‘Siwezi kuamini kama nipo nje…, na kuwa nipo hai,…..hadi
hivi sasa nawaangalia watu kwa uwoga, siwezi kuamini kama ingelifikia
hapo..hapana, jamani …ogopeni sana mke wa mtu,….’jamaa yangu alianza
kunisimulia tukio lake ambalo lilimkuta, nilisikia tu watu wakiongea lakini
sikuwa na uhakika.
Jamaa huyu ni mpole sana, mcha mungu,na ni nadra sana kumuonaa
kwenye makundi mabaya, sasa nikasikia hayo yaliyotokea, sikuamini, ikabidi
nifike kwake kumuona, akiwa ndio katoka jela,…kwa dhamana, baada ya kukaa huko
karibu miezi mitatu sasa.
‘Kwani ilikuwaje…?’ nikamuuliza
‘Unajua zamani watu wakisema, ….ni shetani tu kanipitia,
kila wakifanya jambo nilikuwa nawazarau sana na kusema hayo wamejitakia, lakini
sasa limenikuta mimi…na ..hakuna anayeweza kuniamini tena…’ akatulia
‘Maneno mengi mabaya yameshapandikizwa juu yangu,..eti
nilikuwa simba mwenda kimia,..nimejivika
ngozi ya kondoo wakati mimi ni chui, najifanya mcha mungu kumbe ni shetani
aliyevaa miwani ya jua, n kila neno baya limetupiwa kwangu….yaani siwezi hata
kuamini..natamani hata dunia ipasuke nizame chini..’akasema akishika kichwa
‘Hapana usifanye hivyo….’nikasema
‘Sasa nina thamani gani tena..mke niliyempenda keshafungasha
virago, kaenda kwao,..na zaidi kaondoka na watoto….hapa nilipo hata kazi sina
tena, muajiri wangu alishanifukuza kazi …sasa ni mawazo, mawazo na mimi, afya
ndio hii, maana jela sio mchezo, pasikie tu..’akasema
‘Unajua mimi,…najiuliza ni kwanini, ni kwanini ikanitokea
hivyo… ni kwanini watu hawanielewi, ina maana hili tu, ina maana wao hawafanyi
makosa, hawajawahi..yaani hili tu,…ndio limenichafulia jina langu..hapana, …walimwengu
wana hila, wanakuchukia tuu….labda ni kwa vile nilikuwa napendwa na watu kuwa
ni mtu mwema,..labda…mmh,, sasa imetokea hili ndio wameamua kunichafua…’akatulia
‘Mhh,kwani ilikuwaje..?’ nikauliza
‘Kweli nimeamini huo usemi kuwa, ukitaka kumuua mbwa kwanza
umuite majina mabaya…nilishaanza kupakaziwa hayo, kuwa mimi….hata siamini….walikuja
hata kumpandikizia mke wangu kuwa kweli nina tabia hiyo chafu….sasa,..yaani
walishataka kuniua, aliyekuja kunikoa ..ni..ni….’akatulia
‘Kwani ilikuwaje….?’ nikamuuliza
‘Unajua ni huyo mdada, mimi namuitaga madamu,…. alianza
kunizoea sana..mimi nilichukulia poa tu, si jirani yangu, mwenza kibiashara tu
..kumbe nyumba ya pazia kuna jambo linasukwa, sikujua kabisa, na mpaka sasa
sijui ni nani alikuwa nyuma ya hili…., wakati mwingine nahisi ni kama walipanga
ili itokee hivyo, ili wanaiharibie jina na ndoa yangu…’akasema
‘Ehee, kwahiyo … kwahiyo unataka kusema kuwa ulisingiziwa,
..maana nilivyosikia sio mara ya kwanza mlikuwa mkitoka naye,…ndio mkawekewa
mtego, mkanaswa..ndivyo nilivyosikia..’nikasema
‘Ni kweli nilikuwa natoka naye..lakini sivyo kama
walivyosema walimwengu….mimi nilikuwa namsaidia madamu tu, kwenye mambo yake ya
kibiashara, …..’akasema
‘Walisema hilo la kuwa mlikuwa na mambo ya kibiashara mlilitumia
kama kisingizio tu..’nikasema
‘Walimwengu hao….sio kweli,..si kweli kabisa ..naambieje ili
mnielewe…’akasema akionyesha huzuni machoni
‘Sasa ukweli ni upi , hebu tuambie…?’ nikamuuliza
‘Huyu madamu…..siku moja, alikuja kuniomba, nimsaidie
mahesabu yake ya biashara, na alipoona kuwa mimi ni jua mambo hayo ya mahesabu,
ndio akaniomba kuwa niwe naye kwenye biashara zake, ana wateja wake, wakati
mwingine wanakutana kwenye mahoteli, au hata kusafiri, Zanzibar..nchi za
jirani, kwahiyo alihitajia mtu wa kumsaidia,… ambaye san asana anajua mahesabu……kwa
vile mimi najua mambo ya mahesabu, basi nikamkubalia, ..si unajua mambo ya
biashara yalivyo..’akasema
‘Ok..sasa hebu kwanza nikuulize hayo mume wake anajua, kuwa mkewe
yeye ni mfanyabiashara wa kihivyo, au yeye na mume wake wapoje…?’ nikamuuliza
‘Hayo ya familia yao wanajuana wenyewe, ila alinigusia kuwa
yeye na mume wake kuna kutofautiana kidogo, lakini hakupenda sana kuongelea
mambo yake ya ndani,…ila aliniambia kuna muda mume wakealitaka mkewe aachane na
hiyo biashara, lakini madamu alimwambia
mume wake, yeye hawezi kuacha biashara zake kwani walioana akiwa na biashara
zake kama hizo,..
‘Madamu alisema kinachomsumbua mumewe ni wivu, akazidi kusema
mbona yeye hamfuatilii mumewe kwenye mambo yake ya kikazi kwani mumewe kuna
muda anasafiri na anaweza kukaa huko mwezi, na wanakwenda na katibu wake
muhutasi, na huyo katibu wake ni mwanamke, yeye anasema hawezi kumzuia maana
anajua ni mambo ya kikazi na cha muhimu ni kila mtu ajichunge ajue umuhimu wa
ndoa yake....’akasema
‘Lakini sasa sio ndio hivyo wamethibitisha,..kuwa kweli
hamkuwa na mambo ya kibisahara tu, siku hizi kuna utaalamu, kila kitu kimeonyeshwa wazi kwenye kanda za video..’nikasema
‘Ndio maana nasema baada ya hilo, wanadamu hawatanielewa
tena…walimwengu wanachukulia mambo juu, juu tu…, hili ni kama lilipangwa ili
linikute, na dhamira yao itimie, wanimalize...’akasema
‘Alipanga nani sasa, mume wa mke, …au mkewe, na kwanini
wafanye hivyo, ..?’ nikamuuliza
‘Hapo sijui ….sana sana ninaweza kusema labda walitaka
kuniharibia jina langu tu na ndoa yangu,..yawezekana ikawa ni mume ili
kunikomoa na kumkomoa pia mkewe…’akasema
‘Lakini..kwanini …ndio mpaka yatokee mauaji, na mbona mume
mtu nasikia hakuwepo , alisafiri kikazi, je anahusikanaje na hilo…..?’
nikauliza, na jamaa akatikisa kichwa, kuonyesha masikitiko makubwa
‘Yaani inaniuma sana….na inavyoonekana, ni kuwa mimi ndiye
muuaji..lakini sijafanya hivyo,…na mpaka sasa wameshindwa kulithibitisha hilo,kwanini
mimi nifanye hivyo…inaniuma sana, nilishazoeana saana na madamu,…siamini..kwanini.…’akasema
kwa uchungu
‘Ok..hebu elezea ilikuwaje?’ nikamuuliza
‘ Ni hivi, huyo madamu alipokuja kwangu kuniomba nimsaidia
hayo, nilikubali,…lakini kwanza nilimtahadharisha kuwa yeye ni mke wa mtu,
kwanini mumewe asihusishwe, tukaongea pamoja, akasema kila mtu ana mambo yake,
na biashara yake haihusiani sana na mumewe..labda ikibidi..lakini mume wake ana
kazi yake ambayo haimpi nafasi hiyo…’akasema
‘Basi nikakubali, nikawa kweli natoka na huyo mke mtu,
nikawa kama mwenza wake kibiashara, ni kweli alikuwa mfanyabiashara mnzuri tu,
na alikuwa akipata tenda..yaani anakutana na wafanyabiashara wanaohitaji mizigo
mbali mbali, ambayo yeye anaiagiza kutoka nchi za ughaibuni…
‘Ni kweli kwa njia hiyo…., anapata wateja wazuri tu, hata
mimi sikuwa nimeamini hivyo,…basi kwa shughuli hiyo na mimi nikawa naambulia
kipato humo humo..,kuna kipindi hata
mume wake anakuwepo…hasa tukiongelea nyumbani….’akatulia
‘Lakini kiukweli nilihisi.. kuna hisia fulani kwa mume
kwake, hasa akiniona mimi, zilijionyesha
wazi wazi machoni,….nilimuona kama ananiangalia kwa jicho baya, na hata
nikifika kwao kwa ajili ya kukutana na mkewe, akiwa kaniita au kuna mkutanio
fulani, nikimkuta yeye na kumuulizia mkewe, anakuwa kama hapendi, …hanijibu
vyema…’akatulia
‘Basi nikamuelezea mke wake kuwa mume wake anaonekana
hapendi, akiniona nikiongozana na yeye ….mkewe akasema ndivyo mume wake alivyo
niachane naye hayo ni mambo yake ya nyumbani…basi mimi nikaamini hivyo…’akatulia
‘Ok..kabla hujaenda mbali, je wewe na mkeo wako ilikuwaje je
yeye alikuwa hana wasiwasi na wewe, kuwa unakwenda na mke wa mtu kibiashara nk…?’
nikamuuliza
‘Mke wangu alikuwa ananiamini tu, anajua ni katika shughuli
zangu za kibiasahara ,…, siwezi kusema hakuwa na wivu, alikuwa nao..kuna
kipindi nikipigiwa simu, akiona ni huyo madam, anakasirika, analalamika, kuwa
madamu kazidi, ...lakini nilimuelewesha, akawa ananielewa, japo kwa shingo
upande,..na mimi nilijua ni swala la muda tu…na mke wangu hakuwa na chuki kama
niliyoiona kwa huyo mume mtu…’akasema
‘Ok, sasa ikawaje..?’ nikamuuliza
‘Kuna tenda moja, ilikuwa madamu anakutana na wazungu kutoka
Afrika kusini,..hawa walikuwa ni wateja wapia, na mwanzoni tulikutana hoteli
kubwa, baadaye hao wazungu wakasema wanahitaji kuona jinsi jamii yetu ilivyo,
maana biashara hizo zilihusu jamii san asana…, kwahiyo wakaomba twende kwenye
hoteli ndogo ndogo…basi tukafanya hivyo,na tulipofika huko, wakawa wanakunywa
pombe,..mimi hwaga sinywi pombe ..kabisa,..kabisa…’akasema akionyesha kiapo
‘Ehe..lakini nasikia wakati mumefumaniwa wote wawili mlikuwa
mumelewa, au sio…sasa ilikuwaje..?’ nikamuuliza
‘Subiri nikuambie ukweli, mimi sinywi pombe hata mke wangu
analifahamu hilo..siku hiyo, wao ndio walikuwa wakinywa, na madamu, …..madamu
yeye huwa anakunywa, lakini sio kihivyo…siku hiyo sijui ilikuwaje,…alikunywa
sana,..na hao wazungu wakawa wanapiga picha za video huku na kule, wakisema ni
katika mambo ya kujitangaza kibisahara,…mimi sikuipenda ile hali, lakini
ningefanya nini
‘Basi , …ikatokea muda mimi nikaenda maliwatoni…’akatulia
kama anatafakari jambo….
‘Nikiwa huko nikapigiwa simu na mtu nisiyemjua,..ilikuwa
namba ngeni, na nilihisi kama kaigiza sauti, yaweza ikawa …sina uhakika, lakini
ni kama mtu anagiza sauti ya kibabe hivi, akasema;
‘Ndugu yangu jinasue..huyo ni mke wa mtu,….usije ukaja
kujilaumu…’ kabla sijamuuliza akakata simu…
Basi nikatoka pale maliwatoni, …wakati natoka nikawa na
mawazo sana kuhusiana na hiyo simu, ni kama nafsi mbili, moja inaniambia
niondoke, na nisirudi pale mezani na nyingine inaniambia nirudi tu, hakuna
tatizo…
Wakati nawaza, nikawa natembea na nikajikuta nimeshafika
pale mezani, lakini akili , au nafsi ikaniambia niamuage madam, kuwa mimi
naondoka,….
Nikapanga hivyo kweli, na nilipofika mezani kiuungwana,
nakamalizia kinywaji changu- ilikuwa soda, sprite,..nilipoimaliza tu ,
nakumbuka kabisa, hapo nikaanza kuhisi vingine…hapo ninahisi .., waliniwekea
kilevi…sijui ni nani, maana huyo madamu alikuwa kalewa hajitambui,..na hao
wazungu ..sio watu wakufanya hivyo..kabisa, siwezi kuwasingizia..’akatulia
‘Sasa ni nani alifanya hivyo.?’ Nikamuuliza.
NB: Hili ni tukio la ina yake, ni kisa kigeni kabisa, nimeona nikiweka hewani
kabla hakijapoa
WAZO LA LEO: Tuweni
makini sana, na wake au waume za watu, hasa tunapojikuta kwenye maungano au
ukaribu wa aina mambo mbali mbali, yawezekana ikawa ni ya kikazi au ya kibiashara,
kama ni lazima, ya kusafiri au kufanya mambo ya kuwa wawili kati ya wanandoa
tofauti.. .tuhakikishe kuwa tunachukua tahadhari, tukijiuliza hivi mimi
ningefanyiwa hivyo ningekubaliana nalo, na ni vyema kukawa na makubaliano
manzuri kati ya wanandoa. Ni kweli mtu hachungwi, na kila mtu anajua jinsi gani
ya kujilinda, lakini dunia ina mengi… na tukumbuke hisia za watu kwa wenza wao
wa ndoa zipo ndani, wivu hauwezi kukwepeka, ndiyo asili ya mwanadamu ilivyo.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment