Kuna mambo mengine ukihadithiwa unaweza kusema ni hadithi tu, au ni visa tu vya kutunga tu na wengine wanasema wewe unayaandika haya, umesaidia wangapi....kweli tuone tusiseme, kweli tumeona , tumesikia, tusiseme tukae kimia tu kwa vile hatuwezi kusaidia,..mimi naona kusaidia tuliojaliwa nako ndio huku kusema, kuyaelezea yale mabaya yanayotokea, huenda ikawa ndio sabau ya watu kubadilika...
Na haya wengine hawaamini,...kutokana na mitizamo mbali mbali...lakini hakuna aliyeomba,..labda tusuibiria, yatukute ndio tutaamini maana ndio hulka zetu, tunaamini kwa mifani, tunasaidiki kwa kuona, na ndio maana mabeberu wanatunga uwongo, ili kutupumbaza akili zetu, si ndivyo tunataka kwa mifano ndivyo wanadamu tulivyo, …watu wanafikia hata kutokumuamini mwenyezi-mungu
kiukweli kutoka moyoni, wanaamini tu mdomoni, mpaka wapatwe na mitihani mikubwa
ndio utamsikia mtu akisema mungu wangu nisaidie.
Wakati naliwazia hili, nikakumbuka kisa cha binti, ambaye
alikuwa mfanyakazi wa ndani, ambaye wakati ananihadithia kisa hiki, alikuwa
kambeba mtoto mgongoni, sasa ni mama mlezi,…hajui watakula nini, lakini
hajakata tamaa!
Nilimuangalia yule mtoto aliyembabe, akahisi ninataka kusema
nini, akatangulia kusema;
‘Sasa nina huyu mtoto, lakin mpaka sasa sijajua baba yake ni
nani…’akasema
‘Kwanini, kwani huyu mtoto ulimpataje..?’ nikamuuliza.
‘Mungu ndiye shahidi yangu kwa kauli hiyo…, maana hata
niongee nini, ni nani atanisikiliza, nimejionea nijinyamazie tu…, na kuna
kipindi nilitaka kwenda mahakamani, lakini nilichokipata nikasema basi tena..,
nimuachie mungu japokuwa duwa la kuku halimpati mwewe….’akasema aionyesha uso w
majonzi.
‘Kwanini usinisimulie kisa cha matatizo yako, huenda ikawa
ni sababu sio kwako wewe tu, bali na iwe ni sababu ya wengine kuliona hili
jambo kwa ukweli wake, kutoka kwako, maana kwa hivi sasa watu hawalijua au
sio..kama ulivyosema,…, na wanasema mengi ..si ndio hivyo, watu si wanasema mengi
ambayo sio sahihi kuhusu huyo mtoto..?’
‘Ni kweli, na sitaki tena kuwaambia lolote nimewaacha
waongee tu, lakin siri ya matatizo haya nayafahamu mimi mwenyewe, na nimeamua,
nitahangaika na huyu mtoto, mpaka atakua mkubwa.., na ipo siku ataniuliza baba
yangu ni nani, ndio hapo nitampa jibu ambalo hatalisahau..’ilikuwa kauli ya
huyo mdada, aliyekuwa mfanyakazi wa ndani.
‘Haya niambia ilikuwaje, …huyo mtoto ulimpataje, na baba
yake ni nani..?’ nikamuuliza.
‘Hivi uniamini….Nimeshakuambia baba yake mimi simjui,..hadi
hii leo, sio kwamba naongea hili kwa kuogopa kumtaja, hapana, naongea hivi kwa
vile kiukweli simjui hasa baba wa huyu mtoto ni nani….mungu mwenyewe ndiye anayemfahamu,
na huenda kafanya hivi ili iwe mtihani kwangu na kwa hao walionifanyia hivi…’akasema.
‘Hao waliokufanyia hivyo, ina maana ni wengi, labda
samahani,..walikubaka..au..?’ nikauliza
‘Walinibaka!!…Mhh,…hata sijui…nakuambia simjui,…na ..oh,
tuyaache tu…’akasema
‘Sawa labda unisimulia ilikuwaje,..’nikasema, na yeye
akaniangalia machoni, halafu akatizama chini, baadae akasema;
‘Naogopa sana kulisimulia hili,…nilitaka nije kumsimulia
huyu mtoto akikua,…najua yeye atakuja kuniamini, wengine hawataki kuniambi…waliniona
ni Malaya…niliipata kwa …wapiga debe , kama alivyosema huyo mama na mumewe….’akasema
‘Mama yulee, aliyekuchukua kwa mama yako na mumewe au sio…?’
nikamuuliza
‘Ndio….hata huwezi kuamini…yaani ni watu wema kabisa,…ukiwaona
wakiongea hivi, huwezi amini, na hata mimi sikuamini hilo mpaka siku …ulipotokea
huu mtihani…’akasema.
‘Sasa naanza kupata picha…huyo baba huyo anaweza kuwa baba
wa huyu mtoto au sio..?’ nikauliza.
‘Hapana….siwezi kumuhukumu huyo baba wa watu..sijui, kama
ningelijua ningelimtaja, kwanini nimfiche..lakini mama alinifundisha kitu,
nisiwe muongo, na nisiseme jambo kama sina uhakika nalo,….’akasema
‘Sawa, ….nimekuelewa.
‘Mimi nitakusimulia, kisa hiki, ..nimekusikia sana kwa jinsi
gani unavyoandika visa vyako vya kuwasaidia watu kama mimi, nitakusimulia kwa
sharti moja, usije kunitaja jina langu, au la hao walionitendea hivi..’akasema.
‘Hilo usijali,…’nikasema.
Kwanza akaanza kulia,…mmh, nikajiuliza kwanini tena, baada
ya kuongea anaanza kulia, na nikaona nimuache kwanza alie..huenda itasaidia
kumuondoa hicho kilichopo moyoni mwake, baadae akatulia, na kusema;
‘Jana alinitokea mama yangu, akaniuliza kwanini sijafanya
alichotaka nikifanye…’akaanza kusema hivyo.
‘Oh, alikutokea mama yako mzazi, kwa vipi..?’
‘Mimi ni yatima, sina baba wala mama, baba yangu alifariki
zamani kidogo, na baadae akaja kufariki mama, na tangia nianze matatizo mama
amekuwa akinitokea, akitaka nilipize kisasi kwa haya yaliyotokea kwangu na
kwake, lakini mimi mtu kama mimi nitafanya nini…’akasema.
‘Kwa vipi mama yako akutokee wakati alishafariki, … hizo si
ndoto tu, ..’nikasema.
‘Ni ndoto tu eeh!.. hahaha,..wewe unasema tu kwa vile
haijawahi kukutokea,…na kuna mambo aliwahi kunitokea akaniagiza, nikayafanya,
na ikafanikiwa, nilitaka ku…..itoa hii mimba, akanizuia, kwa namna ya ajabu
kabisa, siwezi hata kuamini..’akasema.
‘Unazidi kunipa hamasa ya kukisikia hiki kisa, …hebu tuanzie
awali kabisa, ilivyoanzia, tuanzie, eeh, huko kwa wazazi wako ilikuwaje.
‘Nitaanzia, pale nilipoagana na mama yangu,..huko kijijini,
siku ambayo alikuja, mama mmoja, yeye, ni mwenyeji huko kijijini kwetu…ila wao mungu amewajalia kuwa na uwezo, wamejaliwa
kuwa na maisha mazuri, huko kijijini na huku mjini halikadhalika, ..’akatuliza.
‘Basi huyo mama akaja kwa mama yangu kiwa hai, …huko kijijini
tunajulikana sisi kama masikini wa mwisho ..hata ndala hatuna, nilikuwa
natembea peku peku nikipita kuomba mitaani…, na siku alipofika huyo mama ndio
alininunulia ndala,..nashukuru, kwani alininunulia ..sio ndala, kwangu
nilikiona kama kiatu cha ufahari.., kwangu mimi nilikiona cha thamani kubwa
sana, haijawahi kutokea au kuvaliwa kwenye huu mguu wangu…na alimnunulia mama
pia.
‘Sasa mama nani hii,… nimekuja kukuomba jambo, najua nyie
mpo wawili tu, na huyu binti ndiye anakusaidia sana…lakini hata akikaa hapa
pembeni yako, anakusaidia nini, …’akasema akinitupia jicho.
‘Ndio hivyo, kuomba omba, mitaani, anachokipata ndio riziki
yetu tutafanyaje…’akasema.
‘Na hivi kile kishamba chenu vipi..?’ akauliza huyo mama.
‘Watu wanakitaka, …lakini tukikiuaza si ndio basi tena,baba
yake huyu binti yangu, alisema tusikiuze, kije kumsaidia huyu binti yetu,..lakini
inafikia mahali hatuwezi,..hapa naumwa, sina pesa ya dawa, ni huyu binti apite
pite mitaani akiomba ndio ..nipate dawa..’akasema kwa unyonge.
‘Sasa sikiliza, je
huyu binti akiondoka,…nataka akawe mfanyakazi wangu wa ndani, na atakuwa
akikutumia pesa za matumizi , unaonaje..?’ akauliza.
‘Oh, jamani…mimi nitaishije,..lakini kama atanitumia pesa za
matumizi,..si bora , kuliko kuomba omba hivi, sipendi kuomba, inaniumiza sana,
lakini nitafanyeje… basi ni heri…..’akasema akiniangalia mimi, sikuamini kama
mama angelikubali hivyo, walishafika watu wengi akawakatalia, sijui huyu mama
alikuwa na bahati gani.
‘Mimi nitakusaidia dawa, na nitakuachia pesa za matumizi,
kwa siku kadhaa.. na vyakula nimekuja navyo, nitakuachia, unga, maharage, ..na
mchele kidogo, vya kukusaidia siku kadhaa,..angalau uweze kupata chochote
wakati, huyu binti akiondoka, na kila mwisho wa mwezi huyo binti yako atakuwa
akikutumia chochote alichokipata, unaonaje..?’ akauliza.
Mama yangu alipoambiwa hivyo, akampigia magoti, huyo
mwanamke, kwa kumshukuru, na kweli akapewa vyakula, na pesa, na usoni mama
alionyesha ile furaha yake, ambayo sijawahi kuiona, japokuwa hiyo furaha yake, ilikatika pale aliponiona sasa naondoka
machoni kwake, aliniangalia kwa macho ya huzuni,..macho ambayo nayakumbuka hadi
leo,…macho ya kuniaga macho ambayo, yananijia kila mama akinitokea,…’akasema.
‘Yaani mama, sitakuona tena, zaidi ya kunijia kama ndoto…mpaka
leo nakuambia siamini..nahisi kama mama yangu yupo huko kijijini ananisubiria…’akasema.
Hapo huyo mwanadada akawa analia, na mtoto wake , ni mdogo
tu wa kukaa, hajaanza kutembea akawa anamfuta machozi, kile kitendo cha mtoto
mdogo kama yule kumuonea mama yake huruma na kumfuta machozi, kilifanya hata
mimi machozi yanilenge lenge., dunia hii jamani, kwanini…we yaache tu.
‘Sikujua kuwa siku ile mama ananiaga, na machozi yanamtoka,
akiniambia binti yangu nenda, maana huenda ndivyo mungu alivyotupangia, nenda
ukijua kuwa mimi mama yako nipoje, hapa nilipo ni masikini wa kutupwa…wa mfano,
na sina thamani yoyote hapa kijijini, ..na kila mtu akitaja umasikini
ananifananisha na mimi.
‘Binti yangu, huko unapokwenda ni mji wa watu una mitihani
mingi …,..sijui hawa watu wapoje, mimi nimeona uende nao tu, lakini moyo wangu unasita, nahisi,unakwenda
kwenye mitihani ya maisha, kwa umri uliofikia, wanadamu wasio wema, wanaweza
kukutia kwenye majaribu, ,,ila wewe nenda tu, muhimu mungu wako muweke mbele.
‘Sisi hatukuomba tuwe masikini,..likumbuke hilo, …ila
umasikini upo, na sisi ndio zawadi yetu, usije ukaenda huko ukinilaumu mimi,
kuwa mama, wazazi wangu ni uzembe wao….mimi nina imani kuwa umasikini wetu,
sehemu yetu ya maisha, na mungu ndiye aliyotupangia…..
‘Kila siku nalia…kwanini sisi…maisha yetu ndio hivyo, tokea
baba yako, atutoke, kila kitu kimeondoka, na maisha yetu yamekuwa,..ya jana ni
bora kuliko ya leo..leo hii kwa mara ya kwanza tutaweza kula chakula cha
kujipikia wenyewe…nataka nikupikie na mimi, ule chakula alichokupikia mama yako…’akasema.
‘Hapana hatuwezi kusubiria, yeye atakula huko mbele…’akasema
huyo mwanamke.
‘Mwanangu usije kunisahau,..na safari ni hatua, sijui
itakuwaje huko mbele, sijui itakuwaje ukiondoka nikabakia peke yangu, sijui…maana
hata hicho kidogo tulichopata, kuna wengine wanakitamani, unakumbuka jana
walituibia ile ndoo tuliyopewa, yaani hata sisi masikini wanatuibia,..’akasema .
‘Basi mama inatosha mimi sitakusahau mama yangu, nakupenda
sana mama yangu..’nikasema na yule mwanamke alikuwa akinisubiri…niende yeye
sasa alishatangulia kwenye gari lake.
Mama, akanishika mkono, akaniangalia machoni, akasema;
‘Kwaheri mwanangu,..nahisi kama sitakuona tena…’
‘Kwanini unasema hivyo mama…’nikasema sasa nikiingiwa na
wasiwasi.
‘Kwaheri mwanangu…’akasema na kuondoka kuingia kwenye
kibanda chetu, ambacho kilikuwa mbavu za mbwa.
.
Basi nikaingia kwenye gari la huyo mama, kwa mara ya kwanza
kuingia kwenye gari, nikawa nahangaika kumuangalia mama, lakini mama hakutoka
nje, na ikawa mwisho wa kuonana na mama yangu.
Kisa kipya kipya, je nikiendeleze.
WAZO LA LEO:
Masikini wapo, kama walivyo matajiri, haya yote sio kwa ujanja wetu, walijaliwa
wengi wanaona labda kuwa hivyo ni kwa ujanja wao, wangapi wangapi wanajitahidi
hawafanikiwi, au waliojaliwa wanakuja kukosa kabisa.., mola peke yake ndiye
anayejua ni kwanini akaweka hizi hali mbili. Ilivyo, kama alivyotuagiza
mwenyezimungu matajiri wanatakiwa wawasaidie masikini, na wawasaidia bila
kuwanyanyapaa, wawasaidie wakijua ni wajibu wao, na masikini wasiwaonee wivu
matajiri, kwani riziki zetu zimepangwa hivyo, muhimu ni kujitahidi,
tusijipweteke, kwani vyote hivyo vinapatikana kwa jitihada,..na kumtegemea
mungu!
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment