Docta akiwa
amepumzika mara simu yake ikaita, alipoangalia akaona ni simu ngeni kwenye simu
yake…, akaipokea, akilini akijua ni mmoja wa wagonjwa wanaotaka kuwasiliana
naye,…, au ni mtu anayehitajia huduma yake,..mara sauti ikatanda sikioni na
hali kama kwikwi ya kilio.
‘Wewe ni nani, na
unalia nini…?’ akauliza docta
Mpiga simu akajieleza,
yeye ni binti aliyekuwa akiishi na jirani yake..aliposema hivyo ndio docta
akamtambua, akashangaa ni kwanini huyo binti kaamua kumpigia simu tena anaonekana
kama analia, akamuuliza kuna nini,ikabidi huyo binti amsimulie ni nini kinachoendelea
huko kijijini, na alipomaliza docta akamuuliza;
‘Kama wazee wako
wamefikia hatua hiyo.. wewe unataka mimi nifanye nini,?’ docta akauliza.
‘Mimi ninachoomba
kwako ni kitu kimoja tu…ninataka wewe uwapigie simu wazee wangu ili wapate
ushahidi kuwa kweli marehemu ndiye alitaka mimi niolewe na huyo jirani yako,
nataka nisije kuonekana kuwa mimi sikujitahidi, sina jinsi, siwezi kuwapinga
wazazi wangu, lakini pia siwezi kupinga kauli ya marehemu, nilimpenda sana, na
nilishakuwa tayari kuolewa na huyo aliyekuwa mume wake, lakini sasa....…’akasema
binti na kukatiza kwa kwikwi , kama anataka kulia.
‘Je wewe ulikuwa
tayari kuolewa na huyu jirani yangu, ni kweli kuwa unampenda, au ulitaka
kuolewa naye tu, kwa vile marehemu alitaka iwe hivyo…?’ akaulizwa docta
‘Docta, mimi
nimeishi na huyo mtu humo ndani, nimemzoea sana, kuna kitu anacho…kimenifanya
nimpende, na najua nikiishi naye tutaishi kwa amani…huyo mtu ana utu, ana ubinadamu,
ana hali ya kujali, siwezi kukuambia mpaka uishi naye..…japokuwa alikuwa na
madhaifu yake ndio..lakini kwasasa kabadilika kabisa, hayo madhaifu yake hayapo
tena, ..ni mtu mpya, mpendevu…’akasema binti.
‘Lakini mwanzoni
alikuwa akikuchukia au sio, mpaka ukanilalamikia,..unakumbuka…?’ akauliza
docta.
‘Ndio…awali alionyesha
wazi kunichukia, ni kwa vile alikuwa na kumbukumbu ya mkewe..hata hivyo, kuna
muda nilikuwa namfuma akiniangalia sana, kuashiria kitu fulani moyoni mwake..kuna
wakati ananifananisha na mkewe….’akatulia kidogo.
‘Ni kweli alikuwa
mtata awali, hata mimi ilifikia wakati
nikamchukia kwa matendo yake ya kunitukana..kunikashifu….., kwa jinsi
alivyokuwa akinitendea..ilihitajia subira kwakweli…, lakini siku aliponitamkia
kuwa anataka kunioa, kweli ananipenda, na nikakumbuka mkewe, alivyokuwa mpendwa
wangu… nikawa tayari nimeshampenda, na hakuna cha kumlia mkewe zaidi ya kuolewa
na ..na…’akasema kusita kumalizia.
‘Mhh, hebu niambie
ukweli, ulikuwa unampenda huyu jamaa tokea lini, yaionyesha labda ulikuwa
ukimpenda tangia awali, au sio…?’ docta akauliza
‘Hapana, hapana,
docta…yaani nikuambie ukweli, kumpenda, imeanza siku za karibuni tu..sikuwa na
wazo hilo kabla..mimi nilimpenda marehemu tu,kama dada yangu sio yeye,…., mimi
siwezi kumpenda mume wa mtu..kamwe, sina tabia hiyo mbaya…, hata hivyo aah,
tuyaache,….mimi ninachokuomba kwa sasa ni wewe uongee na wazazi wangu….’akasema
‘Lakini si umesikia
kuwa huyo mtu ana matatizo, ….’akaambiwa
‘Matatizo gani…?’
akauliza huyo binti kwa mashaka
‘Ya kiafya….’akasema
docta
‘Lakini mbona mwenyewe
kasema ameshapona,..hana tena hayo matatizo…nina uhakika ameshapona, mungu
keshamponyesha…’akasema huyo binti.
‘Mhh…sawa kama kweli
umempenda, mimi sina kizuizi, nitajitahidi kuongea na wazazi wako, lakini kama
wataendelea na dhamira yao hiyo…, basi …nikushauri kitu, ni kweli huyu jirani
ni rafiki yangu, lakini nakuomba usiende kinyume sana na matakwa ya wazazi wako…lakini
jitahidi kuwaelezea msimamo wako…hadi mwisho’akasema docta.
‘Kwahiyo, unataka
kusema nini hapo docta….?’binti akauliza, na mara ikasikika sauti kama sauti ya
kukemea, na simu ikakatika, yaonyesha huyo binti alikuwa akiongea kwa uficho na
sasa keshafumwa akiongea na simu.
********
Docta hakuona shida,
akawapigia simu hao wazazi wa huyo binti, na kuanza kuwaambia ukweli kuhusu huo
usia wa marehemu...
‘Kwanza ni nani
kakuambia utupigie simu, haya yanakuhusu nini wewe…?’ akaulizwa
‘Mimi nilitaka
kuliweka hilo wazi kuwa ni kweli, marehemu alisema hivyo, isije kuonekana kuwa
huyo binti kajitungia, lakini pia ni vyema na nyie mkalijua hilo, ili baadae
msije mkasema , kwanini hatukusema hivyo….samahanini wazee wangu…’akasema docta
‘Lakini sasa
atawezaje kumuo binti yetu wakati huyo mtu anafahamika kuwa sio kamilifu, mnataka
binti yetu aende akawe majaribio au sio…au ndio ndoa za siku hizi, za
kuangaliana tu, kama picha, ina maana wao hawataki watoto, au ndio mwanzo wa
kubambikiwa watoto wasio halali, au unataka kumpandikiza mtoto wetu mbegu kama
ng’ombe…?’ akaulizwa docta.
Na kabla docta hajajibu baba akaingilia kati,
maana sauti iliwekwa hewani kila mtu asikie anachoongea mjomba,…
‘Hebu tuambie wewe
ni docta sio, je huyo mtu anaweza kuzaa…?’ baba akauliza
‘Kwani ni nani
alisema kuwa huyo mtu hawezi kuzaa…?’akauliza docta
‘Tunakuuliza wewe
sasa, utuambie…’akasema mzee
‘Mimi hilo kuwa
hawezi kuzaa silijui…..’akasema docta
‘Docta,au ndio umeungana
kutuangamizia binti yetu ujue wewe ndiye utabeba lawama zote…’akasema baba
lakini mjomba akadakia na kusema
‘Hata hivyo sisi
hatuwezi kukubaliana na hiyo kauli ya marehemu, ni kauli yake, lakini hakuwa na
amri ya binti yetu, kwa mfano umeulizwa una uhakika kuwa kweli huyo jamaa
kapona hana matatizo tena, umeshindwa kutupatia majibu ya uhakika, huna
uhakika,..kama docta, inaashiria akuwa unaficha jambo..’akasema
‘Aaah, nisikilizeni…’akasema
docta, lakini akakatishwa
‘Sisi sio watoto
wadogo, kauli yako tu inaonyesha una mashaka,..na tukuambie ukweli, sisi
tumeshapokea mahari,na kila kitu kimeshapangwa,…kwahiyo hayo na mengine kwetu
kwasasa hayana nafasi tena…’akasema baba
Docta alijaribu kunitetea, lakini haikusaidia
kitu, ikabidi docta asalimu amri
Docta alipomaliza kuongea na hao wazee, ikabidi atoke
hapo nyumbani kwake, kwenda kwa jirani
yake,akijua huenda hajaondoka, alitaka kumwambia ukweli, na ilibidi amshauri
aachane tu na huyo binti, lakini alipofika nyumbani kwa huyo jamaa akakuta mlango
umefungwa, na alipouliza majirani wengine, akaambiwa jamaa kasafiri kwenda
kijijini.
‘Mhhh, huyu rafiki
yangu kafanya nini…’akasema lakini akawa hana jinsi ikabidi asubiria asikie
kitakachoendelea huko Kijijini
**********
‘Kwahiyo wewe
uliamua kwenda kijijini,.. ili iweje sasa, ili ukaizuie hiyo ndoa, au ….hebu
tuelezee hapo vizuri…?’ nikamuuliza msimuliaji.
‘Ni kweli, wakati hayo yakiendelea, na mimi
nilikuwa nafuatilia kwa namna yangu, ndio nikasikia kuwa huyo binti yupo karibu
kuolewa,….
‘Ina maana binti
ilifika sehemu akasalimu amri, akakubali kuolewa na huyo mchumba waliotaka
wazazi wake…?’ nikamuuliza
‘Ndio…., unacheza
na wazazi wewe,…binti wa watu alijitahidi mwishowe akasalimu amri, na tarehe ikapangwa, na watu wakawa kwenye
maandalizi ya ndoa…niliumwa kwa muda
mfupi, nikawa kama mtu aliyechanganyikiwa….…’akasema
‘Mhh kwahiyo sasa
ikawaje…..’nikamuuliza na mimi nikivunjika nguvu, sikutarajia itakuwa hivyo.
‘Mhh, ninachoshukuru
…sasa hivi nina mke na watoto,..mimba ya kwanza tu ilianza na mapacha....,hiyo
ilikuwa ni mimba ya kwanza; mapacha…watu
hawakuamini..lakini utasema nini , kwani watoto waliozaliwa tunafanana kuanzia kichwa
hadi vidole, sura na kila kitu…’akasema akitabasamu
‘Sasa…sijui labda tabia..na
nisingelipenda waje kurithi tabia yangu ya awali….na na.., mimba ya pili ya
kawaida tu….’akasema akizidi kutabasamu
‘Rafiki, …mimi
nimeamini mungu ana maajabu yake maana wengine walishaanza kusema mke wangu kapandikizwa
mbegu, hamna kitu kama hicho …weeeh, mnacheza na mungu,…hiyo ni siri ya toba,….lakini
toba ya ukweli…’akawa anatikisa kichwa.
‘Sasa hebu
tufafanulie hapo, ina maana wewe ulikuja kuoa mke mwingine tofauti na yule,..sio
huyo binti tena, au ilikuwaje…maana kwa taarifa ya docta, wazee walishapitisha
kuwa hataolewa na wewe, na ….hata wewe umesema hivyo, sasa ilikuwaje…?’ nikamuuliza
‘Sitaweza kumsahau marehemu
mke wangu, na kila nimuonapo mke wangu
huyu mpya, naiona taswira ya mke wangu waziwazi…, kiukweli wawili hawa kumbe
kweli wanafanana sana..’akasema msimuliaji.
‘Kwahiyo ina maana
gani, huyo mke mpya uliyempata ni ndugu na na….’nikasema na yeye akatikisa
kichwa kama kukataa na kusema;
‘Hapana sio ndugu….Unajua
namuomba mungu sana,….namuomba mola wangu aiweke roho ya marehemu mke wangu mahali pema peponi,…’akasema akiinua mikono
juu.
‘Mhh, hapo mimi
sijakuelewa…kwahiyo, unatubia kwake kuwa alichotaka yeye hakikuweza kufanyika
au sio..?’nikamuuliza.
‘Unajua kilichotokea
siku hiyo,…kama nilivyokuambia, mimi sikuweza kuvumilia, niliamua kwenda huko
huko kijijini, nia ni kutata kuthibitisha mwenyewe huyo binti akifunga ndoa,…na
kweli hata siku hiyo ya ndoa nilikuwepo
hapo kwenye eneo la harusi, huku moyoni ninalia…’akasema,
‘Mhh….sasa wewe
ulishajua kuwa umeshindwa, kwanini sasa uliamua kwenda kujitesa hivyo..?’
nikamuuliza
‘Sikuamini kuwa
maneno ya mke wangu yanaweza yasifanikiwe, sikuamini kuwa binti ambaye baadaye
nilikuja kumpenda, ataolewa na mtu mwingine…sikuamini kuwa kauli ya wakuu wa
imani yanaweza kwenda kinyume, sikuamini kuwa mungu anaweza kunikosesha, baada
ya juhudi zote hizo..ndio maana nilitaka kuthibitisha kwa macho yangu mwenyewe…’akasema
‘Sasa ilikuwaje..?’nikamuuliza
‘Ngoja nikusimulie
ilivyokuwa siku hiyo ya ndoa, maana ilikuwa ndoa na harusi ya aina yake haijawahi
kutokea…’akasema akijiweka sawa kusimulia.
NB: Nimeona niweke
sehemu hiyo ndogo ya hitimisho, mtandao unasumbua sana,nitakuja kuweka sehemu
iliyobakia, mungu akipenda…. mniwie radhi.
WAZO LA LEO: Mpende akupendaye, na asiyekupenda achana naye, maana huyo
asiyekupenda ana wake anayempenda, ukilazimisha mapenzi, maisha yenu yatakuwa
ya mashaka, kwanini uhangaike na huyo wakati wengine wapo, kwanini uumie na mtu
mmoja, wakati wapo wengi wazuri tu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment