Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, May 26, 2016

YOTE NI MAPENZI YA MUNGU-9

 


Simu ikawa hewani na sauti iliyosikika ilikuwa sauti ya kukatika katika, yaonyesha huyo mtu yupo kwenye hali mbaya, ….na mawasiliano yalikuwa sio mazuri…

‘Da -da-lali, ha-ha-halooh,…’ilianza hivyo, na dalilia akasema
‘Haloo ni mimi kuna nini…mta-alamu?’ akauliza dalali akimgeukia mpelelezi, na mpelelezi akamuashiria aendelee kuongea.

Sauti ilikuwa ni shida,….mwanzoni nilijua labda huyo mtaalamu alikuwa mikononi mwa polisi na sasa yupo kwenye mateso…lakini kwa hali kama hiyo polisi wasingemruhusu kuongea kwenye simu,…labda kama kuwe kuna kitu wanakihitajia wakipate…, lakini kwa jinsi alivyozidi kuendelea kuongea  nikagundua vinginevyo, sauti ikaendelea kusema;

‘Da-dalali wewe mmmmh, ….’akatulia akigugumia,

‘Mtaalamu vipi…kuna nini,….mbona unaongea hivyo?’ akauliza Dalali akihisi na wasiwasi.

‘Yaani wewe…ndi-ndio unanifanyi-a oooh, hivi…’sauti ikatulia na mngurumo wa kugugumia ukawa unasikika,  halafu sauti ikaendelea kusema;

‘Sasa sikiliza mmmh,….ehuuuh, …mimi nimekwepa kuwaambia polisi mambo yako….eeeh, oooh,unasikia lakini ujue kuwa ,….sitaweza kuvumilia zaidi, nilichoongea nimeongea, na ni kweli sikutaka kuwaficha…’akawa anajitahidi kuongea vyema, na kauli hiyo ilimfanya dalali ageuze jicho kumuangalia mpelelezi.

‘Hata ….oooh, najiuliza… ni kwanini ni – ni-teseke hivi,….aaah…., ‘sauti ikatulia, nilimuona Daalli akihangaika nahisi alikuwa akitafuta njia ya kuizima hiyo simu, lakini mpelelezi alikuwa ndiye kashikilia ile simu kuhakikisha kuwa dalali haizimi .

‘Na….na….wakati ni mambo yenu…sasa …ooh, nasema..mmmh,….oooh, utajua mwenye,. ‘akatulia

‘Mtaalamu,….’akataka kusema lakini mwenzake akaendelea kuongea

‘Nisikilize..sina muda….kwanza ujue… walichonifanya, ooh….watanijua mimi ni nani….na …si…achilia mbali…..mazindiko,..kazi  yako, mimi basi, …., sasa ni juu yako…hayo nime-ya-ondoa…utajua …we-we- mwenyewe…usinitegemee mimi …ni –wewe ..oooh, oooh..ooh….mwenyewe…’kukawa na ukimia kidogo, na Dalali alikuwa anataka kukata simu, lakini mpelelezi akamzuia, na huyo jamaa akasema;

‘Unajua wengi hawanielewi…hahaha….mimi, ….mtaalamu,…hahaha..oooh, nitawafanyia kitu mbaya sana, hawa watu..oooh, …wanafikiri mimi ni mtu hivi hivi tu,…achachachacha…..mhhh, mhh, tatizo ni masharti,…haya mambo ya mizimu, wame-goma, kosa…nimekiuka miiko….kosa, …..yatima…ooh, yatima,…oooh,….haikutakiwa hivyo….ooh, umeniponza…umeniteketeza…lakini….kabla ya mimi,ni wewe….naapa,…utajuta…’ akatulia.

‘Vipi mtaalamu ….kwani kuna nini, wanakutesa  polisi au?’ Akauliza dalali.

‘Aheri wange…nitesa ,….aaah,  mimi wanitese…hahaha…tatizo, ni miiko… hainiruhusu, lakini, siwezi tena….ngoja, kwasababu kufa nitakufa tu……oooh, lakini kwanza nitaanzia kwako, sijawahi kufanyiwa hivi …hata siku moja….mmh, wewe umeniharibia kazi yangu, kwa tamaa zako,….taireeeeh, mizimu taireee….hapana..hapana…sitaki kufaah…hapana…oooh’akatulia

‘Mtaalamu kuna nini ndugu yangu…?’ akauliza dalali sasa akionyesha wasiwasi, lakini jamaa alikuwa kama analia..ni kilio cha kweli, halafu sauti ikasema;

‘Mimi….ndugu yako, ..oooh, wakati nakufa…unaniacha nakufa, udugu ga-gani -ooh, huo…..yote haya uliyayataka wewe na…na huyo…’hapo akatulia

‘S-sasa kabla sijafa, maana sizani kama nitaishi, naona wahenga wananiita, oyoyoyoyoyo…oyoyoyo, mhhh, kifo kichungu….oooh, sitaki kufa …oooh, sifiiiih, oooh…’kukawa na ukimia kidogo.

‘Mtaalamu.upo wapi…?’ akauliza dalali akigeuka kutaka kuondoka. Na mpelelezi akamuashiria atulie

‘Nipo….karibu kuelekea ahera, …mhhhhhh, sasa sikiliza, hata nikifa, nataka pesa yangu uifikishe kwa familia yangu..umesikia,….ooooh, ni-ni ahidi,…dalali niahidi…na nataka wewe, sio huyoo…ni wewe….’akatulia
‘Umesikia,..oyoyoyoyo, oyoyoyo, wahenga wa jadi,…oyoyoyo…..chachacha….Dalali ,unasikia...usipofikisha hiyo  pesa kwa familia yangu kitakachokupata hutaamini, nitakutokea kama mzimu, na kuyaangamiza maisha yako, umenisikia, …’akatulia

‘Mtaalamu sijakuelewa, pesa ipi…?’ akasema akigeuka kumuangalia mpelelezi.

‘Pesa ipi….unadiriki kusema hivyo….oooh, utaumia, wewe mtu utaumia, unamsikiliza huyo…hahaha, eti pesa gani,…..una hatari wewe,…kweli nimeona, ….niliona, lakini nilifumba macho,..kuna hatari kubwa mbele yako….umegusa kubaya…mmhh, siwezi kukusaidia tena….kwaheri,…utajuta,….utanikumbuka….uta—ooh,’akatulia, kulikuwa kama minong’ono ya kuimba, au …sauti ilikuwa ndogo, halafu;

‘Da-la..li….umenisikia…..’akatulia

‘Kwani kuna nini mtaalamu..upo wapi… nimekuelewa, usiwe na shaka, nitafanya hivyo, utakavyo…usiniangamize mimi ni ndugu yako…upo wapi.?’ Akauliza Dalali.

‘Usiniulize nipo wapi…mjinga mkubwa wewe…wewe ni mpuuzi tu, …utapata shida sana..utatamani kifo hutakipata, aheri yangu mimi…oooh, oooh, ooohh…oookokokokoh…umechelewa---koroooooh.’sauti ikakata, na kukawa kama kukoroma hivi.

‘Mtaalamu, mtaalamu…..mtaala….m’Dalali akawa anaita, lakini zaidi ya sauti za uvumi wa upepo, hakukuwa na sauti nyingine.

Dalali akashika mikono yake kama kawaida yake, anavishikisha viganja mbele kama anaomba halafu anavipuliza…, akasimama, akashika kichwa,…akageuka kuangalia mlangoni, halafu akamgeukia mpelelezi, akamgeukia shemeji yake….halafu akanigeukia mimi, akanikunjia uso kwa hasira, akataka kuniambia jambo lakini hakusema, akamgeukia mpelelezi, na kusema;

‘Tafadhali mkuu..nipo chini ya miguu yako, …huyu mtu anahitajia msaada wangu, ..siwezi kumuacha kwa hali hiyo, …niache niende nikamuone…’akasema

‘Sasa unajua huyo mtu yupo wapi…?’ akaulizwa na Mpelelezi

‘Atakuwa polisi, …wanamtesa huyo…nyie polisi kwanini mnafanya hivyo….’akasema

‘Unahakika na unachokisema…?’ akauliza mpepelezi

‘Uhakika gani?’ akauliza akimtolea macho mpelelezi

‘Kuwa polisi wanamtesa,…polisi wamtese halafu wamuachie simu aongee na wewe….?’ akaulizwa

‘Kwa mara ya mwisho mlisikia nyie wenyewe akisema kakamatwa,…sasa alikamatwa na nani , …?’ akauliza na mpelelezi akachukua simu yake kutaka kupiga lakini kabla hajafanya hivyo simu yake ikaanza kulia, akaangalia mpigaji,.

Hakuipokea hapo akatembea kuelekea nje huku akiisikiliza, hakuchukua muda akarudi, na alionekana mwingi wa wasiwasi usoni, akamuangalia Dalali kwa makini, halafu akasema;

‘Wewe unajua wapi mtaalamu alipo , ..?’ akauliza mpelelezi

‘Sikuelewi afande…’akasema dalali akionyesha uso wa mashaka na alikuwa anahaha, kachanganyikiwa kabisa,  hapo nilimuona kumbe huyu jamaa naye anachanganyikiwa hivyo!

‘Huyu mtu katoroka polisi, na wakatii anatoroka akapigwa risasi ya mguu, lakini aliweza kuwakimbia polisi, …alikimbia kama anapaa….ndivyo walivyoniambia…’akasema mpelelezi

‘Mimi nawaambia huyo mtu si wakawaida, mumeona wenyewe…..’akasema dalali hapo akawa kama kapaat ahueni.

‘Kama sio wa kawaida mbona hakuweza kuzuia risasi,….na huko alipo atakuwa kwenye hali mbaya, sasa eleza wapi anaweza kupatikana ili akaokolewe….’akaambiwa dalali.

‘Akaokolewe au akakamatwe, na mimi siwezi kujua wapi alipo ….’dalali akasema sasa alionekana kama hali imemrejea , aliingiwa na unafuu fulani.

‘Usipoteze muda, wewe mwenyewe umemsikia hapo, …kwa jinsi walivyoniambia atakuwa kapoteza damu nyingi sana,…sasa uache ndugu yako afe,….’akaambiwa

‘Hawezi kufa huyo,..i mtaalamu ..nyie hamjamfahamu vyema, Yule aliwahi kupambana na majamazi akakatwa koromeo, wakajua wamemuua, lakini akajizuia kwa shingo kuiminya, hadi akafika hospitalini..akapona, iwe hiyo risasi ya mguuni….’akasema

‘Umemsikia hapo…hiyo ni sauti ya kukata roho…na ufahamu huyo mtu akifa, makosa yote yatakuwa kwako, ni bora twende tukamuokoe ili adhabu za makosa yake ayabebe yeye mwenyewe…’akaambiwa

‘Kwani yeye ana makosa gani,…au mimi nina makosa gani…?’ akauliza

‘Unapoteza muda….sema wapi jamaa yako yupo…hapa unacheza na uhai wa mtu, sema wapi anaweza kupatikana…’akaambiwa kwa sauti ya ukali, na hapo akanywea na kusema;

‘Hata sina uhakika….’akasema kama anawaza, akapiga simu, lakini sasa simu inasema haipatikani.

Dalali akakunja uso kama kufikiria halafu akasema;

‘Lakini sina uhakika,…twendeni tukajaribu….’akasema na mara mpelelezi akawasiliana na watu wake haikuchukua muda jamaa wawili wakafika, wakamfunga pingu Dalali

‘Sasa kwanini mnanifunga mimi pingu….?’ Akauliza

‘Unaisaidia polisi, usiwe na wasiwasi…’akaambiwa na kitendo kile kilimfanya Dalali akunje uso aliponiangalia, na shemeji yake alikuwa sasa kasimama, kama anataka kufanya jambo, lakini hakuweza akabakia kusimama tu.

Sasa mbona mwamfanya hivyo shemeji yangu…’akaweza kusema hivyo

‘Shemeji, …usijali nitayamaliza…’akasema dalali…na mimi nikasimama nikianza kuwafuta hao watu, na mpelelezi akaniambia;

‘Na wewe tusubiri hapa hapa, usiondoke….’mpelelezi akaniambia , nikatulia na kugeuka kumuangalia shemeji na watoto sasa walishaamuka, lakini bahati nzuri hawakuhai kukiona kile kitendo cha baba yao mdogo akitoke nje na  polisi.

                                 ************

Mimi nilibakia pale na Yule mama mjane, tukiwa na tunasubiria kwa vile  nilipewa amari nisondoke pale, nikaona nitii amri nione mwisho wake utafikia wapi,  masaa yakapita, ….

‘Shemeji,  eeh, dada wewe waandalie watoto, naona usiku unaingia,….’nikasema

‘Kila kitu kipo tayari…labda wewe tukuandalie chakula…?’ akaniuliza

‘Hapana….nyie endeleeni, nitaondoka muda sio mfupi…’nikasema

‘Uondoke unieche humu ndani, …siwezi kukaa peke yangu na watoto,….’akasema

‘Kwanini, mbona mlikuwa mnaishi wenyewe humu ndani…?’ nikamuuliza

‘Mara nyingi alikuwa akija jamaa yao shemeji, au mlinzi..hata hivyo..bado ukiwa chumbani usiku kuna vitu vya ajabu vinatokea, mara mipaka inalia…hata hujui wametokea wapi…mara mipanya…kunatisha kweli kweli…’akasema

‘Nina imani sasa havitatokea…jipe imani , na mungu atawalinda…’nikasema

‘Kwanini, visitokee, wakati nilipokuwa ndani, nilisikia sauti ya ajabu ndio maana nikaamua niondoke kwenye hii nyumba, kwanini una uhakika huo…?’ akauliza

‘Muamiini mungu wako, na kabla ya kulala hakikisheni mumemuomba mungu …fanyeni ibada, swalini….ombeni, mtayashinda haya yote, kama haya ulishamkabidhi mungu, ujue sasa ushindi unakuja,…’nikasema na mdada huyu akaniangalia kwa muda bila kusema neno. Halafu akasema

‘Nakushukuru sana kaka yangu…mungu akuzidishie…’akasema

‘Nendeni…mkapumzike, mimi nipo hapa kwa muda….’nikasema na kweli.wanafamilia wale wakaingia chumbani kwao kujipumzisha na mimi nikabakia pale mlangoni nikisubiria, huku nikawasiliana na watu wangu.

                                           ***********

Watu wangu walisema kwa hivi sasa wanashindwa kufanya jambo, kwani polisi wamewazuia,na wanafuatiliwa , kwahiyo wao wameona wasubirie kwanza wakitegemea wasamaria wetu wanaojitolea kutupatia taaifa ndani ya kundi lao;

‘Au mkuu unasemaje , tuendee, hatushindwi kufanya hivyo , lakini inaweza kukuletea athari kisheria…’akasema mmoja wa watu wangu

‘Msiendee…mtanipatia taarifa ..kesho, au…’nikatulia nikiwanza jambo, halafu nikakata simu, nilichukua ile simu yangu niliyokuwa nimeweka mezani na kuanza kusikiliza yale yaliyojirekodi mle, …kuna kitu nilikuwa nakitafuta…

Mara simu yangu nyingine ikalia, alikuwa mmoja wa watu wangu akasema  mtaalamu keshapatikana, lakini akiwa hana fahamu, kumbe wakati anatoroka alipigwa risasi ya mguuni, na amepoteza damu nyingi sana, na  hali yake kwasasa ni mbaya sana, inawezekana asipone …

‘Vipi huyu mtu wetu, Dalali, kaweza kuongea lolote na polisi…?’  nikauliza

‘Mpaka sasa kashikiliwa kwa ajili ya kuisaidia polisi, ila kakataa kusema chochote, anataka wakili wake awepo…, lakini polisi hawajamruhusu kwa hilo, na pia anataka kuongea na wewe…!’

‘Kuongea na mimi, kuhusu nini…?’ nikauliza kwa mshangao

‘Anasema wewe ndiye umeyasababisha yote hayo, kwahiyo anataka mkabiliane wewe na yeye ili athibitishe mbele yako kuwa yeye hana kosa…’nikaambiwa

‘Atathibitishajekwangu, wakati mimi ananiita tapeli…na polisi wamesemaje…?’ nikauliza

‘Kwa hivi sasa walikuwa wakihangaika na huyo mtaalamu, na walikwenda kuchunguza nyumbani kwake, wamekuta familia yake haipo…imeshaondoka kuelekea  kijijini kwao, ni kama walishafahamu kuwa hilo litatokea…’akasema

‘Kijijini kwao ni wapi…?’ nikauliza lakini kabla hajajibu hilo nikauliza swali jingine kwa haraka;

‘Kwanini polisi hwajaruhusu wakili wa dalali aitwe,na ni nani huyo?’ nikauliza, na kukawa na ukimia, nikasema

‘Halloh vipi…kuna nini kinaendelea mbona upo kimia, kwani upo wapi …?’ nikauliza

‘Hebu subiri nitakupigia naona kuna kitu kinaendelea …’akasema mtu wangu na kukata simu, na mara simu yangu ikaita tena, na aliyepiga simu kwa sasa alikuwa mpelelezi, akaniambia nipo huru kuondoka ila kesho nahitajika kituo cha polisi .

‘Nahitajika polisi kwa kosa gani?’ nikauliza

‘Dalali anataka kuongea na wewe..’akasema

‘Kuhusu nini…?’ nikauliza

‘Kasema yote umeyaanzisha wewe na yeye anataka kuthibitisha kwako kuwa yeye hana makosa,…kwahiyo anataka muendelee na hayo maswali yako, na mwisho wake itathibitika kuwa kweli hana makosa hahusuki…’akasema

‘Kwahiyo mimi sio tapeli tena…?’ nikauliza

‘Ndio anataka kuthibitisha kuwa wewe ni mwongo, umempakazia makosa na sisi polisi tumekuamini hivyo….’akasema

‘Kwani nyie polisi mlinifuata mimi, ..au nikutokana na uchunguzi wenu?’ nikauliza

‘Ni manenoya mfa maji…na sisi hatutaki kumharakisha kwani kuna mambo bado tunayafuatilia, na mlango wa kuyapata mambo mengine ni kwa kupitia kwake, …ndio maana tumemkubalia ombi lake,….kesho ufike saa tatu…’akasema mpelelezi

‘Je wewe umeshamuuliza yale maswali yako uliyoyataka kumuuliza?’ nikamuuliza

‘Hataki kunijibu, …anasema kwa hivi sasa hataongea lolote mpaka wakili wake awepo, na mpaka amalaizane na wewe..kwani chanzo cha yote ni wewe…’akasema

‘Vipi kuhusu mnada wa kesho,  maana ni amri ya mahakama, je huo mnada utakuwepo….?’ Nikauliza

‘Huo mnada wa kesho eeh, ngoja,…bado tunafuatilia taratibu zake,…japokuwa hakimu hajasema lolote, yote itategeema hiyo kesho…’akasema mpelelezi.

‘Je ulitaka kumuuliza nini Dalali, mnahisi kaka yake hakufa kifo cha kawaida, ….na kwanini mnauliza hayo maswali hivi sasa?’ nikauliza

‘Kiukweli awali nilizuiwa kuendelea na hii kesi kipindi cha nyuma, lakini nilishangaa kuambiwa niendelee nayo hivi sasa….nahisi ni kwa vile jalada lake lilikuwa halijafungwa, na mimi nimewaambia siwezi kulifunga mpaka nihakiki baadhi ya mambo…, kiukweli ajali ya huyo jamaa ilionekana ni ajali ya kawaida, lakini sio kutokana na uchunguzi wangu….hata hivyo, kwa vile wanafamilia wenyewe walikuja kusema hawahitaji uchunguzi zaidi, ikabidi tuachane nayo….’akasema

‘Unahisi  ni kwanini?’ nikauliza

‘Hata sijui….sababu walizotoa wao ni kuwa  ndugu yao ameshakufa, hawataki mambo mengine, mambo mengine yatakuwa ya  kifamilia zaidi..na hiyo ajali ni ya kawaida tu….na ilitokea hivyo kwani  watu wa usalama barabarani  walihibitisha kuwa ni ajali ya kawaida, gari lilishika moto, na dereva akashindwa kutoka kwa mshituko… wao waliangalia kwa upande wao, kwa upande wangu nilikuwa bado naendelea na uchunguzi….’akasema

‘Unahisi kuna mtu alikuwa nyuma ya hilo, labda…anajuana na Dalali, labda kuna mgawo, akashinikiza mambo hayo yafukiwe, iishe kihivyo au…?’ nikauliza

‘Hapana…ni kuwa kipindi hicho kulikuwa na kesi nyingi sana, na hiyo kesi ilionekana haina uzito, kwa vile uchunguzi wa awali wa watu wa usalama barabarani uliona ni ajali ya kawaida tu…na taarifa ya dakitari ilionyesha kuwa dereva yaani huyo marehemu alipatwa na mshituko kabla ya ajali….mshituko huo ndio uliomfanya ashindwe kulidhibiti gari….na moto ulipoanza kuwaka hakuweza kujiokoa…’akasema

‘Kwahiyo wewe uligundua nini,…?’ nikauliza

‘Nilichogundua , ni kuwa kuna sababu ya hiyo ajali, …na nilikuwa naitafuta sababu hiyo ni nini, ulipoanza kumuhoji huyo mtu, kuhusu hilo deni, nimeweza kuunganisha kati ya hilo deni na hiyo ajali…na huo mshutuko una sababu, yaonekana marehemu alikuwa anaongea na simu…sasa alikuwa anaongea na nani, je hiyo simu ndiyo ilisababisha hayo…na mabaki ya hiyo simu hatukuweza kuyaona…kipindi hicho nilitaka kufuatilia kampuni ya simu…lakini nislishindwa, wangeliweza kutafuta namba yake na kuweza kuyanasua hayo mazungumzo…lakini sikufanikiwa…..’akasema

‘Kwahiyo unataka kusema ajali hiyo ilipangwa au….?’ nikauliza

‘Hayo tutayajua hapo kesho, ndio maana hata mimi nimependelea wewe uendelee kumuhoji huyo mtu na mimi nitakuwepo…’akasema

‘Mhh..lakini mimi , japokuwa hajakubali, kile nilichokitaka kwa kiasi kikubwa nimekipata,…sikuhitajia kuongea naye zaidi, labda tuje tukutane niwapatie ushahidi wangu tuliokuwa nao…vinginevyo hata nikimuhoji itakuwa  ni hitimisho tu,…na…’akanikatiza

‘Hilo hitimisho ndilo nalitaka,…..kwani  japokuwa vijana wangu na wamelifanyia kazi hilo , kutakakujua kuhusu hilo deni, lakini bado kuna maulizo mengi, maana kilakitu kipo sahihi,…hata hivyo kuna mambo wameyagundua,lakini bado kuna maswali mengi ya kujiuliza….’akasema

‘Wao wamegundua nini….?’ Nikamuuliza

‘Walichogundua…ni hayo hayo,….naona hayo tutayajadili hiyo kesho,kwanza nataka kusikia kauli yake, nitaweza kuingilia kumuuliza maswali japokuwa mimi kanikatalia nisimuulize mpaka wakili wake awepo, sitojali sana, ila nataka kabla uanze na yeye, ili nikiingilia kati iwe rahisi kumnasa….’akasema

‘Kwahiyo vijana wako hwakugundua jambo jipya, mbona huniambii,…nakuuliza hivyo ili kesho nijue jinsi gani ya kumbana….’akasema

‘Kiukweli, vijana wangu walichogundua ni hayo hayo yaliyokuwa yametokea kipindi hicho , na tukio hilo japokuwa bado halina uhakika,linaonekana lilishirikisha watu wengi, na kati ya hao wengi , miongoni mwao hatujaweza kuwapata, sasa tulijaribu kuangalia kwa upande huo wa benki, wafanyakazi wengi wa kipindi hicho hawapo, na wengine walikuwa wameshafukuzwa kazi, ….

‘Kwahiyo kiujumla kulionekana kulikuwa na tatizo, kuna namna ilifanyika, swali likabakia je kuna uhusiano gani kati ya ajali na hilo deni…..’akasema

‘Je vijana wako waliwahi kuwahoji hao wafanyakazi, ambao huenda walihusika…?’ nikamuuliza

‘Wachache….wengine wamekataa kutoa ushirikiano, na hata hivyo, ikibidi nguvu za dola zitatumika, ili muda ukifika wawepo mhakamani….’akasema

‘Ni kuwa hawapatikani au hawataki kujibu maswali, kuelezea ukweli….?’ Nikauliza

‘Yote mawili,….maana wengine kuwapata inachukua muda, hata hivyo hao waliopataikana ni kama wamesahau au wanajifanya wamesahau..….nina imani hadi kesho tutakuwa tumeshawapata wote muhimu, tutawakumbusha tu ,….ndio maana nikasema  sasa mlango wetu wa kulimaliza hili ni kwa kupitia huyo huyo dalali, je kuna mahusiano gani kati ya hilo deni na kifo cha kaka yake…’akasema

‘Je wakili wake keshapatikana?’ nikauliza

‘Kesho atakuwepo, kwahiyo unatakiwa uwe makini katika kumuuliza hayo maswali yako, ulenge kwenye jambo sio dhana.., si unamfahamu huyo wakili wao alivyo mkorofi sana, sema na yeye hapendi kuingiliwa kazi yake…mteja akimuingilia anaweza kukasirika na kuicha hiyo kazi hewani…hata hivyo , mara nyingi mimi simuamini huyo wakili, natafuta jambo, nihalalishe hisia zangu,lakini bado sijalipata, ni mjanja sana …’akasema mpelelezi

‘Swali jingine kabla hujakata simu, ni kuhusu  huyu mjane na watoto wake, maana walisema kesho wanaondoka, niwaambieje…?’ nikauliza

‘Hawezi kuondoka kwa hivi sasa, wameshapelekewa taarifa,  ila kama utapitia hapo,…mwambie aendelee kusubiria,… kwani vipi hali ya mtoto wake ulipoondoka..?’ akauliza

‘Hajambo….sijaona dalili yoyote ya homa, ila mama mjane anasema humo ndani kuna mambo ya ajabu ajabu yanatokea, ….sijui hilo linatokana na huyo mtaalamu na mambo yao waliyoyapandikiza humo ndani, au ni kuchanganyikiwa tu kwa huyo mama…’nikasema

‘Kuna kitu kingine kimejitokeza, …naona utapenda kukifahamu…’akasema mpelelezi lakini alikuwa kama anasita kuniambia, hata hivyo  akasema

‘Dalali ana nyumba ndogo, hii nyumba ndogo tuliona  ikatusaidia sana…’akatulia

‘Kwanini….?’ Nikamuuliza nikikumbuka vijana wangu walivyoniambia kuhusu huyo mdada, na mpelelezi akaongea yale yale niliyoambiwa na vijana wangu.

‘Huyo mdada…., sasa hivi ni tajiri sana, anamiliki nyumba nne, za nguvu, uchunguzi wetu unaonyesha ujenzi wa nyumba hizo ulifanyika kipindi cha nyuma baada ya kufariki marehemu,…au  inawezekana ujenzi ulianza nyuma kidogo kabla hajafariki huyo marehemu,…’akatulia

‘Unahisi huenda huo mkopo ndio ulifanya hiyo kazi….?’ Nikauliza

‘Ndio hapo, ….nakupa hilo kama angalizo,…ukimuhoji  vyema huyo jamaa tunaweza kuligundua hilo…’akasema

‘Hilo la huyo mdada, au nyumba ndogo, nalifahamu sana, na hilo lina ugomvi mkubwa kati ya Dalali na mke wake wa ndoa…vijana wangu walijaribu kulifuatilia, lakini si unajue tena, hizo ni kazi zenu,tunaogopa kuwaingilia, ila yaonyesha kuna mgongano kati ya mke na hiyo nyumba ndogo…. je hiyo nyumba ndogo mumeshaipata….’nikasema na kuuliza

‘Huyo mdada katoweka,….’akasema

‘Katoweka , kwa vipi…?’ nikamuuliza

‘Kiukweli,…kwa hivi sasa haijulikani hasa wapi alipo…na tumekuja kugundua kuwa nyumba mbili alizokuwa akizimiliki keshaziuza...na nyingine bado zinatafutiwa soko na madalali….’akasema mpelelezi

‘Haiwezekani..mbona vijana wangu hawajaniambia hilo…na je Dalali analifahamu hilo…?’nikasema na kuuliza

‘Ni siri kubwa sana, Dalali hajalijua na kama anajua basi itakuwa ni siri kubwa kwake…nahisi vijana wako hawajakuambia kwenye simu…lakini kwenye ripoti yao utaliona hilo,…’akasema

‘Sizani kama madalali wenzake wanaweza kuifanya hiyo kazi bila jamaa kufahamu…..’nikasema

‘Tutaliona hilo kesho, ….unafikiri nyumba hizo zimeuzwa zamani…ni jana tu , na muda huo dalali alikuwa na wewe huko…na ….’akasema

‘Na kwanini huyo mdada atoroke….unahisi kafanya utapeli, kumtapeli mwenzake…?’ nikauliza

‘Huyo mdada katoroka usiku…nahisi na gari la kukodi,…asubuhi vijana walipofika waliambia huyo mdada kaenda site…kuna sehemu walikuwa wanajenga….wakafika huko, wakaambiwa kaenda kununua vifaa vya ujenzi…huko kwenye vifaa vya ujenzi wakaambiwa kweli alifika…lakini kaenda kutafuta vifaa vingine…aliweka alibi ya hali ya juu….’akasema

‘Una maana gani kusema hivyo….?’ Nikauliza

‘Ina maana aliweka ushahidi ambao ulionyesha kuwa yupo…kumbe yupo njiani anasafiri….na hakuna aliyejua kuwa katoroka hadi ilipofika jioni hii,….’akasema

‘Sasa atakuwa wapi, na kwanini atoroke…?’ nikauliza

‘Kwa uchunguzi wa haraka,yawezekana atakuwa kavuka mipaka yupo nchi ya jirani, ambapo ndio asili ya mzazi wake mmoja,  yeye mzazi wake  mmoja sio asili ya Tanzania,…lakini yote tusubirie hiyo kesho, Dalali anaweza kulifichua hilo ukimbana vyema…’akasema na alionekana anataka kukata simu, lakini mimi nikamuwahi kwa swali;

‘Kama nyie mumeshindwa na ndio kazi yenu mimi nitawezaje…?’ nikauliza

‘Sisi hatujashindwa…ila bado wakati wetu, tukitaka ataelezea kila kitu, kwa hiari yake au kwa nguvu ikibidi,…lakini kwanza tunampa muda,…tuone lengo lake ni nini…wewe uhakikishe umefika hiyo kesho kituoni…, na mjane atakuwepo pia…’akasema

‘Kwani na yeye ana umuhimu gani kuwepo, naona kama tutamsumbua tu, au….?’ Nikauliza

‘Anahitajika kwa matakwa ya Dalali, ni dalali mwenyewe kahitajia  anataka shemeji yake awepo pia,…’akasema.

‘Kwahiyo itakuwa ni siku ya hukumu au..’nikasema na mpelelezi akaguna na kusema

‘Mhhh..naona ni  siku kabla ya hukumu..’akasema na kukata simu.

NB: Je kulikoni, mara nyumba ndogo…ina nini hii…je dalali analifahamu hilo….ngoje tuone sehemu ijayo!

WAZO LA LEO:  Kuna tabia ya mtu akishafanikisha lengo lake, hata kama anajua ni la uwongo, lakini ili kuhalalisha pato lake hilo…au kile alichokifanya, iwe ni madaraka, mali…au jambo lolote, mtu huyo, atatafuta vipengele, viwe vya kisheria au hata maandiko ya vitavu vitakatifu…kuhalalisha dhuluma yake…anajipa matumaini…, ili tu ajiweke kwenye uhalali. Kiukweli tunajidanganya, dhuluma ni dhuluma tu, na tunachofanya ni kujidanganya wenyewe, lakini sio muumba wetu. Ipo siku tutaumbuka tu!

Ni mimi: emu-three

No comments :