Kilio cha mtoto kilinifanya nisimame,..kwangu mimi mtoto
akilia, nahisi moyo ukiumia, maana najua mtoto mdogo kama huyo akilia anataka
kutoa ujumbe wake umfikie mtu..hawezi kuongea kwa umri huo, kilio chake ndio
ishara yake ya maongezi.
Kwa haraka nikamgeukia Yule mama, aliyekuwa kambeba huyo
mtoto…Alikuwa ni hawa akina mama wanaouza mihogo mibichi barabarani, na kwa
muda ule alikuwa na sinia lilipangwa mihogo mibichi, kichwani mwake, na mkono
mwingine kashika muhogo ulibakia nusu, na mwingine kashikilia kisu. Ni hawa wajasiriamali
wa barabarani, ukitaka muhogo mbichi anakukatia kipande kutegemeana na pesa
yako. Anapata riziki yake halali…
Nilisogea hadi kwa Yule mama, kwa muda huo alikuwa
akihangaika kuulizia wateja, abiria waliokuwa kwenye daladala, kama kuna mtu
anayetaka muhogo, mimi nikawa sasa nipo nyuma yake karibu sana na yeye, nikawa najaribu kumchekesha Yule mtoto ili
aache kulia…
‘Toto nyamazaee…’nikasema na sauti hiyo ikamfanya huyo mama
ageuke, na kuniangalia
‘Nikukatie wa shilingi ngapi…?’ akaniuliza
‘Mtoto analia…na kwa jinsi ulivyombeba , na nguo
ulizomvalisha na kwa hali hii ya hewa utamuathiri kiafya…’nikasema..ni kweli
mtoto alibebwa kwa kitenge kilichochanika na kama kafungwa mgongoni, na
asilimia kubwa ya mtoto yupo uchi.
‘Nikukatia wa shilingi ngapi…?’ akaniuliza sasa akiwa anataka
kuanza kukata kipande.
‘Mia mbili…’nikasema na kwa haraka aka-kata kipande kidogo,
kiukweli sikuwa na haja ya muhogo, huruma
yangu ilikuwa kwa Yule mtoto. Alipomaliza kukata kile kipande akaanza kukimenya.
‘Mtoto analia sana, muonee huruma…’nikasema , yeye wakati
huo anasubiria nimkabidhi pesa.
‘Nikimuonea huruma atakula nini….acha alie akichoka
atanyamaza, kwani kulia kaanza leo… au wewe unajua maisha ya huyu mtoto….kwani
wengine wanaumwa huko wananitegemea…’akasema huku akiniangalia kwa macho
yaliyojaa chuki. Uso umeumbwa kwa aina yake, uso unaweza ukaelezea kile kichomo
moyoni mwa mtu.
‘Kwanini unaonekana una chuki hivyo, mimi ni mteja wako
watakiwa uninyenyekee au sio..?’ nikasema
‘Kwasababu nawachukua sana wanaume…’akasema hapo hata wale
wanaume waliokuwepo pembeni waligeuka kumuangalia, na mmoja akasema
‘Ukiwachukia wanaume ujue unamchukua hata baba yako mzazi…’wakasema
‘Kauli yangu ni hiyo hiyo, nawachukia sana wanaume, habari
ndio hiyo, wewe nipe pesa yangu…’akasema na mimi nikatoa noti ya elifu moja
nikampa, akanitupia jicho kama kutaka kusema , kwanini nanunua kipande kidogo,
kumsumbua kutafuta chenji.
‘Usijali hiyo chenji ni ya mtoto…’nikasema , hapo akanitupia
jicho tena, na mmoja wa watu akasema,;
‘Haya huyo ni mwanaume …kataa hiyo pesa anyokupatia…’sauti
ikasema
‘Siwezi kukataa maana haya madhila yote ninayoyapata kisa ni
wanaume..unamuona huyu mtoto, baba yake alimkataa, wakati yeye ndiye aliyeni…..’akasita,
halafu akaendelea kusema
‘Anadai kuwa huyu mtoto sio wa kwake, wakati anafanana na huyo
mwanaume kwa kila kitu, na mimi sikuwahi kumjua mwanaume mwingine zaidi yake,…yeye
ndiye aliyenifanya nifukuzwe shule…akiniahidi atanioa….’akawa anabadili sauti
kama anataka kulia.
‘Sasa hilo utamlaumu nani, kwanini ulikubali , si kwa ujinga
wako, kwani alikubaka, wewe si uliona ni peremende, …kwanza wewe yaonekana
ulikuwa mapepe, mtoto wa shule unatembea na wanaume wakubwa….’mmoja wa wauza
vitu barabarani akasema.
‘Nilikuwa mapepe mimi hebu uliza..huyo mwanaume alikuwa
mwalimu wangu…, hebu fikiria mwalimu wa shule… na mimi nilikuwa mwanafunzi
wake, msitake niongee ambayo sikutaka kuyaongea. …’akasema, na kuanza kuondoka.
Mimi niliingiwa na hamu sana ya kutaka kujua ni masahibu
gani yaliyompata huyo mdada, nikaahidi kumtafuta.
Hutaamini jioni wakati narudi toka kwenye mishughuliko
yangu, nikakutana na huyo mdada kwenye treni, bila ajizi nikajitambulisha kwake
na kumuuliza, maisha yake ya nyuma, …mdada Yule alikuwa katulia,..niliona kama
macho yamevimba..alikuwa analia, na nilipomuuliza kulikoni, ikawa kama
nimejichongea, akaanza kulia kwa kwikwi, nikabakia nimeshangaa.
‘Mbona unalia..?’ nikamuuliza
‘Bibi yangu amefariki..bibi ambaye ndiye alikuwa baba na
mama yangu, na juhudi zote za kuuza mihogo, ni kuhakikisha napata pesa ya
kwenda kumtibia, sasa amekufa…….siwezi kuamini, ..kwanini dunia hii
inanieleleza, sasa sina baba, sina mama, sina hata mlezi,….nitaishi na nani…nitakwendaje
kumzika bibi yangu, wakati hata pesa kidogo niliyokusanya leo wameniibia…’akasema
akilia
‘Wamekuibiaje…?’ mmoja akauliza
‘Nilijua tu…kuna tatizo, ..’akasema akitikisa kichwa
Haya jamani sijui bado mnahitajia visa vyangu, hiki kingina
kinaitwa kisa cha ….
‘Kisa cha binti yatima….’
Hiki ni moja ya kisa
cha haraka nilichokipata jana, na sikupenda kukilaza, nikakiingiza kwenye
shajara yangu, japokuwa kwakweli kinasikitisha,…nilijaribu kukiandika kwenye
simu, lakini sikuweza kuendelea, simu iliisha mfuta, chaji , sikukata tamaa!Lakini
huo ndio utangulizi wake, na tukijaliwa tutakiendeleza
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment