Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, March 22, 2017

KITANDA HAKIZAI HARAMU-24


‘’…ni lazima nimuwajibishe huyu mtu, ili iwe mwanzo na mwisho wa kuwasumbua watu, na humo humo ninaweza kujua kama kweli aliyoyasema kuhusu baba yana ukweli au anamsingizia tu mzee wa watu, ili atimilize tamaa zake za kupata mali, …mmh,..lakini sasa …ushahidi, huyu mtu anasema ana ushahid wa kaka wa mke wangu, huyu shemeji namtafuta sana..

‘Ngoja, kama Dereva ana ushahidi kumuhusu Shemeji, ni lazima niongee naye, ili niweze kuupata hup ushahidi, na ili nifanikiwe hilo, itabidi,..ooh, shida sasa, hapa kuna mtego, nikubali kushirikiana na dereva, au…’ hapo ndio akageuka kumuangalia dereva, kuhakikisha kama bado yupo…, sasa badala ya kumuangalia dereva….akaona mambo mengine,,

Tuendelee na kisa chetu…

************

Macho ya Soldier yakavutika na jambo jingine, ikawa sio kumuangalia dereva tena,  na alichokiona kilimfanya ayatoe ya kutoamini, akajawa na mshangao, mshangao wa aina yake, ilikuwa kama miujiza kwa anachokiona, akajikuta sasa akigeuka mzima mzima, kuhakikisha,..hakuamini macho yake...

 Alitizama kule walipokuwa wengine wakiwa wamezunguka kitanda alicholala baba yake, nia ni kumuangalia dereva kuhakikisha kuwa yupo..lakini hilo halikuwepo kichwani tena, alichokiona kilivuta mawazo yake yote….

Ilichukua muda kuamini, alichokiona, na baada ya kujirizisha kuwa anachokiona ni kweli, sasa akavutika kusogea kule walipokuwa wenzake, huku uso wake ukiwa umechanua kwa furaha, akasogea hatua kadhaa hadi kuwakaribia wenzake ambao nao walikuwa kwenye mshangao, lakini kwa tofauti tofauti…

‘Mzee umepona…’akasema huku akizidi kumuangalia baba yake…,, na wakati huo baba yake naye alikuwa kakodoa macho akiangalia jambo jingine mbele yake, kule walipokuwa hao wageni waliongia, mshangao aliokuwa nao baba yake Soldier hakuwa tofauti na mshangao wa Soldier mwenyewe, japokuwa kila mmoja alikuwa akishangaa jambo lake…

Unajua baba yake Soldier alifikia sehemu hawezi hata kuinuka, mwili ulikuwa kama umepooza, kila akijaribu kuinuka anahisi maumivu makali, na ikawa ni mtu wa kitandani kila kitu kinafanyikia kitandani, sasa kwa maajabu hayo yalitokea mzee alikuwa kaweza kuinuka na kukaa kitandani peke yake bila msaada wa mtu, ….

Soldier alimuangalia baba yake kwa shauku kubwa na kusema tena…:

'Baba umepona...umeweza….ku-ku-inu.-' akawa anaongea huku anashindwa kumalizia maneno yake, macho yakiwa yamemwangalia baba, na kidigo akamwangalia mama yake ambaye naye alikuwa kwenye huo mshangao..na kwa haraka akarejesha macho kumuangalia baba yake kama vile hataki kuikosa sekunde moja ya kumuangalia baba yake…

Mama yake naye alikuwa ameshikwa na butwaa, na sasa yeye alikuwa akinua mikono juu kushukuru, kumshukuru mungu, na kwa sauti akasema….
‘Siamini…ahsante muumba wake…’akasema mama yake.

Dereva yeye alikuwa kama baba yake alikuwa kaelekeza uso wake kule baba yake alipokuwa akitizama alikuwa naye kashikwa na mshangao wa aina yake, haamini hicho anachokiona, na hakutaka ageuke ili aweze kuona vyema, lakini mke wa Soldier alikuwa usawa unaomzuia kuhakikisha hicho alichokiona,
Kuna mwingine naye alikuwa kwenye mshangao lakini sio wa kuzidisha kama walivyowengine, yeye alikuwa akitabasamu huku akitikisa kichwa, kuashiria kuwa kuna jambo kaliona na kuliona kwake kumempa furaha fulani, huyu alikuwa kaka wa mke wa Soldier.

Soldier sasa aliamua kusogea kabisa hadi pale kitandani alipolala baba yake, akiwa na furaha usoni, akaenda kukaa karibu na baba yake, kuhakikisha kuwa anachokiona kipo sahihi, akawa anamkagua baba yake mwilini, maana kuinuka huko kulimfanya sehemy ya kifuani kuwa wazi, alikuwa kavuliwa shati, soldier akarudia tena yake maneno,;

'Hatimaye sasa baba umepona..'akasema, na baba hakujibu kitu, bado macho yake yalionyesha kuangalia jambo, ambalo lilimfanya naye awe kwenye mshangao, mshangao uliompa kitu kama mshtuka na kumfanya aweze kuinua mwili uliokuwa hauwezi kuinuka na kujikuta amekaa mkao wa kawaida pale kitandani.

Kutokana na ile hali, ya baba yake kuangalia huko mbele, kwa wale wageni, soldier naye akavutika kuangalia huko, kuona hicho baba yake alikuwa akitazama, na kitendo hicho kikafanywa pia na mama yake…

'What..'ilikuwa sauti ya Soldier, lkn alikuwa kachelewa, hakuweza kuhakiki hicho kitu, na kwahiyo ubongo wake haukuweza kunasa lolote la msingi zaidi ya kuingiwa na kiwingu kidogo cha mawazo , lakini kwa vile hakuweza kwa haraka kufahamu ni kwanini moyo na akili yake ilishtuka kidogo, akapotezea, na kumgeukia baba yake..

‘Naona tumuite docta…’akasema

‘Wa nini…?’ mama yake akauliza
‘Huoni kaweza kuinuka, docta anaweza kumkagua na kumuongezea sdawa za kumsaidia zaidi…’akasema Soldier.
.
Kwa muda ule, huyo baba yake alikuwa katizama chini, kama anawaza jambo lakini baadae akainua uso wake kutizama huko mbele, sasa hakukiona kile alichokuwa akikitizama, …mke wake alikuwa keshajua mume wake alikuwa akitizama wapi, lakini hakuelewa ni kwanini mume wake apate mshituko wa namna hiyo mshituko ulioleta neema.
.
'Ndio yeye..'ilikuwa sauti iliyotokea kitandani, na sauti nyingine miongoni mwa watu waliokuja kumuona mgonjwa ikatamka maneno kama hayo ila yeye alisema:

'Ndio wewe..lakini umefuata nini huku, hujui hairuhusiwi…'huyu alikuwa dereva
Na mwingine naye akasema kwa sauti ya bashasha,…
‘Oh, hatimaye umejileta mwenyewe….’ilikuwa sauti ya kaka wa mke wa Soldier

'Umefuata nini huku..?'huyu alikuwa dereva alikuwa akiuliza akiwa kawageukia wale wadada wawili, haikueleweka, anamuulizia nani kati ya wale wadada wawili.
.
Kukapita ukimia fulani, hakuna aliyesema neno, na aliyeuvunja huo ukimia alikuwa yaya, alisema:

'Jamani huyu ni dada yangu pacha, japokuwa hatufanani sana, alikuja kunitembelea, na tumekutana naye kituoni akinitafuta, hakujua tunaishi wapi . .ana kibali rasmi..'akasema.

'Lakini huo uvaaji wake unatia mashaka, ni kama anajificha, anaogopa nini sasa...'akauliza Soldier.

'Ninajua ni kwanini unafanya hivyo, ulifikiri sitakuona tena, kwanini ulinitoroka?' alisema kaka yake mke wa Soldier, sasa akimsogelea na yule msichana akawa kainama chini.

'Mlikutana naye wapi, haishi huku huyu, baada ya kupatwa na matatizo ndio alikuja kujiunga na sisi pale kambi ya wakimbizi..'akasema Yaya akiwa kama anamkinga dada yake kutoka kwa kaka wa mke wa Soldier.

'Ninafahamu, namfahamu sana huyu ndugo yako muulize mimi ni nani kwake…hakuwahi kukuambia mtu gani alimsaidia,…na anajua nilivyomwambia, kuwa nipo tayari kumsaidia zaidi,..lakini nilishangaa kutoroka, kule alipokuwa akiishia…na..na..’ kabla hajamaliza, yule yaya akasema;
‘Hakutoroka ilibidi afuate utaratibu…’akasema Yaya,

‘Nafahamu kiutaratibu wakimbizi hawatakiwi kuwa uraiani, mpka uwe na kibali, lakini yeye alikuwa na tatizo, yeye alikuwa bado sio mkimbizi...'akasema jamaa.
,
Kitu kingine kilichomshangaza Soldier ni tabia ya huyo Yaya, kumbe ni muongeaji hivyo, mbona awali alikuwa anaongea,kwa mashaka, sasa akawa anamuangalia makini, ni kama aliwahi kumuona mahali, lakini hakuweza kukumbuka ni wapi…halafu akageuza uso wake kumuangalia mkewe, macho yao yakakutana, kumbe mkewe naye alikuwa akimuangalia, na kwa haraka kila mmoja akaangakia kwingine. Aliyeona hicho kitanda alikuwa mama yake Soldier, na kitendo hicho kilimfanya mama huyu atabasamu

*********

'Hata mimi namfahamu huyo binti,..ningelifurahi kama ungeacha uso wako wazi, unaogopa nini,…kama ni wewe yule…sioni kwanini ujifiche, na kama una kibali kuwa huru,,,lakini hebu ondoa hayo mawani uache uso wazo ili nihakikishe, nahisi ndio maana ulikuwa unaogopa kuingia...'akasema dereva.

'Wewe… na tabia yako kila mtu unamfahamu,...’akasema Soldier, na Dereva akacheka kwa kama mzaha fulani, na Soldier hakutaka kuongea zaidi na huyo ndugu yake badala yake akamgeukia baba yake na kusema;

‘Mzee vipi, na wewe je, maana mpaka sasa nakuona macho yako hayabanduki kwa hao wageni, vipi kuna jambo gni limekuvutia kuwaona, maana huyo ni Yaya wa mtoto na huyo mwingine, sijui…kama alivyosema yaya, ni ndugu yake, kwani mzee unamfahamu huyo binti?.'Soldier akamuuliza baba yake

'Hata siamini, dunia hii, hapana, na sijui kwanini nilipoiona sura yake nilishikwa na mshituko wa namna hiyo,…unajua, hata sielewi ni kwanini,…hebu binti, samahani hebu sogea huku nikuone vyema, wewe ni nani hasai,...?'akauliza mzee.

'Mume wangu, hebu kaa vizuri, naona macho yako yamekuwa hayabanduki kwa huyo binti....umeshaambiwa ni ndugu yake Yaya, wewe unazidi kumtamani, huchoki, mtu bado unaumwa, ..bado ..?'akasema mkewe.

'Mke wangu bwana, wivu…utakupoza, hujui ni kwanini nasema hivyo, wewe hujiulize ni kwanini mpaka nikapatwa nah u mshtuko, hadi nikaweza kujiinua,..unajua, nilihisi kitu kinakata kwenye kiuono, nilipojilazimisha kuinuka, na sasa…ooh, nimeweza….’akasema.

‘Sasa tuambie ni kwanini, maana huyo ni mgeni,…wa Yaya..’akasema mke wake.
‘Mgeni wa Yaya, ni mgeni wetu au sio…huyo binti kama ni yeye....ana kesi ya kujibu, lakini kwa vile ni mgeni wetu, naomba mumkaribishe vyema, ila baadae nataka kuongea na yeye, ni muhimu sana kwangu...'akasema mzee.

'Kuhusu nini mzee..?'akauliza Soldier, sasa naye akimuangalia huyo binti kwa makini, lakini kn usingeliweza kumuona sura yake, alishajifunika, na sasa likuwa amegeukia upande mwingine.

Soldier, hakupata bahati ya kumuona vyema usoni, kwani wakati anamuangalia ndio wakati binti huyo anajifunika, inaonekana kuna kitu alikuwa akimuonyesha mke wa Soldier wakati wanaongea,... na alipogundua watu wanamuangalia akajifunika kwa haraka.
.
'Huyu binti ndiye yule aliyekuja na mtoto akamtelekeza kwenye mlango wa chumba cha hoteli niliyokuwa nakaa nikiwa huko nchi ya jirani, kiukweli niliapa siku ya kuonana naye namsweka ndani, maana kanisababishia majanga...'akasema mzee.
'Ndio yeye mzee, sijahakikisha lakini nilivyomuona alipojifunua hapo, nikajua ndio yeye,..hata hivyo mzee, mimi ndiye niliyemtuma afanye hivyo, nikiwa na maana muhimu sana....'akasema dereva.

‘Ulikuwa na maana gani…kunizalilisha..’akasema mzee kwa hasira.
‘Mzee tulishaongea hayo, usitake tumwage mtama kwenye kuku wengi, hayo yalishapita, au..?’ akasema dereva kama anauliza, na Soldier akadakia kwa kusema;

'Sawa kabisa, nilijua tu haya yote wewe ndiye muhusika, haya dereva tuambie ukweli, ulivyo, kumbe wewe ndiye umempachika mtoto wa watu mimba..halafu unamsingizia mzee….'akasema Soldier akimuangalia Dereva..

‘Mtoto wa watu yupi ..huyo mtoto sio wa huyo binti, huyo binti alimuokota, mtoto huyo ni wa mke wako…muulize mke wako kaipatia wapi hiyo mimba, …kama mnataka tuanze kueleza ukweli mbele za watu…mke wako ndiye wa kuulizwa, sio …..’akasema dereva, na Soldier akamgeukia mke wake, lakini kabla Soldier hajasema kitu, aliyeongea kwa kumkatiza dereva alikuwa kaka wa mke wa Soldier.

‘Subiri..subirii…mnasema nini…?’ akasema kaka mtu akimgeukia dereva halafu Soldier..

NB: Kazi kweli kweli

WAZO LA LEO: Muumba wetu anafahamu ni lini , na kwa namna gani atupatie haja zetu, wengi wetu hufikia sehemu ya kukata tamaa, na hata kulalamika kwanini mimi…naomba sipati, kwanini mimi nakuwa mtu wa shida, kwanini mimi…na hali hii inafikia mtu kupungukiwa na imani zetu za dini, na kujiingiza kwenye shiriki. Ni kweli matatizo, shida, nk, yanafikia ukomo wa akili zetu, ukomo wa kuvumilia, lakini yote hayo tumkabidhi mola wetu , yeye ndiye anajua zaidi,..kamwe tusikate tamaa na kukufuru, tutashindwa mitihani hii ya maisha.
Ni mimi: emu-three

No comments :