Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, May 16, 2016

YOTE NI MAPENZI YA MUNGU-7



Mara mpelelezi akaingia… cha ajabu sasa alipoingia alikuwa kashikilia pingu mkononi, ….akawa  anatembea mwendo wa hatua za kuhesabu, akinijia mimi, pale nilipokuwa nimekaa, akilini nikawa najiuliza kuna nini, nikakumbuka yale maneno ya jamaa wakati akiongea na shemeji yake alisema;…

 ‘Nilijua tu…hawa ni matapeli, sasa ngoja waionje joto ya jiwe….shemu usiwe na wasiwasi, hawa sasa hivi wanakamatwa, wewe utaona tu…

Yule mpelelezi akawa sasa kanifikia pale nilipokuwa …., na akawa ananiangalia kwa jicho la kujiuliza, yaonyesha , kwa jinsi nilivyomuona alikuwa akishindana na dhamira, inawezekana kitendo hicho anachotaka kukifanya kilikuwa hakimpendezi au hana uhakika nacho, au…, lakini hana budi,… akawa sasa keshanifikia lakini alikuwa hajatamka neno,nikajua sasa  kuna tatizo…

Tuendelee na kisa chetu
                                                   ************

‘Vipi afande mbona unanijia na pingu mkononi…?’ ikabidi nimuulize mimi kwanza kwani niliona kusubiria kunanitesa zaidi.

‘Nilijua tu…’sauti ikatoka kwa jamaa  yetu dalali, akiwa na tabasamu tele mdomoni. Mpelelezi likuwa keshanifikia akawa kasimama akiniangalia; Yule mama mjane akawa naye kainua kichwa anamuangalia huyo mpelelezi kwa macho ya mshangao!

‘Kwanza nikuulize hii kazi unayoifanya una kibali nayo…?’ akaniuliza yule mpelelezi.

‘Afande si unajua kazi yangu, kazi kama hizi ni za kujitolea tu, …mara nyingine hazihitaji kibali, mimi nikiona jambo linaigusa jamii, huwa nalifanyia kazi na nikipata ushahidi wa kutosha naukabidhi kwa polisi,  na mara nyingi imekuwa hivyo, na nia yetu ni kuhakikisha  tunasaidia jamii , na haki itendeka…na sisi tumegundua kuwa hapa kuna tatizo, kuna dhuluma  inataka kutendeka, ….’nikasema

‘Dhuluma gani wewe, hakuna dhuluma yoyote hapa, …muongo huyo afande…ni tapeli huyu.’akadakia jamaa akinionyeshea mkono.

‘Kwanza afande nikuulize kuna nini cha ajabu…?’ nikamuuliza

‘Kwa amri ya wakubwa zangu, wewe umeingilia amri halali ya mahakama, na umejaribu kuvuruga ukweli, na kuleta mtaharuki ….umejenga fitina kwenye jamii, na nimeamuriwa ni nikukamate, na mengine utaambiwa huko kituoni,…kazi yangu ni hiyo kwasasa,…kuna watu wanahusika na hilo,… kwahiyo upo chini ya ulinzi…’akasema akiwa kashikilia pingu yake.

‘Nimeingiliaje amri ya mahakama!….hebu lifikirie hilo, mimi nimefanya kosa gani kwa hivi sasa la kuingilia amri ya mahakama?,..Sisi tumeliona hili jambo lina utata, na tunahisi kuna tatizo, ndio tukawa tunautafuta ushahidi, tena kwa njia halali, ya kuulizana maswali….hatujatumia nguvu yoyote kuzuia amri ya mahakama, na kuja kwangu hapa sikuwa nimepanga,sikuwa nimelifahamu hili, imetokea tu…..je kuwasaidia wajane na mayatima ili wapate haki zao ni kosa?’ nikauliza

‘Afande huyo mwongo, tangia afike hapa imekuwa ni balaa….mtoto anateseka kwa ajili yake, …maana hilo tulishaliweka sawa, ikawa haitokei tena, mtoto akawa hana tatizo tena,  sasa huyu  kaja, kaanzisha balaa,mtoto anaumwa, muulize mama yake….’akasema akimuonyeshea shemeji yake.

‘Muulize, … kisa eti anatafuta ukweli, ukweli gani ambao nyiewatu wa usalama mumeshindwa kuupata, anainglia kazi zenu, …huoni huyu ni tapeli, mwongo…ana lake jambo…’akasema jamaa na mpelelezi akawa hamuangalii yeye, alikuwa akiniangalia mimi tu,na kwa upande nilimuona Yule mama mjane akiwa kaduwaa, japokuwa alikuwa na machozi machoni.

‘Ilivyo ni kuwa umekiuka amri halali  ya mahakama, kwasababu ilishahukumu kuwa nyumba hii ipo kwenye taratibu za mnada baada ya mahakama kurizika na ushahidi,  kuwa kweli hilo deni lipo, na mwenye deni aliweka nyumba hii kama dhamana,…na wenyewe wamekubaliana na hilo,..na huenda ulishaambiwa yote, sihitaji kukufanulia, …na hukumu ikapitishwa kuwa nyumba hii ipigwe mnada kwani mkopaji hana uwezo tena wa kulipa hilo deni…’akasema

‘Hebu nikuulize afande, huyo mkopaji ni nani na ni nani alikubaliana na hilo kuwa nyumba ipigwe mnada?’ nikauliza

‘Kutokana na mahakama ni mwenye nyumba hii…’akasema

‘Ni nani…na huyo aliyekubaliana kuwa mnada uwepo ni nani?’ nikauliza

‘Hilo swali sio muhimu kwangu kujibu…ila kwa maelekezo niliyopewa ni  mwenye nyumba hii…’akasema

‘Ambaye ni marehemu au sio…sasa yeye alikubalije kuwa mnada upigwe wakati ni marehemu?’nikasema kwa kuuliza

‘Awe ni marehemu, haijalishi, kwani wapo watu wanaoendelea kumiliki hizi mali, sio kwamba mtu akifa basi kila kitu chake kimekufa, madeni ni lazima yalipwe, hata kidini wanasema hivyo kama kuna mtu anamdai marehemu ajitokeze, si ndio hivyo ?..........

‘Na jingine marehemu aliweka dhamana, na ujuavyo dhamana inawekwa kwa mali zisizohamishika…unanielewa hilo…na taratibu zote za kisheria zimefuatwa , sio kwamba ni maamuzi tu..na kosa lako ni kuwa, wewe umeanza kuzikiuka, kutaka kuzuia…ni kosa au sio…’akasema

‘Sawa kabisa afande, nakubaliana nawe,maana …kutokana na deni hilo kaka anatusumbua…mzimu wa kaka unatujia…., anatutokea kwa kupitia kwa mtoto…na kama ulivyosema hata dini anasema deni ni lazima lilipwe sasa huyu tapeli anajifanya anajua zaidi, ana lengo lake…..hebu muulize lengo lake ni nini….ili upewe nini, na wakuruhusu apate kitu ni mimi, sasa nakuambia hapati kitu hapa….’akasema huyo jamaa na mimi sikumjali nikaendelea kuongea na huyo mpelelezi

‘Afande nikuambie kitu,…tuna ushahidi kuwa deni hilo sio la marehemu, na  kama marehemu angelikuwepo hai, …hili deni lisingelikuwa lake huenda angelibambikiwa mtu mwingine hilo tutalithibitisha, na ndicho nilitaka kukithibitisha hapa kwa kumuhoji huyu mwenye mamlaka sasa hivi….’nikasema nikimuangalia huyo jamaa halafu nikamgeukia mpelelezi na kuendelea kusema;

‘Hili deni lilikuwepo bila marehemu kufahamu na ilitakiwa lijitokeze baada ya kifo cha huyo marehemu, aliyekuwa mume wa huyu mama, huyu mama ana uhakika kabisa hilo deni sio la mumewe, kwani anamfahamu vyema,…, na sijui… huenda hata hicho kifo kimepangwa,  lakini hilo tutakuja kulijua baadaye …’nikasema na jamaa akacheka kweli.

‘Hahahaha…..Unaona huyu mtu alivyomshirikina…ina maana kuna mtu alijua kaka atakufa liini, …hivi kweli kuna mtu anaweza kujua mwenzake atakufa lini, ….tena akiwa mnzima hana ugonjwa….?

‘Hahaha…hapo sasa unadhihiri uwongo wako, wewe kweli umeshindwa hoja, utapeli wako hauna hata maana,…nilijua wewe ni mjanja, kumbe ovyooo, haaaa, eti  kifo kilipangwa, na nani, nani ana mamlaka na mungu hahaha, unalo hilo…’akasema

‘Afande tulichogundua sisi kwa muda mfupi tu, hilo deni limewekwa kwa marehemu kinamna, …hilo deni sio  la marehemu,…nina ushahidi….unataka nikuonyeshe….’nikasema na jamaa alishtuka kidogo halafu akacheka tena kicheko cha dharau, na kusema;

‘Ni deni la nani, hizo hati aliweka nani sahihi , unasema eti una ushahidi, hana lolote huyo, asikudanganye,…mwongohuyu…unajua wewe unaongea tu bila kufikiria, ….ujue hilo deni lipo benki, ni nani anaweza kuwadanganya benki…eti afande, hebu muulize huyu mtu, …. anafahamu taratibu za benki zilivyo, hivi kweli hilo linawezekana….huyu ni tapeli, mpeleke kunakohusika….’akasema.

‘Kwanini unaogopa nisiuonyeshe huo ushahidi…?’ nikauliza

‘Nionyeshe…kama utanionyesha mimi nipo tayari kufungwa…’akasema kwa kujiamini

‘Nikuonyeshe ushaidi sio, ushahidi wa kwanza….’nikaanza kusema na mpelelezi akanikatiza na kusema;

‘Sasa hivi hayo mimi siyajui, na hili la kukukamata wewe sio kesi yangu…unajua tuna taratibu zetu, na moja ya taratibu zetu ni kutii amri ya mkubwa wangu, na hili ni lazima lifanyike hayo mengine utayaongelea huko mbele yao kwa muhusika, ….natumai unanielewa….’akasema mpelelezi sasa akinikabili.

‘Nakuelewa sana….lakini kwanza nina ombi kwako, mimi sikatai kwenda huko polisi tutakwenda tu, lakini kwanza nina ombi….maana hilo linagusa keso unayoishughulikia wewe…’nikasema

‘Afande usimsikilize huyo ni tapeli, anataka kutumia ujanja wa kukulaghai, deni hilo lipo kweli….na  ni kutokana na nyaraka zilizopo benki,…hebu fikiria mimi ni ndugu yake, nimelikubali…yeye huyu mtu baki  ana uchungu gani zaidi yangu mimi,..huyu , yeye anajifanya anajua sana, na nia yake ni kuleta fitina na matatizo kwenye hii familia yetu,…kamwe usimsikilize..’akasema jamaa na yulempelelezi hakumuangalia, alikuwa akiniangalia mimi,akasema;

‘Una ombi gani….na ushahidi gani ulio nao amabo unaigusa kesi yangu ninayoifuatilia?’ Akauliza

‘Nataka kwanza uniruhusu nimuhoji huyu mtu, kuna maswali nilitaka kumuuliza kuhusu uhalali wa hilo deni, na yeye anaweza kunisaidia kwa hilo,na hilo deni ndicho kisa cha hiyo kesi yako utakuja kugundua mbeleni., maswali yangu ni kutaka kujua ukweli,..akinijibu hayo maswali, basi tutaondoka,…’nikasema

‘Ni ushahidi gani ulio nao ….’akauliza mpelelezi

‘Mwongo huyo , hana lolote….’akasema jamaa

‘Nionyeshe au niambie huo ushahidi…’akasema mpelelezi

‘Ushahidi wa kwanza ni yeye mwenyewe….’nikasema na mpelelezi kwanza akatulia akiwaza jambo halafu akauliza

‘Kwa vipi….?’ Akauliza huku jamaa anacheka kweli .

‘Haiwezekani mtu awe na uchungu na familia, awe na uchungu na kaka yake, atokee mtu mwingine kutaka kusaidia kuupata ukweli, halafu yeye awe mstari wa mbele kumpinga huyo mtu, huo ni ushahidi namba moja, tumie hekima utaugundua…..’nikasema na huyo mpelelezi akaangalia saa yake, halafu akageuka kumuangalia jamaa na jamaa alikuwa bado anacheka kwa dharau, na alipoona mpelelezi anamtizama akatulia

‘Sawa….muulize hayo maswali…’akasema mpelelezi

‘Afande…huyu anasema nini,…eti mimi japokuwa ni ndugu lakini sionyeshi uchungu…hata kama angekuwa ni mtoto wangu wa kuzaa kakiuka sheria siwezi kuipuuza sheria, mimi tabia yangu ni kufuata sheria, na jingine ni muito wa marehemu anataka deni lilipwe,…’akatulia

‘Afande…sasa kwanza amri ya mahakama, nitawezaje kuipinga, pili muito wa kaka,….yote hayo yana uzito, ndio maana nikawa mstari wa mbele kuhakikisha deni hilolinalipwa sasa kwa njia gani,…mimi sina pesa, shemeji hana pesa, ulitaka tukaibe….huo ushahidi wako hauna mshiko….hahahaha.’jamaa akasema .

‘Kama ni hivyo kwanini unaogopa kuulizwa maswali,  ….?’ Akauliza mpelelezi

‘Sijaogopa kuulizwa maswali…unasikia afande, … lakini kwa utaratibu gani, na kwa nani….huyu tapeli ndiye aniulize maswali,….mtu anayekiuka sheria za mahakama… akama anataka kuniuliza aulize kwa utaratibu unaotakiwa mimi nitamjibu kila kitu, sina cha kuficha, sina cha kuogopa….’akasema

‘Kwahiyo upo tayari kuulizwa hayo maswali na yeye…?’ Akauliza afande,

‘Mimi nimesema hivi, kama ni kwa utaratibu unaokubalika, mimi  siogopi hayo maswali yake..nimeshajua ni nini anakilenga, mimi ni mjanja, naona mbali, najua ana duku duku gani siwezi kumlaumu, lakini wenzake walikuwa hivyo hivyo, nikawaridhisha, benki wana kila kielelezo,sasa tatizo lipo wapi…., ila huyu mtu anaonekana ni mjanja sana, ni tapeli aliyekubuhu…’akasema.

Yule mpelelezi akaenda kukaa kwenye sofa, na kusema ;

‘Haya kama huna kikwazo, na upo tayari kuulizwa hayo maswali, ngoja tuyasikie, anza kumuuliza…’akasema mpelelezi, na jamaa kwanza alionyesha uso wa kushangaa, na baadaye akajirekebisha. Huyu jamaa anajua kweli kujiigiza…anabadilika kama kinyonga!

‘Afande…!’ akasema kwa kushangaa, na mpelelezi akawa kimia.

 Sasa akaniangalia akiwa na tabasamu la dharau mdomoni….akakunja nne, na mguu mmoja ukawa unatikisa tikisa akinisubiria nimuulize maswali. Mimi nikagueza uso kumuangalia shemeji, nilimuona bado analia, akilini nilijiuliza ni kitu gani aliongea  huyu  jamaa kwa shemeji yake ambacho bado kina mliza mpaka sasa…huo unaweza ukawa ushahidi mwingine.

Niligeuka kumuangalia jamaa yetu, alikuwa akiendelea kuutikisa mguu wake akijifanya kama vile hana wasiwasi,…lakini kiukweli hakuweza kunidanganya mimi.  Hapo alipo ana wasiwasi kibao ….

Mara simu yake ikaanza kuita, na kwa haraka bila kutazama mpigaji akaipokea, yaonyesha kuna kitu alikuwa akikisubiria kwa hamu, …akasikiliza, niliona uso wake ukibadilika, akamtizama mpelelezi kabla hajasema neno, halafu akasema;

‘Una uhakika,…ndio nakuuliza una uhakika hayupo kwake, kaenda wapi, ….?’ Akauliza na akawa anasikiliza halafu akasema;

‘Ndio….nimemtumia ujumbe wa maneno hajibu, nikampigia simu yake, hipatikani,…..kuna nini kwani..?’ akasikilza  baadaye akakata simu,kwa hasira …usoni akawa kakunja ndita, makunjazi,kuashiria kukasirika... akageuka kuniangalia mimi , akajaribu kukunjua hizo ndita,  akasema;

‘Uliza maswali yako haraka nataka kuwahi sehemu, na wewe ukapambane na nguvu ya dola…hahaha, unafikiri utapeli una tija, sasa utajua kuwa mimi ni nani, afande anakusubiria, uliza haraka, au ni mbinu za kujichelewesha, mhhh...’akasema, akitabasamu sasa kwa  dharau, na mimi nikasema;

‘Haya,…Tuanzie pale tulipoachia,….’nikasema na kabla hajasema neno nikasema;
‘Kawaida za mwizi ni arobaini..na mungu ana namna yake ya kumnasa mnafiki..hata ufanyeje, itafika muda ukweli utajulikana…na haki ipo juu, …ngoja tuone’nikasema na yeye akijifanya kutabsamu bila wasiwasi, akatikisa kichwa kama wafanyavyo wahindi kukubali ,….. akasema;

‘Wewe uliza hayo maswali yako ndugu…na sijui utaanzia wapi, wewe  mwenywe unajua wapi pa kuanzia, mimi sikumbuki uliachia wapi…’akasemaakizungusha shingo kama kunyosha.

‘Mimi nataka tuende sawa, sio kwa ugomvi, na kwa kuelimishana …tulishaanza kuulizana awali, au sio…sasa tuanze mwanzo au tuendeleze pale pale, unaonaje afande…?’ nikamuuliza mpelelezi.

‘Nyie endeleeni tu….’akasema

‘Afande huyu anataka kukupotezea muda wako,  kwa uwongo wake wa kitapeli, kwanini haanzi kuuliza maswali yake,  mimi nitakujibu na mwisho wa siku utaumbuka wewe mwenyewe…., mimi sio mnafiki, mnafiki ni wewe unayeingilia maswala yasiyokuhusu….’akasema akajifanya kutabasamu, lakini nahisi kuna kitu kaambiwa huko kwa watu wake na kimemgusa.

‘Hebu nikuulize tena, …kuhakikisha tu, je wewe ulijua lini kuwa kaka yako anadaiwa benki?’ nikamuuliza

‘Nilijua kipindi kidogo, nilishakuambia hilo, unakumbuka kuwa  nilikuambia kuwa, nilijua hilo deni pale nilipokwenda kuchukua pesa benki, unakumbuka…?.... au unauliza kwa faida ya afande, haya hilo ndio jibu lake,au hutasheka na jibu hilo, …?’ akauliza akiigiza kama muungwana fulani.

‘Nikumbushe vyema, kwa kutoa ufafanuzi…’nikasema

‘Ok,… ni hivi, nilikuambia kuwa  mimi ndiye niliyachaguliwa na wanafamilia wote kuwa niwe msimamizi wa hii familia ya kaka,…ni taratibu za mirati hizo zipo waazi, pande mbili zinakutana sawa unahitaji nielezee inavyo kuwa au… ?’ akauliza na mimi nikabakia kimia yeye akaendelea kusema.


‘Kama unaelewa ndio hivyo, mimi nikachaguliwa kuwa ndiye msimamizi….na kwahiyo kila jukumu, ikiwemo matumizi,…nakadhalika yalikuwa mikononi mwangu, na ukumbuke shemeji alikuwa hajiwezi, mgonjwa, yupo kitandani hata kugeuka hawezi. Kwahiyo mimi ndiye niliyekuwa msimamizi wa kila kitu, huku nikimsaidia, japokuwa awali kulikuwepo na watu wanamsaidia kibinadamu lakini sio kimatumizi, unajua…yupo hapo muulizeni..’akatulia akimuonyeshea shemeji yake.

‘Na ujue kuwa  matumizi yanahitajia pesa, kwahiyo kile tulichokuwa nacho kilifikia mahali kikaisha,….sasa tufanyeje, ndio  ikabidi niende benki kuchukua pesa , huko kulikuwa na akiba ya kaka, eeh,… sikujua ni kiasi gani, na kama shemeji angelikuwa anaweza angeniambia labda kuna salio kiaisi gani….’akatulia akimgeukia shemeji yake.
‘Kwa maana kuwa kwa muda huo, hata kuongea ilikuwa shida,….angelisema kuna kiasi gani, lakini mimi nikajua tu,  huko benki kuna kitu,….hizi kadi za siku hizi , huwezi kujua mpaka uende benki au sio..au kwenye mashine zao..na nisingeliweza kwenda kwenye mashine, lazima nifuate taratibu za kujitambulisha kuwa mimi sasa ndiye msimamizi wa mirathi…’akatulia kidogo

‘Sasa siku hiyo…nikadamkia benki…nafika nikajaza fomu zao, nikiimbatisha na barua kuwa mimi sasa ndiye msimamizi…’akatulia

‘Na mara nikaambiwa subiri…baadaye ndio nikaambiwa kuwa siwezi kuchukua pesa kwasababu kuna deni….’akatulia.

‘Alikuambia nani…?’ nikamuuliza na yeye akacheka kwa dharau kama vile nimemuuliza swali lisilo na maana

‘Na mtu wa benki, …ok, nani kwa jina sio ndio unataka hivyo, unataka …..eeh labda uwasiliane naye kuhakikisha, …kiukweli mimi siwezi kumkumbuka jina….na ukumbuke kuwa ni siku nyingi, huenda hata sura nimeshamsahau…’akajibu  akibenua mdomo wa dharau

‘Ulipoambiwa hivvyo ulichukua hatua gani?’ nikamuuliza

‘Kama umeshapewa jukumu la kulea familia, utafanya nini hapo…unahitaji pesa, nisingelirudi nyumbani  na kusema hakuna pesa, au sio…?’ akaniuliza na mimi nikabakia kimia, alipoona simjibu akaendelea kutoa maelezo.

‘Mimi sasa kama mkuu wa familia ikabidi akili ya ziada ifanye kazi…ukumbuke na mimi nina familia yangu nayo inahitajia kula na kila kitu, huu ni mzigo mwingine wa ziada…, lakini sikujali kwa vile hawa pia ni watoto wangu, watoto wa kaka ni wangu pia, au sio…kiujumla, ilibidi nianze kutafuta njia, ili watu hawa waweze kuishi, mgonjwa aweze kuendelea na matibabu…’akasema akimuonyeshea shemeji yake kwa mkono.

‘Je ulipopata taarifa hizo uliwahi kumwambia shemeji yako…maana licha ya kuwa hajiwezi lakini najua kuna mambo ulikuwa unafika umamwambia au sio, je kuhusu hilo deni uliwahi kumwambia shemeji yako?’ nikamuuliza

‘Hapana mimi sio mjinga kiasi hicho ….sikumwambia shemeji….nilikwepa kabisa kumwambia hilo…maana lingemchanganya akili, mtu keshachanganyikiwa unamzidishia dozi, ulitaka nimuue shemeji yangu..hapana mimi sikumwambia kabisa…’akatulia

‘Hukuamwambia mpaka lini…?’ nikamuuliza

‘Ilifikia hatua niliona nisimuambie nipambane mwenyewe…lakini maswala hayo hayana siri, wakaja kutuma barua ya kukumbushia ndio shemeji akaja kujua, ….lakini mimi bado nilikuwa na mashaka, , ndio maana hadi inafikia hatua mbaya, nilikuwa bado nasita kumwambia ...’akatulia.

‘Kwahiyo wewe ulikwenda benki  kwa vile ulichaguliwa kuwa  msimamizi ,hebu tufafanulie ulivyofanya pale benki, kiutaratibu wa mirathi,…ulipofika pale ulifanya nini?’ nikamuuliza

‘Wewe mwenyewe unazijua taratibu za benki,….kuna haja ya kulijibu hilo swali?’ akaniuliza

‘Ipo haja, na muhimu sana kwangu….’nikasema

‘Haya ndugu, nilifika pale nikajaza fomu za kuchukkulia pesa, ile fomu nikaambatisha na ile barua ya kuwa mimi ndiye msimamizi wa mirathi….ok, sasa wataka nikuambia kila kitu nilichokifanya, hata kama nilenda chooni, au sio…, nilimkuta nani, nikakaa foleni..ikafika zamu yangu…hivyo au…?’akaniuliza.

‘Ina maana ilivyo wewe ulipewa barua na kikao cha wanafamilia, upeleke benki, au sio…kwenye hiyo barua ukatambulishwa wewe na picha yako,..na sahihi  yako au sio…,na benki wana taratibu zao, huwezi kuchukua pesa mpaka uwe umeidhinishwa kama signatory, unanielewa nikitumia hilo,…?’ nikamuuliza

‘Nakuelewa bwana, mimi nimeenda shule, endelea…’akasema

‘Kwahiyo  ili hilo lipite kulikuwa na taratibu zao, si ndio hivyo…?’ nikamuuliza

‘Ndio hivyo,….hahaha, kumbe unajua, sasa kwanini unaniuliza, ndio hivyo…ni mambo ya kawaida hayana kuremba…benki hawana jinsi unafuata wanavyotaka wao, na sio wanavyotaka wao ni utaratibu dunia nzima au sio...’akasema kama ananiuliza.

‘Labda swali la kujikumbusha, nyie mpo ndugu wengi, na kuna wakubwa zaidi yako au sio, ni kwanini walikuchagua wewe uwe ndiye msimamizi wa familia?’ nikamuuliza akatabasamu kidogo, lakini akilini alihisi kuna mtego, akawa makini kulijibu, akasema;

‘Nimeshakuambia  kwenye kikao hicho walikuwepo ndugu wa pande zote, hakukuwa na swala la kampeni hapo, ni wao wanavyokuona,…upande wa shemeji …walimtegemea ndugu yao, lakini alikuwa hajiwezi kwahiyo kwa kiasi kikubwa walitegemea upande wetu…sasa kwa upande wetu..’akatulia akikohoa kidogo.

‘Kwa upande wetu…, nahisi ni kwa vile mimi nilikuwa karibu sana na marehemu,labda ndio sababu kubwa ya msingi ya kunichagua mimi…na labda ni kwa vile mimi najulikana sana kutokana na shughuli zangu za hapa na pale,kwahiyo kukihitajika kitu  haitakuwa vigumu kwangu kukifuatilia, na wananifahamu kuwa mimi nakutana na watu wengi, na nakumbuka wateja wangu, hasa wale ninaoingia nao mkataba, siwezi kuwasahau, …ndio wakanipendekeza mimi, nikapita ’akasema.

‘Hebu sasa turudi huko benki, wewe ukafika pale wakakuambia kuwa kuna deni …ilikuwaje kwanza?’ nikamuuliza

‘Ilikuwaje kwa vipi… ni pale nilipotaka kuchukua pesa, … ndio nikaambiwa kuna deni kubwa, nikashituka kuna deni, wakasema ndio tena deni kubwa na kutokana na mkataba, hilo deni lilitakiwa kulipwa kila baada ya muda fulani,  lakini halikuwahi kulipwa,…’akatulia kidogo.

‘Ndugu yangu kiukweli mimi mwenyewe nilishangaa, kaka achukue mkopo mkubwa hivyo bila ya mimi kujua, na, sijui alichukua kwa minajili gani, sijui, na nisingeliweza kwenda kumuuliza shemeji kama anafahamu hilo, unajua sio… ‘akatulia kidogo akitaka nisema neno lakini mimi nikabakia kimia ndio akaendelea kusema;

‘Pale pale nikawaambia watu wa benki ,… mimi sijui kuhusu hilo deni,…nikaja juu kweli, …namfahamu kaka yangu vyema , asingelikopa bila kuniambia, mimi,…yawezekana alimwambia mkewe..lakini kwa ufahamu wangu kitu kama hicho angeniambia, tulikuwa karibu sana na yeye, ….nimjuavyo kaka asingelinificha, ….lakini kila kitu kilionyesha, utasema nini...’akatulia

‘Kila kitu kwa vipi…?’ nikamuuliza

‘Nilitakaa kuthibitisha hilo deni kama kweli ni la kwake…nikaambiwa nisubiri, baadaye nikaambiwa niingie nikaonane na mhasibu,…..nikaingia na huko nikaonyeshwa vielelezo vyote,….ujue mimi kutokana na kazi zangu nimezoea sana kukumbana na makaratasi,…na macho yangu huwa mapesi sana …niliyapitia yale makaratasi kwa macho kwa haraka nikaona  kila kitu kipo sahihi….kwahiyo hata alipoanza kunionyesha kwa hatua, nilisharizika..lakini hata hivyo, nilikubali tu…’akatulia

‘Baadaye nikaomba huo mkataba….maana pale mtu wa benk alikuwa akinionyesha nyaraka nyingine, mimi kitu muhimu kilikuwa ni mkataba, ndio…akanionyesha huo mkataba,…deni hilo lilitakiwa kulipwa kila mwezi,…kuna kiasi kilitajwa, na chini ndio kuna hilo rungu, usipolipa ni nini kifanyike na ndio huyo mhasibu akasema mimi kama msimamizi natakiwa kulisimamia hilo ili lilipwe kwa wakati na ni muda mrefu hakuna malipo yaliyofanyika…’akatulia.

‘Hebu hapo….kwahiyo walikuambia hivyo, siku ile ile ulipowenda kuchukua pesa au sio….huku nyuma hukuwahi kuchukua pesa, au?’ nikamuuliza.

‘Ndio ni siku ile ile ya kwanza ….’akatulia kama anawaza jambo.
‘Ni siku ile.., nilipotaka kuchukua pesa, ndio yote hayo yakajulikana,  wakasema siwezi kuchukua pesa, kwani kuna deni, na deni hilo ni kubwa,…’akasema

‘Ikawaje sasa….?’ Nikamuuliza

‘Ndio hapo nikawaomba waniruhusu nichukue kiasi kwa ajili ya kusaidia familia,wakakataa, ..nikaomba na kuomba, nikaona hawa hawanifahamu, nikawaambia nataka nionane na meneja wao wa benki….’akatulia

‘Mnafahamiana  na huyo meneja, au…?’ nikamuuliza akasema

‘Sio swala la kufahamiana , hata angelikuwa nani mimi ningemuingilia tu,…ili familia iweze kwenda choo…’akasema

‘Sawa ikawaje?’ nikamuuliza

‘Mimi kutokana na kazi zangu, najua nifanye kipi…hawakunifahamu, nikaenda kuonana na meneja, nikamuelewesha, …unajua tena, ukiwa muongeaji, kuna raha zake, meneja akakubali kuwa sasa nichukue pesa lakini iwe bado ni deni, kwani pesa yote iliyokuwa  nayo kaka kwenye dhamana yake,….kwenye akiba yake,  imelipia sehemu ya hilo denii, kwahiyo ndio maana ukiangalia kwenye statement utaona deni liliongezeka…’akasema

‘Ngoja kwanza hapo…umesema uliambiwa hivyo siku ya kwanza, si ndio hapo kuwa huwezi kuchukua pesa kwa vile kuna deni..?’ nikamuuliza

‘Ndio…kwani kuna tatizo gani hapo…?’akasema na kuniangalia kwa mashaka.

‘Na tangia marehemu afariki, hukuwahi kuchukua pesa..?’ nikamuuliza hapo akasita na akawa kama anawaza

‘Jibu swali….hilo halihitajiki kufikiria je tangia  kaka yako afariki hukuwahi kuchukua pesa kablaya kuja kuambiwa kuna deni…?’ nikamuuliza
‘Sikumbuki…’akasema

‘Hukumbuki, ….lakini wewe uliagiza statements, ambayo inaoinyesha kila kitu…na wewe ndiye peke yako ulikuwa na mamlaka ya kuchukua pesa ndio au sio…?’ nikamuuliza

‘Yawezekana, lakini ….’akageuka kumuangalia shemeji yake.

‘Shemeji yako alikuwa mgonjwa, asingeliweza kuchukua pesa,…ndio maana nimekuuliza hilo deni uliambiwa siku ipi, ….umesema siku ya kwanza tu ulipopewa hilo jukumu..haya turudi kwenye statement, hakuna maingizo yaliyotokea kabla ya kuongeza hilo deni…?’ nikamuuliza

‘Nimekuambia hilo sikumbuki mpaka tuangalie hiyo statements, nikiangalia hiyo, nitakumbuka….’akasema

‘Hiyo ni ushahidi mwingine…’nikasema nikimgeukia mpelelezi..Mpelelezi akawa kimia tu

‘Unasema nini….ushahidi gani huo….wewe tapeli kweli, hilo lina maelezo, ngoja nikiangalia hiyo statement  nitakuambia kama ni mimi nitakumbuka maelezo yake,…..hebu shemeji  samahani , tunaomba hiyo statement ya benki, nikiona hiyo pesa na tarehe nitakumbuka maelezo yake, …’nikasema

‘Pesa ipi…?’ nikamuuliza na yeye akashtuka, akajiona keshaingia kwenye mtego, lakini keshachelewa

‘Nakumbuka umesema kuna pesa ilichukuliwa kabla,….ndio maana nataka nione hiyo statement kama ipo ipo itakuwa na sababu…’akasema

‘Hiyo nyaraka ya benki haina haja kwasasa hivi….’akasema mpelelezi

‘Umeona afande huyu ni mjanja tu…hana lolote, yawezekana kweli ipo au haipo, mimi sikumbukI na kama ipo ina sababu..na huenda benki  kwa wakati huo walikuwa hawajaweka mambo yao sawa,…kuhusu madeni, ndio maana nasema, mpaka nione hiyo statement…lakini kama ni ushahidi wake, sawa tutapambana mbele kwa mbele, mimi siogopi, maana sijafanya kosa…’akasema

‘Huyo mhasibu wa benki uliyekutana naye unamtambua kwa jina.. unaweza ukamkumbuka?’ nikamuuliza

‘Nimekuambia siwezi kuwakumbuka, kwanza ni siku nyingi…simkumbuki kabisa, ni siku nyingi jaman, hivi kweli unaweza kukumbuka kila kitu, kila mtu wa mwaka wangapi huu, na huenda keshakufa,..maana sikumbuki, na binadamu ni mpita njia tu….’akasema

‘Nakumbuka ulisema kutokana na kazi zako wewe huwaga husahau hasa watu, sura za watu hasa wale mnaoingia nao kwenye mikataba huwezi kuzisahau au sio…., sasa ilikuwaje huyo muhasibu ukamsahau…?’ nikamuuliza, na yeye akajifanya kutabasamu kabla hajajibu na mara simu yake ikaita, alipoangalia mpigaji, akasimama, na kusema;

‘Nahitaji kuujibu hii simu nje ni wateja wangu, sawa afande….’akasema na afande akasema

‘Unaweza kuijibu hiyo simu hapa hapa, kama huwezi mwambie utampigia baadaye,  au sogea pale , sisi hatuwezi kusikia mtakachoongea ,…kwani  tukisikia kuna ubaya, ni mambo halali au sio?’ Akauliza mpelelezi, na jama akaizima ile simu kwa haraka. Mpelelezi akawa kama anataka kusimama,nikajua anataka kufanya nini…ushahidi mwingine!

NB: Kibano kingine, Maswali yanaendelea muwe wavumilivu hapa, kwani ukweli uligundulika humo humo kwenye maswali…ndivyo ilivyokuwa, na hapa  utaona dua ya mwenye kudhulumiwa ilivyo na nguvu. Huyu mama mjane aliinua mikono yake juu, akasema yote anamuachia mungu…ogopa sana dua hii!


WAZO LA LEO : Moja ya dalili za mnafiki ni uwongo, akiongea hupenda kudanganya, uwongo kwake ni jambo la kawaida, na hujiona mjanja kudanganya, na hajali kupata kipato kwa njia hii ya urongo, kwake uwongo ni fani.…lakini tabia hii haishii hapa, mtu huyu hata uaminifu wake utakuwa na walakini, na huwezi kumwamini kwasabbau haaminiki,, hawezi kutunza siri…maana hulka ya uwongo imeshajijenga.  Tumuombe mungu atunusuru na tabia ya uwongo, na kama tunayo tuiache, kwani tabia hii inakuwa mama wa dalili nyingine za mnafiki, na athari yake ni kubwa.
Ni mimi: emu-three

1 comment :

Samira said...

Wanasema anaesema uwongo basi asiwe msahaulifu na mwisho wake ni aibu tupo pamoja m3