‘Hivi mbona mambo yanazidi kuwa magumu, maisha yanakuwa
magumu sijawahi kuona, ina maana kumbe, ufisadi, dili, rushwa…ilikuwa na neema
fulani, japokuwa ilikuwa ikitutafuna kama kansa…’ilikuwa kauli ya jamaa kwenye
treni.
‘Kwanini unasema hivyo bro..?’ akauliza mwingine na wote
tukatega sikio kusikia hoja hiyo.
‘Mimi nilikuwa nimeshanunua kiwanja, na kuanza kujenga,
nilijua mwaka tu nitamaliza, na sio mimi tu, wenzengu wengi walishaanza azimio
hilo,..lkn tangia kasi hii mpya ya sasa kazi tu, iingie tumekwama kabisa,
majengo hayaendelei…., hakuna hata mmoja ameweza kusogea mbele..’akasema
‘Sasa kwanini ina maana mlikuwa mkijenga kwa pesa za
dili..au?’ akaulizwa
‘Hamna bwana...ni kubangaiza huku huku tu, upo ofisi, lakini
nje una vijimradi vya hapa na pale…lkn sasa utabangaiza wapi, wenye kampuni wenyewe
wanafunga virago…, wenye biashara biashara haziendi tena, wanasema kodi
zimewaziba pua,..haya hata vidili vidogo vidogo havikamatiki tena, mtu kati
yupo wapi hakuna…sasa nitafanya nini…?’ akauliza
‘Oh..kumbe, sasa MTAISOMA NAMBA..’mama mmoja akasema, na
kauli hiyo ikaanzisha mjadala mkali, kichwa cha habari, ni kwanini sasa, ambapo
watu walitarajia neema, maana mafisadi wananyea ndoo, dili za rushwa,
zimejificha chooni, …watu wanalipa kodi bila kupenda,..eeh, sasa kulikoni…ina
maana hata watoto wetu wasisome shule za kulipia…haya warudie shule za kata,
maziingira yapoje…kazi kweli kweli….
'Mliotegemea dili...maisha ya uchochoro chochoro, mtaukimbia mji sasa, hamkuelewa waliposema tutahamia Dodoma,...sio serikali tu,..ilikuwa na maana ndefu tu, kuwa hata sisi, tunatakiwa kuhamia wapi....makwetu...hahaha mtaisoma namba....'akaongeza mwingine
'Unajua ni kweli, kwenye dili, ..tulikuwa tunasaidiana, ukipata na ndugu naye kapata..kutoa mkono unakuwa mwepesi tu...., lkn kwenye dili serikali haipati,...inaumia kwa kubeba mzigo usiobebeka... ndio maana sasa serikali inabana, ili ipate haki yake..umeonaeeh, ...'akasema mzee mmoja
'Nakuunga mkono mzee,...., hivi hamkukaa mkajiuliza hili jambo, siasa ni sehemu nyeti..kuongoza watu sio mchezo, , lkn ilifikia hatua watu wanaacha biashara wanakimbilia huko, wanaacha kazi zao za maana wanakimbilia huko, siasa ikawa dili,...sasa hivi siasa imekuwa KITI MOTO, ...umeonaeeh, kiukweli madaraka sio 'dili' madaraka ni wajibu, ni wito...usipowajibika, utaulizwa, sasa ni zamu ya serikali kuwauliza viongozi, bado zamu yetu inakuja,..watu wataamuka, na kuanza kuhoji, kiongozi wetu anafanya nini, katufanyia nini....'akasema huyo mzee mwingine.
'Na kwanini watu wake tu wasifanye kazi, wale walale , waangalie tv,..wakavute bangi, madawa ya kulevya,..hivi sasa walevi, wabugia unga wanapungua, kidogo kidogo...maana pesa za dili zipo wapi...mtaona wenyewe , mdogo mdogo, tunahamia wapi....?' akauliza mzee
'Dodoma...'vijana fulani wakasema na kucheka
'Sio Dodoma,...kijijini....'mzee akasema na kikawa kicheko
‘Mimi nimeamua kuwafukuza ndugu zangu warudi kijijni,
nitawalisha nini tena…, sasa hamuoni kuwa maisha kama haya, ubinadamu haupo
tena, ndugu tutanuiana…ina maana tutaishi kila mtu na lake..ndio tunataka
hivyo, hata ndugu yako akitoka kijijini kukutembelea asije bila taarifa na akija
unampa mgeni siku tatu, ya nne arudi kwao…?’ mmoja akauliza swali kwenye
mjadala wetu .
Maisha sio mchezo,
kila jambo awali yake huwa ni gumu sana, wengi tulizoe hivyo, maendeleo mpaka
dili, ukifika ofisini, ili ufanikiwe inabidi usuke mpango wa kupata teni
parcent, vochaa, vocha..sped up, mara hivi na vile,..usaidie kampuni kwenye
zabuni fulani na humo unaweka dili yako…ukifanya biashara ili utoke, unakwepa
kodi…nk…ikafikia mahali kila kitu mpaka kuwe na mtu kati, ..yaani madalali ,
hawa jamaa wakatajirika kweli, mdomo tu..,….hayo ndio yalikuwa maisha yetu,
sasa yanabadilika, ….ugumu wa maisha mengine, umeanza..
Mtindo huu wa maisha ya sasa inabidi utafute upate na lazima ulipe kodi, kodi ni malipo kwa serikali kwa huduma inayokufanyia, kwa maana hiyo basi Mwenye nacho, atafanikiwa na hata kuongezewa, kama atawekeza kihalali na
kujibidisha kwenye njia sahihi, ....anapata analipa kodi anabakiwa na faida...na asiyekuwa nacho,..ITAKUWAJE,... hata hicho kidogo
alicho nacho atanyang’anywa, kwani wanasema; asiyefanya kazi na asile….na ukumbuke, utalipa kodi upende usipende…
Tumuombe mungu wetu, tuliombee taifa letu, tuwaombee
viongozi wetu, tujiombee wenyewe, maana kiukweli sio kazi rahisi, sio jambo la
mazaha kama watu wanavyofikiria, kujibadili kunahitajia ‘jasho’ , juhudi ya
kweli na maarifa ya uoni wa mbele,..kama wengine kipindi hicho maisha bado
yalikuwa magumu, je kipindi hiki itakuwaje,… ni kumuomba mungu tu, ili tuweze
kulivusha jahazi hili kwa amani na salama, maana mafanikio ya taifa ni
maendeleo yetu na vizazi vyetu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment