Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, May 20, 2016

YOTE NI MAPENZI YA MUNGU-8


Dalali  alipopigiwa simu aliomba akaisikilizie hiyo simu nje, lakini mpelelezi akamuagiza aisikilizie humo  homo ndani au amwambie  huyo aliyempigia wataongea baadae ,  dalali  akaizima simu yake, na kitendo hiki kilimfanya mpelelezi ashuku, ahisi kuna jambo….na mpelelezi huyu akasimama na akawa kama anamuendea  huyo dalali….
Tuendelee na  kisa chetu…

                                                **********

Mpelelezi aliposimama , dalali akahisi huyo mpelelezi anataka kuja kwake, …alichofanya ni kuweika ile simu yake kwenya mfuko wake wa suruali, akawa anamuangalia mpelelezi anataka kufanya nini, akatabasamu, na kusema;

‘Huyu ni mmoja wa wateja wangu…nitaongea naye baadaye, naona tuendelee tu…’akasema

‘Tafadhali naomba hiyo simu yako….’akasema mpelelezi akimkazia macho

‘Unaomba simu yangu ! Aaah, mkuu, ya nini, na kwanini, …si unayo simu yako, huna salio au…?’ akauliza.

‘Ninaomba kikazi, sio swala la salio…ninataka kuhakiki  jambo linahusiana na kesi yangu, …’akasema

‘Afande hapana, humu kuna wateja wangu , na sio vizuri kuwatangaza kwa watu, si unajua masharti na mikataba, ….unielewe afande…’akasema akitikisa kichwa kukataa.

‘Nakuelewa sana, na mimi sina nia hiyo ya kuwatangaza hao wateja wako wau siri zako…, kuna kitu nahakiki mara moja halafu nitakurejeshea, usiwe na wasiwasi…’akaambiwa

‘Hapana afande, haiwezekani,…siruhusiwi, sio haki, hapana, siwezi….’akasema

‘Kwa mujibu wa mamlaka niliyopewa,  nina haki ya kuchunguza kila ninachoona kinahusikana na kesi  ninayoifuatilia…,ili tusipotezeani muda, nipe hiyo simu yako….’akaambiwa, na Dalali akaona sasa hali sio shwari,kwanza akajifanya anataka kuitoa, halafu akageuka kuniangalia mimi.

‘Uliuliza swali gani vile..’akasema akijipapasa mfukoni.

‘Nipe hiyo simu yako…’ilikuwa sauti nzito ya mpelelezi, sasa akiwa kabadilika.

‘Afande nitakupatia, usiwe na shaka,…unafikiri, mimi sina shaka ila sizani kama ni sahihi…’akasema Dalali, na sasa akawa anaitoa mfukoni,.

‘Mimi nafanya kazi yangu, …’akasema mpelelezi

‘Unajua afande sikuelewi, badala ya kufanya kazi yako kazi uliyoagizwa ya kumfikisha huyu tapeli kituoni, unaingilia mambo mengine, wewe unamsikiliza huyu tapeli, nilikuambia awali kuwa huyu ni mjanja, naona …keshakuhadaa  ..’akasema

‘Kama unajiamini kuwa huna makosa, nipe hiyo simu, kuna kitu naangalia, kama hakuna  kitu nitakurudishia, na unavyozidi kuchelewesha kunipatia hiyo simu ndivyo unavyonipa mashaka…..nipe hiyo  simu….’akaambiwa na sasa alikuwa keshaitoa na vidole vikawa vinahangaika kutka kuzima, lakini mpelelezi akaiwahi kuichukua mkononi  mwake.

‘Usiwe na shaka…’akasema mpelelezi,na ile simu sasa ilikuwa mkononi mwake, na mara ikaanza kuita tena…, na mpelelezi akaitupia jicho na kuona jina la huyo anayepiga simu, akaminya kitufe cha sauti ya spika ya nje kwa haraka, halafu akabonyeza sehemu ya kupokea na kunyosha mkono kumkabidhi Dalali.

‘Pokea hiyo simu yako…’akaambiwa,

‘Haina haja ,…’akasema na mara sauti kubwa ikaanza kusikika, huyo mpigaji akaanza kuongea kwa sauti kubwa na kwa hasira.

‘Wewe Dalali...kwanini hupokei simu yangu, unajua nipo wapi mimi…natafutwa na polisi, kwa ajili ya taama zako,sasa sikiliza…unisikilize kwa makini…usinihusishe na mambo yako tena, na ole wako unitaje, umenielewa,…nitakupigia tena baadaye…’akatulia

‘Umenisikia…?’ sauti ikauliza na mara simu ikakatika
Mpelelezi akamuangalia Dalali,..Dalali, kwanza alitulia tuli kama aliyemwagiwa maji, akajikuna kichwa, halafu akawa kama anataka kupiga simu, halafu akasita na kusema ;

‘Huyu mtu mpuuzi tu…naona labda kaharibu mambo yake, unajua hawa wataalamu wakati mwingine wanaweza kuchanganya wateja wake, sizani kama alikuwa anataka kuongea na mimi, ngoja nitaongea naye, …unajua mimi sijamuelewa,  …nitaongea naye…’akasema

‘Lakini kakutaka Dalali,ina maana alikuwa anauhakika anaongea na wewe…’akasema mpelelezi

‘Nitaongea naye, nitajua anataka nini...ila kuna kitu naona ni muhimu kwasasa, unajua ili mnielewe na ili mambo haya yawe kisheria,  mimi naona wakili wangu awepo, maana nyie watu siwaelewi, haya maswali yenu yaannitia mashaka….’akasema

‘Wakili wako wa nini…kwani unahisi  una kosa?’ akauliza mpelelezi

‘Maana maswali yenu yananipa mashaka, mnakuwa kama mnanishuku jambo, na mimi sina makosa, na mnaweza kunitega jambo nikaongea bila kujielewa….’akasema

‘Mimi ninahitajia kuhakiki kesi ya kaka yako ili nifunge jalada lake, hilo linakupa mashaka, mashaka gani?’ akaulizwa

‘Ni maswali ya huyu mtu tapeli, mimi nilitarajia ungemuhoji yeye, au uondoke naye, sasa naona unazidi kumchelewesha au kuna kitu….’akasema akiniangalia mimi

‘Sawa endelea naye malizana  na maswali yake, ili tuendee na mimi,…’akaambiwa.

Mara simu yake ikawa inaita tena,…akabakia kimia, na mpelelezi akasema

‘Pokea simu yako, sogea pale uipokee, ukumbuke nilikuja hapa kuja kukuhoji wewe, na sio kuhusu huyu mtu wa mitandao…., tatizo la huyu ni jambo jingine kabisa…’akasema na jamaa akaichukua simu kutaka kuipokea na sasa akasogea pembeni, akaanza kuongea kwa sauti ya chini, alishasahau kuwa mpelelezi alikuwa kabonyesha kitufe cha sauti kubwa.

‘Mtaalamu kakamatwa na polisi sasa hivi, na anavyoonekana keshakutaja kwahiyo sisi tunahitaji malipo yetu sasa hivi, maana naona dili yako umenuka…’sauti ikasema

‘Unasemaje, kakamatwa, poa nimekuelewa….nipo kwenye kikao nitakupigia…nini…unasema nini malipo, malipo gani, nitaupigia baadaye….’akakata simu, na kubakia amesimama, kawa kuduwaa kama anawaza jambo, na mpelelezi akamuendea, na  kunyosha mkono.

‘Hebu nipe hiyo simu yako…nitakaa nayo,….’akaambiwa

‘Itakusumbua bure, huoni watu wanapiga simu mara kwa mara, kwanza simu yangu ina nini afande …’akasema

 ‘Sikiliza mimi nipo kazini, na tendo lolote utakalolifanya kuanzia sasa litachukuliwa kama kitendo cha kunizua nisifanye kazi yangu. Sogea ukae pale ,umalizie maswali yako na ndugu hapo,…ukimalizana naye nitakuuliza maswali yanayohusiana na kifo cha kaka yako …’akaambiwa

‘Afande, kaka yangu alifariki kwa ajali hilo lipo wazi, lakini anyway, mimi siogopi maswali yako, hawa watu nia yao ni kuniharibia,  sijui wana mashaka gani na mimi na hili nitalimaliza tu, ….’akasema

Na mara simu yake ikaita tena,….mpelelezi akaangalia mpigaji, akaoa jina limeandikwa,….’mtaalamu’  akanyosha mkono kumkabidhi dalali huku akibonyeza kitufe cha kuweika hewani, na sauti ikasemai;

‘Haloooh, dalali…’sauti ikasema mpelelezi akamsogezea Dalali mdomoni, na kumuashiria aongee

‘Unataka kusema nini…tutaongea baadaye sasa nipo kwenye kikao, unasikia nipigie baadaye ….’akasema dalali na sauti ikasema

‘Ni hivi , nimeshakamatwa na polisi, sasa sikiliza….unasikia, niipate pesa yangu kama ulivyoniahidi, na kesho, sijui kama itawezekana kuhusu huo mnada ulioniambia, uhakikishe sehemu ya mshiko wangu naipata, vinginevyo,…. na mbona sauti ya simu yako ipo hivyo,nasikia sauti mbili mbili…unajifanya mjanja eeh, unanirekodi, mpuuzi mkubwa wewe….’akakata simu.

Mimi nilibakia kimia, nikiangalia hayo yanavyoendelea, nikageuka kumuangalia mama mjane,ambaye alikuwa akimuangalia shemeji yake anavyohangaika na simu naona sijui kama alikuwa akimuonea huruma shemeji yake au alikuwa naye akimuhisi vibaya, na alionekana kutaka kusema neno lakini sauti ilikuwa haitoki, akabakia kaduwaa tu.

‘Haya maswali yaendelee…’akasema mpelelezi

                                                                 ********

‘Dalali,  tuendee na maswali yetu,..’nikasema

‘Maswali gani ,mimi nimechoka na maswali yako ya kujirudia rudia,… naona wewe ni kama unanishuku jambo, na mamabo ya shakashaka kwangu sitaki, sasa mimi naona twende kisheria, nahitajia wakili wangu awepo…’akasema

‘Haya ni maswali ya kuhakiki, …uhalali wa hilo deni, hayajakushuku jambo, kwanini unaanza kujihami, nia yanu,  ni kutaka kuhakiki kama kweli hilo deni  llilikuwa deni la kaka yako au la….vinginevyo useme ukweli tu tumalizane…’nikasema

‘Nisema ukweli upi,….nimeshakuambia hilo deni ni la kaka kama huamini nenda huko benki ukawaulize….’akasema

‘Nilikuuliza  hilo deni la pili, ulilichuukua kwa  makubaliano gani,…tuangalie taratibu za benki zilivyo…wewe ulifika ukaonyesha barua kuwa wewe ni msimamizi….na wakaja kusema huwezi kuchukua pesa kwasababu kuna deni..si ndio hivyo  kutokana na kauli yako ya kwanza au sio…?’ nikamuuliza

‘Sasa kuna tatizo gani hapo…ndio unataka kusema nini ?’ akauliza

‘Kiutaratibu wewe bado ulikuwa hujawa signatory..ulitakiwa kwanza ujaze fomu ya kuwa signatory, na taratibu hizo zinachukua muda, sio kitu cha siku moja,…ilikuwaje wewe wakakubalai kwa siku moja tu..’nikasema na kumwangalia mpelelezi kama amenielewa hapo.

‘Na pili ni kwanini kwanza wakimbilie kukuambai kuwa hakuna pesa, kabla hawajakuambia kuwa mbona wewe sio mwenye akaunti umenilewa mashaka yangu hapo,  iweje siku ya kwanza tu uanze kuchukua pesa.. ukimbilie kuchukua pesa, na benki wakimbilie kukuambia kuwa hakuna pesa kuna deni, hebu tuambie hapo..?’ nikamuuliza na hapo akawa kama kashituka, akacheka kidogo na kusema;

‘Nimeshakuambia, tulikuwa na shida ya pesa, kwahiyo mimi nilipofika tu na kuwaonyesha zile nyaraka, kuwa mimi ndiye msimamizi wa malipo, nikawa nimeshajaza tayari karatasi ya kuomba kulipwa kiasi fulani cha pesa nilijua hili laweza kufanyika tu, huku wanaendelea na mambo yao  mengine…sijui  hayo mambo yako ya signatory… …’akatulia

‘Kwahiyo kwanza kabisa ulijaza fomu za kuchukua pesa…hata kabla hujakubaliwa kuwa wewe ni signatory….si ndio hivyo?’ Nikamuuliza

‘Ndio kuna ubaya gani hapo, usitake na wewe kunichanganya, nilijaza vitu vyote kurahisisha kazi…’akasema kwa hasira

‘Ulipojaza hiyo fomu ya kuchukua pesa ….uliweka sahihi yako au sio…?’ nikamuuliza

‘Hahaha…sasa ningeliweka saini ya nani, mimi ndiye nachukua pesa ningeweka saini ya nani, kwa vipi kwanza, hebu hebu fafanua swali lako unataka nini hapo….’akasema  sasa akitoa simu nyingine akitaka kumpigia mtu.

‘Wewe uliweka saini yako, na unajua kabisa kuwa kabla ya kuchukuliwa pesa mlipaji hulinganisha sahihi yao na ile ya kwenye karatasi ya maombi…ndio maana nakuuliza wewe uliweka sahihi  yako…?’ nikamuuliza

‘Ndio niliweka sahihi yangu yangu  na nikiwa na kila kitu tayari, na ukumbuke nilikuambia nilishaongea na meneja,…sasa hayo mengine ni juu yao kunifahamisha….’akasema

‘Benki walikuwa bado hawajakukubalia wewe kuwa ni signatory… huwezi kuchukua pesa..?’ nikamuuliza

‘Waliniambia siwezi kuchukua pesa kwasababu kuna deni, hiyo ni kauli yao ya awali….’akasema

Na wakati huo ulikuwa umeshajaza fomu, ukawaomba, na unasema wao wakasema hawawezi kukuruhusu  pesa kwa vile kuna deni …lakini hawakukuambia mbona sahihi yako na ile ya mwenye akaunti hazifanani,….na bado wakakukubalia kuchukua deni jingine,…na bado hujawa signatory… hebu elezea hapo tukuelewe.?’ Nikamuuliza

‘Sasa hapo kuna tatizo gani, ..wakati nina kumbukumbu za kuniidhinisha kuwa mimi ndiye nitakayesimamia kila kitu cha marehemu, na kwenye kumbukumbu hizi kuna sahihi yangu, hayo mengine ni juu yao, sio mimi…mimi sioni mantiki ya swali lako…kabisa kabisa wewe unataka kunitega tu hapo….’akasema kwa hasira.

‘Nakuuliza hayo maswali nikiwa na maana …tunachotaka ni kuona jinsi gani huyo mtu aliweza kuchukua pesa kwa jina la kaka yako….unielewe hapo, ili nijue hilo ni lazima nianze na wewe…kwani wewe kwanza ulikuwa mtu wa karibu kwa kaka yako….sasa…iweje...’akanikatiza kwa kusema

‘Sikiliza, hakuna mtu mwingine alichukau hizo pesa, hilo ondoa akilini mwako, hakuna…usitake kutunga kitu ambacho hakipo…kama hawa wapuuzi wengine wanafikiri watanifanya nibabaike, ….sina wasiwasi, maana sina kosa…’akatulia kidogo halafu akaendelea kusema.

‘Wapuuzi gani…?’ nikamuuliza

‘Wewe uliza maswali yako….mimi nashughulika na mambo mengi, na akili yangu inafanya kazi ..huwezi ukanichanganya…nina uzoefu wa kudili na watu zaidi ya kumi, sibabaiki…endelea ,,’akasema akijifanya anajiamini.

‘Shaka yangu ni jinsi ulivyoweza kukubaliwa kwa siku moja, wakati hujawa signatory…na ni kwa vipi wakimbilie kukuambia hakuna salio, ni kipi kilitangulia, unasema walianza kukuambia hakuna salio…lakini hawakusema mbona sahihi hazifanani…na mwenye akaunti…’nikasema

‘Sasa labda niseme ukweli, maana mambo mengine unataka wewe mwenyewe uelewe tu…tulikuwa tumekwana sana, mimi sina kitu muda huo,…unajua kazi zangu sio za moja kwa moja kupata pesa, kuna muda unakuwa kwenye hali mbaya kweli, …ni muda huo nilikwama kweli…kwahiyo mimi Ilibidi nipige magoti,…sasa ningefanyaje, shemeji anaumwa, na anaumwa kweli,sina pesa ningefanya nini,…’akawa kama ananiuliza

‘Kwahiyo kupiga magoti kwako kukawafanya watu wa benki wakiuke misingi yao…?’ nikamuuliza

‘Hapana sio hivyo…’akasema

‘Ni vipi….?’ nikauliza

‘Kupiga magoti ni kweli nilifanya hivyo, mbele ya meneja, kwanza nilianzia kwa muhasibu….acha wee….ukitaka cha mvunguni sharti uiname….Kwahiyo nilikwenda mpaka kwa meneja,…katika kuomba sana ndio wakanikubalia kuchukua deni…na siri moja nikuambie,  mimi nikitaka kitu nitakipata tu, kwa njia yoyote…,si unajua bongo hii, siwezi kusema yote, natumai umenielewa….’akasema kwa majigambo.

‘Yaonkena hivyo ukitaka kitu ni lazima ukipate,…..lakini mimi bado hapo nina mashaka…bebu nikuulize tena hizo famu za kuchukua pesa uliweka sahihi gani….?’ Nikamuuliza

‘Sahihi gani, kwa vipi, mbona unarudia rudia hilo swali,… si nimeshakuambia ni ya kwangu..sahihi ina nini sikuelewi.?’ Akauliza kwa hasira kidogo, halafu akawa kama kushituka kidogo.

‘Benki ili uchukue pesa sahihi ni kitu muhimu sana, sura yako na kaka yako mnafanana sana…lakini sahihi sizani kama zinaweza kufanana au sio…na benk wanalinganisha sahihi yako na ile iliyopo kwenye kumbu kumbu zao, wewe ulikuwa hujakubaliwa kuwa signatory iweje wakukubalie, iweje wasikuulize kwanza kuhusu maswala ya sahihi….?’ Nikamuuliza

‘Unajua maswali yako sikuelewi…kama meneja wa benki keshakubali, hawa wa chini wa naini, waliniruhusu, kwasababu kumbukumbu za hizo fomu zilikuwa mikononi mwake, keshaona sahihi yangu mle, yeye ni kutoa maagizo tu, kinafanyika, sasa tatizo lipo wapi hapo…’akasema

Ok,…kwenye huo mkopo,…si umesema ulikubaliwa sasa uchukua kama mkopo, na mkopo unahitajia mlolongo wake, huo mkopo uliuandikaje,  kama wewe au kama familia husika?’ nikamuuliza

‘Kama familia husika,mimi ningechukuaje kama mimi, ….ila kwa vile mimi sasa ndiye mwenye dhamana, ndiye nimepewa mamlaka ya usimamizi wa hii familia,  kila kitu kiliandikwa kwa jina langu, …’akasema

‘Kwenye hiyo fomu,…kwa ajili ya huo mkopo,  je, ulijaza kuwa wewe peke yako ndiye unawajibika na huo mkopo kwa vile wewe ni  signatory,au pamoja na mtu mwingine?’ nikamuuliza

‘Hapana,we-we-we…mhh,hilo ni deni bwana, ….niliweka na mtu mwingine, nilimweka na shemeji…’akasema na shemeji yake akainua kichwa kutuangalia lakini hakusema neno

‘Lakini shemeji alikuwa anaumwa au sio….?’ Nikamuuliza

‘Ilibiidi nimuweke tu, ukumbuke tangu mwanzoni yeye alikuwa kawekwa na mumewe kwenye hiyo akaunti yao, na mimi nilifuata hivyo hivyo… lakini katika maelezo ni kuwa yoyote kati yetu anaweza kuchukua pesa, ila …kuwe na barua ya makubaliano kama kuna tatizo, kwahiyo kilichogomba kwa muda ule ilikuwa ni sahihi ya shemeji…’akasema

‘Ndio maana nauliza je kwa muda huo shemeji  alikuwa anaumwa, angewezaje kuweka sahihi yake..?’ nikamuuliza, akasita kidogo, halafu akasema;

‘Kulikuwa na  muda shemeji hali yake ilikuwa inajirudi, anaweza….kujitambua, unajua alikuwa ..akili inafanya kazi,ila viungo, kwa sehemu kubwa ilikuwa haifanyi kazi,mwili ulikuwa hauwezi kujiinua, lakini muda mwingine alikuwa  akiongea kwa shida,…kwahiyo  hapo ndio aliweza kuweka sahihi yake,…, …’akasema

‘Hapo sijakuelewa, kuna muda alikuwa anaweza kujitambua, ina maana ulipochukua hizo fomu, ulisubiria mpaka huo muda ufike  au sio, ndio ukamwambia shemeji akusainie..si ndio hivyo au?’ nikamuuliza. Akahema kwa muda kama kuchoka na maswali yangu, kama nampotezea muda wake,  akasema;

‘Hivi  kwanza….hebu nikuulize na wewe ni kwanini unaniuliza maswali yote hayo, unataka kuhakikisha nini…kuwa  huniamini, ukumbuke mimi mdogo wake marehemu, …mimi ni mzazi wa hii familia nina uchungu zaidi ya huyu shemeji…’akatulia akinikodolea macho.

‘Kwani  una wasiwasi gani…ni maswali tu ya kuhakiki , inawezekana ulifanya makosa bila kujua ?’ nikamuuliza

‘Mimi nimechoka na maswali yako, ya kujirudia rudia, na yananilenga mimi kama mkosaji vile, badala ya kuulizia benki kama unakuja kuniuliza mimi, kwangu utakuwa unapoteza muda wako, mimi najua ni nini ninachokifanya, sio zezeta mimi, ….’akaangalia saa yake, halafu akamuangalia mpelelezi, akasema

‘Sasa  mimi nataka kuondoka, mukitaka zaidi utaniita huko jela,…au kituo cha polisi, unampeleka wapi huyu tapeli, maana hana jipya,…’akasema akimuangalia mpelelezi.

‘Kwani amemaliza kuuliza…?’ akauliza mpelelezi na kumfanya jamaa atoe jicho la kushangaa, halafu akageuka kuniangalia mimi, na mimi nikamuuliza

‘Mimi nazungumizia hili deni jipya, na wewe ndiye uliyechukua hizo pesa au sio, …sasa kwanini nikawaulize benki,….tuendelee , umesema ulipofika benki kuchukua pesa ndio ukagundua hilo deni, sawa si sawa..?’ nikamuuliza

‘Nimeshakujibu hilo swali, siwezi kukujibu tena..’akasema

‘Na akaunti iliyotumika ni ya mume na mke, ya kuwa mume hawezi kuchukua pesa mpaka mke aweke sahihi yake, sasa wewe ukapewa majukumu ya kuchukua pesa, ina maana mlifanya utaratibu na benk mkapeleka nakala za mirathi kuwa wewe ndiye utakuwa unachukua pesa, je katika makubaliano hayo na benki  …’nikatulia nilipomuona akishika shika simu yake,

‘Unajua wasi wasi wangu , ni jinsi gani shemeji yako alivyoweza kuweka sahihi yake na wakati yeye alikuwa mgonjwa, je sehemu hiyo ya mke ilikuwaje,….ulisubiriaje mpaka aweze kuweka sahihi na wewe ulisema ulikuwa unahitajia pesa kwa haraka,walitoaje pesa wakati  sahihi ya shemeji yako ilikuwa bado…?’ nikauliza

‘Nimekuwambia japokuwa alikuwa anaume kuna muda alikuwa na hali nzuri ya kuweza kuweka sahihi sasa mengine sijui , nenda kaangalia kama hakuweka sahihi yake,… na au muulize…’akasema na kumgeukia shemeji yake.

‘Na  je wewe ulimwambia  hiyo sahihi ni ya nini ?’ nikamuuliza

‘Kiukweli….unajua mambo mengine niliyaacha tu, sikutaka kumwambia shemeji, ….na pesa tunahitajia, kwahiyo,sikumwambia shemeji kuwa hizo fomu ni kwa ajili ya deni,  niliogopa kumshitua, nilimwambia ni ili tuweze kuchukua pesa ya matumizi…’akasema

‘Kwahiyo yeye hakuweza kuuona huo mkataba wa kuchukua mkopo, yeye hakuweza kusoma kilichoandikwa na wala hukumsomea, wewe ulimuonyesha tu sehemu ya kuweka sahihi,….?’ Nikamuuliza

‘Ndio nilifanya hivyo, kuogopa kumshtua…’akasema

‘Na kwenye huo mkopo mpya, nyumba pia  iliwekwa kama dhamana…?’ nikamuuliza na ilikuwa kama nimemzaba kibao usoni, akabadilika usoni, akasema.

‘Unajua unielewe….huomkopo ni muendelezo tu, kwahiyo mambo mengine yalikuwa yale yale..’akasema na simu yake ikaita tena, alikuwa nayo mpelelezi, mpelelezi akaiangalia na kufanya kama awali, na Dalali akaipokea na kuangalia mpigaji, akasema;

‘Huyu mtu ana nini na mimi, oh, sio yeye ni….’akasema akiwa anasita kupokea

‘Pokea…’akaambiwa na  kwanza akataka kuminya sehemu ya kuzuia sauti na mpelelezi akasema

‘Pokea kama ilivyo…’akaambiwa, na mpelelezi akasogea na kubonyeza sehemu ya kupokea.

‘Mpenzi, wangu, vipi,  mtaalamu kapiga simu, anasema atakachokufanya hutamsahau, unamfahamu huyo mtu alivyo, kwanini humalizani naye, unajua bila yeye usingafanikiwa, mpe pesa yake, au  na huo mnada ni keso au sio, …?’ akauliza mkewe

‘Achana naye, nitakupigia nina maswala mengine muhimu, unasikia nitakupigia….’akasema na sauti ikauliza tena

‘Huo mnada upo au haupo….?’ Akauliza

‘Nitakupigia,…..’akasema akitaka kukata simu

‘Ukitoka huko uje, kwani  kuna wapelelezi wamefika wamenihoji kuhusu nyumba na …..’dalali akakata simu simu akitamka neno

‘Wapelelezi…mhh’akasema na kuguna

‘Kwanini unakata simu, huoni kuwa angekupatia jibu ya swali unalojiuliza mwenyewe …?’ akauliza mpelelezi na jamaa akawa kaduwaa, naona sasa alihisi mambo yanamwendea kombo, akatikisa kichwa kama kuondoa kitu.

‘Swali, swali gani…huyo mwanamke anatupotezea muda , tuendelee naomba tufanye haraka naona nina mambo mengi ya kufanya….’akasema

‘Huyo ni nani, nyumba ndogo…?’ akauliza mpelelezi akitabasamu. Na jamaa aliposikia hivyo na yeye akajilazimisha kutabasamu na kusema;

‘Ndio maana nimekuambia hiyo ni simu yangu ina mambo yangu binafasi, halafu afande, wewe unataja nyumba ndogo wakati shemeji yangu yupo hapa anasikia,..’akasema kiutani huku akitabasamu akimwangalia shemeji yake , shemeji yake alikuwa kama hayupo, alionekana  kazama kwenye mawazo  huku sasa akiwa kaangalia nje.

‘Hiyo nyumba anayoishi huyo mpenzi wako, umemjengea wewe…?’ akauliza mpelelezi na jamaa akajibu kama anashtuka akasema;

‘Nani kasema hivyo…?’ akauliza akikunja uso kuonyesha halitaki hilo swali, akageuka kumwangalia shemeji yake na shemeji yake sasa alikuwa akimtizama kwa haraka akakwepa kumuangalia na akaweka mikono yake mbele kama anaomba akaipuliza na akageuka kumuangalia mpelelezi, lakini hakusema kitu na mpelelezi akasema;

‘Jibu swali….’akaambiwa na simu ikaita tena, akaangalia mpigaji ni nani, akaona jina

‘Mtaalamu…’ akataka kuminya sehemu ya kukata, lakini mpelelezi akamzuia na mpelelezi akaminya sehemu ya kupokea,…..sauti ikaanza kusema;

NB: Mambo yanazidi kujileta, je simu ya pili inasemaje


WAZO LA LEO: Hata tujifanye wajanja wa kuongea, wajanja wa kudanganya, wajanja wa kupata vitu visivyo halali, tusisahau kuwa waliodhulumua wanalalamika, na wengine wameshashitaki kwa hakimu wa mahakimu, ambaye anajua kila kitu, na kwahiyo  hata kama tumepata kipato hicho sumu, ambayo itakutafuna kidogo kidogo na muda ukifika, ni majuto. Ewe mja tubu dhambi zako, acha hiyo tabia, dhuluma ni mbaya sana.
Ni mimi: emu-three

No comments :