Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, August 26, 2015

RADHI YA WAZAZI-34


 Hakimu akawaruhusu upande wa utetezi wamuulize huyo shahidi maswali, na wakili mtetezi akasimama, kwanza akawa kama anawaza jambo, alishika mkoba wake kama anataka kutoa kitu, halafu akasita, akatulia pale pale kwa muda, kama anawaza jambo....

Halafu kwa mwendo wa taratibu akamsogelea mshitakiwa kama anataka kumuambia kitu, lakini hakufanya hivyo, akageuka kuelekea alipo shahidi.Akitembea mwendo ule ule wa taratibu.....

Alipofika kwa shahidi, alimuangalia usoni akiwa kama anamchunguza akamuangalia huyo shahidi moja kwa moja usoni..., na shahidi naye akawa anamuangalia huyo wakili bila kuangalia pembeni au chini.... 

Shahidi naye alijitahidi kumuangalia wakili, huenda alishaambiwa ujanja wa mawakili kuwa asimuogope wakili pale anapomuangalia usoni au pale anapotoa maswali ya vitisho, kwahiyo shahidi huyu akajitahidi nay eye kumuangalia wakili huyo usoni.

Wakawa wanaangaliana

Baadaye wakili alisema....

‘Wewe shahidi ni muongo, ....’

Tuendelee na kisa chetu...

********

Baadaye wakili huyu akasogea nyuma, lakini bado akiwa anamuangalia huyo shahidi,....na mdomoni akawa anatabasamu,kama vile kagundua kitu.

Wakili huyu  akageuka  upande wa watazamaji, watu waliofika hapo mahakamani, walikuwa ni wengi, na kwa sauti kama ya kunong’oana akasema...

‘Shahidi huyu ni muongo....’akasema  na watu wakaguna na minong’ono ikatanda,....hakimu akapiga rungu lake na kusema kuwe na utaratibu halafu akasema;

‘Wakili mtetezi unapoteza muda,....’akasema na wakili akamgeukia hakimu, akainama kama vile anataka kuondoka au kusema hana swali,lakini kwa haraka akamgeukia shahidi na kusema;

‘Wewe ni muongo,....unaidanganya mahakama,....hilo kosa....’akasema na shihidi akabakia kimia, lakini hakuacha kumuangalia huyo wakili , lakini usoni kwake alikuwa keshakunja alama za kuashiria kuwa kakasirika.

‘Baba yako na mama yako ni nani.....?’ wakili akamuuliza akiwa kamkazia macho,lakini mdomoni akiwa anatabasamu,

Shahidi hakujibu kwanza, alimgeukia  wakili wake, na wakili wake akamuashiria ajibu hilo swali.

‘Siwajui....’akasema huyo shahid kwa sauti yenye kuonyesha kukerwa na hata sauti ilikuwa ya kukasirika.

‘Kwahiyo wewe ulizaliwaje, kama huna baba au mama...?’ akaulizwa swali tena na wakili huyo, huku wakili huyo akitabasamu.

‘Nimesema siwajui,... hata kama wapo sijawahi kuwaona...’akasema akionyesha dharau.

‘Unaona ulivyo muongo,..dharau, ndio tabia yako sio, je hujawahi kuwaona baba na mama yako..waliokuzaa...?’ wakili akauliza sasa nay eye akionyesha  ukali katika sauti yake,  na wakili muendesha mashitaka akatoa pingamizi kuwa wakili huyo kuwa wakili huyo anamlazimisha shahidi kuongea kitu ambacho keshajibu, na hakimu akamuonya wakili huyo.

‘Wewe unasema wapo, lakini kama hawapo hujawahi kuwaona....au sio...?’ akaulizwa

‘Nilishajibu ...sijawahi kuwaona.....’akasema

‘Ila wapo...?’ akaulizwa

‘Sijui....’akasema

‘Sasa kama hujui, nikuwa alitokea msamaria mwema akahangaika kukutafutia wazazi wako, baada ya yeye kukuokota ukiwa maporini, ukitaka kuliwa na wanyama....’akatulia

‘Huyo msamaria akahangaika kuwatafuta wazazi wako, huku akihangaika kutafuta jinsi gani utasoma,...yeye akafanya uchunguzi , na katika kukukagua akagundua kuna kufanana fanana fulani na ndugu yake..., siunajua damu ya mtu haipotei....’akasema wakili.

‘Mimi sio damu yake kabisa....kakudanganya tu...’akasema shahidi

‘Huyo msamaria mwema, akahisi wewe ni damu yao...’akaendelea kusema huyo wakili bila kujali maneno ya huyo shahidi

‘Wewe wasema ....’akasema shahidi

‘Sijakuambia unijibue,.....’hatimaye wakili akasema kumuashiria huyo shahidi aimuingilie, wakati anaongea

‘Unatunga uwongo, nashindwa kuvumilia huo uwongo wako....’akasema sahahidi.

‘Sasa kama huyo msamaria mwema, kaja  kugundua kuwa kumbe wazazi wako pia ni ndugu zake, je kufanya hivyo ndio kafanya makosa...au kwa vile tu umeona kuwa watu hao ni masikini, wanaishi kijijini,  hawana kitu...?’ akaulizwa

‘Ndio kafanya makosa,.....kwasababu sio kweli,...na sijawakataa kwasababu ni masikini, mimi sijui kama ni masikini, ila hayo unayatunga wewe mwenyewe kutoka kichwani mwako...’akasema shahidi

‘Una uhakika gani kuwa sio kweli, kuwa natunga kutoka kichwani kwangu....kuwa hao uliowaoana sio wazazi wako?’ akaulizwa na hapo muendesha mashitaka akataka kuingilia lakini akaonekana kusita, akatulia.

‘Akina nani nani hao.....?’ akauliza kwa sauti ya hasira

‘Hao uliowahi kutambulishwa kwako kuwa ni wazazi wako , baba na mama yako, wewe ukawakana....’akaambiwa

‘Niliwakana kwasababu kweli sio wazazi wangu,...nilishawashitukia, nikajua kuwa  ni mbinu tu zao, za kutaka kupata pesa kupitia mgongo wangu,....’akasema

‘Swali...je una ushahidi gani kuwa hao sio wazazi wako, ...wakati wewe unafanana na baba yako...?’ akaulizwa

‘Nafanana na yule mzee, unanichekesha kweli,....Kwanza nikuambie ukweli, mimi sura yangu haifanani kabisa na huyo mtu, hujawahi kumuona kama ungemuona ungekubaliana na mimi....yeye ni mweuzi tiii, na mimi ni maji ya kunde, si unaniona nilivyo...’akasema na watu wakacheka,

‘Na pili tabia na mienendo zetu hazioani kabisa, kama angekuwa ni baba yangu, angalau kungelikuwa na kijitabia fulani kinachofanana na mimi,..lakini hakuna kitu kama hicho kabisa, huyo jamaa anamihasira utafikiri nini....’akasema

‘Na tatu...unawaona walivyo, matendo yao, hasa huyo mshitakiwa, tapeli, mwizi, ...anapenda pesa,na anaonekana kabisa anaweza kufanya lolote ili tu apate pesa bila kujali sheria...na zaidi ya hayo, hakuna ushahidi kisheria kuwa watu hao nina uhusiano nao kabisa....’akasema.

‘Hakuna ushahidi kisheria kuwa watu hao wana uhusiano na wewe, wewev unajua ushahidi gani wa kisheria wa kukuonyesha kuwa wewe una mahusiano na hao watu.....?’ akauliza na wakili akaingilia kati hilo swali.

‘Hilo swali limetokana na majibu yake...’akajitetea wakili mtetezi, na hakimu akasema lijibiwe

‘Hiyo ni kazi yako wewe, mwanasheria, unaniuliza mimi.....’akasema

‘Ndio nimekuuliza wewe, ni ushaidi gani ambao unautambua, wa kisheria, wa kukuonyesha kuwa wewe una mahusiano na hao ....?’ akaulizwa

‘Kuna vyeti vya kuzaliwa, kuna...kitu chochote cha kuonyesha kuwa mimi nina damu, au ...hata labda kurithiwa,ni lazima kuwe na nyaraka za kisheria, unafahamu unanidhihaki tu,....kama angelitaka niwe mwanae angetafuta hata hicho cheti cha kunirithi,.hana, najua hana ....’akasema

‘Una uhakika na hilo....?’ akauliza wakili huyo akimuangalia kwa makini.

‘Ndio nina uhakika, wewe si wakili wao nionyeshe huo ushahidi kama unao, kama sio unatafuta pesa tu kwa kuwatetea wahalifu hao....’akasema na wakili akatabasamu.

‘Je nikikuonyesha ushahidi kuwa hao ulio onyeshwa kule kijijini ni wazazi wako halali utasemaje....?’ akaulizwa na wakili ,na shahidi huyo akacheka kwa dharau na kusema

‘Hakuna kitu kama hicho,..labda  huo ushahidi uwe wa kugushi, wa kitapeli, maana huyu mtu chochote anaweza kufanya, hata kusingizia kuwa yeye ana udugu na raisi ili apate pesa za familia ya raisi yeye anaweza kusema hivyo.....’akasema na watu wakacheka, na walipotulia alipoona wakili mtetezi naye katulia akaendelea kusema

‘Mimi ...siwezi kuwa na wazazi kama hao,....kabisa kabisa nakataa kwa nguvu zangu zote, hakuna na hakutaweza kuwepo na ushahidi wowote zaidi ya maneno ya uwongo, kuonyesha kuwa mimi ni mtoto wa hao watu, hao watu ni waongo, matapeli....’akasema,na huyo wakili akamgeukia na kusema;

‘Wewe  shahidi ni muongo, umefundishwa kuongea hivyo, hadi kufikia kuukana ukweli wa asili yako,unafikia hatua ya kuwakana hata wazazi waliokuzaa, unamkana mama yako mzazi, unajua jinsi gani mama yako alivyokuhangaikia, ukiwa tumboni, akakuzaa kwa shida, unafahamu mama yako ...’akasema na wakili muendesha mashitaka akaingilia na kusema wakili analazimisha shahidi aseme uwongo, na shahidi akasema kwa hasira

‘Huyu wakili ni muongo, mimi ninachosema mbele ya mahakama hii ni ukweli mtupu,na sijawahi kuukana uasili wangu, nilichokikana hapa ni tabia chafu  za hao watu,,...utapeli, wizi, ....nk mimi sina tabia chafu, kama asili yetu ni tabia chafu basi mimi sitakubali kuwa na asili hiyo,..na hao watu sio wazazi wangu.’akasema na watu wakamshangilia.

Wakili mtetezi  kwanza akatabasamu, halafu akasogea kwenye makabrasha yake, akatoa karatasi, ilikuwa kuu-kuu, akaiangalia kwa makini kama anasoma kitu, akatulia kama anawaza jambo, halafu akageuka kumuangalia shahidi akasema;

‘Wewe ulisema kuwa hakuna ushahidi wowote wa kuonyesha kuwa wewe huna mahusiano yoyote na familia hiyo....siku hizi hakuna ujanja bwana, huwezi kumkana mzazi wako....’akasema na shahidi akawa anaonyesha uso wa kujua ni kitu gani, akageuka kumuangalia wakili wake, na wakili muendesha mashitaka naye akawa anaangalia ni kitu kashika huyo wakili mtetezi.

‘Huu hapa ni ushahidi unaoonyesha kuwa wewe ni mtoto wa damu wa kaka wa huyu mshitakiwa ...’akasema akiwa kashikilia ile karatasi, sasa akiwa kamsogelea shahidi.

‘Wewe si umesoma, hebu angalia hapa kumeandikwa nini....?’ akawa anaonyeshwa hiyo karatasi,

‘Its fake..najua lazima atatafuta nyaraka za uwogo....’akasema

‘It’s a fake....wewe ni msomi, kitu kama hiki kinaweza kufojiwa, wewe ulizaliwa huko anapotokea huyu mshitakiwa,na mshitakiwa ni baba yako mdogo, ushahidi huu hapa.....’akasema akimkabidhi huyo kijana karatasi hiyo, na wakili muendesha mashitaka akainuka pale alipokuwa amekaa na kwenda hadi pale aliposimama shahidi, akaichukua ile karatasi,....

‘Huu sio ushahidi sa-hi-hi.....!?’akasema kwa kuuliza muendesha mashitaka na akayamalizia hayo maneno ya mwisho kwa taratibu.

‘Umeitoa hii kama ushahidi....?’ akauliza wakili muendesha mashitaka, na wakili mtetezi akasema;

‘Sijaitoa hiyo na kuikabidhi kama ushahidi , kwani natambua fika,  muda wangu wa kufanya hivyo bado, ila nimeitoa ili kumuweka sawa huyu shahidi wako kuwa asiendelee kuongopa,....’akasema

‘Hiyo sio kazi yako kuoana kuwa anaogopa...ni kazi ya muheshimiwa hakimu...’akasema wakili muendesha mashitaka.

‘Najua,...lakini shahidi wako alitaka kuuona huo ushahidi, ili akili yake itambua kuwa hapa sio sehemu ya kuongopa, anatakiwa kila anachokiongea ajue kuwa ni sahihi, hapa yupo mbele ya mahakama, kaapa,...na zaidi ni msomi...sio kwamba kuwa haelewi anachokiongea, hata kama kafundishwa aongee hivyo,....

'Kwanini wewe shahidi ukubali kurubuiwa, uje kuwakana wazazi wako mbele ya mahakama, mbele ya mungu utakuja kusema nini,.....sio vizuri....’akasema huyo wakili, wakati huo, wakili muendesha mashitaka akawa bado anaendelea kuichunguza ile karatasi

It’s a fake...sio ushahidi sahihi huo, anawadanganya...mimi siwezi hata siku moja kukubali huo ushahidi hadi kufa.....never..’akasema huyo shahidi akumuashiria wakili muendesha mashitaka kwa kidole, na kiganja cha mkono, na wakili mtetezi akasema;

‘DNA, sio ushahidi sahihi.....?’ akauliza wakili mtetezi, akimuangalia wakili muendesha mashitaka na wakili muendesha mashitaka akasema

‘Kila kitu chawezekana mbele ya wanadamu .....’akasema na akawa anatembea kuelekea sehemu yake ya kukaa huku akiwa bado kashikilia ile karatasi, na wakili mtetezi akasema

‘Sijaikabidhi hiyo nyaraka kama ushahidi muheshimiwa na hakimu akasema;

‘Taratibu zifuatwe mawakili...., wakili mtetezi endelea na maswali yako kwa shahidi...’akasema hakimu, na wakili mtetezi akageuka kumuangalia shahidi, na shahidi sasa alikuwa kainama chini, kama anawaza jambo,....

NB: Mahakama inaendelea, tuishie hapa kwa leo kwa swali, kwa tafakari,...kauli za ‘sitakubali kamwe ,au hata nikifia asije, au  sitakwenda hata nikifa,..au ....kauli za viapizo ambazo sio rahisi kutimizwa, zina maana gani kutamka midomoni kwetu,.....haya tuone kama kijana ataweza kutimiza ahadi yake hiyo kuwa hatakubali kuwa ni wazazi wake kamwe,....


WAZO LA LEO: Tujifunze kujijengea tabia njema, kwa kauli  na vitendo. Kusema ukweli ni moja ya tabia njema, tusiogope kusema ukweli hata kama ukweli huo, utaumiza watu, hata kama ukweli huo utakuumiza hata wewe mwenyewe, ukweli ni silaha, na ukweli ni ngao, ukiwa mkweli,utashinda wakati wote, kwani ukweli ni uaminifu kwako kwa jamii na mbele ya mwenyezimungu muumba.
Ni mimi: emu-three

No comments :