Mpenzi wa facebook, kazua mambo,...kafukua dhuluma iliyokuwa imejificha, ni kisa kinaendelea, na docta kaamua kulifuatilia hili tatizo, je ni kwanini docta aamue, kulifuatilia, badala ya kutoa tiba, ni kwanini aamue waende mguu kwa mguu hatua kwa hatua, hadi kwenye chimbuko la tukio,..hebu tuone sehemu hii muhimu uone wenye kujua taaluma yao wanavyofanya kazi,
************
‘Siku moja nikaamuuliza baba
yake huyo binti, kwanini binti yake hataki kuolewa, na ana bahati ya
kupata wachumba wazuri tu…?’
Baba yake hakuwa na jibu zaidi ya kusema, hajui….mimi
nikasema moyoni, huenda bado wanachuja, ili wampate mwenye nazo zaidi…lakini
muda ulishapita, makamo ya huyo binti wengi walishaolewa.
‘Sasa baadae ndio nasikia, msiba, kwa bwana mashauri,
nauliza msiba wa nani, wanasema msimba wa mtoto wa kwanza wa huyo bwana…mimi
mbio mbio nikafika kwake,…kilio, kila mtu kataharuki, namuuliza baba mtu ni nini,
hana la kusema.
Basi nilisubiria hali ikatulia, nikamdadisi vyema, ndio
akanitonya kuwa binti yake kazidiwa, na dalili za mwanzo zaonyesha kama kanywa
sumu, lakini bado hana uhakika, …nilishikwa na butwaa, kwanini binti mrembo
kama huyo mpole, ..afikie hatua hiyo…
‘Kwanini amejiua..?’ nikamuuliza
‘Sijui…aheri ningelijua ingekuwa bora…’akasema
Sasa wakati anachunguzwa na madocta nilikuwepo, na ripoti
inakuja kwa baba mtu na mimi nipo nyuma, akaambiwa binti yake kanywa sumu…,
‘Na zaidi alikuwa na mimba, bado change…’akaongeza docta.
Baba mtu alinywea, aligeuza uso huku na huku, hasira, chuki,
kutahayari, maana alikuwa mtu kajijenga heshima zake, watoto wake ni watoto wa
geti kali, …na zaidi huzuni kwa kufikiwa mtoto kipenzi chake.., baadae ndio
nikamuuliza baba mtu.
‘Ulikuwa unajua kuwa huyo binti yako ana mimba, akasema
alikuwa hajui, …labda mama yake, na mama yake alipoulizwa naye akasema alikuwa hajui,…
‘Basi iwe siri yenu, msije kulisema hilo…’nikawashauri..na
kweli ikawa siri ya familia, na mimi kwa mara ya kwanza ndio nawaambia nyie…’akasema
huyo mzee
‘Ahsante sana mzee, umetusaidia sana…’nikasema
‘Lakini hiyo kauli yake ilinitisha,….’akasema.
‘Kauli gani…?’akauliza docta.
‘Kuwa siku akimpata huyo aliyemfanyia hivyo huyo binti yake,
atakachokifanya anakijua yeye mwenyewe, ama zake ama za huyo mtu…alitamka hayo
mbele yangu…na jamaa anajulikana kwa hasira, tokea enzi akiwa jeshini…mimi
namfahamu sana, akidhamiria jambo ukae mbali na yeye’’akasema huyo mzee.
‘Mhh…’mimi niliguna nikajua huko hakuendeki tena, nikamtupia
jicho docta, na docta akaendelea kumdadisi akitaka kujua mengi, mimi kwangu
niliona haina umuhimu tena, muhimu ni kurudi huko tulipotokea…
‘Kwani huyo marehemu alizikwa wapi…’nikamsikia docta
akiendelea kumdadisi huyo mzee, hapo na mimi akili ikafunguka, nikatega sikio
kusikia jibu..,
‘Amezikiwa sehemu inayojulikana kama ‘Makaburini ‘
Hapo utasemaje tena…kama
huamini tena basi ujue una uhimili wa ina yako..
Tuendelee na kisa chetu..
***********
‘Siulisema wewe huna hulka ya kuogopa, au sio, sasa unasemaje…twende tukakabiliane na hiyo
familia, au unasemaje?’ nikaulizwa na docta, muda huo tulishaachana na yule
mzee mwenye nyumba maana alikuwa na safari zake nyingine, tulifanya hivyo baada
ya kubadilishana namba za simu.
‘Mhh, docta, hapa sio swala la kuogopa,…. ni kwamba nikienda huko nitaenda kutonesha
kidonda, na na nakwenda kufanya nini, hebu niambie hapo na wewe,…unielewapo
hapo docta, sio kwamba naogopa, haya,..fikiria mwenyewe kwa makini utaona ni
kwanini nachelea kwenda huko!..’nikasema na docta akaniangalia huku
anatabasamu, hakusema neno na mimi nikaendelea kujitetea.
‘Kumbuka docta, tatizo hili lilitokea siku nyingi, na hao watu watakuwa angalau wameshaanza
kuzoea, japokuwa sio kusahau…kiukweli inasikitisha sana, na inaniumiza
ikizingatiwa kuwa tatizo na chanzo cha hayo yote kimeelekezwa kwangu,…lakini,
mimi sikujua hayo yote…’nikasema.
‘Kwahiyo unasemaje?’ docta hatimaye akaniuliza akiniangalia
usoni.
‘Tuachane kabisa na hili jambo…huo ndio uamuzi wangu…’nikasema
na docta akatulia kimia kama anawaza jambo fulani halafu akasema.
‘Kwahiyo wewe upo tayari kuendelea na huyo mpenzi wako wa
facebook, au sio..upo tayari kuendelea na matatizo yako hayo ya kuchanganyikiwa
au umeshapona baada ya kusikia haya…?’ akaniuliza.
‘Mhh…mimi sijawa na uhakika kuwa huyo mpenzi wa facebook ndio
huyo marehemu, je wewe una uhakika na hilo docta,..?’ nikamuuliza docta na
docta hakunijibu hapo hapo, na mimi nikaendelea kusema;
‘Kama ni swala la kuachana na huyo mpenzi wa facebook, kwani
kuna tatizo mzee…, naweza kuachana naye, tu, si najitoa facebook, au
nabadilisha akaunti, … ‘nikasema.
‘Na hizo njozi, na huko kupagawa, …unaongea peke yako, au uniambie
huko kuongea peke yako labda kuna mtu unaongea naye, ni nani huyo…., mbona
husemi,…au hujioni kuwa haupo sawa..hebu jiangalie ulivyo, ndivyo ulivyokuwa
siku za nyuma, usharobaro wote kwishinie…, sasa hivi upo kama muokota makopo
barabarani, hivi hujioni…’akasema na mimi nikajikagua na kusema.
‘Docta ndio maana nipo kwako, …mimi kiukweli sijijui kabisa…kuna
muda nakuwa kama sio mimi….sielewi,…kama nimewakosea, basi wanisamehe….mimi
sijijui docta…’nikasema sasa nikitaka kama kulia.
‘Kama unahitajia msaada wangu inabidi ufuate yale
ninayokuambia, …’akasema docta.
‘Lakini docta hayo mengine mbona utanitia kwenye kuamini
mambo hayo, wakati mimi sitaki kuyaamini, na kwa mfano, mimi ninaamua kumuuliza
huyo mpenzi wa facebook, kuwa nimegundua kuwa yeye sio mtu, huni kuwa atanicheka
sana…’nikasema
‘Kwanini akucheke…?’ akaniuliza docta
‘Unajua docta katika maongezi yetu mimi na yeye huko nyuma, mambo
tuliyokubaliana ni kutokujishirikisha a mambo ya kishirikiana, yeye alisema
mambo hayo hayaamini na hajishirikishi nayo, na nikaona ni mtu tunaendana, leo
hii nimwambie kuwa nimegundua kuwa yeye sio mtu….’nikasema.
‘Nani kakuambia mwambie hivyo…..au hayo anayokuambia wewe
umeshaniambia yote, au mengine unaficha…’akasema docta
‘Docta kiukweli mimi sina imani ya kishirikina ndivyo nilivyo,…kama
nikuota, ni ndoto tu, hata nikukuambia itasaidia nini..ina maana nikikuambia
nitakuwa nayaamini mambo hayo, mimi sio mshirikina docta…’nikasema
‘Kwahiyo haya mambo tunayoyafanya sasa hivi ni mambo ya
kishirikina…?’ akauliza docta.
‘Kama itakuwa mambo ya kuamini uchawi, mashetani, ..hakuna
jina mbadala na hilo, mimi siwezi kuwa mnafiki, …docta mimi nazungumza ukweli
kutoka moyoni mwangu, kwa jinsi ninavyoamini, kama ninakosea basi unisamehe….,huko
tunakoelekea tutajiingiza kwenye mambo yakishirikina,…. au nimekosea,..tunakuwa
tumejiingiza kwenye imani za giza…mimi docta nashauri tuachane kabisa na mambo
haya…’nikasema.
‘Kijana, ujue hili sio swala la jinsi unavyofikiria wewe, na safari yetu hadi
kufika hapa ni kuhakiki, je huyo mpenzi wako wa facebook, yupo hai,…. anaishi,
na kama yupo tutampataje, haya tumefika hapo kwa huyo mzee, tumeambiwa
alishafariki, hapo unataka kusema nini….’akasema docta.
‘Basi sio yeye,…huyo wa facebook ni mwingine,…huyu na huyo
marehemu hawaendani kabisa ….docta, mimi kitu kinachonilinda nisiamini hilo ni sura…na
kwasababu hii, kwangu mimi ninaona huyu tumtoe katika kufuatili kwetu,….labda
tuanze kumtafuta mwingine…’nikasema.
‘Ni nani mwingine mwenye hulka na tukio kama hilo, kuwa
uliachana naye kwenye mazingira kama hayo, ulimtenda,…ulimdhulumu…. na ukaja kuachana
naye, bila ya masikilizano, ni nani, nitajie mwingine…?’ akauliza docta
akinikagua usoni.
‘Mwingine mwenye tabia kama huyo marehemu au huyo mpenzi wa
facebook….maana hapo unanichanganya,…?’ akauliza.
‘Kama huyu marehemu…’akasema docta.
‘Mhh, kama huyo marehemu hakuna..., na nilishakuambia hao
wengine walikuwa ni wa kupita ti, sina kumbukumbu nao,…sasa labda hao wawili,
lakini haoo wawili wengine walishaolewa, na nakutana nao, tunaongea vizuri tu…,
sijui hata nikumbukeje, inakuwa kazi kubwa, muhimu docta tuachana na hili
zoezi, unasemaje docta…’nikasema
‘No…unajua nikuambie kitu, sisi kuja kuonana na hii familia
ni sehemu muhimu ya tiba yako, sio kwamba najifanyia tu kama mshenga….na kwa
jinsi jambo lilivyo, hutaweza kupona mpaka uonane na hiyo familia,ili kupatikane suluhu fulani, na itapatikanaje
kama usipokutana na wazazi wa marehemu..ulitenda kosa, unakubali hukubali…?’
akauliza docta.
‘Ndio nakubali, kuwa nilitenda kosa, na kipindi hicho
nilikuwa sijatulia,….na nilitenda bila kukusudia…sikujua….mbona wengi wanapitia huko docta...ni kipindi tu cha ujinga...’nikajitetea.
‘Bila kukusudia, wakati ulisema ulifanya juhudi za kila
namna ili umpate huyo binti wa watu, na ukafikia kununua pete ya dhahabu
badnia, ukaitisha shughuli, ukamvika pete,..baada ya hapo sijui ulimfanyaaje
mpaka akakubali, ukatembea naye, kweli si kweli..je hiyo ni bahati mbaya…?’
akauliza docta.
‘Ni ujana tu…’nikasema
‘Ni ujana, ulikuwa na umri gani…?’ docta akauliza
‘Aah, ..unajua docta umri unaweza ukawa mkubwa lakini akili
bado ikawa haijatulia, hujasiki wazee wanafanya mambo ya ajabu….’nikajitetea.
‘Muhimu ni jinsi gani ya ….tunachokifanya sasa kwenye sehemu
ya tiba yako, ni kutafuta jinsi ya kuliondoa hilo kosa, sio jinsi y akutafuta
visingizio vya kukwepa kosa, je unajua jinsi gani ya kuliondoa kosa
ulilomfanyia mwenzako…?’ akauliza docta.
‘Ni kutubu, ni kuomba msamaha, hilo nalitambua sana docta, I
wish angelikuwa hai ningelimuendea na kumpigia magoti mpaka anisamehe…’nikasema
‘Sasa utakwenda kutubu na kuomba msamaha kwa nani,..?’
akaniuliza
‘Si ndio hapo sasa docta…, huyo ambaye nilimkosea hayupo
duniani…basi mimi nitamlilia mola wangu ninajua mungu ni mwema, atanisamehe tu…’nikasema
‘Ni rahisi hivyo, kwa vile sio wewe uliyendewa au sio…’akasema
docta.
‘Sasa docta nitafanya nini , maana hao waliobakia, hawawezi
kunisaidia kwa hilo…na nikiwaendea wao, inaweza ikawa chanzo cha kuzua uhasama
na chuki nyingine dhidi yangu, unamfahamu huyo mzee au unamsikia, mzee Mashauri
alishawahi kutuchapa mimi na mtoto wake mbele ya wenzetu, sitasahau, mpaka
nikikutana naye nanywea, hapana siwezi kwenda kuonana naye…’akasema
‘Ili tiba yako ikamilike, inabidi kufukia haya madhambi
uliyoWAHI kuyafanya, na hatua ya kwanza ndio hiyo,….kuhakiki kama kweli kitu
kama hicho kilikuwepo…’akasema
‘Sawa hata mimi nimelikubali hilo, nakiri nilifanya kosa…’nikasema
‘Na kama tumegundua ukweli kuwa ulitenda kosa, na katika
kutenda kosa, kosa likizaa makosa mengine, haya tusema kosa la kwanza, kama
ulivyodai utamuomba mungu akusamehe, au sio…kwa vile uliyemtenda hayupo tena
duniani, lakini ukumbuke, kama alivyosema mzee pale, kuna mlolongo wa makosa
mengine yamekuja kujitokeza kutokana na kosa la awali, nikuulize je hayo makosa
mengine, utayafanyaje, na je unahisi hayataendelea kuzaa makosa mengine…?’
akauliza docta.
‘Sasa docta unatia chumvi, unakuza haya mambo,….maana hayo
mengine sihusiki tena mimi..ina maana ukitenda kosa, wengine wakaendeleza kosa
kutokana na hilo kosa , mimi nakuwa lawamani, ndio kinaitwa kizalia, au….?’ Nikauliza
‘Unaniuliza tena mimi swali….’akasema docta.
‘Ndio …..maana hayo mangine sikuwepo kabisa… na kwanini
yazae makosa mengine,…kwanini iwe ni kwangu tu, kwani ni mimi wa kwanza kuanza
kuyafanya hayo, hapana, hata mungu anaona, atanisamehe, maana sikuwepo,
sijawaambie wafanye hivyo …’nikajitetea,
‘Sio wewe kwa vipi, wakati sababu ya makosa haya mengine
tatizo ni wewe,, chanzo ni wewe, usikwepe kosa, hilo, ndio maana tunaambiwa
kuwa dhuluma ni mbaya inaweza kumea, na kuhatarisha maisha mengine, ikazua
dhuluma nyingine,..sasa ni bora kuikwepa hiyo au kutafuta njia ya kuisimamisha
hiyo dhuluma isiendelee…’akasema docta
‘Hata sikuelewi docta…’nikasema
‘Unajua wewe ulimtenda mtoto wa watu, alichokifanya ni nini,
…?’ akauliza
‘Sikumwambia anywe sumu, na wala sikujua kuwa ana mimba…’nikasema
‘Jibu swali…’akasema na mimi nikawaza kidogo na baadae nikasema;
‘Alijiua..wanadai alikunywa sumu…’nikasema
‘Akajiua, yule ni mtoto wa nani..?’ akauliza
‘Wa wazazi wake…au sio’nikasema
‘Wazazi wake walifurahia…?’ akaniuliza.
'Aaah, hawawezi kufurahia, nalijua hilo...'nikasema
‘Mfano wewe ungelikuwa ni mzazi wa huyo binti ungelifurahia hilo tukio..je
unajua ni kiasi gani mzazi alivyoumia,..kutokana na tendo hilo kwa mtoto wake, binti yake aliyempenda sana... huenda mama au baba alipatwa na shock kubwa…kuna
athari zilitokea ndani ya miili yao, unaweza kuhisi ni ukubwa gani wa athar hizo,...kisa ni nani, ni wewe…hujui ni kiasi gani mwanadamu anavyoathirika kwa mshituko, na ukumbuke ni wazee, sio kijana, kuna tofauti ya kuhimili mshtuko kwenye mishipa ya fahamu kati ya kijana na mzee, unalijua hilo…’akasema
‘Wanisamehe sana wazee hao, sijui , sikujua jamani…’nikasema.
‘Tuache hayo....., mzee pale kasema kuna matatizo mengine
makubwa,…mdogo wake alipatwa na nini..?’ akaniuliza.
‘Mhh..lakini…hilo halihusu au...'nikasema.
‘Nakuelezea kuhusu madhara mengine yaliyotokea kutokana an
hiyo dhuluma, mdogo wake hatujui kadhurika kiasi gani, na hayo madhara mengine
hatujui yapo kiasi gani mpaka wanaikimbia nyumba yao wenyewe..., na je huko walipo wanaishije,….na
huyo mdogo mtu anapata taabu gani je itaishia hapo, je akifariki na yeye?’
akauliza na mim hapo nikaa kimia.
‘Sasa kabla haijafikia huko, ni bora kwenda kutubu, kabla
hata hao waliopo duniani hawajaondoka, maana wakiondoka, ujue una msiba mkubwa
una mzigo usiobebeka, mmoja keshaondoka hukuweza kutubu kwake, lakini wengine
bado wapo, tuwawahi kabla hawajaondoka, na kabla hajatkea mpenzi mwingine wa facebook,…’akasema docta.
‘Mhh, hapo docta …unanitia mtegoni..’nikasema
‘Unajua kijana ,…tunapodhulumu awali, tunajiona ni wajanja,
ni jambo la kawaida tu, lakini je, tunajua athari zake za baadae, ni nani na
nani wataumia kutokana na hiyo dhuluma, kama ni mtoto umemfanyia hivyo ujue ana
baba, ana mama ana ndugu…angalia hilo tatizo lako lilivyo, limekuwa chanzo cha
mikosi kwenye hiyo familia, umesikia mwenyewe huyo mzee akisema, sio mimi….’akasema
docta
‘Sasa unataka mimi nifanyeje,…mimi utetezi wangu ni sikujua…maana
sio yeye peke yake, niliyewahi kumfanyia hivyo,..nigelijua hayo yatatokea,
ningelijihami, ningeenda kumsihi asifanye hivyo,..na kiukweli awali niliwahi
kupendana na wengi, tukaachana kwa maridhiano tu…sasa kwanini kwake iwe ni
tofauti…’nikajitetea
‘Kuna ambaye kati ya hao, mlifikia kuwekeana kiapo cha
uchumba, unakumbuka huyo ulimvika hadi pete mbele ya kadamnasi,..si ndio
mnavyofanya hivyo vijana mnaiga eeh…sasa hao walikuwepo uliwaita ili iweje, si
ili wawe mashahidi, kuthibitisha,na tendo hilo lilimpa faraja huyo mdada, na
kuhakiki kuwa kweli unampenda..kweli si kweli…?’ akauliza docta.
‘Mhh…sasa docta…’nikawa nalalamika
‘Huyo binti alikupenda kweli kweli…, na ndio maana
akawakataa wachumba wengine wote, alikuwa binti wa watu, mpole, hana…uhusiano na mtu mwingine zaidi
yako..ulimkatili maisha yake…unasema kwanini yeye iwe tofauti, bado hujaliona
hilo kosa lilivyo kubwa…ndio maana nataka tufike huko kwa wazazi wake ili uone
tofauti yake…’akasema docta
‘Kwahiyo nifanyeje, niende nikajitoe mhanga,..ndivyo
unavyotaka docta…’nikasema
‘Ufanyeje, cha kufanya ndio hivii tumeanza, hatua ya kwanza
imeshapita sasa ni hatua ya pili, ni
lazima ufike kwa wazazi wa huyo marehemu, ukajieleze,… vinginevyo, ndugu yangu,
ipo siku utakwenda kuungana na huyo mpenzi wako wa facebook, huku ukiwa na
mzigo mkubwa wa madhambi, na hutapata msamaha tena, maana mlango wa toba
ulishafungwa….’akasema docta
‘Docta, kufa ni siku zako zikifika kama ndivyo nimepangiwa,
siwezi kuwa na mjadala wa hilo,…au sio, siwezi kuogopa kufa kwasababu hiyo,
ila…nisaidie tu jinsi ya kulitatua hili tatizo bila kuzua tatizo jingine, maana
nionavyo mimi kwenda kwa huyo mzee, ni kuzua tatizo jingine…’nikasema
‘Je unakubali kuwa huyo mpenzi wako wa facebook, ndio huyo
marehemu..?’ akaniuliza
‘Kiukweli hilo nalipinga, ..na..na docta mimi sijui, maana hao watu wawili hawafanani,
ngoja, …kama nitakuwa na picha ya huyo mdada, kipindi hicho, utalinganisha
mwenyewe na picha za huyu mpenzi wa facebook, utakubali mwenyewe kuwa hawafanani
kabisa…’akasema
‘Una hakika na hilo..?’ akaniuliza docta
‘Kwanini nisiwe na uhakika nalo wakati wote wawili nina
mahusiano nao…, docta mimi vitu vya kuangalia na kumbukumbu sisahau, …nikipita
njia mara moja au ukinielekeza jambo, linakaa kichwani, ni nadra sana kusahau,…au…picha
za watu, kumbukumbu za watu, nikikutana na wewe kukusahau ni nadra, sina
udhaifu huo wa ubongo..’nikasema
‘Mbona huyu umemsahau…’akasema docta
‘Sio yeye docta, kama unabisha turudi kwa yule mzee
tumuonyeshe hii picha asema ni huyo binti au la….’akasema
‘Kesho tunakwenda kuonana na familia ya huyo binti…’akasema
docta sasa kitaka kufunga mjadala.
‘Huko- mzee, hapana, huko-utakwenda-wewe-peke yako docta…nisaidie kwa hilo...’ nikasema kwa
msisitizo nikitamka neno moja moja, na mara nikahisi kichwa kikima, ni kama sindano
imedungwa kichwani, nikashikilia kichwa kwa muda, nikawa nimetulia, na docta
akaniangalia kwa makini, sikusema neno.
Kitambo kikapita, halafu hiyo hali ikatulia na docta
akaniuliza;
‘Kwahiyo umeshaanza kuogopa,….umeanza kukhalifu hulka yako
wewe mwenyewe, mwanzoni ulisema wewe huogopi, …sasa kipo wapi, kwahiyo
unasemaje, tutakwenda au mimi nirudi kazini kwangu,…?’ akauliza docta. Na kabla
sijamjibu docta, mara simu ya docta ikaita,...
Na docta akaiangalia
simu yake, akawa kama anasita kuipokea baadae akaipokea na kuuliza;
‘Halooh, ni nani mwenzangu…?’ akauliza docta na akawa
anjibiwa kwenye simu, halafu akauliza
‘Umesema nani, imekuwaje…?’ akauliza docta huku akiniangalia
mimi kwa mashaka. Halafu akasema.
‘Mungu wangu imekuwa hayo….oh, ....’akasema na akawa anasikiliza…..
NB: Kwa leo naishi hapa
WAZO LA LEO:
Usiogope changamoto pale unapotaka kuutafuta haki na ukweli, wakati mwingine
haki na ukweli haviwezi kupatikana kirahisi, na changamoto zitakazojitokeza
mbele yako ni namna njema ya kuuweka huo ukweli katika uwazi unaokubalika kwa
kila mtu, ukiyumba, ukarudi nyuma basi utaungana na hao wenye kupotisha huo
ukweli.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment