, au kulionyesha, lakini sasa umenichefua, unataka nionekane mimi
ni muongo, mbele ya wazazi wangu hawa, wakati ni kweli….’akasema.
‘Mimi nipo tayari niione hiyo video,…ionyeshe….’akasema mume
wake na mkewe akamuangalia kwa uso wa mshangao, na kusema;
‘Wewe…unataka nionyeshe huo uchafu wako mbele ya wazazi
hawa,….’akasema mke wake.
‘Mimi najua hakuna kitu kama hicho ndio maana nataka uionyeshe,
sijwahi kufanya kama anavyotamka yeye, ni uwongo mtupu,….’ Akasema.
‘Una uhakika kuwa kanda hiyo ya video inaonyesha kila kitu,
ambacho kinadhihirisha kuwa mume wako ndiye anayafanya hayo…?’ akaulizwa
‘Ndio…niliiangalia mimi mwenyewe, nikarududia tena na
tena….kiukweli baada ya kuiona hiyo kanda ya video, nikasema basi, ….yale
mapenzi niliyokuwa nayo kwake, yakaondoka, na ikabakia chuki, nasema ukweli
huo,chuki, sasa haivi namchukia huyu mwanaume …sizani kama hali hiyo ya zamani
itarejea tena, sizani….’akasema.
‘Aonyeshe, …kama anavyodai ni kweli, aonyeshe, maana mimi
sijafanya hivyo…, lini jamani, …hapana, huo ni uwongo,mke wangu una uhakika na
hilo…usiseme kwa kujifurahisha, na usije ukadanganywa na mashoga kuwa utengeze
kitu kama hicho ili kunizalilisha, …samahani sana, mke wangu kwa hilo mimi
sikuamini….’akasema na wajumbe pale wakaangaliana, na ilikuwa kama
hawakupendelea hilo tendo lifanyike, na mkuu wa dini, akauliza.
‘Je kama ikionekana ni kweli, utasemaje ..?’ akaulizwa baba
mwenye nyumba.
‘Hakuna kitu kama hicho….sio kweli,…labda iwe ni ya kugushi,
lakini kama ni kweli, ilichukua matukio ya ndani, mimi nina uhakika sikuwahi
kufanya kitu kama hicho, …jamani mimi nimechanganyikiwa, hapana, mke wangu,
tafadhali sema ukweli….’akasema jamaa.
‘Wewe unampenda mke
wako?’ akaulizwa na kwanza akamuangalia mkuu huyo kwa mshangao, halafu akasema;
‘Sana tu, nampenda sana mke wangu, ni yeye tu na dhana zake
potofu…’akasema na wazee na mkuu wa dini wakaangaliana na mkuu wa dini akamuuliza
mke mtu.
‘Wewe unampenda mume wako..?’ akamuuliza.
‘Nimeshasema awali, mume wangu nilimpenda sana, na
ningeendelea kumpenda, kama angekiri kuwa ana tatizo, lililomsukuma hadi
kufanya tendo hilo, maana hata ukiangalia hiyo video, ni kama analazimishwa,
…anakuwa kama sio yeye….’akasema
‘Mimi kwa uni wangu, naona sio vizuri kuonyesha kitu kama
hicho mbele ya watu, lakini kama mume mtu unazidi kukataa, na mke unaona huo
ndio ushahidi wako, basi hatuna jinsi, ila kwa ushauri wangu,..baba mkwe utuwie
radhi, mimi na baba yake tutaangalia, na kama ni kweli tutakuthibitishieni huo
ukweli…’akasema hivyo.
‘Sawa, ni vyema…’akasema baba mkwe.
‘Aaah, kwanini, mimi nataka wote tuone, ili tubainishe
uwongo, mimi najua jinsi gani watu wanavyogushi video, wanachukua mapicha ya
watu wengine wanawekeza vichwa, kwenye mapicha hayo,…nataka nije kumuumbua mke
wangu,…’akasema baba mtu kwa kujiamini.
‘Hapana, ….mimi na huyu mfanyakazi wenu wa kazi za ndani
tutatoka nje…’akasema na wakati wanajiandaa kutoka, mara mlango ukagongwa, na
aliyeingia alikuwa yule bint wa kazi wa zamani
‘Mimi nimekuja kufuata muito wenu….’akasema
‘Oh karibu lakini tunakuomba usibirie nje kidogo…’akaambiwa.
‘Hapana mimi sina muda zaidi, ila nataka niseme ukweli,
nimeona siwi na amani…’akasema.
‘Ukweli gani..?’ akaulizwa
NB: Bint anataka kumwaga radhi, au kuna jingine
WAZO LA LEO: Mwanadamu
ana staha zake, ndio maana sehemu zake nyingine zinaitwa za siri, sio vyema
kudhihirisha viungo hivyo vya siri kwa kila mtu, kwa kufanya hivyo unakiuka
haki za binadamu. Wengi wamekuwa wakipiga picha za wengine na kuzituma
mitandaoni, sio vizuri jamani,…Mwenyezimungu katuwekea mipaka, ya maumbile
yetu..kuwa ni nani na nani wanatakiwa kuonana maumbile yao ya siri. Na
kuyadhihirisha maumbile ya siri ya watu wengine huko ni kuzalilishana ni dhambi
kubwa sana, tutakuja kuulizwa madhambi hayo siku hiyo ya hukumu, kwa kuwakosea
wanadamu wenzetu…. Tuweni makini jamani.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment