Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, November 7, 2016

TOBA YA KWELI-17




‘Shemeji, sasa mimi ndio ninaondoka..

‘Hata hivyo shemeji..mimi, nitajitahidi nipitie kwenu, ili mmoja wa ndugu zako waje, kwa hali kama hiyo huwezi kubakia peke yako..

‘Mimi ..najua nakwenda kinyume na maagizo dada yangu mpendwa, lakini huko alipo atanielewa, anisamehe sana,..

‘Najua kabisa nilimpenda sana dada yangu na niliahidi kuwa nitafuata yale yote aliyoniagiza lakini sasa nifanyeje mimi..ndugu zangu wamanisusa kwa kujitolea hivi, na wamesema litakalonipata ni juu yangu mwenyewe, wameniambia niondoke, na jana tu wamepiga simu kuwa nahitajika nyumbani haraka, sijui kuna nini…. ,

‘Hebu shemeji niambie mimi nitafanya nini na mimi ndiye niliyekuwa msiri wa dada yangu, …ndio maana nimejitolea kuwa nawe japokuwa naumia, Napata shida, sina amani,na sijui itakuwaje kesho au kesho kutwa …nielewe tu shemeji, sina budi niondoke….’ hapo aliguna na kumezameza  hayo maneno ya mwisho...nilijua kabisa alitaka kusema nini…

‘Nilitaka kumwambia, ..huondoki unasubiria nini..lakini kauli ilikataa kusema kwani kuna kitu kingine kilikuwa kinaanza kujijenga akilini….

‘Lakini nitafanyeje mimi jamani..…mimi mwenyewe sasa ninaanza kuogopa, uvumilivu wangu umefikia kikomo..…ninaogopa chochote chaweza kunipata, nakumbuka yaliyowahi kutokea huko nyuma, nahisi kuna dalili kama hizo, kwahiyo unisamehe tu..unisamehe sana shemeji, kwaheri…’akasema huyo mdada, kwangu mimi nilimuona kama binti,

Ilikuwa kama salamu ya kuagana kwa mtu uliyemzoea, ..ilikuwa kama kitu fulani nilichokizoea sasa kinaondoka, ..ilikuwa kama mtu ambaye nilikuwa tayari kusema niwezavyo, lakini bado anakuvumilia, anakupatia huduma zote bila kujali, ni kama mzazi wako....sijui nisemeje, kwani huyu binti alishatokea kuwa mtu wangu muhimu…sasa ndio huyu anaondoka.

 Mara nikahisi kichwani sauti nyingi zikiwa zinanikemea,..hizo sauti zilitokea kwa pamoja, kila mmoja akisema lake, niliweza kubahatisha kuzigundua badhi ya sauti, zilikuwa sauti za mke wangu, za docta, za mke wa docta, za wazazi wangu..nyinginae za wanandugu…na kila mmoja alikuwa akisema lake..na walikuwa wakisema kwa pamoja…, lakini cha muhimu zaidi ilikuwa kunisihi… nisimuache huyo binti aondoke..

Ukimuacha akivuka kizingiti cha mlango, basi umemkosa, hutampata tena…’ilikuwa sauti …ambayo sikufahamu kaongea nani, na hapo ndio huyo binti ilishafika hatua ya tatu, ili sasa akanyage au kuvuka kizingiti cha mlango, ..sikusubiria….

*****************

Kwa haraka nilikurupuka kama mtu aliyeamrisha kwenye mbio za mashindano ya mbio fupi..na tahamaki nikawa mgongoni mwa huyo binti, nilichofanya nikimshika begani, nahisi mkono wangu ulimgusa kwa nguvu,….kwasababu,sijui vipi huyu binti alinifikiria, maana alishtuka, mpaka akadondosha lile begi alilokuwa kalishika.

Na zaidi, akanigeukia, ....kwa haraka akapandisha mkono kuzuia mdomo wake uliokuwa umepanuka tayari kwa kupiga yowe la kuomba msaada…na mimi kwa haraka nikawahi kuongea…

 ‘Binti tafadhali, ninakuomba nisamehe….’ Nikasema na nilimuona akiniangalia kama kaona shetani au kitu gani cha kutisha, macho yamemtoka pima kwa woga…sasa akawa anajirudisha kichwa nyuma.

‘Nipo chini ya miguu yako,….nielewe binti..’nikasema nikijribu kumsihi.

 Kwa jinsi nilivyomuona nilijua kwa vyovyote atapiga yowe, na ikitokea hivyo sijui jamaii itanielewaje, na sijui kwanini kawa hivyo..mimi kwa sauti ya kusihi, nikasema;

‘Binti, ninakuomba kabla hujaonaoka, kwanza… unisamehe…nisamehe sana ,kwa hayo niliyokutendea….’nikasema nikijua nikisema hivyo hiyo hali aliyokuwa nayo itamuondoka…

Yule binti sasa akawa anahema, unajua kule kuhema kwa mtu anayeogopa kitu, …ndivyo ilivyokuwa kwake, na sijui kwanini alipatwa na hiyo hali, sijui alikuwa akinionaje mimi…. mara ghafla akayumba yumba….mara huyo akaporomoka chini, sikuweza hata kumzuia, akadondokea begi lake na ku-lala sakafuni. Na huko nje nikasikia gari likisimama….

‘Oh ni nani huyo..kama ni mtu baki nimeumbuka, lakini atakuwa ni …ni….DOCTA..’ nilikisia hivyo…

Kitendo hicho kilitokea kwa muda mfupi sana, nikabakia sasa mimi kuduwaa, nilishikwa an bumbuwazi ya ghafla….., nikijiuliza imekuwaje mlango ukagongwa.

Na muda huo ndio binti keshalala sakafuni…mlalo wa kuonyesha kapoteza fahamu….

**************

 Macho yangu yalikuwa yamekodoka, yakiangalia pale alipolala huyo binti sakafuni ni mbele kidogo na pale nilipokuwa nimesimama mimi, maana alipodondokea begi aliweza kusogea kidogo akawa mbali na mimi.

Mimi pale nilipo..niliogopa hata kumsogelea, …na muda huo, mlango ndio ukafunguliwa…ujue nilihisi tu kuwa docta, hata sauti ya kusema hodi, haikuwa sawa sawa na docta, lakini mimi akilini nilihis kuwa ni yeye,… ni docta, na niliombea awe ndio yeye, kwani angelikuwa mtu mwingine, ingelikuwa ni balaa…,

Na kweli alikuwa ni docta…

Docta akajitokeza, na macho yake yakawa pale alipolala huyo binti..

‘Umefanya nini jirani…’akasema sasa akimwangalia huyo binti kwa macho ya tahadhari pale alipolala..

‘Sijamfanya kitu docta,..naomba msaada wako,..msaidie huyo binti apone, sijamfanya kitu kabisa docta…naapa mbele ya mungu…sijamgusa kabisa…’nikawa nasema , ujue muda huo nilikuwa kama natetemeka.

Docta kwa haraka akachukua leso yake akaiviringa mkononi, na kwa tahadhari akamsogelea huyoo binti, alifanya alichofanya, na aliporidhika, akamweka huyo binti sawa, na kuanza kumkandamiza kifuani mara tatu…mara huyo binti akakohoa.

‘Nilipumua ile ya kuchoka,..nikajitahidi kujisogeza pale walipo, docta na huyo binti, lakini docta aliniashiria nisisogee, akawa anamfanyia hudum a ya kwanza, na alipojirizisha akanigeukia,..

‘Haya niambie kulitokea nini..?’ akaniuliza, na mimi nikawa namwangalia yule binti pale alipolala, siongei kitu, na docta akawa anaangalia saa yake kuonyesha ana haraka kutaka kuondoka.

‘Docta samahani sana usiondoke,..nakuomba uhakikishe huyu binti yupo salama..sitaki tena itokee..sitaki tena nimkose,….’nikasema nakushindwa kumalizia.

‘Yupo salama..nahisi alipatwa na mshutuko..anahitaji muda wa kupumzika, kama hali itabadilika basi itabidi apelekwe hospitalini….’akasema docta.

 Aliposema hivyo, mimi kwa haraka nikataka kwenda pale alipolala huyo ….docta akanizuia na kusema;

‘Kwa hivi sasa jitahidi kuwa mbali na yeye, hatujui kwanini ikatokea hivyo, ni kwanini anakuogopa kiasi hicho, kama ulivyosema ni sahihi… kama ni hivyo, hiyo ni hali ya kawaida tu itakwisha…jitahidi kumuondoa wasiwasi…’akasema docta, akawa sasa ana-angalia begi la huyo mdada.

‘Kwani vipi..alikuwa anaondoka…?’ akauliza na mimi sasa sikumjali alivyoniambia ..nikasogea pale alipolala huyo binti,binti na kumuinamia, alikuwa katulia kimia, na ile hali ilinifanya nikumbuke mke wangu siku nilipokwenda kumuona baada ya kuambiwa kafariki,….alikuwa katulia hivyo, hawezi kusema tena…

Haraka nikapiga magoti,na kumuinamia huyo binti, na machozi yakaanza kunitoka, na muda huo docta akawa kasogea na kusimama nyuma yangu, alikuwa kama haniamini, na mimi nikageuza kichwa kumuangalia docta nikasema;

‘Docta nisaidie nifanye nini..kwani hata sijui kimenitokea nini… mimi mwenyewe najiona kama sio mimi tena…’nikasema

‘Kwahiyo kuna kitu ulitaka kumfanya huyo binti…?’ akaniuliza

‘Hapana sio hivyo docta, sijakusudia kufanya lolote, mimi nilitaka kumsihi tu asiondoke,..ila mimi mwenyewe najihiis sipo kawaida,…mwili wangu umebakia buwa tupu, sina nguvu....nikuambie ukweli mke wangu alikuwa ndio mwili wangu na keshaondoka,…sasa huyo tena..hapana, nisaidie docta…’nikasema.

‘Nikuulize kitu ndugu yangu, jirani yangu, rafiki yangu…, je unampenda huyu binti..?’ aliniuliza swali ambalo sikulitegemea, na ilinifanya nipepese macho, nikashindwa nisema nini, nikawa natikisa kichwa tu,….na hapo akili yangu ikaanza kufikiria nyuma…

Kwanini nisimpende..au….

Binti huyo ni binti aliyejitolea sana kipindi nikiwa na shida, hakuna ambaye angeliweza kunivumilia, ilifikia muda, nilizidiwa, akawa anasafisha na maji, kama kunikanda,..na nikizindukana namtukana , namfukuza..bado akaendelea kunivumilia..

Binti huyu alihakikisha hali chakula, mpaka ahakikishe mimi nimekula, na kama nikikataa, atafanya kila njia ili nile angalau kidogo, nilikuwa nakasirika akinibembeleza mpaka naamua kula kwa hasira…

Binti huyu alihakikisha napata dawa kwa wakati, na mengine mengi….binti huyo alikuwa kipenzi cha mke wangu, akisikia mke wangu ana tatizo, alikuwa wa kwanza kuja kumsaidia…lakini pamoja na hayo, niliwahi kutaka kumdhalilisha…bado aliendelea kujitolea kwa ajili yangu.

‘Oh…nimefanya nini mimi docta, hata sijui nimefanya nini…jamani,lakini sikumgusa kabisa, ..’ nikageuka kumuangalia huyo binti,

‘Ewe binti mtiifu kwangu….ina maana na wewe unataka kunitoka,kama alivyonitoka dada yako, hapana, ..hapana, usiondoke na wewe,nitabakia na nani kwenye hii dunia, nisamehe kwa hayo niliyokutenda, najua hii hali inakutokea kwasababu ya ujianga wangu, kwasababu ya ukipofu wangu…mimi…najua yote ni sababu ya kukufokea, kukukutendea vibaya, lakini bado umeendelea kunijali….

Docta alishika begani, kama kunituliza akasema;

‘Tulia usijali, huyu bint kwasasa yupo salama, ila kwasasa nahisi anakuogopa, …ngoja tusaidiane tumlaze hapo kwenye sofa, na ingelikuwa vyema ukamuacha peke yake kwanza… muache apumzike kwanza…’akasema docta.

‘Hapana docta, siwezi kumuacha, ataondoka huyu, ataniacha peke yangu, ninasema ukweli, ..nampenda sana, nampenda sana docta…, japokuwa hawezi kuziba nafasi ya mke wangu, lakini nimekubali..nimekubali, …nimeitikia wito wa mke wangu, nipo tayari,….docta,….nisaidie docta…’nikasema sasa nikiwa nimesimama na kumng’ang’ania docta.
Docta akatabasamu…akasema;

‘Pamoja na hayo,…ujue una kazi kubwa sana, kazi ya kumshawishi kuwa wewe sasa sio yule …unanielewa hapo…..’akasema docta akigonga gonga mgongoni baada ya kuhakikisha huyo binti kalala vyemaa kwenye sofa.

‘Kwa taarifa yako tu, …nimesikia juu juu, kutoka kwa wife wangu, kuwa huko kijijini watu wengi wanamtaka huyu binti…, sasa kazi kwako , chelewa chelewa utamkuta binti sio wako,…. mimi ninaondoka….’akasema na mimi nikageuka kumuangalia yule binti pale tulipomlaza kwenye sofa, alikuwa akihema kwa mbali…vitita viwili vikipanda na kushuka!

‘Mhh,watu wengi wanamtaka….oh…’nikawa najisema moyoni, sasa hali fulani ya kukosa, hali fulani..ya kutaka …hali fulani kama wivu vikateka nafasi yangu….

Niligeuka kumuangalia docta alikuwa keshaondoka,, nikageuka kumuangalia tena huyo binti, sasa kwa macho ya kipekee, yule binti niliyekuwa nikimchukia,…yule binti ambaye nikimuona hali ya chuki inanipanda, yule binti ambaye nikimuona namuona kama ndiye sababu ya kunikosanisha na mke wangu, sasa sio huyo..ni ajabu kabisa…, kuwa mwanadamu anaweza kubadilika kama kinyonga…

 Sasa moyoni ninajuata,kumbe binti wa watu hakuwa na hata chembe moja ya ubaya niliokuwa nikimdhania mimi..
‘Oh, sasa huyu binti nitamlipa nini….hata kama nitamfanyia nini, sidhani kama naweza kulipa fadhila zake,…na sasa ndio huyo, kijijini anatafutwa kama alimasi…’nikajisemea nafsini mwangu.

Nilikuwa peke yangu na huyo binti nikiyawaza hayo, muda huo alishaondoka, keshaniachia kazi ya kufanya, ..kazi ambayo sasa naiona itakuwa nzito ajabu, nilijiona sasa nipo kama mvulana mdogo mwenye aibu, anayetaka kumposa binti mwenye hadhi, …yupo mbele ya huyo binti, anashindwa hata aseme nini…
 Kwanza cha muhimu nikaona nitii agizo la docta, kuwa nikae mbali na huyu binti, lakini sikutaka kucheza mbali, nia yangu ikawa kutoka nje, na kukaa karibu na mlango, asije akatoka na kuondoka.

Nikachukua begi la huyo binti kuhakikisha nimeliweka mbali, na wakati nafanya hivyo, mara nikasikia huyu binti akimumunya maneno,…ni kama kutaka msaada..nikayakumbuka hayo maneno, aliyatoa mdomoni ni kama ya siku ile nilipotaka kumdhalilisha…na baadaye akatulia, halafu tena akawa anasema kwa sauti ya usingizini..

‘Dada mimi simtaki huyu mtu,…, simtaki…ataniua…’halafu akabakia kimia…

‘Oh….hanitaki mimi au hamtaki nani, na huyo dada yake ni nani, ni mke wangu au…?’ nikasema sasa nikiwa nimenyong’onyea, nikawa kama mtu ambaye sasa anakikosa kitu muhimu sana maishani mwake..nikageuka kumuangalia tena pale alipolala…, alikuwa kalala…uso mwororo, binti mwelekevu..mrembo…oh, ama kweli mtoto huyu aliumbika…eti sasa namuona hivyo…

Nikatoka nje… na wakati ndio nataka kufunga mlango, mara nikasikia sauti
‘Ananibaka ananibaka, njoo nisaidie….niokoe niokoe…simtaki simtaki,….’baadae kukawa kimia, nikageuka kutaka kurudi, lakini nafsi ikanikataza, nikataka kuondoka, lakini nafsi haitaki…..

NB: Naishia hapa naona salio, na muda, tukijaliwa tutamalizia sehemu hiyo ya mwisho, ya mvulana mwenye aibu akitaka kumtongoza binti mwenye hadhi yake..

WAZO LA LEO: Upendo wa kweli hujengeka kutoka moyoni, haijalishi mtu yupoje, haijalishi hali ya mtu, au maumbile yake…wangapi wangapi wameoana, lakini sura au maumbile hayaendani…tunawaona eti wana sura mbaya
Kiukweli…. Tabia njema, kauli na jinsi gani unavyojali watu, huna dharau, uvaaji wako,..maadili mema ya dini , yatakuwa mapambo mema ya kumvuta mwenza wako. Tujitahidi sana kujivika mavazi hayo.


Ewe mola tuongoze kwenye njia sahihi, na utujalia tuwe waja wako wema, Aamin.

Ni mimi: emu-three

No comments :