‘Ina maana kweli uliwahi
kuua…?
‘Je na hilo ulitubu,
ulitubu kwa nani sasa….?
Ni maswali
niliyomuuliza , na hapa anaendelea kusimulia…..
************
‘Unataka
nifungwe….hapana, hilo la kuua, nilimuachia mungu,maana kitendo hicho
kilifanywa na wenzangu, mimi nilishirikishwa tu, maana na mimi muda huo
nilikuwa natafuta, natafuta mali, natafuta utajiri. Nilijua mali na utajiri ni
kila kitu, lakini nikuambie ukweli, hivyo ndio kila mtu anavitaka, lakini mali
ya haramu, haina usalama moyoni, asikudanganye mtu…’akatulia kidogo halafu
akasema
‘Kwahiyo kweli
uliua kwa ajili ya kupata mali..?’ nikamuuliza tena.
‘Hilo swala..hapana,
tuliache tu, siwezi kulihadithia lote….lakini sikuliacha hivi hivi, nilikwenda
kwa wanafamilia tuliowakosea, na mimi nikawaelezea ilivyokuwa…unajua tena
kwenye udhia tumbukiza rupia..na mengine tukamuchia mungu..lakini, nisamehe kwa
hilo, siwezi kuliezea zaidi kwako…’akasema
‘Mhh..hapo sizani
kama ulitubu kisawasawa, kama ndivyo ulivyoelekezwa na huyo kiongozi wako wa
imani…, uliambiwa useme kila kitu kwa wahusika,je uliwambia kila kitu,
wakakusamehe….?’nikamuuliza na akakunja uso kama hataki kuliongelea hilo, na
nilipoona hivyo nikasema
‘Sawa
nimekuelewa…’nikasema
‘Hilo…siwezi…maana
hata haya nimekuambia tu kwa vile wewe ni rafiki yangu lakini ninaumia
sana….unajua kuumia..ninateseka, sijui kama kuna mtu atanielewa….’jamaa yangu
akasema huku akitikisa kichwa na alipotaka kutamka jambo jingine nikamuwahi na
kusema;
‘Hilo tuliache tu…nimekuelewa
rafiki yangu…, turejee kwa mkeo, maana hapa ndio naona kuna ngoma ya kucheza,
mlimalizanaje na mkeo, je alikusamehe…?’ nikamuuliza
‘Rafiki yangu, kuna kitu nikuambie, wake zetu,
mungu kawajalia sana…ni wepesi sana kusahau na kusamehe..kama wasingekuwa na
uthibiti huo…sijui kama wangeliweza kuzaa tena….nitalihakikisha hili kwenye
hiki kisa..utajionea mwenyewe…’akasema
Kiukweli kutokana na yale niliyomwambia mke
wangu, siku hiyo nilijua kabisa…mke wangu hataweza kunisamehe..maana ilifiki
mahali akagoma kunisikiliza mpaka nikaona basi tena, kama hataki nifanyeje,
lakini haraka nikakumbuka jambo…
‘Mke wangu
nimekuambia, yote hayo ya kutembea na ….mdogo wako, binti wa kazi, na…yule
yatima…na …na…’nikasita na mke wangu akageuka na kuniangalia kwa jicho baya, na
kusema;
‘Sizani kama mungu
atakusamehe kwa hayo, yaani hata siamini…haya umenielezea hayo kwa nia ya kuniomba
mimi msamaha, je hao uliowatendea,tuachie mbali mdogo wangu maana kama
ulivyosema wewe na yeye mlikubaliana, mkiwa na malengo yenu…je mimi…mliyenidhulumu,…je
mimi ..oh,… ulikubaliana na mimi kuhusu hilo…hapana..
‘Haya tuche mimi,
maana…oh…je huyo binti yatima, uliyeudhulumu utu wake, ukamdhalilisha kabla ya
ndoa, ulikwenda kumuomba msamaha, akakukubalia ….usiniambie ulikwenda ukamhonga
tena, ndio akasema amekusamehe, najua naweza lakini kumbuka muda ule wakati
unamdhalilisha, alisononeka kiasi gani, sizani kama unaweza kuilipia ile hali…’akasema
‘Mke wangu usinione
hivi, ..nilumia sana, baada ya lile tendo, nililia sana…huwezi amini, lakini
yalishafanyika, sasa nifanyeje..ndio maana natubu,…nimemtaka mwenyezi mungu
msamaha, na hao nimekutana nao, ..huwezi amini mke wangu…’nikatulia
‘Nilienda mguu kwa
mguu kwa kila mmoja wao, nimeongea nao, nimewaomba msamaha..ni kweli, ….ilibidi
nifanye chochote cha kuwaliwaza, huyo binti yatima keshaolewa, lakini nilifanya
chochote cha ..kumliwaza…nashkuru sana kuwa alinielewa, akanisamehe…’nikasema
‘Ama kwa mdogo wako
naye ana mume wake kwa sasa, mwanzoni hakutaka hata kuongea naye, kwani alisema
nilimuhadaa..ni kweli nilimuahidi kuwa nitamuoa kama akishika mimba,
lakini.anyway, tuyaache hayo nisamehe tu mke wangu,..’nikasema
‘Mke wangu unajua kwa
vile wote niliowatendea hiyo dhambi sasa wana waume zao, haikuwa kazi ngumu
kwao kunisamehe..tatizo ilikuwa huyo mke wa jirani, bado kidogo..anasema we tu
yaache tu haeleweki…’nikamwambia mke wangu.
‘Mke wa jirani yupi
huyo…?’ akaniuliza
‘Mke wangu hayo ya
kwao naona tuyaache, lakini ninachotaka kukuambia ni kuwa lengo langu lilikuwa
ni mtoto, kuachia hayo mambo mengine ya kimaisha, je mke wangu wewe hutaki
tupate mtoto, niambie ukweli..hutaki mtoto?’ nikamuuliza
‘Swali langu , je
una uhakika gani kuwa ukifanya hayo yote utapata mtoto…..?’ akaniuliza
‘Una maana wewe
humuamini mungu…?’ nikamuuliza
‘Sijasema simuamini
mungu..lakini …’akasita na mimi sikutaka kumchelewesha nikamwmbia;
‘Mke wangu, usihofu
kabisa, niliongea na kiongozi wetu wa dini, si unamfahamu alivyo, akikuambia
jambo, ufanye…eeh, ukifanya kama
alivyokuelekeza mara nyingi wengi wamefanikiwa…yeye ana makarama yake…’
nikamwambia na mke wangu akatikisa kichwa kama kukataa, na mimi nikasema;
‘Mke wangu wewe ni
mcha mungu, nikuulize ukiwa na tatizo ukataka kurejea kwa mola wako akusaidie
kwanza unafanya nini…?’ nikamuuliza.
‘Najua ..hilo, kuwa kwanza unatakiwa utangulize toba, uombe
msamaha kwa yale uliyoyakosa…utubu madhambi yako…na pia na wewe uwasamehe
waliokukosea, ili moyo wako uwe safi, ndio tena uanza kuomba..lakini, swali
langu ni je uliowakosea una uhakika gani kuwa kweli wamekusamehe..na je
umeangalia ukweli wa hicho unachokitaka, kuwa kweli kinawezekana…?’ akaniuliza
‘Mke wangu mbona leo waonyesha kuwa na mashaka na imani yako
ya dini, wewe mara nyingi mambo yako unayafanya kwa kumtegemea mungu..vipi leo
unalitilia mashaka hili..?’ nikamuuliza na mke wangu akainamisha kichwa chini
kama anawaza jambo, nikahisi kuna tatizo, ..na nahisi hajaweza kunisamehe
kiukweli moyoni mwake.
Kiukweli mke wangu alikuwa mcha mungu sana,
kwani hata yeye hayo matatizo yetu yalikuwa yakimuumiza sana, aliweza kuamuka
usiku na kumuomba mungu, akikesha kwa kuswali.. alikuwa akifunga,..na kushiriki
kwenye ibada mbali mbali, kusaidia mayatima, …
Nilijua pamoja na
matatizo mengine lakini lakini hilo la mtoto lilikuwa kipaumbele kwake pia,
hebu fikiria tuna miaka kumi sasa tupo naye na hatujajaliwa kupata mtoto, mali
tulikuwa nayo lakini hatukuwa na raha nayo, ....unajua,..kama nilivyosema mali
ninayo lakini siwezi kuitumia, nina kisukari, nina presha,....ugonjwa wa
moyo, hayo kwa uchache...nitaitumiaje hiyo mali, naiangalia tu...'akasema
rafiki yangu.
‘Pole
sana…’nikasema
Kwakweli
Mke wangu baada ya kuwaza sana, baada ya kutulia sana, akanielewa, na kusema ni
sawa;
‘Mume wangu,
tumetoka mbali, pamoja na …ubaya ulionifanyia, lakini..nitafanyaje, wewe ni
mume wangu, na tunahitajika kuwa pamoja kwa kila jambo, japokuwa wewe uliamua
kufanya mambo mengine kivyako,..na matokea yake ndio haya, ni kweli madhambi
huzaa matatizo, na mola anatujaribu ili tuweze kutubia na kumrejea yeye…’akasema
mke wangu na mimi hapo nikapumua
‘Kwahiyo
umenisamehe mke wangu..?’ nikamuuliza
Hutaamini mke wangu
alisema kuwa kanisamehe ...
‘Mimi ninaweza kukusamehe
mume wangu, na ninaweza ili tuyasahau yaliyopita na tuwe pamoja, tusaidiane…maana
toba ni muhimu sana, na nimefurahi kuwa lile jambo ambalo mimi nimekuwa
nikilifanya kwa muda mrefu, …la kuwa karibu na mungu, kumuomba msamaha..sasa
wewe ndio umelianza..ni kweli mimi najua kabisa toba ya kweli ya kutoka moyoni
hukubaliwa na mola wako…lakini iwe sio kwa ajili ya….’akatulia
‘Ni mkuu wa imani
kanishauri na mimi yakaniingia, ..ndio mwanzo huo…niamini mke wangu…’nikasema
‘Sawa mume wangu,
sasa mimi sijui,…. maana nionavyo wewe lengo lako ni kupata, hutubu kwasababu
umekosa,au sio…hapo nina mashaka,..je usipopata, utasemaje, utarejea kwenye
dimwbi la maasi…?’ akaniuliza
‘Hapana mke wangu,
lengo langu ni kuwa msafi,..nataka maisha yetu yabadilike, lakini wewe
unalionaje hili, tumehangaioka wewe, kizazi chaki hakina matatizo na mimi
tatizo ni hiki kisukari na presha,ndio vimelete huu udhaifu, vikiisha mambo
yatakuwa safi..lakini haya yanatakiwa tuwe pamoja au sio..’nikasema
‘Mhh…’mke wangu
akakubali kwa kutikisa kichwa.
‘Mke wangu wewe
hulioni hili,..tukiwa hivi peke yetu huoni kuna walakini, ilitakiwa wawepo
watoto karibu yetu, hilo ni moja ya ombi langu kwa mungu…kama huna tatizo na
mimi, tatizo linaweza kuondoka..na shida sana au sio…ni haya madhambi tu,
ninauhakika toba hii ikikamilika, kila kitu kitakuwa sawa…’nikasema
‘Mungu humuombi
makosa yako kwa ajili ya kupata ….muombe makosa yako ili akusamehe, kupata sio
dhima yako, hayo yapo kwenye mamlaka ya muumba,.yeye anaweza kukupa hata kama
una madhambi, yeye anaweza kukupa kwa wasaa wake, kwa jinsi aonavyo ni sahihi,
kutubu dhambi ni kitu muhimu …haya, lakini hayo tuyaache, maana sijui mumeongea
nini na huyo mkuu wako wa imani..
‘Mimi nimekuelewa,
na ..japokuwa nimeumia sana, lakini..sioni kwanini nisikusamehe,..’nikasimama
nikitaka kumkumbatia mke wangu, lakini akaninyoshea mkono wa kunizuia akisema;
‘Ila kabla ya
msamaha wangu, kabla ya kutoa kauli yangu ya kukusamehe, ..moyoni nimeshaamua
hivyo, lakini kabla sijakutamkia ..maana na mimi ni binadamu kama wewe, na mimi
nina makosa yangu, na mimi nahitajika kutubia kwako pia kama wewe ulivyofanya kwangu
au sio...’akasema mke wangu.
`Kweli eeh mke wangu mbona itakuwa jambo jema’
nilimuambia mke wangu nikiwa na furaha tele moyoni, najua mke wangu ni mcha
mungu haswa…, hana makosa makubwa kama yangu,..kwahiyo sikutarajia kubwa zaidi
ya makosa madogo madogo.
Mke wangu aliposema
hivyo, kwanza akainamisha kichwa chini, alikaa hivyo kwa muda, baadaye akainua
kichwa, nilishangaa kuona mchozi yamejaa machoni mwake,…alikuwa akilia, kwanza
nikashikwa na mshangao, lakini baadaye nikajua ni namna ya kwake ya kutubia. Mke
wangu mara nyingi nilimfuma usiku akiwa katika ibada zake akilia..akimlilia
mola wake…ndivyo alivyo..
Alipotulia,
akaniangalia machoni na kusema;
'Mume wangu hili ninalotaka kukuambia niliapa kuwa
sitakuambia, kwa vile ninakufahamu ulivyo… niliona iwe ni siri yangu ya moyoni
mpaka kufa kwangu…, lakini kwa vile wewe umeanza, na kiukweli nimeona dhamira
ya kweli ya kutoka moyoni mwako, ...sioni kwanini nisikuambie,sioni ni kwanini
niendelee kuteseka maisha yangu yote..'akasema mke wangu.
‘Ninamuomba mola
anisamehe …na namuomba mola siri hii isiwe siri tena, na nikiitamka iwe na heri
…isije ikawa ni sababu, na kama…hutanisamehe..sijui..maana nilipata, sasa
navunja kiapo hicho…kwa vile tu..nimeona una dhamira ya kweli…’akasema mke
wangu
Kiukweli sikuwa na
shaka yoyote dhidi ya mke wangu, nilimuamini, na usingeliweza kuniambia jambo lolote
baya kumuhusu mke wangu nikakukubalia, mke wangu ni mcha mungu,
mnyenyekevu…kila mtu mtaani anamsifia, sembuse mimi… hapo sikusita kusema;
'Niambie mke wangu, usiwe na shaka, mimi
nitakusamehe, na tena nitafurahi sana, tukiwa hivi, mmoja akikosea , akimkosea
mwenzake anamwambia, tunasameheana, mimi naona ni jambo jema sana,..na huenda
mola akatusaidia tukaondokana na mashaka haya… na akatujalia tukapata
familia,…mimi hilo la watoto ..mmmh, mke wangu, wewe niambie, sema yote na mimi
nitakusemehe….'nikamwambia...
Mke wangu akaniuliza swali kwa mashaka,
'Je kweli mume wangu una uhakika,.kweli wewe
nikujuavyo …kweli utaweza kunisamehe wewe....?' akaniuliza na mimi nikasita
kidogo, na kumuangalia machoni mke wangu, nikijiuliza ni kitu gani hicho mke wangu
anataka kuniambia ambacho anahisi sitaweza kumsamehe…sikusita kumwambia
,nikasema;
‘Mke wangu ina
maana huaniamini…Usiwe na shaka mke wangu wewe niambie tu, hahaha, mke wangu,
leo naona huaniamini, kama wewe umeweza kunisamehe kwa makosa hayo
niliyokufanyia, kwanini mimi nishindwe kufanya hivyo….’nikasema.
Kabla mke wangu
hajaanza kuniambia, nikuambie kidogo kunihusu mimi, mimi nina tabia ya ajabu
sana, mimi pamoja na kuwa mpole sana kwa mke wangu, lakini nina tabia moja,
..hasira..huwa sijui ni kwanini, na nikikasirika naweza kufanya jambo ambalo
huwezi amini..na kushuka kwa hasira yangu ni mpaka nikulipizie, nifanye jambo
la kisasi..sijui ni hulka gani niliyojijengea.
Ndio maana mke
wangu aliniuliza mara mbili,…
'Je kweli una uhakika,..utaweza kunisamehe mume
wangu....?’ akaniuliza tena
NB: Tuishie hapa
kwa leo…nilipanga tukimalize hiki kisa leo, lakini kuna maswala nataka kuyaweka
sawa kwenye hitimisho la kisa hiki..ili tupate mafunzo sote…, sehemu ijayo
inaweza kuwa hitimisho la kisa hiki, ili
tuendelee na kisa chetu cha `Yote mapenzi ya mungu…’
WAZO LA LEO: Ahadi ni deni…,
wengi wetu ni wepesi sana kutamka maneno bila hata kufikiria au kuona athari
zake mbeleni. Tunaweza kufanya hivyo tukiangalia masilahi zaidi, au tukitarajia
kupata,…au kuwa na manufaa Fulani, hata
kama yale tunayoyatamka hatuna uhakika nayo. Tunajiapiza, tunakubali au hata
kukataa wakati tunajua kauli hizo sio sahihi, ni kauli za kimasilahi
zaidi..utasikia ndio nimekubali..naapa ni kweli, au sio mimi wakati kweli ni
wewe uliyefanya…
Nawausia wenzangu na kujiusia mwenyewe kuwa
tuache hizi kauli hasa zenye mfumo wa ahadi, tuwe makini nazo maana ukiahidi
ujue hilo ni deni. Ewe mola wetu tunajua wewe ni mwingi wa kusamehe, tusamehe
kwa yale tuliowahi kuahidi na tukashindwa kutekeleza, tusamehe kwa makosa ya
ulimi, makosa ya kauli zetu ….aamini
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment