Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, March 6, 2017

KITANDA HAKIZAI HARAMU-10


‘Rafiki yangu mimi ninaumwa sana, sijui kama nitapona..’ akasema mgonjwa.

‘Utapona tu rafiki yangu kuumwa sio kufa..jipe moyo wewe ni askari bwana, kufa ni kufa tu…’akamwambia.

‘Unajua rafiki yangu, nilikuwa nimedharau sana tatizo hili….nilijua ni maumivu tu ya nyonga, lakini kumbe tatizo hilo limekwenda na kuathiri uti wa mgongo, hapa nilipo kiuno chote hakifanyi kazi…ulishawahi kuteguka nyonga, basi hiyo adhabu ndio inanipata mimi mara kwa mara...’akasema.
‘Pole sana, naelewa..lakini utapona tu…’nikampa matumaini.

‘Sawa, ni kweli imani yangu ni hiyo, nipone…’akasema

‘Oh, unajua wewe ni dharau zako nilikuambia mapema kamuone dakitari bingwa, ukadharau sasa hali imefikia hapo ulipo, lakini usikate tamaa rafiki yangu, utapona tu…’akamwambia rafiki yake, kipindi hicho bado wapo kazini.

 Miezi ikapita, na siku moja, nikaitwa na rafiki yangu huyo, akiwa kitandani, huwa alikuwa anapona anendelea, hali inarudia tena anakuwa ni wa kitandani, siku aliponiita ndio anakaweza kuniambi jambo moja ambalo lilinifanya niwe na wakati mgumu…ndio linanitesa hadi leo, sikutakiwa kuliongea, hadi kaburini, lakini nitafanyaje kwa hali kama hii…’akasema.

‘Rafiki yangu, hizi kazi zetu bwana, ….niliumia nikiwa vitani, lakini nani ataelewa,..ukiumia ni unaambiwa ni uzembe wako…sasa nilichokuitia hapa ni kuwa, nimeenda kupima, kipimo kinachoaminika kabisa…’ akasema.

‘Ehe, umeambiwaje?’ akamuuliza

‘Uti wa mgongo umeathirika sana, wamenipa matumaini,…nitapona, nitapona… lakini muhimu walichonishauri ni kuwa niachane na kazi ngumu,…na sana sana kama inawezekana nichana na hii kazi yetu,… sasa sina jinsi inabidi niandike barua ya kustaafu kabla ya muda wangu…’akasema.

‘Oh..unajua awali nikushauri usifanye hivyo, lakini kwa sasa kama hali iimefikia hapo basi kapumzike tu….najua umuhimu wa kazi , lakini afya yako ni bora kwanza,mambo mengine tutaendelea kusaidiana usijali rafiki yangu…’nikamwambia.

‘Sawa ila kuna jambo muhimu nataka kukuomba,..unielewe na ulikubali, maana sina jinsi na ..nimefikiria sana nikaona wewe peke yake ndiye unaweza kunisaidia…’akasema.

‘Rafiki yangu hivi mimi nikiwa na tatizo nahitaji kukuomba, unanieleza tu, tunasaidiana, uniamini mimi, hakuna jambo linaloweza kushikindikana kati yetu wawili, tumesaidiana mangapi, nashukuru kuwa hata wake zetu ni kama tulivyo, wameivana hakuna mpaka watu wanatuonea wivu…niambie ni tatizo gani…?’ nikamuuliza.

‘Oh…, rafiki unaweza kuniona mimi ni mtu wa ajabu sana…, sijui kama nitakuwa nimekosea, lakini hapana, mimi naona tufanye hivyo, nakuomba sana, unisaidie hili bila kusita,ni amri kama amri za kijeshi lakini, lina masharti muhimu sana, unielewe na uyazingatie…..’akasema.

‘Wewe bwana, wewe…wewe sema, toa amri mimi nitatekeleza, kwasababu kwanza kwa kuandikishwa jeshini ulinitangulia, japokuwa tuna cheo sawa, lakini wewe ni senior kwangu lazima nikutii, afande, toa amri nitatii…’nikaongea tukiwa tunatabasamu tu, lkn rafiki yangu hakuonekana mwenye furaha kama ilivyokuwa siku nyingine.

‘Rafiki yangu kutokana na tatizo hili sitawezi kuzaa tena…’akasema hapo nilikuwa na chupa ya maji ikaniponyoka.

‘Unasema nini…?’ nikamuuliza

‘Hayo ni maneno ya dakitari bingwa, …, na hakuna jinsi hata kama nitapona, ..ndivyo alivyoniambia huyo docta bingwa, umenielewa, ….’akasema

‘Hapana,…nawaamini sana madakitari lakini, kuzaa ni majaliwa ya mungu..utapona utazaa tu..muhimu kwanza ni wewe kupona, mengina yatafuta, tutahangaika pamoja usijali hilo kabisa….’nikamwambia.

‘Nisikilize kwa makini, hili ni siri kati yangu mimi na wewe, sitaki hata shemeji yako afahamu..unasikia vyema, nataka tufanye jambo, angalau na mimi nipate mrithi…’akasema.

‘Jambo gani…?’ nikamuuliza sasa kwa mashaka, moyoni nilihisi labda anataka mkewe akapandikizwe mbegu au kitu kama hicho, sikuwa nimewazia jambo kama hilo.

 Ukumbuke wawili hawa walishibana sana, na ungeliwaona ungelifikiria ni mapacha,…kwanza mungu kawajalia wanafanana ...utafikiri ndugu lakini sio ndugu wa baba na mama mmoja, na wakiwemo kazini hadi nyumbani wapo wawili…,na usingeliwaambia kitu cha kuwatenganisha, watakuumbua. Na mmoja wapo akiumwa, inakuwa kama na mwenzake anaumwa, asiyeumwa anakuwa hana raha utafikiri ni yeye anaumwa.

 Basi kukatokea maelezo marefu tu.....

‘Nimekusikia rafiki yangu,….lakini ujue hilo ni gumu sana, kwanza kwa shemeji , pili kwa mke wangu, huoni tunakufuru, ni dhambi kubwa sana…’nikamwambia, lakini akazidi kunisihi sana,..

'Kitanda hakizai haramu bwana...usiniangushe..'akasema lakini kwa sauti ya huzuni.

Ukumbuke kipindi hicho damu inachemka, na unajua tena sisi maaskari tukiwa jeshini ni kama wanafunzi tu..watu wa mazoezi kwahiyo uimara wetu wa viwili wili unakua ni chachizo.... Nililichukulia kirahisi tu, japokuwa sikupenda, japokuwa, nilielewa ni nini maana ya ndoa nilijua nima kosa, lakini urafiki wetu niliuweka mbele,…si tunasaidiana, yeye na mimi ni rafiki, lakini tatizo ni jinsi gani ya kulifanya hilo jambo.

‘Sikiliza kama nilivyokuambia hilo ni kati yangu, mimi na wewe, asifahamu yoyote yule, hasa shemeji, na hata mke wangu hatafahamu,…..jinsi gani ya kufanya niachie mimi, nitakuja kukuambia….’tukamalizana hapo

***********

Siku baadaye rafiki yangu akanitumia ujumbe nikiwa kwenye lindo,kuwa nikitoka huko nipitia moja kwa moja nyumbani kwake,..tulikuwa maeneo ya kambini, na kuna nyumba zimejengwa familia kwa familia, kutokana na kuumwa kwa rafiki yangu yeye akahamishiwa sehemu tofauti, ni utaratibu tu wa kawaida, lakini wake zetu, wanakuwa pamoja karibu mchana kutwa, …

Kwahiyo hiyo shughuli aliyonialika ilikuwa kwenye eneo lake…na kwa ujumla muda huo alikuwa hajambo anavuta vuta muda kusikilizia barua yake ya kustaafu kwasababu ya afya…, anafanya shughuli ndogo ndogo tu hapo kazini…barua ikajibiwa kuwa anaweza kuondoka, kwahiyo aliamua afanye shughuli ya kuwaaga marafiki zake..

Aliniambia mapema tu, lakini kutokana na kutingwa na kazi, nikawa sipo kwenye kuitayarisha hiyo shughuli..basi nilipotoka lindoni, nikaelekea nyumbani kwake, ..watu walikunywa, wanaokunywa, ..baadae wakatawanyika..wakimpa mkono wa kwaheri kuelekea uraiani…

‘Rafiki yangu njoo, lile jambo linatafanyika leo…’akaniambia watu wakiwa wameshaondoka, hata mke wangu alishaondoka.

‘Jambo gani..?’ nikamuuliza.

‘Aaah, bwana, ingia huko ndani shemeji yako kalewa chakari, hajitambui..niliamua kumlewesha leo sasa kama nilivyokuambia, kila kitu kipo tayari,..fanya ufanyavyo, mimi ninatoka, usiniangushe,..’akasema akiwa anatoa machozi.

‘Lakini rafiki yangu…’nikajitetea

‘Nielewe, nalia, sio napenda, lakini sitaki kumuacha mke wangu bila kumzalia mtoto, nampenda sana mke wangu, na nilimuahidi ni lazima tutapata mtoto, sijamueleza kuwa siwezi kuzaa…nataka unielewe hilo , hilo ni kati yangu mimi na wewe….nakuomba tafadhali, usipoteze muda, jitahidi, na mungu atatusaidia…oh…hakikisha shemeji yako hakufahmu taa zimezimwa...’akaondoka huku anasikitika.

Nilijiuliza sana, na kabla sijatulia kulifikiria hilo jambo mara sauti ikaita kutoka ndani

‘Wewe mume wangu mbona unaniacha hivi..njoo, bwana….’ilikuwa sauti ya shemeji, bila ajizi mimi nikaingia ndani, namkuta oh…kama alivyozaliwa…hebu fikiria na ujana wangu, damu inachemka, na jeshini usiniambie kitu,……siwezi kuelezea hapo zaidi, lakini ..sitaweza kuisahau hiyo siku imenitesa.lakini ungelifanyaje.., kweli pombeni ni shetani.

Masiku yakapita na rafiki yangu alishaondoka yupo kijijini, tunawasiliana , tunajuana hali,..tunasaidiana, na miaka ikapita,.. lakini hatukuwahi kuliongelea tena hilo jambo,kama alivyoniagiza tuwe hivyo…na hayo yalishapita, na kuyasahau kabisa. Na mimi ikafikia muda wangu wa kustaafu,…ilikuwa tustaafu naye, lakini yeye aliharakisha kutokana na afya yake.

Na mimi nikarudi kijijini,…yeye sasa alikuwa kijijini cha pili, ila hapo kijijini , yaani hapa,  yeye pia alikuwa na nyumba na makazi yake, tulikuwa hatuachani, hata makazi, maeneo, mashamba tukinunua tunanunua pamoja..kwahiyo huwa anafika na kuondoka, na mara nyingi hafiki na mkewe,..anasema mkewe ana kazi nyingi, kukawa na kutengena kwa namna fulani,.

Kuna kipindi mke wangu anakwenda kusalimia, hata mimi mwenyewe…lakini uone ilivyo ajabu kila tukifika huko tunawakuta wapo wao wawili, yeye na mkewe, wazazi wake wanakuwa hawapo kwasababu mbali mbali..na mtoto anakuwa sheleni, alikuwa anasoema mbali, analala huko huko, tulishajua kuwa wamejaliwa kupata mtoto,….

 ‘Rafiki yangu nitahamia huku, ila mtoto atabakia na bibi yake…’akaniambia siku moja alipokuja kunitembea akikagua nyumba yake, ambayo aliipangisha.

‘Mtoto..wako sijawahi kumuona...ni ajabu kabisa miaka yote hii ’ nikamwambia

‘Ndio…mara nyingi wanakuwa na bibi yao, si unajua tena… namshukuru sana mungu, angalau nimepata mrithi, ni dume kweli la nguvu…’akasema.

‘Si nilikuambia, usiamini madocta,..unaona sasa..’nikasema na kiukweli wakati tunaongea hayo sikuwa nafahamu kuwa huyo mtoto ni yule wa mipango, nilijua kabisa ni mtoto wake,..muda ukafika wakahamia, tukawa tunaishi pamoja, tunasaidiana, lakini huyo mtoto hakuwahi kufika huku, hadi amekuwa kijana mkubwa tu..

Siku zikapita, rafiki yangu akawa na hali mbaya,..tunashukuru kuwa aliweza kuishi muda huo wote tofauti na tulivyodhania,…tokea astaafu, miaka kumi nane ikawa imepita..hebu fikiria, hatukwahi kumuona huyo mtoto wao…jamaa kuna muda anateseka na maradhi, lakini afya haikuwa mbaya kama kipindi hicho, alizidiwa kiasi kwamba tukajua safari imewadia, na siku hiyo yupo kitandani, anagulia maumivu nipo naye,…mara akaja kijana mmoja.

‘Shikamoo, baba, unaendeleaje..?’ kijana akamsalimia baba yake.

‘Sijambo kiasi, aheri umefika, ….nilijua hutaniwahi, leo umenyoa mindevu yako,...hahaha, na bibi yako kakuruhusu ajabu kabisa…’akasema.

‘Kwanini baba unasema hivyo mara nyingi unaumwa kama hivi unakuja unapona, usikate tamaa baba..’akasema mwanae.

‘Mwanangu, wewe ndiye mrithi wangu…na huyu hapa, ni yule baba niliyekuambia, mimi sina ndugu wengine,ndugu wengine walishafariki, aliyebakia ni huyu peke yake na huyu ni ndugu tu wa kufikia, lakini ni zaidi ya ndugu, huyu ni baba yako muheshimu sana..’akamwambia mwanae

‘Sawa baba shikamoo baba…’akanisalimia na hapo akaniangalia usoni, unajua,..nilishtuka,…hapo nilikuwa kama ninamuangalia mwanangu soldier, nilishangaa nikasema hivi…

‘Soldier, umefuata nini huuku..?’ nikauliza kwa mshangao.


NB: Haya siri imekuwa sio siri tena, itakuwaje..


WAZO LA LEO: Urafiki wa kweli unaonekana kipindi cha dhiki na shida. Inashangaza kweli pale mmoja anapokutwa na mitihani ya maradhi au umasikini, wengi humkimbia…lakini akiwa anajiweza watu hujaa tele. Jamani mpaji ni mungu, leo kwa huyu kesho inaweza kuwa kwako, onyesheni upendo wa dhati kipindi cha shida. Tumuombe mungu atujali kwa hili tupendani kwa dhati hata ikiwa kipindi cha shida.
Ni mimi: emu-three

No comments :