Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, March 2, 2016

SIKIO LA KUFA HALISIKII DAWA-13



Nilimtizama aliyeingia pale mlangoni jicho la kwanza lilitua kuangalia kile alichokibeba,….hisia zilikwenda mbali sana, akili yangu haikuwa sawa, …mawazo, na hisia zangu za kwanza, nikajua sasa ni shari,  akili ikajenga taswira ya hofu, ….woga , ukanitanda…akili ikaona hivyo , kile kilichotokea nikajua ndio hicho….ubongo  haukuona hali halisi uliona taswira , tukio la usiku,….

Aliingia mtu, ….na mtu huyo alikuwa kajifunika usoni, lakini baadaye akaondoa ile nguo….mimi sikuweza kumuangalia usoni moja kwa moja, niliangalia kile alichokuwa kakibeba,…..silaha…kwa muda ule nilikuwa nipo peke yangu chumbani, nikitandika kitanda!

Nilichofanya nikuachilia kile nilichokua nimekishika, na kuanza kusogea nyuma, nikitaka kupiga yowe, lakini sikuweza kufanya hivyo, mdomo ulikuwa mkavu, kiu na njaa vilikuwa vimeniandama…kwahiyo hata sauti haikuweza kutoka, ilibakia kufungua mdomo tu,…

Nilisogea kinyume nyume, na huyo aliyeingia akawa kasimama pale pale mlangoni, ni kama kunipima au kunizidishi aliendeela  kasimama  kwa muda huku akinitizama mimi…lakini cha ajabu mimi sikutaka hata kuangalia uso wake…ili nilijua ananitizama mimi…macho yangu yalikuwa yakitizama ile silaha;

‘Mhhh, naona unaogopa eeh…hahaha, kumbe na wewe ni mwoga eeh…’akasema huku akicheka, na alipocheka ndio nikamtizama, maana kicheko chake kilikuwa kama mwangwi..ooh, huo mdomo, oh, hayo meno….na kila akicheka meno yake yalionekana kama ya shetani , na nilipoona hayo maumbile ndio nikazidishia kuwa na wasiwasi, woga…yeye alikuwa bado kasimama pale pale mlangoni.

‘Mimi naona ajabu sana,inawezekanaje utembee na mume wa mtu na tendo hilo ni hatari zaidi ya hii silaha, na hukuogopa, ….eeh hebu nambie, maana tumeambiwa mke wa mtu  au mume wa mtu ni sawa na kaa la moto huwezi kulifumbata mkononi….lakini wewe uliweza, huogopi, .sasa iweje, kuiogopa silaha hii, hii ni kitu zaidi ya tendo hilo, ….’akasema sasa akiizungusha hewani ile silaha.

Nilitaka kumwambia mimi sijatembea na mume wake..na wala mume wake simjui, lakini sikuweza kutamka neno….mdomo umefunguka, lakini sauti haitoki….

Akaanza kusogea kuingia ndani, huku akitikisa kichwa huku akichezesha ile silaha kuonyesha jinsi ya kuitumia, naona lengo lake ilikuwa kunijenga hofu tu… huenda hatanidhuru…nikajipa matumaini.

‘Nikuambie ….basi kuhusu hii silaha, unaona ilivyo tofauti na silaha nyingine... ‘akainua juu  na kila ikifika hewani inameta meta kuonyesha yale makali yake. Ungeliweza kuona yale makali yake na kuyahisi…nikahisi kuwa yaweza kuukata mwili wangu, na hapo mwili ukasisimuka.

‘Siku mimi naolewa, nilipewa silaha hii na babu yangu, babu yangu alinipenda sana, kwasababu ,mimi nilikuwa jasiri yeye alipenda kuniita mke-dume, sikuwa napenda sana kucheza na wanawake wenzangu mimi nilikuwa napenda kucheza na midume, na nilikuwa napambana nayo kidume. Ndio maana muda wote nipo kama dume…sio ….lege lege..si unaniona, akainua mkono ulioshika hiyo silaha kiujasiri.

‘Nashukuru kuwa babu  yangu aliweza kuishi hadi kuhudhuria ndoa yangu na siku naolewa ndio nikashangaa ananikabidhi silaha hii…, akaniambia mjukuu wangu mimi  sina cha kukupa, ninachoweza kukupa ni silaha hii…’akatulia na kuinua ile silaha hewani.

‘Silaha,!!! Silaha ya nini babu…?’ nilimuuliza

‘Ya kulindia ndoa yako….usikubali mtu aiharibu ndoa, yako, na muhimu kata magugu na mizizi kabla mtu haujashika chini…hakikisha unangoa na mizizi yote…’alisema hivyo kimifano….mhh, unajua sikumuelewa kipindi hicho, kipindi hicho ningeelewa nini zaidi ya kuolewa,…nilijua ndoa ni ndoa tu, najua huko ni upendo tu, hakuna chuki, hakuna wabaya kama nyie, ….hata nilipofika kwa mume wangu sikuwa nimeelewa ni nini lengo la babu kunipa silaha hii na maneno yake.

‘Lakini siku nilipowafumania, …..kumbukumbu za kauli ya babu zikanirejea...nilishaisahau, kumbe, silaha hii ilitakiwa ifanye kazi yake, na unajua silaha hii niliiweka kwenye vifaa visivyotumika nikawa nimeishahau, nilipokumbuka tu nikaanza kuitafuta nilihangaika sana kutafuta hii silaha, na mara nikaiona…siku nilipowafuma, sikuwa na …kumbukumbu hii, ila leo nimekumbuka…’akasema

‘Kunifumania…!’ nilisema kimoyo moyo..

‘Sasa natumai wakati wakuifanyia kazi silaha hii umefika, bado sijachelewa..…’akasema na sasa akaingia ndani, na mimi nikazidi kurudi nyuma nikiogopa, ..na yeye akaniangalia kwa macho yaliyojaa  chuki, …chuki kweli ya kuua, ….alinikazia macho halafu akasema:

‘Unajua ….sisi wanawake ni wema sana, lakini ikifikia kwenye chuki, chuki ikatawala nafsi zetu ….mioyo yetu inageuka kuwa mibaya sana, roho mbaya inachukua nafasi…na mwanamke akiwa na roho mbaya anakuwa mkatili kweli,mimi sikuwa na  roho mbaya, lakini kwasababu yako sasa nina roho mbaya…wewe hujui tu, hivi sasa nakuchukia,..unajua kuchukia,…nakuchukia…’akasema na sauti yake ilikuwa kali mpaka nikahisi kichwa kikiuma.

‘Sasa nataka kuhakikisha silaha hii inamaliza hasira zangu,…wewe unatembea na mume wa mtu, halafu umeshamwambukiza ukimwi , ….ili na mimi aniambukize…hahaha…sasa kabla sijaambukizwa nataka kwanza wewe ufe…’akasema akinisogelea.

‘Ukimwi….! Mimi nina ukimwi….?’ Nilijiuliza kimoyo moyo, sasa akawa anasogea kunikaribia
Na mimi nikawa nasogea  kinyume nyume mpaka ikafikia sehemu siwezi tena kurudi nyuma, kukawa na kitu kimeziba kwa nyuma, …sijui ni ukuta au…sikutaka hata kugeuka nyuma, niliogopa nikigeuka nitavyekwa na ile silaha nikabakia kutoa macho tu ya uwoga,..alipokuwa hatua chache kutoka nilipo, ni karibu sana, akasimama na kusema;

‘Unajua hadi sasa najilaumu, ni kwanini sikufuata usia wa babu,sasa ni lazima nifanye hivyo, nikate shina kabla halijaweza mizizi, na hatimaye ning’oe mizizi kabisa  (akainua lile silaha juu kama anataka kuitumia)

Akanisogelea sasa akiwa kainua ile silaha juu….

Nikafunua mdomo kutaka kupiga yowe, …lakini mdomo haukufunguka….yeye sasa keshapandisha hasira anakuja kwa kasi kunikabili…nikajua kweli kadhamiria nisipojitetea huyu mtu kweli anaweza kunidhuru, aliponijia kwa kasi, huku silaha ipo juu nikajitutumua na kusogea pembeni, huku nikitumia mikono yangu miwili kumsukuma pembeni. Ilikuwa nusura ya mungu tu,…akapepesuka, na kwenda upande.

‘Kumbe…wajifanya mjanja sio, ngoja sasa nikuonyeshe, na ole wako upige yowe, sasa hivi hakuna wa kukutetea, sitakubali kamwe kuingiliwa, ni lazima nikuumize…kabla hujaondoka, nataka nifyeke magugu yote,nakutoa na mizizi, na kuhakikisha kuwa hutaweza kuota tena…..’akasema na sasa akaishusha ile silaha  kuelekea kichwani nilikwepa na nikakoswa koswa na ile silaha akanikate  begani, nilihisi maumivu makali kweli. Nilijua bega limetoka!

Silaha ile ilikuwa ni aina ya panga, lakini ni nyembamba…kama jambia…

Alipokuja kwa kasi safari hii, kutokana na maumivu kwenye bega sikuweza kumzuia , sikuweza kumsukuma kama awali, akaniweka kwenye usawa wake,….macho ya ukatili, ya uuwaji yakawa yananiangalia moja kwa moja usoni…huku akiwa kainua ile silaha juu, silaha ile ikawa inakuja sawa sawa na paji langu la uso, niliyaona makali yake …nikajua sasa nimekwisha, kichwa sasa kinapasuliwa vipande viwili….

Na mara nikasikia sauti ….oooh, nilikuwa usingizini, nikazindukana…kumbe nilikuwa naota..na hapo nikasikia mtu akigonga mlango wa nje, kumbe  ilikuwa ni asubuhi, kumbe ilikuwa ni ndoto ya kutisha,  nikakumbuka tukio la jana,….oh,  nilipokumbuka hilo tukio niikamuka haraka, nikijua natakiwa kuondoka hapo nyumbani,…

‘Hii ndoto ina ishara mbaya…’nikasema

                                    **********

Aliyekuwa kasimama mlangoni ni mama mwenye nyumba,….akinitizama kwa udadisi, akaniona ninavyoogopa,…nilivyo na wasiwasi, nikiwa na uwoga usiofichika….akatikisa kichwa kama kunisikitikia vile au kunidharau..

Kumbe wawili hawa hawakuwa bado wameelewana, japokuwa mzee alipoondoka alikuwa kawaweka sawa, lakini mzee alipoondoka mume alianza kuongea na ndio ikawa sababum mke mwenye nyumba akataka nifukuzwe humo ndani haraka iwezekanavyo, lakini mume mwenyenyumba akasema ni bora wasubiria maamuzi ya kikao

‘Mzee kasema tusubiria maamuzi ya kikao, kama tutamfukuza tutakuwa tumempuuza, subiria kwanza..’akasema

‘Je kikao kikiamua kuwa aendelee kukaa humu mpaka ajifungue, unafikiri nani ataweza kuishi na mtu kama huyo….nani atamuhudumia, unajua watu kama hao wanahitajia huduma zao tofauti…hapana mimi siwezi kukaa naye tena, najua unamtetea kwa vile keshakuwa hawara wako..’akasema mke mtu.

‘Kwani kuna tatizo gani ukimsubiria huyo mzee..?’ akauliza mume mtu

‘Mimi nilishaweka mipango yake tayari…’akasema

‘Mipango gani…mke wangu..?’ akauliza mume mtu akionyesha mshangao

‘Huyu mtu anatakiwa kuondoka hapa nyumbani haraka,…akiondoka ndio tunaweza kusikilizana mimi na wewe la sivyo, msimamo wangu utakuwa ule ule..unipe talaka yangu….’ akasema

‘Mke wangu maswala ya talaka achana nayo, mimi ninachoona cha muhimu tunamsubiria mzee arudi, yeye ndiye atatuambia la kufanya..najua kikao kitaweza kutafuta ufumbuzi wa haya na mambo mengine ya ndani hayana tija kuyaongea kwa watu….mimi sivyo kama unavyofikiria wewe…..ilitokea tu..kana nilivyosema awali, na wewe ulifika muda nikiwa namtuliza alale…..’akasema mume mtu

‘Sikiliza mimi siwezi kurudi nyuma, kwani tulikubaliana au sio, mengine ni yenu, na niwaambie kitu, huyu hapa anaondoka, na ahame kabisa hiki kijiji, maana nikimuona nitakumbukia, na hata watu watanicheka, nimeshachukua maamuzi na ni lazima yafanye kazi…’akasema mke mtu

‘Kwani mke wangu una haraka gani, huyu mtu ataondoka kama ulivyotaka wewe, lakini hatuwezi kumfukuza kama mwizi….tujaribu kuwa waungwana..’akasema mume mtu

‘Waungwana eeh, nyia mliyokuwa mkiyafanya mlifanya kiungwana eeh, huo ndio uungwana  sio….?’ Akasema

‘Haya hebu niambie wewe unataka tufanye nini….?’ Akauliza mume mtu alipoona mke kadhamiria

‘Kama nilivyokuambia mimi nilishamuandalia huyu hawara wako kila kitu,…anatakiwa kuondoka, tena sasa hivi, hata tiketi yake ya kusafiria nilishaiagizia kwa simu….siwezi kusubiria tena, …

‘Unakumbuka yule mtu aliyekuja kugonga  mlango asubuhi asubuhi ni wakala wa usafiri, alileta tiketi ya basi, ….sasa haya ya kumsubiria huyo mzee yatachelewesha, muda unakwenda na mzee hajarudi, sijui wameamua nini huko, …vyovyote iwavyo huyu mtu anatakiwa kuondoka, na tukiendelea kusubiria hapa huyu mdada atakosa usafiri na pesa yangu itapotea…’akasema

‘Mke wangu tiketi ya kwenda wapi…?’ akauliza mume mtu kwa mshangao

‘Anakwenda huko kunakomfaa, anakwenda sehemu ambayo najua atapata huduma zinazomstahiki….’akasema

‘Mke wangu…..’mume akatakakuongea lakini mke akasimama akaingia chumba kingine na mara akatoka, akiwa kashikilia begi la safari..’

‘Mimi nataka kukuonyesha kuwa mimi namjali huyo hawara wako kuliko nyie, wewe kinachokuongoza hapo ni tamaa zako za kimwili, lakini mimi kinachoniongoza hapa ni upendo wa mstakabali wake wa baadaye..jinsi tutakavyoweza kumsaidia huyu ili aweze kusogeza siku zake za kuishi, na hicho kiumbe huko tumboni kizaliwe kikiwa salama…’akasema mke mtu

‘Unajua mke wangu, hayo mnayozaungumza ni maneno ya kusikia tu..hayana ushahidi, …na nikuambie kitu, kauli hiyo ya kuwa kaathirika, ni bora usiiongee kabisa una uhakika gani, ….je kama sio kweli, huoni mtakuwa kwenye dhambi kubwa sana…’akasema mume mtu

‘Hahaha……nikuambie kitu, hilo mimi  nina uhakika nalo…huyo mtu kaathirika,…hilo sana shaka nalo, nimethibitisha…. ndio maana nataka na wewe , huyo hawara  wako akiondoka tu, mimi na wewe mguu kwa mguu tunaende ukapime. …hilo sharti lazima litimizwe kama nilivyomuambia mzee…’akasema

‘Lakini sasa kwanini hukumwambia mzee kuwa umeshakata tiketi ya basi, na….?’ akauliza

‘Najua Mzee asingekubali,. ..sijui huyo mwanamke kawapa nini nyie wanaume…huyu mzee kabadilika kweli,…kisa  huyo mwanamke humwambii kitu,…hebu  wewe fikiria alisema nikipata ushahidi tu..yeye hatasubiria nini wala nini…atamfukuza huyo mwanamke, sasa kipo wapi…, sasa eeeh, mpaka kikao  eeeh, subirini  eeeh…nimechoka! Sasa nyie sisubirini , mimi nachukua maamuzi, hapa sasa ni kazi tu, aondoke….’akasema

‘Mke wangu…..sio vizuri hivyo,  wema wetu wote utakuwa hauna maana, ..hebu niambie utamwambia nini,…aondoke?, unamfukuza?.....mimi sipendi tabia hiyo kabisa, basi mpe pesa hii ije imsaidie, kama umeamua hivyo….’ Akauliza na kusema mume mtu

‘Wewe subiri tu utaona nitakachokifanya, ….ataondokana akiwa anajuta,…na  kwa hili….sitaki uniingilie, wewe ukae humu humu ndani…huyu atatoka na hatarudi tena, na hutamuona tena maishani mwako…..’akasema na kutoka akimuacha mumewe akiwa kaduwaa tu,…

Mume mtu alishika kichwa akiwa kajiinamia, na baadaye akaona hawezi kuvumilia, akashindwa kujizuia, akasimama na kuanza kumfuatilia mkewe kwa nyuma….

‘Huyu anaweza kuzua balaa, ngoja nikamuwahi kumzua,  ….’akasema


NB: Hivyo ndivyo ilikuwa, je na hapo kuna rejea nyingi!  Visa vyangu ni maandalizi ya tamithilya, …movies !


WAZO LA LEO: Uchungu wa kuibiwa ndoa, aujuaye ni mwanandoa, huwezi kuutathimini uchungu huo mpaka siku likukute. Hala hala, wale wenye tabia hiyo, ndoa ni kitu kitakatifu, hakitakiwi kuchafuliwa ovyo, na ikitokea kuchafuliwa madhara yake ni makubwa sana…acha, na tubu kwa mola  na kama hujaoa au kuolewa muombe mola wako akusaidie umpate mke au mume mwema.

Ni mimi: emu-three

No comments :