Bila ajizi japo kwa kusita Soldier akamchukua yule mtoto kutoka
kwa yaya, alimtambua huyo binti kuwa ni yaya, kwa vile ndiye aliyekuwa muda
mwingi kambeba huyo mtoto, na mkewe kuna muda alitamka maneno yakuashiria hivyo
kuwa huyo ni yaya, lakini alikuwa hajamtambusliha rasmi,..
‘Ni yaya…yaya wa mtoto, …mtoto wetu…’akajikuta akisema hivyo
huku akimuangalia mtoto usoni.
Mtoto mnzuri mwenye afya tu…
Kila alivyozidi kumkagua huyo mtoto alikuwa akihisi mwili
ukimcheza, na hali hiyo ilimuanza pale mtoto alipofika mikononi mwake,..alishangaa…na
kilichomshangaza zaidi ni …ni machozi, yeye.ni kawaida yake hasira zikimzidi sana
hutoa machozi, na akitoa machozi kama ni adui yake atafute sehemu ya
kujificha..na pia....hata furaha, akiwa na furaha sana huwa anajikuta akitoa
machozi, sasa hapo hata yeye mwenyewe hakufahamu kuwa machozi hayo ni ya furaha
au hasira.
Akawa kampakata yule mtoto vizuri, huku akimkagua,..sura…anafanana
na nani huyu mtoto,....labda mama yake,..hakuweza kulithibitisha hilo, ndio
mkewe anamfahamu sura yake,..lakini hakuweza kumfananisha na huyo mtoto…
Kitu kilichompa shikinikizo la damu ni….umri,…mmh, hata mtoto
mdogo atatambua tu kuwa huyo mtoto ni kati ya miezi mitatu, au mitano…sasa hii
ina maana gani,…
‘Huyu mtoto ana umri gani…?’ akajikuta anauliza, lakini hakuna
aliyekuwa karibu yake kumsikiliza,…akawa anajizuia, maana alihisi machozi
yakimjia kwa kasi..
‘Whats the problems…’akajiuliza mwenyewe
Wakati huo mtoto yupo mikononi mwake, akiendelea kumkagua,..mkewe
na yaya, pamoja na dereva walikuwa kwenye shughulika za kuingiza mizigo kwenye
gari....yeye hakujali tena, hakujali tena kuwa kuna zawadi nyingi tu kaja nazo
na alitaka ahakikishe zimefika kwa walengwa hasa mkewe..kwa muda huo,..alichojali
ni kuhusu huyu mtoto..
‘Mume wangu kuna mzigo mwingine, naona yote iliyoandikwa jina
lako imeingia kwenye gari..?’ ilikuwa sauti ya mkewe
‘Ok, hakuna mingine ni hiyo tu,,…’akasema sasa akizungusha
kichwa kukagua lile eneo alilokuwa ameweka mizigo yake, na alipona hakuna mzigo
uliobakia, akahema kwa nguvu.
‘Haya twendeni…’mkewe akasema sasa akitaka kumpokea mumewe mtoto
lakini mumewe akawa anatembea kuelekea kwenye garii, kama vila hamuoni, huku
akiendelea kumkagua yule mtoto machoni, mtoto alikuwa kalala…kafumba macho.
Wakati wanataka kuliingia
kwenye gari, yule yaya, akataka kumchukua mtoto, yeye akasema;
‘No…hapana acha nikae naye…’akasema na kweli akaingia kiti cha mbele
na kumweka mtoto vizuri mapajani kwake. Hapo sasa kuna muda akashindwa
kujizuia, akawa analia, anatikisika mwili mnzima akijizuia hiyo hali
isionekane.. …mpaka dereva akashangaa, …na bahati nzuri tendo hilo mkewe na Yaya
hawakuliona maana walikuwa kiti cha nyuma wakihangaika kupanga vitu vizuri, …
‘Vipi bro, ni kawaida, mtu ukitoka vitani salama.. huwezi amini ,
ni jambo la kushukuru sana…, na naona una bahati sana kuwa umerudi na una
zawadi ya mtoto..’akasema dereva
‘Mhh…’akaguna.
‘Huko ulikaa muda gani vile…?’ akauliza huyo dereva
‘Miaka mitatu….’akasema
‘Miaka mitatu!, Mingi sana….Oh, kwahiyo ulikuwa unarudi rudi
hivi…na bahati, ukajaliwa kutengeneza mtoto,…maana huyo mtoto ni miezi mitatu
au mine hivi au sio…, ulikuwa mjanja sana, hukutaka mkewe abakie mwenyewe,
lakini uliwezaje kurudi rudi, kwani mlikuwa nchi gani..?’ yalikuwa maswali ya
dereva ambayo hakutaka kuyasikia.
‘Usijali nitakuja kuwasimulia kila kitu, lakini sio sasa,…endesha
gari….’akasema kwa sauti iliyomfanya dereva ashtuke, na sijui ni kama vile
dereva alielewa au vipi…akatulia kimia akiendesha gari….mara huyo dereva akaanza
kuimba huku anaendesha gari…
‘Kitanda hakizai haramu, hakizai haramu, pupupupu..titititi
dindidi…kitanda hakizai haramu, haramu
haramu, …’
‘Wimbi gani tena huo dereva…?’ aliyeuliza swali hilo ni mke mtu.
‘Si unajua mambo zangu, nafanya mambo mengi, ilimradi riziki
iende kinywani, wakati mwingine nashughulika pia, na eeeh, kuimba, nina kundi
la ngoma za kienyeji,…sasa huo wimbo wa ‘kitanda hakizai haramu, ndio upo
kwenye chati, na jana ulishika namba moja kwenye harusi ya jamaa mmoja,
tukianza kuuimba, wakina mama wanasimama..…’akasema.
Kitanda hakizai haramu eeh, kitanda hakizai
haramu..tinditindi..tititi…..’akawa anaimba huku akachezacheza kwenye kiti
Kiukweli, huo wimbo na maneno yake ilikuwa
kama kitu kimemgonga Soldier kichwani, ni kama vile alizinduliwa kutoka kwenye
dimbwi la ubumbuwazi, mnzito, sasa akaanza kuelewa, …ina maana gani hii, ina maana mke…kani…kafa..kani…ka,
..haiwezekani, sio mke wake,…
‘Hawezi kunifanyia hivyo, hapana…’akajikuta katoa sauti, na
dereva akamgeukia na kusema;
‘Ni kweli…..’akasema dereva
‘Ni kweli nini..?’ akauliza Soldier
‘Ninaimba kwenye kikundi cha ngoma…waulize hata familia yako
wananifahamu…’akasema dereva.
Hapo Soldier, akageuka nyuma kuwaangalia mkewe na yaya, wote
walikuwa wakitabasamu kwa furaha hakuna aliyeonyesha mashaka yoyote…, hasa
mkewe, mkewe alikuwa na furaha mpaka unaihisi.
‘Mume wangu samahani sijakutambulisha,…huyu ni yaya wetu…nilimchukua
maalumu kwa ajili ya mtoto….’akasema mkewe.
‘Mhh…’jamaaa akaguna tu.
‘Utampenda sana, ni mchapakazi, anajua kulea, usafi…yaani
nashukuru mungu, nina imani kuwa mtoto wetu yupo kwenye mikono salama…’akasema
mkewe
‘Sawa kabisa…ni vizuri…’jamaa akajibu.
‘Anaitwa Switie…sijui kwanini walimchagulia jina hilo…’akasema
mkewe
‘Labda ni mtamu sana…’akasema dereva na huyo yaya, akasema;
‘Mama yangu aliniambia kuwa jina hilo ni kwasababu kipindi akiwa
mja mnzito alikuwa akipenda sana vitu vitamu, ndio akapenda kuniita jina hilo,
kutokana na docta mzungu aliyemzalisha, alimuambia aniite jina hilo….’akasema.
‘Kitanda hakizai haramu eeh, kitanda hakizai haramueeh…tindi
tindi tindi….’dereva akawa anaimba wimbo wake.
‘Sitaki huo wimbo..’ilikuwa sauti ya Soldier, na jinsi alivyotoa
sauti ilimfanya dereva ageuze kichwa
kumuangalia huyo jamaaa kwa mashaka, halafu akatulia na baadaye akasema;
‘Sawa bosi,…sawa afande…’akasema akigeuza geuza kichwa
kumuangalia Soldier, na huyu askari sasa alikuwa kajiegemeza kichwa kwenye kiti
akiwa kazama kwenye mawazo…
***********
Huyu mtoto ni damu yangu
kweli…miezi mitatu..haiwezekani,…kama sio damu yangu, … ni nani kampa mimba mke
wangu,…
Hapo akainua kichwa na kugeuka kumuangalia mkewe, na mkewe kwa
muda huo walikuwa wakiongea kitu na yaya, wkawa wanacheka,…
‘Huyo mtu…kichwa chake ni halali yangu…tutkula sahani moja, mimi
na yeye…., ile hasira ya kumkosa adui yangu mmoja vitani itarudia kwake,
alikumbuka jinsi alivyomkosa adui yake kwenye vita, .ilikuwa ni ambush, waliianda vyema kabisa, wakawazingira
maadui,…lakini kiongozi wao aliweza kutoroka, sasa hiyo hali ya kumkosa
kiongozi wo ilimuuma, sana, akasema atafanya juu chini mpaka ampate huyo
kiongozi wao..wa maadui.., lakini mpaka wanamaliza huo mkataba hakuweza
kumpata.
‘Baba wa huyu mtoto atalipa….’akajikuta akisema kwa sauti, japo
ni ndogo, lakini dereva alisikia,
‘Baba wa mtoto, nani huyo, kwani wewe sio baba wa huyu mtoto…?’
akauliza huyo dereva kwa sauti kama ya utani!
‘Nani kakumbia hivyo…?’ askari akauliza akiwa kakunja uso, na
dereva alipokutana na hiyo sura, alitikisika, karibu ayumbishe gari
‘Oh..samahani nimesikia tu, ukisema ;’baba wa huyu mtoto atalipa…’akasema
dereva.
‘Sawa, wewe endesha gari, …’akasema Soldier, na dereva akawa
anaendesha gari kimia, na mara kwa mara anageuka kumuangalia huyo askari, na
muda fulani wakakutanisha uso, kila mmoja akimuangalia mwenzake,…, na sijui
ilikuwaje, Soldier akahisi jambo,.. kuna kitu kikamvuta, sura ya huyo
dereva,..mbona..hapo kwa kuhakikasha akamtizama mtoto, kwa muda huo kitoto
kilikuwa kimeamuka kimefungua macho…
‘Oh….’akaguna, na muda ule dereva alikuwa ameshafungua mlango
kutoka nje ya gari…
‘Tumefika jamani….’ilikuwa sauti ya mkewe, na ikawa sasa ni
shughuli ya kushusha mizigo na kuingiza mizigo ndani ya nyumba,
Soldier, akawa naye anateremka kwenye gari huku kambeba mtoto,
hakutaka kumuachia, alikuwa kama kashikilia ushahidi, hataki umponyoke, lakini
sasa alikuwa akitaka kumkagua usoni, dereva, kuna kitu kahisi, lakini ikawa sio
rahisi maana watu walishafika kuwapokea,..wazazi, ndugu..na hatimaye mtoto
akawa kachukuliwa na mkewe..
‘Ngoja mtoto akanyonye…’alisema mkewe akimchukua mtoto kwa
mumewe, ambaye alikuwa hataki kumuachia,lakini hakuwa na jinsi, akageuka
kumtafuta dereva,..alikuwa hayupo , akawa anageuka huku na kule,..alipoona
hamuoni akamwambia mkewe…
‘Ok…na naomba dereva asiondoke…’akasema
‘Kwanini!!, mbona yupo kazini, …tumemkodi tu mara moja, ..’akasema
mkewe akiwa anataka kuondoka na mtoto hakuonyesha wasi wasi wowote.
‘Nasema hivi, dereva asiondoke,…nataka awepo..si kuna sherehe, na
yeye awepo basi, au,…?’akasema akiangalia jinsi kulivyopambwa kishughuli, na
alijua ni kwa ajili yake, … shughuli ya kumkaribisha, na mkewe hakusema neno,
akaondoka kuelekea ndani yeye na mtoto, pamoja na yaya.
Soldier akaangalia huku na kule hakumuona dereva, ila gari lake
lilikuwa bado hapo nje,…akaanza kutembea kuelekea ndani, akili ilikuwa
imeshawekwa kwenye uwanja wa vita, lakini hamjui adui yake ni nani….
‘Nitamjua tu…’akasema akiangalia huku na kule, akijaribu
kumtafuta mtu wake, na mara akagongana na jamaa akiwa ametokea ndani,..akiwa na
haraka.
‘Oh sory….’alikuwa ni dereva, na soldier alipogundua kuwa ni huyo
dereva akasema;
‘Usiondoke,…ukaribie kwenye shughuli….’akasema askari
‘Bila shaka, hata kama nitaondoka, ..nitarudi tu, hapa ni
nyumbani mkuu…’akasema huyo dereva akitabasamu, na haraka akawa anatembea
kuelekea kwenye gari lake huku akiimba wimbo wake…
‘Kitanda hakizai….’akakatiza huo wimbo alipokumbuka kuwa
aliambiwa asiuimbe,..akageuka kumuangalia askari ambaye kwa muda huo alikuwa
akiingia mlangoni huku anatizama nyuma kumtizama huyo dereva…
NB: Jamani shida kutokuwa na chako,…jembe limeharibika
WAZO
LA LEO: Hisia, au dhana, inaweza ikakufanya ukakufuru, hasa unapokuwa
kwenye mitihani ya matatizo, inaweza kukufikia hali ya kumdhania kila mtu ni
adui yako, kumbe sio…Muhimu tuwe na subira, tujitahidi kuchunguza kwanza,
kujirizisha kwanza,…subira na kuhakikisha tunatenda yaliyo mema, tutafanikiwa.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment