Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, February 11, 2017

ALIYEKUPA WEWE, NDIYE ALIYENINYIMA MIMI...


 Ni kisa cha binti Maringo, hilo sio jina lake halisi, jina lake halisi aliitwa Maua…alikuwa maua kweli,..kwa uzuri na umbile .... na kwa vile alijaliwa kuwa na wazazi wenye uwezo, basi alikuwa akijiona, akajawa  na dharau..kutoka utoto hadi usichanani..

Umri ulivyokwenda , ndivyo alivyozidi kunata, ..... Ikafikia hatua wanaume nao wakamdharau, ila kwa wale wenye nazo hawakusita kumtaka. Na wengine wakataka kutumia pesa kumkomoa! Siunajua tena wanaume wengine, hawashindwi wakiamua..lakini kwa binti huyu wakagonga mwamba!

Pindi tukasikia kaolewa, na kila mmoja akawa na shauku ya kufahamu ni nani kamuoa huyo binti Maringo,…mhh, kweli aliolewa na kibopa mmoja,…ni tajiri wa uhakika,…lakini..mmh, kila mmoja aliposikia kuwa jamaa huyo ndiye kamuoa huyo binti, aliishia kuguna tu.

Kiboba huyu hakujulikana wapi anapatia pesa zake, ilikuwa ni siri yake kubwa hata familia yake ilikuwa haifahamu. Pesa kwake ilikuwa kama makaratsi tu,…anabadili magari kama nguo, nyumba anajenga kama uyoga…

 Hata hivyo za mwizi ni arubain, siku kadhaa tukasikia jamaa, yaani huyo kibopa kakamatwa huko Uchina, na madawa ya kulevya,…

‘Oooh, kumbe ndio ilikuwa kazi yake….’watu wakaanza kusema.
Siunajua tena Uchina hakukopeshwi, ukikamatwa huko na madawa ya kulevya, adhabu yake ni kifo…tukasikia jamaa kanyongwa…na binti maringo akawa mjane.

Siku zimepita binti maringo, kabakia mpweke, kila anayekuja kutaka kumuoa, yeye hamtaki, kisa hana hadhi, …hana uwezo, ..na kauli za kejeri kibao…mmh, akaja kuolewa na jamaa mmoja…Jamaa huyo anazo, lakini sasa , tatizo lake ni ngumi mkononi,…Binti Maringo kavumilia vikamshinda, akamwaga manyanga, na kurudi kwao, na jamaa akasema;

‘Hata mimi sikutaki…chukua talaka yako…, kwanza mtu mwenye unanipa shida tu..’wakaachana kwa kashifa kihivyo.

**********

Ni kisa kirefu…mwishoni mwa mwaka 2016 nikakutana na binti maringo, yupo maeneo ya kariakoo, anatembeza nguo za mikononi,..sikuamini, kwa hali niliyomkuta nayo, ana makovu usoni, wakati awali uso wake ulikuwa mwororo wa kuvutia....nikajiuliza kulikoni, kwa vile nilikuwa namfahamu na mara kwa mara tulizoea kuongea,….nikamuuliza…

Binti huyu , akaishia kulia,…

‘Mhh…natamani nife tu, lkn siwezi, wadogo zangu wataishije, wananitegemea mimi sasa..ila,hapa nilipo…natamani niende kwa wazazi wangu huko walipo…’alilia na kuongea maneno ya kusikitisha sana.

Kiukweli nilimsikitikia binti huyu…., lakini ndio maisha, mola ni mwingi wa rehema, mola humjalia mja wake kwa wakati fulani, na anaweza akamnyang’anya kila kitu kwa wakati fulani,..yeye anajua ni kwanini,.

‘ Ila nimejifunza jambo moja,..kiburi cha neema za mungu, hatutakiwi kukiringa , na dharau, ni tabia mbaya sana, mimi nilikuwa na tabia zote hizo, kisa mali ya baba, mali ya wazazi wangu, sasa hawapo tena duniani….mola wangu nisamehe….’akasema akilia.

Akilini niliwaza mbali sana, nikikumbukia maisha ya huyu binti,..ama kweli, aliyekupa wewe leo, ndiye aliyeninyima mimi, na huyo huyo anaweza kunipa mimi pia….tukipata kamwe tusimsahau mola wetu, kwani dharau, kiburi, hulipizwa hapa hapa dunia..nasema hili sio kwasababu ya huyu binti ila mengi tumeyaona, tunayaona…,….

**********

 Kumbe binti maringo, masikini, baba yake alikuja kufariki, ..na utajiri wa wazazi wake, aliouacha baba yao, ulianza kupukutika kidogo kidogo, wakaja hata kuuza jumba lao la kifahari, jumba ambalo binti huyu aliliita ‘KASIRI YA MFALME….’

‘Hii ni kasri ya kifalme,…’alikuwa akisema hivyo, maana kweli ilikuwa kasri, kila kitu ndani,…
Ilifikia mahali, wakaamua waiuze hiyo nyumba, lengo lilikuwa kumtibia mama yao ambaye alikuwa akiumwa kwa kipindi hicho, kwani zilihitajika pesa za kwenda kumtibia mama yao nchi za nje…wakabakia na kibanda cha uani, ….

Mama yao alitibiwa kweli, akarejea akiwa na afadhali, lakini hali yake iliendelea kuzorota na pesa walizokuwa nazo kama akiba walijaribu kuziwekeza kwa biashara hii ni ile, lakini waliandamwa na mitihani mingi, wakaja kuibiwa, kutapeliwa, na huku mama anaumwa hapo…, ikawa shida, kumtibia,..

‘Mama alivumilia, kumbe alikuwa akiteseka kwa maumivu, hakupenda kutuambia, akawa anajitahidi hivyo hivyo akijua yeye ndiye baba, ndiye mama….’akatulia.

‘Siku nilipogundua, nikajua..sasa mama atatuacha…nilimuona anavyoteseka, kwa maumivu, na huenda moyoni aliomba afe tu, ili akapumzike na mume wake huko alipo, lakini akitufikiria sisi, …lakini hata hivyo ikafika muda wake,…akatangulia mbele ya haki…akituacha hatuna mbele wala nyuma..nililia sana siku hiyo,…hadi kupoteza fahamu siku tatu…’akazidi kunisimulia.

***********

Binti maringo alikuwa ndiye mkubwa kwenye familia, akabakia na wadogo zake, wadogo zake walikuwa wakiwategemea wazazi wao, walisoma shule za bei mbaya,..lakini hawakufanya vizuri, walikuwa wamelemaa  na utajiri wa wazazi wao, sasa wazazi hawapo, mali hazipo…hawana ndugu wa kuwasaidia, wamebakia mayatima na masikini….

Binti maringo, akaanza kuhangaika,…

‘Nilifikia hatua nikaanza kujiuza,…tusife njaa, wadogo zangu wapate kula, wanaume wakatumia mwanya huo kunizalilisha, badala ya kunisaidia, hawajui kuwa na wao ipo siku na wao yatawakuta, hata kama sio wao …inaweza ikawkuta watoto wao, maana mimi sikuomba kadhia hiyo inikute..ndio mimi nilikuwa naringia mali ya wazazi wangu, lakini sikujua, aliyekuwa anajua ni mola peke yake, sikujua kuwa ipo siku na mimi nitakuwa omba omba, nizalilike hivi…. …..’akakatisha akilia.

‘Nilifikia hatua nikauza bar..unakumbuka nilivyokuwa nikiwazarau wanaofanya biashara hiyo nilikuwa nikisema bora nikalime …..lakini nigelifanya nini mie…nilifanya hivyo sio kwa ajili yangu tu, ila kwa ajili wadogo zangu, nawapenda sana wadogo zangu……’ akasema ….

Kwakweli kila hatua ya kisa hiki…alivyokuwa akinihadithia, ilikuwa ni aheri ya jana, na alikuwa akinihadithia kisa cha maisha yake huku analia,…ni kisa cha aina yake, lakini ….simu haiwezi kukiandika chote kwa marefu yake…, tukijaliwa ipo siku nitakitohoa kwa mapana yake.

 WAZO LA KISA HIKI KIFUPI: Katika maisha haya ya hii dunia, tukipata, tusisahau kuwa kuna leo na kesho. Iwe tumepata kutoka kwa wazazi, tumepata cheo….tusiwadharau wenza wetu, au kuwdhulumu, kuna mabosi, wanatumia vyeo kuwadhulumu wenza wao..hii sio sahihi jamani maana hutujui ya kesho yatakuwaje,..

Pia, tusitegemee sana utajiri wa wazazi wetu, waume zetu, wake zetu, ndugu zetu…tujaribu sana kujitahidi  kusimama kwa miguu yetu wenyewe kwa kujaribu kujifunza, kuwekeza, kusaidiana na wenzetu, au kufuata nyayo njema za wazazi wetu, waume zetu au wake zetu walivyofanya wakafanikiwa.

 Tumuombe mola wetu atujalie tuweze kuishi kwenye njia sahihi, anazoziridhia yeye, atusaidie , atuongoze maana mitihani ya dunia ni mingi sana, tunaweza kujiona tupo sahihi, kumbe tunakengeuka na uwezo wetu wa kujua ghaibu ni mdogo. Aamiyn!


WATUMIE WENGI TUJIFUNZE NA TUKIO HILI.

Ni mimi: emu-three

No comments :