‘Sawa tupo pamoja…mimi nipo tayari kwa lolote lile ilimradi
hilo deni lilipwe….na kama mnasema sio deni la kaka, niambieni ni la nani, unajua mimi ninawashangaa
kwanini hamtaki kunionyesha huo ushahidi wenu ambao umewaonyesha kuwa hilo deni
sio la marehemu kaka….nimeshawauliza mara nyingi kuhusu hilo, lakini hamjaweza
kunitolea hata ushahidi mmoja…na uwe ushahidi wa kimaandishi, ambao tunaweza
kusimama nao mahakamani…’akasema
‘Sawa wewe tuliza kichwa, natumai kesho tutaongea, na
tutaulizana maswali yetu, tuone tutafikia wapi, uwe tayari kwa hilo…’akaambiwa
‘Maswali ,… maswali..hivi mnafikiria mimi mtaniweza kwa
maswali…hahaha…haya karibuni sana…mnajidanganya kweli, …kiujumla nyie mnanipotezea
muda wangu bure….’akasema akifunika shuka, kama vile anasikia baridi .
Jioni tulirudi tena kumjulia hali, alionekana yupo vizuri
tu, na sijui kwanini docta hakutaka kumruhusu, lakini hatukutaka kulazimisha,
sasa wakati tunatoka na mama mjane nikaweza
kumuuliza;
‘Huyu docta ana udugu wowote na familia ya mume wako….?’
nikamuuliza na mama mjane akasema;
‘Mhhh, hapana huyo docta nisikiavyo, ni kaka wa ……huyo
mwanamke wake wa siri, hawa watu wana damu za nchi mbili….’akasema mama mjane
akitizama nyuma kwa mashaka.
‘Mke wa siri…una maana waitavyo nyumba ndogo au…?’
nikamuuliza
‘Mhhh…mimi sijui hayo, ila ndivyo nisikiavyo…’akasema hivyo
tu , na alionekana hakutaka kuliongelea hilo zaidi nikajua ni kwanini…
*********
Siku nyingine tulifika na Dalali, alikuwa sasa yupo katika
hali nzuri tu, na ilivyoonekana alishajiandaa kuondoka, kwani alisharuhusiwa , alikuwa
akisubiria kibali kutoka watu wa usalama, na aliyesubiriwa kufika ili aweze kukipata
kibali hicho ni mpelelezi, ….
Mimi nilipofika tu…akasimama, na kuniangalia kwa jicho la
dharau na kama kawaida yake akacheka huku akinyosha nyosha suti yake kwa
majigambo akasema;
‘Eheee, wewe mtu umefika, nakutafuta sana, ..yaani ungelijua
ninavyoku-mind…nikuambie kitu sasa hivi mimi nipo tayari kupambana na nyie
watu, wewe na huyo mpelelezi….msifikiria baada ya haya yote mimi nimerudi nyuma,
..hapana, sasa ni hivi,….. mimi nikitoka hapa nakwenda kuonana na watu wa benk nijue wamefikia wapi…kama msimamo wao ni huo
huo wa kupiga hiyo nyumba mnada basi mimi sina budi kutii amri ya mahakama…’akatulia
kama anawaza jambo halafu akainua kichwa na kuniangalia akasema;
‘Ehe, nambie…wewe ulifikia wapi…au hujaenda hata huko benki
au huko mahakamani kuwauliza, maana sikuelewi, ..haya mambo huwezi kuyamaliza
kwa kupoteza muda na mimi,…nakushauri wewe kama ndugu, au sio nenda benki,
nenda mahakamani ujuaribu kuongea na wao, au umeshafanya hivyo…?’ akaniuliza na
mimi nikabakia kimia
‘Sasa ndio hayo mambo siyataki,… mimi siwezi kuumia tena, mimi
nitakachofanya ni kutoa go a head… waendelee,
unajua, mimi nimechoka, …hapa akili imechoka, mumenisumbua sana nyie watu,
haijatokea hivi………’ alirudi kwenye kitanda akakaa huku akionyesha shauku ya kuondoka.
‘Kwahiyo wewe hupendezewi na hizi juhudi zetu za kutaka hiyo
nyumba isipigwe mnada kwa masilahi ya mjane na watoto wake….si ndio hivyo?’
Nikamuuliza na yeye akiwa ananionyeshea kwa mikono akasema;
‘Unielewe ndugu….sio kwamba sipendelei hilo, lakini je hilo
deni litalipwa eeh, na litalipwaje, na
nini, na nani,…that’s is my point…sijui
unanielewa,….’ Akaniangalia , halafu alipoona sisemi kitu akaendelea kuongea.
‘Au kama mumepata mfadhili mniambie,hahaha… sijui nani
atakubali kubeba mnzigo wote huo,….maana deni kama deni lipo pale pale, vinginevyo…..mhh,
labda benki aweni shemeji zenu,…eti,
…haiwezekani, kuna mkataba wa kukubaliana, au sio…kwamba mumeshakubaliana nao kuwa hilo deni lifutwe,
au…’akaniangalia huku akitabasamu kidharau
‘Unaona…hahaha, hamna jipya nyie…eti deni lifutwe hata kama ingelikuwa
ni mimi ndio hao benki nisingelikubali hilo..pesa yote hiyo, hebu jaribuni
kufikiria na nyie, anyaway, mimi
sijui…unafikiri, hao watu hawawezi kukubali hilo, piga ua hilo deni lipo na nyumba hiyo itapigwa mnada..wewe si
utaona tu….unajua, hata mimi sipendi
lakini sasa tufanyeje…tufanyeje sasa, hebu niambie ndugu..?’akatikisa kichwa
kama anasikitika huku akiniangalia akitaka niseme neon.
Mimi nilimtizama kwa makini, nikiwazia ….maana ukimwangalia
jamaa unaweza kusema yupo sahihi, na anavyojua kuigiza, kiukweli huwezi
kumfikiria lolote baya,…lakini akilini sikukubali, nilitaka kuthibitisha hofu
yangu, yaweza asihusike moja kwa moja…hapo nikasema;…
‘Benki wana haki na taratibu zao, na ni wajibu wao kufanya
hivyo, ..lakini kwanza ni lazima tutafute ukweli wa hilo deni, tujirizishe, …ni
kweli kuwa bado benki wanataka mnada ufanyike, na hata sijui kama watavumilia
zaidi. ..lakini hata hivyo, na wao…’nikatulia,
pale nilipoona mpelelezi anaingia na
askari mwingine, ….
‘Na wao wana…wana nini..?’ dalali akaniuliza lakini
sikumjibu, nilitulia nikimwangalia mpelelezi aliyekuwa akiingia.
**************
Mpelelezi aliingia huku moja kwa moja akimuangalia Dalali
pale alipokaa,…kwanza hakusema neno, alionekana kama kuna jambo zito, kama sio
tabia yake ya kukunja uso…nilimuona akijaribu kulazimisha kutabasamu,
alipomwangalia Dalali, na mimi anatikisa kichwa tu kunisalimia, hakutamka neno,
akasogea hadi pale alipokaa Dalali na kuanza kumuuliza hali yake…, na Dalali akawa
anamjibu kwa mkato, mkato tu kuashiria ana donge au hasira na mtu huyo.
‘Sasa Dalali…sisi bado tuna maswali mengi dhidi yako, na
kama ulivyoambiwa na docta unatakiwa uwe na afya ili uweze kupambana na misuko
suko mingine,…na nia yetu ni njema kabisa, ni kutaka kumalizana na hili tatizo,
kiufupi bado kuna utata mkubwa, ….’akaanza kusema mpelelezi, na Dalali
aliposikia kauli hiyo akataka kumkatiza mpelelezi , lakini akaghairi na katulia
, na mpelelezi akaendelea kuongea;
‘Utata upo kwenye huo mkopo wenyewe, kuna walakini nyingi
…lakini huko kwenye huo mkopo, mimi sipo sana ,nashukuru yupo mwenzetu hapa
kaamua kujitolea kuutafuta ukweli, nimemruhusu asaidiane na rasimi na sisi,
kwahiyo keshapew kibali, mkuu sasa fanya kazi..’akaniambia akinyosha mkono kama
kunisalimia.
‘Lakini pamoja na hayo…na, mimi nina yangu hatujamalizana na
wewe,,nilishakuambia awali,..sijafunga jalada la kesi ya kifo cha kaka yako..ni
ajali ndio..lakini hatujajirizisha …kuna utata pia…lakini hilo tutaulizana ,
muda ukifika…’akatulia mpelelezi
‘Unasema kuna utata, sasa kwanini msiulizane wenyewe,
na huyo aliyesema kuwa ilikuwa ni
ajali..ina maana hamuaminiani…?’ Akauliza Dalali akimuangalia mpelelezi.
‘Nilitaka tu kukuambia hayo, kuwa hata report ya ajali ya kaka yako, sijaweza kuimalizia, faili lake bado
lipo wazi, kuashiria kuwa kuna jambo linahitajia ufuatiliaji, kuna maulizo
mengi, kifupi kuna utata, lakini hili litasubiria….’akasema mpelelezi na jamaa akainua kichwa na kumuangalia mpelelezi,
akiwa kakunja uso na kusema;
‘Hayo ni yako,…mimi nijuavyo, tena sio mimi ni nyie wenyewe
mlitoa ripoti kuwa kaka alikufa kwa ajali, au sio, sasa huo utata unaokuja sasa
hivi, mimi sijui ni utata gani , niambie kuna utata gani….?’ Dalali akauliza
kwa sauti yenye kukereka, huku akikwepa kuangaliana na mpelelezi.
*************
‘Nilitaka kwanza umalizane na mwenzangu, kuhusu hilo swala
la deni, ili nione kama kuna kitu kinaweza kuingia kwenye upelelezi wangu,
unajua kazi zetu hizi, kila jambo lina umuhimu wake,…sasa kama upo tayari
tusipoteze muda,…tunachotaka kwako ni ushirikiano, ili tujirizishe,..na muhimu
uwe huru, ujitahidi kutoa ushirikiano, ili mwisho wa siku tuachane nawe kwa
amani…..’akasema mpelelezi.
‘Sawa haya niulize….unataka niseme nini, maana ukweli wote
nimeshawaambia, labda sasa ni nyie mniambie mnataka niseme nini, niambieni,
mnajua mimi nina familia inanitegemea, na kazi zangu nikiwa sipo zimesimama,
mnionee huruma na mimi…’akasema kwa sauti ya kinyonge, akageuka kuniangalia mimi;
‘Haya wewe, niambia unataka nini kwangu….’akasema
akiniangalia mimi na mimi nikaanza kwa utani;
‘Unaonekana una haraka sana, kuna mishe mishe gani
unaifuatilia…au ndio kuhusu huo mnada wa nyumba…maana nyie madalali kila kitu
kina cha juu chenu, …usiniambie hata huo mnada una asilimia yako hapo…. ,
tuambie tujue na sis tuambulie,…’ nikasema na yeye akaniangalia kwa jicho moja
…halafu akasema;
‘Ndugu, nikuambie kitu, ukiwa hai, unapumua,.. .ni lazima
upambane na maisha,..huwezi ukakaa hivi hivi tu ukafikiria utapata…., kila mtu
anahitajia maisha mazuri,sasa wewe ukilala, wengine wameamuka zamani
wanachakarika, wanayafaidi maisha na mimi nikuambie kitu, …silali, kila siku nahangaika,
natafua kwa njia yoyote…inayofaa…umenielewa,…..’akasema akitikisa kichwa kama
kukubali jambo
‘Sasa bwana Dalali, mimi naona tusipotezeane muda, tukuulize
swali, je upo tayari kutoa ushirikiano wote uujuawo wewe, ili tuweze kulimaliza
hili, kwasababu sisi tulijua baada ya huo mtihani uliokutana nao, ungekuja na
jambo jingine kabisa..’nikasema na yeye akabenua mdomo kutabasamu kizarau
Fulani hivi.
‘Kawaida tu…..’akasema hivyo
‘Mimi nilijua mitihani yote hiyo ni jinsi ya kukumbushwa jambo…..na sisi kiukweli tunahisi kuna jambo, kwenye
hili tatizo, …..kuna kitu kimejicha, ishara na dalili zinaonyesha, kuachia
mbali ushahidi ,…nsjus ksms ulivyosema
watu wanatakiwa kuhangaika, na kila nafasi unatakiwa uitumie kwa faida, lakini
kuna muda tunatakiwa kujitolea, hasa ukiangalia wahanga, hapa tuna mama mjane,
kuna watoto,…tufikie mahali tuingiwe na utu, ubinadamu….’nikasema
‘Unajua sijakuelewa….unataka kusema nini, unauhitajia ukweli
upi kutoka kwangu, hebu niambieni jamani, hivi mnataka nisema nini….?’ Akauliza
sasa akikunja sura
‘Kwahiyo ina maana mpaka sasa umeshikilia msimamo wako…?’
akauliza mpelelezi
‘Msimamo upi…?....kwanii mimi nilikuwa na msimamo gani…?’
akauliza
‘Msimamo kuwa hilo deni
kweli ni deni la kaka yako?’ akaulizwa
‘Kuhusu hilo,…’kwanza akatulia halafu akasema
‘Kiukweli msimamo wangu ni ule ule..maana mimi nimesimamia
kwenye ukweli, siwezi kusema uwongo mnielewe hivyo na nataka mjue hivyo kuwa
mimi ninachotambua ni kile kile tulichoongea awali sasa kama nyie mna jipya,
mna ushahidi nionyesheni..’akasema
‘Tunafahamu tabia yako kuwa ukitaka kitu mpaka ukipate…au
sio..?’’nikasema na akaniangalia akitabasamu kwa dharau, akatikisa kichwa na
kusema.
‘Wewe mjanja sana…sawa ndio hivyo, ….Ok, sasa niwaambie
kitu, nipeni huo ushahidi kama bado mnasema deni hilo sio la kaka, ili
tumalizane na hilo,na mimi nitashukuru sana, lakini hamuwezi kufanya hivyo
maana hamna jipya, na kwanza,….’akakatiza pale akiangalia mlangoni
‘Aheri shemeji umekuja, utuambie madalali walifika
wapi…maana hawa watu bado hawan jipya,…’akasema akiangalia mlangoni.
Shemeji yake alikuwa akiingia mlangoni…na baadaye ukapita muda
wa kusalimiana, na Dalali akauliza swali lile lile
************
‘Haya shemeji tuambie hao watu wa kupiga mnada
walikuja…maana nimekuwa nje ya dunia…?’ akauliza, na shemeji yake akasema;
‘Ni kweli walifika hao watu, kampuni gani sijui…. lakini
walikuta karatasi mlangoni kuwa mnada hautafanyika mpaka kuwe na
muafaka,…wakaondoka, lakini wao wakaweka kufuli lao pale mlangoni wakidai wao
wanachofuata ni amri ya mahakama, kwahiyo
hakuna mtu kuingia humo….’akasema mjane
‘Sasa nyie mlilala wapi..?’ nikauliza
‘Kwenye mabanda ya uwani, kuna kitanda…’akasema mjane
‘Mhh, Dalali, umesikia hayo, familia iliyopo chini yako
imelala nje, kwenye mabanda ya uwani wakati nyumba yao ipo….sasa ndio mwanzo
huo, je nyumba ikichukuliwa, watakwenda kulala wapi?’ Nikauliza na jamaa
akaniangalia kwa macho yenye hasira na kusema;
'Hivi kwanini unasema hivyo!, …ina maana mimi ndio
nimesababisha hayo yote..usinipakazie ubaya wewe ndugu…ni mimi au ni benki
waliofanya hivyo? …wewe mtu una lako jambo…wao wamelala mabanda ya uwani na
mimi nimelala wapi…? Na mimi si ndio nateseka huku, ulitaka mimi nifanyeje, na kiukweli yote
haya ni nyie, haya yangelikwisha isha tukajua moja…’akasema akinionyeshea
kidole, na mpelelezi akaingilia kati na kusema;
‘Naona tuulizane hayo maswali tuone tutafikia wapi,….maana
mimi nina kazi za kufuatilia, hili jambo linanipotezea muda…., lakini lazima leo
tufikie muafaka, ili hatua nyingine
zifuatwe, hatuwezi kuvumilia tena, kama ukweli upo,basi sheria ichukue mkondo
wake…’akasema mpelelezi, na Dalali kusikia hivyo akamtupia jicho la haraka
mpelelezi, akataka kusema jambo lakini mimi nikamuwahi
***************
‘Umesema wewe unataka ushahidi wangu kuwa ni kwanini mimi
nasema kuwa hilo deni sio la kaka yako au sio…?mimi awali nishakuonyesha ni
kwanini nimevutika kufanya hivyo na kuamini kuwa huo mkopo una walakini, ya
kuwa huenda huo mkopo hakuuchukua kaka yako…sasa kama hakuuchukua kaka yako
aliuchukua nani,….ndio hoja yetu hapo umeona eeh?.’nikasema hivyo kwa kumuuliza
na Dalali akasema kwa haraka;
‘Ndio…hiyo ndio hoja yako…, na mimi ndio maana ninasema ninataka
ushahidi wa kuthibitisha hoja hiyo yako…tusiongee tu kama hadithi, je unao
ushahidi kuthibitisha hoja yako….?’ Akaniuliza, na mimi sikumjibu mioja kwa
moja, yeye akaendelea kuongea
‘Mimi wakati wote huwa
nasimamia kwenye ukweli wa
ushahidi wa vidhibiti, kumbukumbu na nyaraka,….na kwa hili, nimethibitisha
hivyo kutokana na nyaraka za benki… ‘akatulia kama anataka mimi niongee jambo,
na mimi nikaendelea kukaa kimia.
‘Sasa ndugu, kuliko kuniuliza maswali, maswali wee…hebu
unionyeshe angalau ushahidi mmoja kuwa, ni kwanini hadi sasa unang’ang’ania
kuwa hilo deni sio la kaka wakati
benki walipeleka hadi wakili wao
mahakamani kulithibitisha hilo…na pili ni kwanini wewe badala ya kuwauliza
benkii unaniuliza mimi!’akasema , sasa kwa sauti ya ukali na nilimuona
akimtupia jicho mpelelezi, nahisi kuna kitu kimemtia mashaka.
‘Sawa nilishakuambia kuwa ushahidi wangu wa kwanza ambao
ulivuta kulifuatilia hili ni wewe
mwenyewe…’ nikasema na yeye akageuka kumuangalia mpelelezi akionyesha kwa mkono
wa kuuliza, au kulalamika lakini hakutamka neno na mimi nikaendelea kusema;
‘Sasa kama ushahidi wangu wa kwanza ni wewe mwenyewe siwezi kukuachia mpaka nijirizishe
nawe, siwezi kuwakimbilia kwanza benki , wewe ndiye ninaweza kupata njia ya
kuwaendea hao benki kuwa hilo deni sio la marehemu…umeona eeh, kwahiyo haop
benki kwangu, watafuatia baadaye kwa muda muafaka,….’nikasemaa na yeye
akatikisa kichwa kama kukataa.
‘Na ndugu Dalali ukumbuke hapa tunaongea tu, hatupo mahakamani,
nia ni kujirizisha….’nikasema na yeye hapo akacheka kweli, halafu akasema ;
‘Nilikuambia kuwa mimi nahimiza hivyo sio kwa kupenda, sio
kwamba nililikubali hilo deni hivi hivi tu, uliza utaambiwa,….lakini hadi
kufikia mimi kuamua hivyo, ujue nimeamini kuwa kweli hilo deni kaliacha kaka…’
akatulia.
'Hebu niambie, kama nimethibitisha hilo, na …. mimi kama
ndugu yake ulitaka nifanye nini, ….nikae tu, au kwa vile kafariki basi…hata
mimi siwezi kukaa kimia, mali hizo, nyumba, mashamba yalikuwa ni yake, kwanini
niache kaka ateseke huko alipo..na ni nani atamsaidia kama sio sisi tuliopo
duniani...Pili, mimi ndiye nilipewa majukumu ya familia yake, hilo sawa, siwezi
kuitupa, nitajitahidi kadri ya uwezo wngu kuhakikisha haizaliliki, lakini
kwanza ni kuhusu marehemu…’akatulia akiniangalia kwa makini.
‘Sasa nakushangaa, na kushangaa kauli yako ukisema mimi ni
ushahidi, ushahidi kwa vipi…?.’akatulia
na kumwangalia mpelelezi kama vile anahitajia msaada kwa hayo aliyoyaongea.
‘Kwanini unishangae…! Mimi si ninatoa ushahidi wangu
bwana,..au wewe ushahidi unauelewaje, au wewe ulitaka nimuite mtu mwingine ,
ushahidi wangu wa kwanza ni wewe, sawa…’ nikasema.
‘Najua ni kwanini unasema hivyo, eti ni kwa vile wewe
unaniona eti labda mimi nakomalia hilo deni, kwa masilahi yangu …labda, nikuambie kitu kama unafikiria hivyo, unakosea
kabisa…, na huo ushahidi kama huu, eti ushahid
wa kwanza ni mimi mwenyewe, huo hauna nguvu..toa ushahidi mwingine…,’akasema
‘Kwanza kabla hatujaenda mbali, kuna kitu nataka shemeji yako anikumbushe
kumuhusu marehemu mume wake, eeh,…..’nikasema na Dalali akawa kama kashtuka,halafu
akatulia, halafu akageuka kumuangalia shemeji yake huku akisema;
‘Hapana hilo sikubaliani nalo…sitaki shemeji yangu
umuhusishe na hili, hili ni kati yangu mimi na wewe…shemeji hawezi kuvumilia
hii mikiki mikiki, ….mnafahamu afya yake
ilivyo, kama ni maswali niulizeni mimi….’akasema akipiga kifuani
‘Nafahamu hilo……, lakini ni hivi, wewe huwezi kufahamu kila
kitu kumuhusu kaka yako zaidi ya mke wake…, au sio…?’nikauliza na yeye kwanza
akamuangalia tena shemeji yake, na kabla hajajibu hilo swali wakili wake
akafika, na kukawa na muda wa kusalimiana….
‘Ohh, muheshimiwa aheri umefika…, hawa jamaa wameniwahi ,
lakini usijali, mimi nitamalizana nao, wala usiiingilie, kaa hapo usikilize tu,
haya niachie mimi, huu ni mpira wangu, hawa hawaniwezi , si unanifahamu nilivyo, mimi
nilitakiwa niwe wakili ,lakini ndio hivyo…..’..akasema na kweli wakili wake akakaa na kutulia, hakusema neno. Wakili
wake hakutaka kuingilia maana tangia awali alishaambiwa hivyo kuwa yeye ni
msikilizaji tu.
Mama mjane, akaamua kuingilia kati na kusema;
‘Jamani mimi samahanini sana…,mimi nisingelipenda kuongea lolote maana mimi nilisha
waambia tokea awali kuwa yote nimeshamuachia mungu, nikifanya lolote zaidi kwa
sasa kulalamika, ku-ku-hapana, jamani mnionee huruma, nimechoka, mimi namuamini
mungu wangu,…na nasubiria mapenzi yake
tu yatime….., basi….’akasema huyo mama mjane.
naona…ahsante sana shemeji yangu….’akasema Dalali,
akitikisa kichwa kama wafanyavyo wahindi wakikubali jambo
‘Dada,ni kweli, nimekuelewa sana, lakini kwa hili mimi
nahitajia kauli yako ya ukweli , na hilo siwezi kulipata kwa mtu mwingine zaidi
yako wewe. Mume wako hayupo hawezi kujitetea, lakini wapo waliokuwa wakimfahamu
na kumjua vyema, na hakuna anayeweza kumfahamu vyema yeye zaidi yako wewe
uliyekuwa mkewe…,na naitaka kauli yako ili kila mtu aisikie…’nikasema na jamaa
akadakia akisema
‘Lakini ulimsikia mwenyewe shemeji alivyosema, kasema hapendi kuongea lolote kuhusiana na hili…..,keshamuachia mungu, sasa kwanini
unataka kumlazimisha…ina maana wewe una ubavu zaidi ya mungu…acha kuchezea
imani ya shemeji yangu…’akasema Dalali, na shemeji yake ghafla akasema;
‘Kwani mlitaka kuniuliza kuhusu nini..?’ akauliza mama mjane
na kauli hiyo ilimfanya Dalali abakie mdomo
wazi, akataka kusema neno lakini akasita, na mimi sikutaka kuchelewesha,
nikamuuliza shemeji swali …
NB, Naona tuishie hapa ili kuwekana sawa, kujikumbushia kisa
kilivyokuwa kikiendelea, swali hili linafungua mambo, je ni swali gani, na kwanini
Dalali anakwepa shemeji yake asiulizwe….
WAZO LA LEO: Usiogope kuusema ukweli pale panapohitajika,
usiogope kwa vile labda ukiusema huo ukweli, mtu Fulani au bosi wako,
atakasirika, au huenda ukapoteza
kazi,…Ukweli huo utakulinda leo hadi mwisho,…kuliko kusema uwongo, kwa
masilahi…!
Ni mimi:
emu-three
1 comment :
raha kweli like a movie.
Post a Comment