'Usiogope bwana mdogo, ..ujue wewe ulifanya makosa kwenye hiyo familia, unastahiki kuadhibiwa na wao ndio wa kuamua adhabu gani upewe..kwahiyo, ili kuweka mizania nzuri kati yako na hiyo familia, basi muhimu na sahihi ni wewe kumuoa huyo binti,..
'Kwa vipi wakati wote wanamchukia huyo mbaya wao, na hawajamfahamu kuwa ni nani, je siku hiyo wakinigundua huoni ndio itageuka kuwa chuki, hasira chuki visasi vitageukia kangu..?' nikauliza
'Ndio hivyo hakuna jinsi lakini wema hufuta madhambi au sio, muhimu tumeshaanza kutenda wema, najua mara nyingi madhambi huonekana zaidi...lakini ukumbuke kuwa,..hayo madhambi yalifanyika zamani, siku baada ya siku hasira za hao watu zilishaanza kufifia,...sasa basi, ili tuliweze hili, endelea kuitendea wema hiyo familia...'akasema docta
'Kwa vbipi docta..?' akauliza
'Kwanza ni kubainisha ukweli...kwa vipi,..tutaanzia hapa hapa, kwa namna ya kipekee kabisa, unapotaka kubaisnisha jambo nzito, anza kwa namna ya kupunguza makali, hilo niachie mimi,
‘Haya twende wanatusubiria,
Tuendelee na kisa chetu....
**************
‘Docta karibu,…karibuni madakitari wangu,… au tukipisheni maana
naona mumesimama hapo mkishauriana jambo, kwa muda sasa, halafu mnaongea kwa
kunong’ona, na msaidizi wako, mnaogopa kusema tuwapishe nini, msijali mimi
narudi kwenye wodi yangu au binti yangu unasemaje…maana tumejisahau na kujiona kama tupo nyumbani…’akasema mzee
Mashauri akimuangalia bint yake.
‘Usijali baba, mimi nipo na mama, lakini sitaki uondoke, ….eti
mama, unataka baba aondoke..?’ akamuuliza mama yake.
‘Ngoja baba yako akapumzike,…anahitajika huko wodini kwake,
hairuhusiwi , alipewa muda kidogo tu, lakini wewe umemganda baba yako kama
ruba,.. hata hivyo kajitahidi sikutegemea, hii sasa inanipa faraja kuwa
mtapona…ila sijui kama utaweza kurudi peke yako,…?’ akauliza mama.
‘Nipo na mkwe wangu hapa..’akasema.
‘Mkwe kwa nani..?’ akauliza binti yake kwa hamaki.
‘Usijali binti yangu, mbona unakuwa mkali hivyo, unafikiri mimi
baba yako naweza kukutafitia mtu mbaya,…hilo sahau, ..nitahakikisha umempata
unayempenda lakini pia awe na sifa za mume mwema,…na tulishakubaliana kuwa
tutaongea wawili ili mama yako asisikie au sio ngoja niondoke maana hapa
tatakesha..’akasema baba.
‘Aaah, baba, sasa naona unakwenda mbali, ..kwanza mimi sitaki kuolewa,
sitaki yaje kunikuta kama yaliyomkuta dada, sitaki sitaki…..na sitakii niwe mbali
na nyie wazazi wangu nyie ni kila kitu kwangu.., mnajua kuwa mimi ndiye mtoto
wenu pekee….’akasema binti.
‘Lakini ni lazima uolewe au sio,..huwezi kukhalifu amri ya mungu,
kama watu wangeliamua kuishi watakavyo, dunia hii ingekuwaje, ni lazima tufuata
taratibu njema za muumba wetu, au sio..na hata ukiolewa, bado tutakuwa karibu..’akasema
baba.
‘Baba bwana usitake kuiharibu siku yetu hii muhimu…’akasema binti.
‘Lakini kwani nimekosea nini,..,kwani wewe ulitakaje, kuwa uolewe
uzunguzni au marekeni au ughaibuni, hapana utaolewa hapa hapa,…na huenda
tukaishi pamoja wewe na mume wako,..hiyo yawezekana au sio… lakini hilo
tutaongea baadae, ngoja, nikajipumzishe kidogo, au docta unasemaje..?’ akauliza.
‘Ndio maana nimekuja, ..kwanza nataka kumuhudumia mgonjwa wangu, na
wewe unahitajika wodini kwako, docta anakusubiria, na muda sasa umepita, …kama hutojali lakini, ni muhimu uwahi kurudi
wodini kwako….’akasema docta.
‘Haya docta msaidizi njoo unipe mkono maana ooh, huu uzee jamani,
mmh, nautamani ujana urudi,…aah..’akasema akitahidi kusimama, alionyesha kuhisi
maumivu, lakini akawa anajitahid kuficha ili binti yake asihisi kitu.
‘Unajua mimi bado,… lakini haya yoye ni sababu ya huyo mtu,
nilikuwa bado na nguvu zangu,..unajua yule …eeh, aliyewaleta hapa, yeye ni
mkubwa kwangu kiumri, lakini mnamuona bado anaokana kijana kuliko mimi,..ni
haya matatizo tu..’akasema na muda huo nilikuwa nimeshafika kumsaidia kuinuka.
‘Mzee usijali, mimi nitajitahidi kuwa karibu na wewe mpaka upone
nataka uzisahau shida zako zote.., japokuwa na mimi matatizo yamenifanya nifike
hapa, lakini nina imani, hali yangu itarudi kama zamani …nipo na mwalimu wangu
atanisaidia..’nikasema.
‘Na wewe docta msaidizi una matatizo, wakati wewe unaombea watu
wanapoa..?’ akauliza mama akimuangalia kidogo halafu akaendelea na shughuli
zake.
‘Mganga hajigangi, kila mtu ana shida zake hata docta bingwa wa
magonjwa fulani anaweza kusumbuliwa na magonjwa hayohayo anayoyatibia, ..ni
mipangilio ya mungu, sisi kama wanadamu hatuna mamlaka nayo…’akasema docta.
‘Ni kweli…, lakini niulize jambo kabla baba hajaondoka, na huyo
msaidizi wake..…’akasema binti akiniangalia mimi usoni.
‘Lakini lisije kumkwaza baba yako, ..huu ni muda wake wa kupumzika,
na kinachotakiwa sasa ni yeye kufurahi, ulitaka kuuliza kitu gani..?’ akasema
mama yake.
‘Basi mama, naona umejihami…baba usiwe na shaka na mimi,
nitajitahidi kesho nifike wodini kwako nikuchukue turudi nyumbani…mimi
sitakikukaa hapa hospitalini tena..’akasema huyo binti, bado akiendelea
kuniangalia mimi machoni, na mimi nikawa najitahidi kumkwepa kumuangalia
machoni.
‘Oh, nitapona haraka, yaani kesho ukitembea na kuja wodini kwangu,
sijui nitasemaje…na mimi nitasimama tufanye mazoezi pamoja…na mama yako akiwa
nyma yetu , tuone ni nani atashindwa..au atachoka haraka..’akasema baba mtu.
‘Basi baba usijali, tumuombe mungu tu…na wewe docta msaidizi
samahani lakini ukimfikisha baba urudi nina maongezi na wewe…samahani lakini…’akasema
na mimi moyo ukawa unadunda dunda, nikijua sasa wakati umefika ukweli
kubainika.
‘Na wewe ina maana aliyosema baba yako umeshayachukulia uzito,
hutaniwi acha hizo, huo ulikuwa ni utani tu, si unamfahamu baba yako alivyo…’akasema
mama yake.
‘Mama kuna kitu nahisi …na kila nikiwaza nashindwa, huyo docta
msaidizi nahis nilishamuona mahali,…mama kwani huyo aliyekuwa akiongea na mimi
nikiwa..sijui ni ndoto au ni kweli, nilikuwa na wewe …ulikuwa na mimi hapa sio,
na huyo hapana lakini sio hapa, nilishawahi kumuona kabla, mmh, sijui..nahisi
kichwa kama hakikumbuki mambo, atakuwa ndio yeye tu mama…’akasema na muda huo
mimi na mzee Mashauri tunatembea kutoka nje.
‘Umemsikia binti yangu, anasema anahisi amewahi kukuona mahali ..nahisi
ni kwa vile, ulikuwa unamtibia, na ukiwa umezimia, au kupoteza fahamu unaweza
ukayachukua matendo ya watu wanaofika kukuguza kukuongelesha kama njozi, si
ndio hivyo…nakumbuka wakati nilipofanyiwa upasuaji..ilikwua hivyo hivyo…’akasema.
‘Ni kweli kabisa mzee, inatokea hivyo,.na kwa vile mimi nilikuwa
nafika kumuona kumuuguza, ..basi akili yake inajua kuwa alishaniona mahali…au
labda katika mihangaiko aliwahi kuniona mahali, yawezekana siwezi kukataaa…’nikasema.
‘Lakini hata hivyo, unajua hata mimi nahisi sura yako sio ngeni
kwangu, hebu niambie kuhusu wazazi wako?’ mzee akawa kama ninizaba kibao
shavuni, sikutaka kuongea na huyu mzee chochote kwanza, nilitaka kwanza
nielewane na bint yake ili niweze kupata msaada. Kama binti yake atanisamehe,
akawa karibu yangu nina uhakika baba hawezi kumuuzi binti yake..lakini sasa
nitamdanganyaje huyu mzee.
‘Wazazi wangu walihama muda mrefu kutoka maeneo ya kule kijiji
cha..eeh, (nikamtajia) ,..wakaenda kuishi maeneo mengine, na mimi sikuwa naishi
na wazazi wangu sana,nilikuwa naishi na baba zangu wengine, kwahiyo sio rahisi
watu wa huko kunifahamu, labda nilikuwa nakuja mara moja moja..’nikasema.
‘Ndio maana nakumbuka sura yako, yawezekana sio wewe, ila mnafanana
na watu ninaowafahamu, …kuna jamaa mmoja alikuwa akiishi maeneo sio mbali na
mahali nilipokuwa nimepanga, ambapo nilianzia maisha, alikuwa mweupe sana , na
tena akaoa mke mweupe,….si ndio wazazi wako..?’ mmh mzee huyu ana kumbukumbu.
‘Ndio yawezekana ndio hao…’nikaitikia kwa mashaka, na mara nesi
akaja kwa haraka, akasema mzee anahitajika haraka wodini kwake, kwahiyo inabidi
amchukua na kigari cha wagonjwa.
‘Oh, nataka kuchukua zoezi la kutembea, ..’akalalamika mzee.
‘Najua , hilo ni muhimu sana, lakini kila kitu kina muda wake,
docta wako anataka kuondoka na anataka kuhakikisha keshakufanyia matibabu
yanayostahiki…samahani mzee..’akasema sasa akielekezwa kukaa kwenye hicho
kigari.
‘Na mimi nirudi au..?’ nikauliza
‘Aaa, wewe rudi tu kaongee na binti yangu, kasema ana maongezi na
wewe ila uwe makini, usije kumuhadaa binti yangu, tutakosana, na ukija, kama
bado nipo hospitalini au nyumbani ninataka kuongea na wewe kwa kirefu,
hatujajuana vyema..’akasema.
‘Mzee, acha waoane…’akasema nesi.
‘Waoane nani na nani,..hata wakioana mimi nina shida, ila kwa
utaratibu uliokubalika, sio kihuni huni…, mimi sina shaka, na huyo eeh, ..hata
akisema leo anataka kumuoa binti yangu ninampa tu…, lakini kwa utaratibu
unaokubalika au sio,..hata hivyo lazima nijue historia yake ya nyuma..’akawa
anaongea na huyo nesi huku wanaondoka.
‘Siku hizi mzee, hayo yamepitwa na wakati,..kuwa mpaka wazazi
wamkubali wafanye uchunguzi, familia zipoje, mmh, hayo yalikuwa kwenu, siku
hizi wakikutana wawili wakapendana, ya huko nyuma ni ya wazee na uzee wao…
'Siku
hizi tunakwenda kidigitali, kwenye facebook unapata mchumba hamjui hakujui,
ukipenda sura yake na maneno yake matamu, haya, uchumba, …na hata kuoana humo
kwa humo, na inaweza ikafikia hata talaka, watu hamjakutana ..kuna mambo huko
mzee wangu we acha tu..’akasema nesi.
‘Na mimi nitakuoa wewe…’akasema mzee akitaniana na huyo nesi, na
mimi nikatabasamu, huku nikigeuka kurudi kwa huyo binti…nikikumbuka kauli yake;
‘….Na wewe docta msaidizi samahani lakini
ukimfikisha baba urudi nina maongezi na wewe..’ hiyo
ilikuwa sauti ya huyo binti, ikirudia rudia kichwani mwangu.
*************
Nilirudi wodini kwa binti, nikakuta docta, mwalimu wangu akiendelea
kumfanyia masaji huyo mgonjwa wakishirikiana na mama, na baadae walipomaliza,
akatoa dawa na kumuambia mgonjwa azinywe, haikupita muda huyo binti akalala…
‘Keshalala, sasa mama unaweza ukaenda nyumbani, ukirudi atakuwa kasha-amuka,
mnaweza kuendelea na mazoezi, cha muhimu sasa ni mazoezi tu..na kumpa faraja,
maneno yenye kumjenga, na kwa vile bado nipo nipo nitakuwa nakuja tu…’akasema
docta.
‘Nitajitahidi sana kwa hilo,…lakini muda mwingi wanakuwa na baba
yake, tatizo la baba yake ni mtu wa hasira, unakuta wanaongea ghafla
wamekosana, baba kakasirik,ainabid mimi niingilie kati…ndio hivyo, lakin
kiukweli hatuna jambo baya kwa huyo binti wetu..’akasema mama.
‘Pamoja na hayo mama, baba anahitajia kubembelezwa, kurekebishwa,
ili aondokane na tabia yake ya hasira, unajua mume kwa mke ni kama mtoto,
unatakiwa umlee, umbembeleze na hivyo hivyo mke kwa mume, ndio raha ya ndoa, au
sio, ..najua mumeo ana mafundo moyoni mwake, jaribu sana kumfanya hayo mafundo,
ya visasi hasira yaondoke..bila hayo kuondoka ..hataweza kupona …’akasema
docta.
‘Mhh, kwa mzee, hapo sijui nifanyeje, nitajitahidi..si unajua tena…
lakini siwezi kukuahidi kwa hilo, maana nimeishi naye miaka mingi, namfahamu
sana, ubishi, hasira, visasi,..ooh, hapo usimwambie kitu, lakini umri
unavyokwenda na yeye anabadilika…’akasema
‘Na kiukweli mume wangu ,kabadilika sana mume wangu sio yule
niliyekuwa namfahamu, enzi hizo, akirudi unakunyata, unajiangalia mara mbili
tatu usije kufanya kosa, lakini sasa mmh, mume wangu kawa mwingine kabisa…ana
mapenzo, ananyenyekea, yaani, unatamani hayo yangelikuwa enzi hizo..
..kilichomkorofisha ni baada ya huyo binti yake kufarikia…’akatulia.
‘Poleni sana, lakini hayo ni mapenzi ya mungu, je unafikiri nyie
kama wanadamu mungeliweza kulizuia hilo…?’ akauliza docta.
‘Najua ni mapenzi ya mungu, lakini..hata wewe fikiria, mtu
aliyefanya hivyo, halafu hata kujitokeza, angalau angelifika basi, akaomba
msamaha,..hakuwahi hata kujitokeza, hatumjui hadi hii leo, hebu fikiria, ni
lazima utafikiria vibaya,..si mlaumu mume wangu kwa hilo maana hata mimi ..aah,
hata sijui…’akasema.
‘Mama sisi tunakutarajia wewe, maana mama, au mke kwenye familia ni
nguzo muhimu sana..ndani ya familia, yeye ndiye anajenga daraja kutoka kwa baba
na watoto, kutoka kwenye familia na jamii ya nje,unaona umhimu wake ulivyo
..mke mwema ndiye anaifanya familia ijengeke vyema, mume awe na furaha, akirudi
nyumbani ajihisi yupo peponi, sio jahanamu, ..najua mume ni kichwa cha familia,
lakini mume sio mlezi, mlezi ni mama, unanielewa hapo..’akasema.
‘Nakuelewa sana…’akasema mama.
‘Kwahiyo kubadilika kwa baba, kutoka kwenye hasira, kutaka kulipiza
visasi,..na mafundo moyoni kunategemea sana juhudi zako..na ndio tiba yake
muhimu, vinginevyo hiyo stroke ikirejea tena,sijui itakuwaje,…nakuomba sana,
jitahidi. Kila iwezekenavyo mumeo ajirudi, aachane na tabia na hulka za asili,
najua hilo ni gumu, lakini jitahidi sana sana mama…’akasema docta.
‘Lakini sasa, …unajua mimi nionavyo, bila ya huyo mtu kupatikana,
sijui kama mzee ataweza kutulia,..huyo ndiye anampa shida sana mzee, mzee anasema
kuwa akifa kabla hajakutana na huyo mtu itakuwa ni deni kubwa sana mbele ya
mungu,..unajua siku ile ya mazishi, aliapa
kwenye kaburi la binti yake, kuwa ni lazima huyo aliyefanya hadi binti yake
akajiua,ampate na kulipiza kisasi…sasa hapo unafikiri nitafanya nini mimi…’akasema.
‘Unaweza, na utaweza…kumbuka jambo moja, anachotaka kufanya mume
wako ni kulipiza kisasi, je anafahamu makosa ya huyo mtu, je anajua ni kwanini
mpaka ilifikia hapo,… lakini hata hivyo hebu jiulizeni na nyie, je hamjawahi
kuwakosea watu wengine, mkasamehewa..au nyie ni watakatifu sana,
hamkosei..makosa ni mengi tuantendeana aus io…muhimu na lililo bora ni
kusameheana..’akasema docta.
‘Unajua mtu akipatwa na jambo, ndio anajua uchungu na maumivu ya
hilo jambo, na ni nadra sana mtu kukumbuka machungu hayo kwa wengine kila mtu
anaangalia nafsi yake,..sisi yametukuta hayo, tunajua uchungu na shida gani
tumepitia, tulifikia kujiona ni wafu tu hatuna maana..mpaka jamii inatukimbia,…' akasema.
'Yaani we acha tu, yaliyokuwa yakitokea ndani ya nyumba…we acha tu,…sasa kwa hali kama hiyo, huwezi kusema
je kwa wengine, walio na matatizo kama hayo,..inakuwa vigumu kibinadamu,
lakini..mimi nitajitahidi sana…kusahau, kumuomba mungu, …lakini moyoni nimeumua
sana,na huyo mtu akijitokeza akaelezea ukweli, huenda,..sijui..maana nafsi ndio
itajua hayo…’akasema mama.
‘Mama, nikisema nitakuja na huyo mtu utasemaje..’akasema docta na
mama akashtuka na kumuangalia docta, halafu akasema;
‘Utakuja naye,ina maana unamfahamu huyo mtu..?’ akauliza mama kwa mshangao.
‘Nitawasaidia kumtafuta huyo mtu kwa juhudi zangu zote.., ila
akipatiakana nataka dhamana yako, nataka wewe unihakikishie usalama wake…maana
sio kwamba hakutaka kuja, ila anaogopa..anawafahamu hasira mlizo nazo, na
amejaribu mara nyingi kuja kwenu lakini kila akija anakuta mpo kwenye hali
ambayo mtu hawezi kuongea na nyie..’akasema docta.
‘Oh, sijui, kama utamleta huyo mtu, ..kiukweli sijui nitakupa
zawadi gani, najua unatudai gharama nyingi sana,..hizo gharama zako tutazilipa
tu wala usiwe na shaka,,…hilo na wala usiogope kuweka gharama zako zote,
nimeshaongea na watu wangu, pesa yako ipo…’akasema mama.
‘Usijali mama hilo la gharama lisiwape shida, tutaona itakavyokuwa…’akasema
docta.
‘Najua na wewe unahitajia
kula, una familia, umeacha shughuli zako huko, ..na ni nani atashindwa kulipa
fadhila kama hizi, …siwezi na mtu kama huyo yupo, basi hastahiki kufanyiwa
wema,…wema wako ni mkubwa sana, ..ni lazima tulipe, japokuwa nina uhakika hata tulipe
shilingi ngapi hatuwezi kufidia huo wema wenu…’akasema huyo mama.
‘ Sasa mama, mkiwa tayari mimi nitamleta huyo mtu...lakini mkiwa tayari, ninaomba sana, hii ichukulieni kama sehemu muhimu sana, katika maisha yenu, muombeni mungu sana, safisheni mioyo yenu,...kwangu mimi niliposikia tatizo lenu kwa haraka nikaanza uchunguzi, nikagundua kuwa huyo ni sehemu muhimu sana katika matatizo yenu,..kwahiyo ikanibid nianze kufany auchunguzu wa haraka, nishaanza kuwasiliana naye, kwa mawasiliano tu....lakini sasa....'akatulia.
‘Ongea tu baba…’akasema mama akimuangalia docta halafu binti yake pale kitandani.
‘Ni hivi mama, nyie kwa hivi sasa, mnahitajia muda wa kujiweka
sawa, mlitafakari hilo jambo maana nyie ni wazazi, na huyo pia mtoto wa wazazi
wenzenu, wanakosa na wakikosa wanaadhibiwa au wanasamehewa, mimi nitachukua dhamana kwa huyo kijana au mwanaume, maana atakuwa mkubwa au sio...'akasema docta
'Sawa tutakutana na hao wazazi wake ikibidi ili tuone ..lakini mmh, hata sijui...'akasema mama
'Mimi nawaomba tena sana,…tumieni hekima zeni
katika kuhukumu makosa ya wengine waliowatendea ubaya, najua dhuluma ni mbaya na matokea yake ni kama haya, lakini tusihukumu na sisi tukaja kuhukumiwa kwa kutokuwa waadilifu,.., utaona kwa vile sio mtoto
wenu basi mje kumkomoa, itakuwa sio busara…unanielewa hapo..’akasema docta.
‘Nimekuelewa sana, ila yaonekana kama kweli unamfahamu sana huyo mtu, kwanini
unamtetea kihivyo,...hujaangalia kwa upande wetu, je ni haki alichokifanya,...uangalie pande zote, au sio...nikuulize tena, kweli unamfahamu huyo mtu..?’ akauliza mama, akimuangalia docta.
‘Mama usijali hiyo kazi nitaifanya maana ni sehemu ya matibabu ya
wagonjwa, ninajua bila kupatikana kwa huyo mtu mzee hawezi kutuliza akili yake,
nafsi yake imeshasadikisha kuwa hiyo ni dhima kwake, sasa ili matatibabu yangu
yakamilike, basi,..hilo kwangu ni muhimu sana…’akasema.
‘Na huyu msaidizi wako naye anamfahamu huyo mtu.?’ akauliza
akiniangalia usoni.
‘Hapana, yeye ndio ikibidi, nitampa kazi ya kumfuata huyo mtu akaja naye, unajua mimi nafanyia kazi mikoani, sasa sijui lini mtakuwa tayari , kama bado ..maana yote inategemea hawa wagonjwa, ..ni sehemu ya matibabu lakini je wapo tayari kuhimili, ..sasa mwenznagu hapa ndiye nitamtumia zaidi, atapatikana tu usijali mama.’akasema
docta.
Mama sasa akawa ananiangalia kwa makini mimi, baadae akasema;
‘Lakini hii sura sio ngeni kwangu..’akasema mama akiendelea kuniangalia kwa
makini
‘Wengi wanasema hivyo, sijui kwanini, hata baba alisema hivyo hivyo, sura yangu yaonekana ni...tofauti au…’nikasema nikijihami.
‘Usijali, kinachonifurahisha na kunipendeza kwako, unaonekana wewe ni mtu
mwenye tabia nzuri,..na ukichanganya na kipaji chako, hakuna mzazi ambaye
hatafurahi kuwa na mtoto kama wewe…’akasema mama.
‘Na wengi wangelipenda awe mkwe wao..’akaongezea docta huku
akicheka.
‘Hahaha, docta hayo ya ukwe, ni wao wenyewe wakikubaliana
wakapendana, sisi wazazi ni kutoa ushauri tu kuwa anafaa au hafai..ndio mambo
ya siku hizi, kama mzazi inabidi ukubali wakati au sio…’akasema.
‘Ni kweli, ndio mtihani wa wakati huo mama kila mabadiliko huja na changamoto zake…’akasema docta.
‘Lakini sasa docta mbona hamjaniambia vizuri, huyu msaidizi wako ni nani, ..nahisi
namfahamu, nahisi nimeshawahi kumuona mahali, nahisi nahisi, mmh, ni nani wewe,
tumeonana wapi…?’akasema mama akijaribu kukumbuka.
NB: Mama huyoooh
WAZO LA
LEO:Tunapotaka
kuhuku jambo, kwa wengine tujiulize kwanza kuhusu sisi wenyewe, je hatujakosea hivyo,
au kama hivyo…wengi wetu tunakosea sana, lakini mara nyingi tunaona makosa ya wengine
zaidi ya makosa yetu..kwa kufanya hivyo, tunajenga uadui badala ya kusaidia
kuondoa matatizo. Tumuombe mungu atujaze hekima ya kuhukumu sawa, kwa haki na
uadilifu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment