Soldier aliposikia mama yake akisema;
‘…sijawahi kukufumania
wewe na mjane, au unataka niongee kila kitu mbele ya watoto…?
Kwa mshangao wenye kukereka, Soldier, akamkazia baba yake
macho, na kumuuliza swali la haraka;
‘Ina maana baba kweli uliwahi kufaminiwa…?’ akauliza Soldier…
Baba yake akiwa na tabasamu mdomo la dharau…, akiwa hajali,
akamuashiria mtoto wake kwa mkono kuwa atulie,..na Soldier akiwa katahayari
akamgeukia mama yake, akitamani kusikia zaidi kuhusu hiyo kauli,..lakini mama
yake alibakia kimia, na baadae baba akasema;
‘Umemaliza mpenzi…?’ mumewe akamuuliza.
Tuendelee na kisa chetu….
**************
‘Unataka nisema kila kitu …naogopa kuwa nikiongea zaidi
nitaharibu mambo mengii, hata watoto hawatanielewa,…sasa ni wewe, …useme ukweli,
kiri mbele ya watoto wako kuwa umefanya madhambi, kiri na mtambulishe huyo
mwanao wa nje ya ndoa, na baada ya hapo mimi nitajua ni nini cha kufanya maana
mimi nimevumilia na sasa naona ni bora nichukue maamuzi, najua nitaumia,
nitaumiza wengi, lakini nitafanyaje….’akasema
‘Umemaliza…?’ baba akauliza sasa akiwa kakunja uso.
‘Nimemaliza nini...kama unataka nisema zaidi ..haya,…’akasema
mkewe.
‘Sema, si umetaka kuongea, ongea kila kitu kilichopo moyoni
mwako, sema kila mtu asikie,…uwanja ni wako sasa…’akasema akijiegemeza kwenye
kitu akiweka mikono nyuma kama anaigemea.
‘Inatosha…’akasema mkewe, na baba mtu akasubiria kwa muda,
halafu akasema;
‘Kwanza kabisa nakupa hongera, maana ni kwa mara ya kwanza
kukusikia ukitoa siri za mumeo, ..sio kwamba nakubali kuwa hayo uliyosema ni ya
ukweli,..kuwa labda ilikuwa siri yetu mimi na wewe.. hapana, ila ki kawaida mke
ni msiri wa mumewe kama alivyo mume kuwa msiri kwa mkewe…najua una mengi moyoni
na ndio maana leo nataka uyaongee yote, ili moyo wake uwe huru…’akageuka kwa
mzee mualikwa na mzee alikuwa akitikisa kichwa kama kukubali.
‘Mke wangu, najua hayo yote yametokea wapi,…na mimi ni mtu
mwenye subira sana, ule ukali wangu wa ujana, sasa haupo tena…, ndio maana
nimekuwa kimia kwa muda wote huo, watu wakisema hiki na kile…wakaanza kukuambia
kwa uwazi sasa na wewe ukiyapokea tu kama pakacha la taka, bila hata kufikiria,
unazidi kuumia ndani kwa ndani..…lakini kila jambo lina mwisho wake….’akatulia
‘Lao nataka hiki kikao kugeuka mahakama tuulizane maswali…ukweli
uwe bayana, tuyamalize haya mambo, na kile mwenye maamuzi yake, ayachukue, mimi
siwezi kumzuia mtu afanye atakavyo….sasa mke wangu, nataka nikuulize maswali
unijibu mbele ya kadamnasi, nilitaka hili alifanye mzee wangu hapo, lakini
hapana, yeye abakie tu kama shahidi….’akasema na kumgeukia mke wake.
‘Wewe unasema uliwahi kunifumania, mimi na mke wa marehemu,…una
uhakika kweli ulitukuta tukizini..sema ukweli wako, ulipofika uliniona
nikitenda hilo tenda,..nataka usema kinaga ubaga ulivyonikuta…usifiche kitu….?’akasema
akiuliza na mkewe akawa kama anacheka, na kutikisa kichwa akasema;.
‘Najua utajitetea, kuwa sikukuta mkiwa mnatenda hilo tendo…,
lakini dalili zote za dhambi hiyo zilikuwepo,…kuzini kuna dalili zake..kukaribia
zinaa ni dalili mojawapo…kiukweli mimi niliwakuta mkiwa kitandani, haya
nikuulize kitanda cha watu na mke ambaye sio mkeo ..mlikuwa mkifanya nini..na
ile hali uliyoonekana nayo,..jasho linakutoka,…mimi sio mtoto mdogo…’akasema
mama.
‘Sawa kabisa mke wangu, ni kweli ulinikuta nikiwa kitandani,
kitanda cha watu..ni kweli kabisa mtu kama mimi niingie kwenye kitanda cha
watu, na mke …wa watu,…sio sahihi, ni lazima kulikuwa na jambo, ama huko kuwa
na dhamira ya kuzini…au kulikuwa na jambo jingine, sasa.. wewe hujataka
nikuelezee ukweli, kuhusu mimi kuwepo pale kitandani, hutaki kunipa nafasi
hiyo,….’akatulia.
‘Hivi ..kweli jamani… upo kitandani na mwanamke, mnataka
kufanya nini, au mlifanya nini…na mwanamke yupo…nusu uchi, ndio alikuwa kavaa khanga
moja…chui na mbuzi wake zizi moja…,kwa hali kama ile..huniambii kitu…yaonyesha
kabisa mlikuwa…jasho lilikuwa la nini….muda kama ule..hebu niambie..’akasema
mkewe.
‘Nikuulize tena,..kunifumania huko, ni kwa kuhisi kuwa kwa
vile uliniona kwenye kitanda cha watu, na mwanamke asie mke wangu,…basi wewe
ukahitimisha kuwa nimetenda hilo kosa, sio kwamba ulinikuta natenda hilo kosa,
nataka hapa uwe muwazi…uliniona nikizini au ni hisia zako tu…’akasema.
‘Kwahiyo wewe unataka nitamke maneno yasiyofaa mbele ya
watoto, hayo niliyooangea kwangu yanatosha kuelewa jinsi gani ulivyokuwa…muhimu
uwe mkweli, …maana hiyo sio mara ya kwanza, kama unataka niendelee kuongea,
kuna siku..nilikutafuta ukanidanganya kuwa upo kikaoni, nikapitia kwa ..huyo …mke
wa marehemu nikakuta..hapo ndio kikaoni…na hali niliyowakuta nayo.., mpo
mumekaa kiti kimoja mumeshikana…kimahaba..si ndio unataka niongee hivyo…je huo
mkumbatio…aah, usitake kunichefuke...’akasema mkewe akikunja uso kwa huzuni.
‘Nataka uongee kila kitu, dalili, ushahidi,..kila kitu, …ongea
na jingine,..na kingine, nataka ushahidi sio kukisia,…’akasema baba na Soldier akaona
aingilie kati na kusema;.
‘Baba lakini mimi sioni kuwa kuna haja ya mama kuongea
yote,..hayo aliyoelezea yanatosha tu,sisi tumeshaelewa,…’akasema Soldier.
‘Umeelewa nini hapo wewe mtoto…, kuwa baba yako ni mnzizi
kuwa kweli mimi natembea na huyo mama mjane,…usiparamie haya mambo kwa pupa,
acha mama yako aongee kwanza, au unataka kusema nini..?’ akamuuliza mwanae.
‘Siwezi kusema hivyo baba, lakini kwa jinsi mama alivyoongea
yaonyesha kuwa kuna mahusiano kati yako na mama mjane…ndivyo anavyoona yeye,
sasa mimi nionavyo, kama kweli yapo, au hayapo, basi tuyamalize,..sioni haja ya
kuingia kwa undani zaidi…’akasema Soldier.
‘Huna akili kabisa wewe....usikubali kuhitimisha maneno ya
akina mama hivi hivi,..hawa wanapenda kuhitimisha mambo kwa haraka sana, …nikuulize
wewe, huko kazini, mkiwa na sherehe, haitokeo siku ukakaa na wanawake, na hata
kukumbatiana, kwa…kufurahishana tu, sio kwa mapenzi..haijatokea hivyo..utani
utani tu, lakini akilini unajua wewe ni mume wa mtu unajua mipaka yako…haipo
hiyo?’ baba akauliza
‘Hapana baba, sio kwa kiasi cha kuvunja miiko ya ndoa, mimi
nijuavyo,….ukishaoa, kuna mambo unatakiwa uwe makini nayo…mojawapo ni hilo..kuwa
mbali na yale yatakayohatarisha miiko ya ndoa…sasa mama anasema alikuona ukiwa kwenye
kitanda na mke asiyekuwa wako, huo ni ushahidi mkubwa sana baba…., lakini mimi
naona tusiende huko zaidi…’akasema mwanae.
‘Una uhakika na hilo unalolisema mwanangu, maana hiki kibao
kitakugeukia wewe, na utatafuta sehemu ya kukimbilia usiione,..mimi ni mtu
mnzima, nina akili zangu, na kwa utu uzima huu ninaweza kufanya jambo kwa
minajili fulani..kihekima tu,…naweza kufanya mambo kwa ajili ya kumliwaza mtu…na
kumfanya aondokane na huzuni,..na ndivyo nilivyofanya kwa mke wa marehemu…’akasema
‘Labda nikiri kuwa ucheshi wangu wa kupindukia,..kuliwaza
huko, kwa kupitiliza, labda ndio mnaona ni kosa, lakini hayo nimekuwaq nikiyafanya
hata hapa nyumbani…, wanakuja shemeji zangu tunataniana na tunafika sehemu tunakumbatiana
kimzaha, mke wangu,… my love…, ni jambo tu la kufurahishana lakini mimi nina
akili zangu timamu,….siwezi kuvuka mipaka ya ndoa..’akasema
‘Kwahiyo kwa kauli yako hiyo baba, unamuhakikishia mama kuwa
hukuwahi kwenda zaidi ya hayo ya kukumbatiana,…ni ucheshi wako tu...tunakuonaga
hata hapa nyumbani,..ndio, lakini ..baba hilo la kuingia hadi kukaa kitanda cha
mke wa mtu, asiye kuwa mke wako, hata kama ingelikuwa ni wewe baba, ungelimuona
mama kakaa na mwanaume mwingine kitandani, sidhani kama ungelifurahia, ni
lazima ungelihisi vibaya najua huenda hukuwahi kufanya tendo, labda ulikuwa na
sababu ya msingi, sasa mimi nionavyo, tuyaache hayo….’akasema na baba yake
akawa kakunja uso kwa hasira.
‘Unasema tuyaache wakati hata nyie mumeshanihisi vibaya,
haya hayaachwi, mpaka ukweli ubainike, nataka…ushahidi, nataka ukweli…unasikia,
mama yako abainishe..kwanini nisingiziwe,…kwanini, sasa mwambie mama yako atoe
ushahidi,….vinginevyo…’mzee sasa akawa anakuja juu.
‘Samahani baba nakuuliza haya nikitaka usahihi…, ili mama
asiendelee kuteseka, ajue kuwa ulikosea na hutarudia tena, …kwanini baba usikiri
tu kuwa hapo ulivuka mpaka na umekosea..,..au hata kama hukufanya, ukisema
nimekosa samahani mke wangu sitarudia, tena,..yaishe, ….si ndio hivyo mama…?’
akauliza.
‘Hata kama hakufanya..hahaha…mungu hamfichi mnafiki…alifanya
kwa siri lakini ukweli umemuanika…ukweli upo ….sasa sijui anataka kusema nini…’akasema
mkewe
‘Hahaha, wewe mtoto wewe…ngoja ya kwako yanakuja….na
nikuambie kitu ili mtu moyo wake uwe na amani , inahitajika ayaonge yote
yanayomkera….asifiche, mimi nipo tayari, kama kweli nimekosea nitasema ..lakini
hilo la kusingiziwa,..sipo tayari…na umemsikia, kasema anao ukweli bayana,
nataka usikiwe mbele ya hadhara hii….’akasema.
‘Lakini mama kasema kakuona ukiwa kitandani..hiyo hali
inamtesa, huo ni ushaidi au sio baba, au sio mama, narudia baba kukuuliza jemfano
ungemkuta mama yupo na mwanaume kama alivyokukuta wewe, ungelifikiriaje,...hebu
chukulia hapo baba..inauma kwa kweli baba….’akasema Soldier
‘Nakuelewa sana..ila nikuambia ukweli mwanangu..maana mimi
nimekuwa jeshini, hunidanganyi kitu, nimekuwa kiongozi, na unafahamu kabisa
jeshini kulivyo, …wakati mwingine inabidi utende jambo kwa nia ya kumaliza
tatizo....haya ya kwangu ninayoshukiwa nayo hapa ni dhana tu, ni madogo…hunidanganyi kitu mwanangu, kuwa
huko ulipokuwa ulikuwa humgusi mwanamke, huchezi mziki, hamkumbatiani…hamfikii
hata hatua ya labda ukaenda ukakaa kitandani kwa wanawake, kwasababu fulani,
mwanamke anaumwa, ana tatizo, je huwezi kwenda kukaa kitandani kwake….wewe
usitake nikuumbue...’akasema baba
‘Baba..huko ni kambini, na mnapokuwa huko mnakuwa wakati
mwingine kama wanafunzi, mnaweza mkafanya hivyo,…lakini hayo ni ya huko,
yanaishia huko huko…. sasa hivi…tunazungumzia mambo ya uraiani…mazingira ya
kule ni tofauti na ya hapa baba, tukitaka tufanye yale ya kule huku,..tutakosana
na familia zetu, ndoa zitalega lega, …na kama ulivyosema awali, nia hapa ni
kuliweka hili bayana, halafu tuombeane msamaha yaishe,…mimi ndivyo nionavyo, …’akasema
‘Niombe msamaha kwa kosa gani…sasa nasema hivi mimi ninataka
mama yako abainishe hayo makosa yangu awe muwazi..anaogopa nini sasa?’ akauliza
akimuangalia mzee aliyekuwepo hapo, huyo mzee alikuwa kimia tu.
‘Baba …mimi naona tusiende mbali zaidi, mkachafuana zaidi na
zaidi, tusiende huko,…mama keshaeleza ni kwanini anakushuku ni kwanini hali
imefikia hapo,..najua kwa umri mliofikia hayo yaliyowahi kutokea huko hayawezi
kutokea tena, au sio, tuombeane msamaha yaishe….’akasema Soldier.
‘Mwanangu.., utakuja kuona kuwa sijafanya kitu..nakuelezea
unielewe…mimi sijafanya kitu cha kuharibu ndoa yangu, mimi ninafahamu maana ya
ndoa kuliko wewe,..mimi ni kiongozi najua jinsi gani ya kusuluhisha haya mambo,
ninakutana na kesi hizi kila siku….ninajua, …nianze vipi na nitamaliza vipi,
hii ni kesi yangu,niachie …’ akasema
‘Baba nakuelewa, lakini tupo hapa ili tusaidiane kama
familia, mimi ni mtoto wenu mkubwa, haya niliyoyakuta hapa yamenipa wakati
mgumu sana,..kwanza kuhusu nyie wazazi wangu, ..imefikia hatua mama sasa
anaathirika, shinikizo la damu…ni hatari, kisa ni hayo mambo, tufike mahali
sasa tymalize, mama awe huru, asiwe na mashaka tena, yeye ni binadamu atasamehe
yaishe au sio mama…’akasema
‘Wewe tulia, haya yataisha yote hii leo….mimi ni askari
nimeanzia chini hadi juu…sio kwa kupewa pewa cheo tu, ujue, mimi nilisota ile
mbaya, najua watu,..naufahamu vyema uongozi wa kuongoza watu,..nafahamu tabia
za watu, …. ..ndio maana nataka mama yako anailewe, twende hatua kwa hatua,
athibitishe kwa ushahidi,….’akatulia
‘Aaah, mimi sitaki kuongea tena….basi inatosha,…basi..’akasema
mkewe akitaka kuondoka.
‘Mke wangu,..unataka kwenda wapi, hapa ndio sehemu ya
kuyamaliza haya,… mimi ninachotaka ni wewe utoe ushahidi ulivyonifumania, na
kufumaniwa maana yake umenikuta natenda….tendo…sio kudhania dhania tu…haya hilo
la kutenda tendo, halipo,…aseme ukweli wake..hilo halipo na halikufanyka…ni
dhana tu…au ..sema mwenyewe, je aliwahi kuniona nikizini....’akasema.
‘Nimeshakuambia…sitaki kuongea mambo mengine mabaya mbele ya
watoto, nilichoelezea hapa kila mtu anaweza kuona ulivyo, kamwe sikupenda
kuyaongea haya unanifahamu nilivyo,…na kuzini unakofikiria wewe…ni kupi, sio
lazima mkutwe mpo kwenye tendo,..dhamira,…kukaribia, kushikana yote hayo ni
kuzini tu….’akatulia na mumewe akawa anamuangalia, na mkewe alipoona bado
anasikilizwa akaendelea kusema;
‘Unaonaeeh….kwahiyo wacheza mziki wote, wanacheza jukwaani
wanashikana, au waigizaji wote, wanaigiza …wanazini…..kifupi huna hoja hapo,
hujawahi na hutwahi kuniona ni kizini….nataka hili libanikie na liwe wazi
kwenu, hizo shutuma za mama yenu sio kweli….’akasema
‘Haingeliwezekana, mimi nije nikukute bayana, …maana
sikujua,..na sikuwa na lengo la kukufuatilia, hiyo ilitokea mimi nimefika tu,
kwa jambo jingine nikwafuma,…sasa ukijitetea, ukapindisha maneno, ni upendavyo
wewe, ila kwa kifupi .wewe ulivuka mipaka ya ndoa, lakini hata hivyo mimi
nilikuvumilia,…kwa vile unajifanya mcheshi, ushike-shike wanawake za watu ,
tena wakati mwingine mbele yangu,mimi nikuangalie tu, je mimi nikifanya hivyo
utafurahi…mbona mimi unanikataza hata kukaa karibu na mwanume….hivi nyie
mnafikiria sisi wanawake tuna miyo ya chuma, hatuumii….’akasema mama kwa
huzuni.
‘Pole sana mke wangu..sikujua kuwa nakumiza, lakini ndivyo
nilivyo..ila nasema tena, hilo la kuzini , hilo la kufamaniwa halipo, sijawahi
kufanya hivyo..na mama yenu hana uhakika na hilo kama ana ushahidi mwingine
aseme nataka kwanza hilo liwe bayana, ana ushahid gani kuwa mimi nimezini na
huyo mjane, autoe, na akiutoa, hapo nitaweza kukiri kosa langu…’akasema
‘Unataka ushaidi wa vipi, kwanza hilo ulilofanya hujakiri
kuwa ni kosa, wewe unaona ni jambo la kawaida tu…, …au wewe unataka tuonyeshe
matokea ya dhambi zako,....na huyo mtoto wa nje sio ushahidi, kila mtu
anafahamu kuwa huyo mtoto ni wako ..au utamkana kuwa sio mtoto wako…’akasema
mkewe
‘Mtoto yupi huyo ?,….huyo dereva..? Lakini hilo si
nimeshalieliezea,..huyo sio mtoto wangu, anafanana na mimi kwa vile baba yake
alikuwa akifanana na mimi…hilo lipo wazi,…. Sawa…sasa ni hivi, maana tulikuwa
tunakwenda huko,…, kwa vile umelitaja hilo, sasa mimi nataka kukuthibitishia
kuwa huyo sio mtoto wangu, nitamuita hapa huyo kijana,..na kama mama yake
angelikuja pia ingelikuwa ni bora, nilitaka wote wawili waje watamke hapa
bayana je huyo mtoto ni wangu...’ akasema
‘Hata wakija si umeshaongea nao, umeshawapanga wasema hivi…maana
wote mpo kitu kimoja, huyo dereva awali alikuwa anakubali….,sasa ulivyomuweka
sawa anakataa..na huyo mwanamke wako akija hapa hawezi kusema ukweli, kwasababu
ni mpenzi wako…atakusaliti vipi…na nijuavyo mimi, mwongo ataumbuka tu,…anajua
hilo ndio maana kaogopa kuja..’akasema mkewe.
‘Kama ni mtoto wangu kwanini anikane, …atajiharibia yeye
mwenyewe, ngoja aje, tumuulize, asema ukweli wake,..je mimi ni baba yake,
je mama yake anasemaje kuhusu hilo,..au
unaogopa uongo wako utakuumbua wewe mwenyewe,..tatizo lako ni upole na wivu,
hakuna jingine…muiteni hapa huypoo dereva yupo nje, aingie…’akasema baba
‘Haina haja….umeshamkataza asisema, …kasema yeye mwenyewe
kuwa wewe umemkataza ….sasa hata akija atasema nini , na mama yake niliwahi
kumuuliza, majibu yake ya dharau tu..ananidharau kwa vile mnajuana…..’akasema
mkewe, na Soldier akaingilia kati na kusema;
‘Mama tafadhali, mimi naona huyo dereva aje hapa, tumuhoji,
tusikie na yeye kauli yake, anavyosikia, na je kweli yeye anakubali kuwa huyu
ni baba yake au la, na mama yake anasemaje, na tutamwambia hapa ndio suluhu…,
akikataa kuwa huyu sio baba yake, ndio imetoka hivyo…, isije ikatokea …hatuombei
mabaya, aje tena akisema mimi ni mtoto wa familia hii…hilo tuliweke hapa bayana
, mbele ya baba..na hata hivyo hata mimi nina maswali ya kumuuliza huyo mtu…’akasema
Soldier,
‘Sawa …muiteni dereva aje, …’akasema baba mtu kwa sauti ya
mashaka mashaka.
Dereva akaingia…na ajabu akawa kafuatana na mtu mwingine,…..!
NB: Haya tuendelee kidogo, au…
WAZO LA LEO: Unapofanya
jambo, ambalo huenda linaweza kumuathiri mwingine, kabla ya kulifanya hebu
kwanza jiulize je nikifanyiwa mimi nitalipokeaje..je nio tayari kuliona , au
kulipokea akinifanyia mwingine, kama utaona haupo tayari, basi liache…ukumbuke akiumiza
mwenzako moyoni na wewe utakuja kuumizwa hivyo hivyo,..
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment