Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, June 3, 2017

MPENZI WA FACEBOOK-43



‘Yupo humu ndani ya mahakama, ..hajatoka, nahisi yeye ndio kavichukua hivyo vitu,…sikuwahi kumuona, nimefika na kukuta askari wakifanya vitu vyao, nahisi hata wao, hawajui ni nani kavichukua…

‘Sasa fanyeni hivi, kabla ya kumuua, ni bora kuvipata hivyo vitu kwanza, …na msaidizi wake ..ndio yule msaidizi wake, atakwua ndio yeye, kavichukua, lakini hanavyo,…yeye, …ndio….yupo nje ya mahakama,…hajaingia huku, sijui kama wameweza kum-maliza…ndio … naona bora na yeye amalizwe ili tubakiwe na watu wachache …

Ilikuwa sauti ya huyo mzee, ndio akilini nikajiuliza kumbe na huyu mzee naye yumo

**************
‘Kama huamini, eeh,…basi mimi na wewe mguu kwa mguu twende huko…najua hapa huruhusiwi kuondoa, mpo kwenye ulinzi, au sio..kwa usalama wenu, au sio, hivi mikitoka hapa mnapelekwa wapi..?’ akauliza

‘Mimi sijui,..leo hapa kesho kule..sina uhakika kuwa tutakwenda wapi, lakini huenda leo wakaturuhusu tukaenda majumbani kwetu..’nikasema

‘Kama itakuwa hivyo, itakuwa ni vyema sana,…mimi na wewe tutakwenda huko, lakini kwa sharti moja….najua huenda usiamini, lakini utaamini tukifika huko,…’akasema huyo mzee.

‘Huyu mzee anataka nini kwangu..’nikajiuliza kichwani, kabla sijamuuliza swali kuwa hilo ni sharu gani.. kichwani nikawa nazingirwa na kauli yake hii:

' Unajua nimegundua kitu,kumbe yule msichana hajafa..yupo hai..

Unajua hayo matukio yote, yamegubikwa na ushirikina, sasa kama nilivyosikia, huyo bint hakufa...kuna mazingaumbwe yalichezwa…’

Tuendelee na kisa chetu

*************

 'Kwa vipi, na sharti gani hilo….?’ Nikauliza sasa nikikumbuka maneno yake aliyokuwa akiongea kwenye simu,(… Sasa fanyeni hivi, kabla ya kumuua, ni bora kuvipata hivyo vitu kwanza, …….naona bora na yeye amalizwe ili tubakiwe na watu wachache …’)
Japokuwa kwa sasa huyu mzee anasema alifanya hivyo, kwa vile anataka kuwatega hao watu ili waje kunaswa na polisi.

 'Nitakuambia ilivyo,… lakini  kwanza nikuulize,…. unajua mimi ni mjumbe wa nyumba kumi, kwenye eno langu na sasa nilikuwa nataka kugombea udiwani…?’ akaniuliza.

‘Mimi hayo siyajui mzee…’nikajibu hivyo, nikijiuliza kichwani hilo linakujaje hapo, lakini akilini nikasema ngoja niende naye taratibu, maana hawa watu ni wajanja sana.

‘Ili nipate kura, ili wananchi wanikubali ni lazima nionyeshe juhudi zangu ,na moja ya juhudi zangu ni kuhakikisha matatizo kama haya, yanaondoka…nitaonyeshaje hilo, kama nisiposhikirikiana na polisi, kwahiyo,..nataka na wewe iwe siri yako, kama nilivyoongea na polisi kuwa nitashirikiana nao, lakini sitaki nijulikane..umenielewa hapo…?’ akaniuliza akiniangalia machoni moja kwa moja.

Nikakumbuka kauli ya docta, kuwa watu hawa hutumia macho, kama njia ya kukuteka akili, akikuangalia sana na wewe ukamuangalia, anakuteka akili na anakuja kujua unachofikiria,…au unavutwa na hisia zake…

Hapa nikaminya macho kama simuangalii…akatikisa kichwa kama kukubali, halafu mimi nikasema;

‘Hebu nifafanulie maana mzee, mimi sijakuelewa unachotaka ni nini  kwangu, sawa ulitaka ukutane na mimi, kuhusu huyo mtoto…huyo binti wa mzee au sio…., ambaye sisi sote tunafahamu kuwa ni marehemu….ila wewe….’nikasema, na yeye akanikatisha kwa kusema;

‘Ndio hivyo, hiyo ni siri,…na hata polisi hilo sijawaambia, ni kwanini unajua,… kwasababu bado sijaweza kukusanya ushahidi wa kutosha, naweza kuwaambia hivyo, wakaingiwa na kimuhe muhe cha kutaka kuona, si unajua polisi walivyo, wanapenda kutumia nguvu …sasa hao watu wakifahamu,….maana hao watu sio mchezo, wana viona mbali, hata hapa tunapooongea sijapaamini…’akasema akigeuka huko na huko.

‘Lakini hapa ni mahakamani, kunalindwa, na kila mtu anapaheshimu, sizani kama kuna mtu anaweza kuja kuweka vitu vyake humu…’nikasema.

‘Umesema kweli…lakini huwezi jua,…sasa ni hivi, sio jana na juzi, siku hizi uchawi upo hadi kwenye mitandao, unaweza kuamini hilo…’akawa kama ananiuliza huku akitafuta macho yangu.

‘Sasa ni hivi… unielewe sana vyema…, kwa vile mimi nataka kuwa kiongozi, nataka watu wakunisaidia mambo fulani fulani, ya kampeni , si unajua tena, na mbinu za kisiasa…eeh! Mbinu za kisiasa bwana.., zinatakiwa uume na kupuliza..huku ujifanye upo, na huku unapalilia unga wako…hapo nafikiri nimekuacha mbali…au sio’akasema

‘Sana…bado sijakuelewa mzee…’nikasema sasa nikiangalia pembeni, na yeye akaangalia huko kwa mashaka.

‘Mbinu yangu ni hii, mimi ni mtu wa serikali, unasikia sana....sasa ili nipate faida kwa ajili ya-serikali, kwa ajili ya- watu-wangu, …na, na…kwa ajili ya kufanikiwa kwenye kupata kura…hahaha, kula….wengine wanasema hivyo…, natakiwa nifanye kama ulivyosikia, nikiwadanganya, sio  kweli..mimi sio mnyama kiasi hicho..ni mbinu, ili waje..eeh, waingie mkenge…’akatulia halafu kama ananinong’oneza akasema;

‘Natakiwa niwe na mawasiliano na hao watu nijue wanachokifanya na huku upande mwingine,..natafuta kula yangu…unga wangu baba, mjini hapa, umenielewa eeh…’akasogea kama kunikaribia, halafu akatulia na badae akasema;

‘Unielewe hapo, huko nafanya hadaa, …..huku kwenue jamii, nahakikisha wapo salama, na kuwa kwao salama eeh, ni kushirikian na polisi,…umeona hapo…’akatulia akinikagua machoni, nahisi aliona kama simuamini au kuna jambo halimuendei vyema, halafu akasema;

‘Lakini wakati huo huo,… sitaki kuwapoteza wafuasi wangu,…lakini hebu ona hapo, baadhi ya wafuasi wangu, eeh,…ni wahalifu…unaona ilivyo ngumu hapo..sasa natakiwa nitumie akili ya hali ya juu, nisiwapoteze, kwa wao kujua kuwa nawatekeleza kwa polisi,….nakuwa upande wa hao watu..kinamna…, ili niwachote akili, na wakati huo huo….nipo karibu na nani…’akatulia kama ananiuliza.

"Lakini mzee watu gani hao…." maana unatumia neno watu, watu… nahisi unawafahamu hao watu ..ni watu gani hao..?’ nikamuuliza

'Ni hao wahalifu…’akasema kwa sauti ya kunong’ona, halafu akaendelea kuongea;

‘Lakini ..tatizo ni hilo..hao watu hawajulikani ni akina nani…., kwasababu hakuna ushahidi wa kuthibitisha uhalaifu wao,…sasa mimi ni mjanja,..nautafuta huo ushahidi kwa namna yangu,…nitaupataje huo  kivyangu, eeh,..mimi hapo ndio natumia mbinu za kiraia…mbinu na kupuliza na kuuma….unaona nilivyo mjanja, kufanya nini, kuuma, na kupuliza, umenielewa…ndio hivyo…’akasema

 'Sawa nimekuelewa mzee, sasa niambie kuhusu huyo binti…., unasema hajafa kwa vipi, wakati akizikwa na wewe ulikuwepo,…si ulihudhuria mazishi yake, au sio… ukashuhudia mazishi yake, kwa macho yako, …. iweje sasa aonekane yupo hai..?’ nikamuuliza.

‘Hapo sasa..eeh, … ndio nataka ukubaliane na masharti yangu, ili twende sana, unajua mimi ni mzee, nimeona mengi na ninajua mengi, nyie vijana mnakurupuka tu…mlitakiwa mkae na watu kama sisi, muelewe dunia inavyokwenda kwanza..….umenielewa…’akasema akijaribu kuniangalia machoni,lakini nikawa mjanja, nikawa natumia mbinu za kumkwepa….nikasema.

‘Nikubaliane na masharti gani zaidi mzee….?’ Nikauliza

‘Kwanza,..tukubaliane hili, kama umenielewa vyema, nataka… hili… li-we-siri, kati yangu mimi na wewe….unasikia, mimi-na-wewe, asijue mtu mwingine..hata huyo docta wako, eeh, si unamuamini sana, lakini kwa hili, unisikie sana na unielewe, nata yeye asilijue hili kwanza, utakuja kumuambia baadae, baada..!Hivi nikuulize kitu, hivi wewe unamuamini sana huyo docta wako…?’ akauliza akiniangalia kwa macho ya udadisi

‘Kwanza mzee, hapo mimi unanitia mashaka….’nikasema

‘Kwa vipi tena, si umesema umenielewa au ?’ akauliza

‘Nimekuelewa ndio..lakini…huo usiri unaoutaka wewe, sijakuelewa kwanini uwe usiri hadi , hata kwa docta,..….sawa naweza kufanya hivyo, lakini sasa…kwanini hata docta, najiuliza sana hapo…unajua docta ni ndugu yangu,….’nikasema

‘Ndugu ndugu..hahaha, mimi nimeshuhudia ndugu wanauana, sababu ya mali, sababu ya vitu vidogo tu….wewe niamini mimi..najua, na nimeshamjua yeye ni nani….unasikia sana, kwasasa huwezi kuamini, lakini utakuja kunikumbuka…’akasema

‘Kwani docta ana nini, mpaka nisimuamini, nimeshakuambia yule ni kama ndugu yangu….yeye ni mimi, tumetoka mbali…’nikasema

‘Hahahaha..yule jamaa mjanja sana,..unajua kila mtu anayeingia hapa kwenye huu mji wangu,…maana mimi ni aliwatani, nimezaliwa hapa nimekulia hapa, nazeekea hapa, na huenda nikafia hapa, ya mungu mengi,..ndio maana watu wameniamini na kunichagua mimi kuwa kiongozi wao wa eneo lile…kama mjumbe, sio huku, huku kuna watu wengine, unajua ni …kwanini…’akawa kama ananiuliza

‘Ni, kwasababu najua mengi,..masikio yangu yamesikia mengi na macho yangu yameona mengi..na akili yangu ….ipo bara bara…hekima, na ufahamu, …sasa kuhusu eneo hili nalijua awali hadi sasa..kule ninapoishi napajua mwanzo mwisho…, na kitu cha mumimu..mimi nina hekima ya uongozi….shule. eeh,...’ hapa akashika kichwa, halafu akasema

‘Ukiguzia kuhus shule, kuwa nimesoma hadi wapi,..ndio nimesoma, sio saana…lakini akili ninayo…maana nimepitia hata uaskari,..huyo mzee mwenye..rafiki yangu, eeh, wanamuandama sana…tuli..niliwahi kumpangisha, namjua sana…ni rafiki yangu, namuonea huruma sana..lakini wakati mwingine yeye ni mbishi, hanielewi…sasa ndio hivyo, yatakwisha tu…’akatulia alipoona askari wanapita.

‘Hawa watu,..’akasema akinielekezea kwa kichwa…

‘Eeeh, wakati mwingine.. unatakiwa uwe makini nao,..ni watu wetu, vijana wetu,...lakini wakati mwingine hawaaminiki…’akasema alipoona namshangaa kwa kitendo chake cha kuwaangalia askari kama anaogopa vile.

‘Sasa tusipoteze muda, upo tayari kwa masharti yangu…’akasema sasa alipoona hao askari wamepita.

‘Yapi hayo..?’ nikamuuliza

‘Kwanza na la muhimu, iwe siri , kati yangu mimi na wewe, pili..wewe siunataka kuonana na huyo mrembo, eeh, ujana una mambo yake bwana nakumbuka enzi yangu, nilikuwa hivyo, ..na yule binti..alikuwa mnzuri..ni mnzuri..sasa wewe si unataka kuonana naye,ili uhakikishe niliyokuambia au sio…wewe na mimi…, tufuatane, ili nikuonyeshe hapo nilipomuona huyo binti, sio ndio hivyo…’akasema

‘Una uhakika mzee…?’ nikamuuliza

‘Uhakika uhakika gani…utaupata mimi na wewe tukiona kwa macho yetu…ila naona vyema ili kuyaweka haya sawa…muhimu kwanza tukutane ….eneo la siri. Sio hapa….’akasema.

‘Wapi..?’ nikamuuliza, na yeye akageuka huku na kule kama ana wasiwasi na jambo fulani.

‘Kule makaburini…’akasema sasa akageuka kuangalia upande mmoja, askari walikuwa wakikagua watu, na yeye akaonekana kama hana amani….akasema;

‘Umesikia, si umenielewa eeh,naona muda,..unajua muda ni muhimu sana, na naona hao jamaa wanatekeleza wajibu wao,..sasa…basi, mimi naondoka, eeh…’akasema sasa akiinu amguu kuondoka.

‘Sikiliza wewe… ukiwa tayari nipigie, tukutane huko,..nilipokuambia… na kumbuka niliyokuambia,..hilo ni mimi na wewe, sawa… ‘akawa kama kasahau kitu akageuka kuniambia.

‘Umsikia,…na hayo, uliyosikia, usimwambia mtu, …maana ukimwambi amtu, umevuruga upelelezi wangu, na jingine uwe makini na docta, yule ana ajenda ya siri, ya kutaka kukutumia ili afanikiwe mambo yake…hilo, tukikutana tena nitakuambia,..ila..sasa ukifungua mdomo,..shauri lako…’akasema na kutabasamu, na kuna kitu nilikiona kwenye macho ya huyu mzee, ana kitu kama makengeza, lakini sio makengeza..ukiyaangalia unahisi mwili kusisimuka, lakini kwa vile nina asili ya kutokuogopa niliona kama ya kawaida.

‘Kwaheri…’akasema na kuondoka kwa mwendo wa haraka huku kainamisha kichwa chini , kama vile hataki mtu amtambe.

***********

‘Docta, docta,..docta….’nikawa sasa natamka hivyo, mara kadhaa, huku nikimuangalia yule mlinzi,..alikuwa sasa anakoroma, nikajua sasa kalala..wakati huo namuwaza docta kwa kitendo kile lichokifanya …ilikuwa kama ananitelekeza, japokuwa awali alionyesha kunijali sana…

Kwanza vitendo vya huyu mtu nashindwa kumuelewa…ana mambo ya siri siri mengi… , sasa naanza kuingiwa na mashaka,…sio kwamba namuwaza hivyo kutokana na maneno ya huyu mzee, hapana, …

Lakini kwa jinsi alivyoweza kufanya mambo kama askari, basi hata kama ni docta, lakini atakuwa ni askari, ungemuona alivyofanya pale…alivyoweza kukwepa zile risasi, na kuniokoa na mimi..mmh, sawa..yawezekana ni hawa maaskari kanzu..'niliwazia hivyo,

‘Kwa jinsi alivyofanya pale alipokuja kuchukua vile vifaa, bastola na ule ufunguo wa ajabu,…kweli sio mtu wa kawaida, sio raia yule..atakuwa ni njagu…’nikasema kwa suti ndogo.

 Ile sauti ya amri…lala chini, ..geuka..inuka, geuka kule..fanya hivi… hivi..nk….zile n amri za kijeshi,….’ kiukweli aliokoa maisha yangu…lakini sasa baada ya kuona askari wanakuja, ambao badae mimi niligundua kuwa sio askari hasa, na kama ni askari hasa basi ndio hao wanaotumiwa na hao watu..pale akaniacha njia panda..

 ‘Aliniacha njia panda ndio…’

Na kwa jinsi alivyoniacha….akatahamini vile vitu zaidi ya uhai wangu, vile vitu vina thamani gani.eeh,…’ ni kwanini vile vifaa vilipofika mikononi mwake, vikawa ni muhimu sana kuliko maisha yangu.’  Eeh…akaniacha mikononi mwa adui, ili eti akavifiche hivyo vitu…hapa kuna jambo sijalijua, hapa kuna ajenda ya siri, na hapa naungana na mzee, kuwa docta ana jambo,…’nikawaza hivyo na kutikisa kichwa kukubaliana na hilo wazo.

 Hapo na mimi nikaingiwa na mawazo ya kufanya utafiti wangu, …docta alinituma kwa njia zake nikafanikiwa, …na ndio nikaweza kumfunga yule mtu kamba..na sijui huyo mtu kama bado yupo pale, au la,..huyu mtu anaweza akawa ndio kiongozi wa hili kundi, na kama ndio yeye,  kiongozi basi, atakuwa anafahamu….kuhusu….mmh, ..kwanza

‘Mpenzi wa facebook…’ huyo kwangu ndio muhimu, hilo la mzee kuwa huyo binti wa mzee yupo hai,..haliniingi akilini,..hivi  kweli yawezekana huyo mpenzi wa facebook, akawa huyo binti..hapana, ..hapana…

‘Mpenzi wa facebook….’ Hapo nikatamka kwa sauti kidogo, na nilipogundua nimetamka hivyo nikainua kichwa kumuangalia yule askari..alikuwa sasa kalala, …sina shakana hilo, sasa nifanyeje..nikajiuliza

‘Lazima niende kule kwa yule mtu…nina uhakika yeye atanisaidia kumpata mpenzi wangu wa facebook….kama mzee anasema kweli basi nitaweza kumuokoa huyo mpenzi wa facebook…yes kumuoko,…, kutoka kwa hawa jamaa,…haina haja hata ya kumtumia huyo mzee, nitalifanya mimi mwenyewe.. ..nikishindwa , eeh, nikishindwa hapo, ndio..nitamtafuta huyo mzee..

‘Na kuhusu docta…?’ nikajiuliza

‘Huyo nitakuja kupambana naye baadae, najua nitagundua ukweli wake, kama yeye ni askari,au ana ajenda gani, kuhusu hivyo vitu, sawa…nilimsikia yule kiongozi wakati anapambana na yule mama, akisema kuwa hivyo vitu ni vya thamani sana..vina siri kubwa sana ndani yake…, lakini ..aah, hata sijaelewa, nitaelewa nikikutana na docta, lakini sio sasa, sasa hivi, nafanya mambo kivyavyangu..simuamini mtu tena..’nikawaza hivyo.

Nikasimama  na kuanza kutembea..nikitaka kutoka nje…

'Wewe unataka kwenda wapi...’ nikagwaya kumbe yule askari alikuwa makini, nikasema;

‘Nataka kufika nyumbani kwangu mara moja..mimi sio mfungwa, najua mnatuweka hapa kwa ajili ya usalama wetu, lakini kuna mambo binafsi, natakiwa kuyatatua,…usiwe na shaka na mimi, nitakwenda na kurudi mara moja..’nikasema

‘Huwezi kuondoka hapa, hii ni kwa usalama wenu..na ukiondoka hapa nitakuwa nimevunja amri…unasikia, kama kuna kitu, ukisema atatafutwa mtu wa kukifuatilia, unasikia…’akasema

 Sikutaka kubishana naye, nikarudi na kujifanya nimelala, na yule askari alipoona nimelala na yeye akaendelea kulala…nikachukua mto wangu nikawekeza kama mtu amelala,…hapo sasa, sikumpa muda..taratibu nikanyemelea,…. taratibu, nikatoka mle ndani,..

Nilipotoka nje tu, huyo nikajua usafiri wa haraka ni hizi bajaji zetu,..nikaipata moja..nikamwambia jamaa naenda wapi, na yeye bila kuuliza zaidi akawasha kibajaji chake mbio mbio tukaelekea huko, nilipomuelekeza…

 'Nitampata tu....mpenzi wangu wa facebook...'nikasema huku bajaji ikikari eneo hilo la makaburini…sikutaka afike karibu sana na eneo hilo nilijua lazima kutakuwa na walinzi au watu wanalinda, au kuchunguza eneo hilo…na bahati nzuri nikaona watu wanazika..na mimi huyo nikajifanya ni mmoja wao..

Nilishiriki kwenye hayo mazishi, nikasikia watu wakiongea mengi kuhusu eneo hilo, na mmojawapo akasema;

‘Nasikia humu kuna kundi limezuka, watu hao mkizika wanakuja kuchimbua makaburi, wanachukua sehemu ya miili ya watu…’akasema mmojawapo

‘Hao sasa ni wanga,…’akasema mwingine

‘Ndio hivyo,lakini hao sio wanga kama hao ninaowafahamu mimi, hao wanachukua vifaa wanauza…nasikia viungo vina bei kweli..’akasema

‘Huo ni uwongo, mtu keshakufa, damu haifanyi kazi, …labda useme ni wachawi wanatumia kwa mambo yao ya kichawi, na wachawi wanakula nyama za watu..mungu anawajua, na kifo chao kinakuwa kibaya we acha tu.…’akasema

Kukawa na malumbano kidogo, na kiongozi wa dini aliyekuwa akisimamia mazishi hayo akaanza kuongea na moja wapo ya maongezi yake akaliongelea hilo, na mwisho akasema;

‘Wapo watu wana imani potofu, wamejiingiza kwenye nguvu za giza, niwaambie kitu , nguvu hizo za giza kiongozi wake ni shetani, na shetani ni adui wa mungu, ukijiingiz huko ina maana umekuwa mfuasi wa shetani, umemuhalifu mwenyezimungu, mwenyezimungu hazuriki na hilo,…mwisho wako utafika utafika mikononi mwake.

Kwahiyo basi, sisi kama wanadamu tukumbuke kuwa duniani hapa ni mapito tu mwisho wake ni hapa, wangapi walitamani wawe hai, walikuwa na malengo mengi tu, wakajenga, wakawa matajiri, leo hii wapo wapi…angalia leo hii tumemzika mwenzetu,
hajaumwa, …ghafla tu , kafariki,… kesho au hata sasa hivi inawezekana ukawa ni wewe au mimi….sasa umejiaandaje kwa safari, hii….achanane na imani hizo za kishirikina,..’ akaendelea kuongea na mimi nikaona nichomoke hapo kiaina maana watu walishaanza kuondoka’.

Hilo kaburi la yule binti ambalo sasa nimegundua ni kaburi kwa juu, kumbe kwa ndani sio kaburi…lilikuwa limejificha kwenye miti…kwahiyo nilijifanya kama nakojoa, nikafika eneo hilo, na nikaanza kazi ya kuusukuma ile sehemu ya juu, haikuwa kazi rahisi, …na nikajitahidi sana baadae ikaanza kusogea, kidogo kidogo, kukaanza kuwa na uwazi..na ilipofikia sehemu ya kuweza kuingia, ..

‘Umekuja..nilijua utakuja, …’sauti iilishitua kutoka nyuma, na sijui ilikuwaje nilihis kama mwili unaisha nguvu.

NB; Ni nani huyo

WAZO LA LEO: Sasa hivi watu wangi wametekwa na imani za kishirikina, …kila kikitokea kitu, kuna mkono wa mtu, ni kwa vile ilikuwa hivi na hivi…na hata matajiri wengi wanatumia mbinu hizo kwenye utajiri wao..imefikia hatua watu wanadanganyika kuwa viungo vya wanadamu wenzao huleta utajiri, au wanajiunga na makundi yenye mlengo wa kishetani, kwa kutoa makafara ya damu za watu...


Jamani huo ni ushirikina na hizo ni njia za ibilisi, ukijiingiza huko umekuwa matumwa wa ibilisi, shetani aliyelaaniwa, na mwisho wa yote ni kuenda motoni. Jiulize waliokuwa magwiji wa mambo hayo wameishi milele,…haipo hiyo, kila mtu siku yake itafika,..na huko, zawadi, kitu cha kukusaidia ni matendo yako mema, na hayo mambo ya shetani, yatakuangamiza na adhabu yako itaanzia hapa hapa duniani. TUMUOMBE MUNGU, ATUJALI TUWE NA IMANI THABITI YA KUMUABUDU YEYE, NA SIVINGINEVYO..Aamin.
Ni mimi: emu-three

No comments :