Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, October 23, 2015

RADHI YA WAZAZI-48




Ni siku ya pili Profesa haonekani huko kijijini.....

‘Huyu mtu kaenda wapi...?’ kaka mtu akajiuliza

Kaka mtu akajaribu kuwauliza majirani na hata watu wanaomfahamu huyo ndugu yake huko anapofanyia biashara zake huko mjini, lakini hakuna aliyeweza kumsaidia,kila alijubu sijui,...

Mwisho wa siku uamuzi ukapitishwa, kuwa ni bora kwenda kumtafuta huko huko  mjini...mji una mengi, na isitoshe ndugu yake huyo ni mgonjwa, huenda alizidiwa, huenda.....

Tuendelee na kisa chetu...

Siku iliyofuata kaka yake Profesa alifika mjini na kwenda kwenye nyumba ambayo alielekezwa kuwa profesa alionekana akiiingia hapo, na watu hawakumuona akitoka

‘Ataingiaje apotelee humo humo....’akauliza kaka mtu

‘Labda ufika ukawaulizie walinzi...’akaambiwa na watu waliowahi kumuona mtu akiingia humo ambaye anafanana na maelezo ya huyo kaka mtu.

Akaikagua hiyo nyumba, akiona mabadiliko makubwa, nyumba aliyokuwa akiifahamu zamani haikuwa hivyo, ina maana nyumba hiyo imefanyiwa ukarabati mkubwa hadi kubadilika, lakini alikuwa na uhakika ni hapo ndipo ilikuwepo nyumba ya ndugu yake...

Japo hakupenda kufika kwenye nyumba hiyo, hakupenda kabisa kuyaingilia maisha ya Profesa na watu wake, hasa baada ya kusikia maelezo aliyosimuliwa na mdogo wake,...lakini hakuwa na jinsi , ndugu yake hajaonekana leo siku ya pili, na sio kawaida yake na mtu mwenyewe ni mgonjwa.

‘Ni lazima niwaulize nijue .....huenda, yupo humo ndani, au...., na kwanini kama kapatwa na tatizo, mbona hajapiga simu, ...’akawa anajiuliza huku akielekea kwenye hiyo nyumba.
Wakati anaondoka huko kijijini alipitia kwa jirani yake mmoja ambaye naye ana biashara mjini,kama anaweza kuwa na taarifa yoyote...

‘Hapana, kiukweli sina chochote nikijuacho kuhusu yeye....kwani hajafika huko nyumbani kwake,....?’ akauliza huyo jirani

‘Hajafika siku ya pili sasa...’akasema kaka mtu..

‘Muhimu ni kwenda huko mjini, mtu mwenyewe mgonjwa labda kazidiwa, na wengi wa pale hawamfahamu sana, watu waliopo sasa ni wageni wageni tu..’akaambiwa na jirani

‘Lakini hali yake sio ya kuzidiwa, kajaribu kufuatilia masharti, ..hakuwa na hali mbaya, si mnamuona mwenyewe alivyo, kanenepa, sio yule maiti aliyefika hapa....’akasema kaka mtu

‘Hahaha, na wewe bwana ina maana ulifikia kumuita ndugu yako maiti..’akasema jirani yake

‘Wewe ulimuona alivyokuwa,kipindi anafika ...aliisha ya kutisha hadi mifupa yote unaihesabu..kweli kuumwa sio kufa, na mungu kamjalia, sasa kanawiri, na alivyo mshari, huenda kafika mjini kalianzisha...’akasema kaka mtu

‘Ina maana unajua kaenda huko kwa shari?’ akaulizwa

‘Hapana, hajasema hivyo, huwa anakwenda kuuza uza dawa zake, ili apate kujikimu..dawa zake zinatibu, watu wanazitafuta....lakini huwezi jua, ya mjini mengi....’akasema

‘Sasa kwanini hajapiga hata simu?’ akauliza jirani

‘Ndio hilo linanitia mashaka, na kwa vile nina safari ya mjini, nitayajua huko huko, na kama kuna mtu kamnyanyapaa ndugu yangu tutapambana huko huko, nasikia kuna watu wenye tabia hizo chafu..’akasema kaka mtu

‘Siku hizi mambo hayo hayapo bwana...kwanza sasa hivi mtu anaumwa na mwili wake, na huwezi hata kumdhania kuwa mtu huyo ni mgonjwa, ....’akasema jirani

‘Kuna watu wanaweza kumfahamu alipotokea, si unajua tena, lakini hayo nawazia tu sina uhakika nayo ....’akasema kaka mtu

‘Sizani,..tuombe mungu kuwa yupo salama, labda kuna mengine kakutana nayo,..au watu wa manispaa wamemkamata, kwani biashaar zake zina kibali cha kuuza hayo madawa...?’ akaulizwa

‘Tena cha kimataifa...ana kadi yake ya kuhalalisha biashara yake, imethibitishwa huko ulaya, hilo la kukamatwa na watu wa manisipaa, sizani,...lakini nitajua yote nikifika huko...’akasema

Basi kesho yake asubuhi na mapema akapanda gari la kwanza na kufika mjini, wakati anahangaika kutafuta vifaa vyake huku anaulizia, na baadaye akafika sehemu maalumu ambayo aliambiwa kuwa ndugu yake huyo huwa anauzia dawa zake, mara kwa mara

Na akakutana na jamaa mmoja ambaye alimuelezea ilivyokuwa;

‘Ndugu yako jana alipomaliza kuuza dawa zake alisema kuna sehemu anapitia...’akaambiwa

‘Sehemu gani?’ akauliza kaka mtu

‘Hajasema, lakini nahisi ni pale ilipokuwa nyumba ambayo anadai yeye alikuwa akiimiliki....ina maana hayupo nyumbani ?’ akasema jamaa na kuuliza

‘Hajafika leo siku ya pili, Una uhakika atakuwa alikwenda huko?’ akauliza kaka mtu

‘Sina uhakika sana...., lakini kinachonifanya nihisi hivyo, yeye siku ile, aliondoka mwanzoni, akafika huko, na baadaye akarudi akasema huko alipokwenda hakuwakuta wenyeji,...’akasema

‘Wenyeji gani?’ akauliza kaka mtu

‘Mimi hapo sijui,..ila yeye alisema alitaka kuonana na watu wanaoishi kwenye  nyumba hiyo...mimi sijui ni nyumba gani...’akasema mtu ambaye naye anauza madawa, na huwa wanajuana na Profesa, kwa kipindi hiki, japo hajui maisha ya nyuma ya Profesa.

‘Ilikuwa muda gani alipokwenda huko?’ akauliza kaka mtu

‘Ilikuwa muda wa mchana hivi, ni kama saa nane hivi,...nahisi kuna kitu kilikuwa kikimsumbua, hakuonekana kama ilivyo siku za kawaida...’akasema

‘Hakusema anaumwa?’ akaulizwa

‘Hapana, alisema yupo na afya njema kabisa,...ila mimi nilihisi kuna kitu anafikiria sana...’akasema

‘Kwahiyo alipokwenda mchana akarudi, halafu akaenda tena muda gani, jioni,..kwanini?’ akauliza

‘Bro kiukweli mimi sijui mambo yake, jamaa ni msiri sana na mambo yake, unajua hata jioni mara nyingi tunaongozana, lakini siku ile,...hatukuongozana kituoni kama kawaida, yeye alisema kuna sehemu anapitia, sikuwa na muda wa kumuuliza maana ilikuwa ni muda kila mmoja anahangaika kutafuta usafiri....’akaambiwa

‘Kwahiyo ni vyema niende huko nikaulizie..ooh, sipendi kabisa kwenda huko,...kujiingiza kwenye mambo yake, lakini sina ujanja , ni lazima niende nione kama alifika huko..’akasema

‘Sawa utatufahamisha basi kinachoendelea kama kuna msaada unahitajia, utatuambia, maana yule ni mwenzetu japo hatujaanzisha ushirika, tuna wazo hilo la kuanzisha ushirikiano wa kuuaza madawa, ngoja tukae vyema...’akaambiwa

‘Sawa ni wazo zuri, ngoja nifike, nitakuja kuwapa taarifa.....na huu mzigo wangu nauacha hapa...’akasema

Ndipo akaelekea huko....

Akafika kwenye hilo jengo na kugonga mlango, na mlinzi akafungua mlango mdogo wa kupitia watu, akamuangalia huyo mzee juu hadi chini, akauliza

‘Una shida gani mzee?’ akauliza

‘Ndio salamu hiyo...?’ akauliza huyo mzee naye akimkagua mlinzi kama alivyofanya yeye

‘Shikamoo mzee, nikusaidie nini...?’ akauliza huyo askari

‘Kuna ndugu yangu alifika hapa siku mbili zilizopita, nasikia aliingia humu, na hajaonekana akitoka tena, ...je humo ndani anafanya nini?’ akauliza na huyo mlinzi akatulia kama anawaza

‘Una uhakika na unachokisema,...mtu aingia halafu asionekane, ni nani huyo, au umekosea nyumba...’akasema

‘Sijakosea ni hapa hapa....’akasema

‘Yupoje huyo ndugu yako?’ akauliza huyo mlinzi akionyesha uso wa mashaka.

‘Ni mwembamba-mbembamba  hivi,....ananyoa kipanki..kimtindo wake....’akasema na huyo mlinzi akamchunguza huyo mzee halafu akasema

‘Mhh,....’akaguna hivyo, na akawa anaendelea kumkagua huyo mzee, halafu akasema

‘Naona kidogo mnafanana naye, ...ndio alifika mtu kama huyo, alifika hapa akitaka kuonana na wenye nyumba, na bahati mbaya, ...’ hapo akatulia kidogo, halafu akasema

‘Hivi huyo ndugu yako ana matatizo gani?’ akauliza

‘Bahati mbaya nini, kapatwa na nini?’ akauliza mzee huyo akionyesha wasiwasi

‘Alidondoka tu na kupoteza fahamu....tuliambiwa na mabosi zangu walipotoka hositalini, maana walitoka na gari kwa haraka hatujui kuwa ndani kuna mtu, kumbe ndio yeye alizidiwa huko ndani, ni mgonjwa mgonjwa eeh,...’akasema kama anauliza

‘Hospitalini, kalazwa, au imekuwaje na alidondokaje, ....hadi kupoteza fahamu, hivi hivi tu ..bila sababu. yoyote...?’ akauliza

‘Ndio kwa maelezo ya mabosi zangu ndivyo ilivyokuwa,  kama una zaidi nenda hospitali hii hapa....’yule mlinzi akatoa karatasi aliyopewa, na mabosi zake kuwa kama atakuja ndugu akiulizia kuhusu huyo mtu, aelekezwe huko, ya kuwa huyo mgonjwa kalazwa kwenye hiyo hospitali zaidi watapatia maelezo huko...

‘Nataka kujua kilichomtokea hapa hadi akadondoka na kupoteza fahamu...lazima kuna sababu...’akasema huyo kaka mtu

‘Sisi kazi yetu ni ulinzi, yaliyotokea huko ndani hatujui,..tunachojua na tulichoambiwa ni kuwa ndugu yenu alidondoka na kupoteza fahamu, na ikafanyika juhudu za kumtibia, kwa kupelekwa hospitalini,...na yuko huko akiendelea na matibabu, mengine zaidi utayapatia huko huko hospitalini...’akasema mlinzi

‘Naweza kuonana na wenyewe, wapo ndani au sio....?’ akauliza

‘Hujanielewa mzee,kiachotakiwa ni wewe.uende hospitalini, huko ndipo utamuona mgonjwa wako, na huko ndipo utayapata maelezo zaidi, hapa huwezi kupata lolote, na wenyewe hawapo, wamekwenda kazini....’akasema mlinzi

‘Wanarudi saa ngapi?’ akauliza Mzee akiwa kamkazia macho huyo mlinzi

‘Kwani lengo lako ni nini, kuwaona wenyeji au kumuona ndugu yako?’ akaulizwa Mlinzi akimuangalia huyo mzee kama anamkagua chini juu...

‘Ni vyema nikajua kilichotokea,...na nini sababu iliyofanya ndugu yangu kudondoka na kupoteza fahamu...nani ataniambia kama sio hao watu aliokuwa nao kipindi anadondoka, na kwanini adondoke humo ndani asidondokee nje,...mpaka afikie kupoteze fahamu, nakaa naye haijawahi kutokea hivyo...’akasema

‘Ndugu yako anaonekana ni mgonjwa,...hata ukimuangalia hivi kwa macho anaonekana ni mgonjwa, sasa labda tukuulieze wewe ndugu yako ana matatizo gani...’akasema mlinzi

‘Nani kakuambia ndugu yangu ni mgonjwa,...hata kama ni mgonjwa, haijatokea kudondoka na kupoteza fahamu nikiwa naye, na sio kwa vile unamuona ni mwembaba ndio useme ni mgonjwa, watu wengine wanakuwa hivyo kutokana na nakama za maisha tu....’akasema

‘Hahaha, nakama za maisha eeh, kumbe....’akasea

‘Kumbe nini....?’ akauliza kaka mtu

‘Kumbe , alikuja hapa kuomba, au.na njaa zake..nyie watu nyie, mnatafuta sababu,   au....?’ akawa kama anauliza

‘Ni nani kasema kuwa ndugu yangu  alikuja hapa kuomba....’akasema mzee akionyesha kukasirishwa na kauli hiyo

‘Wewe si umesema kakonda kwa maisha magumu,....si umesema wewe mwenyewe...’akasema mlinzi

‘Nimekuambia alikuja kuomba...’akasema kaka mtu

‘Sasa tunabishana bure , mimi nimesema ndugi yako anaonekana anaumwa, wewe umekataa, ukasema kakonda kwa nakama za maisha,...sasa sikiliza ....hayo nakumegea tu, ila mengi utaambiwa ukifika huko...unanielewa mzee,....yeye alifika hapa, akawa anaulizia wenyeji, tukampeleka ndani, yaliyotokea huko sisi hatujui....sasa kama na wewe umekuja na nakama za maisha, hapa sio sehemu ya kutoa misaada....’akasema mlinzi kwa dharau

‘Sijakuelewa una maana gani...’akasema mzee

‘Umenielewa sana, ila unatafuta sabau kama ndugi yako...’akasema

‘Sasa sikiliza mimi siwezi kuondoka hapa, mpaka niwaone hao waliokuwepo wakati ndugu yangu anapoteza fahamu, yule kupoteza kwake fahamu ni lazima kuwe na jambo,, ...huenda waligombana, akasukumwa, au kuna kitu kilimfanya apate mshituko,...ndio nataka kulifahamu hilo, na wewe umesema hujui, ..’akasema

‘Mzee tuelewane....’akasema

‘Kwanza umeanza na kashifa zako naomba zikome..umenielewa wewe mlinzi.’akasema akinyosha kidole.

‘Sio kashfa mzee, umesema mwenyewe, shidaa ndio imemfanya akonde kihivyo, sasa kama ni shida ndio uivalie kibwebwe, kugonga majumba ya watu, tuambizane ukweli au,nimekosea kukuambia ukweli ...ukweli unauma sio....’akasema akitabasamu kwa dharau

‘Ukweli gani huo,...?’ akauliza mzee sasa akionyesha kukasirika kiukweli

‘Yaishe mzee....ile ujumbe umefika ....’akasema mlinzi

‘Unajua wewe sasa umevuka mpaka, nimekuvumilia sana,....sasa nilitoka kuondoka, sasa siondoki, mpaka nionane na hao mabosi zako,,..’akasema

‘Kama wataka kupoteza muda  wako kusubiria haya endelea, lakini usisimame hapo..nenda 
kulee...ila hapa hakuna sehemu ya kutoa misaada...’akasema mlinzi

‘Umenichefua kabisa, hata hivyo siwezi kurudi kijijini bila kuwa na taarifa kamili, nitawaambiaje ndugu na jamaa, na pili wewe mtu wewe..ni lazima niwaambie mabosi wako jinsi gani usivyo na adabu, kuzarau watu, hivi wewe unajiona umefika sana kwa kazi hii ya ulinzi, kuwalinda wenzako wakiwa wamelala...unajiona una kazi eeh..’akasema kama anauliza

‘Sikiliza mzee,..wewe kwanza nenda hospitali, unasikia mzee, huko utapata taarifa, kama zitakuwa sio kamilifu hapo sasa ukija,..utaweza kuwauliza wenyewe, au ndio kama unataka kushitaki utafanya hivyo, kama wanaweza kuongea na wewe, au kuwasaidia shida zenu......’akasema mlinzi akitikisa kichwa kwa kujiamini na dharau

Kaka mtu akafikiria halafu, akageuka kama kuondoka, akawa kama kakumbuka jambo, akauliza

‘Kwanza hivi watu gani wanaoishi humu wafrika au wazungu?’ akauliza akiwa karudi eneo lile ambalo mlinzi hataki huyo mzee asimame

‘Mzee, mbona unarudi nyuma tena...nimeshakuambia, nenda hospitalini, hawa wenye nyumba wawe wazungu au waafrika hawatoi misaada, ....wewe unachotaka ni nini....ndugu yako au wenye nyumba, hata wakiwa wazungu wanakuhusu nini?’ akauliza huyu mlinzi akiwa anachezea rungu lake

‘Nina hitaji niongee nao,si nimeshakuambia, ....’akasema

‘Hapo mzee sasa unataka mengine...mzee, sisi kama walinzi tumetimiza wajibu wetu,zaidi ya hapo, hatuna la kusema..ondoka eneo hili....’akasema huyu mlinzi akionyesha rungu kama onyo

‘Hivi wewe unafahamu historia ya hii nyumba ...?’ akauliza akipuuza lile onyo, akawa anaichunguza hiyo nyumba

‘Hilo halituhusu...’akasema

‘Inaweza kuwa ndio sababu ya huyo ndugu yangu kupoteza fahamu,.....nahisi kuna jambo lilitokea,... na kutokana na hilo itabidi niende nikatoe taarifa polisi wafanye uchunguzi..’akasema akiendelea kuchunguza

‘Sasa hayo ni juu yako mzee, kama alichofanyiwa ndugu yako shukurani zake ndio hizo, endelea ..ila nikupe angalizo, kuwa hawa sio watu wa kuogopa polisi, hawa ni wazungu, wanajua sheria, ni wasomi, ..wanajua wanachokifanya...’akasema mlinzi

‘Kumbe ni wazungu.....’akasema kwa kushangaa

‘Ndio....’akasema mlinzi

‘Hata kama ni wazungu, wasomi, lakini hawawezi kutumia ujanja ujanja wa elimu yao,kudhulumu wengine,  ...waje nchini kwetu wachukue jasho la mtu kirahisi tu....hili tatizo lazima lifike kwenye vyombo vya sheria, kama kweli serikali inawanajali raia zake, itafanya jambo, maana huu sasa ni ukoloni....’akasema sasa akigeuka kutaka kuondoka

Yule mlinzi akiwa kasimama katikati ya mlango, akasita kuingia ndani, akageuka kumuangalia huyo mzee, akaingiwa na shauku fulani, akatoka pale mlangoni na kurudishia ule mlango vizuri,

Akatembea kuelekea pale aliokuwa yule mzee, ambaye alikuwa kasimama, lakini akionyesha dalili za kuondoka,...., akamsogelea huyo mzee, na mzee alipogundua huyo mlinzi yupo nyuma yake akageuka akionyesha wasiwasi, alihisi labda huyo mlinzi kaamua kumjia kwa shari, akiwa kakunja uso akamuangalia huyo mlinzi

‘Samahani kidogo mzee, unajua tena unaweza ukasikia jambo, ukaona ni muhimu kulifuatilia...’akasema na mzee akabakia kimia

‘Hebu mzee niambie kuna nini kinachoendelea maana huyo unayesema ni ndugu yako wakati alipofika aliongelea kuhusu hii nyumba, lakini sikumuelewa,....unajua tena kazi zetu, wanakuja watu wengi, inakuwa wakati mwingine ni usumbufu....’akasema na mzee akabakia kimia

‘Sasa naona ajabu hata wewe umeongelea kuhusu hii nyumba, kwani. mzee..hii nyumba ilikuwaje,....unafahamu nini kuhusu hii nyumba?’ akauliza huyo mlinzi

‘Wewe si umesema hayakuhusu kwanini unaulizia mambo yasiyokuhusu...?’ sasa mzee akasema hivyo, akiwa kamuangalia huyo mlinzi

‘Aaah, mzee, mimi nataka kujua tu, maana nimedadisi watu wanajua eneo hili, wanasema kweli nyumba hii ilijengwa awali na mtu mwingine, nani sijui,...lakini wengine wanasema huyo mtu wa awali, alisafiri kwenda kutafuta maisha ulaya,  ...nasikia amekufa kwa huu ugonjwa wa kisasa...’akasema akicheka kwa dharau.

‘Nashangaa nyie mnakuja na ndoto za ajabu nyumba nyumba, mwenyewe ni marehemu tena kafa kwa ...huu ugonjwa...lakini baada ya kuuza hili eneo na nyumba,...pesa nahisi alizitumia kujibia lakini haikuwezekana....mungu kampenda, huo ndio ukweli...’akasema akishusha sauti

‘Ondoa uchuro wako hapa...ni nani kakudanganya hilo..’akasema kaka mtu kwa hasira na huyo mlinzi akawa kama kashtuka kusikia kauli hiyo kutoka kwa huyo mzee

‘Nimesikia hivyo, na ni taarifa za ukweli mzee, kama mlikuja kutapeli, hiyo mtaumbuka..., kwani aliyeniambia, ni mtu wa uhakika, ...watu wa usalama wa taifa,...hawawezi kudanganya, mimi namfahamu jamaa yangu anayemfahamu huyo jamaa.. sasa nyie jidanganyeni na utapeli wenu, mtaenda kunyea debe, na uzee huo,....’akasema akionyesha kuzarau

‘Unasikia, huyo aliyekuambia na wewe nyote hamna akili,...’akasema huyo mzee na mlinzi akacheka na kusema

‘Hahaha, mzee, mimi nakusadia, ...unaniambia mimi sina akili,...nyie watu wa ajabu kweli, mataka kutaeli hata visivyotapelika, hivi mnajiamini vipi.....’akasema kama anauliza

‘Unajua kwa kauli yenu hiyo, ni vyema kweli niende polisi, ili ukweli ujulikane, ,...na kama ningeonana na hao wanaishi humu, ningelijua ni nini kinachoendelea,watu wanavuisha uwongo, na wewe chunga mdomo wako.....’akasema mzee akimkazia mlinzi macho

‘Hawa watu wanarudi saa ngapi...?’ akauliza

‘Mzee, hawa watu wamekwenda kazini, huwezi kuonana nao kwa hivi sasa....mimi nimekusaidia kwa hilo, sasa kama unataka kujiabisha haya endelea...’akasema

‘Watarudi tu, mimi nitaonana nao, nataka nisikie ukweli kutoka kwao, huenda hata hawajui lolote, wameuziwa tu,.....’akasema mzee

‘Mzee kabla, hapa kulikuwa na kibada kibovu tu, halafu hawa wakaja kununua eneo kukiwemo hicho kibanda kibovu...wakakibomoa hicho kibanda, ndio wakajenga hili hekalu, ..’akasema huyo mlinzi .

‘Kibanda kibovu!, wewe waulize waliokuwepo hapa kabla, watakuambia ukweli kama kweli kilikuwa kibanda kibovu....wewe wa kuja tu, hujui lolote...’akasema mzee

‘Sasa mzee, huo ndio ukweli,...najua kwa utapeli wenu utasema sasa hata huyo jamaa aliyekuwa na hicho kibanda ni ndugu yenu, ...hahaha, nyie watu bwana, huyo alikufa kwa ngoma, yeye, alifika uzunguni badala ya kusoma akakalia uhuni, hahaha, unajua wengi wakifika ulaya wanachofanya ni umalaya...’akatulia na mzee akawa katulia akimuangalia huyo mlinzi.

‘Halafu mzee nikuulize kitu, maana huyo aliyekuja hapa na kudondoka, ana matatizo gani, au na yeye ndio ugonjwa nini...anavyoonekana eeh, mmmh, yule naye anao tu, lakini kwanini hajaenda ushauri nasaha , inasaidia, wanaumwa siku hizi wanakuwa a hali nzuri tu, wakifuata ushauri, ...’akasema na mzee akawa kimia tu

‘Halafu mtu anaumwa, anataka kutapeli nyumba,..hivi anataka afe na nyumba, badala ya kutulia, anakuja kudai nyumba yake, hahaha, wizi mwingine bwana, ....mzee,. wewe rudi kijijni ukafuge,....mnafikiri mtaonewa huruma mahakamani, ....acheni tabia hiyo mbaya.....’akasema

‘Unajua wewe mlinzi nimekuchoka kwa dharau zako,...mimi siogopi kuwa wewe ni mlinzi, ..mlinzi gani hata silaha huna...mimi nimepitia mgambo, nimepambana na simba...’akasema sasa akionyesha kukasirika

‘Mzee, sina lengo la shari, nilitaka kukushauri...maana mnatutia aibu, siku hizi hapa jijini kumejaa watu matapeli, watu wanauza nyumba za watu wenyewe wakiwa ndani, pia watu wanaumwa wanataka visababu tu, njaa hii itatuponza kweli...’akasema

‘Kwahiyo mimi ni tapeli,...unaendelea kunitusi,....umesema ndugu yangu ana ngoma,....tuna shida.., wewe askari  uchwara nahisi wewe hunitambui nilivyo eeh....’akasema mzee na huyo mlinzi akaona isije kuwa shari akageuka kutaka kundoka, na hapo akawa kalikoroga, akasikia bega likishikwa, na wakati anageuka, akakutana na ngumi nzito, iliyompeleka aridhini.

‘Hiii itakufundisha adabu.....’akasema mzee
Mlinzi hakutarajia hilo kabisa, alijikuta yupo chini, na kichwa kikawa kimegonga kwenye mawe yaliyokuwa yamepangwa hapo...

‘Aaaah, wewe mzee....’akasema huyo mlinzi akishika kichwa...

Na kabla hajaamuka kupambana na mzee  mara magari mawili yaliyokuwa yameongozana yakawa yanakuja, ilionekana kuwa ndio mabosi wa hiyo nyumba, maana mlinzi badata ya kupambana na mzee, akakimbilia ndani, kwenda kufungua geti, na mzee akawa anatetemeka kwa hasira,..

‘Na bado ngoja nionane na hawa watu.....’mzee akasema akiangalia hayo magari yakiwa yamesimama getini, kutaka kuingia, yeye kwa haraka akalifuata lile gari la mbele akasogelea kwenye kiyoo na kugonga maana huwezi kuona ndani....

***********

Mlinzi ambaye kwa muda huo alishafika kwa ndani akiwa kashikilia kichwa kikivuja damu, huku mkono mmoja ukifungua mlango ili magari yapite, moyoni akiwa kajawa na hasira,...alisukuma mlango, na alitaka afanye hiyo kazi haraka atoke nje akapambane na huyo mzee,...

‘Huyu mzee nitamuonyeaha kuwa mimi ni nani, ngoja...aaah, damu....kichwa, hata ...’akawa analalamika

Lakini jao mlango wa geti ulikuwa wazi, alishangaa kuona hayo magari hayapiti,....hakutaka bosi wake amuone alivyoumia, kwani maswali yatakuwa mengi, lakini kwa hali hiyo alitakiwa kutimiza wajibu wake kuona kwanini magar hayaingii,
Ikaabidi asogea kuangalia kuna tatizo gani, ...akamuona yule mzee kasimama pembeni ya gari,.....akigonga dirisha la gari!

‘Huyu mzee sasa , ngoja nimuonyeshe kuwa mimi nipo kazini...hawezi kunifanya hivi....’akasema, sasa akitoka kwenda kupambana na mzee, akiwa tayari na kirungu juu, akimuendea mzee nia amgonge hicho kirungu huyo mzee kichwani, atoke damu kama alivyotokwa yeye

Lakini alichelewa,...

Mlango wa gari ukafunguliwa, na aliyetoka ni bosi wake mwenye nyumba akiwa kaiva kwa hasira......Bosi wake aligeuka kumuangalia mlinzi akitaka kuanza kumlaumu kwanini anamruhusu huyo mzee kuzuia gari, akamuangalia mzee, halafu akamgeukia mlinzi,

'Kwanini ..' lakini alichokiona kilimfanya abakia mdomo wazi....

Tuishie hapa kwa leo....

WAZO LA LEO: Kauli za kuongea na watu zinaweza kutafsiriwa vibaya kutokana na jinsi mtoaji ulivyozitamka, kuna watu wengine kauli zao ni za kejeli , kuzarau, hata pasipostahiki. Wengine hufanya hivyo kwa vile ni mabosi, matajiri, au watoto wa watu, au hata mfanyakazi tu...

Tujifunze jinsi gani ya kuongea na wenzetu, kutegemeana na mtu au mazingira, ili kukwepa uhasama au sintofahamu zisizo na msingi, kauli nzuri yaweza kujenga mvuto wa heri, na kuleta maelewano mazuri tu, lakini kauli mbaya zenye zarau, zaweza kuvuruga amani na hata kujenga chuki...tukumbuke, hekima ni bora sana kuliko hata mali.
Ni mimi: emu-three

No comments :