Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, August 5, 2016

TOBA YA KWELI-9



Niliachana na dakitari yule hasimu wangu, nikatoka ofisini kwake na kuelekea chumba alicholazwa mke wangu, moyoni nikiwa tayari nimeshajaa mawimbi ya hasira, na mimi nikishaingiwa na hasira nakuwa kama mtu aliyechanganyikiwa..yale maneno ya dakitari yaliniumiza sana moyo wangu..

‘Ni kosa la nani….?’


‘Ufahamu!…ufahamu wako ni mdogo sana….


Huyu mtu ananidharau mimi..kwa vile yeye ni dakitari ananiona mimi sina ….haiwezekani …ni lazima nitamuonyesha kuwa mimi nina akili zaidi yake..ngoja nimalizane na mke wangu, nikitoka huko nitamrudia, ..yaani haiwezekani..’akilini mwangu nilikuwa nachemka,..hadi nikafika mlango wa kuingilia, bila hata kujijua…nikajikuta nimeshaingia kwenye hicho chumba alicholazwa mke wangu.

‘Paaah….’moyo ulishtuka!

Na pale nilipoingia chumba alicholazwa mke wangu, nilipatwa na mshituko, …wasiwasi na mashaka vikaugubika ubongo wangu, na kwa ile hali ya hospitalini, na kile chumba kilivyo, ghafla hata lile wimbi la hasira likaondoka, na huruma ya kibinadamu ikaanza kuniingia!.

Nilitupa jicho mbele yangu pale kilipotakiwa kuwepo kitanda,…..nikabakia nimeduwaa,…mmh, ..haiwezekani…macho yaliona lakini ubongo haukutaka kukubali nafsi ilisema vingine..haiwezekani...

Pale kwenye kitanda kumezungushiwa uzio, mapazia, na ile ilikuwa na ishara nyingine, ..

‘Haiwezekani..’nikasema huku mwili ukianza kuishiwa nguvu.
Sikuweza kusogea,…wasiwasi ukanisonga….woga, mashaka….na hata majuto…
            Tuendelee na kisa chetu
                                         *******
Kwanza nilisimama nikawa nimeduwaa tu..na mara nikaona mtikisiko fulani kwenye lile pazia,..nikakodoa macho kuhakikisha…na mara nikaona mtikisiko ule ukizidi,..na mara, akatokea nesi akiwa kashika beseni likiwa na vifaa …mara akatokea dakitari.

Nikapumua kwa nguvu, lakini bado …maana lile pazia lilikuwa halijaondolewa, yawezekana, walikuwa wakimuweka sawa…mmh, niliogopa hata kulitamka hilo neno..
‘Hapana haiwezekani..’nikajikuta nimesema kwa sauti.

 Mara Yule dakitari akaniona,…na haikupita muda wote wawili wakaanza kulisogeza lile pazia lilokuwa limezunguka kitanda, ..na kitanda sasa kikawa kinaonekana na mtu kalala pale kitandani,akili ikawa inajiuliza je huyo mtu ni mzima au….

‘Oh…nani kakuambia uingie..’Ilikuwa sauti ya dakitari iliyonishtua, toka kwenye dimbwi la mawazo na mashaka.

‘Ni- ni..dakitari mkuu…kaniambia naweza kuja kuonana na mke wangu, …’nikasema

‘Haiwezekani….lakini sawa hata hivyo nimemalizana naye, anasubiria …upasuaji tu…’akasema

‘Upasuaji! Upasuaji wanini,..? Kwani mke wangu anaumwa nini…?’ nikauliza na Yule dakitari hakusema kitu,…akanipita na kuanza kuondoka bila kunijibu kitu, kitu ambacho kinifanya nizidi kuwa na mashaka, na nesi akatabasamu naye akiwa anataka kunipita , akasema;

‘Usiwe na wasiwasi utaambiwa baada ya vipimo…’akasema na wote wakaondoka na nikabakia mimi na mke wangu, na wakati huo mke wangu alikuwa kama vile kalala hatikisiki ndivyo nilivyomuona nilipogeuka kumuangalia.

Nilianza kutembea hadi pale kitandani, kiukweli mke wangu kwa siku hizo mbili alikuwa kabadilika kabisa, alikuwa kama sio yeye, mwili umemuisha, usoni kakunjamana kama mzee wa siku nyingi.

‘Unajisikiaje…?’ nikaanza kusema na ni kama vile mke wangu hakujua kuwa nimefika, maana nilipotoa sauti yangu ndio akageuza kichwa kuniangalia, kwani muda wote ule alikuwa kalala kafumba macho huku akiangalia juu.

‘Aheri umekuja, maana nilijua safari yangu itafika, na tusiweze kuonana tena…nilikuwa namuomba mungu sana, ili utokee, ili uje tuyamalize….na kama usingelitokea, sijui ningekuja kusema nini mbele muumba wangu…’akasema.

‘Safari ya wapi, utapona tu mke wangu..’nikasema.

‘Ningelifurahi kama ingelikuwa hivyo,..lakini mungu mwenyewe kapanga iwe hivyo, ishara zote zinajionyesha, na nimeomba iwe hivyo, kuliko kuendelea kuteseka, kifupi… sina budi kuitikia…’akasema.

‘Kwani mke wangu tatizo ni nini..maana nashangaa mimi mumeo sijui ni nini kinachoendelea, naona hata aibu kuwauliza madakitari,..kwanini umenificha kiasi hicho,kwani unaumwa mke wangu…?’ nikamuuliza.

‘Najua…, unisamehe kwa hilo, na nimefanya hivyo kwa vile nakupenda, sikutaka kukutwika mzigo mwingine kichwani mwako …’akasema.

‘Lakini ugonjwa haufichwi..ikizingatiwa mimi ni mume wako, ni nani wa karibu kama mume au mke wako….’nikasema

‘Ninajua..na ..sasa kila kitu kitakuwa wazi, utajua kila kitu pindi…’akasema akijaribu kuinua mkono kuniashiria nisogee nikae karibu naye. Kiukweli mkono ulionekana mdogo, na hauna nguvu, nilianza kujilaumu, maana kumbe nilikuwa naishi na mtu anateseka, anaumwa lakini mimi sijui, mimi na maisha ya kutafuta pesa tu.

‘Nisamehe sana mke wangu,….’nikajiukuta nimesema

‘Nashakuru sana kama hayo maneo yanatoka moyoni, na sijui huo msamaha unaoutaka wewe ni kuhusu kitu gani hasa…’akasema.

‘Kwa vile unaumwa na mimi hata sijui…ni ajabu kabisa…inaonekana kama vile tulikuwa hatuishi pamoja,…, nimekua sikujali, sikuulizi, ..mimi nilijua ndivyo ulivyo, kuna siku niliwahi kukuta …unalia, nikakuuliza ukasema ni maombi yako kwa mungu….nikajua ni kweli ni hizo ibada zako za kila siku…’nikasema.

‘Hayo sasa yamepita mume wangu na nina imani toba yangu, maombi yangu yamekubaliwa, ila imebakia kitu kimoja, ...’akasema.

‘Na hicho ndicho nilichokuwa nikikiombea, …sasa mume wangu nilichokuitia hapa ni yale mazungumzo yetu,…nakumbuka nia yetu ilikuwa kutubia madhambi yetu,..ulianza wewe, na ikafikia hatua yangu, na mimi kwasasa ninataka kusikia kauli yako, je umefikia wapi, upo tayari kunisemehe…?’ akauliza.

‘Mke wangu muhimu ni wewe upone hayo mengine hayana maana kwangu, na mengine yote tuyaache tushughulikie afya yako…’nikasema.

‘Yana maana sana kwangu…nataka kusikia kauli yako kutoka moyoni,kabla hatujachelewa …’akasema

 ‘Mke wangu, hayo ya nini..na kwanza hebu niambie kwanza unaumwa nini maana hata madakitari nawauliza wanasema wewe utaniambia, au …sasa wamesema wanasubiria vipimo…kuna tatiz o gani, ni nini kinachoendelea…?’ nikauliza

‘Nataka kwanza kusikia kauli yako kuwa je umenisamehe, na ninataka itoke moyoni, isiwe kwa ajili ya shinikizo la kwa vile ninaumwa…’akasema.

‘Kwa hali kama hii uliyo nayo, nina haja gani ya kutokukusamehe..mimi ninachotaka ni wewe upone,..utibiwe upone ili tuweze kurejea maisha yetu, na najua hili litapita afya yako itaimarika, na kwa vile…sijajua kuwa wanakusafisha tumbo au vipi, sizani kama itazuia wewe kupata mtoto, kwani si lile tatizo la kizazi au sio…?’nikasema kwa kuuliza.

‘Kwahiyo wewe mawazo yako yote ni huko, mtoto, au sio, ninajua, lakini kwanza fuata masharti ya toba yako, ili uje kufanikiwa, je umeshajifunza, au bado una hasira na mimi…?’ akaniuliza.

‘Mke wangu kwanza upone, ndilo muhimu, na haya matibabu yasaidie ili kila kitu, kiende sawa….na wewe mwenyewe unaelewa kuwa hata wewe linakugusa sana, au sio…’nikasema

‘Kwahiyo kama sitakuzalia mtoto wewe itakuuma sana…, kwako muhimu ni mtoto au sio…?’ akaniuliza.

‘Sijasema hivyo,unielewe mke wangu, ..lakini hata wewe hilo la mtoto si muhimu kwako pia…, eti mke wangu?… najua hata wewe kuumwa hivi inatokana na mawazo ya kukaa muda mrefu bila ya kupata mtoto, hali hiyo imekuwa ikikutesa sana, ndio maana hata mimi nimekuwa nikihangaika sana kwa ajili yako..’nikasema

‘Muda unakwenda mume wangu niambie hicho nilichokuulizia, .. je umenisamehe…?’ akauliza.

 Nilihema kwa nguvu, na sio tu kwa vile namuonea huruma, sio kwa vile tu ..lakini moyoni nilianza kuingiwa na upendo wa ajabu, nikakumbuka maisha yetu ya nyuma ..nikakumbuka jinsi nilivyompata …kiushandani kweli kweli na hatimaye tukajikuta tumekubaliana..kumbe hata yeye alikuwa akinipenda….

Kumbu kumbu hizi zilikuja kwa haraka kichwani, na sijui kwanini..

‘Rafiki yangu nikuambie ukweli, mimi ni jasiri sana, na huwezi kuliona chozi langu kirahisi ..lakini kwa hali niliyomuona mke wangu, na kumbukumbu hizo za nyuma ziliponijia akilini machozi yalinilenga lenga, sijui kwanini!

‘Nimekusamehe mke wangu, sina kinyongo na wewe, iliyobakia ni wewe upone tu..ninajua kosa ni langu..mimi nimekuwa mkosaji sana, …lakini ndio hivyo nilishaanza safari ya kubadilika,…kutubu,….’nikasema

‘Mungu akusaidie mume wngu utimize lengo lako…’akasema

‘Ni kweli mke wngu..mimi nina imani nikiweza kutimiza yote hayo…mungu akanisamehe madhambi yangu,na watu niliowakosea,…. wakanisamehe, basi shida zote tulizo nazo…zitaondoka na wewe utaweza kupona kabisa…na nina imani…uta…’nikasema nakukatisha kauli.
‘Nitakupatia mtoto…natamani ingelikuwa hivyo…’akamalizia yeye.
‘Itakuwa hivyo mke wangu..unafikiri…wewe utaona tu..’nikasema
‘Mume wangu , …mimi nina tatizo kubwa sana…najua kilicho kipaumbele kwako ni nini, lakini mungu anajua zaidi….’akaanza kusema

‘Tatizo litaisha mke wangu…., mimi naamini sana alichoniambia Yule mtu wa mungu, na Yule mcha mungu akisema neno lake kawaida hadanganyi, ana karama, ana kipaji cha kuona mbali, alivyonielezea na hata kufikia kuubadili moyo wangu, mimi nimemuamini sana, tutafanikiwa tu…’nikasema

‘Ni kweli, mungu akipenda na kwa jinsi aonavyo kwake kuwa ni sahihi, lakini kwanza unisikilize kwa makini kuna kitu ninataka nikuambia mume wangu…’akasema

‘Mke wangu docta kasema nisikuongeleshe kwa muda mrefu,kwani hali uliyo nayo haitakiwi uongee sana, ….wewe subiria ukatibiwe, na mimi nipo pamoja na wewe, tutakuja kuonge tu, kwani mimi naenda wapi..’nikasema

‘Ninajua wewe haja yako kubwa ni kupata mtoto..na yote hayo uliyoyafanya nia na lengo lako ni mwenyezi mungu akujalia upate mtoto..sawa ni heri kwako..na nikuambie kitu.., mtoto utakuja kumpata, kwani mwenyezi mungu hamnyimi mja wake anachokiomba, ..na nina..oh…kwanza mimi ninashukuru kwa kauli yako kuwa umenisamehe, najua hiyo kauli yako kweli inatoka moyoni…’akatulia

‘Kabisa mke wangu, nakupenda sana mke wangu …nimekusamehe leo na kesho kiama….’nikasema na ukweli huo sasa ulitoka moyoni, na ukumbuke hadi hapo nilikuwa bado sijafahamu ni nini hasa kinachomsumbua mke wangu,..nilijua labda ni kutokana na kizazi baada ya kuharibika mimba.

‘Ninajua baada ya haya utasahau…na utanisahau, yote ndivyo maisha yalivyo, na ningelipenda iwe hivyo, ifike muda usahau yote haya, usihuzunike sana, endelea na maisha kama kawaida, kwani yote ni mapenzi yake muumba, ufanye hivyo tafadhali…’akasema.

‘Mke wangu kwanini..’nikasema lakini yeye akaendelea kuongea

‘Mume wangu, nilikupenda sana, nabado ninakupenda…japokuwa tuliambiwa mpende umpendaye lakini ipo siku itafika mtaachana naye…na ukweli ni ukweli, kwani sisi ni nani, ni wanadamu tu, ‘akasema

‘Sasa mume wangu unielewe, maana hata mimi sikutarajia kuwa yote haya yangelitokea..lakini ya mungu mengi, huenda ilitakiwa itokee hivi ile iwe ni sababu…’akasema.

‘Usijali mke wangu hayo yamepita tugange yajayo..kwanza ni wewe upone..’nikasema na yeye akaendelea kuongea;

‘Mume wangu, …nasikia ulimpiga docta, kwanini..’akawa kama anauliza lakini hakunipa muda wa kutoa jibu.

‘Mimi..najua hasira zako zipo karibu sana, lakini mume wangu, yeye…docta hana kosa kabisa, wengi wanamuonea tu, najua utasema hivyo kwa vile..au nina mtetea,..lakini ukweli ni kuwa yeye sio mkosaji…, ni sisi tunaokwenda kwake kumuomba iwe hivyo, na inafikia na yeye kiubinadamu anaingia kwenye majaribuni ….na kwa hilo, kama ni kosa basi hilo ni kosa langu mimi mwenyewe…’akatulia.

‘Achana naye..sitaki kumuongelea huyo mtu…’nikasema.

‘Ni lazima tumuongelee, ili niweze kukuondoa kwenye giza la hasira dhidi yake, na ili ujue kuwa nilifanya hayo kwasababu gani..huwezi kuamini, ila kiukweli nilifanya hayo kwa vile ninakupenda wewe mume wangu, hutaweza kuelewa kwasasa…, na huyo docta amekuwa msaada mkubwa kwangu…’akasema na alipoendelea kumtaja huyo docta moyo wangu ukaanza kwenda mbio….niliona kama anataka kuzifufua hasira zangu.

‘Kwanini tusiachane naye tu mke wangu…’nikasema;

‘Ulikuwa unataka mtoto…na umekuwa ukihangaika, ukiumia, nakumbuka hata siku moja wakati tunataniana, uliwahi kusema ..hivi jamani kwanini nisipate hata mtoto wa kusingiziwa,..iliniuma sana…sio kwamba nilichukulia hilo kama kigezo,..hapana hilo nililifanya kwasababu nyingine kabisa….’akatulia

‘Kwakweli mke wangu…nakuomba usiliongelee hili…maana unanifanya nirudi nilipotoka, hasira dhidi yake ni kubwa sana…sijui…hata..wewe yaache tu’nikasema

‘Uliniambia kuwa , kati ya mmojawapo uliyemkosea ni yeye,..ulimtaja kwa jirani..nilijua tu ni yeye…. lakini nashangaa hukuonana naye, ukaonana na mke wake tu….sasa najiuliza kwani uliyemkosea ni mkewe au ni yeye…?’ akauliza.

‘Sijui…hata sijui…..’nikasema

‘Mkewe mlikubaliana au sio..eti kwa vile mlikuwa mkinishuku mimi…au sio, kuwa nina mahusiano na docta au sio…hivyo ndivyo mlivyokuwa mnafikiria tokea awali, au sio.., lakini awali ilikuwa sio kweli, hilo lililokuja kutokea lilitokea tu , na ni siku moja,..kiukweli hata sijui ilikuwaje, ipo siku utajua….’akatulia.

‘Ndio hivyo…ukipona tutaongea tu mke wangu, sasa…, yaishe, sasa..tulia kuongea….’nikasema lakini alikuwa kama kaseti iliyorekodiwa hakuwa akinisikiliza akawa anaongea tu.

‘Ukweli ni kuwa huyo mtu alikuwa akihangaika sana na mimi kupambana na tatizo nililokuwa nalo,…nilipimwa kwingine , nikaja kumwambia yeye,akaanza harakati za kunisaidia..hata hivyo mimi nilimuomba sana iwe siri kati yangu mimi na yeye…..’akatulia nilitaka kumuuliza swali lakini akaendelea kuongea.

‘Kwa vile yeye ndiye alikuwa dakitari wangu , tukajikuta tumejenga ukaribu,…lakini sio ukaribu wa kimapenzi, hilo halikuwepo kabisa…na alijitahdii kadri ya uwezo wake kutimiza wajibu wake kama dakitari…amejitolea hata kugharamia kwa pesa zake, sijui utaweza kumlipa nini…mungu peke yake ndiye anajua hilo..’akasema

‘Kiasi gani anakudai…?’ nikauliza, lakini hakunijibu akaendelea kuongea

‘Na kwa hilo,…juhudi zake , gharama, kujitoa mhanga kwake,..uvumilivu wake, mimi ninakuomba mume wangu ukitoka hapa uende kwake ukamuombe yeye msamaha, kama kweli nia yako ipo safi ya kusamehe wale wote waliokukosea na uliowakosea, huyo umemkosea , kama mimi umenisamehe, na huyo anahitajia msamaha zaidi yangu, wewe unastahiki hata kumpigia magoti…..’akasema

‘Mke wangu…achana na huyo mtu…siwezi hata siku moja….’nikataka kumkatisha lakini hakunipa nafasi.

‘Wewe ulidirikia kwenda kwa mkewe mkaongea, na yeye , mkewe akakukubalia kuwa hata yeye kaligundua hilo, kuwa mimi na docta tuna mahusiano…ujanja wenu ukapitia hivyo,…mkajenga usuhuba,..kweli si kweli, yote nimeyajua , niliongea na mke wake…’akasema

‘Na…kwahiyo mkafanya kama kulipiza kisasi lakini pia ukihangaikia kutafuta mtoto, lakini je mlimpata huyo mtoto..je wewe una tatiz gani, jiulize sana hilo?..mungu alitaka kukuelelesha ili ujue kuwa mambo mengine yanapatikana kwa uwezo wake, na sio kwa utashi wetu…’akasema.

‘Kwahiyo unataka kusema nini..lakini hata hivyo mke wangu hayo yameshapita sawa, ..sasa nimejua kosa langu tuyaache hayo, na ni kwanini unazidi kunipandisha munkari…’nikasema

‘Mume wangu, ujue ni kitu gani unachokifanya…na ni lazima nikuambie hilo kama hujaelewa,..mimi hilo nimeliona kwa matendo yangu mwenyewe, mimi nilianza kutubia mapema kabla yako, ila ilibakia kwako tu…’akatulia

‘Hali iliyokukuta wewe, kwangu ilikuwa ni zaidi….mmh, najua umenisamehe….na sijui kama mungu atanisamehe kwa hili, namuomba sana anisamehe… lakini muhimu ni wewe kwanza unisamahe….kama hutaweza kunisamehe wewe kutoka moyoni mwako, basi….sina budi kwenda kupata adhabu kali …inaniuma sana,…lakini maji yameshamwagika hayazoleki..’akasema kwa uchungu.

‘Oh…’nikaguna hivyo
‘Ni kweli mume wangu tatizo la kutokuzaa lilinisumbua sana mimi huwezi mimi nimehangaika hadio kwa waganga wa kienyeji…lakini hayo niliyafanya kwa siri..meng nimeyafanya,na kwanini nilihangaika hivyo, hata bila ya kukuambia,…..huenda mimi na wewe tungeliweza kuvumilia, lakin jamaii iliyotuzunguka, ilikuwa ni tatizo….

‘Jamii hasa ndugu zako, ….ilinifanya nishindwe kuwa na amani, kila siku naulizwa,..mwishowe nikaanza kuitwa mgumba…je ni kweli mimi ni mgumba..’akawa kama anauliza.

‘Hilo ndilo swali nilijiuliza na hatimaye shetani akaniingia , nia ni kutaka kuhakikisha, kuwahakikishia watu kuwa mimi sio mgumba, ila kulikuwa na tatizo jingine..najua hata wewe ulishafikia hatua ya kunifikiria hivyo, na wewe ukaanza kufanya hayo uliyoyafanya,..japokuwa mkuki ni kwa nguruwe…’

‘Sitaki kulalamika sana juu ya hilo....ila nataka unielewe…kwavile mimi nimeshaionja adhabu yangu hapa duniani,..ninajua kabisa hii ni adhabu,sijui huko mbele itakuwaje…’akatulia nikaona kama anakunja uso..kuashiria anahisi  maumivu makali.

‘Upo sawa kweli wewe..kwanini hutulii mke wangu, inatosha…’nikasema na yeye kwa shida akaendelea kuongea.

‘Mume wangu nakupenda sana,..hata kama nilifanya kinyume cha ndoa yetu,…na kinyume cha uhalisia wa kupenda , maana tendo nililolifanya ni kama vile humpendi mwenzako, au sio..hapana , ..nakupenda sana mume wangu, na hilo nililifanya ili usihangaike, ili uweze kuwa na kile unachokitamani,..ambacho ni mtoto…na na mtu wa kunisaidia akawa ni do-do-ctaah’naona hapo sauti ikaanza kufifia.

‘Mke wangu wewe pumzika sasa inatosha, inatosha sitaki kusikia tena hayo.. tu…’nikasema

‘Nita-nitapu-pumzika, hilo halina jinsi,…na nikipu-pu-mzika, najua ndio moja kwa moja…’akasema

‘Kwanini unasema hivyo mke wangu, docta kasema unakwenda kufanyiwa upasuaji na baada ya hapo utakuwa huna tatizo tena..utapona tu mke wangu, sasa tulia usiongee.., na …’akanikatisha.

‘Ni hivi mume wangu, docta hana makosa, siku alipokuwa akinichunguza, yeye aligundua, hakuniambia akanielekeza kwa docta bingwa wa mambo hayo..na huyo docta akagundua kweli kuwa nina tatizo,..na nilimuuliza tatizo hilo ni la muda gani, nitaweza kuhimili kwa muda gani, akasema hata mwaka, lakini itakuwaje..’hapo akatulia
‘Unasema…?’ nikajikuta nimeuliza
‘Basi , kwa vile nakupenda mume wangu, nikajiuliza nina maana gani hapa duniani,..unataka mtoto na mimi sijui nitawezaje kukupatia mtoto...na kiukweli , siku aliponiambia kuwa sina muda hapa duniani…nikaanza kuyaacha yake masharti yote niliyoambiwa…ili tu unipatie huo ujauzito..lakini haikuwahi kutokea….nikawa sina raha…’akatulia
‘Nikajiuliza itakuwakuwaje maana mimi sina muda hapa duniani, nifanye nini ili ubakie kuwa na raha..ili angalau upate mtoto, hahaha,… sio nacheka ila nikakumbuka kauli yako ulivyopenda kusema..nipate mtoto..tu, hata kama wakufikia..basi nikaona kumbe ninaweza kuutumia huo mwaka kwa ajili yako..ili niweze kukupatia kile unachokitaka, kabla muda haujafika,..hata kama… lakini ..’akatulia.

‘Mke wangu achana na hayo maneno,ukifanyiwa upasuaji, utapona tu…,hilo  nina uhakika nalo baada ya huo upasuaji kila kitu kitakuwa sawa..’nikasema.

‘Ni kosa kubwa mume wangu nilifanya, kwanza nikakiuka masharti , pili nikavunja miiko ya ndoa, tatu..aah..na kiukweli docta alinishauri sana, lakini mwishowe ..mmh..mwishowe..mhhh, nikajitolea mhanga, sasa kipo wapi…’ akasema

‘Sasa kipo wapi..tuacheni jamani…unajua mimba hiyo ilikuwa kama sindani nimeimeza tumbaoni, kila mtu ananichoma…nikawa nahisi maumivu makali sana..ikafikia muda siwezi…siwezi..maumivu, yalikuwa …ni makali sana, nikaona pamoja na mengine niliyowahi kukuelezea awali kuwa…unaku-ku-mbuka, nika-nika-shindwaah kukupatia..na-na- sijui tena, …’mara akaanza kuhangaika, kama anapata shida fulani,…’nikageuka huku na kule, kuona kama naweza kusaidia au kumuita docta.

Chumbani mle kulikuwa hakuna mtu mwingine, …nilikuwa mimi na mke wangu tu, na nilipoona mke wangu anazidi kuhangaika ikabidi nipige ukulele.

‘Docta, njoo haraka..’nikasema lakini hakukutokea mtu, nikaendea kengele ya dharura nikaibonyeza na haikupita muda docta akaja, na kuniambia nitoke nje. Nilikataa lakini wakanilazimisha kwa kunitoa kwa nguvu.

Nilifika nje nikiwa sasa natetemeka, mwili hauna nguvu, miguu haina nguvu kabisa, na hii hali ilinianza siku za karibuni, sikuwa na tatizo hili kabla, …sijui kwanini..

Na kwa muda ule akili yangu ilishindwa kufanya kazi, nikaenda kwenye kiti pale nje na kukaa,nikasimama, nikakaa nikasimama na kukaa ! Mtu aliyeniona alijua labda nimepewa adhabu ya kukaa na kusimama, …

Yaani sijui ilitokeaje, yalikuja maumivu makali kichwani, …na mara maumivu makali yakatokea moyoni, kilichofuata hapo ni giza kutanda usoni, nikajikuta naelea gizani, na sikujua kilichoendelea…

Nilipoamuka nilijikuta nipo kitandani…hospitalini..

NB: Naishia hapa kwa leo
WAZO LA LEO: Kipindi mtu anaumwa, au akiwa na shida kubwa kubwa, ndicho kipindi mtu huyo anastahiki kupendwa, kusaidiwa kuhurumiwa na kila mtu mtu anayemuhusu, hata kama ulikuwa ni adui wake, inabidi uadui huo, au chuki hizo kuziondoa. Imani ya kweli ya dini, inaonekana kipindi hicho, kwani tumeambiwa hivi;-

‘’Hatoamini mmoja wenu (kikweli kweli) mpaka atakapompendelea ndugu yake kile anachojipendelea nafsi yake…’ ni nani asiyependa siha njema,…afya, maisha bora …nk
Ni mimi: emu-three

No comments :