'Je kweli una uhakika,..utaweza kunisamehe mume
wangu....?’ akaniuliza tena
mke wangu na hapo nikatulia nikiwaza, ni kwanini mke wangu aniulize hilo swali
mara mbili, ana nini, kuna nini alifanya, hapo nikamtupia jicho,nilimuona bado
machoni kuna machozi, nikasema;
‘Mke wangu mbona
huniamini…?’nikasema kwa kumuuliza
‘Kwasababu
nakufahamu sana mume wangu…’akasema
‘Hata mimi
nakufahamu sana mke wangu, wewe ni mcha mungu, na ukitenda kosa itakuwa ni
bahati mbaya sana….’nikasema na hapo mke wangu akainamisha kichwa chini kama anamtiii
bwana wake, akawa kafanya vile kwa muda kidogo…
Nilianza kuhisi
mashaka, lakini nikajipa matumaini , nikijua kua mke wangu hawezi kufanya
madhambi yoyote, kwa jinsi nimjuavyo, haiwezekani, nikataka kusema neno lakini
kabla sijasema yeye akaanza kuongea…
Tuendelee na kisa
chetu
*********************
'Mume wangu unakumbuka ile mimba iliyoharibika
miaka kumi iliyopita,...?’ mke wangu akaanza kuniuliza hivyo, na mimi
nikatikisa kichwa kukubali, huku nikivuta kumbukumbu za tukio hilo,
Kiukweli ni tukio ambalo liliniumiza sana,
siku hiyo nililia…utafikiri mtoto alishazaliwa na kukua, halafu akafa….nililia
mpaka mke wangu akanionea huruma sana….sikuamini,…siku hiyo ilikuwa moja ya
siku ambayo sitaisahau maishani.
‘Mume wangu usilie,
haya yote ni mapenzi ya mungu….’aliniambia mke wangu.
‘Lakini kwanini, …mungu
wangu kwanini, tunahitaji mtoto, tumekaa sana, kila mtu amekuwa akituuliza nyie
vipi mbona hamzai..sasa bahati imekuja, ..halafu ndio hii imeondoka, inaniuma
sana mke wangu..’nilisema.
‘Tumuombe mungu,…atatujalia
tena, tutapata mwingine…’akasema mke wangu.
Kiukweli ilipita
muda nikiwa sina raha, na siku zikapita, nikitrajia itashika mimba nyingine,
lakini haikuwa hivyo …na mke wangu akawa anaumwa umwa sana,….akaanza kukonda,
nikampeleka hospitali, akapimwa, na docta alikuja kuniambia mke wangu
anahitajika kusafishwa kizazi.
‘Kwanini kusafishwa
kizazi kwani kuna nini, je kizazi kipo salama, ataweza kuzaa tena….?’ Nilimuuliza
docta
‘Ni kawaida tu,
mimba iliyoharibika imeacha uchafu, ….ni jambo la kawaida…usijali kizazi kipo
salama…’alisema docta. Na tendo hilo lilipita, na siku zikaenda, lakini
haikutokea mke wangu kushika mimba, na mimi nikaanza kuumwa, kupimwa nina
kisukari,…sijakaa sawa, shinikizo la damu, mara matatizo ya moyo..ndio katika
kuhangaika, nikaja na agizo hili la kutubu;
*********
Mke wangu akasema;
‘Ni miaka mingi
sana, lakini mimi kila siku nahisi ni juzi, maumivu yale bado yananiandama hadi
hii leo….kila muda unaopita tukio hilo linakuwa kama lilitokea jana,
….linanitesa sana…’akasema mke wangu
‘Oh, mke wangu….Lakini
hayo yalishapita mke wangu sio kosa lako au sio..?, hayo ni mapenzi ya mungu, mungu hakupenda
tupate mtoto kwa muda huo,…ndio maana nahangaika,..’nikasema na mke wangu
akatikisa kichwa kwa kusikitika.
‘Unajua mke wangu
nilipogundua kuwa wewe huna tatizo, kizazi kipo, nilijipa matumaini kuwa ipo
siku…ipo siku tutapata mtoto tu,…unaona… ,..ndio maana unaniona, nahangaika, yote
haya nia yangu ni sisi tupate mtoto..eeh, labda tungesema tatizo ni mimi,
lakini hapana docta kasema matatizo yangu hayanizuii mimi kupata mtoto na hiki
kisukari na presha vitakwisha tu….’nikasema
'Ni kweli mume wangu, hata mimi nasema hivyo
hivyo kuwa hayo yaliyotokea ni mapenzi ya mungu, lakini mbona ndani ya nafsi
yangu haitaki kuikubali hiyo hali kuwa kweli hayo yalikuwa ni mapenzi ya
mungu…’akasema mke wangu kama ananiuliza
‘Kwasababu wewe
kama ilivyo mimi tunahitajika kupata mtoto au sio,…lakini muda unapita
hatupati, kikawaida nafsi itajiuliza…lakini docta mwenyewe alisema hatuna
matatizo, sasa tatizo ni nini, unaonaeeh, ndio maana hata aliponiambia huyo
mkuu wa dini kuwa nikitubu dhambi zangu, itakuwa ni dawa, nikakubaliana naye,
unaona mke wangu...’ nikasema
‘Ni kweli..lakini
kwa vipi…?’ akasema mke wangu kama ananiuliza huku akijikuna kichwa kwa nguvu
kama kinawasha.
‘Kwa vipi! Aah mke
wangu,, ….ni hivyo hivyo kama nilivyoambiwa kuwa kwanza tutubu madhambi yetu,
tuwasamehe waliotukosea, halafu tumuombe mungu, huku tukihangaikia na dawa,
tutafanikiwa tu,…yule mkuu wa imani aliniambia matatizo mengine yanatokana na
madhambi yetu, aah, madhambi yangu maana wewe mke wangu huna kosa, huna kosa
kabisa…’nikasema
‘Hapo hapo….ndio
maana na mimi nikaliwazia hilo, nikaona haya yaliyonitokea mimi, ili nafsi
yangu itulie, yanibidi na mimi nitubu, bila ya toba ya kweli, sizani kama roho
yangu itatulia, najua huenda uhai si kitu kwangu, lakini siwezi kwenda hivi
hivi huku nikiwa nimebeba mzigo huu...'akasema mke wangu huku akilia.
‘Lakini mke wangu
kwani vipi…?’ nikamuuliza swali kama lile aliloniuliza yeye, na taratibu mke
wangu akainua kichwa na kuniangalia, machoni alionyesha huruma sana, nikata kusimama
na kwenda kumpa pambaja, lakini mwili ukawa mnzito, sijui kwanini.
Mke wangu kwa muda
ule alikuwa kakaa kwenye kiti cha kawaida na mimi nilikuwa nimekaa kwenye sofa,
kwani yeye nilimkatiza kwenye shughuli zake, na alikaa tu kwa vile mimi nimemuita,
sasa alipotamka hayo, akainuka kwenye kiti, na mara akaja pale nilipokaa kwenye
sofa, na kunipigia magoti, huku akisema anaomba msamaha kwa kosa alilolifanya…
Kwanza nilibaki
nimeduwaa, sikuelewa anamaanisha nini. Baadaye nikainama nikitaka kumuinua huku
nikisema;
‘Mke wangu haina
haja ya kunipigia magoti…mimi nimeshakusamehe..haina haja, unanipigia magoti
wakati mimi ni mchafu…sistahili kufanyiwa hivyo, mke wangu inuka,….niamini
mimi…’nikasema na hapo mke wangu akiwa bado kapiga magoti, akasema;
‘Mume wangu,…sina budi nikuambie kila kitu,
najua sina muda zaidi..lakini ni haki yako kujua….’ Akasema na mimi akilini
nikawa najiuliza ‘kujua nini, anataka nijue nini…labda, ni kuhusu ..hapana, mke
wangu hawezi kunificha kitu, hana tatizo..’ hayo mawazo yalipita kichwani
haraka sana,
‘Mume wangu tatizo
linaloniumiza mimi ni kuhusu ile mimba iliyoharibika…’akasema na kutulia na
kabla sijasema kitu akaendelea kusema;
‘Kuharibika kwa ile
mimba imekuwa ndio sababu ya haya yote, na huenda….ni adhabu mungu
kanipatia,…’akasema na mimi nikamwangalia mke wangu, kuna kitu kilipiga moyo
paah, lakini nikakitupilia mbali, nikasema;
‘Hapana mke wangu
sio kweli…hiyo sio adhabu, kama ni adhabu ni mimi ninayestahiki, sio wewe, huna
kosa mke wangu, amini usiamini tatizo ni mimi…’nikasema.
‘Mume wangu unajua
ile mimba haikutoka yenyewe…’akasema mke wangu na akaniangalia mara moja halafu
akainamisha kichwa chini.
‘Haikutoka yenyewe,
unataka kusema nini..?’ nikauliza, ni kama sikusikia vyema, na akili haikutaka
kufikiria vingine nikasema;
‘Najua
haikuharibika yenyewe, …yawezekana ni kutokana na mihangaiko, ulikuwa unafanya
kazi sana, huku unaumwa kila siku, nilikuambia utulie..ukawa hunisikii
ulibadilika ukawa mgeni kabisa kwangu..nilijua tu ni mabadiliko kutokana na uja
uzito…!
Lakini huo sio muda wa kulaumiana kwa hilo, hayo yameshapita au sio mke
wangu..’nikasema.
Mke wangu akatikisa
kichwa kama kulikataa hilo, akasema;
‘Mume wangu,
ilimradi nimeamua kulifanya hili, kuwa nikuambie kila kitu, nitafanya hivyo kwa
vyovyote iwavyo na iwe…nitakuambia ukweli wote,….hicho kilichotokea sivyo kama
unavyofikiria wewe…’akasema mke wangu
‘Kufikiria vipi….?’
Nikamuuliza
‘Kuwa hiyo mimba
iliharibika yenyewe,…sio kweli, ile mimba ni mimi niliamua kuitoa baada ya
kushindwa kuvumilia ….’akasema.
‘Nini….mke wangu,
unajua unachokisema…! Mke wangu najua mimba ile ilikutesa sana,..ulikuwa kila
siku unaumwa, …sasa labda mimi nahisi, wewe unahisi labda katika kuteseka huko
kuumwa labda ndio ..kulisababisha iliharibika kihivyo,..hapana,.hiyo mimba
iliharibika kwa vile haikupangwa iwepo, niamini mke wangu….’nikamwambia.
‘Mume wangu…hiki
ninachokuambia sasa hivi ndio sahihi, ya kuwa ni mimi niliitoa hiyo mimba kwa makusudi,…’akasema
na mimi nikashtuka, nikataka kusema neno lakini mke wangu hakunipatia nafasi
akasema
‘Mimi niliamua
kufanya hivyo kwasababu niliogopa,…’akatulia
‘Mume
wangu,..nilifanya makosa makubwa sana…najuta sana,…niliogopa kkubakia na hiyo
mimba, halafu nikijifungua ugundue hilo kosa, moyo ulikuwa ukanisuta,
nisingeliweza, na hata wewe usingeliweza, ninakufahamu sana mume wangu ,
….’akasema na mimi hapo nikashikwa na kigugumizi.
‘Sikuelewi mke
wangu…’nikasema sasa nikihisi mwili ukinisisimuka…nahisi kuna jambo linakuja,
nikatuliza kichwa, akili haitaki kuamini…hapana, hapana ..haiwezekani…!
‘Damu yake ni kali
sana mume wangu , kiushahidi, nilijionea na ..hata watoto wake wote unawaona
walivyo, wanafanana na yeye kabisa,…’akasema
Hapo nikarudisha
kichwa nyuma, ni kama nimezabwa kofi la kushitukiziwa, nikataka akili itulia,
lakini nilihisi kitu kikianza kuchemka, sikuweza kusema neno, nikabakia kimia
na mke wangu akaendelea kusema.
‘Huyu mtu..aliamua
kutumia utaalamu wake vibaya, lakini sio kosa lake, ni mimi..mwishowe niliamua
na mimi,..nijaribu…sasa tatizo ni kuwa kila mtoto aliyemzaa alikuwa kifanana na
yeye…’akasema
‘Mke wangu unajua
nini unachokisema, upo sawa kweli wewe..?’ nikamuuliza
‘Ni kweli…nilijua
hata mimi huyo mtoto kama ningeliweza kuvumilia nikamzaa atakuwa akifanana na
yeye...'akasema na mimi hapo nikatikisa
kichwa, sikutaka kusikia hayo, sikutarajia hayo,
Unajua nilianza kubadilika,…moyo wa kiimani, moyo wa subira
ambao alishanijenga Yule mtu wa imani, ulianza kuyeyuka…nikaanza kuhisi mwili
ukinichemka, ilikuwa kama mtu kanisindilia kisu kifuani, nilihisi maumivu,
mdomo ukanikauka,..macho yakanitoka…
Kuna jambo jingine ambalo sikukuelezea kuhusu mimi, ..mimi nina
wivu sana, na nikihisi wivu mwili mnzima unanisisimuka na damu hunichemka, na
ole wako uwe unahusika …., naweza kukufanya kitu kibaya sana…ogopa
nikibadilika, ogopa shetani mbaya akiniingia akilini, huwezi kuamini kuwa ni
mimi….
'Unasema nini..?' nikamuuliza mke wangu na sauti
hiyo ilimshtua mke wangu, akainua kichwa kuniangalia, macho yake yalijaa
huruma, na machozi tele, huruma ilinijaa, japokuwa kuna kitu kilishaanza
kuuharibu ubongo wangu, nafsi yangu ya siri, ilishaingiliwa…, tofauti na
nilivyodhania awali…
Nilijaribu, na
kujaribu kuirejesha ile hali, lakini…ooh, …hata hivyo kwa vile nilishasema
nitamsamehe, nikajikausha na kujifanya ninatabasamu, tabasamu la kuigiza.
'Tatizo ni rafiki yako, rafiki yako sijui ana
nini..nilijitahidi sana kujizuia, lakini siku hiyo nilishindwa, akanishawishi,
akisema tufanye majaribio …..’hapo akatulia
‘Mhh, mke wangu
sijakuelewa, ni nani huyo rafiki yangu…?’ nikamuuliza nikijaribu kujituliza.
‘Ukumbuke mume
wangu ulisema utanisamehe…’nikasema
‘Ni..na..nataka
unieleze ukweli wote…’hapo nikasema nikijaribu kuizuia hasira. Na mke wangu
akashutuka kwa jinsi alivyoniona nilivyobadilika usoni. Akasema;
‘Rafiki yako,..yeye
anapendwa sana na wakina mama, sijui kwanini, na mimi sikufanya kwa jili hiyo,
ila nilitaka kuhakikisha, je nisamehe tu mume wangu....na shetani alinipanda,
kwa vile ...nikaona nijaribu nione,..mtoto akizaliwa si wetu itakuwa siri
yangu, kwanza tumekaa muda hatupati mtoto,...’akasema
‘Mhh..mke wangu
unauhakika na unachokisema….?’ Nikamuuliza sasa nikiwa sina utani, nilishajua
mambo sasa yameharibika, sijui kama nitaweza kuvumilia.
‘Ninatubu haya
mbele yako mume wangu nisamehe sana, ..nilipanga iwe siri yangu, nilipanga nife
nayo, lakini kwa vile umeniahidi kuwa utanisamehe ndio maana nimeamua
kukuambia, ili hata nikiondoka niondoke kwa amani….’akasema
‘Uondoke kwenda
wapi…?’ nikauliza sasa kwa sauti ambayo ukiisikia , kwa wale wanaonijua ,
wanajua sasa kitakachofuata ni damu kumwagika.
‘Mume
wangu,..uliniahidi ukumbuke..’akasema mke wangu.
‘Nataka kusikia
kila kitu…siamini , siamini…wewe…wewe, kwanini hukuniambia, kwanini….hapana,…hapanaaah’nikasema
kwa ukali.
‘Mimi nitakwambia
na …nipo tayari kwa lolote utakalonifanyia, maana najua nilikosea,…’akasema mke
wangu sasa akiwa kaka chini kabisa, nahisi nguvu zilimuishia.
‘Ile mimba niliamua
niitoe, …japokuwa tulihitajia mtoto…’akasema.
‘Ina maana ile
mimba ilikuwa sio ya kwangu…?’ nikauliza kwa ukali.
‘Mume wangu ilikuwa
ni bahati mbaya sana na wala sijui ilikuwaje,..sijawahi kunywa, lakini siku
hiyo nilikuwa kama nimelewa, sijui ni nani alinilewesha, nilijikuta nikifanya
kila alichoniambia…’akasema
Hapo nikasimama…nikashika
kichwa, nikaruka ruka…halafu nikamkazia macho mke wangu na kusema;
‘Acha uwongo, toka
lini ukanywa pombe wewe…ina maana ulijifanya hivyo ili kutimiza matakwa yako na
hawara yako, na ninani huyo rafiki yangu, maana sijui kama ananifahamu vyema,
sijui..atakimbilia wapi, sijui…sijui, ni nani huyo ni nani huyo….’nikawa sasa
nimebadilika, sio mimi tena, ogopa nikiwa kwenye hiyo hali…
‘Ni kweli mume wangu
haya ninayokueleza ndivyo ilivyokuwa,…nitakueleza kila kitu na wewe unifanye
upendavyo, maana nastahiki kaudhibiwa, nilikukosea sana mume wangu…najua
ulishaamua kufanya toba, na nilijua upo tayari kusamehe, kama ulivyosamehewa….’akasema
na mimi nikamwangalia huku mwili ukinitetemeka.
‘Kusamehe…unasema
nini…mke wangu mwenyewe..hapana, ..ni nani huyo rafiki yangu..’nikageuka
kuangalia mlangoni kama vile huyo jamaa atatokea.
‘Mume wangu,…sijui
kwanini nilifanya hivyo, …siku nilipogundua tu nina mimba nikajua sio ya
kwako,….’akasema na mimi nikataka kusema neno lakini nikashindwa, sauti ilikuwa
haitoki,…
‘Nikajitahidi sana
kujizuia na kuamini kuwa, sio kweli, sina mimba, lakini baadaye ndio ….nikaja kukuambia kuwa nina mimba, na wewe
ukafurahia sana,….furaha yako iliniuma sana, maana nilijua sio mimba yako,
nikajitahidi sana kujikausha lakini kiukweli sikueweza…’akasema.
‘Siku baada ya siku
nikawa naumia,..mawazo, kujuta ilikuwa kama kisu kilichokuwa kikinichoma
tumboni…sikujua lini maaumivu hayo yangeliisha, nikawa naumia, Napata maumivu makali
kila siku ya mungu inayopita…ndio maana muda wote uliniona nikiumwa…’akatulia.
‘Ikafika muda
sikuweza tena kuvumilia…’akasema
‘Na zaidi kuna
mwanamke mmoja alitembea naye, akajifungua mtoto,…oh, nilipokwenda kumuona,
huwezi amini, alifanana kila kitu na ..na ..huyo rafiki yako…’akatulia
Mwanamke mwingine naye
ilikuwa hivyo hivyo, na watatu ilipotokea hivyo nikajua, …hii haitaweza kuwa
siri tena….’akatulia.
‘Waume wa hao
wanawake walipogundua …na …walichokifanya kwa wake zao….kilifanya nizidi
kuogopa…’akatulia.
‘Nakupenda sana
mume wangu….ni hivyo tu, sasa mume wangu…, uamuzi ni wako…kuniua, sawa..hata
hivyo nimeshjifia sitamani kuishi….mateso ninayopata natamani ….oh, mume wangu
nisamehe…’akasema
‘Sikuelewi….’nikasema
sasa nikimsogelea,..nilishabadilika, nilishakuwa sio mimi tena.
‘Unataka niseme
nini zaidi mume wangu…siwezi, naumia,….niache nipumzike, hapa mwili hauna nguvu
tena…lakini mume wangu ulisamehewa,..na wewe jifunze kusamehe…’akasema mke
wangu hapo akanichefua, nikamsogelea na mikono ikakamata shingo yake.
‘Nitakuua….yaani
wewe ndio umenifanyia hivyo…’nikasema huku mikono imeshikilia shingoni, niliona
ulimi ukimtoka, lakini akili haikuwa yangu tena..haikupita muda mke wangu akalegea,
na kulembemka sakafuni, kimiaa, sikujua kama nimemkaba sana, nilipogundua hilo
nikashutuka, akili ikaanza kunirejea, nikagundua kuwa nimefanya kosa, nikainama;
‘Mke wangu..mke
wangu…usife ..hatujamalizana, usife…usife…’nikaanza kulia, nilipoona mke wangu kweli
hainuki, nikapeleka sikio puani kwa mkewe wangu kusikilizia, kimiaah, mwili
wangu ukaisha nguvu, magoti yakaanza kugongana.
Mara nikasikia
mlango unagongwa…hapo nikajua sasa nimeumbuka,sasa naenda jela, akilini nikawa
najuta, nikaijutia hasira , huku naangalia mlangoni nikijiuliza ni nani huyo
aliyegonga mlango….bila kufikiria zaidi, nikambeba mke wangu begani nikaingia
naye chumbani nikamlaza kitandani, haraka nikatoka chumbani, huku nikihakikisha
kuwa nimefunga mlango wa chumbani.
Nilipotupa macho
mlango huo wa kutoka nje, nikaukuta upo wazi, mwili ukaanza kusisimukwa, huku
nikijiuliza jinsi gani mlango ulivyofunguliwa maana huo mlango ukijifunga, ukiwa
umefungwa mpaka mtu wa ndani akufungulie, labda uwe na ufunguo.
Nikaduwaa…ina maana
kuna mtu kaingia..ni nani, na kasikia nini….
Sauti ya kuhema
ikasikika nyuma yangu, nikahisi vinywele vya mili vikinisisimuka, na hali hiyo
kwangu inaashiria hatari…kwa hali kama mimi inakuwa ni kama vile nipo vitani, kila kitu karibu yako ni adui, nikawa
nageuza kichwa taratibu kwa tahadhari kuangalia wapi sauti hiyo ilipotokea…
‘Najua kila kitu…’ilikuwa
sauti iliyonifanya moyo wangu ulipuke,….nikahisi mwili ukinisisimuka,
nikatetemeka, …unajua kutetemeka,
Sio kuetetemekakwa
uwoga, ni kutetemeka kwa hasira, mikono inataka kukamata mwili,…misuli
imekakamaa.. wanaonijua waulize, nikifikia hapo kinachoweza kuituliza hiyo
hali,sijui ….ni kitendo cha kuumiza, kuua, nilifukuzwa jeshini kwa hali hiyo…!
Naishia hapa kwa
leo ….
NB: WAZO LA LEO: Tabia
nyingine ukiziendekeza mwilini, zinaweza kuwa ni ugonjwa,…hasira, uwoga,…visirani,
kuteta, umbeya..nk, haya hujijenga taratibu, na mwisho wake inakuwa ni donda
ndugu. Tabia nyingine pia huweza hata kuathiri maumbile, …ukawa tofauti na
jinsia yako, hii ni kasumba, ambayo mtu hujijengea mwenyewe..ndugu zanguni
tujihadhari na tabia hizi, na tujaribu kuwakwepesha watoto wetu na tabia hizi.
Ewe mwenyezimungu
tujalie sisi na vizazi vyetu kujizuia na kukwepe tabia zenye kuja kuleta
madhara katika maisha yetu,…tupe afya njema tabia njema na riziki za
halali..amini.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment