Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, June 17, 2017

MPENZI WA FACEBOOK-53



‘Basi muondoeni huyo hiyo sura yake ya bandia tumgundue na yeye ni nani, halafu tutaangalia kama tuna muda wa kumsikiliza na yeye …muhimu tumfahamu na yeye ni nani, maana leo …’akasema hakimu, na kila mtu akawa na hamasa ya kutaka kumjua huyo mtu naye ni nani..


Docta akafanya vitu vyake, akafanya kitu kwenye laptop yake,  na mara usoni kwa huyo jamaa, kukafutuka, kama ilivyokuwa kwa mshitakiwa namba mbili,…na ikafunguka kama zipu, na docta akafika pale mbele kumalizia hiyo kazi, lakini cha ajabu alipomkaribia huyo jamaa, akafanya kazi ya kuondoa hiyo ngozi ya sura ya bandia…docta alipoiondoa, kabla hajamaliza kabisa…,kwanza akasita akabakia kwa karibu dakika moja akiwa ameduwaa,….

Kuduwaa kile, kuliwafanya watu waingiwe na hamasa zaidi, docta kaona nini mpaka ashikwe na butwaa, …na muheshimiwa hakimu akauliza;,


‘Vipi docta umeona nini…mbona umeshikwa na butwaa…?’ akaulizwa.


Docta hakujibu,..hakusema neno, akaivuta ile ngozi bandia, na kutembea kurejea sehemu yake kwenye laptop,..akimuacha huyo mtu, ili kila mtu ajionee yeye mwenyewe, …


Watu walijivuta…hata waliokuwa nje wanataka kuingia ndani, askari nao kwa vile wana hamasa ya kuona wakajikuta wanaachia watu wanaingia…, na wale wasio na simile, waliokuwa wamekaa, wakasimama ili wamuone vyema huyo mtu, kwani sasa jamaa alikuwa anaonekana, japokuwa alikuwa kainamisha kichwa chini,…lakini kwa anayemfahamu alishamtambua mara moja,…


Sasa kile kilichotokea kwa docta, kikawatokea na wengine,..watu walibakia mdomo wazi, kwa mshangao, na  tofauti na walivyofanya kwa mshitakiwa namba mbili, ambapo watu walipiga kelele, kwa huyu sasa, watu walibakia kimia, kilichoongea ni macho na midomo yao…macho yaliwatoka , na mdomo ukabakia wazi,..ni hisia ya aina yeka!


Mbele kwa hakimu,…ndio ikatokea mpya, mara nyingi hakimu anajitahidi sana kuficha hisia zake, lakini safari hii, …hakimu alishindwa kujizuia, akafikia kusimama, na usoni, akaashiria kukunja uso, wa kutokuamini,..akawa kama anasogeza shingo kuangalia vizuri, na alipohakikisha alichokiona kuwa ni sahihi, akawageukia wenzake, wazee w baraza, wazee walikuwa nao katika ile hali ya kushangaa..


‘Mungu wangu hii ni nini jamani…’akasema hakimu.


‘Ndio hapo mjionee, wenyewe, ni kwanini tuliamua ushahidi huu uonekane mbele ya mahakama, kiukweli hatukutarajia hili, ila …tulitaka muone jinsi watu wanavyobadilika wakivaa hizo ngozi, lakini sasa imekuwa zaidi ya kubadilika,..tujionee wenyewe….’aliyesema sasa ni muendesha mashitaka.


‘Hii ….imenishitua sana…hebu inua kichwa watu wakuone vizuri….’akasema hakimu, kidogo akionyesha lugha ya unyenyekevu, tofauti na ilivyokuwa kwa mshitakiwa namba mbili!


Jamaa, mshitakiwa namba moja, alikuwa bado kainamisha kichwa chini, taratibu akainua kichwa chake, na sasa akawa anawaangalia watu, na hapo watu hawakuweza kujizuia, wakaanza kuzomea, kupiga kelele…na jamaa akaanza kucheka, kule kuanza kucheka kwake, kukawafanya watu wakanyamaza, yeye akaendelea kucheka, mpaka akawa anatoa machozi, halafu akabakia kimia,…


‘Ni ajabu kabisa…halafu unacheka…hivi unataka sisi tukueleweje, hasa mimi ambaye ninakufahamu sana…lakini sio kukufahamu kwa tabia hiyo, mimi kwangu wewe ulikuwa mwalimu, ulikuwa mzazi, ulikuwa…aah, siwezi hata kuamini hii, ina maana na wewe upo kwenye kundi hilo haramu ..nasikitika sana…’akasema hakimu, sasa akitaka hata kutoa machozi.


‘Unajua ni kwanini nacheka,…nacheka, kwa vile …hahahaha, sikutarajia kuwa ipo siku na mimi nitaweza kusimamishwa hapa, nimezoea kuwasimamisha wengine hapa,..sikutarajia kuwa nitakuja kuumbuliwa hivi, ..lakini zaidi,..na kwa kuona watu walivyotoa macho ya kunishangaa, mnashangaa nini…eti, mnaona kipi cha ajabu, kuwa mimi nami nimo,…jiulizeni mara mbili, kama alivyotangulia kuongea mshitakiwa namba mbili, alisema nini….’akatulia


‘Mjiulize kwanza ni kwanini mtu kama mimi nikajiunga na jambo kama hili..sio kitu kidogo, sio kitu rahisi…..sasa mimi ndio mimi, kwenye sura yangu halisi,…mimi sina kawaida ya kuficha sura yangu…mbele ya watu kama nyie, nina kawaida ya kuficha sura yangu nikiwa kazini ..kwenye kaz zetu…


‘Na ikitokea mmoja wapo akanitambua, basi hatanitambua tena…hataweza kufungua mdomo wake tena…kwasababu gani, ..kwasabau sikutaka nijulikane mimi ni nani, sikutaka,..nije kupata fedheha, kama fedheha, niliyoipata hii leo, sikupenda nije kudhalilika tena nilishadhalilishwa sana, jamani tuliwakosea nini wanadamu wenzetu....nilimuomba mungu sana, ikiwezekana aichukue roho yangu kabla tendo hili halijatokea, lakini haikuwezekana..


‘Najua muda wangu kuishi bado upo...lakini nibado masaa macheche tu..kwani kama ilivyotokea kwa wengine, kuwa wakiniona hawatapata nafasi ya kuniona tena, sasa ni zamu yangu, mumeniona na hamtapata nafasi ya kuniona tena, nikiwa napumua..hamtaamini hili, ila…ndivyo itatokea...’akageuza kichwa kuangali kushoto na kulia, halafu akageuka kuangalia kule alipokaa yule mama, …

Yule mama aliyekuwa kasimama kipindi kile, mshitakiwa namba mbili anaongea sasa alikuwa kakaa, akionekana hana raha,…lakini kwa kuonekana kwa huyu mshitakiwa namba moja, hata yeye, alijikuta akishikwa na bumbuwazi, hakuna aliyetegemea hili kabisa,….na mama alipoona huyo mshitakiwa anamuangalia yeye, akajua kuna neno kubwa linakuja tena dhidi yake, hakujua ni neno gani.


‘Najua wewe mama, una neno la kusema dhidi yangu, ukikumbuka kuwa mimi ndiye niliyekuwa nikizimisha kesi zako zikifika kwangu, sasa umepata jibu sahihi, kuwa ni kwanini ilikuwa hivyo….’akaanza kuongea.


‘Mimi ni hakimu wenu, nimekuwa nanyi kwenye mahakama hii kwa muda mrefu sana, mnanifahamu kwa sera zangu, na mlikuja kushaangaa jinsi gani nilivyoweza kuipiga dana dana kesi hiyo ya huyo mama,…kwa wajanja wangeliligundua hili mapema kuwa kuna jambo, lakini hakuna alieyeweza kulifikiria hili..


‘Huyo docta, alinifanya nihisi kuwa kanigundua, lakini baadae nikagundua kuwa hajanigundua,..na isingelikuwa uzembe wa …hawa jamaa..isingelikuwa kukosea kwa huyo mtaalamu marehemu,…..na isingelikuwa huruma…..iliyonishika, nikawaza mbali, na ..labda bado ingelikuwa kitendawili cha kunipata mimi..lakini wanasema lililopangwa limepangwa, lazima litatokea..hapo akatulia kidogo.


‘Najua hakimu, unataka nijitambulishe rasmi, nasita kukuita muheshimiwa hakimu, maana wewe ulikuwa mwanafunzi wangu kikazi,mimi ni bosi wako, maana nilikupokea, nili..kusaidia ukawa mzoefu, sasa leo unahitajika kunihukumu mimi ni ajabu kabisa..sawa fanya kazi yako….’akasema.


‘Kwenye sheria hakuna mkubwa, …sasa hivi upo chini ya mamlaka yangu, haya, tuambie rasmi wewe ni nani..?’ akauliza.


‘Mimi  kwa jina ni…..(akataja jina)  halafu akaendelea, ‘ Na kwa kikazi, mimi ni, hakimu,…hakimu mkuu wa mahakama hii,  ambaye mnamfahamu sana, ndio maana wengi mlitoa macho karibu ya kudondoka ,  kwa mara ya mwisho mimi ndiye niliyekuwa nikisimamia hii kesi, nikaamua nikae pembeni, maana nilishaona nikiendelea nayo mnaweza kunishuku.


‘Aaah,..nashukuru sana, kuwa leo, na mimi ni mshitakiwa, nashukuru kuwa na mimi nitapata nafasi ya kuelezea, madhalimu nili..yaliyonikuta hadi nikafikia hapa…’akasema kwa kusita sita, ilishaonekana hayupo vizuri kiafya, tokea awali.



‘Kumbe ndio maana…’aliyesema sasa hivi ni yule mama, mke wa mzee.


‘Kumbe ndio maana, hahaha,…ndio… wewe usiongee kabisa, maana wewe ndiye chanzo cha haya yote, ..’akasema.


‘Na wewe unasema hivyo, mimi nilikufanyia nini kibaya wewe, wewe ndiye mbaya maana kila kesi yangu ikitajwa unaipiga kalenda, ni kwanini..?’ akauliza huyo mama.


‘Nashukuru sana, kuwa ni wewe umeliuliza hilo swali badala ya muendesha mashitaka, na mimi sitakwenda mbali sana, sitaongea sana, maana,..muda sina..ila nikujibu swali lako kwa maelezo mafupi tu.


‘Hivi wewe uliposikia kuwa binti yako kafa kwa kunywa sumu, na ukahisi kuwa hakuinywa sumu hiyo kwa kukusudia…, huenda alifanyiwa jambo mpaka akafikia hatua hiyo, uliwazia kufanya nini moyoni mwako, kama kweli kuna mtu alifanya hayo na ndio ikafikia binti yako kunywa sumu, sema ukweli wako..?’ akauliza.


‘Kwahiyo wewe ndiye ulifanya yote hayo..?’ akauliza mama.


‘Unajibu swali au unaniuliza swali…’akasema huyo mshitakiwa.


‘Nakujibu…’akasema huyo mama na watu wakacheka.


‘Na mimi nakujibu ..ndio, ni mimi ndiye niliyefanya yote hayo..ni mimi nilitengeneza namna kufanya binti yako anywe sumu…ili afe, ili tumchukue kama msukule kwa ajili ya kufanikisha lengo letu, unajua tulifanyaje..’akatabasamu kidogo.


‘Mashetani wakubwa nyie….’huyo mama akasema kwa hasira.


‘Wewe unatuona hivyo, lakini nyie hamjioni…Mimi kama mtaalamu wa kupanga mambo, kitaalamu..niliweza kulipangili hilo tukia kwa namna yake,..kwanza kwa kuhakikisha kuwa kuna mfarakano kati ya binti yako na mchumba wake wa siri, haya yalianza mapema sana….huyo mchumba wake wa siri, mpaka leo hajui kuwa mipango ya yeye, kumpata mwanamke mwingine na kuweza kumuumiza mpenzi wake wa siku nyingi..hiyo namna ilipangwa na sisi..hajui mpaka leo, muulizeni..


‘Jamaa akakutaka na msichana tuliyemuandaa, akiwa na sura ya mvuto, hakujua kuwa sura ile sio sura sahihi ya huyo binti, huyo binti alikuwa ni kahaba tu, tulimsomesha, tukamtengeza, akajibu..na akaisambaratisha ndoa ya wapendwa hao..na wengine tuuliotaka wafanyiwe hivyo, hiyo ndio kazi ya shetani, kafarakanisha ndoa…’akatulia.


Siku mdada, binti yako anafika kwa huyo mchumba wake akamkuta jamaa yupo na binti, ..ni nini alichokiona na ni nini kilichomfanya atoke pale akilia, mtakuja kumuuliza yeye mwenyewe..ila lengo letu ilikuwa ashikwe na hasira, na hiyo hasira iwe ni sababu ya tendo litakalofuata..


Binti alipotoka pale, akakutana na ndugu yake, hawakuongea,..ndugu yake alihisi kuwa ni hasira, ni tabia ya ndugu yake..hakujua kuwa ni sisi tulikuwa tunacheza na akili za dada yake..kuna muda dada yake alitamka maneno,…’ni bora nife, ni bora nife..’ haya maneno hakuyatamka yeye kwa kupenda,…yalitamka na mbinu zetu, huyo binti hana udhaifu wa kufikia hapo, huyo binti ni jasiri sana, aliyemfahamu zaidi ni baba yake..


‘Haya, binti akafika dukani kununua dawa…muone hapo…, binti alifika duka la dawa, wakaingia na ndugu yake, ndugu yake, akawa anakagua vitu vingine vipodozi sijui.., huyo dada yake akawa anaongea na muuza dawa, muuza dawa akamuambia ingie chumba kile, …hizo dawa atapewa huko…uone ilivyotokea…


‘Toka lini hizo dawa zikauzwa chumba hicho kingine, na kwanini huyu ndugu yake hakuweza kulishutukia hilo, na kujiuliza ilikuwaje hapo..akili zililala..mara nyingi watu hatuna tabia za udadisi,, hamna tabia ya utafiti..kitaalamu,…, mara nyingi watu hukimbilia kwenye tukio, wakazusha mambo yasiyothibitishwa kitaalamu,..lakini akili zetu hazichimbi ukweli wa jambo.


‘Yule mdada kwa muda huo alikuwa sio yeye, akaingia huko alipoelekezwa, na huko, akakutana na mdada mwingine sura sawa sawa na ya kwake, kama mtaweza kumrejesha kwenye hali yake, mtamuuliza hilo yeye mwenyewe, kama atakuwa na kumbukumbu, maana huyo sijui....ila ninachotaka kuwaonyesha hapa ni muone jinsi gani tulilipangilia hili tukio kitaalamu.


‘Mdada anaingia chumba alichoambiwa anamkuta pacha….sio pacha wa kuzaliwa bali ni pacha wa sura, akashika na mshangao, ni kama anajiangalia yeye kwenye kiyoo…na hakupewa muda, mimi nilikuwa nyuma ya mlango nikasogea nikamweka kitambaa puani kutokea nyuma,na kitambaa hicho kilikuwa na dawa ya kumlewesha na kumtoa fahamu za kibinadamu, na kutokea hapo akawa hayupo kwenye hii dunia.


Yule mdada pacha wake, akatoka sasa akiwa kashika dawa, za maumivu ya kichwa, akakutana na ndugu yake wakaondoka kurudi nyumbani…huyu sasa alipewa aina fulani ya dawa, ni sumu, lakini sio sumu ya kuua moja kwa moja, ni sumu ya kumuonyesha mtu kuwa amekufa..lakini akirudi kwetu kuna dawa tunampa inaondoa ile sumu anarudi tena kwenye hali yake ya kawaida.


‘Binti kafa, bint kajiua..ikaenda zaidi kama tulivypanga, ..kajiua kwasababu mpenzi wake kamkana…na…huko hospitalini, kulikuwa na watu wetu, vipimo vikaonyesha huyo binti alikuwa na mimba..hahaha, huyo binti hakuwa na mimba,ila kwa mbinu zetu, tulimuwekea kitu, mtu akipima anaona kuwa ana mimba, …lakini hakuwa na mimba,


‘Na zaidi binti wa huyo mama, hajawahi kutembea kimapenzi na huyo mchumba wake, muulizeni mwenyewe, huyo msaidizi wa docta,..atawaambia,…na uzushi huo unatokea wakati huyo binti ni marehemu, usoni mwa watu, kwahiyo hakukuwa na mtu wakumuuliza ili aseme ukweli…, umbea ukasambaa, na lengo letu likatimia, na mtu wetu tuliyemtaka sasa akawa mikononi mwetu…kazi ya kwanza kubwa ikakamilika.


‘Unajua ni kwanini tulitaka kumpata huyu binti, kwanza ni kwa ajili ya kisasi, hili lipo wazi, mtasema huyo binti anahusikanaje, sisi tulihusikanaje mpaka tunaswekwa jela…,..lakini zaidi ni baada ya kutambua umuhimu wa hivyo vifaa vitatu,..na zaidi matambiko yote, yalihitajia damu, na damu iliyohitajika ilikuwa ya kutoka kwenye familia husika,..na damu hasa iliyohitajika ni ya huyo binti, huyo binti alikuwa na …viasilia vyote vya mababu zake..


‘Kwahiyo kila tulipotaka kufanya tambiko, damu ya binti ikawa inachukuliwa…mambo yanijipa, lakini..bado kuna jambo lilitakiwa lifanyike,..kuvipata hivyo vitu vingine….bahati nzuri, yakatokea matukio ambayo, yaliwezesha hivyo vifaa virudi huku kwetu, hilo hatukufanya sisi…na hadi tunahangaika awali hatukujua kuwa vifaa hivyo vipo mikononi mwa huyo mzee, baba wa hao mabint, mume wa huyo mama..haya yalitokea tu..ila sisi tukacheza upande wetu, kuhakikisha kuwa, hivyo vifaa vinakuja kwetu…baada ya kuambiwa na huyo ndugu wa huyo mama kuwa vifaa hivyo sasa vipi mikononi mwa mume wake.


Sasa kabla ya hayo, tuliambiwa kuwa ili hilo zoezi likamilike, ni lazima atafuwe mtu,…mwenye damu sahihi, mwenye moyo..wa pendo kwa huyo binti, awe ni vinasaba vinavyoendana na huyo binti…ni kazi kubwa kumpata mtu kama huyo,

Tukabuni mbinu..kwa kutumia mtandao,kuanza kutafuta mtu kama huyo, akili ya mtu akiona sura tu, anaweza kuhisi kuwa huyu nampenda, na hisia hizo, zikienda mbali, bsi viasili hivyo vinakuwa vimeivana,..


Ilichukua muda kidogo, lakini baadae tukafanikiwa, mpenzi wa facebook, akamnasa mtu,…na mtu aliyemnasa ni yule yule mpenzi wa zamani wa huyo mdada, kumbe kweli,.. tukaja kugundua kuwa mpenzi wa binti, yule yule ana viasilia sahihi, ..na zaidi watu hao wanapendana, na wakikutana wanaweza kuoana, hata bila hata ya kutumia uchawi wetu..mungu atupe nini..


Tulipompata huyu mtu, tukaanza kazi ya kuingia kwenye kichwa chake kwa kumtumia shetani,….tukamvuta tukawa sasa tunasoma hisia zake,..ni uchawi , lakini uchawi wetu wa kisayansi,….tumeshampata sawa, sasa atajileta vipi, ndio hapo sasa tukamtumia shetani wetu…mpenzi wa facebook..



‘Mtajiuliza shetani ataingizwaje kwenye mtandao, ..hahaha, kwani shetani ni nani,..hapo tumieni akili zenu vyema, kwani shetani ni lazima awe shetani kama shetani, au matendo ya mtu yanaweza kumfanya mtu akawa ni shetani,… shetani anaweza akawa mtu kutokana na matendo yake, watu hufanya mambo ya kishetani zaidi ya shetani mwenyewe…kwanini tushindwe kulifanya hilo…hilo linafanyika hata bila kutumia uchawi..ni akili tu..


‘Mpenzi a facebook akatengenezwa akaingizwa kwenye facebook, na bila kukosea, akakutana na mlengwa,…sura ikamvuta jamaa, na sisi tukawekeza mambo yetu, jamaa akawa hoi..halali, hali, hanywi…huyu hajanyweshwa limbatwa, tunacheza na akili yake tu,…huyu akawa kalogewa akawa anachati hadi kwenye usingizi , akiwa usingizini anakutana na sisi, tunazidi kumuharibu…mpaka leo mpenzi huyo yupo kichwani kwa jamaa, muulizeni kama natania..


‘Mapenzi ni kitu cha ajabu sana, sisi tuliligundua hilo, tukawa tunatumia madhaifiu hayoi ya kibinadamu ya kupenda .. kuwanasa watu wetu, wangapi tuliwatengenezea ugoni,..ili tuwapate, ili waje kuogopa, maana tukionyesha mapicha hayo mabaya ya ugoni wao, kwa wenza wao, watavunja ndoa zao…ni ushetani ulitengezwa..na akili za watu hunaswa zaidi kwenye shetani huyo wa mapenzi.


Mpenzi wa facebook, akafanya kazi, yake,…matukio yaliyofuata sasa, ni michezo yetu, tukamuita, hadi makaburini, ambapo tulipanga tumnase, lakini nyota ya huyu mtu, ..ogopeni sana mcha mungu, mtu anaweza kuwa mcha mungu kutoka moyoni, lakini msimuone kama ni mcha mungu, anakuwa na imani kweli ya mungu wake..hebu fikiria, tokea ashutumiwe kuwa yeye ndiye chanzo cha huyo binti kuwa alimpa mimba, aliwahi kusema sijawahi kutembea na huyo binti…?.


‘Ni kwanini mpaka leo hajasema hivyo…hahaha, huyu ni mtu aliyeiva kiimani, aliogopa kusema hayo, akamuachia mungu, ..muulizeni, kama nasema uwongo, yeye alisema mungu wewe ndiye unajua ukweli wa haya yote, na siku huyo mpenzi wangu ananifuma, sikuwahi kutembea na huyo mwanamke aliyenikuta naye, ila sijui ilitokeaje…na mpaka leo najuta, je iweje nisingiziwe mimba, ..sitaweza kulisema hili kwa watu, nakuachia wewe mungu wangu…



‘Muulizeni hakuyasema haya akiwa peke yake akimuomba mungu wake,..sasa huyu ni mcha mungu wa kweli, lakini usoni kwa watu hajulikani..na hataki kujionyesha kihivyo, yeye aliweka kipaumbele chake cha kutokuogopa, na hiyo ni pia ilimsaidia sana kama kinga zake ambazo, zilitufanya tushindwe kumpata kwa haraka…, maana ili mashetani yetu yaingie kwenye akili za watu ni mpaka..huyo mtu tumjaze hofu..huyu jamaa ana ujasiri wa ajabu, hajengeki na hofu harakai,…’akatulia


‘Lakini sisa hatukata tamaa, tukawa tunamlewesha kwa namna nyingine nyingine, na kama angeliwahi kuingia kwenye lile pango mapema,…kwa kupitia lile kaburi, tungelishamaliza kazi yetu,..lakini haikuwezekana hivyo…na..na ok…’akashika kifuani, kuashiria anahisi maumivu.


‘Tunamshukuru sana mzee Kigagula, mzee huyo ndiye aliyetuwezesha mambo mengi ya nguvu za giza, lakini ikafika mahali, tukagundua akiendelea kuwepo, nguvu zake za giza zitatugeukia na sisi, maana yeye kila jambo kafara la mtu, kila jambo..kafara kafara, mpaka lini, tukaona huyu hatufai tena, kwanza uhakika wa kuvipata hivyo vitu umeshakamilika, huyo mzee wa nini, hakuwa na umuhimu kwetu, ….


‘Kwahiyo alipotuletea mtu wetu ndani ya pango, tukaona basi yeye, arejee kwa mizimu yake, iliyokuwa ikimsubiria kwa hamu, hatukuweza kumlinda, maana pamoja na mambo yake, sisi tuliweza kumlinda na mizimu yake ambayo ilishataka kummaliza yeye mwenyewe kwa kuvunja baadhi ya masharti, ambayo anayajua yeye mwenyewe.


‘Ndugu zanguni…haya mambo, hatukuyafanya kwa kupenda, narudia, tena sio kila mtu anayefanya mabaya, ni mbaya, kuna wengine wameshinikizwa, kutokana na madhila waliyokutana nayo,..watu wanateseka kizazi kwa kizazi, watu wanateswa familia zao, kila siku watoto wanaumwa, wanapata matatizo mbali mbali, wanafukuzwa shule, watoto wanafelishwa majina yao yanachukuliwa na watu wengine, haya hamyaoni….


Wapo watu..wanafanyiwa mabaya mengi tu…wengine wanafungwa hata bila kosa, na huko jela wanakutana na matatizo, huku nyuma familia zao zinataabika, wananyang’anywa kila kitu, watoto wanaishia kuwa machokoraa, wakati wazazi wake walikuwa na mali… na huyo mtu aliyewafanyia hivyo,yupo, anatesa..anaishi maisha ya raha,..hivi wewe ukitoka huko jela utakuwa na moyo wa jiwe wa kusamehe…sijui, labda sisi tuliumbwa na mioyo ya kishetani…’hapo akatulia na hakimu alikuwa katulia tu.


‘Ndugu hakimu,…sijui kama nimeweza kuwajibu ni kwanini hata mimi niliingia huko, sitaki kuelezea mengi kuhusu machungu niliyopitia, yanaumiza, na nikianza kuyaelezea hapa, nahisi nitegeuka kuwa mnyama,…na kila mara nikiwazia huko nageuka kuwa mnyama…ila wewe chukulia mfano mmoja tu, ulizaliwa ukiwa kamili, mwanaume kamili, unafikia mahali watu wanakufanyia mambo, mpaka unakuwa sio mwanaume kamili…unadhalilishwa, unaumizwa, nyie acheni…sitaki niongee huko zaidi..


‘Ila nawaambieni hapa wazi wazi, walionifanyia hivyo, wote waliyapata yale yale waliyonifanyia, mimi, ..na kama wangeliweza kuja kuongea hapa, mungewaonea huruma, lakini inafikia mahali unajiuliza, ni nani aliyesabisha haya yote, huyo nay eye, na kizazi chake inabidi wawajibike…ooh, aaah…nahisi hapa..ndi-ndi… ndio nafikia mwisho..nahisi muda umefika,…’akashika kifuani.


‘Kwahiyo wewe ulijiunga na kundi hilo kwa vile ulizalilishwa, ..na sasa ni kwanini uilenge hiyo familia, ni kwanini, kwani wao ndio walikufanyia hivyo…?’ akaulizwa, na jamaa akasema;


‘Una-una-jua ni kwanini nilicheka awali…hahahaha, nilicheka kwa vile hata ndugu yangu mwenyewe hakuweza kunitambua mimi ninani, …, kwa jinsi nilivyoweza kujibadili, mi-mi..eeh,..sina kawaida hiyo nikikutana naye…ananijua, lakini ….mlinikamata nikiwa nimejibadili, sikuweza kupata nafasi ya kutokelezea, alivyonizoea….’akashika kifuani, akaanza kuonyesha dalili zile zile za mshitakiwa namba mbili.


‘Kwahiyo wewe ni nani…?’ akaulizwa.


‘Mi-mi.. ndi-ndi-ye pacha wa mshitakiwa namba ..mbili, huyo ni pacha mwenza, na, na…ndio maana, ohhhhh…’akatoa maneno hayo na kuporomoka, akadondoka chini.



NB: Mpaka hapo kisa kimekwisha, yaliyobakia ni nini kilitokea baadae….tutaileta sehemu hiyo kama sehemu ya kumalizia, kama mtapenda.


WAZO LA LEO: Sio kile mkosaji ni mtenda makosa, wakati mwingine mtu hutenda kosa, kutokana na madhila aliyoyapata, ndio maana wenzetu wazungu, mtu akitenda kosa lisilokuwa na kawaida kwanza wanampima akili yake…Kwahiyo kwenye jamii, hasa kwa watoto wetu, tusikimbilie kuadhibu tu, kushutumu tu, kutukana tu, tujaribu kuchunguza, na kuwa washauri nasaha, huenda kosa hilo lina sababu yake muhimu. Tumuombe mungu atujalie tuwe wenye tabia njema, kwani tabia njema, ndio huleta upendo, amani na furaha kwenye maisha yetu.
Ni mimi: emu-three

No comments :