Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, June 30, 2017

DUWA LA KUKU....4



 Mimi nikakimbilia nje, kwa muda huo nilikuwa sijajitambua vyema, akili ipo kwenye ile hali kuwa baba mwenyenyumba alikuwa na dhamira mbaya dhidi yangu, ndivyo nilivyokuwa nafikiria hivyo, kwa wakati huo, lakini pia nilishaingiwa na woga kuwa mama mwenyenyumba hatanielewa,..atafikiria na mimi nilikuwa nina nia mbaya, kwa hali niliyokuwa nayo, nilianza kujilaumu kwanini sikuwa nimevaa vizuri, lakini ni kawaida wakiondoka navaa hivyo kwasababu ya joto, na kwa vile ninafahamu kipindi hicho huwa hakuna mtu.

Na nikamuona yule kijana akiingia getini, hapo nikaharakisha kukimbilia chumbani kwangu kabla hajaniona, niliona ajabu na yeye kwanini amewahi kurudi hivyo, ...baba karudi mapema, na halikadhalika mama, na sasa kijana, kuna nini leo, sikutaka kufikiria zaidi, nikakimbilia chumbani kwangu.

Kwakweli akili yangu ilikuwa imetekwa na mawazo hayo sikuwa nimefikiria jambo jingine, sikuwa na kumbukumbu za nyuma, hadi nilipofika huko nje, nikatulia kidogo, nikajikagua, ooh, hali niliyokuwa nayo, nilivyovaa, sio ya kuonekana na mtu, kwa haraka sasa nikageuka kuelekea ndani, hapo bado akili imeganda kwa tukio hilo.

Nilipofika ndani, nikavaa nguo zangu za heshima, na wakati navaa,ndio akili ikaanza kurejea mahali pale, na hapo ndio nikakumbuka ile barua, kwanza sikuamini, nikahisi labda ilikuwa ni ndoto, nilitaka iwe hivyo, iwe ni ndoto sio kweli,…unajua huwezi kuamini, kufiwa ni kitu kingine jamani, …

‘Haiwezekani, …kwanini , kwanini lakini, kwanini sisi, kwanini jamani, sisi tumewakosea nini hawa watu jamani, na umasikini huu tena, bado, mama yangu kawakosea nini jamani…’ hapo sikuweza kuvumilia tena nikaanza kuangusha kilio, kilio cha kwikwi,….nililia hadi kichwa kikaanza kuniuma, na sijui ilitokeaje, maana nilihisi giza usoni, na kulala sakafuni.

Nilizindukana mtu akinishika shika..nikakurupuka, na kusimama nikitaka kukimbia, lakini nikajikuta nikishikwa na mshangao, kwani aliyekuwa kasimama mbele yangu alikuwa ni mtu mgeni kwangu, ni mdada …mdada aliyekuwa kavalia vizuri tu, akaniangalia usoni, akatikisa kichwa kama kusitikia, akasema;

‘Oh, pole, sana…’ akasema akiniangalia kwa macho ya huruma, sikuweza kumjibu, machozi yakaanza kunitoka kama maji, akili haitaki kukubali, na japokuwa sikujua ananipa pole ya nini…lakini akilini nilihisi labda ananipa pole ya msiba, kama ni hivyo kajuaje…nikataka kumuuliza ila yeye akaanza kuongea;

‘Mimi nilikuwa mfanyakazi wa humu kipindi cha nyuma, najua nikwanini upo hivyo, ila mimi kwasasa nimekuja kuchukua mizigo yangu niliyoacha humu ndani natumai mama mwenye nyumba amekuambia …’akasema.

‘Kawaulize wenye nyumba, mimi sijui, naondoka zangu…’nikasema, sasa nikitaka kuanza kuchukua nguo zangu na kuondoka mbali kabisa na hiyo nyumba, sikujua nataka kwenda wapi.

‘Unaondoka,….!! Unataka kwenda wapi bibi wewe,…hahaha, naona umeshaanza kuionja joto ya jiwe au….! Nikuambie kitu, pambana na haki yako, …usikubali kushindwa, mimi niliondoka hapa kwa vile nilipata sehemu nyingine, vinginevyo, wangelinitambua mimi ni nani…’akasema akitikisa kichwa kwa majigambo.

‘Sasa kwanini uliamua kuondoka..?’ nikamuuliza hivyo, japokuwa sikutaka kuongea sana.

‘Kuna mengi yalitokea humu, ….nilivumilia sana, lakini ikafika muda, nikaona haina haja, hata hivyo, nilikuwa nimepata kazi sehemu nyingine,…ila kuishi humu inataka moyo,…kuna mambo mabaya sana humu ndani,…utajionea wewe mwenyewe…’akasema.

‘Kuna mambo gani…?’ nikamuuliza kwa mshangao, japokuwa nimekutana na mambo mambo..lakini kwangu mimi bado nilikuwa naamini ni ndoto tu.

‘Sijui mashetani, sijui….aah, utajionea wewe mwenyewe…’akasema na hapo nikakumbuka kale kakijitabu, nikajua huenda ni yeye alikiacha hicho kijitabu kidogo.

‘Kwani hayo mashetani yapoje, mimi siyajui………’nikamuuliza na yeye akaniangalia kwa macho ya kushangaa, halafu akaniuliza;

‘Kwani wewe umefika muda gani kwenye hii nyumba na je tangia uje humu huwa unalala kwa amani …?’ akaniuliza;

‘Mhh…sina amani kwakweli, lakini kwani hayo ni mashetani yapoje, yanaonakena, au…maana mimi nahisi kama naota tu, mtu ananikaba, ananifanyia mambo mabaya, ni hivyo tu…’nikasema.

‘Hahaha, wewe wa wapi,….mmh,… hayo ni majinamizi, na majinamizi kwa uelewa wako  ni nini…na baya zaidi, yanavyokufanyia vitu vibaya au sio…, si ukiamuka unajiona ni kweli umafanyiwa vitu vibaya, vibya kwa vipi,…?’ akaniuliza.

‘Aaah kwakweli mimi sijui kitu….’nikasema sikutaka kusema lolote, kwangu mimi bado niliamini ni ndoto, sikuwa na wazo jingine.

‘Hahaha, hujui kitu eeh…., ngoja ubebe mimba ndio hapo utajua kuwa sio ndoto..ni kweli, na ukibeba huo mzigo, utaanza kuina dunia, imeibeba wewe ….’akasema.

‘Mimba itaingiaje wewe, kupitia kwenye ndoto…’nikasema kwa mshangao.

‘Hahaha, ..hebu niondoke zangu naona naongea na mtu asiye-elewa, siku ukielewa utanitafuta….’akasema.

‘Mimi hata sijui…ni mtihani gani huu jamani, nimetoka kwetu nikijua nakuja kupata ahueni ya maisha, sasa tena nakutana na mambo haya,..sasa tena, mama yangu wamemuua…nitakwenda wapi mimi jamani , binti masikini…’nikasema.

‘Eti nini….!!!, wamemuua mama yako, akina nani hao…?’ akauliza kumbe alikuwa hajajua kwanini nipo na hali hiyo.

‘Nilikuwa sijui, walinificha, nimegundua baada ya kuona barua waliyoandikiwa, kutoka huko kijini..sijui kwanini walifanya hivyo…wangeniambia tu, angalau nihudhurie msiba wa mama yangu….nitawalaumu sana kwa hiki kitendo, ….ndio maana nataka niondoke kabisa humu ndani…’nikasema na kuendelea kulia.

‘Unajua hawa matajiri hawana moyo wa huruma kwa watu kama sisi,…wao kwa wao wanaoneana huruma kwa vile wanaweza kusaidiana, sasa wewe utamsaidia nini…., ndio wanaweza wakawa na huruma ya kujionyesha,…kwa vile…unanielewa hapo…., lakini kwa maswala yasiyowahusu, au kwa kuogopa sheria tu…ila kiukweli, kwa watu kama sisi, hawawezi kukutilia maanani hisia zako, kwao wao uwatimizie kazi zao tu, ..na ukiumwa, utaona watakavyokuchukia….’akasema.

‘Lakini kwani wao hawafiwi, hawaumwi…?’ nikamuuliza.

‘Wanafiwa, wanaumwa ten asana…, lakini wao si wao,…hisia zao kwao ni kwao, na kwa wengine hasa watu kama sisi, hawazijali sana, wanaju ukipewa ruhusa ya kwenda kwenu, utakaa huko mwezi, na nani atawafanyia kazi zao, na ukienda utwatia gharama, na gharama kwao, ni hasara, wewe utakuja kujionea tu….’akasema.

‘Lakini hawa watu hapa wanaonekana ni wema, wamekuwa wema kwangu, wamekuwa wakimtumia mama vyakula ....kiukweli mimi sijawahi kuona ubaya wao....kuachilia mbali haya yaliyotokea, na haya yametokea kwa bahati mbaya tu, mimi sikukusudia iwe hivyo…’nikasema.

'Yapi yaliyotokea...?' akaniuliza

'Aaah, ....'nikasema hivyo tu na yeye akasema;

‘Wema wanao, lakini …wema wao ni wa kumpatia ng’ombe majani ili upate maziwa, …chunga sana, humu ndani, utakutana na mambo mengi tu,…mimi niliondoka, ila…ipo siku, watanikumbuka…’akasema

‘Kwanini unasema hivyo…?’

‘Mimi nimetoka kwetu, nimeaga, walichonifanyia,…watakuja kunitafuta, …huo ni ujumbe kwao, kama utawaambia haya,…na umbea wako,… kama hutawaambia, yaache kama yalivyo, nimekuja kuchukua vitu vyangu, na kama hujaanza kupatwa na matatizo, basi, labda mwenzetu upo tofauti, lakini ..mimi ….nimekuja tu hapa kwa vile niliacha nguo zangu, vinginevyo, nisingelikanyaga tena hapa, mpaka wao wanitafute, najua watanitafuta tu….’akasema sasa akipanga vitu vyake vyema.

‘Utawafanya nini….?’ Nikauliza

‘Hahaha, nitawafanya nini, kama walivyonifanyia mimi, na wao nitawafanyia hivyo hivyo, na yoyote atakayekuwa upande wao, atakiona cha moto….’akasema.

'Kwani wao walikufanyia nini...maana ...?' nikauliza

'Mimi kwasasa sitaki kujiuliza uliza, humu kutawaka moto, yoyote aliye humu ndani atauonja ubaya wangu...sitakuwa na huruma na mtu ....mpaka moyo wangu ufurahi....'akasema

‘Ina maana….hata mimi…?’ nikauliza kwa mashaka.

‘Sikiliza ….nikuambie kitu, hapa kuna tatizo kubwa sana, siwezi kukuambia ni nani yupo nyuma ya haya matatizo, awali nilimshuku sana baba mwenye nyumba,…nilimtegea siku moja,…maana walijua mimi ni hivi hivi tu, baadae nikajiukuta nina mimba...aah, …lakini tuyaache kwanza, sitaki nikusimulie kwa hivi sasa kila kitu, muda utafika nitakusimulia, lakini sio kwa sasa hivi….’akatulia.

‘Lakini si umesema ni mashetani au…?’ nikauliza

‘Ndio ni mashetani, hujanielewa nikuambia mara ngapi….’akasema akiniangalia machoni.

‘Sasa hao watu, baba mwenyenyumba wanakujaje hapo?’ nikamuuliza.

‘Inawezekana wao wanayatumia, au wao wanajivika huo ushetani, au …hata sijui,ila mimi sijali kama ni wao au kuna mtu mwingine, hapa hapa nitapambana nao, nilipatia matatizo humu nikaharibiwa usichana wangu humu, nika...we aha tu, sitaki hata kusimulia tena, nashukuru kuwa leo nimefika na nimepaona vyema...'akaangalia huku na kule, na mimi sikusema neno, yeye akaendelea kuongea.

'Siku ..., nilipoondoka hapa....niliondoka na giza usoni,..nalia, nasononeka.....hakuna aliyenionea huruma,.... sasa nimekuja na macho yangu mawili, macho yenye nuru ya ukatili, unasikia, unyama unyama..…’akasema akiangalia huku na kule kama kukagua.

‘Oh….mungu wangu, sasa nitaishije humu ndani, mbona unaanza kunitisha…, kwanza mimi naondoka, mama yangu, kafa…mmh, mama yangu hayupo tena duniani masikini mie..nitakua mgeni wa nani…ooh, mama umeamua kuniacha mama…’hapo nikaanza kulia tena, hadi huyo msichana akanionea huruma.

‘Kwani mama yako alifarikije..?’ akaniuliza akiniangalia na machoni nilimuona na yeye akilengwa lengwa na machozi.

Nikamuelezea kama barua ilivyosema, halafu yeye akasema;

‘Nilisikia taarifa kama hiyo….mmh,  kuna mtu mmoja alitokea huko kijijini, sijui itakuwa ndio hiyo au la…, lakini mbona ilitokea siku nyingi, labda sio hiyo taarifa niliyoisikia mimi…ni mud asana…’akasema.

‘Sijui ilitokea lini,… mimi ndio niliona hiyo barua, sijaangalia iliandikwa lini…’nikasema.

‘Hiyo barua ipo wapi…?’ akaniuliza

‘Aaah, …..hata sitaki kuiona tena…nilitoka humo ndani kwa haraka, sijui ..itakuwa huko huko ndani…’nikasema.

‘Sasa utajuaje mama yako alifariki lini, maana huenda wasikuambie,...nikushauri kitu, ..jaribu kuwa mjanja,..uwe makini kwa kila jambo, usipoteze ushahidi,..unajua kuna kitu nataka wewe unisaidie, kama unataka uwe na amani..vinginevyo, na wewe yatakukuta hayo ninayotaka kuyafanya, …mmh, naona muda umekwenda,..siwezi kukuambia kwa leo….’akasema.

‘Oh, wala sitaki kukaa tena humu ndani….’nikasema.

‘Sikiliza mama yako ameshafariki, huwezi kumrejesha tena hapa duniani, hata ukienda huko kijijini, na kama ulivyonisimulia maisha ya huko kwenu, ina maana huna ndugu huna jirani atakuekuthamini tena, ina maana sasa wewe ni wewe, huna baba, huna mama, wewe ni yatima, masikini…unanielewa…’akasema.

‘Mungu mwenyewe anajua…’nikasema hivyo.

‘Sio mungu mwenyewe anajua,..... wewe kwa hivi sasa unatakiwa upambane kivyako….au  hebu niambie ukienda huko kijijini eeh,, utafanya nini, sana sana watakuonyesha kaburi la mama yako, halafu,..niambie hilo kaburi litakusaidia nini… utafanya nini, …muhimu kwasasa ni kuanza mapambano, kwanza jitahidi upate chako, pili hakikisha haki inatendeka, hao waliomfanyia hivyo mama yako, na wao uje kuwafanyia hivyo hivyo…kwa udi na uvumba…’akasema kwa kujiamini.

‘Nitawajuaje mimi…wewe unakijua kijiji chetu kilivyo..huko kuna watu watemi, wanafanya watakavyo…viongozi wa kijiji wenyewe wanawaogopa…..’nikasema.

‘Kwanini usiwajue, watakuwa ni wanakijiji au ni wageni, …sikiliza nikuambie kitu, hakuna kinachoshindikana chini ya hii dunia, ukiwa bado unapumua,…na ukiamua, lakini ukibakia kulia lia, haya lia, mpaka machozi ya damu labda yatakusaidia, ni kweli hata mimi nililia sana, lakini baadae nikazindukana, …wao kama wamekufanyia unyama, na wewe walipizie kwa unyama, kwa njia yoyote ile usijali ni njia gani…’akasema.

‘Sijui, …hata sielewi, hapa kichwa changu hakipo sawa..unayoniambia mimi sielewi…na sitaki kulipiza kisasi, mimi namuachia mungu tu…’nikasema.

‘Hahaha, haya muachie mungu, mungu humsaidia anyejisaidia…haya muachie mungu, siku yako nayo ifike, huko mbele utalipiziwa na mungu ..maana hao watu wakijua kuwa upo, na wakahisi unaweza kuwafuatilia na wewe watakuua..sasa kabla hawajaanza kufanya hivyo,wewe wawahi…mapema….’akasema kwa kujiamini.

‘Hapana mimi sitaki kufanya lolote baya…nitamuomba mungu tu inatosha….’nikasema.

‘Hahaha, toka lini duwa la kuku likampata mwewe, haya omba, omba usiku na mchana, tuone kama watakuja wakuambia ni sisi tumeua….hahaha, wewe vipi wewe….pambana nao, wapige kiini macho na wao wataabike…’akasema

‘Hapana…, mama yangu alinipa usia, kuwa..nisipende kulipiza kisasi, na pili, nisishndane na wenye pesa, kwani wao wameshikilia mpini,…na …aah, basi mimi sina nguvu tena, ..waache waje waniue na mimi, ni heri tu niende huko mbeleni, nikakutane na mama yangu..mimi sioni kama kuna umuhimu wa kuishi tena kwenye hii dunia, nimezaliwa masikini, nimekulia masikini, na…sizani kama kuna lolote nitafanya linisaidie….’nikasema.

‘Sikiliza wewe, usiwe mjinga,…mimi nitakusaidia kitu,… huyo mtu aliyenisimulia anasema kuna watu anawahisi na wamekimbilia huku huku dar, sasa kwa hivi sasa huwezi kufanya kitu huna mbele wala nyuma, hujaweza hata kuweka mtaji, ili ufanye kitu, unatakiwa uwe na pesa..kuna hata kusafiri, hadi huko kwetu, unakufahamu huko kwetu…kama unataka nikusaidie mimi…’akaniuliza.

‘Nitakujuaje huko kwenu na mimi ni mara ya kwanza kuonana na wewe…’nikasema

‘Kwetu ni ufipa, lyamba liya mfipa,..huko ndani ndani, ukitoka huko kwetu kuja huku, huagi, ..ila mimi sikukulia sana huko,…baada ya kupatwa na matatizo humu ndani, nilikutana na ndugu yangu mmoja, nikamsimulia wee, akaniambia hiyo ni kazi ndogo tu…, twende kijijini….haaah, nilipofika huko nikawekwa sawa, na bado, kazi haijaanza, hawa watu humu watanitafuta…’akasema.

‘Wewe jamani kwanini unataka kufanya hivyo, kwanza huna uhakika kuwa ni wao, umesema ni mashetani, je kama sio wao,..mimi niliona jambo jema ni kuwasamehe tu….’nikasema.

‘Wasamehe tu eeh….haaha….!, unajua walichonifanyia,…wewe unasema tu, niwasamehe tu, niwasamehe, kwanini wao hawakuliona hilo, wakanionea huruma, mimi nimepatwa na matatizo ndio niwasamehe, unajua sasa hivi sina kizazi….’akasema akishika tumbo.

‘Kwanini…?’ nikauliza nikionyesha mshangao.

‘Yatakuja kukuta na wewe…haina haja ya kukusimulia…kwasasa kaza buti, nakuonea huruma sana, lakini vita havina huruma, ama uwe upande wangu au uwe nao, na ukiwa nao, wewe ni adui yangu, kwaheri….’akasema sasa akiwa kachukua mzigo wake wa nguo zake.

‘Mimi hata sielewi kitu, hivi sasa akili yangu haipo sawa, natamani ninywe sumu tu..nimfuate mama yangu, …’ nikasema.

‘Utaelewa tu, dunia itakufunda, ….kama wataka kujiua kajiue…utamkomesha nani….’akasema akikagua humo ndani, kwa macho, halafu akatema mate chini, na kusema;

‘Humu, ilikuwa jela yangu, humu niliteseka, humu, nililia,. ….mpaka machozi ya damu, hakuna aliyenionea huruma, huyo kijana wao, anajifanya ana huruma, lakini moyoni kama baba yake….sasa tutapambana…na wao…’akaanza kuondoka.

‘Sasa mbona unaondoka…’nikasema nilipoona nabakia peke yangu.

‘Nitakufundisha kitu, lakini sio leo, …..ngoja niondoke wasije kunikuta humu ndani…’akasema.

Mara nikakumbuka kitu,…

‘Wewe uliacha kijitabu kidogo hivi…?’ nikauliza

‘Ndio eeh kweli,….nimekitafuta wewe…yaani hicho ndio kumbukumbu zangu zote, nakiomba tafadhali..humu kuna mambo nilifundishwa huko kijijini, …sasa ok…nipe nipe…’akasema .

Basi nikampa kijitabu chake, na kwa haraka akachukua mzigo wa nguo zake na kuondoka, na haikupita muda, mara mama mwenye nyumba akaingia, akiwa kaiva, kakunja uso, ..sijawahi kumuona akiwa katika sura hiyo kabla,…akashika kiuoni, ananiangalia machoni…macho yaliyojaa hasira…mkononi kashika mfuko wa zawadi.

Na kwa nje, nikasikia gari liondoka kuonyesha kuwa baba mwenye nyumba anaondoka !

**************
NB : Ndio ilikuwa hivyo, je itakuwaje baadae

WAZO LA LEO: Ukitendewa ubaya, usikimbilie kulipiza kisasi, kwani hujui ni kwanini ikatokea hivyo, mola wako hajakuacha, na huenda karuhusu huo ubaya ili upate fundisho fulani lenye heri mbele yake. Muhimu ni kuvuta subira, na kuelekeza maombo yako kwa mungu. Hakuna jambo lenye herii kama kusameheana. Kusamehe huvuta heri, na kulipiza kisasi huzaa kisasi kingine.
Ni mimi: emu-three

2 comments :

Anonymous said...

story poa, but sad, ...

Anonymous said...

lini watuma tena