Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, July 26, 2016

TOBA YA KWELI-7



Siku ya pili,

Nikiwa nimelala kwenye hifadhi ya jamaa yangu, kiusalama,

Niliamuka asubuhi sana nikijiandaa kuondoka, kiukweli akili sasa ilikuwa imetulia na nilianza kujilaumu kwa hayo niliyoyafanya, sio kawaida yangu kujilaumu kwa mabaya… lakini sasa nafsi ilianza kunisuta,.

Kwanza nikawasha simu yangu….nilipoona miito mingi ya simu, na ujumbe za maneno zikinitafuta, lakini hakuna ujumbe uliosema lolote zaidi ya kuulizwa upo wapi…nikaizima simu …na wakati nafanya hivyo mlango ukafunguliwa, akaingia mwenyeji wangu,

Tuendelee na kisa chetu…

                         *********

Mwenyeji wangu alipoingia, nilimtupia jicho kwa haraka, nikamuona ni mwingi wa wasiwasi,..ninamfahamu sana maana tumeishi naye kwa muda mrefu, na mimi nina hulka ya kumtambua mtu alivyo nikimuangalia usoni mwake.

‘Kuna tatizo…?’ mimi nikaanza kumuuliza hata kabla hajasema lolote. Na yeye kwanza akasogea hadi kwenye dirisha akafunua pazia na kutizama nje, halafu akageuka kuniangalia akasema;

 ‘Ni vyema ukawahi kuondoka, maana hali sio shwari,…sio kwamba nakufukuza lakini unielewe tu ndugu yangu,  siunajua,…. mimi naweza kuonekana nimeshirikiana na wewe…na mimi nimeamua ..na jamii inafahmu hivyo, sitaki tena kujihusisha na jambo lolote baya…’akasema

‘Ni kweli, usijali., nimekuelewa, nashukuru sana kwa kunihifadhi na matibabu uliyonifanyia,…nisameheni sana kwa usumbufu huo’nikasema

‘Mhh, rafiki yangu kweli umebadilika, …kufikia kunitamkia maneno hayo,…kweli hujafa hujaumbika, kwako neno samahani sidhani kama lilikuwepo kwenye msamiati wako,…’akasema

Ni kweli mimi nilikuwa nduli, amri ndio kauli yangu, kiburi,…sikupenda kuishi kilege lege, ukikosea ni adhabu papo kwa papo…na ole wako uje useme samahani nimefanya hiki nimekosea, nimeharibu, hatukufanikiwa...kitakachofuata hapo ni kipigo..sijui kwanini niliishi hivyo…niliweka masilahi mbele, na sikupenda mtu aniingize kwenye hasara kwenye biashara zangu.

‘Unajua,… awali uliponiambia unataka kufanya toba, sikuamini, kwa jinsi nikujuavyo….lakini sasa naanza kukuamini kidogo…’akasema na mimi nikawa nimesimama, sikusema kitu.

‘Lakini kiukweli…toba ya kweli sio rahisi kihivyo…ni shida tu ndio zinatusukuma, au sio…’akasema kama anauliza

‘Mhh….’mimi nikaguna tu, nilitaka kumwambia mbona yeye kaweza, lakini sikusema neno, nikaguna hivyo tu.

‘Unajua kama kweli tungelifahamu msingi wa kuletwa kwetu hapa duniani, sizani kama kuna mtu angelihangaika sana na hii dunia zaidi tungelihangaika na ibada, na kufanya yale tu tuliyoamrishwa tufanye, nikimaanisha matendo mema..’akasema

‘Hebu chukulia mfano mtu akiamuka asubuhi ni nini cha kwanza anachofikiria kwenye kichwa chake…  cha kwanza atakimbilia kuangalia saa, au kuangalia nje, kuwa ni saa ngapi, …wasiwasi nimechelewa kazini, nitapatia wapi pesa, nitakula nini…mungu hapo hayupo, hata ile kushukuru kuwa umeweza kuamuka,kupumua, ambavyo vyote hivyo ni neema ya mungu hatkumbuki…’akasema

‘Mhh…’nikaguna.

‘Nikuulize ndugu yangu, ulipoamuka leo asubuhi ni nini cha kwanza kuwaza…?’ nikamuuliza

‘Nilikumbuka yaliyotokea nikaona niwahi kuondoka…’nikasema

‘Umeonaaeeh….mungu hukumkumbuka kwanza, kwa rehema zake ukaweza kuamuka, kwa rehema zake ukaendelea kupumua,…kwa rehema…’akasema na mimi nikamkatiza kwa kusema.

‘Ndugu yangu samahani , muda…’nikasema.

‘Ni kweli,muda…ila ninataka kukuweka wazi kabla hujaondoka,…kukujenga kiimani, maana imani ya kweli ni pamoja na kujitambua wewe ni nani, …ni nani kakuleta hapa duniani…ukimjua huyo ukamtii, ukamshukuru ukamuomba, ukamtegemea yeye, mbona haina shida…’akasema

‘Ni kweli….’nikasema

‘Ni kweli..lakini imani hiyo tunayo…, na tungelikuwa na imani hiyo kwa kila mtu mbona tungelikuwa peponi, twaishi kwa amani tu…tatizo wengi wetu au karibu kila mtu anahisi kuwa huenda tumeletwa hapa duniani kushindana katika kutafuta mali, ndio imani yetu kweli si kweli, kama ni hivyo…tunajidanganya,….’akasema na kusogea kuangalia dirishani , kulishapambazuka vyema.

‘Unataka kusema nini, kuwa tukae tu,….tukumtegemea mungu au…?’ nikamuuliza

‘Ni sawa,..kuhangaikia dunia ni muhimu, tunahitajika kutafuta mali, lakini hata hivyo basi,…tuitafute mali hiyo  kwa njia iliyo halali… ni nani anaweza kujithibitishia kuwa mali aliyo nayo ni halali tupu..?’akaniuliza na mimi nikasema..

‘Sijui…..’nikasema

‘Mimi kwa kweli nakutakia mafanikio mema, uweze kulifikia hilo daraja la ucha mungu,maana hayo unayoyafanya ni …kuutafuta ucha mungu wa kweli, na ucha mungu wa kweli huanzia huko,kwenye toba ya kweli….’ Akasema

‘Aamin..’nikasema nikataka kuanza kuondoka.

‘Lakini sikiliza…najua una haraka sana,…mimi ninakufahamu sana wewe rafiki yangu, wewe uliishi maisha mabaya sana kama ilivyokuwa mimi…, lakini nikupe angalizo moja,…. kwa mungu, yeye ni mkwasi,  humsamehe yoyote Yule hata kama alikuwa mbaya kiasi gani, muhimu uwe amedhamiria kiukweli kutubia..’akasema

Mimi nilishakuwa tayari kuondoka ….

‘Ndio nimekuelewa…’nikasema nikiinua mguu kuondoka.

‘Nilikuuliza awali je upo tayari kufanya hivyo, ukasema ndio…, nilijua tu sio kweli, ulikubali tu kwa vile ulikuwa na shida…mungu akakujaribu kidogo tu, naona ilivyotokea,..sasa wazia hilo tena kabla hujaendelea na hicho unachotaka kukifanya..’akasema , nikatikisa kichwa tu, nilitaka kumwambia nachelewa, lakini niliona sio busara.

‘Ndio nimekuelewa…’nikasema

‘Umenielewa sio?….au unanijibu kwa vile una haraka, nakuambia hili nikiwa na maana yangu…huko unapokwenda sasa hivi unakwenda kukutana ni mitihani mikubwa, unakwenda kupambana na wenye dola, kupambana na nafsi yako, sasa sijui…mimi niseme tu nakutakia kila la heri…’akasema

‘Wewe hujui shida gani ninazozipata..sina raha ndugu yangu,…naumwa, mali naiangalia hivi hivi…ina maana gani,sina hata mtoto wa kuniliwaza, ina maana gani,sasa hata Yule niliyekuwa nikimtegemea ndio huyo,kanisaliti….hapana ni lazima ..ni lazima nifanye jambo…wewe huniamini tu…’nikasema

‘Unajua ….mimi nahisi  bado haupo tayari…maana ili  ufanikiwe kwa hilo,kwanza pamoja na kutaka kusamehewa, na wewe ukubali kusamehe….kumbuka uliyowafanyia wenzako ,yaliwauma hivyo hivyo, ulivyoumia wewe natoba ya kweli kwanza kabisa huanzia moyoni mwako, hapo umeongea unalalamika, bado hujaiva…’akaniambia

‘Sasa nifanyeje,…nimejitahidi sana, hebu fikiria na wewe…., hata ingelikuwa ni wewe, mke wako anakufanyia hivyo, ..hapana unajua, inauma sana …natamani kuumiza, natamani kulipiza kisasi…tatizo ni kuwa nilimuamini sana mke wangu…, sikutegemea hata siku moja kuwa atanifanyia hivyo alivyonifanyia ..ni kwanini..’nikasema

‘Na je ni kwanini na wewe ulimfanyia hivyo ulivyomfanyia…., wewe hujuoni tu, uliyowafanyia wenzako yanaweza kuwa ni mabaya zaidi ya hayo uliyofanyiwa wewe, lakini sio rahisi kwa nafsi zetu kujiona, wamnyoshea mwenzako kidole, ni kimoja tu je wewe vidole vingapi vimekunyoshea wewe, chunguza kwanza hilo…’akaniambia

‘Lakini yeye ni mke wangu, na..na yeye hatakiwi kujilinganisha na mimi, yeye ni mtunza dhamana ya mume wake,..kama alifanya hivyo kwa kujilinganisha na mimi,sizani kama anafaa kuwa mke wangu…’nikasema

‘Hahaha unaona eeh, kwetu sisi dunia ni hivyo, umimi tu…mke kwako ni tofauti na wewe…kumbuka huyo ni mwenza wako, utakavyo kutoka kwake nay eye halikadhalika anataka hivyo hivyo kutoka kwako,…tusigeuze dunia hii ni uwanja wa fujo, mwenye nguvu mpishe…mhh..kama bado una hisia hizo, mimi naona bado kabisa hujaiva, hebu sasa nikuulize ukitoka hapa unakwenda kufanya nini huko..?’ akaniuliza

‘Nitajua huko mbele kwa mbele…lakini muhimu nijue kinachoendelea, na dhamira yangu ipo pale pale,….kutubia, kuomba msamaha, lakini lazima niupate ukweli, kuhusu mke wangu, bado nina maswali mengi kichwani hayajapata majibu….lakini nina uhakika nitayapata tu, kama bado yupo hai…’nikasema

‘Haya…lakini usisahau sharti hilo… kuwasamehe waliokukosea….ulinicheka sana kipindi kile.., lakini nione mimi, sasa hivi nipo huru,….nahisi nipo dunia nyingine, ya utulivu...’akasema

‘Hongera…’nikasema

‘Sasa kama na wewe unataka ufanikiwe,…ujue mtihani wake ni mkubwa, sio rahisi kihivyo,…lakini rafiki yangu nisikukatishe tamaa, maana ugumu unakujaje , kwa vile bado hatujajitambua sisi ni nani na tumekuja hapa duniani kufanya nini…hilo nalirudia tena na tena kwako…’akasema huyu jamaa , na mimi nikamwangalia jamaa yangu huyo nikiwazia mbali….

Jamaa huyu alikuwa na mimi kwenye kuhangaika, kwenye kutafuta maisha,…tulikuwa washirika kipindi Fulani kabla hajabadilika, nilimshangaa siku moja akaniambia yeye, kaamua kubadilika, hataki tena mali ya dhuluma, …’

‘Kwani mlikuwa mnafanya mambo gani zaidi wewe na yeye…?’ nikamuuliza na yeye akaendelea kuongea kama vile hakunisikia.

‘Rafiki yangu aliposema kaamua kubadilika …hataki biashara tuliyokuwa tunafanya tena,..nilimcheka sana kipindi hicho, lakini hakurudi nyuma,…aliamua na kweli akabadilika,…na katika mabadiliko hayo alifikia kipindi  akawa hohehahe…nilimuonea huruma sana, nikakata urafiki naye kabisa,lakini sasa huwezi amini, ana furaha, ana familia yake…..kesharizika na maisha yake!

 Sasa uone kinyume chake, mimi sasa namtegemea yeye kiushauri,…yeye alinishauri kuwa, ni bora niende kwa kiongozi mmoja wa kidini, anayejulikana sana kwa kuombea watu, kuwashauri nk….na mara nyingi kiongozi huyo wa kidini akikuambia jambo ukilifuatilia, unafanikiwa,...

 Jamaa yangu huyo aliponiona nimezama kwenye mawazo akasema;

‘Ndugu, una uhakika upo sawa sasa…,upo tayarii kukabiliana na kazi iliyobakia,ujue hiyo kazi iliyobakia ndio kubwa zaidi…kukubali kusamehe,..na kuwa tayari kwa lolote lile hata ikibidi kufungwa , je utaweza…?’ akaniuliza

‘Eti nini, kufungwa…wewe…’nikamkazia macho jamaa na jamaa akatikisa kichwa sasa yeye akigeuka kuondoka.

‘Mimi ninakumbuka vyema, Yule kiongozi wa dini  aliniambia kwamba, nikifanya toba, nikamaliza mambo yangu yatanyooka, sasa wewe unaniambia nini, kwanza hujamambia umesikia nini..?’ nikamuuliza jamaa yangu huyo hakusema neno, akawa anatembea kutoka nje….

‘Sikiliza mimi siwezi kwenda jela,..siwezi kabisa, kama nitafungwa ujue ninakwenda kufia huko, mimi ni mgonjwa…ninaumwa,..unasikia naumwa, usinione nimenenepa hivi….ok, kama hutaki kunieleza zaidi ngoja niende huko huko nitajua mbele kwa mbele,lakini siwezi kujipeleka jela, ……’nikasema na mimi nikaanza kuondoka...


WAZO LA LEO: Hatuwezi tukawa wachamungu wa kweli mpaka tumfahamu mwenyezimungu, na kumkubali ndani ya nafsi zetu. Tuwe na imani thabiti kuwa mwenyezimungu yupo na yeye ndiye katuleta hapa duniani, tumuabudu, tufanye aliyotuamrisha (mema) na tuyaache aliyotukataza (mabaya)

Ni mimi: emu-three

No comments :