Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, October 18, 2016

TOBA YA KWELI-12


Nilipofika nyumbani, sikupoteza muda nikaiendea ile shajara aliyoacha marehemu mke wangu, nikawa naisoma, hatua kwa hatua….na kila hatua ilikuwa ni kama najizidishia mchungu,…

Ikafikia hatua siwezi kujizuia tena…  machozi yakawa yakinilenga lenga…nilishindwa hata nifanye nini..kumbe mke wangu aliteseka sana kwa ajili yangu.., aliyaelezea hayo machungu aliyokuwa akiyapata, .alitoa mfano kwa kusema,’...ilikuwa kama jipu…na mtu analigusa gusa kwa kitu chenye ncha kali..na yalikuwa hayaishi….

Alisema alikuwa hapati usingizi,…maumivu usiku na mchana, akawa anagugumia kwa machungu, na akawa anajitahidi asinionyeshe kuwa anapata hayo maumivu mbele yangu…, akawa usiku halali akimuomba mola wake……ni mateso, kwa mateso, lakini ikafikia mahali akashindwa….

Anasema siku aliposhindwa, alikuwa amepoteza fahamu mara tatu, na kila akizindukana anajipa moyo…lakini ikafika mahali akasema hapana…..siwezi tena, na ilitokea siku hiyo alipohisi kuwa huenda huyo mtoto atakuwa sio sura ya mumewe, ya kuwa huenda mtoto huyo atafanana na docta, yeye alijua kuwa ..mimba hiyo ni ya docta..

‘Nilipoona sura za watoto wa wengine zipo sawa na docta, nikajua na mimi itakuwa hivyo-hivyo.., na mume wangu badala ya furaha atazidi kunichukia zaidi..hapana…siwezi kumuumiza mume wangu zaidi…, ni bora niitoe tu hii mimba…..’akaandika hivyo.

‘Nimeitoa hii mimba, maana sina jinsi, nampenda sana mume wangu, nilitaka nimpatie zawadi japo mtoto wa nje, kama alivyotaka yeye …..lakini nilipenda huyo mtoto aje kufana na mimi ili asije kujua, …ukweli….lakini nahisi, haitakuwa hivyo, nahisi kiumbe cha watu kitazaliwa, na kije kupata taabu, nikiwa sipo duniani..hapana, mungu nisamehe….’akaandika hivyo.

‘Siku hii …sitaweza kuisahau, maana…natenda madhambi, dhambi juu ya dhambi, lakini ni kwanini..mungu wangu ni kwanini…naomba baada ya hili ichukue roho yangu haraka…,..ili nisiendelee kuteseka, ili nisiendelee kumuona mume wangu akipata shida, shida ya kutafuta mtoto….’aliandika.

‘Ninajua…juhudi zake zote hizo, ..za toba nk..si kwa jingine, ni ili tu apate mtoto,..je asipopata huyo mtoto….itakuwaje….itakuwaje..itakuwaje….’aliyarudia hayo maneno nahisi mpaka peni iligoma, maana hayo maneno mengine yakawa hayaonekani vyema…..

Niliendelea kuisoma hiyo shajara, mpaka macho yakaingiza kiza….
 Ilifikia muda nikaishiwa nguvu kabisa, nikajilaza pale sakafuni,…..unajua akili ilikuwa haitaki kukubali, kuwa mke wangu hayupo tena, kuwa mke wangu alikuwa tayari kufa kwa ajili yangu,…ilikuwa nasoma shsjara hiyo ni kama yupo mbele yangu ananisimulia hayo yote.

 Na kuna sehemu aliyandika,…akimsifia na kumshukuru docta…hapo alinifanya nihisi kuwa huenda docta ana mambo mengi zaidi kanificha, na huenda alikuwa ni mpenzi wake wa siri, na kila nikifikia hapo, kumfikiria docta kuwa ni msaliti wangu, najikuta napandwa na jaziba..lakini nikikumbua mateso ya mke wangu, jaziba hizo hunywea…

Sikumbuki nilikaa pale kwa muda gani, ila ninachokumbuka ni kushtuka nikiwa nimeshikwa kwenye unyayo, nikashtuka na kukaa vyema, huku nikihema sana, na mbele yangu alikuwa kachuchumaa yule mdada anayenisaidia akiwa kashikilia sinia la vyakula,

‘Una nini tena shemeji, mbona upo hivi…?’ akaniuliza

‘Wewe weka hilo sinia hapo chini, na ondoka, sina hamu ya kuongea na mtu…sina hamu ya mtu tena mbele yangu..ukitaka ondoka kabisa…..’nikasema na yule binti alifanya hivyo na kuondoka..huyu binti alijaribu sana kuwa karibu name, alijaribu sana kuniliwaza, lakini alikuwa akijua ni wakati gani nipo tayari kuongea na wakatii gani sitaki kuongea, ….mungu alimjalia busara na hekima hiyo.

 Usiku nikaendelea kumuota mke wangu,…tunaongea naye…, mara ananielekeza hiki na kile,…na baadaye akawa ananikumbushia jambo fulani…., lakini nilipozindukana, nakawa nimesahau ni jambo gani alinielekeza nifanya…,..ilinipa shida kuwaza ni jambo gani alinielekeza mke wangu, na ilionekana ni muhimu sana kwake…., na sijui kwanini nilisahau.

Basi wakati nasubiria muda, ili ikibidi niende kwa docta kwa mazungumzo yetu nikapitiwa na usingizi,…na hapo ndio mke wangu akanitokea tena kwenye njozi, na safari hii alikuwa hana raha..

‘Kwanini huna raha…?’ nikamuuliza

‘Kwasababu wewe hutaki niwe na raha…’akasema

‘Nifanye nini ili uwe na raha..?’ nikamuliza

‘Hujatekeleza yale yote uliyoyaahidi,.. wapo jirani zako…umewatendea mabaya, lakini hutaki kuwaomba msamaha…’akasema

‘Ni nani hao..?’ nikamuuliza

‘Ni wale unaowaona ni maadui zako, lakini wamekutendea wema ambao huwezi kuulipa…nenda kabla hujachelewa, timiza dhamira yako ili ufanikiwe unachokitaka, na ili ukipate hicho pia fuata maagizo yangu…’akasema

‘Maagizo gani hayo niyafuate..ni hayo ya kuomba msamaha, au kuna mengine zaidi..…?’ nikauliza na mara nikazindukana kwenye huo usingizi wa mchana-jioni, kumbe ilikuwa simu inaita. Alikuwa docta akisema tayari kesharudi, kama ninaweza kwenda kuonana naye . Sikusubiria, haraka nikakimbilia nyumbani kwake.




***********

‘Docta…samahanini sana..leo nimekuja maalumu,…naomba unisamehe sana…’nikaanza moja kwa moja na kwa kusema hayo huku nikijishusha kupiga magoti, na docta akabakia kushangaa!

‘Nikusamehe! …kwani vipi tena….nakumbuka tulishamalizana…au kuna jingine…?’akasema

‘Hapana, ….hatujamalizana…sizani kama umenisamehe…’nikasema huku nikitembea kwa magoti kuelekea pale alipokuwa…, nikamuona anatoa macho ya kushangaa,  hakunigusa akaniacha vile vile na kugeuka kuangalia dirishani,halafu akasema;

‘Unajua sijakuelewa….’akasema

‘Nisamahe sana kwa hayo niliyokufanyia…najua hutaelewa,,..lakini mimi nimeshakuwa mtu mwingine, nisamehe sana, nipo chini ya miguu yako…bila msamaha wako bado nitakuwa sijatimiza dhamira yangu…’nilisema huku nikitembea kwa magoti,..na docta akageuka kuniangalia, akanitizama kwa muda, baadaye akanishika begani na kusema;

‘Siamini….unajua kiukweli moyoni nilikuwa nateseka,… sijui umejuaje, ni kweli nilikuwa najaribu kukusamehe, lakini nilikuwa najiuliza, je wewe umgundua kosa lako…oh,..utamsameheje mtu ambaye hajui kama katenda kosa,..oh, kwa hilo nisamehe na mimi..’akasema na yeye sasa akinipiga magoti.

‘Wewe hujanikosea kitu docta hustahiki kunipigia magoti mimi,…’nikasema na sote tukashikana na kusimama, tulikumbatiaa kwa muda,..na yeye akanielekeza kwenye kiti nikaa, akasema

‘Ni kweli, nilijiuliza sana, hivi kweli mimi nilichofanya nilikukosea, ni kwanini baada ya yote hayo bado ulikuwa hujanishukuru ...ninajua ni wajibu wetu sisi madakitari,  sisi kama madakitari kazi yetu ni kutimiza kile mola alichotujalia, na …hatuhitaji shukurani..lakini mimi nilifanya hayo zaidi ya dakitari kwa mke wako na kwa nia safi kabisa…huwezi kulielewa hilo mpaka uiweke nfsi yako mahali pangu!

‘Docta nimekuelewa, nakuomba tena na tena unisamehe, na ninashukuru sana kwa wema wako huo….’nikasema

Anyaway…nashukuruu sana, kwa hio,na mimi ..sasa moyo wangu umetulia…’akasema docta.

‘Nashukuru sana na nipo tayari kufanya lolote lile docta, niambie ni gharama gani nikulipe, japokuwa sitaweza kutimiza, fadhila ulizonifanyia, lakini angalau nitakupunguzia machungu na hasara, na naahidi mola akinijalia, nitakutafutia na kukulipa, ….ili tu moyo wako uridhike…’nikasema.

‘Mimi sasa sina kinyongo na wewe, na sina gharama zozote kwako, nilichofanya ni kwa mapenzi ya ujirani mwema, na mkeo alikuwa rafiki yangu, hilo siwezi kukuficha, lakini sio urafiki wa kimapenzi, unielewe hapo, urafiki wangu wa kimapenzi uliisha pale wewe na yeye mlipofunga ndoa…’akasema

‘Nimekuelewa docta…’nikasema

‘Sasa mhh..pamoja na hayo, kuna kitu nakuomba,…ni  mambo mawili tu, ninajua wewe ndiye wa kunisaidia, hakuna mwingine anayeweza hilo…’akasema

‘Sawa kabisa docta mimi, nipo kwa ajili yako, nitafanya chochote, ilimradi,..eeh, yaani wewe niambie tu, ilimradi unisamehe…’nikasema

‘Sawa kabisa,..…, la kwanza ukilitimiza hilo…ndio, nitakuja kukuambia la pili..naomba sana unisaidia kwa moyo wako wote, maana sina namna nyingine,..’akasema docta.

‘Mimi nipo tayari docta,..nimeshaahidi…, niambie ni mambo gani hayo…?’ nikasema kwa kujiamini.

‘Kwanza ninataka wewe…uende,…ukamshawishi mke wangu arudi nyumbani,… turudiane mimi na yeye…, unajua baada ya yote haya, niliachana naye, yeye kwa hasira aliamua kurudi kwao, akasema mimi na yeye basi, na alipofika huko akaongea na baba yake , baba yake akanipigia simu na kunihoji, nilijielezea, lakini mzee akaona mimi nina makosa, na alisema niachane na binti yake kwa amani, na nisije kukanyaga nyumbani kwake tena....’akasema kwa sauti yenye huzuni.

‘ Docta, unasema nini,….sikukusikia vyema, ....unajua pamoja na hayo yaliyotokea mimi..mi- mbona sina mazoea sana na mke wako, … yaani ilitokea tu siku zile, mke wako ni mkali sana, sijui hata siku ile ilikuwaje, …nilichukulia hasira zake na kumshawishi, samahani sana….’nikatulia

‘Hayo sawa nimeyakubali,..yasahafanyika, sasa ombo langu ni hilo….’akasema

‘Docta….mkeo, ooh, mbona kama sijakusikia vyema , unajua baada ya lile tukio, mkeo …alijisikia vibaya sana na akawa hataki hata kunitizama usoni,..alilia sana siku ile…na alisema hataki kuniona tena…., hujui kilichotokea baadaye siku ile, hapana…’nikasema.

‘Ninajua na nina uhakika, wewe ukikutana naye ukamwambia ukweli atakuamini, akijua kuwa kweli mimi sina makosa….. , mimi na mke wako ilikuwa ni kazi ya udakitari tu …muhimu umwambia ukweli, nina imani atakubali kurejea, mimi siwezi kukutana na baba mkwe, najua alivyo, ila wewe hili ni jukumu lako, ni wewe, ulisababisha haya yote…’akasema docta

‘Mimiii…., hapana docta, we-we- we-we…kwanza nitaanzaje, hapana docta..hilo siliwezi, ..kabisa kabisa, siku ile angeliniua,..unajua baada ya ….ilibidi nikimbie, wewe hujui tu,…oh, hapana docta, mengine sawa lakini sio kwenda kuonana na hiyo familia, halafu baba yake wewe si unamfahamu vyema,…, alivyo mkali, anaweza kuniua,….nimekuahidi kuwa nitafanya lolote lile ilimradi unisamehe, lakini kwa hili hapana…’nikasema nikitikisa kichwa kukataa..

‘Ahadi ni deni, na ukumbuke dhamira yako….huna budi kufanya hilo, vinginevyo nami, …sijui kama nitaweza kukusamehe, sijui kama nitaweza kuku…ambia hilo jambo la pili,…ukifanikiwa hilo ombi langu,ukafanikiwa mke wangu akarudi hapa,… basi na mimi nitakuja kukuambia hilo la kwako, na utakuwa umetimiza dhamira yako, nina uhaika huo.., kama uliweza kumuhadaa mke wangu,…mkafanya mlichofanya, kwanini sasa uogope hili, eeh, wewe si kidume…’akasema docta.

‘Kwahiyo docta unataka kusema nini, unataka mimi…nifanyeje…siwezi docta,…nitamuanzaje kwanza,…kwanza nitafikaje kwenye hiyo familia….unanitakia mema kweli wewe….mmh, wewe mwenyewe unaogopa, ndio unanisakizia mimi….hapana, tutafute mtu mwingine, sio mimi, kwanini mimi…ili nikauliwe au?’ ..nikasema na mara simu yake ikaita, akaipokea … , alipomaliza kuongea na hiyo simu akasema;

‘Siwezi kuongea na wewe jambo jingine kwasasa, hapa kichwa kimechoka, unasikia wananiita huko kazini, kuna dharura tena, kuna mgonjwa mahututi kaletwa, hapa nyumbani kuna mambo kibao ya kufanya, hapa sasa ndio naona umuhimu wa mke angelikuwa hapa nyumbani, ..ooh, yaani sasa hivi naiona nyumba kama hema tu, haina raha, kisa ni nini…’akasema akiniangalia machoni

‘Nisamehe sana docta hilo mimi sitaliweza kulifanya…. , kabisa kabisa, hapana, unataka nikauwawe…wewe mwenyewe unawafahamu hao watu, mmh hapana….’nikasema nikitikisa kichwa na kutoa ishara kwa mikono.

‘Mimi ninachokuaomba, wewe, eeh,… katimize hilo, maana ni muhimu sana kwangu, na kwako…hapa kichwa kinaniuma, ninawaza sana, nifanyeje mke wangu arudi, hakujua hili, na alishahadaika na- na, na… wewe, mmh, kichwa kinauma kweli, ‘akasema akishika kichwa

‘Pole sana docta lakini….’nikataka kusema lakini akaniwahi kwa kusema;

‘Ha…hahaha, docta hajigangi au sio…, najua unataka kusema nini, ..lakini najua dawa yangu,.. dawa yangu ni mke wangu….ukinisaidia hilo,  mengine yatafuata, namuomba mungu tu, anipe uzima, ili niweze kukuambia hilo la pili na hilo kwako ni muhimu sana kama ilivyo kwangu kumrejesha mke wangu hapa nyumbani….nisaidie , name nikusaidie…’akasema.

‘Mhh….lakini haiwezekani docta,  nitawezaje kukutana na mkeo..nimeshakuambia mimi siwezi, siwezi siwezi…. alisema hataki kuniona kabisa kwenye macho yake, hataki hataki…sasa wataka mimi nikafanyeje…’nikasema nikiwa sijui nifanyeje…

‘Fanya ufanyalo…..mimi sijui…’docta akasema na sasa akawa anajiandaa kuondoka, na mimi ikabidi niondoke.

Nilifika nyumbani kwangu, nikiliwazia hilo,…kwakweli, kwa hilo nilishindwa kabisa, najua kwenda huko ni sawa na kujipeleka kwenye mdomo wa mamba, nakumbuka siku ile…alisema nisije kukanyaga kwake, na akasema atamwambia baba yake kuwa mimi ndiye nilijenga fitina,..baba yake alikuja kuambiwa, na mzee huyo akasema wazi wazi, kuwa, siku nikukutana naye atajua ni nini cha kunifanya.

‘Mzee, ni, ni shetani tu alinihadaa, alitufanya tuamini hivyo..lakini hata binti yako, anajua kuwa mume wake ana mahusiano na mke wangu, na ilikuwa….’nikasema na mzee huyo akanikatiza kwenye simu na kusema;

‘Nasikia wewe unajifanya una hasira sana,….sasa mimi zangu hazina kikomo na nikiahidi kitu ni lazima nikitimize, nataa tukutane mimi na wewe, tuone ni nani zaidi, wewe si kidume sio, basi mimi ni zaidi yako,….unasikia, umemuharibia mke wangu ndoa yake, ..wewe na huyo mshenzi wako anayejiita docta, mtanitamabua,..’akakata simu.

‘Hivyo ndivyo ilivyokuwa rafiki yangu, sio kwamba nilikataa kwenda kwasababu ya aibu, hapana, nilijua kabisa huko,  kuna hatari , wanaomfahamu huyo mzee wanaweza kukusimulia visa vyake, yaani siku ile niliishiwa nguvu kabisa, nikajua sasa nimeshindwa
‘Sasa nifanyeje,…’nikawa najiuliza, na mara mlango wangu ukagongwa….

NB: Nikuache hapa kwanza nisimalizie yote…kwa leo ili utafakari kidogo, hebu jiulize haya maswali kwanza, je ilikuwaje, na je docta anataka kumwambia nini huyu jamaa kama jambo la pili,  na je huyu jamaa ataweza kwenda huko anapotaka kwenda, na hata akienda labda…. kweli atafanikiwa, na je kama hatafanikiwa itakuwaje…?

WAZO LA LEO: Kukoseana kupo, kama binadamu hatuwezi kuwa sawa, kuna kusigishana kwa hapa na pale. Maudhi...kutofautiana, , na hata kufikia kuwekeana visasi kwa sababu mbali mbali..lakini tujiulize, kwa kufanya hivyo tunapata faida gani….kama unaona kuna faida…sijui…., sawa, lakini jiulize tena je mungu analirizia hilo, au ni mambo ya kidunia tu…hii ni dunia tu dugu yangu…, wapo walifanya hivyo, wababe , wana pesa, watawala nk…lakini sasa wapo wapi..na huenda wanapambana na adhabu kubwa na wanajuta, wanatamani warudi duniani , lakini  haiwezekani tena…tukumbuke jambo moja muhimu:

Kusameheana kuna thamani kubwa sana kuliko kinyume chake!
Ni mimi: emu-three

No comments :