Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, September 19, 2016

KISA CHA BINTI YATIMA-'KWANINI MIMI...'-3


‘Siogopi kuyasimulia maisha ya baba yangu, …maana maisha yake yamekuwa ni funzo pale kijijini kwetu..alipewa majina mengi, mzee tupa tupa…mzee wa matumizi, havinipiti…nk…, kila mmoja amekuwa akiyatolea mfano hayo maisha yake…, hasa pale mzazi anapomuona mtoto wake anapotea, anakuwa mlevi, Malaya..au ana uchu wa madaraka, au kama hamtunzi mkewe, basi watu hutolea mfano kwa maisha hayo ya baba..kwahiyo hata nisipoongea mimi leo…, yameshaongelewa sana…mungu amsamehe tu baba yangu huko alipo…’akasema

Aliposema hivyo huyo binti, niliingia na hamu sana ya kujua maisha ya baba yake yalikuwaje japokuwa nia yangu ilikuwa ni kujua mambo yanayomuhusu huyu binti…kwani na muda nao ulikuwa hautoshi..

‘Kwani maisha ya baba yako yalikuwaje,...?’ nikamuuliza

‘Baba…mmh…we acha tu nyie wanaume ….sijui kama nitakuja kuwasamehe…’akasema

‘Usijali yote maisha…’nikasema

‘Yote maisha …hahaha..haya ya binti yatima yalizidi kiasi….maana ni kizalia…we acha tu…’akasema

‘Sawa hebu tugusie kidogo kuhusu huyo baba yako,…alikuwa chama gani vile…hahaha, hayo ya chama yaache, usije kuleta sintofahamu….hebu tuelezee alivyokuwa, ili tumfahamu, maana yaonekana chuki zako zimeanzia huko…’akasema jamaa mmoja.

********** tuendelee na kisa chetu*******

Kwanza binti aliinama chini kama anawaza jambo, halafu akainua kichwa na kuanza kuongea, alikuwa akiongea kwa haraka haraka, kama mtu aliyekaririshwa hayo maneno, na ilikuwa kama anaivuta hiyo habari kichani mwake, na kuiona mbele yake…

 ‘Baba yangu alikuwa mtu mkubwa sana enzi hizo, nikiwa na maana pale kwetu kijijini… unajua baba alianzia kuanzia kufanya kazi kwenye wizara..akiwa mkuruguenzi fulani.., akaja kugombea ubunge, akapata, baadaye akawa mkuu wa mkoa sijui akawa nani tena, kusoma raha…na ukiwa mjanja kwenye kuongea mdomoni, kushawishi watu baba alikuwa hajambo….

Lakini pamoja na hayo, watu wengi walimfahamu, kutokana na tabia yake, ya kujiona, na hata kunata kuwa, ana pesa, na ni kiongozi, amesoma, mtoaji imla, fanya, ni lazima ufanye, hata kama kuna sababu za msingi za kutokufanyika….ni kweli alisoma, maana niliwahi kuiona vyeti vyake,….alisomea hiki akamaliza , akaja kusomea hiki, yaani alikuwa kasomea nyanja tofauto tofauti….kiasi kwamba ilishindikana awekwe wapi…

Tatizo ni hilo, tamaa, kupenda ukubwa, na kutaka afanye apendavyo..kwasababu yeye si kasoma bwana, anajua zaidi.., na ikafikia sasa anatumia  mali ya umma kama yake…, unajua tena….lakini cha zaidi ambacho ilikuwa ni sifa yake, ilikuwa ni hiyo tabia ya kubadili wanawake kama nguo, madaraka yana mitihani yake…’akasema.

Hakujali kuwa ana mke,..na mama alikuwa mke mremboo tu, alikuwa na Tabia njema, mtulivu…kila mmoja alimsifia kwa tabia yake hiyo, na wengi walimsikitikia kwanini aliolewa na baba, wengine wakamzihaki kuwa kakubali kuolewa kwa ajili ya pesa…ndio hivyo…mama alishinikizwa na wazazi hakupenda,…na hakuwa na jinsi….’akasema

‘Sasa kwanini mama yako alikubali, au alilazimishwa…?’ akaulizwa

‘Hivi hamkunielewa,…..sirudii tena….’akasema kwa hasira

‘ok….sawa endelea…hakuwa na jinsi, …tunmekuelewa…’nikasema

‘Kwa tabia hiyo ya baba, mama hakutulia, alijaribu kumkanya baba kila awezavyo, lakini baba hakusikia,..na hata alifikia kumpigwa mama mara kwa mara, na akaambiwa kama hataki kuishi naye, njia ipo nyeupe aondoke kwao.

Unajua tena maisha ya kijijini, ukishaolewa, umeolewa,…mama ilibidi avumilie tu, lakini ikafika muda, mama akaamua kuondoka na kuachana na baba,…sijui kwanini mama hakuweza kusimamia kwenye uamuzi wake huo,…’hapo akatulia kidogo.

‘Angewezaje, …wazazi wa mama ndio akina mie..hawakuwa na uwezo ukilinganisha na familia ya akina baba, …baba yake naye ndio hao wazee wanaopenda kuwafanya watoto wao kama mtaji, kila kitu sawa bwana mkubwa, …na babu kila akiwa na shida, akitaka pesa za kulewea anamuendea mkwewe, hapo mama angefanya nini….lakini ikafikia muda mama naye yakamfika shingoni, akachukua furushi la nguo zake akaondoka.

‘Kwenda wapi…?’ akauliza mtu mmoja

‘Kwenda wapi…tatizo lenu nyie wanaume mkio, mnahisi kuwa mke hana pa kwenda, ukishamuoa ni mtumwa wako…. mama alikuwa na kwao, sema tu….ndio mfumo dume…mwanamke anachukuliwa kama hana kwao tena, yeye ni mtumwa kwako si ndio hivyo....nyie watu nyie…’akasema

‘Ndio maana huolewi, ukiwa na imani hiyo…’akaropoka mtu mmoja, na mdada akageuka kumuangalia, na mimi nikasema;

‘Wewe endelea usimsikilize huyo…..’ nikasema

‘Nyie acheni tu…..’akatulia kidogo

Kufika nyumbani anakuta ugomvi wa baba na mama…mama analia kivyake, babu anarudi kila siku mlevi, akirudi ni kipigo kwa bibi….mama akasimama mlangoni, akijiuliza afanye nini, arudi alipotoka au …..

‘Na wewe umefuata nini…’ilikuwa kauli ya babu akiwa bwiiii…

 Mama akajaribu kujieleza, lakini nani angemsikiliza, hata kama bibi alimuelewa mama…, lakini ni nani mwenye usemi hapo nyumbani, ni babu, na babu ndio huyo, mtumwa wa baba’ngu, baba yangu ndiye alikuwa mfadhili wa babu, kwahiyo kila alichosema mama hakikusikilizwa, mama akaonekana hana maana, akafukuzwa usiku huo huo arudi kwa mumewe.

‘Mama yako akarudi, mama yake hakumtetea…?’ akaulizwa

 ‘Bibi…hahaha hivi nyie mnawafahamu wazee wa zamani …waume kwao ni ….ni kama afande, amri moja,….bibi alijitahidi lkini wapi,…. mama akabidi arudi kwa mumewe…, ….angefanya nini, na aliporudi akakuta mlango umefungwa ikabidi alale nje, hadi mume wake aliporudi na hawara wake,…maana baba alijua mama hayupo, mama siku hiyo alilala chumba cha wageni, na baba alipogundua mama yupo akajivunga, akamrudisha huyo hawara wake wakaenda kulala , walipolala…uone ni kwanini nikukuambia nawachukia nyie watu msione nawaonea….’akatulia.

‘Bibi anasema mama alikuwa kama mtumwa, baba akirudi amelewa, anatapika ovyo, wakati mwingine anapitiwa na haja..si unajua tena walevi..basi mama kazi yake kumfulia nguo…yaani bibi akikuhadithia , utatamani ulie…lakini mama alivumulia, si mume wake bwana, na keshaambiwa na wazazi wake hakuna kurudi nyumbani ….’akatulia.

‘Sasa ilikuwaje bibi yako huyo, akaja kuishi kwa mama yako….?’ Nikamuuliza

‘Nitakuelezea ni kwanini…..’akasema

‘Basi mama akawa anaishi na baba hivyo hivyo, ikafikia hatua , baba anawaleta wanawake hadi nyumbani, haogopi tena…mama akaona imezidi akaenda kushitaki kwa wazazi wa mume…wewewe…ndio alijichongea,..huko ndio kukawa kubaya zaidi aheri hata kwao…kwanza alianza kuambiwa yeye ni nuksi, yeye ndiye kamuharibu mume wake, ikafikia hatua kuambiwa yeye ni mchawi…..’akatulia akitikisa kichwa.

‘Bibi yangu alikuja kuishi na wazazi wangu, baada ya babu yangu kufariki, babu alipofariki, bibi akafukuzwa kwenye makazi ya hiyo familia,..akawa hana pa kwenda, basi mama akamchukua waishi naye, baba hakupinga …na huyu bibi ndiye aliyekuja kuwasaidia sana wazazi wangu hasa kipindi baba anaumwa, yeye na mama wakawa wanahangaika huko na kule, hata kutafuta riziki…maana ndugu wa mume walipoona baba hana kazi tena, anaumwa, hawamkujali tena..’akatulia.

Bibi anasema baba enzi zake, alikuwa hawajali ndugu zake, ndio maana na wao walikuwa kama wametenga kifulani hivi…walisema baba ana majivuno,na zarau…na hakupenda kuwasaidia ndugu zake, hata hivyo, walimuheshimukipindi hicho  kwasababu ya pesa, na alikuwa kiongozi, …

‘Bibi anasema baba alianza kuumwa siku alipofukuzwa kazi….kwani kulipita uchunguzi wa wakaguzi hapo kazini, wakagundua kuwa kuna ufujaji wa mali na pesa kupotea, na mwisho wa siku wakasema baba ndiye aliyefanya yote hayo, akasimamishwa kazi.

 Siku baba alipopokea taarifa hiyo, akapoteza fahamu..na tatizo likaanzia hapo, sio kwamba hakuwa anaumwa kabla, alishaanza kuumwa umwa, magonjwa mengi tu, na alikuja kujijua tatizo nini…., lakini hakusema kwa mtu, akawa anaendelea na tabia yake ya kuwaharibu mabinti wa wenzake, lakini mungu hamfichi mnafiki

Siku ikafika,…muda mungu aliouweka wa mwanadamu ni mfupi tu… alipopokea taarifa hiyo kuwa kasimamishwa alikuwa na kimada…walikuwa kwenye hoteli,wameshatumia vya kutosha, na hawajalipa….anatarajia akifika kazini achote, taarifa inakuja, hana kazi, na haruhusiwi kuingia ofisini,..ilikuwa ‘surprise..’

Alidondoka….akapoteza fahamu , na tatizo likazua tatizo jingine….utajiri, cheo ..majigambo yakaishia hapo, ..
Akiwa nyumbani hana kazi, ..ana madeni kila kona..ikafiki mahali magari yakapigwa mnada…nyumba, maana alikuwa na zaidi ya nyumba tano hivi……wakabakiwa na kibanda tu,..kile walichoanzia maisha ya mama, hutaamini ilifikia muda wakageuka kuwa omba omba….waliishiwa kabisa...ikawa inahitajika tiba ya baba, hakuna pesa wafanyeje, kazi ikawa kuomba, na kazi hiyo waliifanya bibi na mama yangu….baadaye siku yake ikafika, akafa akiwa hana thamani….mungu amsamehe tu..lkn nyie waume mlio hai siwapendi, …


WAZO LA LEO: Ukiwa na cheo, ukawa na uwezo wako, usijivike kilemba cha majigambo, ukajitanda nguo ya dharau, ukavaa joho la kiburi...ukumbuke hayo yote ni mapambo ya dunia tu, yana mwisho wake, wapo walikuwa navyo na sasa hawapo tena duniani,…na wapo walikuwa navyo, vikageuka kuwa sumu …muhimu, tumshukuru mungu kwa neema hizo kwa kuwajali wenzetu, tuwasaidie kuwainua, tujenge jina nzuri la wema, maana hata tukifa bado majina yetu yataendelee kuwa hai kwa matendo hayo mema.

Ni mimi: emu-three

2 comments :

Anonymous said...

A GUD STORY, LET HAVE A MOVIE ON IT..Unasemaje

Anonymous said...

oh....inaendelea lini