Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, May 23, 2017

MPENZI WA FACEBOOK-34



 Kitendo kile cha kudondoka mzee na kupoteza fahamu, kilitokea pia, upande mwingine, kwa kile mtu aliyekuwa kawekezewa kwenye huo mtandao ambao kwa muda huo ulikuwa kwenye mikono ya docta, ilibidi ahakikishe kuwa kila mtu kafunguliwa kwenye kifungo hicho cha kishetani.

 Na ukumbuke yote hayo alikuwa akiyaona docta, akiwa huko kituo cha polisi, na watu waliotekwa na mambo hayo walikuwa sehemu tofauti tofauti…mimi nilikuwa kwenye jengo la mzee, Mpelelezi alikuwa kwenye nyumba ya kibiashara mtakuja kuiona ni numba gani hiyo. Kuna wanawake watatu, …’ katulia docta akiwa ananihadithia matukio hayo, ambayo mimi sikuwahi kuyaona,

Na pale mzee, alipodondoka na kupoteza fahamu, na mimi ilitokea kwangu hivyo hivyo, na kwa mpelelezi, na kwa hao wanawake…ni kwanini ikatokea hivyo?

‘Ni kwasababu watu wote hao walipandikiziwa mazindiko ya kishetani na uchawi, na walishakuwa watumwa wa hao watu wabaya, na akili zao zilitegewa kwenye mtandao, ..na docta alipomaliza kuondoa hayo mauchafu kwenye vichwa vya haoo watu, ndio kila mmoja akaanza kudondoka kwa wakati wake

‘Ni utaalamu wa aina yeka wa kutumia mitandao…’akasema docta, akinihadithia
‘Lakini ni ujuzi wa kuchanganya mambo ya giza, na utaalamu wa digitali…kama hawa watu wangewekeza utaalamu huo kwenye mambo mema, kama kutibu na madawa wangelikuwa mbali, lakini wao, kama wao, wanasema hivyo haiwezekani….kutokana na masharti ya mambo hayo ya giza…mimi sikuwaelewa…’akaendelea kuelezea docta, kipindi hicho nipo kitandani, mgonjwa.

Ngoja sasa niwarejeshe ilivyotokea kwa upande wangu, baada ya kuondolewa hay mazinduko ilikuwaje,..
Basi ngoja niwarudishe siku hiyo ambayo, nilichukuliwa mimi nikiwa sijiwezi, sijijui,..nikitolewa kwenye hilo jumba la mzee, baada ya matukio hayo ya kutisha…
Tuendelee na kisa chetu.
***********
 Mimi nikiwa ndani ya jumba hili la mzee , ambalo liligeuka kuwa jumba la matambiko la hao watu, nilishuhudia mambo haya ya ajabu….

Kwanza ilifika muda, nikahisi kama masikio yangu yamezibuliwa,  ni kama vile mtu masikio yaliingia maji, na yale maji yakatoka, unahisi hali tofauti..ndivyo naweza kuelezea hivyo kwa upande wa masikio, na akilini..ilikuwa kama mtu aliyetoka kwenye usingizi mzito wenye ndoto za kutisha...

 Na wakati hali hiyo ikiendelea kichwani mwangu, bado nilihisi mwili wangu ukiniisha nguvu,,,viungo vinalegea…lakini sikutaka kuzidiwa na kulala, nilihisi nikifanya hivyo , hao watu watanikuta humo na kunimaliza..kwahiyo nikawa napigana na akili…na kuna muda  nikawa nahisi pumzi inabana, …nashindwa hata kupumua vizuri, nikawa sasa natafuta sehemu yenye hewa.

Kwa hali kama hiyo ikanibidi nitoke mle kwenye kile chumba, na kutembea hadi kwenye ukumbi, ambao muda mfupi uligeuka na kuwa uwanja wa mapambano…wote mle waliwekwa chini ya ulinzi, wamelala sakafuni, wengine ni wameshakufa.

Nilipowaona hao watu wamelala, wengine ni maiti, hali ikazidi kuwa mbaya, nikwa nahisi vibaya zaidi, nikaona ni heri nirudi tu kule nilipokuwa awali,….na nilifanya hivyo, nikikumbuka kuwa yule kiongozi wao, alikuwa bado kapoteza fahamu kule nilipokuwa mimi…lakini kuna mtu mwingine nilikuwa sijamuona…

Niliporudi pale nilipokuwa nikaangalia pale alipokuwa kalala yule kiongozi wao. Sikumuona…na askari aliyekuwa akilinda pale naye hayupo…sijui yupo wapi…

‘Hawa watu vipi…?’ nikauliza nikiangalia huku na kule

 ‘Ina maana hawa watu wamemuachia huyo mtu…muuaji,…, haiwezekani..’nikasema na nikiwa natembea kwa shida, nikaelekea kwenye chumba kingine, kilichokuwa jirani yake, na hapo ndio nikawaona, kumbe wao wawili, waliwekwa chumba kingine, na askari aliponiona nataka kuingia huko akanizuia…

‘Afande nataka kumuona huyo kiongozi, wao, ….nina majukumu naye, …’nikasema na yule askari alishanifahamu kuwa mimi ni nani,..akasema;

‘Una majukumu naye kwa vipi…?’ akauliza

‘Ungemuuliza afande wako angekuambia…’nikasema

‘Haya kama unataka kukaa nao humo ndani, haya ingia, lakini usije kuleta vurugu huko ndani, …maana nyote nasikia mumechanganyikiwa na mashetani ha hao watu..’akasema na nikafunguliwa mlango na kuingia ndani.

Mlango ulipofunguliwa tu, nikasikia zogo, nikamuangalia huyo askari, na yeye wala hakujali, akaniashiria niingie.

‘Wewe si unataka kuingia,..ingia, ukakutane na hao vichaa huko ndani…’akasema na kwanza nikahisi huenda sio yule kiongozi wao, nikasema kwa huyo mlinzi.

‘Yule anayeonekana kuwa ni kiongozi wao yupo wapi..?’ nikamuuliza

‘Ndio yupo humo ndani…’akasema na kufunga mlango kwa nyuma yangu…hapo nikajiuliza itakuwaje iwapo ni kweli, hao watu wamechanganyikiwa na kwanini wawaweke wawili, mke na mume…’nikasema nikisikia sauti ya kike na kiume wakibishana kuhusu jambo fulani.

Kwanza sikuingia moja kwa moja,…uzuri wa chumba hicho unaingia sehemu kama ya mapokezi vile…halafu  unakata kulia ndio uingie kwenye chumba chenyewe…nahisi walitaka kupafanya hapo kama sehemu ya kujisomea. Kuna kabati kubwa linazuia, huwezi kuona kwa ndani.

'Unataka kwenda wapi?..’nikasikia mwanamke akiuliza, nilijua ni mimi naulizwa kuwa, lakini kumbe walikuwa wakiongea wenyewe huko ndani.

'Dada sikiliza,…jinsi muda unavyozidi kupotea hapa ndivyo tunavyozidi kuingia matatani,…sijajua kinachoendelea…ni lazima nipambane hadi damu yangu ya mwisho…hawa watu hawajanijua kuwa mimi ni nani..’akasema

‘Upambane na nani…?’ akaulizwa

‘Dada wewe peke yako ndiye unayenifahamu …sitaki kusikia ukisema lolote,,…najua nikitoka hapa hakuna atakayenitambua tena..tatizo nipo mbali na mitambo yangu…’akasema nikajiuliza ni kwanini anasema hivyo.

‘Unajidanganya, wamegunduaje kuwa umevaa hiyo ngozi, watashindwaje kukugundua kuwa….’akataka kusema, na ghafla akanyamaza.

Nikahisi kuna kitu…au kanyamazishwa au wameona kitu….mimi nikajabanza vizuri nyuma ya kabati, na nikasikia wakisema.

‘Nilisikia kama mlango umefunguliwa,…’akasema mwanaume.

‘Ni huyo askari, alikuwa akijaribu kuona tupo salama, wanajua wewe ni tahira wa mashetani….’akasema huyo mwanamke.
‘Unatafuta nini…?’ mwanamke akauliza.

‘Mimi ni mpiginaji, najua nini nitakachokifanya, ….’akasema na akawa kapata kitu kama chuma, akaenda kwenye dirisha na kuanza kujaribu kupindisha nondo za dirisha, ikawa haiwezekani…

‘Hebu tulia kule…’ilikuwa suti ya huyo mwanamke, …nilishindwa kujua kwanini anasema hivyo kwa kujiamini, nikageuza shingo kumuangalia huyo mwanamke…nikaona ooh, kashikilia bastola.

‘Hahahaha….kumbe unayo hiyo silaha…sasa dada hapo…eeh umecheza, umewezaje kuificha wasikugundue,…unajua wakati mwingine mimi nakuvulia kofia,…, tunaweza kujihami, nipe hiyo kitu, mimi najua vyema jinsi ya kuitumia kuliko wewe…’akasema huyo mwanaume.

‘Nikupe nini…hahaha, ili uniue, nakujua sana wewe, rudi pale ulipokuwa,..na ukae chini…, unajua nataka nini, ninataka wakukute wewe ni maiti, kama ulivyofanya kwa binti yangu…’akasema huyo mwanamke.

‘Sikiliza dada, acha kunielekezea hiyo kitu, kama ndio yenyewe, haikwepeshi labda uwe na dhamira ya kuni…jeruhi tu,..lakini ukiwa na dhamira ya kuniua, kama ndio yenyewe, ni lazima itafanya hivyo, hata kama huna shabaha..acha na nayo, geuza kule,..ujue dada mimi nakupenda sana,… hayo niliyoyafanya , nilifanya kwa ajili yetu, …na kuhusu binti yako, mbona ipo wazi, alijiua mwenyewe, …’akasema.

‘Hahaha..wadanganye wengine…siku zote nilikuwa natafuta uhakika, je kweli binti yangu alijiua mwenyewe au la,..nimekuja kugundua kuwa ni wewe ,…uliyemuua, kwa ujanja ujanja wako, wa kupandikiza ushetani kwenye miili ya watu,…leo nimedhihirisha kuwa ni wewe na mambo yako…na kwahiyo kama nilivyoahidi, kuwa aliyemua binti yangu na yeye ni lazima afe., ….’akatulia sijui ni kwanini.

‘Dada unakumbuka tukiwa wadogo, nilikuahidi nini,…kuwa, japo hatukuzaliwa tumbo moja, lakini sisi tumeungwanishwa kwa babu ni bibi ndio.... na wazee wale walitaka,kutupatia huo urithi, wewe ukakataa......'ilionekana kama  anahisi maumivu au anaigiza kuhisi maumivu…pengine , ili huyo mwanake amuonee huruma.

'Lakini wazee wale hawakutulazimisha kuchukuo huo mkoba,…walituasa ubaya wa hayo mambo,na kama hatutaweza ni bora, wakaharibu, wewe ukasema nini kwa tamaa zako…tamaa za mali tokea ukiwa mdogo,..ukataka kurithi huo ushetani , na baya zaidi mungu akakulaani, ukawa huna kizazi. Sijui ungekuwa nacho ungefanya hivyo hayo mashetani yanavyotaka, …ukaona unigeukie mimi na familia yangu…’akasema huyo mwanamke.

'Dada, sio kweli…mimi nawajali wewe na familia yako, ndio maana nikawa nahangaika kutafuta mbadala wake,…najua walichotaka hao wahenga,…lakini niliomba nipate mbadala wake,… na mbadala wake ni gharama kubwa, damu nyingi ilihitajika..kutafuta watu wenye nyota kama za….’akatulia.

‘Kama za familia yangu, kama za damu yako…hiyo sio damu yako…ni ushetani wako tu,…’akasema huyo mwanamke kwa hasira.

‘Sio ushetani wangu dada…ni masharti yao magumu….ilifikia ikawa mimi au wewe, au watoto..lakini nikawa nakwepesha..ndio maana nilitaka yule …mchumba wa binti yako..yeye ana nyota, …yeye angelifaa, sana, lakini….aah, dada hebu tuyaache hayo, …nipe hiyo silaha…’akasema

'Mimi sikuelewi wewe…, pamoja na kusoma kote huko, una kazi, una heshima, lakini bado, unashiriki kwenye huu uchafu wa ushirikina, mimi sitakusamehe.

'Dada, sio kazi rahisi kama unavyofikiria wewe…hujui jinsi gani nilivyoteseka,..huko chuoni,…ilifika mahali nikawa kama punguani, kisa nimepuuza maagizo ya wale wazee,…hebu niambie, kwa hali hiyo, ulitaka mimi niwe…hapana, ….sikupendelea ..nilijuta kukubali, lakini imeshapita, wewe ulitaka mini nifanyeje…niteseke,..niharibikiwe kabisa, au…?’

'Ungefanyaje, wakati ulijitakia wewe mwenyewe kwanini ulikubali….kwanini hukukataa kama mimi,…?’ akauliza

'Hilo lilishapita,…. haya ilikuwa upumbavu na tamaa zangu, kukubali,…sasa … siwezi tena kujirejesha huko nyuma, huoni adhabu niliyopewa,…kwanza sizai...sina raha, mke..oh, akanikimbia, kisa ni nini…nimekuwa nikiishi kwa taabu, nateseka, usiku ukifika naadibiwa, mchana , nipo kama tahira,,, ..aah..'akawa kama anataka kuanguka..kwa pale nilivyomuona.

 Yule mwanamke huruma ikamjia, akalegeza mkono, bastola ikawa inataka kudondoka mkononi….niliona jinsi gani huyo jamaa alivyoinua jicho, nikajua kuna kitu kitafuatia….

 Ilikuwa kama mshale, yule mtu alivyojirusha, mateke mawili, yakampata yule mama kifuani..yule mama akarushwa na kudondoka chini kama gunia, bastola ikadondokea upande mwingine.

 Nilisikia yule mama, akitoa sauti ya kukugumia na yule mtu naye halikadhalika, kajitonesha, …lakini kwa vile lengo lake ni bastola,…akajitutumua, na kwa haraka akajirusha kuifuata ile bastola, lakini alipotua alitanguliza miguu, na mguu wake mmoja,, ukawa umeipiga teke, ile bastola ikaserereka hadi pale nilipo….akawa anagugumia maumivu damu zinamtoka begani, naona aliumizwa na risasi..walipokuwa kwenye mapambano.

 Ilibidi kwanza atulia kusubiria maumivu kutulia,..na baadae sasa akili ya kuiangalia hiyo bastola ikamjia,…hakujua imeenda wapi alivyoigonga na mguu…ilikuwa karibu name, ni kiasi cha kunyosha mkono kuichukua, lakini nikifanya hivyo wataniona,…na mimi kwa muda huo, ilahali ya kujisikia vibaya ikawa inakuja kwa kasi, nikawa sasa  nahisi mwili mzima, unaniishia nguvu, sijui ni kwann.
 Jamaa sasa akawa kapiga magoti akiitafuta hiyo silaha, na yule mwanamke alionekana kukata tamaa, bado alikuwa kalala pale sakafuni, , na jamaa akawa hajaiona ile silaha, akamgeukia yule mwanamke.
'Hii bastola, ina mashetani,… nimeamini…kama ndio yenyewe..basi …ipo wapi….’akawa sasa anataka kusimama.

‘Hutaipata kamwe…’akasema huyo mwanamke.

‘Unajua wewe sikuelewi…, kwa ujuha wako siku zote nimekuwa nikikuambia umuibie mumeo hiyo bastola na vile viatu,..uniletee mimi, wewe unaogopa, sasa leo, naichukua hiyo bastola, na ikiingia mikononi mwangu, hakuna atakaye niweza tena…na hapo hata hivyo viatu nitavipata…’akasema akionyesha macho ya kikatili.

‘Si mpaka…’akasema huyo mwanamke.

‘Hiyo bastola ipo wapi, unajua hiyo bastola ina umuhimu gani, hata mumeo hajui..kwanza shabaha, haikosi ila ukifyatua uweke dhamira, pili, unaweza ukapambana na jeshi kubwa tu…na….siwezi hata kukuambia..hiyo silaha, imetembea nch nyingi duniani…kama ingelifika kwa yule jamaa…’akatulia

‘Jamaa gani….?’ Akaulizwa

‘Wa dunia yangu…sasa hivi angelikuwa kama nani vile..hahaha, sasa leo ni lazima niipate,..na viatu , unajua dada vina umuhimu gani..vile ukivivaa, usiku unaweza ukuruka kama kangaroo…unajua kangaroo anavyoruka na kukimbia…ni kama unapaa…hahaha, sasa natumai ndoto yangu itatimia, ..unajua dada nilipoipata ile pete ya mtandao..inaitwa ufunguoa, nikajua sasa nitakuwa mwana mitandao,..anayeweza kudhibiti, au kuingie kwenye aina yoyote ya mitandao, huhitaji namba ya siri, hiyo ni nama ya siri, ya kuingia popote pale…nimeipata..lakini…haijakamilika…’akatulia

‘Unataka nini tena, tamaa zako hizo, ndizo zitakuangamiza…na najua mwisho wako umefika,…’akasema huyo mwanamke sasa akijitahidi kukaa. Na yule jamaa akawa anamuangalia kwa makini huyo mwanamke, machoni..alijua kama huyo mwanamke kaiona hiyo bastola macho yake yataelekea huko..lakini kumbe hata huyo mwanamke hakuona wapi hiyo bastola ipo…

Mimi pale nilipo macho yalishaanza kuwa manzito, mwili wote umelegea na wakati wowote ningeliweza kulala chini…na kupoteza fahamu, lakini nilijua ile bastola ni muhimu sana, …kuhakikisha haifiki mikononi mwa huyo shetani,…
Mara yule mwanamke akaiona,…alitupia jicho paaa, akaiona na kujivunga kuangalia upande mwingine, lakini hakuweza kumvunga huyo jamaa , na yule jamaa akatupia jicho upande ule, akaiona….

NB: Ilikuwaje....


WAZO LA LEO: Usipojenga tabia ya kuridhika, ukipata kidogo unataka kingi, hata kama sio halali yako, ukiona mwenzako anacho unataka na wewe ukipate tena sio kwa halali..ujue moyo wangu umetawalia na shetani,..tamaa hiyo ni mbaya, na wengi wenye tamaa hiyo ndio wale hata wakiwa na madaraka, hata wakiwa matajiri, bado hawatosheki..wapo tayari hata kuua..wapo tayari hata kujiunga kwenye makundi ya kishetani..lakini wakumbuke kuwa mwisho wake ni wapi…wangapi wangapi walikuwa hivyo na sasa wapo wapi!
Ni mimi: emu-three

No comments :