‘Jamani naona mimi nianze
kuongea…..’aliyesema sasa alikuwa mke wa Soldier. Soldier hakutarajia
kuwa mkewe ataanza kuongea, yeye alitaka aupate ukweli kupitia kwa watu
wengine…
‘Maana kama nilimuuliza mara kadhaa akanificha, sasa kwanini
nisumbuke naye…’akilini alikuwa akiwaza hivyo.
‘Nitaupata huo ukweli hata kama hutaniambia wewe…’aliwahi
kumwambia mkewe hivyo, sasa mkewe huyu hapa anataka kuusema ukweli mbele ya
watu, je ukweli huo hautamuathiri baba yake,…ngoja ausikie, hapa akajikuta
akimkazia macho mkewe, lakini cha ajabu mkewe alikuwa anatizama upande upande
kama anamkwepe kumuangalia mumewe usoni.
Tuendelee na kisa chetu…
‘Wazazi wangu, na ndugu na jamaa zangu (hakumtaja
mumewe)….naongea hili kutoka undani wa moyo wangu…’akaanza kuongea. Na
alipoanza kuongea hivyo, baba mkwe alijishusha kitandani na kujilaza, maana
muda wote huo alikuwa amekaa, baada ya kuweza kujiinua kwa miujiza na kitendo
kile kiliwafanya waliokuwepo humo ndani kugeuka kumuangalia mzee..kama kazidiwa
nini.., na Soldier akamuuliza baba kwa ishara kuwa yupo ok, baba yake
akaonyesha dole gumba kuwa yupo ok..
‘Najinyosha kidogo tu…’akasema na huku mkewe akiendelea
kuongea;
‘Mimi nilimpenda sana mume wangu, na nilijitahidi sana kuwa
mke mwema, na niliahidi nitafanya hivyo kwa kadri mola alivyotujalia uhai wetu,
ilimradi tupo kwenye ndoa, na mungu alisaidia kwa imani hiyo, kwani kiukweli
nimepitia majaribu mengi …’akatulia.
‘Mume wangu alipoondoka, walinijia watu wengi tu,
wakiniambia hili na lile, na wengine wakaja kunisingizia kuwa mume wangu huko
alipo ana mke mwingine, hapo nilikuwa sijapata taarifa nyingine iliyonivunja
nguvu kabisa, japokuwa nilijitahidi nisiiamini…’akatulia
‘Mimi….?’ Akauliza Soldier akishika kifua, Soldier
akatabasamu kwa dharau, na shemeji mtu ndio akacheka kabisa.
‘Lakini mimi sikuwahi kukubaliana na hayo maneno, na hayo
maneno yalivuka yakaenda hadi kwenye familia yangu, na familia yangu iliniita
na kuniuliza kama nina habari kama hiyo, kiukweli niliwakatalia, lakini bado
walinisisitizia kuwa niwe makini, kwani hao wanaoongea hivyo wanatokea nchi ya
jirani.
‘Haya yalienda , mpaka ikaja hiyo ya baba, baba mkwe, akawa
analewa, nilijua ni sababu labda za ndoa yake, lakini mimi nilijitahidi sana
kumuheshimu baba, kama ninavyomuheshimu baba yangu mzazi, hadi pale alipoanza
kikiuka mpaka,…alikuwa analewa kupita kiasi mpaka anakuja kutaka kulala
chumbani kwangu.
‘Oh…’ulikuwa mguno wa Soldier
‘Mwanzoni nilijua ni pombe tu, lakini ..aah, sikuweza kuvumilia,
na siku moja ndio nikasema basi ngoja niondoke tu….alikuja na kuanza kuongea
akiwa kalewa, anaongea kuwa amesikia mtoto wake amekufa…sasa kama mtoto
amekufa, na mke kamkimbia, kwanini mimi nisiwe mke wake,…’akatulia
‘Sikupenda kuyaongea haya mambo, maana yalikuwa ni maneno ya
kilevi, nayaongea kwasababu ya haya yanayojitokeza, na inavyoonekana
nisipoongea, naweza kuonekana mimi ni mkorofi,sina adabu…matendo hayo ya
kilevi, samahani natumia kauli hiyo baba, yalijirudia tena na tena, mpka kwangu
ikawa ni shida,…uvumilivu ukanishinda, ndio nikaamua kuondoka…’akatulia.
‘Umemaliza…?’ akaulizwa na mama mkwe
‘Kwa upande huo nimemaliza, labda huko nilipoelekea
kulitokea nini, maana naona kuna mengi nimehusishwa nayo hata sijui ilikujaje…’akasema
‘Je katika huko kulewa kwa baba mkwe wako, ..je aliwahi
kukushurutisha kufanya lolote, na je ilitokea akakushika kwa nguvu na tendo
likafanyika..?’ akaulizwa
‘Mama haikuwahi kutokea hivyo maana nilishafahamu kuwa sio
akili yake, na nisipokuwa makini yanaweza kutokea mabaya, kwahiyo nilijitahidi
kuwa mbali naye kadri ilivyowezekana, kero zilipozidi,nikaona njia nzuri ni kuondoka,
na nahisi kama ningeendelea kubakia humo, huenda ningezidiwa nguvu,,…kuna siku
niliamua nimpige hata chupa,…nasema haya kutoka ndani ya moyo wangu,..’akasema
‘Hebu angalieni, unamvumilia mtu kama baba yako na bado
anakukera, unafanya yale hata yasiyofa, maana ukilewa unaweza kupitiwa na haja,
mimi ilibidi niifanye hiyo kazi,..na bado anakukasirikia, kuwa simjali
nk…unajua ilifikia muda ananifokea kama mkewe, ila heshima ya ukwe ikawa haipo…’akasema
‘Nilivumilia nikimuona yeye ni baba yangu , nilivumilia
kwasababu ya mama, kwani mama aliniambia anaondoka, lakini nimsaidie mume wake,
kwani anajua hayo yanampitia ni shetani tu,,lkn ili mume wake aweze kujitambua
ni lazima yeye achukue hatua, mimi..nilitii sana kauli ya mama, zaidi ya kauli
hiyo, kuwa huyo ni sawa na baba yangu…maana kama yeye angejitambua kuwa ni baba
yangu asingeliweza kufanya hivyo…’akatulia.
‘Sasa ndio napata taarifa kutoka huko, alipokuwa mumewangu,…
kwanza nilisikia amekufa, baadae nasikia ana mke mwingine na baadae eti wameshazaa
mtoto…, huku baba ndio huyo haeleweki, huku familia yangu inanisakama na
ilishafikia sehemu imesema kama sitaki kurudi kwetu, basi litakalonipata ni juu
yangu,…kwa hali kama hiyo mlitaka mimi nifanye nini..
‘Ni kweli nafahamu nilivunja miiko ya ndoa, nikaondoka
kwetu, sehemu nilipopewa kama kwangu, ..nilikiuka miiko ya ndoa nikakimbia
sehemu ya mume wangu, nakiri hilo ni kosa, lakini nililifanya hili kwa
makusudi..ili nijiokoe..na sikwenda kwetu, nilikwenda kuishi kwa shangazi
yangu.
‘Huko kwa shangazi yangu, binamu yangu alikuwa amejifungua
mtoto mchanga, na akawa anasoma,..kwahiyo nikawa mimi ndio mlezi wake,..ndio
maana nikawa sipati muda, kulea mtoto sio mchezo, na..sijui labda, hao
walioniona na mtoto ndio walichukulia hivyo, labda…mimi sijui..kwani binamu
yangu alikuja akachukua mtoto wake wakaenda kuishi Dar na mumewe…’akasema
‘Kumbee….’akasema dereva, na kukawa na ukimia kidogo na aliyeongea
sasa alikuwa baba …
‘Pole sana mkwe wangu, nikuombe radhi, nimekosa na sikuwa
nimejijua kipindi hicho, nasikitikika sana, kwa hayo niliyokutenda, nataka
niitoe hii kauli haraka, maana ya mungu mengi,.. ndio maana hata nilipoumwa,
nilitamana nife tu….ila nilipomuona mtu wangu, ambaye ninajua atakuja kuusema
ukweli, na kunisafisha,… nilijua hilo litakuja kufanyika, lakini kwa vipi, niliongea na mke wangu kuwa ili
hilo liweze kusubiriwa hadi wakati muafaka mke wangu amshawishi mkwe, ili
aubebe mzigo, anyamaze na kutokusema lolote, nashukuru kuwa aliweza kulifanya
hilo…’ilikuwa kauili ya baba mkwe pale kitandani.
‘Hebu nyamaza huko, huoni umenitia aibu…’akasema mkewe.
‘Lazima nitubu mke wangu, usione hivyo ukafikiri nilipenda,
mke wangu nilikupenda sana, kuondoka kwako ilikuwa kama nimekatwa sehemu ya
mwili wangu,..kila nikiwaza najikuta naumia, na nikaona pombe ndio dawa , kumbe
ndio najiumiza, nasema hayo kiukweli, mnisamehe sana…samahani kwa kukukatiza
ila liweke moyoni kuwa nahitaji msamaha wenu wewe na mke wangu..’akasema akimuangalia
mkwewe na mke wake.
‘Baba mimi nilishakusamehe, nilijua sio wewe, ni udhaifu wa
kibinadamu na pombe..sipendi kabisa pombe, lakini niliamua kukuvumilia,..na
isingelikuwa hivyo, ningelishaondoka..isingelikuwa ni mama, kuonyesha mapenzi
yake kwako, kuwa pamoja na hayo alikuwa tayari kukusamehe, ila alitaka
ukweli,…alitaka kuhakikisha familia haitaumia baadae, ila ilimuuma sana
ulipoamua kutembea na rafiki yake, na nimejua ukweli huo kupitia kwangu…’akatulia.
‘Sikuweza kuja kuusema ukweli mwingine kwa mama, japokuwa
aliniomba sana nisema, lakini nilijua nikisema je ikiwa sio kweli…lakini watu
walishasema wapo tayari kunipeleka kunihakikishia kuwa mume wangu ana mke
mwingine na wameshazaa naye…’akatulia
‘Sikutaka kulisema hilo kwa mama japokuwa mama aliniomba
sana,…aliniona nilivyokuwa sina raha, ..lakini nilisubiria wakati muafaka, ili
niweze kuupata ukweli, na ushahidi kamili…’akatulia.
‘Na ghafla siku ya siku naletewa mtoto, mtoto anafanana uso
kwa uso na mume wangu,kama nilivyoambiwa kuwa mtoto huyo anafanana na mume
wangu…hebu niambieni hapo unaweza kusema nini….ni kuwa kumbe kweli mume wangu
alikuwa ana mke mwingine…’ akasema akimuangalia mama . Mama mkwe akawa kainama
chini tu.
‘Sasa nichotaka ni ukweli kutoka kwa mume wangu,,…autamke
ukweli mbele yenu kuwa hayo yanayosemwa ni kweli au si kweli..na huyo mtoto
aliyeletwa kwangu ni wake, na kama ni wake, huyo mke wake yupo wapi…na kwanini
asiwe wake na ushahidi upo, unajionyesha, huyo mtoto anafanana na nani…’akatulia
na kugeuza uso , sasa kumuangalia Soldier.
Soldier alikuwa kanyamaza…yaonekana alikuwa
akiwaza….akatikisa kichwa kukataa na akasema;
‘Mimi sielewi kitu….dereva, kama upo nyuma ya haya, utaniona
mbaya…..’akasema na dereva akacheka kwa dharau. Na mke wa Soldier akaendelea
kuongea;
‘Kinachoniuma zaidi ni kuwa mume wangu aliporudi akaanza
kunisakama mimi kuwa sikuwa muaminifu kwake, nimefanya madhambi na mungu
kanidhihirisha kwa kupata mtoto, akaniuliza je huyu mtoto ni wanani,..kama
kweli ni wa baba yeye ataondoka kabisa kijiji hiki ili aniachie nafasi, kama ni
mtoto wa …dereva basi, ajua jinsi gani y akufanya, kwani na yeye ana mke kama
mimi..sasa sijui hapo alikuwa na maana gani….’akatulia.
‘Mimi namuuliza sasa huyu mtoto akiwa ni wake,..mimi
nifanyeje…asema, kama yeye alishatoa maamuzi kama hayo, na mimi nitoe maamuzi
gani ikiw huyu mtoto ni wa kwake….?’
Soldier kwanza alishikwa na kitu kama ganzi, akabakia
ameduwaa, akajaribu kufikiria, hayo yametoka wapi…mbona haelewi kitu,…mbona
anazushiwa kitu ambacho hakifahamu…. baadaye akasema;
‘Umemaliza mke wangu…?’ akauliza
‘Sijamaliza, nitamaliza pindi ukinijibu swali langu ili niweze
kuendelea na kutoa maamuzi yangu...’akasema.
‘Mke wangu, kwanza hebu rejea maswala ya baba, baba
ameshutumiwa na mambo mengi tu, na mengi
ya hayo ni uzushi mtupu,…yamedhihirika hapa, na utaona mengi hutungwa na
wanadamu na wengi wao ni ndugu wa karibu tu,…ukisema mtoto kufanana na mimi
bado kuna dereva anafanana na huyo mtoto mbona yeye humshiki shati…
‘Dereva nilishaongea naye, na nikafuatilia nyendo zake,
..kuna watu walimchunguza kama yeye kama kweli huyo mtoto ni wake, na la
kujiuliza ni kwanini amkatae mtoto wake, kama ni wake…kiukweli inaniuma sana,
kwani nyie wanaume mpoje, kama umezaa umeshazaa, iliyobaki ni kusema ukweli
tu.., jinsi unavyoficha huo ukweli ndio jinsi mnavyotutesa sisi wanawake pindi
tukigundua ukweli.
‘Au unaogopa kuhusu huyo mwanamke uliyezaa naye, itakuwaje
kama unaliogopa hilo kwanini, ulitembea naye, ulipopanda mbegu ulitegemea nini,
na hayo ni maswala ya kukubaliana, maana ni wewe mwanaume ndiye mwenye maamuzi,
kidume, au sio…hahaha’ akasema akijilazimsiha kucheka.
‘Kama ni mtoto wako, mtambulishe, mimi sina wasiwasi, hata
hivyo nimeshachukua maamuzi yangu,nasubiria nikusikie utakavyojitetea,…nilikupa
muda wa kuniambia ukweli, na muda huo umeshapita, na sasa nakupatia muda wa
mwisho, ….’akasema akimuangalia Soldier.
Soldier alitikisa kichwa kama kusikitika, akainama kidogo
chini, halafu akainua uso na kumkabili mkewe, akasema;
‘Mke wangu sijui nikuambieje, kiukweli mimi sijui hayo
yametokea wapi..mimi nilikuwa vitani, nilikuwa maeneo mbali na raia, sasa sijui
hilo la mtoto, la mke,limetokea wapi…na sijui kwanini unakuwa kama unamtetea
Dereva,..jamani kama mtoto huyu sio wa kwangu, basi ni wa dereva,..’akasema
akimgeukia baba yake.
‘Mini sijui kwanini namuhisi vibaya huyu ndugu yangu wa
kufikia, yawezekana ni mbinu zake chafu,,,na niwaulize jamani..hivi mnafahamu
maana ya vita,..ndio kuna muda mnapata nafasi ya kutoka nje…, inatokea mnaweza
mkatembea tembea lakini ni muda mfupi tu, sisi tupo kwenye mikataba ya
kimataifa kuna masharti yake…hebu nikuulize hao watu waliokuambia hivyo walisema
waliniona wapi…?’ akauliza
‘Hilo kuwa wewe walikuona wapi, kwangu, sizani kama lina
mantiki, mimi ninachotaka ni jibu lako la ukweli, Je huyo mtoto ni wako au sio
wako, kama si wako sawa, basi huyu mtoto hana baba, ila mimi nitakuwa mama
yake, hilo nimeshaamua hivyo, na atakuwa mtoto wangu wa kwanza, nitamlea, na
tutaishi naye, nimeshaanza maisha yangu, najua nikiwa naye atanipa faraja, je
ni mtoto wako au sio wako…?’ akauliza
‘Mke wangu huyo mtoto sio wa kwangu, unataka nisemeje
….atakuwaje wangu, ningezaaje, na nani…?’ akauliza sasa kwa sauti ya hasira.
‘Kwahiyo unamkana mtoto wako mwenyewe…’akasema mkewe
akitabasamu ile ya kusikitika
‘Aaah, sasa hapo sikuelewi, hebu niambie wewe unataka
nisemeje, maana huyu mtoto awali alifikiriwa ni mtoto wa baba,…ikaonekana ni
uzushi,…. haya akaja kufikiriwa ni wa dereva, na wengi walijua kuwa huenda
mumeshirikiana naye, lakini wewe umelikana hilo, haya mimi unataka nikubali tu
wakati mtoto sio wangu…’akatulia, halafu akamgeukia dereva
‘Dereva, hebu ndugu
yangu..,sema ukweli tuondokane na shutuma hii tuendelee na mambo mengine,
unajua ukitaka nitumie nguvu nitatumia, na ukifika wakati huo, hutaamini kuwa
mimi kweli ni ndugi yako…’akasema Soldier akimuangalia Dereva.
‘Hahaha, bro bwana..mimi hapo sina usemi,…hayo ni yako wewe na
mkeo, na nikuambie ukweli bro, kama sio baba kama walivyosema watu, basi huyo
mtoto ni wa kwako, angalia mnavyofanana na wewe, …’akasema akicheka kama
mdhaha, hakuonyesha wasiwasi wowote.
‘Hahaha, lakini pia anafanana na wewe…sasa mumebakia nyie
wawili, ni nani mwenye huyu mtoto, mtuambie ukweli…kama baba yenu keshatoka
hapo, sasa ni nyie wawili, au labda mna ndugu mwingine anayefanana na nyie,
maana bab zenu hawaaminiki…’aliyesema ni mama
‘Mama,..kama angelikuwa huyo ni mtoto wa kwangu,
ningemchukua mara moja, mama, ni mwaka
sasa, tunatafuta mtoto mimi na mke wangu..tunataka mtoto hatujampata…unakumbuka
mimi nilioa mapema kabla ya bro…lakini sijachelewa, tutampata mtoto muda
haujafika tu, sasa kama ingelikuwa ni mimi nimezaa nje, mbona ingekuwa poa tu,
maana ningeenda kumringishia mke wangu kuwa mimi nina mtoto, yeye ndiye ana
tatizo..lakini …’akatulia
‘Kwahiyo wewe huwezi kuzaa..?’ akauliza na Shemeji, kaka
yake mke wa Soldier.
‘Nani kasema siwezi kuzaa wewe, mimi nimepima kila kitu kipo
sahihi, ila muda muafaka bado, tutampata mtoto tu mungu akipenda, na…kama huyo
angelikuwa ni wa kwangu, ningelishamchukua,..mke wangu anapenda sana
watoto…’akasema
‘Wawili chini..bado mmoja…’ akasema baba akiwa kitandani, na
wote wakawa wanajiuliza ana maana gani.
‘Hahaha baba kama mtoto, familia hii puuuh, haya sasa Soldier, ongea, si unataka
kutupeleka polisi sisi, unatuona sisi ni wahalifu, je hilo ulilofanya sio
uhalifu,.. kumbe wewe ni kiwembe kama
baba yako, ..simba mwenda pole, nilijua tu…sasa hilo, …ukicheza tu umempoteza
mke,…na uking’ang’ania na dhamira yako, ya kunifikisha polisi, …nitakuumbua
ukweli wa kukuumbua…’akasema Shemeji yake.
Soldier akamuangalia shemeji yake huyo, halafu akatabasamu,
na kutikisa kichwa kama kusikitika,… akageuka kumuangalia mkewe kwa muda tu, halafu
akageuka kumuangalia mama yake, …akatikisa kichwa, hakusema hivyo ila akilini
alijikuta akisema, `hata mama… haniamini..’
Akili haikuelewa chochote, ni kwanini wamemshuku yeye,
haelewi….na mara kikohozi kidogo kikatoka kwa yule mdada mgeni, kuonyesha kuwa
anataka kuongea…
‘Na mimi naweza kuongea kidogo…’akasema huyo mdada, lakini
alionekana akisitasita, kama anaogopa. Dereva, akamuangalia kwa mashaka, na
aliyeonyesha kushtuka zaidi ni shemeji, alikunja uso akimtizama huyo mdada….
Yule mdada kwanza akamtizana sana dereva, halafu Soldier,
kabla hajaanza kuongea…
NB: Mhh, naona imekuwa ndefu sana
WAZO LA LEO:
Uongozi ni dhamana, na dhamana hiyo ni deni kubwa, wengi wetu tunapopewa
dhamana hiyo tunachofikiria zaidi ni masilahi yetu binafsi kabla ya kulipa
gharama ya dhamana hiyo. Uongozi wa kuongoza watu ni dhamana kubwa zaidi,
yahitajia hekima, busara, na kujitolea kwingi, na wakati mwingine inahatarisha
hata maisha ya mtu. Wenye uelewi mkubwa hawapendi kuibeba dhamana hii, hata
kama ina malipo kiasi gani, lakini inabidi, kama mungu kakujalia kipaji hicho
na uwezo unao inabidi, basi kama tumeamua hivyo, kuibeba dhamana hiyo,
tujitahidi kutimiza masharti na miiko ya uongozi la sivyo, tutakuwa tunajibebea
mizigo mizito ya madhambi, na adhabu yake inaweza ikakutesa kuanzia hapa hapa
duniani.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment