Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, April 19, 2017

MPENZI WA FACEBOOK-9

Mpenzi niliyempata facebook amenisukuma hadi nikaingia kwenye matatizo ambayo sikuyategemea, ni kweli kama ilivyoonekana matatizo hayo chanzo ni mimi na sikulifahamu hilo hadi tulipoanza kufuatilia, kutokana na matatizo yaliyonipata, na matatizo hayo yasingelinipata kama nisingekuja kuwa na mahusiano ya mtandao na huyo mpenzi wa facebook.

Katika kulifuatilia hilo tatizo nikiwa na docta, tukafika hospitalini maana Mzee Mashauri, baba wa binti ambaye niliwahi kuwa na mahusiano naye, binti ambaye sasa ni marehmu, ambaye kama ilivyoonekana ndiye chanzo cha matatizo ya hiyo familia, na kuanguka kwa huyo mzee kumetokana na binti yake mwingine ambaye anaumwa siku nyingi, na kuumwa kwake kunatokana na kufariki kwa dada yake, dada ambaye wanasema kajiua kutokana na mimi kumkataa wakati nilishaahidi kuwa nitamuoa..

Ni kisa chenye historia ya nyumba, mambo niliyowahi kuyafanya nyuma, na kuwadhuluma watu, nakuja kupata matatizo yake kwa hivi sasa.

Nikiwa hospitalini, nikimsubiria docta, ili ikiwezekana na mimi niweze kuonana na hiyo familia, ambayo inapata taabu kutokana na tatizo langu… naanza kuchanganyikiwa….nahisi kuna mtu yupo karibu yangu ananifuatilia, lakini simuoni huyu mtu, nageuka huku na kule hakuna mtu karibu yangu….ina nahisi yupo mtu, nahisi akihema, nahisi ukaribu wake…

Tuendelee na kisa chetu..

*************

Nilihangaika nikijaribu kuikwepa ile hali, maana kiukweli nilikuwa nahisi kuna mtu yupo karibu yangu hata nikisogea sehemu nyingine , bado ananifuatilia lakini huyo mtu haonekani, ...na alikuwa sambamba na mimi haniachii.

Nilipoona siwezi kumuona au kumuacha, nikatafuta njia nyingine, kama nilivyosema moyoni mwangu nimejijengea tabia ya kutokuogopa kirahisi, hapo mimi nikatafuta ujanja, nikaanza kutembea kuelekea kule walipokuwa wamekaa watu wengine.

Na hilo zoezi likafanya kazi,…nilipowakaribia watu nikahisi huyo jamaa hayupo tena,  nikasema ngoja nirudi nielekee sehemu nyingine , sehemu ya mapokezi, nikahisi huyo mtu akiwa karibu name tena…, 

'Hivi wewe nani..?’ nikauliza

Sikupata jibu, nikaona narudi muelekeo ule wa awali, pale walipokaa watu, ilikuwa eneo la wodini,… nikagundua, nikielekea muelekeo huo, huyo mtu, au au huo mwangwi wa mtu unapotea.

Basi nikaona nielekea huko eneo la wodini, hadi sehemu watu wanaposubiria kuingia kuona wagonjwa nikaa kwenye benchi, na pale walikuwepo watu kadhaa, sikuweza kuhisi mtu kuwa karibu nami, basi nikatulia hapo, na wale watu waliokuwa wakisubiria kuingia kuona wagonjwa, nikasikia wakiongea jambo…

'Huyo mama wa ajabu kweli, ….kachanganyikiwa lakini akikuelekeza jambo, ufanye unafanikiwa na ukiwa na tatizo lako anakulekeza…na kila mtu aliyeagizwa afanye hivyo, akifanya hufanikiwa ….yaani imekuwa ni ajabu ya mwaka…’akasema mtu mmojawapo.

'Unajua hata mimi jana nilikuwa nabisha , nikaenda kumuona akaniambia shida yangu, sijui alijuaje..basi nikafanya alivyosema nifanye nikaitatua, sasa leo nina shida nyingine nataka nimuone nione kama atasemaje…’akasema.

 Basi nikaona watu wanaongezeka, kila aliyefanyiwa hivyo anakwenda kumueleza mwingine, hapo na mimi nikaingiwa na hamasa, sina imani hizo lakini kwa ajili ya kupoteza muda, nikaona na mimi nijaribu nione huo ukweli, kwanza nikajiuliza nina shida, je inatakiwa ufanyeje…mmh, ..nikaona nisiwaze sana ngoja kwanza niwaulize hao watu.

'Kwani inakuwaje…unatakiw ufanyeje…?’ nikawauliza.

'Wewe unaingia hapo kwenye hicho chumba, kuna mdada kachanganyikiwa lakini cha ajabu, yeye ana sijui miujiza gani, hao manesi wanamtumia kama mradi maana ili umuone ukiingia unaweza pesa mezani,..halafu wewe ukimsogelea tu anakutajia shida yako na jinsi gani ya kuitatua…’akasema jamaa.

'Ni mganga wa kienyeji?’ nikauliza

'Wala, huyo kaleta hapa akiwa kachanganyikiwa tu, ila ndio hivyo, kama una tatizo, ingia, na weka mia tano mbele yake, ndio ushuru wake, utashangaa atakachokuambia.

 Nikataka kuondoka, lakini nikasema kwanini nisijaribu tu kupoteza muda, nikatafuta mia tano mfukoni, nikasubiria, zamu yangu ikafika, nikaingia,…nikamkuta mama mmoja kajifunika gubi gubi,..na nilipomkaribia tu, akasema;

'Una matatizo yako ya kuchanganyikiwa, ukitaka kupona, nenda ukamuoe huyo mpenzi wako wa facebook, shida zako zitakwisha….’akasema

‘Eti nini…?’ nikajikuta nauliza kwa mshangao…

 Huyu m-mama, kajuaje hilo,… mpenzi wangu wa facebook…lakini cha ajabu zaidi eti ili niondokane,na tatizo langu inabidi nimuoe huyo mpenzi wa facebook, nitamuoje wakati sijawahi kumuona..

'Una matatizo yako ya kuchanganyikiwa, ukitaka kupona, nenda ukamuoe huyo mpenzi wako wa facebook, shida zako zitakwisha…’akarudia kusema hayo maneno

‘Simjui na wala sijawahi kumuona…’nikasema

‘Mtafute…hiyo ni kazi yako, unataka nikutafutie mimi , kwanini mimi ninashida, wewe ndiye mwenye shida, mtafute,...…nimemaliza..ondoka…’akasema.

 Basi mimi nikaona niondoke tu,..nikarudi nje na kukaa kwenye benchi, na watu wakawa wanazidi kumsifia huyo mwanamke kwa jinsi anavyojua matatizio ya watu na kuwaelezea njia za kuyatatua. Mimi baadae nikaamua kumuuliza jamaa mwingine,

'Mna uhakika na hayo maneno ya huyo mama aliyechanganyikiwa,…’ nikauliza.

'Ndio… hakuna aliyewahi kuambiwa akashindwa kufanikiwa…’akasema huyo jamaa

'Hata akikuagiza umuoe shetani…?’ nikauliza.

'Hawezi kukuagiza kitu ambacho hakiwezekani..’akasema huyo jamaa.

'Hahaha, hawezi , mbona mimi kaniagiza nikamuoe mtu ambaye sijawahi kumuona na watu wanasema huyo mtu ni shetani..’nikasema na watu wakabakia kuduwaa, na mmojawapo akasema;

‘Hebu rudi ena huenda hukusikia vyema,…’akasema na mimi nikaamua kurudi tena ndani.

'Wewe nimekuambiaje, nenda kamtafute huyo mpenzi wa facebook, umuoe, si una mpenzi wako wa facebook, au…’, akasema kwa sauti ya ukali.

'Huyo mpenzi wa facebook, hayupo, wengine wanasema huyo ni shetani, wengine wanasema ameshakufa, na sijui niamini kipi…’nikasema.

'Na wewe unasemaje, ..?' akaniuliza kwa sauti ya ukali, kabla sijajibu akasema

'Fuata hicho unachokiona wewe ni sahihi,..na tatizo lako litaisha, usipofanya hivyo utaendelea kuteseka, na utakuwa kichaa...nenda kamuoe huyo mpenzi wako wa facebook haraka iwezekanavyo..., haya ondoka na usirudi tena hapa…’akasema kwa ukali na kusimama kama anataka kunivamia, ikabidi niharakishe kutoka nje.

Basi nikatoka mle ndani nikiwa sina shauku tena na hayo mambo niliona ni mambo y akunichanganya tu kichwa changu,..isitoshe huyo mama kachanganyikiwa anaweza kuongea lolote tu.

Nilipotoka nje,..nikawa narudi kule nilipokuwa awali, nikiwa nimesahau yule mtu aliyekuwa akinifuata fuata, sikuweza kuhisi ile hali tena,  nikiwa sasa naangalia huku na kule, kuona kama wenzangu wameshatoka huko ndani kumuona mgonjwa, nikawaona na wao wananitafuta.

'Ulikuwa wapi wewe…?’ akaniuliza docta.

'Nilinyosha miguu kidogo nikaenda wodi zile kuangalia wagonjwa..’nikasema.
 
'Sasa,sikiliza, nimeshapata kibali cha kumuhudumia huyo binti, na nimeweza kumuona, japokuwa sikuweza kuongea naye.. hatikisiki, yupoyupo tu, na dawa ninayoijua kwa hivi sasa ni wewe uende ukaongee naye…’akasema.

'Docta, kama wewe umeshindwa kuongea naye, huyu mwanafunzi wako atawezaje kuongea naye, …?’ akauliza huyo mzee.

'Hilo niachie mimi na mwanafunzi wangu,…huyu mwanafunzi ana kipaji,..ndio maana nikamchukua, akikutana na huyo binti, ataweza kufanya maajabu, wewe subiria tu…’akasema docta, na kiukweli sikumuelewa huyo docta ana maana gani, maana mimi sina kipaji kama hicho.

 Mara docta akanisogelea na kuninong'oneza jambo sikioni, sikuamini alichoniambia, nikabaki nimeduwaa…nashindwa kukataa au kusema lolote, na mara docta akasema;

'Nakupa nusu saa nitakuja kuona matokea yake, usichelewe ni nusu saa tu ukichelewe utaharibu, …, uwanja ni wako, na ole walo uniangushe…’akasema docta.

‘Lakini docta…’nikataka kujitetea, na docta akaniashiria kwa kidole, kukiweka mdomoni kuwa nisiongee jambo, na docta akamshika huyo mzee mkono kumuashiria waondoke,..na kweli hao…..wakawa wanaondoka eneo hilo.

Nikabakia nimeduwaa, na mara akilini nikaanza kusikia sauti ikiniambia, ni ile sauti ya yule mwanamama aliyechanganyikiwa, ilikuwa ikisema;

'Ukitaka matatizo yako yaishe, uende ukamuoe huyo.mpenzi wako wa facebook…usichelewe…la sivyo utazidi kuchanganikiwa zaidi..’hiyo sauti ikasema kichwani mwngu ikijirudia rudia,.

‘Oh..jamani hii ni nini tena…’nikawa nashika kichwa, nikageuka kule walipokuwa docta na mwenzake, wakawa hawaonekani…

‘Huyu mama ananiambia hivyo, sasa huyu docta naye ananiletea hoja nyingine…nitafanyaje..’nikasema na nilipoangalia saa yangu, saa dakika kama mbili zimeshapita, nikainua miguu yangu kutembea kuelekea huko wodini…

'Unakwenda wapi sasa, hutaki kumuoa huyo mpenzi wako wa facebook, hutaki matatizo yako yaishe, ukumbuke, na wewe unaumwa…wewe unajali wenzako zaidi ya kujijali wewe, kwanza fuatilia matatizo yako…, na kupona kwako ni kumuoa huyo mpenzi wako wa facebook,...'nikasikia sauti hizo zikinighasi kichwani.

‘Hawa wanataka nini….mbona mnanichanganya…’nikasema huku nikishika kichwa,

Nenda kwa huyo binti mwambie unataka kumuoa, mwambia unampenda umekuja kumposa…ukifanya hivyo utaona matokea yake...’sauti ya docta ya kunong’ona ikasikika tena sikioni mwangu.

‘Sasa nitamuoa nani…na nitamuoje huyo binti mgonjwa ambaye hajiwezi, keshakuwa kama kilema, wanasema sasa hata kutembea hawezi,..nasikia hata kuona sasa imekuwa ni tatizo..huyu docta ananitakia mema kweli..’nikasema, na nilipoangalia saa dakika tano zimepita.

Nikaanza kutembea kuelekea kwenye mlango wa hiyo wodi aliyolazwa huyo binti..wa sasa ni hatua ya mwisho, kuamua nimuoe nani, mpenzi wa facebook au huyo binti, kilema, aliyechanganyikiwa…

Nikashika mlango, nataka kuusukuma na mara nikahisi kitu, au mtu ananishika begani, nikageuka nyuma simuoni mtu…

NB: Kuna nini hapa,…


WAZO LA LEO: Mitihani mingine inaweza kuwa mizito sana kwetu, kila ukifanya hili hufanikiwi na matatizo yanazidi kila siku, inapofikia hapo, wa kumkimbilia ni mola wetu,… mtegeeme yeye, na yeye ndiye atakupa njia, usije ukakengeuka na kusikiliza kauli zenye mlengo wa kukuingiza kwenye shiriki, kumbuka kumshirikisha mungu ni dhambi kubwa sana.

Ni mimi: emu-three

No comments :