Kesi
ilianza, profesa akasimamishwa kama mshitakiwa mkuu,wa mauaji , mvunjifu wa amani kwa jamii, na muendesha
biashara ya milungula,(blackmailer)....
Kesi hiyo ilkuwa
kesi iliyowavuta watu wengi, hutaamini hata wakubwa walifika, na hata wengine
kutuma wawakilishi wao...
‘Mhh, naona
hii kesi ina jambo...’mmoja wa waandishi wa habari akawa anadodosa
‘Hii sio
kesi ya mauaji tu, nahisi kuna zaidi ya hilo, marehemu hakuwa maarufu kuwavuta
watu wengi kiasi hiki, na weni ni watu
wakubwa na mashuhuri, Unahisi kuna jambo gani....’akamuuliza mtu mmoja.
‘Mhh,
mauaji.....wakati ni hawa watu wamekuja na njaa zao kwenye nchi yetu wanatuleta
matatizo,...hawa watu inabidi wafukuzwe kabisa....’akasema jamaa mmoja, na
wengine wakawa wanamuunga mkono.
‘Lakini
huwezi kumuhukumu mtu mpaka ijulikane kuwa kweli ana kosa, je huyu mtu ana kosa
gani, na kwanini wakubwa wavutike na hii kesi...?’ akauliza
‘Kuna
masilahi binafsi na hii kesi na wahusika watakuwa wanahusika na masilahi yao,
...’akasema mtu mmoja lakini alipoulizwa zaidi hakusema akaonekana akihangaika
kutaka kuingia ndani ya mahakama....
‘Nahitajika
ndani , nimechelewa....’akasema
Hayo
yakiendelea huko nje, ndani ya mahakama, kesi ilikuwa ikiendelea....
*********
Taratibu
mbali mbali za kimahakama zilifuatwa na waendesha mashitaka, walianza kazi ya
kuitambulisha kesi, na kuielezea hiyo kesi ilivyo..kwa ilikuwa sio siku ya
kwanza, kwani kesi hiyo ilishatambulishwa na siku hiyo ilikuwa siku ya kuanza
kesi yenyewe, basi ikaanza kazi ya kuwaita mashahidi.
Muendesha
mashitaka akaanza kuijenga hiyo kesi, ....na kila shahidi aliyeitwa, akawa
anaongozwa na muendesha mashitaka halafu utetezi inamuhoji huyo shahidi.
Wakili wa
mshitakiwa akijitahidi kukabiliana na mashitaka hayo kwa nguvu zote, na kinyume
na walivyofikiria kuwa wataweza kumfunga mshitakiwa hata ikibidi kifungo cha maisha lakini ikawa
kinyume chake, kwani wakili wa utetezi,
alifanya kazi yake barabara, ...
Kuna baadhi
ya hoja zilizoingia kwenye malumban makali, ....
*********
‘Unasema
mshitakiwa alifika kuchukua mzigo alioelekezwa na watu wake, na mzigo huo
angeupata kwa marahemu,....nashangaa hao watu hawatajwi, ....sawa lakini
unasema alipofika kwa marehemu ili kuuchukua huo mzigo, wakakosana na mshitakiwa
akatoa bastola, akamuonyesha marehemu.....’akaanza mtetezi.
‘Huyu
mshitakiwa alipita sehemu ya mapokezi, na sehemu ya mapokezi wanakaguliwa, kutokana
na taratibu za hilo jengo zilivyo, sasa nawauliza,huyu mshitakiwa aliipitaje
hapo na hiyo bastola...?’akauliza mtetezi kumuhoji shahidi aliyesimamishwa.
‘Huyu
mshitakiwa ana historia za uhalifu, asingeshindwa kutumia ujanja kuihifadhi
hiyo bastola sehemu yoyote humo ndani, na wakati anapita muda huo, ili kuficha
uhalifu wake asitambulikane ‘ akasema
‘Huyu
mshitakiwa wakati anapita alikaguliwa na walinzi au sio, kawa ilivyo kawaida,
alionekana na silaha?’ akaulizwa huyo shahidi
‘Kwa muda
huo hakuonekana na silaha....’akaambiwa
‘Ndio
nauliza hiyo silaha ilipatikana wapi , kama sio kulikuwa na mtu mwingine ambaye
alifanya huo uhalifu, na kumbambikia mshitakiwa....’akasema muendesha
mashitaka.
‘Kutokana na
melezo ya walinzi wa hapo kwenye hilo jengo, ni kuwa silaha haziruhusiwi kwenye
hilo jengo, mtu haruhisiwi kuingia na silaha, kweli si kweli,...sasa
msshitakiwa alipitaje bila kuonekana na hiyo silaha...ndilo swali
langu...’akauliza
‘Waulize hao
walinzi....’akasema huyo shahidi na watu wakacheka.
‘Hii ni
kuonyesha kuwa kulikuwa na mhalifu mwingine alikuwepo hapo kabla, akafanya huo
uhalifu, na kwa vile polisi mumeshindwa kumpata huyo mhalifu mumeamua kumbambikiwa
huyu mshitakiwa,......’akasema
‘Hayo ni
maoni yako toa ushahidi kuonyesha kuwa kulikuwa na mtu mwingine....’akaambiwa
‘Hiyo sio
kazi yangu, kazi yangu ni kumtetea huyu mtu mnayemuonea,...’akasema mtetezi
‘Sina swali
jingine, ...’akasema wakili mtetezi.
********
Kati ya
mashahidi waliowavutia watu waliokuwepo hapo mahakamani, ni mmoja aliyetambulikana
kama kijana wa mshitakiwa, japokuwa yeye baadaye alikana kuwa yeye sio kijana
wa mshitakiwa....
‘Huyu ni
kijana aliyelelewa na mshitakiwa, kijana huyu alitolewa porini akiwa
anatangatanga...kuna vielelezo vingi tu vya kuonyesha hilo tukio,....’muendesha
mashitaka akawa anatoa maelezo
‘Kijana huyu
aliishi na mshitakiwa toka akiwa mtoto, kwahiyo anamfahamu vyema mshitakiwa,...kwahiyo
yote anayoyaelezea, anayafahamu , sio uzushi, yeye anamfahamu mshitakiwa tabia
yake na kazi yake, ...na pia ana muheshimu kama mtu aliyemsaidia hadi kufikia
hapo alipo....’akaendelea kuelezea
‘Mbona wewe
ndio unatoa maelezo.....’wakaanza kulalamika watu wa utetezi
‘Nataka
muone ukweli ulivyo, kuwa hata kijana wake alishaona uhalifu wake, ndio maana
tunamuita kama shahidi......’ilielezewa.
‘Muheshimiwa
hakimu, muendesha mashitaka anageuza mahakama yako uwanja wa siasa,
.....tunahitajia ushahidi au shahidi sio maneno yake....’akalalamika mtetezi
‘Namuita
shahidi yangu, ni kijana aliyelelewa na mshitakiwa mwenyewe ......’akasema
muendesha mashitaka.
Huyo
aliyetambulikana kama ‘kijana wake’
alipita na kusimama mbele ya sehemu ya mashahidi, baada ya taratibu zote
kufuatwa muendesha mashitaka akawa anamuongoza kwenye kutoa maelezo yake.
Kijana ,
akielezea kazi za huyo mlezi wake,....akaelezea kuwa mwanzoni mshitakiwa
alikuwa muuza madawa ya kienyeji, na humo akawa anachanganya na madawa
yasiyotakiwa, yapo kama madawa ya kulevya...
‘Ulijuaje
kuwa yapo kama madawa ya kulevya.....?’ akaulizwa
‘Niliambiwa
na mwenyewe mshitakiwa na pia mshitakiwa aliwahi kushitakiwa kwa kosa hilo la
kuuza madawa ambayo yapo katika kundi la madawa ya kulevya....’akasema
‘Kwahiyo upo
ushahidi wa kimahakama kuwa mshitakiwa aliwahi kupatikana na kosa
hilo....’akasema muendesha mashitaka
Katika
kuelekezea tabia ya mshitakiwa, shahidi alisema mshitakiwa ni mtu mwenye tamaa
alipenda sana pesa, na hata pesa zake za matumizi amazo zilikuwa zinapitia kwa
mshitakiwa alikuwa akizitumia mshitakiwa badala ya kupewa yeye, yeye akawa
anasoma kwa shida, na wakati mwingine ilibidi awe anaomba msaada kwa wasamaria
wema....maelezo hayo yaliwashangaza sana watu...
‘Lakini huyu
ni mzazi, mlezi wako, ..kwanini akufanyie hivyo, au wewe ulikuwa humuheshimu,
.....’akaambiwa
‘Mlezi, au
mzazi anaangaliwa kwa utendaji wake kwa mtoto aliyekabidhiwa....lakini huyu
mshitakiwa hakuwa na ubinadamu na mimi yeye alinitumia tu, ili apate pesa kwa
masilahi yake,...’akasema
‘Je pesa
hizo zilikuwa zikitolewa na nani?’ akaulizwa
‘Na
wafadhili waliojitolea kunisaidia....’akasema
‘Kwa tabia hiyo
wewe ulimuonaje huyo mlezi wako...?’ akaulizwa
‘Kwakweli
japokuwa nilimuheshimu sana, kama mlezi, nikawa namuita dad wangu ....lakini baadaye niliona sio mtu anayestahiki kuitwa
mlezi au mzazi wangu , hafai kuitwa mzazi kabisa labda ni kwa vile hajui uchungu
wa mtoto...’kauli hiyo ikawafanya watu wacheke.
‘Hebu
tuambie ni mambo gani uliyoyaona mpaka uone kuwa mshitakiwa hafai kuitwa mzazi
au mlezi wako...?’ akaulizwa
‘Kama ni
mlezi kwanini alikuwa akinidanganya, je mzazi anatakiwa kuwafundisha watoto uwongo,
kuwadanganya, kuwaibia haki yao....’akasema
‘Yeye
alikuwa anachukua pesa zangu kwa wafadhili,...anatumia hanisaidii sana kama
ilivyotakiwa, alitumia mgongo wangu kujinufaisha yeye mwenyewe....,
anawadanganya wafadhili, kuwa kuna hiki na hiki, kila akitaka pesa lakini
hakinunui, ...mzazi gani hana uchungu na mwanae, anachoangalia ni tumbo
lake,starehe zake.....’akasema.
‘Je ulionaje
kuwa alikuwa akitumia pesa zako kwa starehe zake....?’ akaulizwa
‘Alikuwa
mlevi sana, akawa anabadili wanawake, kila siku anakuja na mwanamke mpya, na
wanastarehe mbele yangu....’akasema na watu wakawa wanacheka.
‘Kwahiyo
wewe uliwezaje kuvumilia hiyo, kuwa unaishi na mzazi mwenye tabia chafu, kama
ulivyosema na zaidi uligundua kuwa ni mhalifu...?’ akaulizwa
‘Mwanzoni
niliogopa kuchukua hatua yoyote maana nilikuwa mdogo asiyeweza kufanya
lolote..na kiukweli nilikuwa namuheshimu kama alivyotoa kwenye vyombo vya
habari kuwa aliniokota, nilimuona kama mtu mwenye huruma kanitoa kwenye hatari,
na kunisaidia,....kwahiyo sikuweza kumchukulia hatua yoyote, nilimuoa kama
mlezi wangu...’akasema
‘Kwahiyo
hiyo habari kuwa alikuokota porini uliichukuliaje....?’ akaulizwa
‘Nilipokuwa
mkubwa na kuweza kuchanganua mambo, nimekuja kugundua kuwa habarii hiyo sio ya kweli,....’akasema
‘Kwanini sio
ya kweli maana hadi wafadhili waliamini hiyo habari,....?’ akaulizwa
‘Mimi
nimeishi na huyu mtu, kutokana na tabia yake, anaweza kutunga uwongo wowote ili
tu apate pesa, ni mwerevu sana wa kutunga uwongo uonakane ni ukweli, ...kwahiyo
nilipochanganua niliona kabisa hiyo habari kaitunga tu, mimi siamini kuwa kweli
aliniokota porini....’akasema
‘Sasa
kwanini hukumshitakia .....?’ akaulizwa
‘Kama
nilivyosema mwanzoni nilikuwa mdogo, nilikuwa naogopa, na sikujua nianzie wapi,
lakini kwa jinsi nilivyozidi kukua, .... na kusoma zaidi, nikagudua kuwa huyu
mtu hafai kabisa kuwa ni mlezi...’akasema
‘Na kiukweli
kwa muda ule nilikuwa sina mtu wa kunisaidia kimawazo, au kunieleleza,
....baadaye akili ikanijia kuwa naishi na mtu asiyefaa kuwa mzazi, na pale
nilipopata kazi tu, na kuona kuwa na naweza kusimama peke yangu, ndio
nikachukua hatua,...’akasema
‘Ulichukua
hatua gani....?’ akaulizwa
‘Kwanza
nikaachana naye, niliona nikiishi naye na mimi nitaonekana nina tabia kama
yake, ya uhalifu, na...pili nikawa natafuta njia za kumfikisha mahakamani kama
raia mwema...., maana sikupenda tabia yake hiyo chafu anayowafanyia raia wema.....’akasema
‘Kwanini
umshitakie baba yako, mlezi wako....?’ akaulizwa
‘Muheshimiwa
hakimu, huyo sio baba yangu,na wala sio mlezi wangu...sio damu yangu kabisa...,
siwezi kuwa na baba au mlezi kama huyo,yeye alitumia ulezi kuninyonya tu,..huyo ni tapeli,
mimi nawaambia ukweli maana niliishi naye....’akasema na watu wakacheka.
‘Kwahiyo wewe
una uhakika kuwa mshitakiwa hana uhusiano na wewe.....?’ akaulizwa tena
‘Kiukweli, hawezi
kuwa na mahusiano na mimi, yeye na ndugu zake....’akasema
‘Ndugu zake
ni akina nani....?’ akaulizwa
‘Yeye ana
ndugu zake huko kwao, na alinipeleka kwa ndugu zake ili kuhalalisha uwongo
wake, ...huko wapi sijui,na kunitambulisha kwa mzee mmoja mwenye sura mbaya eti
ni baba yangu, lakini kiukweli, huyu sio baba yangu,walinitumia njia hiyo ili
waweze kuhalalisha utapeli wao..., ili wapate pesa hizo kwa wafadhili..’akasema
‘Unasema
alikupeleka huko kijijini kwao, ili kukutambulisha kwa watu na akasema hao ni
ndugu zake,...na mmojawapo alikuwa ni kaka yake mshitakiwa , na huyo kaka yake
ukaambiwa ni baba yako, kwanini wafanye
hivyo...?.’akasema
‘Ndio alinipeleka
huko nchini kwake, akanitambulisha kwa kaka yake, walifanya hivyo, baada ya
kuongea, kuna siku tukiwa huku alikuwa akipigiana simu na huyo kaka yake kuwa
ana mipango ya kuingiza pesa, na akirudi huko atamuambia ni mipango
gani...’akasema
‘Wewe
kwanini unahisi kuwa huyo uliyetambulishwa kuwa ni baba yako, sio baba yako kiukweli....?’
akaulizwa
‘Hebu
jamani, niwaulize..., kama si uwongo, mimi ni mtoto wa ndugu yake, kwanini
akaja kudai huku kuwa aliniokota maporini, mimi si mtoto wa kaka yake eeh?
usahihi ulikuwa upi, labda aniambia walipanga yeye na kaka yake wafanye hivyo....’akasema
‘Usahihi
ulitakiwa uwe vipi?’ akaulizwa
‘Kama
aliniokota kama anavyodai,... alitakiwa kunikabidhi kwa kaka yake..., si eti
jamani, mtu kaokota mtoto cha kwanza kufanya ni nini, ni kutangaza kwa watu,
kuwa umeokota mtoto, mtoto ni wa nani,.....haya tufanye hata kaka yake
hawajuani vyema, sasa huyo kaka yake ambaye anadai ni baba yangu alikuwa wapi
mpaka nipotee maporini, hakuwahi kutangaza au kuuliza kuwa kapotelewa na mtoto,...jamani
huyu mtu anatufanya sisi wajinga hatuwezi kufikiri....’ akasema
‘Je wewe
hukuwahi kumuuliza swali hilo wakati mnaishi naye....?’ akaulizwa
‘Swali gani,
maana mimi nilikuwa namkera sana kwa kumuuliza maswali mengi tu, kutaka kujua
ukweli, muulizeni mwenyewe hapo, nilikuwa namkera kwa maswali mapaka
anakasirika, na kuamua kwenda kuninywea, .....’akasema na watu wakacheka.
‘Hebu toa
mifano michache ya maswali uliyokuwa ukimuuliza,.....’akaambiwa
‘Niliwahi kumuuliza
swali mara nyingi la uasili wangu, kwani mwanzoni kiukweli nilijua yeye ni baba
yangu, akaja kuniambia yeye sio baba yangu, nikataka kujua kwanini yeye sio
baba yangu, ndio akaja kuniambia kuwa aliniokota tu maporini...’akasema
‘Baadaye
akaja kuniambia kuwa eti amewagundua wazazi wangu ni akina nani, lakini iwe
siri yangu maana akisema hatutapata tena misaada, mimi kama mtoto nilikubaliana
naye, lakini moyoni sikufurahia kudanganya ...
‘Sasa ndio
akaja na uwongo uliopitiliza kuwa eti kagundua kuwa baba aliyenizaa ni kaka
yake, na bahati mbaya kaka yake na mkewe waliachana, na mimi nikawa nalelewa na
mama, eti mimi yawezekana nilimtoroka mama nikapotea maporini...hiyo ndio
hadithi yake aliniyotungia...’akasema na watu wakacheka.
‘Hukuamini
alipokuelezea hivyo?’ akaulizwa
‘Hata
ungelikuwa wewe, je ungeamini uwongo kama huo...., kama ni hivyo, kwanini
asinirudishe kwa huyo mama yangu, si unajua mama walivyo wakipoteza watoto wao
wanavyoteseka, angenipeleka huko kwa mama yangu, au kumwambia kaka yake kuwa
kaniokota, yeye kafanya nini,....?’ akawa kama anauliza
‘Je waliwahi
kukuonyesha huyo mama wanayedai ni mama yako...?’ akaulizwa
‘Ndio, ....kipindi
cha mwisho, nilipokuwa huko, aliwahi kunilipeleka kwa mama mmoja hivi, wakadai huyo ni mama yangu, mama
mwenyewe anaonekana kachanganyikiwa....’akasema
‘Kwa
vipi...?’ akaulizwa
‘Aliponiona
alibakia hivi.....kunitolea macho,...kunikodolea macho, akawa kama anataka
kunimeza, au kutaka kunifanya kitu kibaya, ...nikakimbia...’akasema
‘Unahisi
kwanini walisema huyo ndiye mama yako?’ akaulizwa
‘Mimi nahisi
walimtafuta mama mwenye shida, wakamuhonga pesa, ili ajifanye yeye ni mama
yangu, ..mimi siwezi kuwa na wazazi kama hao, hebu niangalieni mimi, na hao
wazazi hatuendani kabisa...’akasema na watu wakacheka
‘Kwani hao
wazazi wapoje, hawafanani na wewe....?’ akaulizwa
‘Hawafanani na
mimi kabisa, kabisa....huyu mtu ni tapeli,...rejeeni historia yake na
mambo ambayo
amekuwa akiyafanya, anauza dawa zisizo na utaalamu,kachukua majani na magome ya
miti, ... anawahadaa watu kuwa zinatibu,...hana utaalamu wowote, hebu muulizeni
kaenda wapi shule ya madawa, ..eti anajiita profesa...’akasema na watu
wakacheka
‘Na zaidi akashindwa
kutumia akili ya kujenga hoja ya uwongo wake, angalau akatafuta watu wanaofanana-fanana
na mimi....ananitafutia watu wenye sura mbaya...’akasema na watu wakacheka.
‘Wewe
unahisi ulizaliwa wapi....?’ akaulizwa
‘Mimi nahisi,.....
naweza nikawa nimezaliwa huko huko, au hata huku, siwezi kujua maana yeye ndiye
anajua aliniibia wapi, ...yawezekana alikwenda hospitali akaniiba na kuniweka
msituni na kunipiga picha ili ionekane hivyo....’akasema na watu wakacheka.
‘Jamani hili
sio la kucheka,...., wanadamu ndio tumefikia hapo, watu wanaweza kufanya
chochote, ili tu wapate pesa,...bila kujali ni halali au ni haramu, bila kujali
utu wa wenzake, ....hivi hamjasikia katika sehemu za Afrika kuna watu wanakata wanadamu
wenzao viongo vyao vya mwili wakidai eti watapata utajiri kwa kutumia viungo
hivyo...., hamjasikia hizo taarifa, basi huyu mshitakiwa anatokea huko, ....’akasema
na watu wakaguna na wengine kufikia kuzomea.
‘Tufuate
utaratibu hatutaki kelele mahakamani...’akasema hakimu akigonga kirungu chake.
‘Samahani
muheshimiwa hakimu, sikuwa na nia ya kuwafanya watu wapige kelele, lakini ni
muhimu wakalielewa hilo, kuwa mbele ya mali, mbele ya pesa, mbele ya utajiri, cheo ,madaraka, watu hawajali tena
ubinadamu, ....kwahiyo yote haya yanawezekana kwa wanadamu wenye tamaa kama
huyu mshitakiwa,....’akasema muendesha mashitaka.
Wakili
mtetezi akasema muendesha mashitaka anachofanya ni kutoa maoni yake, hayo
maelezo hayana msingi wowote na kesi iliyopo mbele ya hakimu, na hakimu akasema
muendesha mashitaka aendelee, lakini amtumie shahidi kutoa maelezo, sio yeye kutoa maelezo yake binafasi.
‘Sawa
muheshimiwa hakimu.....’akasema muendesha mahitaka.
‘Je shahidi,
... kwanini unafanya hivyo, kwanini unajitolea huyu mtu aliyekuwa mlezi wako
afungwe?, kwani wewe huna upendo kwa mlezi wake.., angalau kwa kumshukuru kwa wema
aliokutendea....?’ akaulizwa
‘Mimi sio
kwamba namchukia mlezi huyu, kweli kuna mengi alinisaidia,....lakini mimi kama
raia mwema natimiza wajibu wangu, nimesoma, nina elimu, nafahamu sheria na haki
za binadamu,... na natambua haki za raia, ..natambua utu wa binadamu,...sasa
elimu yangu itakuwa na fadia gani, kama nitaona mabaya, ...nitaoa udhalimu,
wizi, unatendeka halafu nikae kimia....’akasema
‘Kiukweli
mimi niligundua anachofanya huyu mtu sio haki, hajali utu wa wengine, anafikia
kuwazalilisha watu wengine kwa kuchukua siri zao za ndani, mambo ya chumbani ya
siri, anayatumia kama biashara, huu sio
utu,...hata kama mtu kakosea,njia njema ni kumuendea na kumuelezea,
kumshawishi,..kwa hekima ,na sio alivyokuwa akifanya huyu mtu....’akasema
‘Uliwahi
kuziona hiz siri za chumbani, eeh, japokuwa ulikuwa mtoto huruhisiwi, lakini
labda kwa bahati mbaya, au yeye mwenyewe alwiahi kukuonyesha ...?’ akaulizwa
‘Alikuwa
anafanya sana siri, akija na video zake anajifungia chumbani, hakupeda nizione,
lakini kuna siku niliingia chumbani kwake,
nilikuwa natafua kitu, akiwa nje, nikaona moja ya kanda ya video, nikaona nione
ndani kua nini, nikaweka kwenye komputa aliyokuwa nayo, mamama....sio nzuri,
mwenye niliziba macho, na muda huo huo akawa kaingia
‘Akakukuta
ukiwa unaangalia, akasemaje...?’ akauliza
‘Unafanya
nini wewe,...akaniambia hivyo, nikamuuliza kwaninii anachukua video chafu kama
hizo, wakati hata shuleni tumeambiwa hazitakiwi, akasema hizo zitamuingizia
pesa....’akasema na watu wakecheka
‘Zitamuingizia
pesa,! Kwa vipi, hukumuuliza swali kama hilo?’ akauliza na mtetezi
akaweka
pingamizi, na muendesha mashitaka akauliza kwa namna nyingine, na shahidi
akasema.
‘Alipokufuma
ukiziangalia, ...je aliwahi kukuambia kazipataje, kazinunua au zimetoka wapi....?’
akaulizwa
‘Alisema hajazinunua,
....nikamuuliza zimetoka wapi, akasema, yeye ni mpelelezi huru, wa kuwaadhibu
watu hasa wanaojifanya ni viongozi au waume wanaojifanya ni waume safi lakini
kwa siri ni wachafu..akaniambia anachofanya yeye ni kutafuta uchafu wao kama
huo, na kuwaadhibu,...’akasema
‘Kuwaadhibu!
Kwa kuchukua picha kama hizo anawaadhibu, alikuwambia kwa vipi?’ akaulizwa
‘Ndio
nilimuuliza kwa vipi, akaniambia, akizipata kama hizo anawasiliana na hao watu,
na kuwaambia kagundua huo uchafu wao kama ni waume za watu, na kama kiiongozi,
huenda kakiuka maadili ya kazi, anamwambia hivyo hivyo, ....kuwa kagundua
madhambi yake....’akasema
‘Halafu.akishayagundua,
anakuja nayo nyumbani anayaweka tu...’akasema muendesha mashitaka.
‘Hayaweki
tu, ....akishawasiliana nao, anawatishia kuwa wasipompa pesa anataka kiasi
fulani, basi atayaanika madhambi ya hadharani, au atampelekea mke wa huyo mume....ni
mtu wa ajabu kweli!’akasema na watu wakacheka
‘Uliwahi
kumsikia akifanya hivyo, au alikuelezea kuwa anafanya hivyo....?’ akaulizwa
‘Alinielezea
tu, anasema akiwasiliana na hao watu hawezi kuwasiliana nao nyumbani, anatafuta
simu za mitaani, .....’akasema
‘Sasa
ukasikia hivyo, ukaona hivyo...wewe ukiwa kijana mdogo muda huo, ulilichukuliaje
hilo,....licha ya kuwa wewe ulikuwa ni mdogo...siulikuwa mdogo wakati umezifuma
hizo kanda za video, au...?’ akaulizwa
‘Nilikuwa
mdogo ndio, lakini nilishakuwa na akili,....mkubwa ,nimeshabalehe...Kiukweli,
mtu kama mimi sikupenda hiyo hali, shuleni tumefundishwa maadili mema, kuwa
matendo kama hayo, mapicha machafu kama hayo, hayafai, sasa mzazi, mlezi,
anayaleta nyumbani na anasema ndiyo yanayompatia pesa.... niliumia
sana...’akasema kwa sauti ya uchungu.
‘Kwahiyo
ukawa unaishije na mtu kama huyo...?’ akaulizwa
‘Kiukweli
sikupenda kuishi na mtu mwenye tabia chafu kama hizo, na hata wenzangu walianza
kuninyoshea vidole kuwa baba yangu ana biashara haramu, anauza madawa haramu...’akasema
‘Waligundueja
au wewe uliwaambia...?’ akaulizwa
‘Hata mimi
sijui ...waligunduaje,...labda ni kutokana na ile kesi aliyowahi kushitakiwa
kuwa unauza madawa ..’akasema
‘Kwahiyo
shuleni, au katika hali ya kawaida ulijisikije,...?’ akaulizwa
‘Nilijisikia
vibaya sana, nikawa sina raha, ...lakini nilimtetea mlezi wangu huyo, na hata
kupigana na wengine, waliponitania...ikafika sasa moyo ukaanza kuniambia kuwa
huyu mtu anaweza kuwa kweli sio baba wa
kweli, yawezekana ananitumia tu.....’akatulia.
‘Kwa uoni
wako ulivyomuona alifaa kuwa mlezi wako,au mzazi wako?’ akaulizwa
‘Kwa uoni
wangu japokuwa nilikuwa mdogo, niliona kabisa huyo hafai kuwa mzazi wangu, au mzazi
wa yoyote yule,....’akasema.
‘Ulishawahi
kumuambia hivyo, kuwa yeye hafai kuwa mlezi wako au wa yoyote yule?’ akaulizwa
‘Ndio...,
kuna siku nilimuambia hadi tukafikia kugombana kwa hilo, nikamwambia kuwa yeye
hastahiki kuwa mlezi wangu au dad wangu...’akasema
‘Akafanyaje,
alichukua hatua gani kwako....?’ akaulizwa
‘Alienda
akalewa...huwa akikasirika analewa, akija ni vurugu, basi siku hiyo alipokuja
akaanza kunisema, akasema....ooh, ....wewe ulikuwa hujui eeh,...wewe ni mtoto
wa kuokotwa tu, ..., usiye na baba wala mama....mimi nimejitolea kuwa mlezi
wako, halafu huniheshimu...unasema sifai, unafikiri unakula nini,..kama ni
uchafu kama ni madhambi, lakini.....ndio unakula....’
‘Hebi
nikuulize kwanza, wewe si ulikuwa
unaishi kwa asilimia shuleni, bwenini au....?’ akaulizwa
‘Mwanzoni
ilikuwa hivyo, nilikuwa nakaa shuleni,
lakini baadaye aliamua nikae naye....’ akasema
‘Kwanini...?’
akaulizwa
‘Ni ili
aweze kupata pesa nyingi kutoka kwa wafadhili, mwanzoni sikujua lengo lake
hilo, akaja kuniambia hivyo,...sikukataa, nikakubali tu, nikijua yeye ni dad wangu...’akasema
‘Ukilinganisha
maisha ya kuishi naye nay a bwenini, ni yepi bora?’ akaulizwa
‘Kiukweli
kwa hali kama hiyo, niliona aheri ningelikaa huko huko bwenini,...na
alivyonisema hivyo, kuwa mimi ni mtoto wa kuokotwa,...niliumia sana...ilimuambia
mimi narudi kukaa bwenini..’akatulia
‘Akasemaje,
...?’ akaulizwa, na wakili mtetezi akasema maswali anayouliza muendesha
mashitaka hayana msingi na hiyo kesi, ni kupoteza muda.
‘Ndugu
muheshimiwa hakimu, msingi wa maswali haya ni kujua tabia ya huyu mtu, ili
mahakama yak tukufu ione ubaya wa huyu mtu kwa jamii, ...jinsi gani watu kama
hawa wanavyoharibu kizazi cha taifa,.....na ni moja ya mashitaka yake...’akasema
muendesha mashitaka na hakimu akasema aendelee
‘Lakini
usipoteze muda wa maswali yenye kujirudia rudia...shahidi endelea kujibu swali
uliloulizwa’akasema hakimu
‘Siku ya
kesho yake aliniomba msamaha, huwa anafanya hivyo na mipombe yake ikimuishia
kichwani anakuomba msamaha, na kusema aliongea tu kwa vile alikuwa kakerwa na
kauli zangu, na alikuwa kalewa kuondoa mawazo, ...’akasema
‘Kwa maoni
yako, kabla hatujamalizana na sehemu hiyo unaweza kusema nini kuwaambia wazazi
kama hao....’akaambiwa, na wakili mtetezi akasema wakili huyo anauliza maswali
ya kuhitimisha,na hakimu akasema anaruhusu asikia kauli ya ya huyo kijana...
‘Kama mimi, ninachoweza
kuwaambia watu kama hawa wanaojifanya ni walezi, au wazazi kwa njia ya
udanganyifu, wasifaye hivyo, kwani wanawaharibu watoto, wanawajengea watoto ,vijana
tabia mbaya....’akasema
‘Ndio maana
kwa moyo wangu wote nikaapa siku nikipata nafasi, nitajitahidi kuisaidia
serikali kuwafichua watu kama hawa, kupambana na hawa wahalifu....na nasema
hata nikirudi huko ninakoambiwa nimetokea, ndio ...sitakataa kurudi maaa
huenda, ndio nyumbani kweli, lakini kama raia mwema,nitasaidia kuwapinga wazazi
wenye tabia kama hizi, kuwa hawafai kwenye jamii,...’akasema
‘Kwani wewe
hukubali kuwa umetokea huko alipotokea mshitakiwa...?’ akaulizwa
‘Nakubali
mimi huenda nimetoka huko maana hata ngozi yangu ni ya huko, lakini sitakubali
kupewa wazazi kama hao, waongo...wahalifu matapeli...na hata wakisema vipi kuwa
wao ni wazazi wangu, sitakubali kamwe,...hao sio wazazi wangu
kabisa....’akasema. na watu wakashangilia.
‘Maana
kiukweli wazazi kama hao, kwa tabia kama hiyo, lolote wanaweza kufanya hata
kuua....’akasema na watu wakacheka.
‘Wazazi kama
hao, wanaweza hata kuua, kwanini unasema hivyo....’akasema muendesha mashitaka
na wakili mtetezi akapinga hilo swali,
Muendesha
mashitaka akamgeukia hakimu na kusema
‘Ahsante
wakili mtetezi umenisaidia kunikumbusha kuwa swali hilo litakuja kwenye sehemu
ya pili ya shitaka la muaji..., ndugu muheshimiwa hakimu nimemalizana na shahidi
huyu kwa sehemu hiyo, nitaendelea naye kwenye kipengere kingine...’akasema na
kugeuka kurudi sehemu yake.
Hakimu
akawaruhusu upande wa utetezi wamuulize huyo shahidi, na wakili mtetezi
akasimama kwanza akawa kama anawaza jambo, akatulia pale pale kwa muda, ....
Halafu kwa
taratibu akatembea kumsogelea huyo shahidi huku akamuangalia moja kwa moja
usoni..., na shahidi naye akawa anamuangalia huyo wakili bila kuangalia pembeni
au chini, wakawa wanaangaliana, na hata
wakili huyo alipomkaribia huyo shahidi hakuacha kumuangalia hivyo hivyo.
Dakika moja
ikapita wakiwa hivyo... mpaka watu wakacheka....
‘Wakili
mtetezi, huna maswali ya kumuuliza shahidi huyo,...kama huna maswali tuingie
sehemu nyingine...’akasema hakimu. Na wakili mtetezi akiendelea kumtizama huyo
shahidi machoni moja kwa moja halafu akasema;
‘Huyu
shahidi ni muongo, wewe ni muongo,
unaiongopea mahakama, unajua hilo kosa
kubwa, kuongopea mahakama....’akaanza kusema wakili mtetezi,na shahidi akataka
kujitetea, lakini wakili muendesha mashitaka akamuashiria atulie....
NB, Tuone
mapambano ya wanasheria wakiwa mahakamani, ....na ndio tutafichua siri kubwa ya
mauaji yaliyotokea je ni kweli profesa ndiye aliyefaya hayo mauaji au kuna mtu
mwingine...
WAZO LA LEO:
Uharibifu mwingi, uchafu mwingi, dhuluma....nk, unaenea duniani
kwasababu watu wameshindwa kupambana nao, kuambizana ukweli, kukosoana,
kukatazana,...watu wanamuona mtu ni mkosaji, muharibifu, mfisadi, mdhulamaji,
lakini hawataki kumsema, kumkemea,kumwambia au ....kumuelimisha, au kumchukulia
hatua, eti kwasababu ni mtu mkubwa, eti ni mwenzetu, eti ni ndugu yetu,...
Na matokea
yake mambo hayo yanatapakaa yanaonekana ni kawaida tu, baraka
inatoweka,...uchafu, na ubaya unazidi, unaenea,....
Jamani, tusipoamrishana kutenda mema, na tukakatazana
kutenda maovu, dunia yetu itakuwa hivyo, vurugu, dhuluma, ufisadi,watu wataishi
kiujanja ujanja, ...na amani itakuwa ni kitendawili.
ANGALIZO: Kampeni ndio hizo zimeanza,
tuwapime wagombea wetu kwa kuwahoji mambo yenye tija, tuuone uadilifu wao,...kwasasa
ni kauli zao tu, matendo yao tulishayaona, kwani tuliishi nao, wakafanya
waliyoyafanya wakiwa watendaji, .....je kwa kauli zao wataweza kutuhakikishia
hilo...kutuhakikishia uadilifu wao mbele ya mungu, ili maandiko yawekwe, kumbukumbu ziwepo, ,...Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment