Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, September 4, 2015

RADHI YA WAZAZI-38



Bro...Kesi iliendelea kama ulivyoona, kiukweli wakili mtetezi alijitahidi sana kunitetea lakini ilipofika siku ile, ambapo ndio alitakiwa na yeye sasa atoe ushahdii wake na mashahidi, ili ionekane, kuwa mimi sijaua, wakili akaniambia yeye anataka kujitoa,kisa ni nini, ni kwa vile hajalipwa pesa yake kutokana na makubaliano.

‘Kwani mlikubaliana nini,mtalipana vipi..?’ akauliza kaka mtu.

‘Wakili huyo kwa kiasi kikubwa aliongea na mama mtemi, na mimi nilikuja kukubali tu,  kuwa nipo tayari anisimamie, undani wa makubaliano sikuweza kuusoma,nililitewa huomkataba nikaweka saini yangu, nikakubali yote yaliyyokuwa yameandikwa humo...’akasema

‘Bila kusoma....wewe si msomi, yaani ukubali kitu, hukijui undani wake,unanishangaza kweli,haya ....sasa ikawaje...?’ akauliza kakamtu

‘Bro, siku hiyo nilikuwa nimechanganyikiwa, kesi ya kuua,...upo rumande, bado unaambiwa unapelekwa magereza mabaya,.....nilijikuta nakubali tu, nikafungua fungua yale makaratasi nikaweka sahihi yangu,....basi, ..’akasema

‘Hata hujui utamlipaje....na hapo napo ulitaka kufanya ujanja au...na huyo wakili sio wa bei mbaya, au ni hao wa mitaani tu?’

‘Ni wakili kweli,...na wengi walijua wakili huyo atakuwa kalipwa mapesa mengi sana, maana kazi anayoifanya sio mchezo....’akasema

‘Sasa alilipwa kiasi gani na kwa ujumla alitakiwa  kulipwa shilling ngapi?’ akaulizwa

‘Bro,...,hata sijui mama mtemi aliongea naye nini mpaka akakubali, huyo wakili sio mchezo, ...moyoni nikawa na mashaka kuwa huenda mama mtemi alishazipata hizo pesa,....’akasema

‘Kwani hizo pesa zilipotoeaje, hujatueleza siku ile ilikuwaje....?’ akaulizwa

‘Mhh, hata sijui hizo pesa zilikwenda kwa nani, ...nilisjua kabisa huyo mama mpaka anamtafuta huyo wakili atakuwa keshazipata hizo pesa, lakini cha ajabu nilipokutana naye tena akaniulizia tena kuhusu hizo pesa, na alizidi kunisisitizia kuwa anahitajia hizo pesa,ili aweze kuwalipa watu mbali mbali...’akasema.

‘Sasa....unajua sikuelewi, haya hebu endelea kutusimulia,ukatoka siku hiyo hapo mahakamani, ulirudishwa gerezani, ni gereza lipi hilo, au ulirudiswa kule rumande, sijui..’akasema kaka mtu

Nilirudishwa gerezani, kule nilitolewa, nikafanyiwa mpango kupelekwa kwenye gereza lenye unafuu, lakini huo unafuu sikuuona,....’akasema

‘Lakini siulishawahi kufungwa kabla, kwahiyo unafahamu mazingira ya jela yalivyo au...?’ akaulizwa

‘Niliwahi kufugwa, lakini kipindi kile sikuwa na maadui kiaisi hicho,..safari hii, nilikutana na watemi, maadui zangu, niliwahi kuwafanyia ubaya, na kwa ujanja, nikawashinda, wakafungwa,....walifungwa kwa makosa yao, lakini mimi pia niliwahi kutoa ushahidi kuwa ni wakosaji,....’akasema

‘Gereza hilo nililopelekwa, wanasema lina unafuu, lakini niliyoyakuta humo bro, ni mateso,humo ndani nilikuta pia kuna ubaguzi,...kuna ubaguzi wa rangi, watu weusi walibagulizwa,na kunyanyasika kweli...na pia kulikuwa na makundi ya ubabe ubabe tu....kuna utemi wa hapa na pale...

‘Humo ndani kulikuwa na watu walishajiona wamefika,..wanatumia miili yao,ubabe wao miguvu yao kuwanyanyasa wanyonge kama mimi, kama unavyoniona mwili wangu, mdhaifu tu, mimi ni maneno tu, lakini ikifika kwenye nguvu za misuli sina kitu....

Ndio, pale kulikuwa na sheria,..hata kuna maonyo, kuwa ukiona unateswa utoa taarifa kwa wahusika, walinzi, kuna viranja wa humo ndani,...., lakini  kweli utaweza kufanya hivyo, ..vitisho vyao hao watendaji, vilitufanya tufunge mdomo, hata ukitendewa ubaya....

Nikuambie bro, ile siku nafikishwa hapo utafikiri walifahamu kabla kuwa nitafika humo,...ile nafika tu, nikakutana na mijamaa ikaanza kunikwida na kuniambia;

‘Umekuja eeh...sasa utatulipa pesa zetu...’mmoja wa hao watu aliniambia

‘Lakini sikumbuki kama wewe unanidai, unanidai mimi,..?.’akasema profesa akiwa kakunjwa shati

‘Hukumbuki eeh,, basi tutakukumbusha...’akasema huyo jamaa,na kwenda zake, muda akaja na kundi la watemi, nikawekwa pembeni, nikapewa kibano, hadi mwili wote ukaishiwa nguvu, nilipoteza fahamu, nilipozindukana nikawa nipo chini ya walinzi.

‘keshazindukana huyo mpeleke chumba chake...’amri ikatolewa, nikapelekwa chumbani kwangu, nafika godoro limelowa maji, nasigiziwa eti mimi nimekojolea....
Nilitoa taarifa kwa utawala, na ikawa nimejichongea, siku moja wakati nataka kwenda kuoga, nikanaswa huko na wababe wawili, wakinipiga mpaka nikapoteza fahamu tena,nilipozindukana najikuta nipo chooni, uchi.....na nimetundikwa na suruali yangu kama vile nataka kujiua....mguu mmoja umekanyaga lile sinki la chooni, ilitakiwa niteleze ile nguo inikabe ionekane nimejiua,..

Walinzi wakaja wakanitoa, nikapelekwa mbele ya watawala, maaskari wa magereza, kuhojiwa kwanini nataka kujiua, nikawaelezea, ilivyokuwa lakini hawakuniamini..

‘Kwanini unajiua wakati kesi yako yenyewe unahitajika wewe kunyongwa, ..si umeua wewe,na hukumu yake na wewe uuliwe, haina haja ya kujiua, subiria muda utafika utawekwa kitanzi,...si unataka kufa, kama ulivyoua wenzako,...’akaambiwa

‘Lakini mimi sijajiua, ...walinipiga na kunitundika hapo,...’akajitetea profesa.

‘Acha ujanja ujanja, hapa umefika, subiria hukumu yako,....na tunakuonya, ukirudia tena, utakwenda kulala chumba cha maji,....’akaambiwa.

Bro, hapo nimeambiwa ni gereza lenya afadhali, ..hapo nipo kwenye mateso ambayo sijawahi kuyapata bado naambiwa gereza hilo ni gereza ambao watu wanaombewa wafungwe hapo, kwani kuna unafuu, je hilo gereza la kifi lipoje.

‘Hilo gereza la kifo lipoje,ni kama haya ya huku kwetu huku bongo....?’ akauliza 
kaka mtu

‘Hahaha, ...bro, huko kuna watemi, kuna watu wanakula nyama za watu, ulishasikia hilo kwenye magereza yetu, ...humo ndani kuna mijitu imeshindikana hata wakuu wa gereza wenyewe wanawafahamu, lakini ni mijitu yenye pesa...’akasema

‘Kama ina pesa na ina uwezo huo kwanini wakafungwa?’ akaulizwa

‘Sheria ni kitu kingine bro, wamefungwa kutokana na sheria, lakini humo ndani ya gereza ni nani atajua ni nini kinachoendelea, ni nani atasema, na hata kama wanafahamu, pesa inatenda,...kwanza ukisema unakatwa kidole, unakatwa mkono,..na anayekufanya hivyo, unaweza hata usiomuone..utamshitakia nani....’akasema

‘Kwa vipi...?’ akauliza kakamtu

‘Bro, tuendelee na kisa chetu, tukifika huko nitakusimulia uone watu walivyokuwa wababe, watu wanakata nyama yako na kuitafuna mbele yako...watu wanaua wanaotoa utumbo wa mtu huku anajiona.....watu ni wanga, wachawi, lakini uchawi wao ni wa mchana,kweupe......’akasema

‘Haya endelea maana unaongezea chumvi tu hapa,....sikuelewi....’akaambiwa na kaka mtu

‘Utanielewa tu,....ila sasa nakurejesha gerezani nipo nasubiria kesi yangu,na nikiwa nimepumzika nikiwa na mawazo,mara nikasikia ninaitwa kuwa nina mgeni....

Tuendelee na kisa chetu

****************

Nilipofika sehemu ya kukutana na wageni, nikamkuta mama mtemi, alifika na ajenda ile ile ya...anataka kujua pesa ipo wapi, ili amlipe wakili ili awalipe watu mbali mbali ambao yeye kajidhamini kwao, akijua pesa ipo,...

‘Na humu watakutoa,...kwani wewe hustahiki kuwekwa humu, ukumbuke umewekwa humu kwa mbinu tu....sasa waliokuweka humu, wanataka upelekwe kwenye gereza linalokustahiki....’akasema mama mtemi

 ‘Natakiwa kupelekwa wapi....na wakati kesi bado, sijahukumiwa?’ akauliza profesa.

‘Hukumu ni kitu kingine, hata kama hujahukumiwa bado ulistahiki kukaa humo, kama wanavyofanyiwa wenzako wenye kesi kama yako, kesi yako ni ya mauji,hukustahiki kukaa humu...’akasema mama mtemi.

‘Lakini sijaua, hata ushahidi unaonyesha hivyo....’akasema profesa

‘Ushaidi huo kautengeneza nani,...kazi yote hiyo kaifanya nani, hadi hapo ilipofikia...?’ akauliza mama mtemi

‘Ni huyo wakili, namshukuru sana....’akasema profesa

‘Unamshukuru eeh, unafikiri anatangaza dini pale,...yule anahitaji pesa yake, sasa wewe umedanganya, ukanifanya nijidhamini kwa watu mashuhuri, na nilitarajia kijana wako akija kwako ungemuelekeza wapi pesa zilipo, lakini ukawa unampiga tarehe, hii ina maana gani.....?’ akauliza mama mtemii.

‘Lakini mimi sijui pesa zilipo,...pale nilipohisi zipo ndio hapo nilipomuelekeza huyo kijana na isje mumezichukua halafu mnanizunguka, nikasema , nikiwa hata mimi sina uhakika kuwa kweli zipo hapo au ndio mjanja kaziwahi.

‘Kwakweli umaniabisha sana, hata sijui uso wangu nitauweka wapi, maana hao wakuu waliokusimama hadi usipelekwe gereza la kifo, wanafikiria mimi nimewatapeli...’akasema

‘Sasa mimi nitafanyaje....ningelikuwa huru, ningejaribu kutafuta mwenyewe....’akasema profesa

‘Hapa sasa mimi unanichanganya, hawa watu nitawalipa nini, kwa hali ilipofikia, mimi nakuachia kesi yako mwenyewe, ...wakili kakasirika, nilimlipa mimi kiasi kidogo cha kuanzia, ikijua pesa ipo,....’akasema akionyesha kukasirika kweli.

‘Kwa hali lipofikia,  siwezi kuendelea kumlipa tena, siwezi kuoteza pesa yangu, na hata hivyo, nitapatia wapi pesa, ...hapa nilipo nimechanganyikiwa, hata sijui nifenye nini,...kwanza sina uhakika wa marejesho ya pesa zangu, ukifungwa maisha je....’akasema

‘Lakini,..siwezi kufungwa maisha, mimi sina kosa, sijaua...’akasema profesa

‘Kama huyo wakili ataendelea na hii kesi, uhakika wa wewe kushinda ni mkubwa, lakini kutokana na kukosekana kwa hizo pesa, mimi sina pesa za kumlipa tena, nab ado atakuwa anadai, hata sijui nitafanya nini....’akasema akikunja ngumi kuashiria hasira

‘Ndio maana nilitaka kuongea na kijana wangu anaweza kunisaidia kunilipia,....’akasema profesa.

‘Kijana wako!! Yule mpuuzi, nimeongea naye mengine anakwenda kuongea mengine, mpuuzi mkubwa, kwanza hana pesa kabisa...mwenyewe ana madeni kibao,... ‘ akasema

‘Madeni kutoka wapi...?’ akauliza profesa

‘Mpuuzi yule ....yeye alijua akimpata binti yangu ndio shida zake zitakwisha, halafu anajiunga na hao wajinga, anafikiri wale watamlipa nini,...kaniambia shida zake nyingi, sizani kama nitakubaliana naye amuoe binti yangu, sikubali kabisa, ataniletea shida tu....’akasema

‘Lakini amekubali kukutumikia wewe, naona hata kwenye kesi amesimamia kunikandamiza ili kukurizisha wewe, sio kwamba mumepanga iwe hivyo....?.’akasema profesa

‘Wewe huna akili kweli,... ina maana mimi nimlipe wakili na bado nimtumie yeye kukukandamiza wewe, mimi ninachofanya ni kuangalia masilahi yangu basi..., kama hakuna masilahi siwezi kupoteza muda wangu, nikusaidie wewe kwani wewe ni ndugu yangu, kiukweli wewe ni adui yangu, lakini kama kuna masilahi, uadui nauweka pembeni....’akasema

‘Kwahiyo tufanyeje maana wakili aliniambia anataka kujitoa,... tafadhali mama mtemi nipo chini ya miguu yako, nakuhakikishia akinitetea, nitajitahidi kuzipata hizo pesa ...’akasema profesa akitaka kupiga magoti, lakini moyoni hakujua wai atazipatia hizo pesa na ikizingatia yupo gerezani

‘Mimi siwezi kudanganyika tena,....  labda useme pesa hizo zipo wapi, nikiwa na uhakika, mimi nitajua jinsi gani ya kumweka sawa, ujue nay eye yupo kazini, hawezi kufanya kazi isiyo na malipo, yeye ni wakili binafsi, na kazi hiyo ndiyo inayomweka mjini...’akasema mama mtemi

‘Mimi sijui wapi hizo pesa zipo, nilipotoka pale ule mfuko wenye pesa niliurushia sehemu hiyo, niliyomuelekezea huy kijana, kama hazipo hapo mimi siwezi kujua zaidi....huenda huyo aliyenigonga kichwani alizichukua, akaniachia mfuko mtupu, akawa kaweka vitu vingine nikahisi ni pesa...’akasema

‘Ashindwe kuzichukua muda huo, aje kuzichukua baadaye, huyo naye bwege,....’akasema

‘Unaongea kama vile unamfahamu...’akasema profesa

‘Ningemfahamu si ningeenda kwake,...nisingemuachia aondoke na pesa hizo,...sijui atakuwa ni nani...mmh,mbona katajirika, lakini sitatulia mpaka nimtambue,....ila huyo mtu hana akili kabisa....’akasema akisimama kuondoka

‘Sasa utanisaidiaje,....?’ nikamuuliza

‘Mimi sijui, kukusaidia kwangu ni mpaka niwe na uhakika wa pesa, kama una njia nyingine za kupata pesa niambie,...’akasema

‘Mhh, kiukweli,...kama ningelikuwa sipo kifungoni,  ningekuwa nyumbani , labda ningeliweka dhamana ya nyumba yangu...’nikajikuta nimesema hivyo

‘Nyumba eeh, kweli...umesema jambo la msingi,...nyumba eeh, Kweli hapo umeongea kitu....’ akaruka na kukaa

‘Nilisikia kuwa nyumba yako ina thamani kubwa, waliofika huko wamethibitisha hilo,... sasa tufanye hivi, mimi niongee na huyo wakili, ili aweke mkataba, wa dhamana ya hiyo nyumba, unasemaje ...’akasema

‘Hapana ngoja nifikirie kwanza,....’akasema profesa

‘Hamna muda wa kufikiria hapo, .....kesho wakili atakuja mtaandikishana, kesi ikiisha, ...hata kama utafungwa kidogo, lakini tuwe na uhakika kuwa kutapatikana pesa,....sasa wewe utatoa muda ambao utaweza kuitafuta hiyo pesa,muda ukipita  nyumba inapigwa mnada, ili pesa za watu zipatikane na mimi hapo hapo nitapata pesa ya madeni yangu...hilo wazo zuri sana,...sasa akili imetulia..’akasema akichukua simu yake

‘Nipe muda wa kufikiria kwanza usiharakishie hilo wazo, maana sijajua ni nini kinachoendelea huko nyumbani, na ujue naweka dhamana tu, nikitoka nitatafuta hizo pesa, siwezi kuuza nyumba yangu....’profesa akasema

‘Hakuna cha muda hapa,...wewe unadaiwa pesa nyingi sana, nyumba hiyo ndio itakuwa mkombozi, ....unafikiri, wewe utapatia wapi pesa,....huna jinsi inabidi hiyo nyumba ipigwe mnada, ili hawa watu waliokudhamini wapate pesa zao....’akasema na kupiga namba, na mara akawa anaongea na wakili
Waliongea kwa muda, na baadaye akakata simu na kusema

‘Wakili analifuatilia hilo , ili kuhakikisha kuwa kweli hiyo nyumba yako inaweza kulipa madeni ya watu ikiwemo dharama zake....hapo anaongeza gharama zake za kufuatilia hilo jambo..., nina imani hiyo nyumba italipa, kwahiyo kuanzia sasa ujue wazi nyumba itapigwa mnada, na kama tutapata mteja mnzuri, basi itasaidia.....’akasema

‘Hapana mimi nimesema nyumba ni dhamana tu, mwenyewe nikitoka nitatafuta pesa yenu,.......’akasema profesa

‘Wewe, acha upuuzi, utatoka lini, na ukitoka pesa utapatia wapi, ...mimi nakwambia maana nina uzoefu wa jela,ukitoka jela unakuwa kama bwege fulani, akili hata haifanyi kazi tena....’akawa anashika kichwa kama anapiga mahesabu.

‘Nyumba ndiye muokozi wako...angalau kesi ya mauaji itapata mtetezi,...wewe hebu fikiria, ni lipi jema, ukafungwe maisha, au uuze nyumba hiyo, angalau hata ukifungwa muda mfupi, sio mbaya,...maana kiukweli, una makosa, hata kama sio makosa ya mauaji, lakini kuna makosa mengine.....’akaambiwa

‘Hamjui mateso gani ninayoyapata huko jela, watu wamenikamia, .....na wengine wanataka hata kuniua, nimewadanganya kuwa nikitoka nitahakikisha nawapatia pesa yao, kwahiyo hayo ni madeni mengine...’akasema profesa

‘Hahaha, nikuambie kitu, jela hiyo haina shida,..ngoja ufike jela ya kifo, gereza la kifo, ile kupokelewa tu, ni lazima upoteza fahamu, wanakujaribu, ..hahaha, huko jela ya kifo, ..ni kifo kweli...’akasema

‘Nakuonea huruma sana...lakini ni lazima uonje shida yake, ili ujifunze, nina imani kama utafika huko, ukatoka salama, huwezi tena kurudia tabia hiyo, kamakweli utatoka salama...’akasema

‘Ina maana ni lazima nifungwe, mimi nilijua wakili atanitetea, kesi nishinde, ina maana gani sasa kuuza nyumba yangu....’akasema profesa

‘Wakili atafanya kila liwezekanavyo, kwanza ni kupigania hilo shitaka la mauaji, hilo ndilo muhimu sana....ukishinda hapo ina maana umeokoka na kitanzi, au kifungo cha maisha, haya makosa mengine ni miaka mitano, au sita,....chini sana ni miaka mitatu, ni afdhali kuliko kifungo cha maisha....’akasema

‘Miaka mitatu....sita..mitano.....unatania...siwezi, nitakufa, sasa hivi unaona nilivyokwisha, hata miezi mitatu bado.....’akasema profesa

‘Hahaha...ndugu,..ndugu, ulifikiria nini wakati unafanya hayo madhambi, zawadi ya 
madhambi ni nini....ukijiingiza kwenye madhambi hayo, ujue kuna kufungwa, ujue kuna kufa, ujue kuna kuumia.....huwezi kuwadhulumu watu ukategemea kuishi kwa amani, hata siku moja, ni lazima siku moja utalipa, na malipo yake ndio hayo...’akasema mama mtemi

‘Hata sijui, ....na tatizo nyie watu hamuaminiki...na kama ni hivyo, kwanini huyo wakili asitafute mbinu, nikatoka kabisa, kesi hii ikafutwa kabisa, maana yote hii najua ni fitina, ni wangapi wanafanya haya madhambi na bado wapo mitaani, hawajafungwa kwanini mimi...’akalalama profesa

‘Kwanini wewe....hahaha, hilo swali unalo jibu lake, na nikuambie kitu, huu sio muda wa kulalama, maana unajua kosa lako ni nini, haya yote umejitakia wewe mwenyewe,.....nilikuonya, unakumbuka,...uliza, ukiingia anga za mama mtemi, utajua, lakini sasa..sio muda wa kuyawaza hayo,...au unataka kusema nini?’ akasema mama mtemi.

‘Lakini.....’akataka kusema kitu profesa na mama mtemi akamkatiza na kusema

‘Lakini...nini, unataka kusema nini, ,...huuu sasa sio muda wa kulaumiana, hatujui hakimu atakufunga muda gani, wakili atajaribu kadri awezavyo kukutetea, muhimu kwanza ni kuhakikisha shitaka la mauaji linaondoka, hicho ndicho kipaumbele chetu,...nitaongea naye nitamuweka sawa, .. .’akasema akiangalia saa.

‘Unajua mimi sasa nina imani...kwa vile sasa kuna uhakika wa pesa, kazi iliyobakia ni kupanga mashambulizi kwenye ulingo wa mahakama,... huyo wakili atasaidia wewe mwenyewe  si-umeona kazi anayoifanya...tuombe mungu hiyo, kesi ya mauaji iondoke, yabakie hayo makosa mengine,,...’akasema mama mtemi.

‘Vyovyote iwavyo, ...nimechoka ...kama mwaka utaisha nikiwa jela, sijui kama nitakuwa hai...’akasema profesa

‘Hahaha....bado.....lakini kwanza hebu nikuulize wewe huwezi hata kukisia ni nani mwingine anaweza kuwa kazichukua hizo pesa,maana pesa ingekuwepo,....aah,sijui, pesa inaongea.....’akasema

‘Mhh, hata sijui...sijui nani kazichukua hizo pesa, kwani huyo kijana wangu kasema nini , kwanini hamkuja naye,  ananitia mashaka sana, nilitaka niongee naye nijua alivyofanya, katafuta wapii na wapi, kwanini hataki kuja kuniona...?’profesa akasema kama anauliza

‘Yule achana naye, si umeona ni shahidi wa hao watu, hawezi kukusaidia kitu kwa hivi sasa, na huwezi kumlaumu kwa hilo, unachotakiwa kufanya ni wewe kuwa muwazi kwangu..na ili ufanikiwe, ili wakili aweze kushinda, muelezee kila kitu , jinsi ilivyo kuwa...’akasema

‘Nilishamuelezea kila kitu,...hakuna nilichomficha...’akasema profesa

‘Ulimuelezea hata huko ulipoficha hizo pesa, wewe ni bwege kweli...’akasema huyo mama

‘Sina cha kumuelezea kuhusu pesa maana sijui wapi zilipo, ....niamini hilo, kilichotokea pale siwezi kutambua vyema, niliamuka nikiwa sijitambui, nilipoangalia chini ya meza nikauona huo mfuko, nikajua ndio mfuko wa pesa, nikauchukua na kutoka nao...’akasema

‘Hukutizama kuwa una pesa...?’ akauliza

‘Sikutizama, ....niliubeba tu, nikakimbia nao, nikipitia ngazi za nyuma, sikupitia kwenye lifti, nilipofika eneo lenye uwazi, nikaudosha huo mfuko, sehemu ambayo sio rahisi kuuona, ....’akasema

‘Eneo gani hilo la uwazi, maana pale yapo maeneo mengi, ni kwenye gorofa ya ngapi...?’ akauliza

‘Sikumbuki, nilikuwa nimechanganyikia,....na sikuwa na uhakika kama ulikuwa na pesa, au kulikuwa na kitu gani kingine ni hapo hapo nilipomuelekeza huyo kijana....’akasema

‘Wapi, ...nielekeze wapi nikajaribu kutafuta mimi mwenyewe.....’akasema huyo mama mtemi

‘Nilimuelekeza kijana, najua atakuwa amekuambia ni wapi,lakini sina uhakika ni gorofa ya ngapi, maana nilikuwa nateremka chini kwa kupitia ngazi za watembea kwa miguu....’akasema

‘Nikuambie kitu,.....haya sasa ni mimi na wewe, huyo kijana achana naye,.. ukimueleza kitu ujue kitafika kwa watu wa usalama,...lakini tuyaache hayo,maana hata kama uliweka wapi, huwezi kuukuta tena....watu wengi wamekuwa wakiutafuta,...labda kama kuna sehemu nyingine umeficha...’akasema

‘Sijaficha kitu,.....niamini kwa hilo...’akasema profesa akijaribu kukumbuka

‘Ok,....tuyaache hayo, ....muhimu kwa sasa ni hilo, akija wakili kesho anakuja na huo mkataba, kuwa umekubali hiyo nyumba iuzwe, ili uweze kulipia madeni na gharama za hii kesi, kuanzia sasa mimi sitaki kusikia vinginevyo..tumeelewana kwa hilo...’akasema mama mtemi

‘Nitasema nini tena hapo, najua unachowazia wewe hapo ni pesa tu, hujali mustakabali wa maisha yangu,... hujali afya yangu, mimi siwezi kuishi jela, nitakufa,na sasa unataka kunimaliza kabisa nisiwe na hata na nyumba ....’akasema profesa

‘Hilo ni shauri lako,sema wapi pesa ipo, tuachane na hiyo nyumba....ujue wewe mtu,  ukileta ubishi, ujue kweli unafungwa, na ujue huko jela utakwenda kukutana na maadui zako...kwa hivi sasa huna ujanja...,na kama utabadili huu msimamo, ujue kuwa unakwenda kufa,...usije kunilaumu kwa hilo...’akasema

‘Tatizo hili wazo limekuja kwa haraka sana ....nahitajia muda wa kulifikiria...’akasema

‘Wewe umeshalisikia gereza la kifo lilivyo,...si ulishaambiwa, ....huko, kama uulivyosikia ukiingia huko, uage kabisa, na tatizo la huko, unakufa taratibu huku unajiona, kwa mateso makali, ni aheri ungelinyongwa ikjulikana moja..kwahiyo kesho fanya maamuzi ya busara, nimeshaongea na wakili, na kesho anakuja na huo mkataba...’akasema

‘Nitafikiria na kesho akija huyo wakili nitakuwa na jibu tayari....’profesa akasema na mama mtemi akainuka kwenye kile kiti na kuanza kuondoka hata bila kusema neno zaidi....na profesa akasema;

‘Jitahidi kijana aje tuonane hiyo kesho....’akasema na mama mtemi hakusema neno akawa ameshaondoka.

Bro, mimi sikuwa na la kufanya, na ningekuwa na mawazo angalau ningewapigia simu huku, ili muone jinsi gani ya kunisaidia, si mungeuza hata ngombe, .....lakini hapo akili ilikuwa inawaza jinsi gani ya kuokoka na hicho kifungo.....akilini niliwaza kufungwa zaidi kuliko hiyo nyumba.....usiku ukaingia na asubuhi ikafika...

WAZO LA LEO: ni toba ya kweli:


Tukumbuke dhambi ya kumtendea mwanadamu mwenzako, ukamfanyia ubaya mwenzako, ukamdulumu haki yake, ukajiona wewe ni mjanja, ukapata ukatajirika, msamaha wake ni wewe mwenye kwanza kutubu kwa kukiri moyoni kuwa umekosa, halafu pili umuendee yule uliyemtendea huo ubaya umuombe msamaha, akubali, na akubali kutoka moyoni kiukweli, kuwa amekusamehe, kitu ambacho sio rahisi .... Basi tuache kutendeana ubaya tuache dhuluma, ili tuwe na dunia yenye amani na mbele ya mungu tupate makazi mema.
Ni mimi: emu-three

No comments :