Watu wote walikuwa wamegeukia mlangoni wakiangalia huo ugeni
uliokuja, kumuona mgonjwa, na kilichovuta hisia za hao, ni hiyo tabia ya
kubakie nje. Badala ya kuingia ndani na mama yake Soldier, ni kama wanaogopa ..
'Ni kwanini wageni wanahofia kuingia ndani, hapa ni hospitalini, hamuna haja ya
kuogopana...?'akauliza dereva aliyekuwa na shauku ya kuwaona hao wageni .
'Sio wote wana tabia kama zako wewe...'akasema Soldier.
'Mimi nina tabia gani bro…?'akauliza dereva akitabasamu.
'Utaijua tabia yako pindi ukisimama ndani ya chumba cha gereza..'akasema
'Kwanini niwekwe huko, gerezani, hahaha…Bro mimi ni mtoto wa mjini, najua ni
nini ninachokifanya, nina elimu ya kutosha kujilinda, nafahamu sheria,...siwezi
kuogopa kufungwa, kwa vile mimi nina uhakika sijafanya kosa,...'akasema.
' Unasema una uhakika hujafanya kosa,..kupiga watu kuwaumiza sio
kosa, umewajeruhi watu, angalia hali ya mzee hapo ilivyo kisa ni nani,..haya huku
unawahadaa watu kwa mlungula, ili matakwa yako yatimizwe hayo sio makosa…?’
akawa kama anamuuliza.
‘Hahaha, bro bwana, tatizo lako hujui hayo matatizo, mimi sijui
ilivyokuwa, na sipendi hali hiyo, hujui jinsi gani inavyonitesa…’akasema
‘Sasa...mimi kama mwana usalama nitahakikisha sheria inachukua
mkondo wake, wewe si hujui, basi ukiwa kwa pilato, utajua,.....siwezi kuona
mzee kalala hapo kitandani, hawezi kuinuka sababu yako...halafu unajifanya una
huruma,....maisha gani ya ujanja ujanja, na tamaa za mali...'akatulia alipoona
hao wageni wanaanza kuingia.
‘Sijamalizana na wewe, jiandae kabisa tukitoka hapa tunapitia
polisi…’akasema na kabla Dereve hajasema neno hao wageni walishaingia, na
mazungumzo hayo yakakatika.
Soldier alishaanza kukasirika..kila akiliwazia hilo tukio,
alihisi mwili ukimchemka, na hata wageni hao walipoingia yeye hakuwa na shauku
nao, akilini alikuwa akiwazia jinsi gani ya kumuwajibisha dereva. Jinsi gani
ataweza kumchukua hadi polisi bila kumuathiri baba yake..
‘Huyu mtu inabidi nimuwajibishe, na ….’akatulia kuwaza na
kusogea mbali, ili kuwapisha hao wageni kusalimiana,…
Walioingia mwanzoni walikuwa ni akina dada wawili, wa kwanza
alikuwa yule yaya wa mtoto, lakini kwa muda huo hakuwa na mtoto, ina maana
mtoto kamuacha na mke wa Soldier, na wa pili ndiye aliyevuta hisia za watu
zaidi….
Mdada huyu alikuwa kavaa kitu kama ushungi,…ni kitambaa
kilichoweza kufunika kichwa chote, na kuacha sehemu ya uso..na akavaa na
mawani,…huyo mdada alihakikisha kuwa sehemu yote ya uso haionekani, uvwaaji huo
uliwavutia wengi, hata huko nje alipokuwa anapita…kwani haikuonekana kuwa
alivaa hivyo kiimani ya dini,…kwasababu ya vazi lake la chini, ilionekana ameamua
kuvaa hivyo huenda ni kwa ajili ya
kuficha uso wake, sasa ni kwanini aufiche uso wake…
Baadae wakaingia watu
wengine wawili, hawa walikuwa ni mwanamke na mwanaume, wanajulikana, walikuwa
mke wa Soldier na kaka yake...
Soldier alipowaona hao wawili akazidi kusogea mbali kabisa,
hakutaka hata kusalimiana nao, akafika kwenye dirisha na kuangalia nje…,
**********
'Mtoto yupo wapi?'ilikuwa swali la baba yake Soldier
aliposalimiana na mkwewe huyo, yaani mke wa Soldier.
'Yupo na bibi yake..tusingeliweza kuingia naye huku ndani,
wametushauri madakitari tusiingie naye, kwa taratibu zao...'akasema mke wa
Soldier, na baba yake Soldier akageuza uso kumtafuta mwanae alipo alitaka
kuongea jambo, lakini alipoona mwanae hayupo karibu wakaongea mambo mengine, na
aliyeongea sasa alikuwa dereva.
‘Mambo mengine wanajua wao wenyewe, inabidi uwatii tu, ina maana
mtoto hatakiwi kumuona mgonjwa..kama ni mama yake, au baba yake…’akasema
'Ni sawa wafanyavyo,..unajua afya za watoto ni tofauti na zetu,
wao ni rahisi kuambukizwa magonjwa, ndio maana wanachukua tahadhari hiyo…’akasema
mama wa soldier.
‘ Sawa hamna shida, lakini Soldier yupo wapi…’ akauliza na kabla
hajajibiwa akasema;
‘Hata hivyo ninashukuru mumekuja kuniona,..mimi hali yangu,
usiku ndio ilikuwa mbaya sana, na sikujua kuwa nitaweza kuamuka tena, ndio
maana nilipoweza kuamuka tu, nikawaita wanangu..nashukuru kuwa na nyie mumeweza
kufika, huenda safari yangu imekaribia..’akasema na kumfanya mkewe amtupie
jicho.
‘Si mnajua mtu hafi mpaka awaone wote aliopangiwa wamuone,..yaani
hata mtu alikuwa wapi, kama alipangiwa aonane na ….ni lazima atafika tu, na
yule ambaye hakupangiwa , atajitahidi lakini atakumbana na vikwazo, akifika
anakuta mtu alishafariki…sio nasema kwa vile nahisi ninakufa…, hata chakula, kila
mtu anafungu lake la riziki hawezi kuondoka duniani mpaka fungu lake alimalize,
tunaambiwa hivyo na imani zetu za dini...;akasema
'Wewe sasa umekuwa mtu wa kutangaza dini, na yote hayo ni kuogopa kufa..,
wangapi wanaumwa wanaishi na wazima wanakufa..'akasema mkewe.
'Nimefurahi tu..mke wangu, maana niliowakosea wanafika mmoja
mmoja na kwahiyo napata muda wa kuwaomba msamaha...na ufanyeje sasa, kama sio
kuyaongea hayo…'akasema .
'Hebu achana na lugha yako ya kutuvunja nguvu, wewe hujui jinsi gani lugha yako
hiyo inavyotuumiza wenzako..'akasema mkewe.
'Hahaha kumbe mke wangu bado unanipenda..'akasema na mkewe
akabakia kimia na wengine wakawa wanatabasamu…
Kwa muda huo Soldier alikuwa kasogea mbali kabisa, alikuwa
kasimama akiangalia kupitia dirishani, na mke wake mara kwa mara alikuwa
akijitahidi kumtupia jicho la kujificha, lakini hawakuweza kwenda kumsalimia,
wakawa wamemzunguka mgonjwa.
*************
Soldier alitaka kutoka nje,
lakini alijua bado baba yao alikuwa akimuhitajia, kwahiyo, akawa amebakia pale
pale, akikwepa kulisogelea hilo kundi la watu wwaliofika kumuona mgonjwa.
Alihisi kuwa akisogea kwenye hilo kundi, atajikuta akizozana na
watu, pale, yupo dereva, ambaye ndio katoka kuzozana naye, japokuwa alijitahidi
kujizuia lakini akashindwa, sasa kaja adui yake wa asili, shemeji yake. Huyo
hakuna siku walikutana wakaacha kuzozana, na sana sana wanaishia kutupina
ngumi.
Yupo mkewe, ambaye tangia arudi,wameshindwa kuelewana, mpaka
ikafikia mkewe kuondoka kwenda kwao, kisa hasa ni kwanini mkewe hataki kumuelezea
ukweli kuhusu mtoto, huyo mtoto ni wa nani, kama ni wake kazaa na nani,…na sasa
ndio kasikia jipya ambali hakupenda hata kulifikiria maana haiwezekani, eti
baba yake ndiyo kazaa na mkewe, haiwezekani kabisa, hilo haliingii akili mwake,
na hakutaka hata kulifikiria.
Lakini sasa lipomuona mkewe na alionekana akisalimiana na baba
yake bila kikwazo, akaanza kulikumbuka hilo, na sasa akawa anafikiria kile
ambacho hakukitaka kukifikiria awali,;
‘Je kama ni kweli,…kuwa baba yake ndio kazaa na mkewe,…haiwezekani,
hilo halipo ..sikubali , sitaki, uwongo…’akajikuta akipiga ukuta ngumi.
‘Huyu dereva ni mzandiki, ndio maana nataka akafungwe…’akasema
wka sauti ndogo,
‘Huyo mtoto ni wa dereva,..kama ni wa dereva, ina maana
alitembea na mke wangu, ..haiwezekani, …oh, mbona hali hii inanitesa
hivi,..nitaua mtu…’akapiga ngumi ukuta tena, na kuwafanya watu wageuke
kumuangalia.
Alipowazia hilo akataka kugeuka kuwaangalia hao watu walioingia
lakini bado akili yake ikagoma kufanya hivyo akabakia akiwa kasimama, akiwa
amewapa mgongo wenzake, na alikuwa yupo mbali kidogo na wao.
********.
Na wakati huo ndio baba yake na mama walikuwa wakiongea,
alipenda hiyo hali iwe hivyo, wazazi wake wapendane, waoneane huruma.
Kiukweli moyoni anawapenda sana wazazi wake, na aliapa kuilinda
ndoa ya wazazi wake mpaka dakika ya mwisho.
Ilimsikitisha sana pale ilipotokea baba yake anaumizwa na dereva,
mbele ya macho yake, na mhalifu bado yupo huru, alipowazia hilo sasa akageuka
kutaka kumuangalia dereva, asije akatoroka, kuna mambo mengi yanamfanya
amchukue dereva waende naye kituoni, pamoja na hilo la kuumiza watu, lakini
alishawahi kuongea naye, na inaonekana dereva ana ushahidi utakaomuwezesha
kumfunga kaka wa mkewe.
Kaka wa mkewe anasadikiwa kuwa anajihusisha na uuzaji wa madawa
ya kulevya, lakini bado hakuna ushahidi wa moja kwa moja..lakini dereva
alitamba kuwa anao huo ushahidi na huyo kaka amekuwa akimlipa pesa nyingi tu
kumziba mdomo.
‘Lakini nitaupataje huo ushahidi wakati hatuelewani…na ili
niupate huo ushahidi inabidi nimuweke huyu mtu ndani, niongee na polisi wafanye
hivyo, lakini sasa, ..nikimuweka ndani
nitakosana na baba, baba anampenda mwanae, baba anaogopa kukosana na mke wa
rafiki yake, baba alishachukua dhamana ya kuilinda hiyo familia, baba ana mambo
ambayo amemuahidi dereva na akifanya kinyume chake ataumbuliwa, sasa..nifanyaje
hapo…’akajiuliza
‘Huyu kaka yake mke wangu anadhaniwa kuwa anauza madawa ya
kulevya,…na mimi nimepewa jukumu la kumfuatilia,…’akawaza.
‘Ni kweli ni moja ya kazi zetu watu wa usalama….lakini haya
majukumu mengine ni ya polisi, na wameniomba niwasaidie, hakuna shida,
nitaifanya hiyo kazi,,.. lakini sasa, mbona mke wangu anamtetea sana kaka yake,
anasema watu wanamuhisia tu vibaya kaka yake, na alishasema siku nikimfunga
kaka yake ndio mwisho wangu mimi na yeye, mpaka tumezozana kuhusu hilo, je
nikipata ushahidi kutoka kwa dereva, …ina maana ndio itakuwa mwisho wa ndoa
yangu, .nifanyeje hapo…mmmh, ngoja nione…’akajiuliza.
‘Kwanza ni lazima nianze na huyu dereva,…nitamchukua hadi kituo
cha polisi, akahojiwe, tutambana mpka tutaujua huo ukweli…nitalifanya hili leo
wakati baba akiwa huku hospitalini, na nitahakikisha baba halijui hili…najua
mama yake atakuwa wa kwanza kukimbia kwa baba…’
‘Aaah, baba atanielewa tu, ni lazima nimuwajibishe huyu mtu, ili
iwe mwanzo na mwisho wa kuwasumbua watu, na humo humo ninaweza kujua kama kweli
aliyoyasema kuhusu baba yana ukweli au anamsingizia tu ili kupata mali, …mmh,..lakini
sasa …ushahidi, anasema ana ushahid wa kaka wa mke wangu ..nitaupataje, anaweza
kunitega kwa hilo..ngoja…’ hapo akageuka kumuangalia dereva, kuhakikisha kama
bado yupo…, sasa badala ya kumuangalia dereva….
Macho yake yakavutika na
jambo jingine, na kumfanya macho yake yafunguke kwa mshangao, mshangao wa
kutokuamini hicho anachokiona, akajikuta sasa akigeuka mzima mzima..hakuamini
macho yake...
NB: Ni nini alichokiona
Soldier,
WAZO
LA LEO: Mtenda wema anaweza kujitahidi sana kutenda wema, anaweza
akatenda wema tisa, na bahati mbaya akakosea jambo moja tu,… jambo hilo moja tu
likaja kuharibu wema wake, na akaonekana kama hakufanya kitu, kwa kosa hilo
moja ni kwanini lije liharibu wema wake.., ni kwasababu mtenda wema anapofanya
wema wake anakuwa na maadui wengi, maadui ambao hawataki wema , kwao wao, wema
unawazibia nafasi ya kufanya maasi yao,…Ewe mtenda wema usivunjike moyo kwa
hayo, endelea kutenda wema, kwani wema ni kwa ajili ya wanyonge na wema njia yake ni ya peponi,…
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment