‘Unajua hii familia
naichukia sana, nilimuonya sana dada yangu asiolewe kwenye hii familia, lakini
akaleta ubishi,…unaona sasa, wamefikia hatua hiyo, eti….umezaa na nani na huyu
tapeli, ….hivi kweli mumekosa la kusema..’ akasema huyo jamaa akimuangalia
Soldier.
‘Lakini hakuna aliyesema kuwa dada yako kazaa na
dereva,…kama nimesikia sawa..’akasema Yaya.
‘Haya kazaa na nani…?’huyo jamaa akauliza akimgeukia Soldier.
‘Sikiliza shemu, wewe umekurupuka tu, na jaziba zako…, ngoja
nikuambie ilivyo, huyu dereva, kwa maelezo yake anasema dada yako kabeba mimba
akatupa mtoto…kweli sikweli….?’ akamuuliza dereva.
‘Kweli kutokana na taarifa nilizozipata ..’akasema dereva
‘Kutoka kwa nani..?’ akauliza Soldier
‘Kutoka kwa raia wema ambao walimuokota huyo mtoto, na
mmojawapo ni huyo dada hapo mgeni …’akasema dereva, na watu wakageuka
kumuangalia huyo mdada aliyejifunika uso.
‘Mlikutana naye wapi, akakuambia hayo…?’ akaulizwa
‘Nikiwa kazini, mimi ni mmoja wa watu wanaoshughulikia,
kusaidia wakimbizi, na nilichaguliwa kiongozi wa kundi lililopelekwa huko ncho
ya jirani…’akasema
‘Hao raia walithibitishaje kuwa huyo aliyemtupa mtoto ni mke
wangu…?’ akauliza Soldier
‘Raia wengi tu, akiwemo kiongozi wa eneo lile,…walisema kuna
mdada mmoja alikuja na mtoto, akawa anazunguka zunguka naye, baadae huyo mdada akatoweka…baadae
wakapata taarifa kuwa kuna mtoto ameokotwa, akaletwa pale ofisini …’akasema na
kabla hajamaliza, Soldier akadakia kwa swali jingine.
‘Ndio ulijiridhishaje kuwa kweli huyo aliyemtupa mtoto ni
mke wangu…?’ akaulizwa.
‘Walivyomuelezea sifa zake, mpaka jina,…sura , umbile,…nikasema
huyo mtu namfahamu mimi, sikusema pale palekuwa namfahamu nilitafuta njia ya
kuhakikisha hiyo damu inarejea kwa wenyewe..na hata hivyo nikiwa pale bado
nilikuwa sina mawazo hayo maana majina yanafanana..mpaka nilipofanya uchunguzi ….’akasema.
‘Uchunguzi gani ulifanya..?’ akaulizwa.
‘Nilipotulia, niliamua kupiga simu huku, kwa watu ninao
wafahamu, nikawauliza, kuhakikisha jina, kama ni sahihi..ndio nikaambiwa mambo
yaliyonihakikishia kuwa ni kweli…’akasema
‘Hapo bado hukutakiwa kuhitimisha kuwa mke wangu ndiye
kafanya hivyo, maana hapo kikubwa umefuat ushahidi wa kimaumbile, …hivi wewe
ukifanya kosa mimi nitahukumiwa kwa kosa lako, maana sura na maumbile yetu yanafanana…?’
akaulizwa
‘Mimi nilipomuona huyo mtoto anafanana na na mzee, nikawa na
uwezo wa kufikiria hivyo, ukiunganisha, hayo niliyoambiwa,..na ni kweli mtoto
anafanana na nyie..na kwa vile wamemtaja mke wako kwa jina…, na niliambiwa
shemeji hapa alitoroka nyumbani kwake, ..karibu mwaka sasa…nikauliza uliza
habari za huku…nikajua ni mke wako…’akasema, halafu akamgeukia kaka yake
Soldier.
‘Unabisha kuwa dada yako hukuwahi kufika kwako...akiwa na mtoto mchanga, yule mtoto aliyekuja naye yupo wapi, alikuwa wa nani,...je hukuwa unaishi naye huko…nchi ya
jirani..?’ akauliza na jamaa akawa kimia, jamaa alionekana ana hasira zake tayari.
‘Usiniulize maswali ya kijinga mimi,... ndio dada yangu huwa mara kwa mara anakuja kwangu, na kama alikuja na mtoto au yeye mwenyewe haijalishi , yeye ni ndugu yangu, kuna ubaya gani hapo…’akasema kwa hasira
‘Uliwahi kukutana na mke wangu kabla..?’ akaulizwa dereva na Soldier.
Soldier, hakutaka kumuuliza swali shemeji yake, alijua huo sio wakati muafaka.
‘Zamani sana…kabla ya hapo,…’akasema na kabla hajatoa
maelezo, akaulizwa swali jingine.
‘Kwahiyo hukuwahi kumuona mke wangu akiwa mja mnzito..?’
akaulizwa
‘Sikuwahi…mimi nina muda mrefu sijaonana na mke wako, huwa nilikuwa
nafika huku lakini sikuwahi kukutana naye…kama nilivyosema yote hayo niliyasikia
kutoka kwa watu..na nikapiga simu kuulizia watu wahuku, nikaambiwa huyo mdada alitoroka
nyumbani kwao, kwa visa vya baba mkwe wake…nanukuu walivyosema…’hapo akatulia.
‘Walikuambia alitoroka akiwa mja mnzito..?’ akaulizwa
‘Hapana,..sikuwahi kuuliza hilo swali, ukweli ni kuwa mke wako aliondoka nyumbani kwao muda…sijui
kama alikuwa akirudi rudi au vipi, watu wengi wanahisi alipoondoka alikuwa mja mnzito, …’akasema na mara akaingilia shemeji
yake Soldier akicheka;
‘Hahaha, baba mkwe, hahaha, mumesikia jamani, baba mkwe, anafanya
uchafu huo, dada kama ni kweli niambie...au kama huyu muhuni anakusingizia niambie...'akasema shemeji. halafu akamgeukia dereva
‘Haya wewe dereva elezea, hivi visa vya baba mkwe, baba yenu
vilikuwaje, maana nataka kukusanya data…, ili huyu anayejifanya mtu wa usalama, achukue hatua...'akasema akimgeukia Soldier
‘Ndio maana nimesema sitaki kuliongea hili maana litazidi
kumuathiri baba, na naona mnaongezea mambo mengine ya kuharibu ajenda yetu, mimi nakuomba ndugu tuende kwa utaratibu, wewe sijui mna nini na bro, lakini…’akasema
dereva na Soldier akaingilia kati kwa kusema.
‘Kwanini limuathiri baba, wakati unafahamu fika kuwa wewe
ndiye muhusika mkuu wa haya yote, najua hilo litakuwa wazi, wewe ndiye
mchonganishi ….wewe unatumia ujanja ujanja wako kuwarubuni watu, kugonganisha familia…, na sasa umejaribu
kukwepesha makosa yako yaende kwa mtu mwingine…’akasema Soldier.
‘Nisikilizeni jamani, kwanza sio kwamba naingilia kauli yako mwanangu maana hayo ni mambo ya usalama, lakini nakuomba mwanangu achana na hisia zako kwa ndugu yako,...mimi ninataka tuyamalize haya matatizo ndani ya familia, nataka ukweli wote leo ubainishwe, tuoambeane msamaha…’akasema baba mtu.
‘Baba usijali,…haya tutayamaliza tu…ila kama kuna wakosaji ni lazima sheria ifuate mkondo wake, hilo siwezi kulipinga baba..lipo juu ya uwezo wangu...’akasema Soldier.
‘Sawa Soldier, nimeshakukabidhi kijiti endelea, na ajenda
yetu, mimi nipo sawa, naweza kuhimili lolote lile, kwahiyo, ongeeni tu, ila mimi
nitakuwa msikilizaji tu …msiwe na wasiwasi na mimi…mimi nina uhakika mhalifu wa
haya yote yupo hapa, nimeshamuona ni nani, sasa kama familia tutajua tutamfanyaje sio lazima sheria za kimahakama..’akasema baba yao..
‘Baba mimi nilisikia tu, usinisakame bure mimi, sikuwa na haja ya
kukuharibia hadhi yako , ila niliongea kutokana na watu walivyosema na ni baada
ya uchunguzi, na haya mengine ni kwa manufaa ya familia, je mngelikubali damu
yenu ipotee, mshukuru mtoto wenu sasa yupo mikononi mwenu…’akasema dereva
‘Dereva, wewe muda wote huo,ulikuwa wapi..?’ akaulizwa
‘Muda upi , kama ni kabla ya kufika huko nchi ya jirani
kwenye kambi ya wakimbizi, mimi nilikuwa nasoma, nilikuwa nje ..huko kwa
wenzetu, tulikuwa na mafunzo ya jinsi ya kuhudumia wakimbizi..na mambo mengine
kama hayo…’akasema.
‘Na mlikuwa mnapata nafasi ya kurudi rudi kutembelea
wakimbizi..?’ akaulizwa.
‘Ndio, lakini sikuwahi kupangiwa maeneo ya kanda za huko,
mpaka ilipofikia muda huo wa tukio, unielewe hapo… sikuwahi kufika huko kabla’akasema
dereva.
‘Una ushahidi na hilo, kuhusu ratiba yako….maana nitaagiza
watu wafuatilie,…?’ akasema Soldier.
‘Ndio ninayo,… ratiba zetu hazina usiri, na , …hahaha bro, unafikiri
mimi ndiye baba wa huyo mtoto..hapana bro… nisingeliweza kufanya hivyo, napenda
sana watoto, kama angelikuwa ni wa kwangu nisingelimkataa….na muulizeni huyo mdada
aliyemleta huyo mtoto, kama niliwahi kukutana naye kabla,…’akasema dereva.
‘Kwasababu ni uwongo…wewe umekuwa unafanya kazi za utapeli,
kuhadaa watu ili kupata mali, ilimradi tu upate pesa na mali, ndio maana hakuna
anayekuamini…’akasema baba yake.
‘Lakini baba ngoja kwanini tunazunguka, wahusika wakuu wa
hii ajenda wapo hapa, mimi nahisi tumpatie nafasi huyo mdada mgeni aongee aseme
ukweli, pia yupo shemeji hapa aongee kama kweli huyo mtoto sio wa kwake, na
kama ni kwake je alizaa na nani…?’’akasema dereva akimuonyeshea mke wa Soldier,
na wote wakageuka kumuangalia mke was Soldier.
Soldier akasema, bado hatujafikia huko, sijamalizana na wewe…’akasema
Soldier , lakini watu wengi walikuwa wamemgeukia mke wa Soldier.
Mke wa Soldier alikuwa kimia, akiwa kaangalia upande
mwingine , baadae alipoona kama vile watu wanamsubiria aongee, akamgeukia mama
mkwe wake…alimuangalia mama mkwe wake kwa muda bila kusema neno na mama mkwe
akasema;
‘Jamani haya mambo naona yanatakiwa yamalizike, …hatuwezi
kuzunguka, na kupotezeana muda, wengi naona mnamnyoshea kidole mkwe wangu, kuwa
sijui kazaa,, halafu akatupa mtoto, swali alizaa na nani, wakati mume wake
alikuwa hayupo..au sio?’akauliza mama
‘Ndipo hapo tunautafuta huo ukweli…kama alizaa , alizaa na
nani, maana ukweli wa kuzaa upo wazi, yeye kama sio kweli aupinge, watu
walimuona, sasa ataupingaje, kama anasingizwa basi aseme, …’akasema dereva
‘Dereva wakati nilipokuuliza kuhusu wewe, kuwa watu wanasema
kuwa wewe ni mtoto wa mume wangu ulisemaje..?’ mama akamuuliza.
‘Nilikuambia mimi sijui..maana mimi ni mtoto tu na mengine
yawezekana ni kusingiziwa tu, ila tuache ukweli utasema wenyewe…, na wakubwa
ndio wakuulizwa sio mimi, nilikuambia hivyo au nimekosea…’akasema dereva.
‘Hayo uliyasikia watu wakisema na hukuyachukulia kuwa ni
kweli au sio,…Sasa kwa hili, acheni ukweli useme, na waulizeni wakubwa,
msimsakame mwanangu, huyu binti hapo alipo amefungwa na masharti, sasa labda
nimuulize mume wangu, ..je upo tayari kwa lolote lile…?’ mke akamuuliza mumewe.
‘Nimeshasema, kwani kuna tataizo gani, mimi nipo ok…nafahamu
mke wangu mpaka sasa hujaniamini, unahisi labda kweli yanayosemwa na watu yana
ukweli…mke wangu ni kweli nilikuwa nalewa, ni kweli nilikuwa napitiliza, naweza
kukosea chumba na kwenda kulala kwa eeh, mkwe,..lakini nalala sakafuni,
nilizidiwa kipindi kile, lakini nisingeliweza kufanya tendo kama hilo,..nina
uhakika na hilo …’akasema.
‘Hahaha mzee umejileta mwenyewe, umesikia mdogo wangu..?’
akasema Shemeji akimuangalia dada yake.
‘Huyo ni baba mkwe wako anakiri mwenyewe kuwa ni mlevi,
analewe anapitiliza anakuja chumbani kwako, anakuja kufanya nini, halafu bado
unataka ….kung’ang’ania ndoa,..unataka uchangie mume pamoja na baba
yake…hahaha, mimi hilo sitalikubali kamwe, kuanzia sasa wewe …’akashindwa
kumalizia.
Mama akawa kamgeukia
mumewe, akisubiria kama mume wake ana maelezo ya ziada, na lipoona mume wake
yupo kimia akasema…
‘Mume wangu mimi nimekuuliza je upo tayari kuyasiki hayo
atakayoyaongea mkwe wako, yaani mke wa mwanetu, maana kuja kwake huku, kwanza
ni kukuona , halafu ni kuhitimisha matatizo yake na mumewe..amesema leo anakuja
kuusema ukweli wote,…mimi nilimuambia asubirie kwanza maana wewe hujawa sawa…’akatuliza
‘Mimi naona baba hayupo tayari…tunakimbilia mambo ambayo
yaweza kumuathiri baba, kwanza niachieni mimi nifanye kazi yangu, mnivumilie
tu,… nitawahitaji dereva na shemeji tukitoka hapa tupitie polisi, kuna maongezi
na mahojiano,…ni utaratibu tu wa kawaida, na huko najua tunaweza kuupata ukweli
wa haya yote bila kumsumbua baba…’akasema Soldier.
‘Kwanini unipeleke polisi, kwa kosa gani, …?’ akauliza
shemeji mtu.
‘Nimesema ni maswala ya kawaida, mtahojiwa na mkimaliza
mtaruhusiwa, kama hamna makosa mna wasiwasi gani…?’akasema Soldier kama
kuwauliza.
‘Huko mimi siendi, …kwanza niambie nina kosa gani , naenda
huko kuhojiwa kwa kosa gani, hiyo ni haki yangu kufahamu…kwanza mimi nina aleji
na vituo vya polisi, unasikia , na pili wewe wewe kama nani wa kuniamrisha
niende kituo cha polisi, wewe ni askari wa vita sio polisi, na kwasababu hiyo
mimi siwezi kwenda huko…’akasema
‘Nina RB, ya kufanya hivyo, sio kwamba nakurupuka tu….utaratibu
wote umefuatwa, mimi nimechukulia hivi kama ndugu, kuliko waje wawakamate
wawatie pingu, nikasema mimi nitawachukueni kistaarabu tu…’akasema akitoa
karatasi ya kuonyesha hiyo RBi.
‘Swali bado hajanijibu nimefanya kosa gani…?’ akauliza
shemeji mtu.
‘Huna kosa,..unasikia, kosa ni mpaka lithibitishwe na ndicho
hicho wanataka kufanya, sio nyie tu kuna wengi wanaitwa kwa kuhojiwa, ni mambo
ya kawaida, ya ulinzi na usalama, na sijui kwanini uogope, sijui kwanini
ukatae, ukikataa basi nitaiachia sheria ichukue mkondo wake…’akasema Soldier.
‘Jamani hayo ni yenu, hebu kwanza tumalizane na
hili…’akasema mama akimuangalia mume wake.
‘Mke wangu hilo nalo ni kubwa, linahusu jamaa zetu, au sio
ni muhimu kujua nini kifanyike, hata kama wataenda tuwe tumejipanga kwa lolote
lile, ..mimi kama kiongozi wenu sina shaka, najua hayo ni mambo ya usalama tu,
sioni kwanini mkatae kwenda huko…na mke wangu unasemaje, ….maana akili ilikuwa
imeshutuka, unataka nifanye nini sasa, ok, tumalizane na hili letu au sio..?’
akauliza baba yake Soldier.
‘ Kwa hivi sasa tunahitajia kauli yako, kama kweli utaweza
kuhimili hayo yanayotaka kufanyike, je kweli upo sawa kuhimili lolote, maana
mkwe wako anaweza kuanza kuongea mambo ambayo yatakugusa, halafu ukadondoka kwe
presha…’akasema mkewe.
‘Kitu gani cha kunidondosha mimi kwa presha…, mimi sina
wasiwasi mke wangu, kwa vile muhusika wa haya yote yupo hapa, na yupo tayari
kutoa ushirikiano,…hana ujanja ni lazima atoe ushirikiano,… mimi ni askari
mstaafu, naweza kumuhisi muhalifu kwa kumuangalia tu…’akasema akimuangalia
dereva, na dereva akatabasamu, na kusema;
‘Baba…tatizo labda unahisi bado nipo kwenye yale mambo yetu,
hapana mzee, kule nimeachana nako kabisa nilikuwa na maana yangu na maana hiyo
imeshakamilika, sina shaka tena, na nafahamu bro anataka niende polisi kwasabau
gani, na hilo kwangu halina shaka, mimi siogopi kwenda huko, na itakuwa vyema
kabisa maana sasa mambo yapo hadharani, na yale yangu na baba, tulishayamaliza,
au sio baba, yale yamepita maana ukweli
sasa upo mezani, kwahiyo yanayofaa kuongewa yaongewe tu,…’akasema dereva.
‘Kwahiyo wewe unatuthibitishia kuwa huyo mtoto sio wa
kwako…?’ akauliza mzee.
‘Huyo mtoto sio wa kwangu baba, maana sijawahi kutembea au
kuja huku na kukutana na ..’akageuka kumuangalia mke wa Soldier,
‘Muulizeni…shemeji aseme ukweli,…na kwanini mzee, tunarudi
nyuma, na labda mtasema kuhusu huyo binti mgeni, mimi sijawahi kukutana na huyo
binti mkimbizi kabla, sikuwahi kumfahamu kabla kama unafikiri mimi nilikula
njama na yeye,..unasikia na kulithibitishia hilo,, mpeni nafasi huyo binti aongee
ukweli, aeleze alivyomuokota huyo mtoto, na jingine mnaweza kuwasiliana na
uongozi wa huko , alipookotewa huyo mtoto…’akasema.
‘Mhh…hapa naona hatuwezi kufikia muafaka, maana mara mke wa
Soldier aongee, sasa mnarudi kwa huyo mgeni, yupi na yupi mnataka
awathibitishie lipi…?’ akauliza mama.
‘Soldier…ongoza kikao, mimi nitakuwa msikilizaji…’akasema
mzee.
‘Jamani naona nianze
kuongea mimi…..’aliyesema sasa alikuwa mke wa Soldier, na Soldier
mwenyewe akamkazia macho, kama kuonyesha mashaka fulani, lakini mkewe hakutaka waangaliane, maana
ukitaka kumuua nyani msiangaliane machoni.
‘Wazazi wangu, na ndugu na jamaa zangu….naongea hili kutoka
undani wa moyo wangu…’akaanza kuongea.
NB: Hii sehemu nimejaribu kuweka mambo mengi kwa pamoja, ili
tuharakishe kukimaliza hiki kisa, sijui kama nimekosea?
WAZO LA LEO:
Mnapotaka kutoa hitimisho la jambo, iwe ni hukumu au uamuzi fulani, ni muhimu
kuwe na mizania ya usawa, ya kuwahusisha wale wote wanaokisiwa kuwa watendaji
au wakosaji. Tusipendelee kuangalia upande mmoja eti kwa vile ni ndugu, rafiki
au chama au imani moja, haki itapatikana pale wewe msemaji au mtoa hukumu, utakapoweza
kuwasikiliza wote bila kubagua, na ukaweza kupitia ushahidi, …uchunguzi na
tafikiti yakinifu. Tusipende kuhukumu kwa kusikia tu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment