Pamoja na hayo wakili alijitahidi
kupeleka maombi kuhusu hiyo kesi akielezea mambo mengi, ikiwemo hali ya afya ya
mshitakiwa , na ombi likawa ‘ikiwezekana kesi hiyo iwe ni ya madai tu’ na
ikiwezekana kesi hiyo imalizwe nyumbani, lakini hilo halikuwezekana, Na wakili
alipokutana na Profesa kuyaeleza hayo akasema;
‘Kwanza waliofanyiwa hivyo,
hawajaonyesha ushirikiano, siku ya kusikilizwa ombi letu, walihitajika wawepo,
hawakufika,... na hakuna maelezo yoyote kutoka kwao kuwa wamekubali kuwa kesi
hiyo imalizwe nyumbani...’akasema wakili
‘Lakini uliongea nao kama
nilivyokuomba...?’ akauliza
‘Nilifika nikaongea nao lakini hapo
hapo walikataa hilo ombi, nikaona nipeleke ombi hilo kwa hakimu, na nikajua
wakitwa kulisikiliza hilo ombi watafika tu, lakini cha ajabu hawakufika kama
walivyosema...’akasema wakili
‘Sasa hakimu kwanini hakuwachukulia
hatua kukaidi ombi lake...?’ akauliza Profesa
‘Hilo sio ombi la hakimu, hilo ni ombi
letu, na nia ni kujenga ushawishi, uelewe hapo, nilitaka wao wakiwepo kuwe na
uzito wa kumshawishi hakimu, hakimu asingeliweza kuwaita kwa ombi letu, yeye
anasubiria hayo yafanyike mahakamani...na tunachofanya sisi ni kuyamaliza
kwanza nje....’akasema wakili huyo
‘Halafu kuna jambo jingine,
wameniambia, sasa sijui ni nyie mlifanya hivyo, au wao wameamua kutunga tu....’akasema
‘Jambo gani...?’ akauliza
‘Wanasema wametishiwa amani , eti kuna
watu walifika wakatoa vitisho kuwa wasipofuta hiyo kesi nyumba yao itachomwa
moto, na mambo mengi tu, sasa sijui ni nani alifanya hivyo...’akasema wakili
‘Hakuna mtu aliyefanya hivyo,
wametunga uwongo wao...namfahamu yule anaweza kuzusha mambo tu....’akasema
profesa
‘Mimi nilikuwa na ushauri mwingine
japo umekuwa ukiukataa, mimi naona sasa ni wakati muafaka wewe kwenda kuonana
na wao huenda italeta uzito fulani, ninachotaka ni wao watoe ushirikiano,
utakaoweza kumshawishi hakimu akibali ombi letu....’akasema wakili
‘Kwakweli kwa hivi sasa siwezi kuonana nao, nitazua makubwa
zaidi, ....’akasema Profesa
‘Basi kaka yako afanye hivyo, kwa hali
yake kwa hivi sasa anaweza kufika huku mjini, au sio afike akawaombe
msamaha..huenda itasaidia...’akasema wakili
‘Kaka amesema hawezi kwenda kuwaomba
msamaha kwa vile yeye anaona hana kosa....’akasema Profesa
‘Sasa hilo ndilo linaleta utata, maana
kama nyie pande mbili hamjaafikiana, mnatarajia nini mbele ya hakimu, yeye
ataliona hilo ombi ni muafaka kama nyote mumeafikiana,, mimi inaniwia vigumu
sana, ...’akasema
‘Mhh, kiukweli ni jambo lenye utata,
na najaribu kukwepa maafa zaidi....’akasema Profesa
‘Basi ....iliyobakia tusubirie
mahakamani...’akasema wakili
Kisa
kinaendelea
*********
Siku kabla ya
kesi mama mmoja alifka kwenye nyumba ambayo wanaishi watu hao waliofanyiwa
fujo, mama huyo akiwa na binti mdogo anayemuongoza akagonga mlango na mlinzi
akajitokeza na kuuliza
‘Nyie nani na
mnataka nini....?’
‘Mimi naomba
kuonana na mwenye nyumba hii....’huyo mama akasema
Yule mlinzi
akamuangalia huyo mama, na huyo binti ambaye alikuwa naye, halafu akasema
‘Mna shida
gani na mwenye nyumba....?’ akauliza
‘Nataka
kuongea naye kuhusu kesi iliyopo mahakamani....’akasema huyo mama
‘Jamani
mumeshaambiwa kesi hiyo ipo mahakamani hakuna lolote linaloweza kufanyika kwa
hivi sasa, ...wewe wataka kuongea nini zaidi na mwenyenyumba kama unataka
kuongelea hiyo kesi nenda mahakamani....’akasema mlinzi
‘Mimi
ninataka kuongea na huyo mtu, kwanza nataka nimuone,...ninahisi namfahamu
tafadhali kabla mambo hayajaharibika nataka nionane naye......’akasema na mara
mwenye nyumba akatokea
Kumbe kwa
muda huo mwenye nyumba alikiuwa akitembea tembea nje kunyosha miguu na ndio
akasikia mlinzi akiongea na hao wageni, akaona afike kuona ni akina nani
Akasogea hadi
pale mlangoni, ndipo akamuona huyo mama akiwa na binti, wakiongea na mlinzi
Ni nani hao
na wanataka nini....?’ akauliza
Na yule mama
aliposikia sauti ya kiume , maana huyo mama haoni vizuri, akashtuka, akageuka
kuelekea kule sauti ilipotokea, akasema
‘sio wewe
kweli,....’akasema huyu mama akitaka kusogea lakini mlinzi akamzuia
‘Sio wewe
maana yake nini, wewe mama unataka nini...?’ akaulizwa na mlinzi
‘Ndio wewe nimekutafuta
na sasa nimekuona, mungu wangu, ndio wewe, ndio wewe kabisa, nahisi sauti yako
moyoni mwangu....’akasema huyo mama
‘Wewe mama
vipi umechanganyikiwa nini....’akasema mlinzi na yule mwenye nyumba akawa
kasimama kaduwaa akawa anamuangalia huyo mama, halafu akageuka kuondoka.
‘Waondoke
zao,mimi siwajui...’akasema mwenye nyumba, na huku nyuma yule mama akawa
anaongea
‘Ndio wewe,
nilikuota jana kuwa umekuja upo hapa kwenye nyumba nzuri...., ndio wewe kabisa,
ngoja nisogee nikuguse nihakikishe....’yule mama akasema na wakati huo huyo
mwenye nyumba alishaondoka, na aliyemjibu ni mlinzi akasema
‘Wewe mama
mwenye nyumba hakutambui, kasema muondokei, ....’akasema
‘Kwani wewe
mama una shida gani,....?.’akasema mlinzi
‘Shida gani
nyingine niliyo nayo mimi, jiulize kwanini nitokea kote huko nije mpaka hapa,
huyo binti hajui lolote nimeongozwa na hisia zangu hadi nikafika hapa, ..namtaka
huyo niongee naye nahisi you matatani, .....’akasema huyo mama
‘Ujanja wenu
huo ...mnatumia ujanja wa kuja hapa kuomba omba,leo mwenye nyumba hana pesa za
kutoa , ...kwahiyo ondokeni hapa la sivyo mtakwenda kulala jela,,,,.’akasema
huyo mlinzi na kufunga mlango
***********
Mwenye nyumba
akarudi ndani akawa anaongea na mkewe
‘Unajua kuna
mama mmoja kafika hapo getini akawa anaongea maneno ya ajabu, eti anasema ndio
wewe, nilikuota,...’akasema huku akicheke kwa dharau, na mkewe akashituka na
kugeuka kumuangalia
‘Mhh...kwanini
asema hivyo, ulimuuliza aliota nini, na huyo mama katokea wapi,i?’ akauliza
mkewe
‘Ndivyo
walivyo watu wa huku, wanaweza kutumia kila mbinu kutafuta misaada, mimi simjui
kabisa huyo mama, halafu nashangaa ....huyu mama , lakini sio yeye, kipindi
hicho nilikuwa mdogo, huyu mama ni mzee zaidi, na cha ajabu anaonekana haoni,
ndio hapo naona ajabu, alitambuaje,....’akasema akibenua mdomo kwa dharau
‘Kwanini
unasema haoni?’ akauliza mkewe akionyesha uso wa huruma
‘Anaongozwa
na binti mdogo kashikwa mikono....’akasema
‘Jamani sasa
kwanini usingelimkaribisha ukampa chochote,,...nahisi alikuwa anahitajia
msaada, tatizo la nchi yenu hakuna taratibu za kuwasaidia watu kama hao
wasiojiweza, inabidi nyie raia musaidie...’akasema mkewe
‘Nimechoka na
hawa watu ,...kila siku anakuja huyu mara yule wote wanaomba omba, tutapatia
wapi pesa za kutoa kila mara, achana na hao watu kabisa....’akasema
‘Lakini
nikuulize je yeye alisema amekuja kwa nia ya kuomba msaada au alikuja kwa swala
gani?’ akauliza mkewe
‘Nilisikia
akimwambia mlinzi eti amekuja kuhusiana na hiyo kesi, nikajua huenda ni mke wa
yule mshitakiwa, nikawa na hamasa ya kumuona huyo mwanamke yupoje...., na
nilipofika tu, huyo mama akashikwa na kitu kama mshituko aliposikia sauti yangu
ndio akasema maneno hayo:
‘Ni
wewe....ni wewe,...nilijua tu,..ni wewe nilikuota....alikuwa anaongea kwa hisia
za ajabu, nikahisi amechanganyikiwa.....’
‘Kuna jambo
hapo, huenda kweli ni mke wa mshitakiwa huyo, lakini huyo mshitakiwa yeye siku
ile hukumtambua vyema ni nani......?’ akauliza
‘Hatukuweza
kuongea zaidi, yeye alidai kuwa yule mtu anayejiita Profesa ...kama hivyo,
maana sijawa na uhakika, eti alikuwa ni ndugu yake, aliyepotea....na kwa hali
ilivyokuwa, sikuwa na muda wa kumtambua vyema yeye ni nani.....hata wewe
ungekuwepo, ukashikwa na hasira,...kamuumiza mlinzi na bado analeta kiburi,
...nikampa kichapo, nahisi nilimvunja mbavu, maana ni mbishi hasikii, ....’akasema
‘Hapo na wewe
ulifanya kosa ...’akasema huyo mkewe
‘Kwa hali
kama ile ungelifanya nini, ni mbishi, lakini alichokipata sasa atakuwa
keshajifunza adabu, hii mijitu ni sugu kweli hata ukipiga haiskii
kipigo....’akasema
‘Kama huyo
mama anadai kuwa alikuota....mmh, kuna kitu hapa...tatizo wewe hujataka
kulichunguza hili swala kwa undani zaidi, nahisi hawa watu wanaweza kuwa
wanandugu wa marehemu...?’’akasema mkewe
‘Hahahaha....ungeliona
sura ya huyo baba, ..hahaha sura mbaya, jitu jeusi, sijui wanaweza kuwa na
ndugu naye, sasa kwanini niwachunguze ili iweje....labda kama ni ndugu zake
marehemu naweza kukumbuka aliwahi kuja mzee mmoja mimi nikiwa mdogo, akaai yeye
ni baba yangu, siwezi kujua kama ndio yeye au la,....’akasema
‘Lakini mimi
ninahisi hii kesi inaweza kuzua mambo mengine ....kwanini tusisaidie hii kesi
iishe, tuachane na hawa watu kwa amani....’akasema huyo mkewe
‘Unanishangaza
kweli mwenyewe ulisema umechoka na huo usumbufu wao, jinsi wanavyokuja hapa
mara kwa mara, dawa yao ndio hiyo, akifungwa mtu mmoja watakaoma kabisa kuja
hapa tena, lakini kama hakutafanyika jambo la fundisho, kila siku utakuwa
ukipokea wageni hapa.
Hawa watu hawataki kufanya kazi , wao kuomba omba tu....’akasema
‘Mhh, kweli watu
wenu wamezidi,....kuomba omba, halafu wanakuja kwenye makazi ya watu, bila hata
taarifa, hawajali muda,..kweli nimechoka na usumbufu wao,’akasema mke mtu
‘Ndio maana
nataka wahukumiwe iwe ni fundisho kwao....’akasema
‘Na kama ni
kesi huwezi kukwepa kwenda mahakamani..kama ukiitwa utafanyaje...?’ akauliza
mkewe
‘Mimi
siendi.....na yule wakili wao akija hapa sitaki kuongea naye tena.....’akasema
‘Ili
kulimaliza hili inatakiwa utoe ushahidi kuwa watu hawa ni wakorofi....’akasema
mkewe
‘Kama wewe
una muda wa kufuatilia mambo hayo nenda, mimi sina muda huo, kwanza sasa hivi
tunafunga mahesabu ya mwaka huko kazini ,, ..leo tu nilitakiwa nifike , nimeomba
ruhusa tu, nilitakiwa niwepo huko, baaaye nitaondoka, sijui wewe.....’akasema
‘Hata sisi ni
hivyo hivyo....ila leo mimi napumzika siendi huko kazini....’akasema mkewe
‘Unaona eeh, sasa
kwanini tupoteze muda na mambo hayo ya kujitakia, waache wenyewe mahakama na
hakimu wao, wataamua , hiyo kesi ipo mahakamani, na kama nitasikia hakimu
kawasamehe nitaona ajabu kweli, ndio nitajua hawa watu hawafuatii sheria,...’akasema
‘Kwanini....ina
maana unataka wahukumiwe wafungwe?’ akauliza mkewe
‘Wewe unaona
walichokifanya ni sahihi, mtu afike kwenye nyumba ya watu alete vurugu, ampige
mlinzi ..wewe unaona hiyo ni sahihi kweli ?, kama ingekuwa huko ulaya unafikiri
ingekuwaje...?’ akauliza kwa msisitizo.
‘Kiukweli walichokifanya
sio sahihi,....lakini mpaka sasa najiuliza kwanini hayo yote yatokee,’akasema
mkewe
‘Ni wahuni
tu....’akasema mumewe
‘Lakini
nikuulize kitu, yule mtu aliyekuja na kujiita Profesa, kweli sio ndugu wa yule
marehemu,...mimi bado naliwazia hilo, japokuwa nilipompigia mama alisema yule
Profesa alifariki, yeye ana uhakika huo,...’akasema
‘Sasa una
wasiwasi gani naye...’akauliza mumewe
‘Wanafanana
sana.....nilimwambia mama akasema yule mtu asingeliweza kupona, na aliwasiliana
na watu anaowafahamu huku, wakamthibitishia hivyo,... ila mimi nahisi kuwa
huyu, anaweza kuwa ni ndugu yake,maana wanafanana kweli kweli...hivi kwanini wewe
..haujalifuatilia hilo kuwafahamu hao watu vyema....?’ akauliza
‘Sina muda
huo kabisa...na kama ni hiyo familia sitaki kabida kujuana nayo, na huyu mzee,
mmmh, labda ndio yeye,aliyekuja kipindi kile nikiwa mdogo, na kama ni yeye,
.....sitaki kabisa kufahamiana naye...’akatulia
‘Unakumbuka
nini ulipokuwa mdogo, huyo mzee alikuwaje, kwanini hutak ufahamiane naye...?.’akauliza
mkewe, na mara simu ya huyo jamaa ikalia, na alipoangalia akaona ni namba ngeni
kwenye simu yake,akaipokea,
‘Halooh ni
nani mwenzangu, ....’akasema na akawa anasikiliza kwa muda halafu akasema
‘Kwa kweli
mimi sina muda wa kufika mahakamani, nawaambia hivi, nyie mnafahamu sheria si
ndio..., na mahakama ndio mwamuzi au sio, basi sheria ifuate mkondo wake,
....nyie ongeeni ilivyokuwa na hukumu
itolewe kwani kuna tatizo gani,... lakini mimi siwezi kufika huko kabisa,
....’akasema akatulia kusikiliza , halafu akasema
‘Mimi nitaona
ajabu sana,....’akasema na kutilia akisikiliza na baadaye akasema
‘Ni kweli alikuja
mtu hapa akisema yeye ni wakili, amekuja kuleta maombi ya mshitakiwa, kiukweli sikuweza
kukubaliana na hayo maombi yake, kwa vile hayana msingi,...’akasema na kutulia
kusikiliza
‘Hapana....siwezi
kukubaliana na hilo ombi lao, kwa vile kweli alileta vurugu, alimuumiza mlinzi
wangu,kama nitakualiana na hilo ombi, watakuwa wanakuja tena na tena,mimi naona
ni bora adhabu itolewe ili iwe ni fundisho, lakini zaidi ya hayo kiukweli
nimechoka na hao watu.....’akasema na kusikiliza
‘Ndio alisema
ni wakili wao...’akasema na kutulia
‘Unaona eeh,kama
wamefikia kutafuta wakili basi ujue wamejiamini,....sasa mimi nifanyeje....?’akasema
na kuuliza, akawa anasikiliza kwa muda halafu akasema
‘Muda, sina
.....ooh,.....nilishawaambia mimi sina muda wa kufika huko, ....’akasema na
baadaye akamaliza kuongea na hiyo simu na kukaa kimia, mkewe akawa anasubiria
kusikia ni nini mumewe aliambiwa kwenye simu.
‘Huyo ni
muendesha mashitaka anasema natakiwa niwemo mahakamani kutoa ushahidi siku ya
hiyo kesi...’akasema
‘Nilijua
tu,...sasa itakuwaje...?’ akauliza mkewe na mumewe akajipiga na mikono kama
kukata tamaa, halafu akasema;
‘Anasema kuna
barua italetwa ya mahakama, ni lazima niwepo,...’akasema
‘Kwahiyo ni
lazima uende,.....hao umepatikana, sasa utafanyaje...’akasema mkewe na jamaa
akatulia akiwaza jambo, baadaye akasema
‘Nitaangalia.....’akatulia
akiwa anawaza jambo, na mkewe akataka kuongea jambo, lakini
kabla hajasema neno
mara mlinzi akagonga mlango na kusema
‘Kuna mgeni
getini anataka kuja kuongea na wewe.....’akasema mlinzi
‘Ni nani tena,
si nilishakuambia......?’akauliza mwenye nyumba na kabla hajamaliza, sauti
ikasema kwa nje...
‘Ni mimi.....’
mlinzi aligeuka nyuma kwa mshituko
WAZO LA LEO: Kusameheana ni jambo jema na lenye
busara,na hujenga upendo na mshikamano wa dhati,... lakini tabia ya kusamehe
ianzie moyoni mwa mtu kwanza, uwe nayo katika maisha yako, kwani huwezi
kutazamia kusamehewa, kama wewe mwenyewe huna tabia ya kusamehe. Usitarajia kutendewa
mema kama wewe sio mtenda mema, ....kumbuka mwenye tabia ya kusamehe naye
husamehewa.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment