Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, September 21, 2015

RADHI YA WAZAZI-43



Bro, ndugu yako nilikuwa marehemu, yaani pale mpaka unachukuliwa kupelekwa hospitali ya nje ujue wewe ni wa kufa, au huo ugonjwa wako ni mkubwa sana, ujue unapopelekwa kwenye hilo gereza , ni kwamba umepelekwa hapo ili ukafe, hawasemi hivyo, ila inajulikana hivyo!

Kwahiyo ukiumwa hawakuhangaikiii sana, sana sana watakupiga sindani za kuwasha uhangaike mpaka huo ugonjwa ukimbie,, la sivyo, utapoteza fahamu, ikiamuaka upo hapo hapo..!

‘Sasa ikawaje kwako mpaka wewe ukapelekwa hospitalini ya nje..?’ akauliza kaka mtu

‘Siku zangu zilikuwa hazijafika bro, kwani hali ilikuwa mbaya, mimi mwenyewe nilimuona malaika mtoa roho akinijia,...nilishaiaga dunia, naona ilipangwa nisife hara ili nipate muda wa kutubu dhambi zangu...’akasema

‘Sasa umetubu hizo dhambi zako, wewe uwadhulumu watu haki yao, uwasumbue, uwabie mpaka kufikia watu kufa, halafu useme utatubu, unaweza kutubu kweli dhambi ya mtu, uliyemdhulumu, kama hujaweza kumrejeshea haki yake,...au unajidanganya tu?’ akaulizwa

‘Ohh, bro...nimetubu sana, na kama ni adhabu hiyo niliyoipata imelipia hizo dhambi,sijawahi kumfanyia mtu ubaya kiasi hicho,..kama nimeweza kuwalipa watu madeni yao,...mimi naona nimeimiza hayo, japokuwa sikuwa na jinsi, ...

'Bro kama nyumba imeuzwa , wakasema wanalipia madeni ya hao watu, sasa kama hawakulipia hayo madeni wakajali matumbo yao, hilo sasa, ni juu yao, mungu anajua ..’akasema

‘Ina maana kweli nyumba imekwenda, lile jumba la kisasa limeuzwa...iliuzwa na pesa wakachukua,..kweli wewe huna maana, unaona ilivyo, ubinafsi wenu umewaponza mungetushirikisha tukajua jinsi ya kuwasaidia, japo hatuna pesa....'akasema kaka mtu

'Lakini mbona sielewi, wao wapo ulaya na nyumba ipo huku,waliwezaje kuyafanya hayo?’ akaulizwa

 ‘Nyumba Imekwenda bro, imeniuma kweli,...., vinginevyo wangenitafuna nyama yangu...na hilo kwao ni rahisi unajua kuna madalali wa kimataifa, wanawasaliana, na kwa vile hilo liliwekwa kisheria zaidi, halikuwa na matatizo....’akasema

‘Lakini hata kama imeuzwa, wewe kama wewe ilikusaidia nini,  maana hukutolewa hapo kwenye gereza la kifo, au...., au ilikuwaje....na hivi kijana wetu ilikuwaje, maana sioni ukimtaja taja tena...?’akauliza kaka mtu.

‘Ngoja nikusimulia ilivyokuwa....’akasema

Tuendelee na kisa chetu...

*********
 Siku ya kesi nyingine ilipotajwa mimi nilichukuliwa nikitokea hospitalini,..kama nilivyosema kuwa hali yangu ilikuwa mbaya sana, nilichukuliwa nikiwa sijitambui,walikuwa wamebeba kama maiti,na kilichofanya wafanye hivyo labda, nikuwa mimi sikustahili kufungwa hapo baada ya kubainika kuwa mimi sijau...sasa sijui walipangaje kuwa nikipona nitarudi hukoo au la...

Niliombea nisipone haraka...na hata hivyo kwa hali niliyokuwa nayo haikuwa ya kupona haraka...ila mfungwa ni mfungwa tu,....

Na siku ya kesi, nilipoambiwa nahitajika kwenda mahakamani, nilijilegeza kweli, lakini ilikuwa haisaidii kitu, kwani ilibidi nifike mahakamani, labda kesi iahirishwe tena, kitu ambacho sikupenda kifanyike kwani ilishaahirishwa mara nyingi..

Nilivyokuwa nimejilegeza nilijuwa kuwa huenda hakimu atanionea huruma kwa hali niliyokuwa nayo, hata bila kujilegeza, bado nilikuwa na hali mbaya, niilisha nilikonda, hadi sura ikawa kama sio yangu na kila mmoja aliyeniona akajua huyu anao...

Hutaamini watu waliponiona baada ya huruma wakasema na bado wewe ulijifanya mjanja, kuwabughudhi watu na maisha yao,...umeua.....kwani mama mtemi alikuwa kaongoza kupakazia ubaya kwa kile mtu, propaganda potofu dhidi yangu zilishawafikia watu wegu...

********

Siku nipo hospitalini, nikaambiwa wakili wangu amekuja anataka kuonana na mimi, nilishangaa kusikia hivyo maana muda sasa nimekuwa sionani na huyu mtu kama ilivyokuwa awali, kama kawaida ya wakili na mteja wake...nimekuwa nikionana naye ikitajwa siku ya kusikiliza kesi yetu na tunakutana mahakamani tu.

Kuna siku ilipotajwa kesi na kupigwa kalenda nilitaka kuongea naye, lakini wakili huyo akasema ana haraka, hawezi kuongea nami, ..na ikiwahivyo, kesi inatajwa, na waendesha mashitaka wanatoa udhuru fulani, kesi inaahirishwa.

 Wakili huyo alijitahidi kulalamika kwa kusema kuwa waendesha mashitaka wanapoteza muda,hawana ushahidi zaidi juu ya mteja wake anateseka kifungoni bila kujulikana kosa lake pia anaumwa, lakini kesi inaahirishwa na kusogezwa mbele...

 Ndio siku hiyo nikiwa hospitalini chini ya ulinzi nikaambiwa wakili anataka kuongea na mimi, na ningesema nini hapo, nikatulia tu,na wakili akaja akanisalimia, sikumuitikia, alipoona hiyo hali, yeye akasema;

‘Najua jinsi gani unavyojisikia,lakini mimi nimejaribu kadri ya uwezo wangu lakini waendesha mashitaka ndio wamekuwa ni kikwazo,na nisingeliweza kumlazimisha hakimu...lakini leo nimekuja na suluhisho ...’akaanza kusema na kuniangalia kama nitasema lolote, lakini sikusemakitu nilikaa kimia.

Wakili akaendelea kutabasamu akiniangalia akitaka na mimi nifanye hivyo, lakini sikutaka hata kumuangalia, ni wakili wangu lakini nilishamchukia nilishamuona wote lengo lao ni moja, ...akatikisa kichwa kama kukubali, kwa niaba yangu, akasema;

‘Ni kutokana na hii hali yako imebidi nimuendee hakimu mwenyewe niongee naye kuwa unateseka bila sababu yoyote, haikuwa kazi rahisi hasa kesi inapokuwa mahakamani, wengi hawakubali kuongea na mawakili au washitakiwa kwani itaonekana kama kuna kiti kinachoendelea,...’akatulia

‘Nilitumia njia ya kisheria, niliandika mombi ambayo nakala ilipitia kwa wakili muendesha mashitaka, na hapo hakimu akaona kuna jambo muhimu, na hakuwa na kipingamizi tena, ukumbuke tangia hapo nilishalalamika, na hakimu akawaita waendesha mashitaka wakaongea,na  aliwakemea na kuwaambia kesi ikitajwa tena hakuna kuahirishwa ...’akatulia

‘Pamoja na kumuona ,nilikuwa nimejiandaa kwa mapendekezo muhimu sana...ya kuweza kukusaidia,na nilijua hayoyatakubaliwa tu....’akatulia

‘Sikutaka kukimbilia swala la wewekubadilishwa gereza, maana hilo nililipigania mpaka nikakata tamaa,na nilivyosikia walifanya hivyo wakubwa wa huko kwa vile uliwadanganya,...’akatulia, akitarajia kuwa hapo nitaongea kitu, lakini nilikuwa vile vile kama mtu aliyepooza viungo.

‘Kiukweli mapendekezo ambayo tulikuja kuyaona mimi na mama mtemi, na kijana wako ambayo ndiyo niliyapeleka mbele ya hakimu, niliona yana msingi ,kwa ajili ya kukusaidia wewe, kwani tumeona kwa hali uliyo nayo  ukirudishwa huko gerezani utaenda kufa tu kwahiyo tukaona tuyapeleke mapendekezo hayo,na  mimi japo sikuwa nimeongea na wewe ikabidi niyawakilishe tu kwa niaba yako..’akasema

‘Nimeyapitisha kwa niaba yako kwasababu ya hali yako ya kiafya ...’akasema akitoa makaratasi kwenye makabrasha yake,...mimi nilikuwa nimejiegemeza ukutani kwenye kitanda,nikiwa sina hamu tena ya maisha...’akasema

‘Sijui wewe unasemaje...’akasema sasa akiwa ameshayatoa hayo makaratasi yanayoelezea hayo mapendekezo waliyopeleka kwa hakimu, akawa ananionyesha ili niyasome, lakini sikugeuka wala kujigeuza nilikaa vile vile, na alipoona hivyo, akayafungua mweyewe na akawa kama ananisomea...

‘Ni hivi kesi ya mauaji dhidi yako haipo, japo ni lazima hilo lipitishwe mahakamani...’akatulia

‘Kuonolewa kwa kesi hii ni wao waendesha mashitaka baada ya kuwabana kwa ushahidi ikabidi sasa wakiondoe hicho kipengele cha kuwa wewe ni mshukiwa wa mauajii namba moja...’akatulia

‘Kukabakia hoja ya kuwa wewe ni msababishi, na mshirika wa kulitenda hilo kosa, kama ulivyoona mahakamani hili nililipigania hadi kipengele hicho kikawa hakina nguvu, lakini bado, hakijatolewa na waendesha mashitaka, ...’akatulia

‘Lakini kesi ikitajwa tena nina ushahidi wa kuweza kuwashinda, hoja hiyo kifupi haina nguvu, kwani huwezi kuwa ni sababu,...kama ni msababishaji ni huyo aliyebuni hiyo kazi...lakini siwezi kusema hivyo, nina ushahidi mwingine nitautoa mahakamani, ...’akatulia

‘Waendesha mashitaka baada ya kuoana sasa wataumbuka, kwani wamemkatama mtu asiyestahiki, waakaanza kuhangaika kumtafuta muuaji halisii ni nani...hapo wakajikuta kwenye mtego zaidi, maana walikuja kumpata mtu ambaye ilikuwa vigumu kwao kuamini...’akatulia

‘Sasa hilo likawa ni mtego kwao, kama wanakushinikiza wewe kwa alama za vidole, kama wanakushinikiza wewe kwa kuonekana kwenye kanda za video, basin a wao wamkamate mtu wao....’’akasema nilitamani kumuuliza ni nai huy mtu wao, lakini sikutaka kuongea kabisa

‘Basi kwako ikawa ni mwiba, na yawezekana mtu wao ndiye muuaji, nitahakikisha haki inatendeka, wao wanajifanya watawala bora sasa nataka niuone huo utawala wao bora ni upi, lakini kwa sasa siwezi kushinikiza,...’akasema

‘Ushahidi upo, japo walificha, alama za vidole zimeoenaka pia kwenye bastola, walificha hilo mwanzoni sasa imebidi waliweke wazi, japokuwa bado ni siri kutokana na makubaliano ili ombi letu lipite...’akatulia

‘Mshukuru sana mama mtemi, kwani mama mtemi alipolipata hilo,..maana hutaamini ilikuwa ni siri, lakini ikafika hadi kwa mama mtemi, sijui ilifikaje,....wao wakafikiria kuwa labda ni mimi nimemwambia, lakini sio mimi, mama mtemi alilipata hilo kwa kutumia mitandao yake, unamfahamu tena yule mama ...  na alipolipata tu, akawaendea...'akatlia akitabasamu

'Yeye alikwenda moja kwa moja kwa mkuu wa kituo mwenyewe...alifanya makosa kutokuniona mimi kwanza nikamshauri njia sahihi, lakini hata hivyo ilisaidia...’akasema sasa akiwa kakunja uso kama anawaza jambo.

‘Baadaye, alipomalizana kuongea na mama mtemi, wanajua wenyewe walichoongea,  mkuu huyo akawaita watendaji wake, akiwa kahamaki kweli...

''Ni nani kalifikisha hilo jambo kwa mama mtemi..'' akauliza na watendaji wake, wakabakia kushangaa,kwani hata wao hawakujua ni nani kafanya hivyo....mkuu akawa anahaha huku na kule, wakawa hawana jinsi...’akatulia.

  Wakati wakili huyo akiongea kichwani kwa profesa alikuwa akiwaza...huyu Mkuu, huyu mkuu ana husikanaje na hayo mauaji..profesa akawa anawaza bila kupata majibu,akilini akahisi kuna kitu mkuu kinamgusa kwenye hiyo kesi, ni kitu gani, akashindwa kukitambua, na hakutaka kuuliza, hakutaka kuongea kabisa siku hiyo...

‘Hapo, kikao cha dharura kikaitishwa mkuu akawaita muendesha mashitaka, na mpelelezi,  wakatafuta njia ya kufanya na ili wafanikiwe ni lazima wakubaliane na mimi kuwa hilo shitaka dhidi yako, la muaji ni lazima liondolwe dhidi yako...’akatulia

‘Unajua...eeh, katika maisha haya ya sheria, hasa ukipewa dhamana, ukijaribu tu kupindisha sheria kumsaidia mtu wako, ukumbuke kuwa kuna mtu mwingine ana kosa kama hilo hilo, ...’akatulia

''Sasa hapo... ili na wao wasiwe hatiani..kwahiyo hicho kipengele cha kusababisha mauaji kikawa hakina nguvu,ilikuwa imebakia umauzi wa hakimu tu...na wakikileta mahakamani, wataumbuka.’akasema

‘Najua hawatafanya hivyo...’akasema

‘Sasa ikabakia kosa la biashara ya mlungula, nimejitahidi kila mbinu kwa uzoefu wangu, haikusaidia kitu maana sasa jamii,imekuja juu, watu wa haki za binadamu wamechachamaa, na wale wote uliowafanyia hivyo,wamekubali kutoa ushahidi...’akatulia

‘Mama mtemi yupo kote kote, na umjuavyo zaidi analalia kule kwenye masilahi yake, kwahiyo kwa vile kwako aliona kuna masilahi ilibidi akusaidie, lakini hata hivyo upande mwingine yeye ni kiongozi wa kupigania haki za wahanga wa biashara ya mlungula huko nako ana masilahi ya uongozi na kuna misaada saada wanapata....

'Kwahiyo, ilipofikia kwenye kipengele cha  biashara ya mlungula, akawa hana msaada kwako,....kwa vile ulishatatua lile swala kwa kupitia nyumba, ...na unajua mlishasigishana naye kwenye mambo hayo, kwahiyo, kwenye hicho kipengele akawa yeye ni adui yako, anashinikiza uadhibiwe vikali...’akasema.

‘Kwahiyo hapo nikawa sina ujanja,...hata hivyo sikukubali, kwani mimi ni wakili wako ni lazima nipambane, ..sikujali kuwa mama mtemi ni adui wangu kwa hilo, yeye keshajipanga kutoa ushahidi dhidi yako...mama mtemi ni kigeu geu,...huyu mama achana naye kabisa, kwake masilahi mbele....’akatulia

‘Kwa kipengele hicho, mama mtemi na wanajamii wapo kitu kimoja kuhakikisha wote wanaofanya biashara ya mlungula, wanaadhibiwa ili biashara hiyo ikome kabisa, watu hawapendi mauchafu yao yawekwe hadharani, hawapendi, hizi sheria nyingine unajua tena, ...hapo nitafanya nini, iliyobakia ikawa kusubiria hukumu tu..’akatulia

'Nakuelezea haya ili uelewe, naelezea kinamna yako wewe usiyejua sheria ufahamu ninavyokupigania, usione nakupotezea muda, .....'akasema akiangalia saa yake.

‘Nikaongea na dakitari kuona kama nitapata msaada wowote kutoka kwake, na yeye akasema yupo tayari kuthibitisha kuwa afya yako haistahiki kurejeshwa gereza hilo,...

'Lakini mambo ya magereza wewe upelekwe wapi, hayamuhusu, yeye kama yeye atathibitisha hali yako tu,  nikaona bado sijakusaidia, kutokana na kesi yenyewe, kiukweli....wewe hukustahiki kupelekwa huko.....’akatulia

‘Kwahiyo sasa ikabakia jinsi gani ya kufanya, .....nikaona nionane na hawa watu, niongee nao....nisikie kauli yao..,....unaona hapo, inabidi nikae na maadui zangu, na hapo sikumuhitajia mama mtemi tena, maana angekutosa,..hilo nililipanga peke yangu.....’akatulia

‘Usinione kuwa kimia, nilikuwa nakuhangaikia kweli ndugu yangu....'akasema akimkagua Profesa kwa macho, hakuamini kuwa huyu mtu yupo sawa, lakini akaendelea kuongea

'Kiukweli kutokana na kesi yako nimehangaika sana,  maana hata marafiki, wale mashahidi wote niliowategemea sasa wakanigeuka, ndio hapo nikajua jinsi mama mtemi anavyoheshimika....ikafika sehemu hakuna ujanja, lakini mimi ni mpiganaji wa mahakamani nina uzoefu wa miaka mingi,nikikuambia hapo hakuna ujanja,kweli hakuna ujanja...’akatulia

‘Wazo la kutumia silaha ya afya yako nikaona inaweza kufaa.....japokuwa kisheria bado ingekuwa ni tatizo...’akatulia.

‘Nikawasiliana nao, kuwa naomba tuongee kuhusu hii kesi

''Tuongee nini, tutaongea mahakamani, .....'wakasema, na walikataa, kata kata, nikaona sasa hapo nifanyeje, ....unacheza na mimi, nikawatishia kuwa nitawaumbua....walijua namaanisha nini kusema hivyo,...

'Kwanini wasikubali,.. wakaja kukubali kuwa tukutane tuongee kwenye maswala ya kufanikisha eeh kesi, ...hapo walikuwa waangalifu,,,unajue tena sheria, japokuwa hawakufahamu nimekuja na ombi gani...’akatabasamu.

Profesa akilini alikuwa akijaribu kuwaza hawa watu wana kitu gani ambacho kinafunga waendesha mashitaka mpaka wakubaliane naye,  profesa aliamua kukaa kimia, profesa alihisi kuwa hicho kitu ni cha siri kati ya mawakili hao, na alishamfahamu profesa kuwa sio mtu wa kuaminika kwenye mambo yanayoitwa siri.

 ‘Wakakubali nikutane nao bila mtu mwingine yoyote...’

‘Nikawaambia,..nina ombi,....waliposikia hivyo wakaangaliana na kuniuliza ombi gani...’akatulia

‘Niliwaambia kuwa wewe unaumwa sana..na ni kweli hilo hata wao wamekiri,kwani vyeti  vya dakitari vinaonyesha,wakaniuliza sasa kuumwa kwako kuna nini, maana wewe kweli ni mkosaji hukumu ya makosa yako inajulikana japokuwa hakimi hajatamka,...

 ‘Ilibidi niongezee mengine kuwa wewe sio wa kupona,  japokuwa kuumwa sio lazima ufe,nikawaomba kuwa wewe sio raia wa nchi hii, na ukifa hapa serikali itaingia gharama kubwa za kukubeba,kwahiyo ombI langu kwao ikawa wewe urejeshwe nchini kwako....’akasema

‘Mwanzoni walipinga sana..lakini nikawakumbusha kuwa kwa hilo nipo na mama mtemi na wanamfahamua alivyo walikaa pembeni badaye wakaja kukubaliana na ombi hilo....’akasema

‘Wakasema inabidi wakaongea na hakimu kabla ya siku ya kesi, ila hawana uhakika kama anaweza kukubaliana na hilo....’akasema

‘Hapo nikawa nimeutua mzigo, maana ni wao sasa wakatafute njia za kumshawishi hakimu, mimi hapo simuizi kichwa tena, na walijua wasipofanya hivyo kuna mambo yao mengi yataibuka...’akatulia

‘Najua hakimu hatakuwa na kipingamizi kikubwa sana,kwani ushahidi wa vyeti vya dakitari upo...., na unakumbuka aliwahi kufika kukuona, ilibidi yeye  mwenyewe kufika siku kesi yako ilipoahirishwa...wewe ulikuwa huna fahamu,....’akasema,na mimi nilishangaa kwani sikumbuki kumuona huyo hakimu

‘Hakimu alikuja ukiwa una hali mbaya, alikuona na aliondoka  akisubiria kusikia umeshafariki, alishangaa kusikia wewe bado upo hai, ...kweli wewe una roho ya paka....’akasema kiutani,na moyoni nikasema kumbe hawa watu walijua nitakufa ili mambo yao yafanikiwe.

Moyoni nilipanga nikitoka, nikiwa na afya nitapigania haki yangu, hasa nyumba yangu, lakini nikajiuliza ya nini ,na mimi ni mtu wa kufa tu, kama dakitari keshathibitisha kuwa maradhi niliyo nayo ni swala la muda tu, anachofanya ni kunipa dawa za kurefusha maisha tu ,..imebakia nini....lakini cha ajabu waliona bado ninadunda tu...’akasema akijiangalia.

Basi,wakili akaendelea kusema;

‘Kwahiyo ombi la kuwa wewe urejeshwe nyumbani kwenu, nikaona lina nguvu nikaenda kuongea na mama mtemi, sasa nikijiamini, yeye alilifikiria sana na akaja kukubali akaongea na kijana wako,....kijana wako hata yeye akaoa ni bora maana atakuja kusumbuka ukifa , yeye ataonekana ni mtu wa karibu kwako kwahiyo msiba utakuwa ni wake.

‘Kwahiyo nimewaachia wao hiyo kazi ya kukutana na hakimu kabla kesi haijatajwa tena,...’akatulia

‘Sasa nakusikiliza wewe unasemaje..’akasema

 Mimi sikuwa na la kuongea, kiukweli moyoni nililkuwa kama nimekufa, sikuwa na hamu hata ya kuongea, ..akasema;

‘Sasa kisheria inahitajika wewe uweke sahihi yako kuwa umekubaliana na hayo, kuwa yametoka moyoni mwako, upo tayari kurudi kwenu,...hapa nimetayarisha maombi hayo, unatakiwa uweke sahihi yako...’akasema akinionyesha hiyo karatasi, mimi nilimuangalia tu

‘Bila sahihi yako itakuwa haina uzito, ..na inatakiwa ionekane uliomba siku nyuma kabla...ndio maana tarehe imeandikwa ya nyuma....’akasema, na mara akahisi mabadiliko kwa profesa alianza kama kutingishwa hivi.....alipoona hivyo

Akaiweka peni karibu ya mkono wa profesa akitaka kumsaidia,  lakini profesa alikuwa akitikiswa, ...akatulia kidogo, halafu akaanza tena, hapo wakili akaona hali sio shwari, akatoa, kidau cha rangi, akaweka kwenye kidole cha profesa halafu kwa kushinikiza akaweza kuweka alama ya kidole kwenye hizo karatasi, ....

'Hii inafaa, lakini ingelitakiwa sahihi yako,...ooh, profesa upo sawa kweli, ' akasema huku akimkagua Profesa, kwani ilionekana kabisa hayupo sawa, wakili alipoona hivyo akasema;

‘Sasa mimi natoka kidogo, naona hali yako haipo shwari, dakitari kaniambia, hali hiyo inatokea inakuja na kuondoka, nikiiona nisiogope, ila hapana, hapa imezidi inabidi nikamuite tu, huyo dakitari aje tuone atakusaidia vipi, sahihi yako ni muhimu sana, isipoatikana wanaweza kuweka pingamizi wale watu...’akasema na haraka akaondoka.

Profesa akiwa peke yake, kiukweli hali ilikuwa sio shwari, alionekana kweli anaumwa, na ni moyoni kweli alihitajia kuondoka kurudi kwao, akawa anatamani akafie kwao....akaona ajitahidi tu,akainua mkono na kuchukua ile peni kutaka kuweka sahihi yake lakini mkono ukawa mnzito, akawaka anatikiswa mwili mnzima, akajitahidi na hata kalamu ilipofika kwenye karatasi, akajikuta akikoroga tu...

Profesa hali ikawa ni mbaya, akawa hajiwezi kweli, wakati huo wakili ameshaondoka, kumuita dakitari, akahisi pumzi ikiwa nzito, nguvu zilikuwa zimemuishia kabisa, jasho likawa linamtoka, akawa anatikiswa kweli kweli, na haikuchukua muda akapoteza fahamu...


WAZO LA LEO: Sheria hukata mbele na nyuma, huwezi ukafumba macho ukiona jambo limetokea sehemu inayokugusa..  ukijaribu tu kupindisha sheria kumsaidia mtu wako, ukumbuke kuwa kuna mtu mwingine ana kosa kama hilo hilo naye utasemaje! Kwahiyo ewe mtendaji mwenye dhamana, ewe kiongozi,... timiza wajibu wako kwa kusimamia haki na uadilifu...
Ni mimi: emu-three

No comments :