Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, May 15, 2017

MPENZI WA FACEBOOK-27


Mpelelezi, alipoona dereva kakiuka maagizo yake akaingiwa na shaka, hakuelewa ni kwanini mtu mdogo kama yule asitii maagizo yake, na haijawahi kutokea, na baya zaidi alipompigia simu akawa hapokei,

‘Ni kwanini huyu mtu anafanya hivi…au..?’ akajiuliza na hii ilimpa dalili mbili, kuwa kuna tatizo la kiutendaji , na anatakiwa kuchukua hatua za kinidhamu, lakini kinamna fulani alihisi hatari, au kuna mkuu zaidi yake katoa amri,na kama ni hivyo, basi..huenda kuna jambo nyuma ya pazia kwahiyo inabidi achukue hatua ya haraka, na akilini mwake, alitekwa na ile kauli nyingine ambayo hakupenda kuisikia,..

‘Hakikisha hao watu hawafungui mdomo, wakifungua mdomo wao, basi ujue wa kwako utafungwa..’ hakupenda kauli hii , hakupenda kauli za vitisho, lakini alijua huyu mtu aliyemuambia hivi hatanii….na hapo akahisi mwili ukimsisimuka.

Mpelelezi aliyekuwa akilifuatilia hilo gari kwa nyuma…alikuwa ameliacha nyuma kwa kukingwa na magari matatu mbele yake..,  akaona ni lazima asitishe mikakati mingine yote, kwani ikiendelea itakuwa ni hatari,..ndio hapo akachukua simu na kusema maneno haya;

Mission abort turn back now …’akasema na kukata simu.

 Akiwa na hasira, akamwambia dereva wa boda boda aongeze mwendo,..kulifuatilia hilo gari kwa karibu sasa… lakini kwao haikuwa rahisi maana  mbele yao wakakutana na ajali ya gari, kukawa na folen kuwa, hapo akasema;

‘Unaona hawa watu niliwaambia wasingie njia kuu, sasa unaona kitu kama hiki, nashindwa hata kuchukua hatua, ngoja nione …’akasema na mwenye boda boda akasema

‘Lakini hii ajali ni magari yalikuwa yakiingia njia kuu, na inaoenkana jingine lilikuwa likitoka,… kwa haraka, utafikiri watu wamepanga haiwezekani mtu mwenye leseni akafanya hivyo….’akasema dereva wa boda boda, na mpelelezi hakupendezewa na maneno yake akasema

‘Vyovyote iwavyo amri zetu hazipigwi, maana sisi wakubwa tunajua ni kwanini tunatoa amri fulani, sasa sijui kama wameweza kupita eneo hili, maana siwani huko mbele na dereva hataki kupokea simu yangu,..’akasema akikagua kwa macho kulitafuta lile gari, lakini hakuliona

‘Walishapita mkuu, niliwaona pale tuklipokuwa tunapishana na lile gari kubwa la mizigo…’akasema dereva wa hiyo boda boda

‘Ok, sasa fanya haraka tulifikie,…sitakiwi kuwa mbali na hilo gari…na huyo dereva huko kituoni, atanitambua kuwa mimi ni nani…’akasema na mara akipigiwa simu na sasa akawa anaongea na watu wake wengine, mara akasikia taarifa iliyomfanya ashtuke kidogo, akasema;

‘Hebu simama kidogo,…’akasema na kutoka nje, akawa sasa anaipokea simu, akasikiliza kwa muda halafu akasema;

‘Usijali..nitalifanyia kazi…’akasema na kurudi kwenye boda boda, baadae wakafika kituoni.

Tuendelee na kisa chetu…

**********

Walipofika kituoni, alikuta wale watu wawili wameshapelekwa mbele ya mkuu maalumu wa kesi za ndani, na yeye akafuatilia, kahakikisha taratibu muhimu zimefuatwa, huku akiwapigia badhi ya watendaji wake kuendelea kumsaka binti..

‘Na huyu binti atakuwa sehemu muhimu ya kulimaliza hili, najua kila kitu nitakiweka sawa,na nitahikikisha huyi mtu anayenifanya nisiwe na raha, …namweka sawa, hanijui mimi..’akasema kwa sauti ndogo sasa akielekea kwa mkuu wake wa

‘Nimeshawaleta mkuu, inabidi baadae niweze kuongea nao kiundani, nimeona kwanza niwafikishe huku, halafu mengine yatafuata baadae…’akasema

‘Vizuri, nilishaambiwa wameshafika…’akasema mkuu wake

‘Na nani na mimi ndiye nilikuwa naifanya hii kazi,…’akasema

‘Unajua…nahisi kuna watu walikuwa na mpango dhidi ya hawa watu wawili…’akasema mkuu

‘Mpango gani mkuu, haiwezekani, ni nani kakupa hiyo taarifa mkuu...?’ akauliza mpelelezi kwa mashaka.

‘Kuna mpango wa kuwamaliza hao askari wawili, kwa vile wakiendelea kuwepo watasema kwanini waliachia binti akapita, nina imani kuwa huyo binti hakupita hivi hivi bila ya wao kuhususishwa, kwahiyo hawa askari wanajua mengi, …’akasema mkuu

‘Mhh…sijui kama kuna ukweli wa hilo mkuu…mimi ndiye nastahili kusema lolote maana ni askari wetu nawafahamu sana,, …na kama labda kuna watu wa nje ni akina nani hao,ngoja nitalishughulikia mara moja mkuu na ukweli utafahamika…’akasema

‘Hao watu ni wajanja sana,,,, walipanga kutengeneza ajali, ili magari yote yakwame…’aliposema hivyo mpelelezi akawa kama kashtuka, na kusema;

‘Mkuu hizo habari umezipatia wapi…?’ akauliza.
‘Ni jambo lisilo na mantiki,..na haya yote ni kuonyesha kuwa kuna watu ndani yetu wapo sambamba na hili kundi haramu,  lakini, nitahakikisha hili kundi na hao vibaraka wanafikishwa mbele ya sheria.…’akasema mkuu akionyesha dhamira ya kweli, na mpelelezi hapo akanywea na kusema;

‘Mkuu mimi nipo na wewe, tatizo ni huu utendaji wa kugawa makundi, wengine wanafanya hivi wengine vile huu utendaji unanipa wakati mgumu sana…’akasema mpelelezi akionyesha wasiwasi

‘Tumewakamata  hao watu waliotaka kuwamaliza hao askari, na wao wataingia chumba maalumu , najua humo watataja kila kitu ni nani kawatuma kufanya hivyo, na hiyo ni awali tu, nitahakikisha wote na huyo mkuu wao wamekamatwa…’akasema huyo mkuu, sasa akimtupia jicho la kujiiba kumuangalia mpelelezi

‘Mkuu mimi nitalisimamia hilo zoezi..’akasema mpelelezi

‘Hapana wewe endelea na kazi yako,…najua wewe una majukumu mengi,kwanza kwa hivi sasa nataka tuwe pamoja hapa kituoni, kazi za kuzunguka, nataka msaidizi wako azifanye yeye..nina mambo nataka tushuirikiane,…’akasema mkuu.

‘Kwanini mkuu, unajua kazi zangu zilivyo, kukaa ofisini sio fani yangu…nataka niwe mstari wa mbele kwenye mapambano…’akasema mpelelezi.

‘Najua..ni swala la muda mfupi tu..baadae utendelea na shughuli zako kama kawaida, ni leo tu, baada ya leo kazi zitakuw rahisi..tutamaliza kazi…’akasema mkuu,

Maneno haya ‘ni leo tu..’ aliyasikia kwingine, na sasa kayasikia hapa tena, je ni masikio yake au kuna namna ya taarifa zinavuja, alikumbuka kuambiwa hivyo kabla.

Leo tunataka kumaliza kazi, baada ya leo,…kazi yetu itakuwa kiuingiza..ni leo tu, baada ya leo hakuna kazi nzito….’aliambiwa maneno hayo kabla.

Mpelelezi alihisi mwili ukimsisimuka, akaanza kuwazia mbali, alijua mikakati yake itafanikiwa na mwisho wa siku ataweza kuonekana shujaa, wa kuweza kulizima kundi hilo , lakini kumbe njia yake imekuwa na ngumu, na amejikuta yupo kwenye mtihani mkubwa wakuamua lipi lifanyike kwanza…

‘Oh..nahisi muda umefika…’akasema akilini.

‘Sasa ni hivi ninataka mimi na wewe tuelekeza nguvu zetu kwenye kumpata huyo binti kwanza, najua wapi alipo, lakini hatuwezi kwenda moja kwa moja, mpaka tujue ni kwanini kafanya hivyo, na …yupo nyuma ya nani,…umenielewa mikakati yangu, huu sio muda wa kutumia nguvu, umenielewa..?’akasema mkuu wake

‘Bila shaka mkuu,,,;akasema na kugeuka kuelekea ofisini kwake.

 Na mkuu huyo akawa kasimama akimuangalia huyo mpelelezi akitembea kuelekea ofisini kwake, aliona kuyumba kwa hatua za askari huyo shupavu, alimuamini sna, na alijua kuna kitu kimemsukuma kufanya hivyo anavyofanya, lakini hakuwa na muda wa kubembeleza tena, wakati sasa umefika. Alichukua simu yake na kutoa amri kuwa mtu yoyote asitoke bila ya kibali chake.

Mkuu akarudi ofisini kwake,..baadae akaona aende seehmu alipo docta, ili aone kama anaweza kupata lolote, na ikibidi amuelezee baadhi ya mipango yake, na alipofika chumba ambachp docta alikuwa anakaa, akakuta hayupo…

‘Docta kaenda wapi..?’ akauliza

‘Docta kasema wewe umemruhusu kuondoka..kwenda kwa mgonjwa, anasema binti yupo kwenye hali mbaya anahitajika kwenda kumuhudumia,, ..’akasema askari aliyekuwa akimlinda docta.

‘Nani kamruhusu huyu mtu, mimi sijamruhusu kuondoka, kwanini anasema hivyo, ni lazima kuna jambo…ni kwanini ukafanya hivyo, nilikuambia nini…?’akasema kwa hasira na sasa akawa akimpigia simu docta.., lakini  simu yake ikawa inaita tu haipokelewi.

‘Huyu mtu anataka kufanya nini….?’ Akawa anajiuliza bila jibu, na kwa haraka akaenda ofisini  kwake kuangalia mitamabo yake maalumu, hakuweza kupata kitu cha kumsaidia, hapo akaamua kwenda ofisini kwa  mpelelezi, akakuta naye hayupo

‘Na huyu naye kaenda wapi..?’ akauliza mkuu kumuuliza muhutasi wa ofisi ya upelelezi

‘Kasema kaenda huko ulipomtuma…’akasema katibu muhutasi wa idara ya upelelezi.

‘Nilipomtuma mimi!…hapa kuna tatizo, ofisi hii mnanishangaza sana, kwanini hamtii amri za viongozi wenu, nitaawajibisha ofisi nzima…’akasema akitoka nje kwa hasira, na kuingia ndani ya gari lake..

‘Twende makaburini….’akasema akimuamrisha dereva wake

*************

Docta akawa sasa keshafika kwenye nyumba ya mzee ambayo sasa yaonekana kama imetelekezwa,kwani mpangaji aliyekuwepo hapo awali keshafariki…na katika hisia zake, alijua kabisa mpelelezi atakuwa kaja eneo hilo, hakuweza kumfuatilia kwa karibu lakini kwa jinsi alivyomuona akitoka pale getini , alijua kabisa safari hii itaishia hapa..

Ilikuwa ni bahati tu, wakati alipoamua kutoka nje kupata hewa safi, akawa kasimama kwenye mti, na akiwa kaangalia ofisi ya mpelelezi, mara akamuona mpelelezi akitoke kwenye hiyo ofisi, na akawa anaongea na askari mmojawapo,…na haikupita muda akaja bajaji, na mpelelezi huyo akaingia kwenye bajaji, na kundoka nayo..

‘Nilisikia mkuu akisema mpelelezi leo hatakiwi kutoka, mbona kaondoka , tena anaonekana ana haraka,…’ docta alijiuliza na hakupoteza muda, akaingiwa na maamuzi ya haraka, alitaka kumpigia mkuu, lakini akaona anapoteza muda, na yeye akaingia ndani na kuvalia vazi lake la udakitari, na kubeba mkoba wake, akaelekea getini

‘Unakwenda wapi docta..?’ akaulizwa

‘Nimeambiwa kuna mgonjwa mahututi, natakiwa kumuwahi,…’akasema na ilikuwa ni bahati walinzi walikuwa wakikabidhiana, ..huyu anayeingia alikuwa hajapata maagizo kamili kuwa watu hawatakiwi kutoka leo bila idhini ya mkuu, na huyo mlinzi mpya, akajua docta ni mtu muhimu hawezi kudanganya akageuka kumuuliza mwenzake..Docta hakupoteza muda, akatumia mwanya huo, na kutoka nje na kwa haraka akaiwahi bajaji iliyokuwa ikisuburiwa.

‘Hapa nacheza pata potea,..huenda huyu mpelelezi anakwenda kumaliza kazi,…’ akawaza hivyo docta huku akijua kafanya kosa kuondoka bila kibali cha mkuu wa kituo.

‘Inabidi nilifanye hili, maana huyu mkuu, hata yeye sasa simuamini , ni kwanini ananishikilia mimi hapa kituoni, kama mfungwa, hajui kuwa nina wajibu mkubwa kwa familia ya mzee…hao wazee hawatanielewaje kama lolote litatokea kwa binti yao…’akasema.

‘Mpaka wapi mzee..docta..?’ akauliza dereva wa boda boda

‘Wewe nishushie karibu na yale makaburi…’akasema akimuelekeza dereva wa boda boda.

Docta akafika sehemu aliyoona ni sahihi, hakutaka kuikaribia moja kwa moja nyumba ya mzee, akavua koti lake la udakitari, na kulikunja, na kuanza kutembea sasa kuelekea kwenye hiyo nyumba iliyotekelezwa ya mzee, akipitia kwa nyuma, ili kukwepa macho ya watu…kila alipokuwa akiikaribia hiyo nyumba ndivyo alivyohisi  mwili ukimsisimuka,…

‘Hii ni dalili mbaya…’akasema lakini hakuweza kurudi nyuma, alijua akichelewa tu atamkuta binti wa mzee, ni marehemu na hapo itakuwa mwisho wa uaminifu kati yake  na hiyo familia ya mzee na mkewe!

‘Kwanini mkuu huyu hakuchukua hatua za haraka za kufika huku, najua anafahamu kabisa kuwa huyu binti atakuwa katorokea huku…na kuwepo haap peke yake ina maanisha nini,…kuw ahuyu binti kwa hivi sasa sio yeye, anatembea kama roboti tu, na huenda mkuu anamtumia huyu binti kama chambo, lakini ni hatari kubwa sana…’akasema sasa akiwa kasimama nyumba ya ukuta wa hiyo nyumba, akaangalia huku na kule kwa haraka akaruka ukuta na kudondokea ndani.

Alipohakikisha kuwa hakuna walinzi kwa ndani, akatembea hadi kwenye mlangow a nyuma…

Akachukua ufungua wake Malaya, akaweka kwenye kitasa baada ya kuhakikisha mikono yake imevaa kinga, akafungua kwa kutumia ufungua huo bandia, haikualika mlio wa kufunguka, ina maana mlango ulikuwa haukufungwa kwa ufunguo…akasita kidogo, lakini baadae akazungusha kitasa cha mlango, na mlango ukafunguka.

Ina maana mpelelezi naye alitumia mlango huu…akawaza hivyo, na hakupoteza muda akaingia ndani!

Docta akajua sasa yupo uwanja wa vita, hisia zote zilionyeha yupo kwenye hatari, lakini hakujali, alichojali ni kumuokoa huyo binti, na ..kwa hali ilivyojitokeza hakuamuamini kabisa mpelelezi, ndio inawezekana alijua wapi binti alipo, na sasa alitaka kuonyesha kuwa anafanya kazi yake vyema, atamchukua huyo binti hadi kwa mkuu wake na kusema;

‘Huyu hapa nimempata…’ atasema akimkabidhi huyo binti kwa mkuu wake, na ataonekana mtendaji mwema, na makosa yake yatafijichika, na kuendelea kufanya akzi zake kama mtu mbili…lakini pia anaweza akawa katumwa, kummaliza huyo binti kwani yawezekana ndio kafara lao la mwisho kama alivyoipata taarifa hiyo kutoka kwa mtu wake wa karibu.

‘Wanajiandaa kufanya kafara la mwisho, na ina maana kuna damu itamwagwa, kwa wingi, be careful…’alitumiwa ujumbe na mtu wake kutoka nje ambaye analifuatilia tukio hilo kwa karibu sana.


Alihisi mwili ukimsisimuka, kwa hali kama hiyo inaashiria kuna mashetani, na kwa jumba kama hilo ambalo halitumiki kwa muda, basi wadudu hao watakuwa wamefanya masikani yao humo na watu wabaya hasa..hasa hilo kundi huenda wanalitumia hilo kama makao yao ya usiki,…

‘Na huyu binti atakuwa ndondocha tayari…hajitambui, sizani kama anajijua…’akasema docta.

Akaingia ndani , na  pale varandani au chumba cha maongezi hakukuwa na kitu chochote ni kama palivyoachwa,..chumba kilikuwa kimia, na hali fulani inayofanya mwili uhisi baridi,..ilikuwa kama ni kwenye giza watu wamejificha wanakuangalia,..alihisi hivyo, alijua ni hao wadudu…hakujali, aliweka mbele ujasiri, kutokuogopa,…alijua ni wapi aelekee,… chumba cha mabinti..

Kwa tahadhari akaelekea huko, na alipofika, alikuta mlango upo nusu wazi, akatumia ule upenyo kuangalia ndani, hakuweza kuona kitu, kwa mguu akausukuma mlango taratibu, ukawa wazi, na kwa kasi ya ajabu akajirusha na kudondokea ndani,….akiwa tayari kupambana na lolote japokuwa alikuwa mikono mitupu!

Alivyoruka na kujizungusha kwa haraka, na pale chini akawa kama kachuchumaa, mtindo wa watu wakianza mbioa wanavyokaa, huku macho yakicheza huku na kule..ni mazoezi yake ya muda mrefu, na wakati huo huo hisia zake za mwili zikawa zinafanya kazi, pua ikanasa harufu isiyo ya kawaida,…harufu ya maiti..

‘Oh, maiti…kuna dalili kabisa ya maiti..’akili ikasema hivyo.

Chumba kilikuwa kimia, japokuwa hisia ziligundua kuwa kuna hiyo dalili ya maiti,na damu, huenda maiti hiyo imekufa kwa kumwagwa damu…docta anaijua sana harufu hiyo, na sio ya kubahatisha, hapo mwili ulimuishia nguvu,  ni maiti ya nani, na humo chumbani, kama alivyoona kwenye video mbashara yake aliyekuwemo humo alikuwa mdada…na ambaye angeliweza kuingia kwa muda huo ni mpelelezi, huo sasa ni mtego!

‘Hawezi awe ameshainga na kuifanya hiyo kazi na kuondoka…’akawaza hivyo

‘Au alikuta binti keshauwawa, akaamua kuondoka, maana kuja kwake hapo sio rasmi…vinginevyo kuna mtego humo ndani…’akawaza hivyo docta, lakini mawazo hayo yalikuwa kwa muda mfupi sana, kabla hajaangza macho kitandani ..na macho yake yalipotua kitandani, akamuona,…mdada!.

Akiwa kwenye tahadhari, akawa sasa anachungulia kitandani, binti alikuwa kalala chali, sehemu ya miguu yake imening’inia, kalala akiangalia juu, mdomo wazi, inaashiria nini..ooh, sio yeye, haiwezekani wameshamuua huyu binti wa watu….na alipotizama vizuri akaona damu, sehemu ya kushoto, kwenye bega, au kwapani au sehemu ya titi la kushoto…..

‘Oh wameshamuua…’akasema

Ni kitendo cha haraka na macho yalishaangaza kona za chumba, na ndipo akagundua kitu,…pembeni ya mlango, kulikuwa na mtu kachuchumaa, karibu na mlango, bastola mkononi… ina maana alipofungua mlango huyo mtu alikuwa nyuma ya mlango…lakini ile hali ya kuchuchumaa ilikuwa sio ya kawaida, ni kama kaegeshwa …huyo mtu alikuwa tayari maiti! Paji la uso lilikuwa na tundu la risasi…

‘Oh, maiti wa wawili…’akasema docta sasa mwili ukianza kufanya kazi ya hali halisi na kabla hajakaa sawa mlango ukafunguliwa kwa kasi.

‘Polisi…MIKONO JUU’ ilikuwa sauti kali

NB: Jamani sehemu hii mniwie radhi kidogo nimeandika KWA HARAKA KIDOGO, ili twende na wakati, tumechelewa sana kukimaliza kisa hiki!


WAZO LA LEO: Unapopata kitu, iwe madaraka au kipato, ni kawaida kwa uanadamu wetu kujiona ni zaidi au hata kufikia kuzarau wengine, na kuwaona wengine abda ni wazembe. Ni kweli umepata, mshukuru mola wako, na moyoni uitakidi kuwa hayo yote sio kwa ujanja wako, mpaji ni mola pekee. Yeye ndiye kakupa na kumfanya mwingine akose kwa madhumuni maalumu, anayejua sababu ni mola peke yake,..tusifikie hatua ya kukufuru na kuwazarau wengine kuwa labda wao ni wajinga, cha muhimu ni kusaidia pale inapowezekana, na kuzidi kuwaombea wengine wapate kama ulivyopata wewe, huo ndio wema wa muungwana, kwani leo kwako kesho kwa mwingine!
Ni mimi: emu-three

No comments :