Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, March 13, 2017

KITANDA HAKIZAI HARAMU-16


Nikiwa nimetokea kwenye mikutano, sasa nikawa natembea kuingia hotelini mwangu, kama kawaida nilipitia ufungu wangu wa chumba, wakati sasa naelekea kwenye eneo ambapo kuna chumba changu, ndio nikamuoana mdada mmoja kakaa mlengo wa chumba changu, nikajua labda ni muhudumu tu, nikatembea kwa tahadhari hadi pale mlangoni;

Wakati natembea kuelekea hapo mlangoni nikawa najiuliza maswali mengi, iweje huyo mtu akae mlangoni mwangu, na kwanini kule mapokezi hawakunipatia taarifa kuwa nina mgeni wangu ananisubiri, kama utaratibu wao ulivyo, machale yakanicheza..…yawezekana ni mtego…hapo nikasimama kidogo..

Alikuwa mdada, kajifunika kitu kama shuka nyeupe, imechakaa,..na kuna sehemu ya nyingine kwenye hiyo shuka ni kama imeungua,…na kuna alama za damu damu, hapo mwili ukazizima, damu zimetokea wapi,  na ule mkao ni wa masikitiko, mtu anakaa miguu inakuja karibu na kichwa, kainama hataki kuniangalia… inatia huruma kumuona, ..

Lakini kilichonivuta zaidi ni ..pembeni yake kulikuwa na mtoto mchanga, kalazwa, ikiashiria huyo mama ni mzazi, ….sasa kafuata nini, na ni nani huyo;-

*****************

Nilibaki nimeduwaa…

Nilipeleka macho yangu kumtizama yule mtoto…ni mtoto mchanga, anaweza akawa na umri wa chini ya mwezi mmoja hivi,..au  mwezi mmoja kamilizi, ni sizani ni zaidi ya hapo. Kichanga kile kilikuwa kimelala. Nikamgeukia huyo mzazi, nahisi atakuwa ni mama yake:

'Wewe ni nani, mbona upo hapa?'nikamuuliza nikimkagua vyema, kama nilivyosema nguo zake zilikuwa kuu kuu..zimechanika, na alama za damu na kuungua ungua!

 Na huyo mwanamke aliinua kichwa taratibu kama hana haraka, na kuniangalia, kwa mashaka, na yanyesha alikuwa hataki nimuone, ila yeye alitaka kuniona mimi sura yangu, au kuhakikisha jambo, maana aliinu uso taratibu lakini akaufunika kwa haraka.

Oh..nikahisi mshituka,..uso wa huyu mdada,…oh,… kafanya nini, au kafanywa nini....oh ..hapana;

 'Mbona uso wako upo hivyo,…… uliungua...?'nikajikuta namuuliza.

 Hakusema kitu, nikahisi kama analia...ni kweli analia, alitoa ile sauti ya kulia, moyo unakizizima kwa huruma.

 Kwa muda huo mfupi, mandhari ya hiyo hali , mtoto mchanga, haya huyo mama ana majeraha usoni, kama ya kuungua, vyote hivyo vikanifanya niingiwe na huruma, nikimuangalia kwa makini,  kuwa yawezekana ni mtego, kama ni mtego, nilitaka niwe makini sana,..

Kiuharaka haraka akili yangu ikanituma kuwa huyo mzazi atakuwa ni mkimbizi,! Lakini alifanya nini mpaka yamkute hayo madhila, huenda mumewe kauwawa, na kutokana na hali ya kivita akawa ametengena na familia yake..nikawa hivyo.

Jamani usiombe hiyo hali ya ukimbizi uwakute, watu wanapata shida, wanakimbia majumbani kwao kuishi maporini, kama kuna ambao yaliwakuta kidogo, kumbukeni mabomu ya gongo la mboto, ilikuwaje, sasa hayo ni ya muda mfupi, hawa wenzetu mwaka, wanataabika,..

Inafikia muda…wengine wanapoteana, mke na mume, wazazi na watoto, .. wanaacha nyumba zao na kukimbilia maporini, wanapokimbili napo hawajui usalama wao utakuwaje…

Yaani inafikia muda watu wanawakimbia wanadamu wenzao, …wanadamu wenzao wameshageuka kuwa wanyama,..watu wanauana ovyo, hawaogopi tena kumwaga damu ya wanadamu wenzao, …ni kwanini….watu wanaona ni heri wakutane na wanyama porini, kuliko kukutana na wanadamu wenzao, ndivyo ilivyowakuta wenzetu hawa,…vita sio kitu cha kuombea, na kama kuna watu wanafanya hayo, kwa masilahi yao, sijui mbele ya mungu watakuwa wapi,..

 Sasa kama huyu ni mkimbizi, sheria itanibana sana, hata kama nitataka kutumia ubinadamu , maana mtu kama huyu anahitajia msaada wa kibinadamu, japokuwa huko kambini wanahudumiwa lakini yawezekana kaona huko hapati huduma stahiki…hata hivyo, hakustahili kuja hapo, nashangaa alipitaje kule mapokezi,..na kwanini aje mlangoni kwangu hapo nikabakia na mashaka.

 Mimi mwenyewe kwenye mikutano, kama kiongozi, nililiongelea hilo, kuwaonya wakimbizi kuwa wafuate sheria, wakae makambini mwao niliwaambia wakitoka uraiani wakakamatwa watashitakiwa kwa kukiuka sheria,..

Na pia nilipowhutubia raia, niliwaonya wasije kuwachukua wakimbizi na kwenda nao majumbani, kwa tahadhari, kwani huwezi kujua, unaweza ukafanya hivyo kwa nia njema tu, kumbe huyo uliyemchukua akawa ni jambazi kutoka kwao akaja kukugeukia wewe au majirani.

 Nakumbuka niliwahi kuwatania, japokuwa sio utani hayo yanatendeka kimakosa, niliwaasa hasa wanaume,wasije kuingiwa na tamaa wakiwaona mabinti wazuri wakimbizi, wakawatamani,  wakawachukua na kwenda nao mahotelini, hairuhusiwi, hao wapo kambini kisheria...!

 Sasa huyu yupo hapa kafikaje, mlangoni mwangu tena mimi ni miongoni mwa viongozi? Au sio mkimbizi, na kama sio mkimbizi ni nani?

Alionekana ni mnzuri kasoro hayo mabaka mabaka kama ya kuungua usoni, hebu fikiria pamoja na kasoro hizo bado alionekana anavutia, ..mrembo! Sikuwa na wazo la kufikiria hivyo kwa muda huo, ila nataka kuelezea hali halisi!

 Niligeuza uso na kumuangalia yule mtoto mchanga, alikuwa kalala na sehemu kubwa ya uso imefunikwa. Kiafya ndivyo itakiwavyo, hata hivyo bado niliona udhaifu katika nguo  alizomfunika huyo mtoto…, lakini atafanyeje katika hali kama hiyo, ukimbizi ni umasikini. Nikawa na hamasa sana na yule mtoto. Na utafikiri mtoto huyo alitaka nimuone, ghafla akajinyosha, na vimkono vyake vikasukuma nguo alizofunikwa na kuacha uso wazi.

 Najua mtoto mchanga hatakiwi kuachwa wazi, kwa haraka nikataka kukimbilia kumfunika,..hata huyo mzazi nilimuona akijitahidi kutaka kufanya hivyo, na tukajikuta sote twaelekeza mikono yetu sehemu moja… lakini mimi kwa tahadhari, kama nilivyokuambia inaweza ikawa ni mtego, kwahiyo jicho moja kwa mama yake na jicho jingine nilimuangalia huyo mtoto, …na wakati nataka kuinama, sura ya huyo mtoto ikanivuta zaidi….

 Watoto wachanga huwa wanafanana sura zao, na wakati mwingine unaweza, usiweze kugundua kuwa mtoto huyo anafanana na nani, katika wazazi wao mpaka atimize umri fulani …

 Lakini sio kwa mtoto huyo, sura na hata ile mienendo, ya kujinyosha, kubenua mdomo, kwa haraka sana, nikamkumbuka mtoto wangu Soldier alipokuwa mchanga, wanafana, unajua kufanana, ….oh, nikajikuta natabasamu na bila kujielewa, nikasema;..

'Soldier..'nilijikuta nimetamka tu hivyo.

 Sijui kwanini,  kwani nilivyotamka hivyo tu, ilikuwa kama ishara kwa huyo binti, au sijui kwanini alishtuka na kusimama kwa haraka, usoni akaonekana mwingi wa mashaka, japokuwa alijitahidi kuficha uso wake,...

 'Soldaar...'alitamka hivyo, kwa lafudhi ya kigeni, sijui ni mtu wa wapi, akageuka kuangalia huku na kule, halafu akaniangalia mimi,..na bila kusema neno jingine…, akaanza kukimbia!

 Nilishangaa, mwanamke gani huyu anakimbia na kumuacha mtoto wake...tena mtoto mchanga!

 'Hey you....'nikasema, lakini ilikuwa kama nimemchochea, aliongeza speed, na mimi nikaamua kumkimbilia, lakini nilishachelewa, akawa keshatoka mlango wa eneo la vyumba, na kupinda kulia, kwahiyo nikawa simuoni, nilijitahidi kumkimbilia lakini sikumuona...

 Wazo likanijia, nirudi haraka nikamchukue huyo mtoto nije naye mapokezi, nikawakabidhi… maana hata nikiwaambia hao watu wa mapokezi bila ushahidi haitasaidia kitu, kwanza napoteza muda wangu wa kupumzika, maana mimi usiku kama tisa natakiwa kuwahi ndege ya kurudi kwetu.

 'Nitawapigia simu nikifika chumbani kwangu, waje wamchukue huyo mtoto mchanga, sitaki kujiingiza kwenye matatizo…’ nikasema na kuendelea kutembea, sasa nageuka kushoto, ili nielekee upande wa chumba changu, huku bado nikiendelea kujiongelekesha.

‘Sijawahi kuona, mzazi amkimbie mtoto wake,..huyu ni mwanamke wa ajabu kabisa,  kwanini anafanya hivyo...'nikasema, na kuanza kurudi kuelekea chumbani kwangu.

 Wakati nimefika ile kona ya kugeuka kuangalia kule usawa wa chumba changu, nikawa naangalia pale mtoto alipoachwa, sasa nikaona mtu kasimama, huyu ni mwaname, na mwanaume kweli kwani kapanda juu na pandikiza la mtu, hapo nikasimama kidogo,..hatari..!

Inawezekana ni mlinzi wa humu ndani…kama ni hivyo.., afadhali..atachukua jukumu la huyo mtoto, mimi sina muda, nahitajika kumpumzika….nikajipa moyo,..lakini bado nafsi inasita, natamani nigeuke nirudi mapokezi...

Nikakajipa moyo nikatembea kuelekea pale aliposimama huyo mtu, na nilipomkaribia nikasema;

'Hey, huyo mtoto kaachwa na mama mmoja..nahisi ni mama yake..sasa fanya mpango,…uwaarifu wahusika wa hotel wafuatilie, je wewe ni mfanyakazi wa humu ndani…?’nikasema na kuuliza.

 Yule jamaa akawa kasimama vile vile akiwa hafanyi lolote, mpaka nikamkaribia kabisa, na alipohisi nipo karibu yake, akanigeukia na kuniangalia,…

 Alikuwa kavaa mawani meusi makubwa, yameziba sehemu kubwa ya macho, kwa uvaaji huo,nikahisi kuna jambo, uvaaji wa namna hiyo una maana ya kuficha jambo, nikaingiwa na mashaka, nikahisi kuna hatari….au kuna jambo linakuja lisilo la kawaida!

‘Hey….’huyo jamaa akasema hivyo tu.

‘Hey,…Who are you…?’ nikamuuliza na yeye akageuza uso na kumtizama yule mtoto halafu akasema.

 'Mzee,  I have something for you, ..ni ujumbe wako...'akasema akichanganya Kiswahili na kiingereza.

'Ujumbe gani, unahusu huyu.mtoto au...mimi sijui lolote, unajua..'nikataka kuendelea kuongea, yeye akawa anatoa kitu kwenye mfuko wake wa koti,..hapo machale yakanicheza, nikajua sasa...inawezekana jamaa anataka kutoa bastola, ..

 Nikarudi nyuma kidogo, na mkono wangu ukaingia mfukoni, nikitaka kuishika simu yangu.
 Kwenye simu yangu nimeegesha namba tisa, inapiga namba ya hatar ,tulipewa namba ya hatari kuwa ikitokea lolote uipige namba hiyo, na watu wa usalama watafika haraka kukuokoa,lakini kabla mkono haujazama kwenye mfuko , jamaa akatoa karatasi….na sio bastola.

 'Mzee, don’t worry, mimi ni mjumbe tu,...'akasema na sasa akawa ananikabidhi ile karatasi.

'Ya nini...hii karatasi?'nikamuuliza.

'Imetoka kwa bosi...'akasema

'Bosi, who is the bos...?' nikamuuliza

'Ni mwanao..kama alivyosema nikuambia hivyo,....na mzee, bora umpigia mtaongea na yeye, mwenyewe...'akasema

'Mimi nina watoto wengi,...na na...'nikasema nikigeuka kumuangalia yule mtoto

'Mzee, wewe mpigie simu bosi,..., namba imo humo, nyuma ya hiyo karatasi...amesema uiangalia hiyo karatasi kwa makini....'akasema , sasa kiongea Kiswahili vizuri, nikajua ni wenzetu , …

‘No...subiri kwanza, niambia huyo mwanangu ni yupi..?’ nikauliza sasa nikianza kuwazia mbali.

‘Sijui...kwa vipi ni mwanao...unasikia mzee, usipoteze muda, mpigia mtaongea naye…’akasema.

'Na huyu mtoto...?'nikamuuliza huyo jamaa, lakini sasa hakunijibu akageuka na kuanza kuondoa.

'Hey..wewe...usiondoke kwanza....'nikamwambia lakini hakusimama kwa haraka akaanza kuondoka.

Hatari................

.
NB: Nimeona niandike kipande hiki kifupi kwa haraka , ili tu siku isipite bure, mvua imenifanya nichelewe kufika ofisini ambapo ninapata komputa ya kuadikia…tuwe pamoja na kamlisho la sehemu hii …


WAZO LA LEO: Tuwe wepezi kusaidia wenye uhitaji, wapo watu wanakabiliwa na matatizo makubwa tu, wazazi, watoto…masikini, wasiojiweza, na wengine yanawakuta matatizo na inafikia hatua wanahitaji msaada wa kibinadamu. Tusikimbilie kuwanyanyapaa kwanza hawa watu, tusaidie kwanza, halafu kama kuna la kuongea basi lifuate baadae, wengine mpaka wanafikia hatua hiyo wamehangaika sana…Mola anajua ni kwanini anatoa mitihani hiyo. Tumuombe mola wetu atupe moyo mwepesi wa kusaidiana.
Ni mimi: emu-three

No comments :