‘Huyu
ni nani…?’ mke wangu akauliza sasa akiwa kasimama, na macho yamemtoka
akimuangalia huyo mgeni aliyeingia…alijitahidi kusimama lakini alionekana hana
nguvu akawa anayumba yumba….nikataka kumshika lakini akaniashiria kwa mkono
nisimsogelee..
Mgeni
aliyeingia akawa ananiangalia mimi tu usoni, hakutaka hata kumuangalia huyo
anayemuuliza huyu ni nani. Na alipoona ile hali ya mle ndani, watu
wanamuangalia yeye tu, akasema;
‘M-m-mzee
nina shida na-na-na wewe…’akasema kwa kigugumizi.
Watu
wote mle ndani wakawa wanaendelea kumuangalia huyo mgeni aliyeingia, na mimi
kwa haraka nikasimama na kumshika mkono huyo kijana na kumwambia;
‘Twende
nje…’nikasema na yeye bila ubishi akanifuata …na tulipofika nje, yeye akawa wa
kwanza kuongea;
‘Umemfanya
nini mama yangu…?’ akauliza
‘Kwani
kuna nini kimetokea…?’ nikamuuliza
‘Niliambiwa
na baba kuwa ni kiwa na shida nije kukuona…wewe, natumai mliwahi kuongea naye,
au sio….’akasema sasa akiwa kashika kiuono, hakuelewa kuwa sisi sheria za jeshi
kushikiwa kiuno na mtoto mdogo kam huyu ni dharau…nikamwangalia tu…
‘Sasa
una shida gani…?’ nikamuuliza.
‘Kwanza
nimefika nyumbani, nimekuta mama kalewa,…’akasema
‘Kalewa…?’
nikamuuliza
‘Yaani
chakari…hajitambui…, anachoongea anakijua yeye mwenyewe…ananiogopesha sana mama
huwa halewagi kwanini anafanya hivyo…’ akatulia akiniangalia.
‘Mhh..kuna
tatizo…’nikasema
‘Na
mzee,..katika kuongea kwake, akawa anakutaja wewe na kukulaani, kuna nini
umemfanyia mama yangu…, nataka kujua hilo kwanza…’akasema akiniangalia kwa
upande upande.
‘Kanitaja
mimi kasema nini,kuwa mimi nimefanya nini..?’ nikamuuliza
‘Haeleweki…anaongea,
kilevi levi…..mimi sipendi, mimi unaniona nilivyo, sinwi, kabisa, wengine
wananihis kuwa ni muhuni, lakini mimi sina tabia hiyo, natumia akili
tu….’akasema
‘Sasa
sikiliza mimi nitakuja huko nyumbani, nitaongea na mama yako, kwa hivi sasa mke
wangu anaumwa, unaona…sasa niambie una shida gani nyingine?’ nikamuuliza.
‘Nikuulize
kwanza mzee, ni kwanini watu wanasema mimi nafanana na mtoto wako, ….’akasema
na ilikuwa kama mtu kanipiga rungu kichwani, nikamuangalia huyu kijana na
kusema
‘Nani
umemsikia akisema hivyo…?’ nikamuuliza
‘Na
huyo mtoto wako yupoje mbona mimi sijawahi kumuona..?’ Akaniuliza
‘Kwani
kuna ubaya, wewe kufanana na mtoto wangu, mbona mimi nafanana na baba yako…’nikasema
‘Mimi
sijui… kama wewe unafanana na baba yangu...hayo ni yenu,...,labda mlipokuwa wadogo mlikuwa munafanana, mimi sijui…ila kiukweli nina
mashaka, maneno aliyokuwa akiongea mama leo, yanaanza kunifungua akili,..nahisi kuna jambo, na…mimi
sipendi kuvumilia, kitu kikiniingia akilini nataka nipate jawabu lake
haraka…tena haraka kabla hali haikabadilika...'akashika kichwa.
'Mzee mimi nahisi kuna jambo..na usiponiambia wewe…, nitalitafuta na nitalijua tu.., na
nikilijua kwa jitihada zangu….nitafanya jambo mtashangaa…hamtaamini, mimi sio mtu wa kawaida mzee, muulize mama...’akasema.
‘Unataka
kujua nini sasa..?’ nikamuuliza nikiona ananipotezea muda wangu.
‘Kujua
ukweli, kama watu wanavyosema…’akasema
‘Wanasema
nini?’ nikamuuliza
‘Huenda
wewe ni baba yangu wa damu…’akasema.
‘Baba yako wa damu, una maana gani,...wewe mtoto wewe…una
akili kweli, unaamini maneno ya watu, watu wanaweza kusema maneno mengi, na
lengo lao ni kubomoa tu, hebu niondokee huko na upumbavu wako, una nini wewe …ina maana umewaamini watu wa mitaani, na unataka kumkana hata baba yako,au kwa vile hayupo duniani, eeh, .’nikasema.
‘Mimi
sijamkana baba yangu..na kama ningelisikia hivyo mapema ningelimuuliza baba yangu,..na hata kama angesema ni kweli, yeye ni baba yangu, angelibakia kuwa hivyo.. muhimu
ni kujua tu ukweli, na kama ukweli unafichwa, basi kuna jambo,..na kama kuna jambo
linafichwa,…hiyo ni dili…kwa watoto wa mjini…hiyo ni dili…unajua mzee, dili inalipa, dili ina gharama...’akasema akiangalia
pembeni.
‘Dili!! dili gani, ?…Unataka kusema nini hapo..?’ nikamuuliza nikimuangalia kwa mashaka.
‘Mimi sijui..muhimu ni kujua ukweli…akili yangu inahisi kuna jambo, kichwa hakitulii..naogopa nitabadilika, nitafanya kitu mbaya...hata nashangaa,kwanini imepoa hivi, mtu amchezee mama yangu..haijawahi kutokea, nahisi nimeanza kuwa na mabadiliko..sijui....’akasema akiwa anahangaika hangaika, kama kuna kitu kinamsumbua kichwani.
‘Unajue
uwe na akili ya kufikiri, ..hivi, kama hayo yangelikuwa ni ya ukweli
kwanini baba yako asikuambie, kwani alikuwa na tatizo gani…, achana na maneno
ya watu..rudi nyumbani ukakae na mama yako...’nikasema kwa ukali.
‘Ok…sawa,
nitaachana na hayo..lakini sasa..mimi nimekuja nina matatizo, nahitajia kuendelea
na masomo yangu, sina ada,…unaweza kunisaidia kwa hilo?’ akaniuliza sasa
akiniangalia usoni moja kwa moja.
‘Shilingi
ngapi..?’ nikauliza nikijua labda ni pesa ndogo tu.
‘Lakini
saba kwa sasa..’akasema
‘Laki
saba….ooh! mimi…sina pesa nyingi kiasi hicho si unajua maisha yetu yalivyo,
labda niuze kiwanja…’nikasema
‘Inabidi ukakiuze…maana kama sitapata hizo pesa, ..nikasoma, sitatulia, na nataka niondoke kabisa maeneo haya, nikaishi mjini..lakini ...kama sitaipata hiyo pesa kirahisi,...nitaipata kwa nguvu, ...mzee na wewe si unataka kuwa kiongozi au sio…?’akaniuliza.
‘Unataka
kusema nini..wewe mtoto, unasema nini, sijasikia vyema, uongozi na hayo
yanahusikanaje..?’ nikamuuliza
‘Mimi
ni mtoto wa mjini, masikio yangu yanasikia sana, na macho yangu yanaona
sana..akili yangu inafanya kazi usiku na mchana….baba alikuwa ni askari wa
silaha, mimi askari wa kalamu na karatasi, nimecheza sana na mitandao,
nimejifunza mengi…..kwahiyo, ujue ya leo sio ya jana,..umenielewa
mzee…?’akaniangalia kuonyesha kuwa ana dhamira ya kweli.
‘Sikuelewi…nahisi wewe una
matatizo, mbona baba yako hakuniambia, upoje wewe…’nikasema sasa nikiwa nimekasirika.
‘Mzee….,nikuambie kitu siasa ni kitu rahisi ukiwa mjanja,..na wanaotaka kupanda juu, wanahitaji sapoti,
kitu cha kushikilia, unajua..., na wengine nao wanatamani kupanda huko huko, ukumbuke
mti ni mmoja, wengine wanaweza kukuvuta mguu, hasa wakiona udhaifu wako au sio…..sasa
mimi nimesikia, na nipo mbioni kuona ukweli, kuna kitu
nimekisikia…nikikithibitisha, mzee, nitakifanyia kazi, kama hatutaelewana,utaniona mbaya, ...'akasema
'Mbona mimi sikuelewi...unataka kusema nini..?' nikamuuliza
'Mzee mimi ninachotaka ni ada..laki saba tu, …’akatulia
akiniangalia machoni.
Nilimuangalia
huyu mtoto bila kummaliza, haya..anayoyaongea nimeyaona kwenye sinema, nimesoma
kwenye vitabu,…siamini kuwa huku kwetu kuna watu wenye tabia kama hizo…na huyu
ana asili ya damu yangu, japokuwa nilishamtoa kwenye damu yangu kwa ahadi..kama kweli ni damu yangu…hata hivyo hiyo tabia ni aya ajabu kwangu, sisi hatuna hulka kama hizi,..hapana, hii sio
damu yangu, haiwezekani…
‘Sikiliza
wewe mtoto, unanifahamu kuwa mimi ni nani…nitakuchapa viboko na ukubwa wako huo ..siogopi kukuzaba vibao..na ukileta ubishi tutapigana ngumi...msijione mumekuwa mkafiria mna nguvu sana...baba yako alinikabidhi wewe kama mwanangu, sasa usione nimezeeka hivi, napiga,
na nikipiga kweli..….’nikasema nikimkodolea macho ya ukali.
‘Baba,….usije
ukaja kujutia baadae haya ninayokuambia, kwani mimi nitakosa nini, nikiusema huo ukweli, watu wakaujua jinsi ulivyo…mama kaanza kusema ovyo…na nimeunganisha
maneno yake, nimegundua jambo, wewe una kitu na mama, na huenda kilianzia huko kwa baba….ni heri isiwe hivyo,
lakini ikiwa ni hivyo, mzee, hutaamini, mzee kama hatutaelewana utakuja kuniona mtu wa ajabu sana,…’akaniangalia halafu akaangalia
pembeni.
‘Kitu
gani mimi na mama yako wewe, hebu acha huo uhuni, mtoto mdogo kama wewe unachunguza
chunguza mambo ya wakubwa, umeyapatia wapi hayo maneno…unajua mimi na baba yako
tulikuwaje..sikiliza hayo unayotaka kuyafanya sisi ndio askari wa kuyakomesha,
sasa jifanya unajua uone utakachokipata…unataka kuwa nani wewe…huo ni
ujambazi..unalifahamu hilo..?’ nikauliza
‘Ohh..ujambazi,
au sio…mimi siibi, sivunji nyumba za watu, situmii silaha, natumia akili yangu,
macho na masikio….sasa, kama unataka kunipima, ngoja niifanay kazi yangu..bado
natafuta ukweli, nikija kuugundua,…sitojali mzee…unisikie, jambo muhimu,…
sitaki mama yangu apate shida, nimejua wewe ndiye shida ya mama…sasa nilikuja
mara moja kuona kama nitapata ada,…nakuuliza tena mzee, utanipa ada au
hunipi….?’ Akauliza
‘Sina
pesa nyingi hivyo, unafikiri mimi ni tajiri…’nikasema
‘Una
shilingi ngapi .?’ akaniuliza akiniangalia machoni.
‘Sasa
hivi sina pesa, subiria niuze mazao…’nikasema
‘Mzee,
nakushauri, uza kiwanja,..nataka ada kwa haraka sana…’akasema kama anatoa amri
‘Siwezi
kuuza kiwanja…kiwanja ni mali ya familia, …ni mpaka tukae na
familia,tujadiliane , sio kitu rahisi kihivyo nitaongea na mama yako kama
anaweza kuuza sehemu yake ya ardhi..mna maeneo ya kule chini, , …’nikasema
‘Ongea
naye..lakini mimi nikirudi tena nataka pesa kutoka kwako sio kwa mama,
vinginevyo, hutaamini nitakayoyafanya…bado nakusanya ‘data’….mzee mimi ni mtoto
wa mjini, kwanza nataka kujua mimi na wewe tupoje, halafu wewe na mama
mpoje..unanisikia,…nimemuona na mke wako ananiangalia kwa mshangao….ana hamu ya
kujua mengi au sio…’akasema akitabasamu kwa dharau.
‘Kujua
nini…?’ nikauliza.
Mzee…ngoja
nikuambie kitu kimoja kunihusu mimi…siku muulize mama atakuambia…akakaa mkao wa
kutaka kunihadithia jambo, na mimi nikatulia kumsikilia..alikuwa akinipotezea
muda, lakini sikuwa na jinsi…
‘Ni
hivi mzee…watu wanasema mimi ni hatari sana nikibadilika….mimi sijui, maana huwa wananisimuliaga tu, wakati mwingine siamini na sipendi initokee
lakini sijui nina tatizo gani....
Mimi
ni adui kwa yoyote yule anayemliza mama yangu, huyo kwangu ni adui, haijalishi
ni nani, nikiwa mdogo, nilipambana na baba…nilikuwa kama paka, wanavyosema
wao,…, walihisi nimechanganyikiwa, kisa baba alimzaba mama kibao mbele yangu,
mama akawa analia.....baba ilibidi akimbie,...
Wakati
nikiwa mdogo, shuleni kuna siku walinikorofisha, alikuwa ni mwalimu mmoja
alipenda sana kutuchapa, na katika kuniadhibu, akaongea jambo la kumkashfu mama
yangu….nasikia walivyonisimulia, nilitutumuka,..na nilichokifanya siku hiyo,
niliacha historia…
Wanasema
nilibadilika, na kuanza kumpiga huyo mwalimu na kila mwalimu aliyekuja
kusaidia,niliweza kumuinua mnzima mnzima na kumbamiza jinni kama gunia…walikimbia
walimu wote na wanafunzi….
Nikiwa
chuoni, ilitokea hivyo hivyo mpaka wakaita polisi, na hata,polisi walipokuja
hawakuweza kunizuia niliwarushia mbali, unajua ni kitu cha ajabu wanasema
namrusha mtu kama mpira…
Ni
hali inayoniingia mwilini na kuwa mtu tofauti na mimi, sijijui, na hata hali
hiyo ikiisha siwezi kukumuka kama nilifanya hivyo..na hakuna anayeweza
kunidhiti,..ndivyo wanavyoniambia…
Na ili
hali hiyo iishe wanasema ni mpaka huyo mtu atimiza takwa langu, na aliyenikosea
ajikate mahali ajitoe damu niione,....
Sijui
kwann nimekuambia hayo,...
Mimi
nilimsikiliza kama mtu anayetoa hadithi za kufikirika, nikatabasamu na kusema;
‘Kama
una mashetani mimi najua jinsi gani ya kukabiliana nayo, usijaribu kunitolea
vitisho visivyo na maana mimi ni askari, nimepambana vita..kuna kitu kinaua
kama risasi…sasa mimi nilikabiliana na risasi ..kwahiyo usinitishe kijana,
unasikia..’nikamwambia
‘Hahaha
mzee hapo patamu, hapoo eeh, napenda namna hiyo…, unanipa changamoto, sawa mzee, kamliwaze mkeo,
maana siku nikija inabidi anifahamu rasmi kuwa mimi ni nani, si hupendi
anifahamu , sasa jitahidi asinifahamu maana namshukuru mungu, kanipa macho,
akili na masikio…kwangu hivyo ni hazina kubwa sana….sifanyi makosa ….utaona…’akasema,
halafu akaweka mikono mbele kama muombaji na kusema kwa sauti ya unyenyekevu..
‘Lakini
mzee mimi sitaki shida, …sipendi mabaya yakukute, …tumalizane tu…, si unajua
cha kufanya, ada tu…basi usisahau, samahani mzee kwa usumbufu, kwaheri,
usisahau….’akageuka na kuanza kuondoka huku anaimba imba wimbo...
Nilibakia
nimeishiwa nguvu….
‘Sasa
hili ni tatizo…’Mzee mzima alishika kichwa, akatulia kwa muda akiwaza visivyowazika, akatamani aje kufanya jambo baya....na ghafla, akashtuka mtu anamshika bega,
..akajua ni yule kijana karudi, akasimama kwa hasira, ...
'Nimekuambia....' akatulia, na kunywea alipomuona mtu aliyemsimamia mbele yake.
NB:Niendelee....
WAZO
LA LEO: Usipoziba ufa utakuja kujenga
ukuta kwa gharama kubwa sana, mtoto umleavyo ndivyo akuavyo…tuwe makini
kuyakabili matatizo yetu yakiwa machanga, kwa kuelezana, kushauriana,
kusaidiana..kwani hatari ikianza kutokea huenda ikaharibu yote yale mliyokuwa
mumeyafanya…
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment