Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, December 16, 2016

TOBA YA KWELI-22 (MWISHO)


‘Ngoja nikusimulie ilivyokuwa, maana ilikuwa harusi ya aina yake haijawahi kutokea…’akasema msimuliaji.

‘Mhh..tuambie maana watu tuna hamasa sana ya kusikia, ilikuwaje, na ulikuja kumuoa nani, mpka mkapata watoto, na huyo binti aliolewa na nani,….’nikasema

                         **********

 Siku ya ndoa..., hapana usiku wake, ndio mambo yalianza kujitokeza. maana hayo nilikuja kuambiwa .

 Wanasema huyo bwana harusi, alionekana kwenye nyumba moja ya starehe akiwa na kimwana, usiku huo ambapo kesho ndio anatakiwa kuoa...na huyo kimwana aliyekuwa naye, kumbe alikuwa mshikaji wake wa siku nyingi,…

Wanavyosema, eti huyo bwana harusi alikuwa hajatulia, unajua tena watoto wa wakubwa wengine walivyo..wanajua kutumia tu mali za wazazi wao,...hawana uchungu nazo, wanaringa, wanajidai kwa jasho la wazazi wao. Pesa ni mtihani, huyo kijana akawa, huku anataka kule anataka, kwahiyo alikuwa na matatizo mengi, ni kama mimi enzi zangu,..hahaha’ msimuliaji akasema  na kucheka.

‘Kwahiyo ilikuwaje..ulikwenda kuweka pingamizi, na kuwaelezea kuhusu huyo kijana au...?’ nikauliza

‘Haikuwa hivyo ndugu,..sikuwa na lengo hilo abadani,....'akasema

'Kwahiyo harusi ilifungwa, wewe ukashuhudia tu, au sio...?' nikauliza

‘Subiri kwanza nikuelezee kuhusu huyo bwana harusi, hiyo kukutana huko na huyo mwanamke wake wa siku nyingi ilikuwa namna ya kutafuta mbinu ya kuzimisha moto uliokuwa umeshaanza kuwaka…kulikuwa kuna tatizo kubwa, na hilo tatizo lilitokea baada ya huyo bwana harusi mtarajiwa alipotangaza ndoa.

Kumbe huyo mwanamke mwingine alishapata ujauzito,lakini awali hakuwahi kumwambia bwana harusi, ndio akaja kumwambia usiku huo wa ndoa, na huyo binti baba yake ni kigogo fulani, alijua asipomshinikiza huyo jamaa akaenda kwako kusema ukweli kuwa hiyo ni mimba yake, atakuja kupata shida!'

‘Nimeshasema huwezi kumuoa huyo Malaya wako…’akaambiwa.

‘Lakini nimeshatangaza ndoa…na huyo sio malaya kama wewe....’akalalamika muoaji

‘Mimi leo ni malaya sio...na kwani hukujua kuwa mimi ndiye mwanamke wako… kwanini ukanisaliti, na wakati nina mimba yako…’akaambiwa.

‘Mimba…hapana, sio kweli, huna mimba yangu wewe..usitake kuniharibia ndoa yangu…’akasema mtarajiwa.

‘Kama unabisha twende tukapime,…nilikuwa natafuta muda wa kukuambia na mara ndio nikasikia unataka kuoa,…sasa sikiliza, hiyo ndoa haipo tena, na kama utaifunga hiyo ndoa, …utakachokipata utakuja kuniambia…nitaweka mauchafu yako yote hadharani,…’akaambiwa.

‘Usinitishe wewe…mapenzi yetu yalikuwa ni ya starehe tu, sikuwa na mpango wa kukuoa wewe…’akasema bwana harusi, kukatokea kujibishana maneno mpaka akotokea msuluhishaji.

 Kilichoendelea baadaye hapo hakikujulikana, maana kesho yake bwana harusi, akawa anasita kwenda kwenye harusi, lakini baba wa huyo bwana harusi akatoa amri huyo kijana aende kufunga ndoa,…amri ya baba ni baba, muoaji akajiandaa akaelekea kwenye harusi

************
 Kama ilivyo ada, waowaji wakafika sehemu ya harusi, wakiwa wameshajiandaa kwa kila kitu, wakiwa wameshaingia ndani sehemu ya kufungia ndoa, sasa wamekaa wanaubiria amri , na taratibu za ndoa, mara bwana harusi akadondoka…’

‘Vipi jamani….’watu wanauliza, na wapambe wakawa wanamchunguza bwana harusi, wakasema bwana harusi kupoteza fahamu, wakamuhudumia wakijua labda ni mfadhaiko tu wa ndoa..ilichukua muda, mpaka akaitwa dakitari.

Baadaye bwana harusi akazindukana….’akatulia

‘Alipoamuka anauliza nipo wapi…akaambiwa, ‘upo kwenye harusi,..’

‘Ya nani…?’ akauliza na watu wakashangaa,

‘Ya kwako,…’

‘Ya kwangu, mimi nilishawaambia simtaki kumuoa huyo binti..simtaki,s imtaki,..’akasema kwa hasira .

‘Lakini … kwanini…?’ akaulizwa.

‘Kwanini,… hayawahusu, kwani muoaji ni nani, si mimi, kama mnataka nyie fungeni ndoa, lakini sio mimi,..nilishamuambia hata huyo binti harusi kuwa simtaki, wazazi tu wananishinikiza, simtaki, nimeshaamua sasa… ‘akasema na sasa akitaka kuondoka.

Wanandugu wakajaribu kumsihi, wakamwambia ni bora hiyo harusi iahirishwe ije kufungwa siku nyingine kama anajisikia vibaya…, lakini bwana harusi akasema hataki na hamtaki tena huyo binti harusi, na aliposema hivyo ….akaondoka, na ndoa ndio ikavunjika hivyo…, sasa…hebu fikiria, wazazi, na huyo bibi harusi, walivyojisikia.

Japokuwa binti harusi alikuwa hakutaka hiyo ndoa awali…, lakini ilishafika hatua ikabidi akubali tu, na kuna zile imani kuwa ndoa yako ikivunjika siku ya harusi ni nuksi, hatakuja kuolewa tena.

Kwahiyo ilivyotokea ivyo…binti, na wazazi wakajua ndio basi tena binti yao keshaharibikiwa, kilichofuata baadaye, baada ya kutangazwa kuwa kuna tatizo bwana harusi kaondoka, na ndoa haipo tena, wakina mama wakaanza kulia….ikawa sasa ni taharuki, mama analia kwanini wamemfanyia hivyo binti yake, wanafamilia wakawa wamechanganyikiwa, sasa kila mmoja anasema lake!…

***********

  Wakati hayo yanaendelea huko mimi sijui, nilikuwa kwenye mgahawa uliokuwa karibu, kwani nilishakata tamaa,…nilisubiria nione magari yakitoka ya bwana na bibi harusi,..nikaona kimia, baadae vilio…

‘Kilio cha nini…?’ nikajiuliza , ndio nikatoka pale mgahawani, na kuelekea kwenye hiyo nyumba,  wazo la kwanza labda kumetokea ajali,….

Nilipofika hapo, nikawauliza watu kumetokea nini, hakuna anayeongea , watu wameshika kichwa, wengine wakisema;

‘Nuksi hiyo….haolewei tena huyo….’

‘Kwanini….’hakuna aliyenijibu, hapo sasa nikaona nisubirie nione mwisho wake itakuwaje.Kwa ujumla mimi nilikuwa nasubiria tu kupoteza muda.., sikuwa na tumaini tena na huyo binti, maana hata kama hiyo ndoa imevunjika kuna sababu, na sababu hizo zinaweza kusawazishwa au sio.

‘Hiyo ndoa haipo tena, nilijua, tu…yule kijana hajatulia…’nikasikia mtu mmoja akisema.

**********

Muda ukapita, baadaye kitu kikanivuta, kwanini nisiingie huko ndani tu, ili nijue moja, halafu niondoke zangu..ilikuwa wazo tu,  na bila hata kufikiria, nikatembea hadi mlangoni,…mlango ulikuwa wazi, nikaingia  ndani, muda huo hakuna anayeshughulika na mtu, kila mtu kainamisha kichwa chini,..ni aibu, fadhaa, kuchanganyikiwa,..

Mimi nikaingia hadi ndani na kuwakuta wazee wamekaa,..ilikuwa ni wazee wa hiyo familia, wamekaa lakini wote wamainama kama wanaombeleza…nikabakia nimeduwaa pale ndani, sikujua sasa hata nifanye nini.

Nikaona kwanini nisiende kumliwaza huyo baba, baba wa huyo binti ananifahamu, ila sikuzoeana sana na yeye, nikasogea hadi pale alipokuwa amekaa…

‘Mzee poleni sana..mimi naombeni msikate tamaa, hii ni mitihani tu itakwisha tu…na binti yenu ataolewa, …’yule mzee, aliinua kichwa akiwa kakunja uso kwa hasira, nikajua sasa naweza kupigwa ngumi.

‘Wewe ni nani….?’ Akaniuliza, na kabla sijamjibu akaiona sura yangu, kwa haraka  akasimama na kunishika mkono na kunivuta sehemu nyingine ya chumba , sikujua anataka kunifanya nini…ni kama vile alitaka kunipiga au ..hata sielewi…tulipofike sehemu nyingine ya chumba, akaniangalia kwa hasira huku akisema;

‘Haya niambie umefuata nini wewe mtu..ndio umekuja kutusanifu au sio..?’ akaniuliza kwa hasira.

‘Mzee sina nia mbaya, nimesikia haya yaliyotokea, najua hali mliyo nayo..na najua nyie hamunitaki nimuoe binti yenu,….mimi nimekubaliana na hali halisi, …lakini hili limtokea mimi kama binadamu lazima nije kuwapa pole..’nikasema.

‘Kutupa pole, ili iweje….sitaki tena kuwasikia hao watu, na kama akijitokeza mtu wao, sijui.. nitakwenda kufungwa tu kwa hicho nitakachowafanyia, siwezi kuabishwa kiasi hiki….wewe subira nitakavyowafanya, haya ondoka hapa, sitaki kukuona mbele yangu…’ Akanisema kwa hasira.

‘Mzee, labda nisema neno moja tu, nawaombeni kama itashindikana kwa huyo mchumba wake,wala msiwe na wasi wasi,,eti mkosi au nuksi,…, mimi bado nina dhamira ya kumuoa binti yenu, kama ikishindikana kwa huyo basi niozesheni mimi…’nikasema

‘Eti nini, ndio ulikuwa unaombea hilo litokee, una wazimu nini wewe..nimekuambia uondoke , na nyie ndio mumeitia mkosi ndoa hii..sitaki hata kukuona, toka humu ndani kwangu….’akasema kwa hasira, kumbe wazee wengine wamesikia , na mara akaja mzee mwingine huyu ndiye mjomba mtu, na wakati anaingia ndio mimi najitetea.

‘Sio hivyo mzee, yote ni mapenzi ya mungu….’nikajitetea

‘Jamani kuna tatizo gani tena huku….’akauliza mjomba mtu.

‘Huyo …mtu sijui kaja kufata nini hapa, hebu sikia eti kaja ili tumfikirie, kwa vile hii harusi imevunjika, basi yeye atamuoa binti yetu, ….utafikiri mchawi,…’akasema baba wa binti.

‘Oh… kwahiyo, yeye anasema hivyo, kuwa , ..yupo tayari, kumuoa..baada ya haya yote, mimi naona tumetatua tatizo mzee mwenzangu,  haya mambo yana imani zake ikifikia jioni ya leo tusipofanya jambo, binti yako atakuozea humu ndani,..hataolewa tena, sasa muda wakulitatua tatizo hili ni sasa…kabla muda haujaisha…’akasema mjomba mtu.

‘Kwahiyo unasemaje…?’ akauliza baba wa binti.

‘Njoo huku tuongee….’akachukuliwa huyo baba wa binti na huyo mzee ambaye ni mjomba wa binti, wakaenda huko walipokwenda, kuongea, baadae baba mtu akarudi, na kunikuta mimi bado nimesimama hapo hapo, naogopa hata kuinua mguu!

‘Ulisema nini, …kuwa upo tayari kumuoa binti yangu, …si ndio hivyo…, basi sawa, nitafanyaje sasa,,..sina cha kufanya, sawa..si wewe unamtaka binti yangu haya,  utamuoa leo hii,..sitaki hata mahari yako, ninachotaka huu mkosi uondoke… unasikia utamuoa leo hii…. umenisikia leo hii, sawa..?’ akaniuliza

‘Leo hii, lakini mbona sijajiandaa…!’ nikasema

‘Hakuna cha lakini tena hapa,… tusipoteze muda, …’akasema na kuondoka, akiniacha nimeduwaa

Baadaye akaja mtu mwingine kuniita, nikapelekwa chumba kingine nikakuta nguo za kuvaaa, …nikaambiwa nizivae… ni maalumu kwa ajili ya harusi,…nikawa sina la kufanya, nikafanya nilivyoambiwa, … ..na huko nje ninasikia tangazo:.

*************

‘Nawaombeni watu msiondoke, harusi ipo kama kawaida..’tangazo likarudiwa mara nyingi tu na msemaji mkuu,…Na haikupita muda,watu wakarudi, sasa wakiwa wengi zaidi na hata wale wasiokuwepo awali, kila mmoja na mihemuko yake,

Wengine walitaka kujua ni nini kinaendelea, kwanini huyo bwana harusi kaamua kurudi tena, hakuna aliyejua kuwa muoaji sio yule wa awali…

Hutaamini, tukafungishwa ndoa, bwana kapata bibi, bibi kapata bwana…harusi ikafana tena sana,..lakini nilkuja kutoa mahari..usije kusema nilioa bila mahari,…hahaha..’akasema kwa furaha.

‘Oh hongera…’nikajikuta nikisema mimi msimuliwaji na kusimama kumpa mkono msimuliaji.

‘Hicho ndicho kisa changu cha ukweli… toba ya kweli….nimemaliza…’

                                           MWISHO
WAZO LA LEO: Lililopangwa na mungu litokee, litatokea tu, ..muhimu ni kufanya subira, huku tukimtegemea mola. Tusifanye subira huku tukikufuru..tukalalamika, tukalaani, hata kujenga chuki na hisa mbaya kwa watu wengine. Hiyo sio sahihi, hujui ni kwanini mola wako analisubirisha hilo jambo, yeye anatujua zaidi ya tunavyojijua weneywe, tusubirie, na.., muda muafaka utafika, na kwa kudra zake maanani utapata ufumbuzi wa tatizo lako.


NB: Nawashukuruni sana wote mliokuwa mkikifutilia kisa hiki, najua kuna wenye kusema hili na lile, lakini nia na lengo langu ni kutoa visa vyenye mafundisho. NATOA visa ambavyo hata watoto wangu wanaweza kuvisoma, iwe ni kwa manufaa ya jamii ya leo na kesho. Ahsanteni sana.
Ni mimi: emu-three

No comments :