Docta ambaye alikuwa akishirikiana na muendesha mashitaka,
alisimama na kumuomba hakimu kuwa, hao wanaosemwa ni wagonjwa wafikishwe
mahakamani, kwasababu hali yao sio mbaya ya kushindwa kufikishwa mahakamani
kutokana na kesi yenyewe ilivyo, akaendelea kusema;
‘Nimewaomba watu wa usalama watu hao wafikishwe mahamakani hii
leo kama walivyo,hata kama ikibidi na vitanda vyao…’akasema docta na wakili
mkuu upande wa utetezi akaingili kati na kusema;
‘Kwanini wagonjwa waliothibitishwa kuwa ni wagonjwa,…waletwe
mahakamani na hali zao hazistahiki, muheshimiwa hakimu, hii sio haki…?’
akauliza wakili huyo na hakimu akamgeukia docta na muendesha mashitaka kusikia
hoja zao.
‘Kwasababu kuna njama zimepangwa, kubatilisha ukweli,…’akasema
docta.
‘Kwa vipi, wakati nyie mna ushahidi wenu tayari, au mlikuwa
mnadanganya kuwa mna ushahidi, na kumbe mnataka kupoteza muda, kuwasingizia
watu makosa ambayo hamna ushahidi nao, hao watu kwenye jamii ni watu wema
kabisa, ulizeni watu watawaambia, mnawapotezea muda wao , unalijua hilo,…’akasema
wakili mtetezi na Muendesha mashitaka akamkatili kwa kusema;
‘Huwezi kusema tunadanganya, hiyo sio kazi yako, na utaratibu
wetu wa kuthibitisha ukweli wa makosa yao, tunaujua sisi wenyewe,
tutathibitisha hilo hatua kwa hatua.., kazi yenu nyie ni kujitetea,…’akasema
muendesha mashitaka.
‘Muheshimiwa hakimu, ukiangali ukweli, washitakiwa wapo mikononi
mwao… wametukatalia kupata muda wa kutosha wa kuongea nao..sisi tumekubali kutokana
na sababu waliyotoa kuwa washitakiwa wanaumwa hawatakiwi
kusumbuliwa,..tukakubaliana kutokana na sababu hizo, sasa kwanini tena mnakiuka
masharti yenu wenyewe,…?’ akasema wakili mtetezi,na hakimu akamgeukia muendesha
mashitaka.
‘Kuna tatizo la utambulisho wa washitakiwa hao, na hatuwezi kulielezea
hilo hapa mpaka hao washitakiwa wawepo humu mahakamani,….kama alivyoshindwa
kuelezea mke wa mzee,…kuna mambo tunatakiwa tuyabainishe mbele ya mahakama hii
tukufu wakiwemo hao washitakiwa wenyewe kabla hatujachelewa,.., na si
vinginevyo…’akasema muendesha mashitaka, na alipomaliza hivyo, akawa anateta na
docta.
‘Bado hujairidhisha mahakama yangu, kwa hoja yako hiyo,
muendesha mashitaka..unaelewa taratibu za mahakama, aus io…, docta wanaowatibu
hao watu, wamethibitisha, kuwa baadhi ya washitakiwa hao ni wagonjwa…’akasema
hakimu.
‘Ndio muheshimiwa hakimu lakini…..’akasema na hakimu akamkazia
macho akisema;
‘Sijakuruhusu uongee…’akasema
‘Na kutokana na hali zao, bado wanahitajia muda wa matibabu ili
waweze kufika hapa mahakamani,..hizi hapa nyaraka nimekabidhiwa za madocta
wanaokubalika kisheria,…sasa nyie upande wa mashitaka, nileteeni nyaraka za
kubainisha kuwa hili sio kweli, au nipeni sababu za msingi,..’akasema hakimu.
‘Muheshimiwa hakimu,…ukweli wetu utabainika hao watu wakiletwa mbele
yako…,ya mahakama yako tukufu, na sisi tutaweza kubainisha huo ukweli kuwa
taarifa ulizopewa, kuhusu hali zao, na wao wenyewe jinsi walivyo, sio sahihi,
kuna njama za kubatilisha ukweli halisi…’akasema muendesha mashitaka.
‘Muendesha mashitaka,wewe sio mgeni wa sheri, au unataka
nikufundishe sheria, je hayo unayoomba yanaendena na mpangilio wa sheria za
kuendesha kesi kama hii, …?’ akauliza hakimu
‘Muheshimiwa hakimu, kuna dharura,..na hii ni dharura ambayo,
kweli mimi nimethibitisha kuwa inahitajia hivyo, kuwa hao wagonjwa ambao ni
washitakiwa wanahitajika kusimama mbele ya mahakama hii ,na taarifa hii
nimeipokea muda sio mfupi, na …’akasema muendesha mashitaka na wakili upande wa
utetezi akaingilia kati kwa kusema;
‘Kwa vipi na wao ni wagonjwa…muheshimiwa hakimu, hawa watu
hawajali utu wa mtu, na sheria ipo wazi kumuhusu mgonjwa, mgonjwa ana haki
zake, anaweza kuongea jambo ambali hakukusudia, kutokana na hali yake…’wakili
mtetezi akasema.
Hakimu akamgeukia muendesha mashitaka kama vila anataka
kumuuliza swali, halafu akasema;
‘Kwa namna hiyo mimi naona muendesha mashitaka hamjawa tayari, hatuwezi
kuwaburuza wagonjwa hao mahakamani,vinginevyo, utoe ushahidi kuwa madakitari
hao wanasema uwongo, …kwa hali ilivyo,
basi inabidi tuahirishe hii kesi…
‘Muheshimiwa hakimu..isipowezekana leo, basi haitawezekana
tena,na kama haiwezekani leo, basi sisi hatuna uaminifu tena na mahakama
hii….’akasema docta na muendesha mashitaka akamsogelea docta, kukawa na
mazungumzo ya watu hao wawili, halafu muendesha mashitaka akamsogelea hakimu
kuteta naye…lakini ikaonekana hakimu hajakubaliana naye…
‘Kesi imeahirishwa…’akasema hakimu akisimama akuondoka na mara
mlangoni akaingia binti, akiwa kavalia vizuri tu, lakini usoni alikuwa kava
mawani meusi, yaliyozibz sehemu kubwa ya uso wake,…kichwani alikuwa kavaa
mtandio..na alipoingia tu, akawa anakimbilia mbele ya mahakama, na walinzi
wakawa wanajaribu kumzuia…
Tuendelee na kisa chetu…
*******************
Ile hali ya mlinzi kumzuia huyo binti, na wakati yeye
anataka kuingia na kuelekea kule mbele alipo hakimu, ikazua mtafaruki, na
kumfanya hakimu, ambaye alishasimama kutaka kuondoka, asite kidogo, na baadae ikabidi
yeye mwenyewe aingilie kati na kuuliza;
‘Kuna nini huko…walinzi kuna tatizo gani,…?’ akauliza
kwa sauti ya ukali.
‘Ni huyu binti….’akasema mlinzi.
‘Huyo binti anataka nini…?’ akauliza tena kwa sauti ya
ukali.
‘Analazimisha kuja huko mbele muheshimiwa hakimu…anadai
kuwa ana jambo muhimu ambalo halitaki kusubiria…. anataka kuliongea sasa hivi
mbele ya mahakama yako tukufu muheshimiwa…’akasema mmoja wa walinzi.
Hakimu akatulia kidogo, halafu akasema
‘Ehe, wewe binti unataka nini,..?’ akauliza na tendo
hilo liliwashangaza wengi wanaomfahamu huyo hakimu kwa msimamo wake…, kwani ni
hakimu mwenye msimamo, akitoa amri ni amri, hana kugeuka nyuma…na kitendo hicho
kikawavuta watu wabakie kimia wasikie huyo binti anataka kusema nini…
Docta..ambaye kwa muda huo alikuwa akiteta na
muendesha mashitaka akashikwa na butwaa, kwani hakuamini…, ina maana ni kweli
walichosema hao watu..hao watu walisema kwenye ujumbe wa awali;
‘Docta
tumeshafanikiwa kuurudisha mtandao wetu, kama awali, sisi hatutaki matatizo na
wewe na wala hatuna nina mbaya kama unavyohisi wewe…tunakuomba uache tabia yako
ya kuingilia mambo yasiyokuhusu..la sivyo, tutaanza kupambana na wewe kisheria….’
Ujumbe huo aliupata siku ya ile ya awali aliposhindwa
kuufungua huo mtandao, na baadae kukawa kunakuja ujumbe za ana tofauti tofauti
nyingi zikitaka kuonyesha wao, hawana tatizo ..hawana jambo la baya, kinyume
cha jinsi docta na wenzake wanavyofikiria…na mwishoni wakaleta ujumbe wao
ukisema hivi;
‘Sisi tuna
kitengo cha kusaidia wenye matatizo ya akili na matatizo, ya kimashetani,..na
mmoja wa wagonjwa wetu, ni watoto wa mzee…na mmojawapo keshapona tayari.., na
siku ya kesi atafika mahakamani, kulithibitisha hilo …’
‘Ina maana ujumbe ule matokea yake ndio haya,..’akasema kimoyo moyo.
Kwahiyo pale alipo docta alijua moja kwa moja, kuwa
huyo binti atakuwa kapandikiziwa mambo ya kuongea …, kuashiria kuwa yeye
alikuwa anaumwa, na katibiwa na hao watu, kwahiyo hao watu ni watu wema, kinyume
na jinsi watu, au waendesha mashitaka wanachoongea watu kuwa hao watu ni
wabaya, …
‘Hawa watu ni wajanja sana,….’docta akasema kimoyo
moyo, huku akigeuka kumuangalia vizuri
huyo binti, hakuwa na muda wa kwenda kumzuia,..alikuwa keshafika mbele…na akawa
jana jinsi zaidi ni kusubiria asikie hicho anachotaka kukisema kwa hakimu au
mbele ya mahakama, ni ni lazima watakuwa wamemtuma hao watu kufanya hivyo, ili
kuiharibu hiyo kesi.
Muendesha mashitaka akamsogelea docta na kusema;
‘Unahisi kuna jambo huyo binti katumwa na hao watu…?’akauliza
‘Ngoja tusikie atasema nini,…’akasema na muendesha
mashitaka akatulia akiangalia kule mbele, na mara akasikia hakimu akaisema;
‘Mlete huyo bintu huku mbele…’akasisitiza hakimu, na
muendesha mashitaka akamshika docta begani tena na kumuuliza
‘Unafahamu lolote kuhusiana na huyo binti, ni nani
huyo binti…?’ akauliza
‘Hata sijui, ngoja tumsikilize…’akasema docta, docta
alishajua huyo binti ni nani, japokuwa huyo binti alijaribu kuvaa kinamna
ambayo hataweza kugundulikana kuwa yeye ni nani…alijitahidi kwa kweli…
Yule binti
akatembea kuelekea mbele ya mahakama, akisindikizwa na walinzi wawili, na
alipofika sehemu karibu na hakimu , hakimu akamkagua kwa makini, akasema;
‘Hebu vua hiyo miwani yako tukutambue vyema…’akasema hakimu
na kwanza binti alisita kufanya hivyo, na askari akataka kumvua kwa nguvu ,
ndipo huyo binti akavua mwenyewe, …
Watu wakaguna kidogo, na hakimu akaashiria kwa mkono
kuwa watu wanyamaze..
Yule binti akafanya hivyo,..na kuondoa sehemu kubwa ya
nguo iliyokuwa imefunika uso wake, na sasa ungeliweza kumuona vyema na kumtambua
kuwa yeye ni nani kwa mtu anayemfahamu…, na docta, akaguna na kusema;
‘Hawa watu wamecheza, lakini mungu mkubwa, ngoja tuone…’akasema
kwa suti kidogo, na safari hii muendesha mashitaka hakuwa makini na
alichokiongea, mawazo na akili yake ilikuwa kwa huyo binti, halafu akamsogelea
docta na kusema;
‘Huyu sio binti wa mzeei..?’ akauliza muendesha
mashitaka
‘Ndio yeye, …’akasema docta na wote sasa wakawa
wametulia wakiangalia kule mbele…na mara kule upande walipokaa washitakiwa kukatokea vurugu nyingine, na watu wakageukia
huko kuona kuna tatizo gani.
Mama , mke wa mzee, alikuwa akizozana na wakili
mtetezi, yaonekana walikuwa hawaelewani, ilikuwa sasa ni kazi ya walinzi, kuwatuliza
, na hakimu hakuwatilia maanani, naona mawazo yake yalikuwa kwa huyo binti
aliyefika. Na vurugu zilipozidi ndipo hakimu akasema;
‘Kuna vurugu gani tena huko, walinzi kuna nini huko…?’
akauliza hakimu, na watu wakatulia, na baadae yule binti akamsogelea hakimu,
hakimu akasema;
‘Unataka kuongea na mimi au na mahakama, ?’ akauliza
hakimu akimkazia macho huyo binti.
‘Nataka kukuelezea wewe mbele ya mahakama yako tukufu
muheshimiwa…’akasema huyo binti.
‘Wewe ni nani,… hebu jitambulishe kwanza.., na unataka
nini, ujue umevuruga taratibu za mahakama, kwahiyo uongee jambo lenye msingi nah
ii kesi, lasivyo, sheria itachukua mkondo wake…’akasema hakimu na binti
hakuonyesha wasiwasi akasema;
‘Nina jambo muhimu muheshimiwa hakimu, ni kuhusu hii kesi
ya leo,…’akasema huyo binti akiwa kaangalia mbele, hakumuangalia hakimu .
‘Kuhusu kesi hii,…! Ehe, hilo jambo linasemaje, ongea
kwa haraka, sina muda wa kupoteza tena hapa…’akasema hakimu.
‘Ni kuhusu washitakiwa wa hii kesi,…’akasema huyo
binti, na hakuonyesha kuongea haraka haraka kama alivyotaka hakimu.
‘Wana nini…?’ akaulizwa
‘Wamejibadili sura zao…’akasema, na watu wakaguna, na
hakimu kwanza alibakia kama kuduwaa, halafu akauliza;
‘Wamejibadili sura zao kwa vipi?’ akauliza hakimu sasa
akionyesha kukerwa, na akawa kama anataka kutoa amri huyo binti ataolewe,
lakini alishauliza swali.
‘Mimi nimewaona kwa macho yangu, nikiwa hospitalini….yule
kiongozi wao, alivua ngozi ya juu, akawa sio yule wa awali na walipokuja
madocta akajifanya yeye kaja kuona wagonjwa, akawa anaulizia mgonjwa, na
akaambiwa hayupo,…baadae akasema atakuja baadae, akatoka nje, hivi hivi namuona,
na pale kitandani akaja kulala mtu mwingine…’akasema kwa haraka haraka hapo.
‘Oh,….una uhakika na unachokisema?’ akauliza sasa
akiwageukia washitakiwa halafu muendesha mashitaka, kama anatafuta neno.
‘Ndio nina uhakika muheshimiwa hakimu…’akasema huyo
binti.
‘Una uhakika gani, na kwanza wewe ulifuata nini wodi
ya wanaume…?’ akaulizwa
‘Nilikuja kumuona mmoja wa wagonjwa, na kabla
sijaruhusiwa nikawa nimesimama dirishani na kuona hicho kitendo, kikitokea
muheshimiwa hakimu…’akasema huyo binti.
‘Una ushahidi gani wa hilo..?’ akauliza.
‘Bahati nzurii muda huo nilikuwa na simu yangu, kwa
haraka nikaanza kuwapiga picha bila y awao kuniona,…’akasema.
‘Ni nani alikutuma, …?’ akauliza wakili mtetezi.
‘Nimesema nilikwenda kuwaona wagonjwa, nikaona hilo
tukio, je…na nina ushahidi huo hapa kwenye hii simu yangu…’akasema na hapo
muendesha mashitaka akasogea mbele kutaka kuona hilo tukio kwenye simu..na
halikadhalika wakili mtetezi naye akasogea.
‘Sijawaambia msogee huku mbele,..’akasema hakimu.
‘Samahani muheshimiwa hakimu…’akasema wakili mtetezi,
lakini muendesha mashika hakusema na hakusogea akawa anajitahidi kuona ni nini
kipo kwenye simu.
Muheshimiwa hakimu akawa anaangalia kile alichokuwa
akionyesha huyo binti, na alipomaliza akasema;
‘Sawa ushahidi huu umepokelewa, na ….haya nyie wawili
njooni hapa..’akasema na muendesha mashitaka na wakili mtetezi, wakasogea mbele
ya hakimu wakawa wanateta,kwa muda, kukawa na mabishano kidogo, baadae hakimu
akasema;
‘Kesi yetu, itasikilizwa tena, tarehe…’kabla
hajamaliza binti akasema;
‘Lakini muheshimiwa hakimu, sio hao tu, na wengine,
walifanya hivyo hivyo, na mwisho wa siku waliobakia hapo walikuwa watu wengine
tofauti kabisa..’akasema huyo binti.
‘Ina maana kuna wengine walifanya hivyo…,zaidi ya huyo
uliyenionyesha hapo..?’ akauliza.
‘Ndio…’akasema.
‘Na matkio yote hayo uliwezaje kuyapiga picha?’
akaulizwa.
‘Utaona sehemu ya pili nilikuwa nazungusha huku na
huku ili niweze kuwachukua wote, …inaonyesha na kila mmoja kwenye kitanda
chake, japo sio kwa ukamilifu kama hiyo ya kwanza, muheshimiwa hakimu…’akasema
‘Nikuulize kwanini uliamua kuchukua hatua hiyo, wewe
ni kama nani..?’ akauliza wakili mtetezi.
‘Mimi ni mmoja wa watu waliathirika na matatizo haya
yote, baba yangu kwa hivi sasa kalazwa ana hali mbaya tatizo hili limeikwanza
sana familia yangu, na naogopa kuwa mambo mabaya zaidi yanaweza kuikumba
familia yangu, ndio maana nimeamua kusema mbele ya mahakama hii, ili kila mtu
asikie,, ..’akasema huyo binti.
‘Lakini wewe ni mmoja wa washitakiwa ..ila hukutajwa,
kwenye orodha ya leo, sijui kwanini,..?’ akasema wakili mtetezi.
‘Ndio sijui kwanini hawakunitaja,mtajua wenyewe,…labda
ni kwa vile wanajua nafahamu mengi, awali si ndio hao…walinipandikizia uchawi
wao,..na nyie mnatetea, nguvu za giza, ..mungu atawalaani..’akasema huyo binti,
na watu wakacheka.
‘Ni nani anatetea, nguvu za giza wewe binti umetumwa
au,…wewe yasemekana unahusika, na hata dada yako amefariki kwa kupitia wewe,halafu
unasema nguvu za giza,…’akasema wakili mtetezi.
‘Dada yangu hajafariki….’akasema
‘Eti nini…?’ aliyeuliza sasa ni mama , mke wa mzee.
‘Nasema hivi dada yangu hajafariki, yaliyofanyika huko
nyuma ni viini macho, walimchukua dada yangu msukule, lakini nimegundua kuwa
hajafariki,..yupo kafichwa kwenye vyumba vyao…, na aliyefanya hivyo ni huyo
huyo aliyejigeuza huko hospitalini, na kutoroka, …kama hamuamini haya, ukweli
ndio huo…’akasema na watu wakaguna na kukawa na kelele.
‘Hahaha, wewe umechanganyikiwa muheshimiwa hakimu,
nahisi huyo mtu kachanganyikiwa, bora akapimwe akili yake kwanza…’akasema
wakili mtetezi.
Hakimu akawa anateta na wenzake, baadae akasema;
‘Kesi imeahirishwa kama nilivyosema awali…, na
wahusika, mchukueni binti huyo, kwanza akapimwe akili yake kama yupo sawa,
halafu, awaelezee vyema..hiyo ni kazi yenu,…, na siku ya kesi, ni tarehe…’kabla
hajamaliza mama mtu akasema kwa sauti.
‘Hatuna imani na wewe hakimu…siku ya terahe ijayo
tunahitajia hakimu mwingine,…wewe ni mmojawao, ukija tena mimi nitatoboa sori
yote….’akasema mama , mke wa mzee, na kukawa na vurumai kidogo, na hakimu akawa
ameshatoka mahakamani, …
Docta kwa haraka akamuendea binti, na kumshika mkono,
kabla hajazungukwa na waandishi wa habari, walijipenyeza na kuingia ndani, na
wakati huo huo, mama akawa anapambana na walinzi,..alikuwa anataka kuondoka ile
sehemu kabla hawajachukuliwa na walinzi
‘Tatizo ni nini tena,…?’ akauliza muendesha mashitaka,
akiangalia upande huo, na mara sauti ya huyo mama ikasema;
‘Mimi sitaki kukaa na hawa watu tena, sipo upande wao,…najua
hatima yangu nini, nahitajia ulinzi wenu…’akasema na wakili mtetezi akataka
kusema jambo, mama akadakia na kusema;
‘Najua wewe ni nani kwenye hilo kundi…usitake niongee
mengi zaidi, ongea zaidi na mimi nitamwaga ukweli wote…’akasema na huyo wakili
akaonyesha kama kunywea fulani hivi.
‘Unataka nisema wewe ni nani…?’ akauliza huyo mama
akimuangalia huyo wakili mtetezi,…na yule wakili mtetezi, akawa kamkazia macho
huyo mama, bila kusema kitu…yule wakili mtetezi, akabakia kimia
Docta akamsogelea yule mama akamuuliza;
‘Huyo ni nani…, sema haraka kabla hawajaondoka..?’
akauliza
Na yule wakili akageuza uso kuangalia upande wa pili
na kujifanya kama anaongea na wenzake, halafu akainua mkoba wake,na kuangalia
saa, kama vile anataka kuwahi jambo…na kwa pembeni akaangalia kule mama alipo,
alifanya hivyo kinamna, na docta akamuona na muendesha mashitaka.
Yule wakili mtetezi, sasa akawa anaanza kuondoka,
muendesha mashitaka, akamkabili…., na wakili huyo sasa akawa anaondoka kwa
haraka, muendesha mashiaka,akaongea na askari kuwa huyo mtu akamatwe kabla
hajatoka,….
NB: Kisa kinaendelea, mnasemaje mpaka hapo.
WAZO LA
LEO: Kufunga ni ibada ya ndani sana, mtu ana chakula chake,ana mali
yake, ana uwezo wake, lakini kipindi cha kufunga vyote hivyo, anaviacha, hawezi
hata kujificha akala kwa siri, au akatenda matendo mabaya kwa siri, hii ni
kuashiria jinsi gani ibada hii ilivyo nguvu ya peke yake. Ni imani kati ya mja
na mola wake. Tujitahidi, kuitimiza ibada hii kwa imani ya kweli,…kwa taratibu
zake, ili mwisho wa siku tuweze kufaulu badala ya kushinda na njaa tu.
Tunawatakia Ramadhani kareemu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment