Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, July 31, 2015

RADHI YA WAZAZI-25


‘Jana nilikutana na kijana wako..., mmh sikuwa nafahamu kuwa wewe  ulikuja na kijana huyo kutoka huko kwenu, unajua tena nafahamu jambo pale ninapolifanyia kazi, kama halina umuhimu kwa kazi zangu sina muda wa kulifuatilia, ....’akasema akitegemea kuulizwa swali,lakini swali halikutoka, na kwahiyo akaendelea kuongea.

‘Na kama unavyofahamu kazi zetu, kitu kidogo kinaweza kukuvuta kutaka kujua zaidi...ili kupata ushahidi halisi kwa jambo unalolifanyia kazi.....naikizingatiwa kuwa niliwahi kufanya kazi fulani kabla kumuhusu huyo kijana...’akaanza kuongea na hapo moyo wa profesa ukaanza kudunda.

‘Ni kazi gani...’ alitamani kuuliza hivyo, lakini akajizuia kufunua mdomo wake, na kusubiria huenda jibu litatokea.

‘Unajua maisha yalivyo,....mh huwezi kujua jinsi gani mwenzako anavyohangaika, unaweza kumuona katulia, ukaona  karizika,ukasema mhh yule hana shida,...lakini kuna mwingine hawezi kutulia, shida zake zote zitajulikana, kiukweli watu tunatofautiana kwenye kuonyesha ubinafsi wetu....’akatulia

‘Mbona kachanganya mada, ana maana gani huyu mtu...’akawa anajiuliza huku akichunga kufungua mdomo wake.

‘Sasa mimi nina shida..kwa mfano ,mimi nina shida...unaelewa hapo, natolea kwa mfano..nina shida, ...lakini huwezi kunisaidia mpaka ujue ni shida gani,hata kama una uwezo au sio.....na ....’akageuka kumuangalia Profesa,na profesa alikuwa kimia, kwa muda huo alikuwa akimuwazia kijana wake, ...

Ni muda sasa hawajawasiliana,na hata kaka yake akipiga simu kuulizia, hajui hata atamuambia nini, japokuwa kaka yake alikuwa kakata kauli tena ya kuwasiliaa naye baada ya wao kuondoka bila kuaga,...na hata yeye hakuwa anataka kumpigia simu, ni kama mahusiano ya udugu uliokuwepo awali yalikuwa yamefutika,....kisa ni huyo kijana.

Pia akakumbuka kuwa tangia wahasimiane na huyo kijana, japo alijitahidi kujipeleka kwake, lakini ilifikia mahali akaona haina haja tena, kwani hakuwahi kukaribishwa, ...

Ikawa sasa hakuna kukutana, au hata kupigiana simu, na hata ikitokea wakutane njiani, ikitokea ni kusalimiana kwa mikono, hay, hay. Ili tu ionekane kuwa hakuna uhasama dhidi yao, na hata ile dad, dad, ikawa haipo tena.

Na baadaye ndio akasikia kuwa kijana wake huyo kajiunga na mama mtemi kutafuta ushahidi wa kumuweka yeye ndani, ...kusikia hivyo, akajua kuwa kijana sasa anamchukia,...na keshapandikizwa chuki , na kwa vile kijana anamfahamu sana...kweli anaweza kutumika kumuangamiza..

Moyoni akajijutia mwenyewe kwa kumfanya huyo kijana awe rafiki na binti wa huyo mama,....mwanzoni alijua huenda kwa kufanya hivyo, atajenga udugu, ataweza kupata mengi kwa huyo mama kwa kupitia wawili hao kumbe imakuwa kinyume chake,....imekuwa kama kajipalilia ubaya zaidi

Sasa alivyoanza kuongea huyu mpelelezi kuhusu huyo kijana, akajua ni yale yale ya mama mtemi, lakini alipoanza kuongea kuhusu jamaa kutoka India, akajua ehe,huenda mpelelezi kaajiriwa na huyo jamaa, lakini kwa jinsi anavyochanganya mambo, huwezi kujua msimamo wa huyu mtu.

Profesa alishamsoma huyu mtu kuwa lengo lake ni kumchanganya,,...unahitajika kuwa makini kwa  huyu jamaa, kwani wakati mwingine anataka kukuchimba kupata taarifa fulani...

‘Kama unavyonijua mimi, nilikuwa askari wa serikali, ...baadaye nikatoka huko, kwasababu zangu binafsi,...nikaona nijiajiri, na kiukweli, japokuwa ni ngumu kujiajiri kwa kazi kama hizi, maana unajiweka mtu kati,..., lakini nimeweza kujiendeleza...’akatulia

‘Usionine hivi profesa,...mimi huko kwetu ,... unajua hata mimi natoka afrika japo wazazi wangu ni mchanganyiko...ndio maana nipo half cast, nusu ni mwafrika,....huko kwetu ninapotoka nina miradi yangu, nikirudi nyumbani naweza kujivunia...ndio maana nataka kukushauri..uwe kama mimi....najuahata wewe umewekeza au sio....’akasema

‘Lakini kama ujuavyo maisha ya hapa,...yanahitaji gharama nyingi sana...watu hawaelewi hasa huko nyumbani, ....huko kwetu hakuna tofauti sana na huko kwenu,...kwahiyo tabia ni zile zile...hawajui kuwa kile unachopata kinaishia kwenye ...malipo mengi tu, hapa huna ujanja wa kukwepakodi,...si unaona ilivyo, nyie wakati mwingi mnatafutwa kwa kukwepa kodi,mimi siwezi kukwepa, hata sekunde moja,...’akatulia

‘Mimi nawafahamu sana nyie, kwa jinsi gani mnavyokwepa kodi, katika kazi zangu hizi nimeliona hilo, lakini huko tupaache, siwezi kuwashitaki kwa hilo...’akatulia na profesa akajua ni katika namna ya kumtisha.

‘Lakini sasa ni kuhusu huyu kijana wako...’akatulia, na hapo profesa akajua kuna bomu linakuja

‘Huyu kijana wako kamchumbia binti wa mama mtemi,...hahaha....’akasema na kucheka, na hapo profesa akapumua

‘Unajua niliposikia mara ya kwanza, sikuamini....’akatulia na profesa alitaka kumuuliza kwanini, lakini hakutaka kufungua mdomo wake, akatulia tuli

‘Sio kwamba huyo kijana ...hamfai huyo binti, ...hapana ila yule binti alivyo tu, sizani kama wataendana..., si unamfahamu yule binti alivyo...najua wewe uliishi pale ukamuona huyo binti alivyo, wengi wanajiuliza...mbona kitabia hafanani na wazazi wake au sio,...kuna siri kubwa sana...lakini hayo hayatuhusu....’akatulia

‘Na hapo ndio watu kama nyie mnatumbukiza mikono yenu kuwachunguza, ila ...nakukanya tena na tena usije kujaribu kitu kama hicho tena pale kwa huyo mama,...kwani hata hivyo, sijui kama utaweza kumalizana na huyo mama, umeshaweka sumu na sumu hiyo inakurudia mwenyewe, nakupa hilo kama angalizo, yule mama anakuchukia....’akatulia

‘Hayo tuyaache, ....mimi nazungumzia huyu kijana .....mmh,huyu binti, huyu binti ni kila kitu kwa huyo mama,...kwa wazazi wake,  na ukitaka ukosane na huyo mama ujaribu kuingilia mambo ya binti yake, kiujumla wanampenda sana binti yao, nawaheshimu kwa hilo, sijui kwanini hawaki kupata mtoto mwingine, ni siri yao, na mimi sipendi kuingilia siri za watu kama hawajanihusisha,ndio kawaida yangu...’akatulia

Profesa alitaka kubishana naye kuhusu hilo, lakini akagundua jamaa kaongea hivyo kumtega, ili aongee, ili aweze kutegwa kimaswali, akafunga mdomo wake, japokuwa aliona kupotezewa muda kwa mambo yasiyoungana...na profesa alijua kuwa jamaa alifanya hivyo kwa malengo fulani, .....

‘Siku kijana wako alipogundulikana kuwa ana mahusiano na binti wa huyo mama, nikaitwa....’hapo akageuka kumtupia jicho profesa, akitarajia swali, lakini profesa akawa makini.

‘Unajua tena yule mama ni mtu kanizoea sana, akitaka kujua jambo ananitafuta, na mimi namsaidia na wakati mwingine bure tu, ...sasa kunipa kazi kama hiyo....mhh, niliona kama kunipotezea muda wangu...maana hiyo sio kesi ya kunipa mimi...lakini sikumkatalia, nikijua ni kazi ya siku moja nampa taarifa yake....’akaegemea usukani

‘Mhh...hutaamini, ..kitu nilikiona kidogo, kikanifanya nisafiri hadi Tanzania kwa mara ya kwanza....’akasema hapo profesa akashituka, na akataka kusema neno lakini akaona atulie kwanza.

‘Wanasema tembea ujue mambo,...ukikaa sehemu moja tu, unakuwa huelewi, dunia hii ina mambo, unaweza ukamkuta mtu barabarani anaongea peke yake, ukasema ni kichaa, kachanganyikiwa, lakini....we acha tu....’akatulia

‘Sasa nisikupotezee muda wako, najua hili utalipokea kwa mikono miwili, maana kiukweli nimeshakusoma, nimeshakufahamu, na wapi unapotokea...na mengi kuhusu wewe nimeshayafahamu tu,....’akakuna kichwa kama kinamuwasha

‘Kwako wewe kukujua,... sihitaji kabisa hata kwenda kwa mtaalamu, maana na yeye anajifanya mjanja,...unajua ka-utalamu kake ka mitandao, watu wanamuona kama mganga wa kienyeji wa kupiga ramli, wakiwa na shida,...hata shida ndogo tu, wanapoteza pesa zao kwenda kwake, basi anavimba kichwa,..eti wanakwenda kwake kutaka kujua hili na lile....mmh, kweli wajinga ndio waliwao....

‘Sasa ubaya wa binadamu, watu wanakuamini,watu wanakuona msaada kwao,lakini inafikia mahali unatakabari, unajiona wewe ni zaidi....wewe ni mtaalamu....unawasaliti....’akatulia

‘Na baya zaidi, kaona kuna njia nyingine ya kupata kipato kwa kubuni kazi ...basi ingelikuwa ni kazi halali basi, ...yeye kaamua kubuni kazi za ....hata ujambazi, huyu mtu ni mbaya sana,...atawaingiza wengi jela,...mimi sijui, lakini huko anapokwenda ni kubaya sana, tena sana...’akatulia

‘Najua ni rafiki yako, najua unaweza kwenda kumuambia haya, lakini mimi simuogopi, anajifanya eti anajua mambo yangu mengi, eti nina ubaya umejificha, mimi nilimuambia aupeleke huo ubaya mahakamani tukapambane huko kisheria, mbona haupeleki,...’akatulia

‘Yule jamaa anaishi kihivyo,.. yeye anachotishia ni kuniharibia jina langu, nionekane sifai, eti ninyang’anywe leseni yangu, nimemwambia ajaribu, kama hataumbuka,...hawezi , hata siku moja hawezi...’akatulia

‘Kwahiyo na wewe nakuona mpo naye sambamba, nakuambia kama rafiki yangu, uwe makini na huyo jamaa , haaminiki...., uwe makini sana....ukiataka kunisikiliza haya, ukiona labda mimi nakupekenyua its up to you.., ..ila ipo siku utayakumbuka haya ninayokuambia...’akasema

‘Ni hayo tu, au kuna jingine...’akauliza profesa akitaka kutoka nje ya gari

‘Ni kuhusu kijana wako...’akasema mpelelezi akiwa hamuangalii profesa, kama vile anajua akitaja kuhusu kijana wake jamaa atataulia.

‘Ana nini..,?’ akauliza profesa akimkazia macho mpelelezi japo moyoni alikuwa na wasiwasi.

‘Kanipa kazi, ...’ akasema sasa akimtupia macho profesa akionyesha uso wa kutahayari kama vile hakutaka kuliongelea hilo,....

‘Unajua kazi nyingine ni siri...lakini wewe ni rafiki yangu, nikaona nikudokezee hilo, na unajua mimi sitaki wewe uje kuishia jela,....’akatulia

‘Kijana wangu kakupa kazi ya kunichunguza mimi...usitake nikuamini....hilo halipo!’ akasema kwa kuonyesha uso wa mshangao, akilini alijua kuwa inawezekana kweli kafanya hivyo, lakini hakutaka huyo jamaa amuone anamuamini.

‘Sijakuambia hivyo....kwanini anipe kazi ya kukuchunguza wewe,....hapana sivyo ninavyomaanisha, kwani wewe  una kosa lolote dhidi yake...au?’ akasema kwa kuuliza.

‘Tatizo lako hueleweki, najua hapa kuna kitu unanitafuta, na huna uhakika nacho, unachofanya ni kinichimba, kunichezea akili, unajua unanipotezea muda wangu, nimekusikiliza wee, sijaona lolote la maana, sasa nakuambia muda wangu wa kukusikiliza umekwisha, mimi naondoka, kama una jingine nitafute kwa muda wako....’akasema sasa akifungua mlango wa gari.

‘Kijana wako alikukana, akasema wewe sio baba yake halali,....’akasema

‘Kwani ni uwongo....’akasema profesa

‘Kijana wako anasema wewe ulitumia mbinu, na kujifanya wewe ni mlezi wake, ili tu upate pesa kwa kutumia mgongo wake...’ akasema

‘Ina maana hao wafadhili ni wajinga, ....kawaulize kama mimi niliongea uwongo,....’akasema

‘Na zaidi ya hayo, kijana wako amekiri kuwa wewe unajishughulisha na biashara ya mlungula,....ana ushahidi kwa hilo,.....na yupo tayari kuutoa mahakamani ikibidi..hata ukifungwa yeye hana cha kujutia kwa vile anajua ni kweli, hata yeye haimfurahishi kusikia ana mtu kama wewe unayejifanya ni mlezi wake, kumbe ni hadaa za kujinufaisha tu.....’akasema

‘Ndio hilo, au kuna jingine....’akasema profesa sasa akiwa keshafungua mlango akijivuta kutoka nje,

‘Akasema wewe unauza madawa ya kulevya, na pia una madawa ukichanganya na pombe humfanya mtu asijielewe, afanye mambo kinyume na matakwa yake,na akizindukana,...unakuwa umeshamfanyia mambo ambayo hayafai, unamfanya kama zezeta, na kujituma kufanya kile unachotaka, na hapo unatumia huo uchafu alioufanya kwa mbinu zako  kuja kum-blackmail.huyo mtu ili kupata pesa....’akasema

‘Mhh, hahaha, na wewe ukaamini hayo, ...au ndio kazi aliyokutuma, na sasa unataka kuhakiki kuwa ni kweli au si kweli...?’ akauliza

‘Niliposafiri kwenda Tanzania,....kabla sijayajua hayo, nilifanya utafiti, kuchunguza kutaka kujua uhalali wa dawa zako,....profesa unajua wewe ni mtaalamu sana, ....unajua ungetulia ukaweka mambo yako sawa, ungejipatia jina kwa dawa zako....’akasema

‘Dawa zangu....?’ akauliza

‘Ndio dawa zako za tiba mbadala...na...hizo unazotumia kwa kuleweshea na kupumbaza watu..’akasema na profesa hapo akabakia kimia

‘Dawa zako zina nguvu  sana...ila wewe unazitumia vibaya....na hiyo ni kutokana na tamaa yako...’akasema

‘Zile dawa zingesaidia katika upasuaji....unaona eeh, na..hata katika mambo ya usalama, kwa wahalifu,....hayo ni mambo halali, kiukweli ungefaidika sana kwa hizo dawa......mimi kwa vile nimepitia polisi,naweza kukusaidia, unachotakiwa ni kuniambia ukweli na tuone jinsi gani ya kusaidiana, ili ufike mbali...’akasema

‘Sihitaji msaada wa mtu yoyote, maana hayo unayoongea usifikiri sikuyafanyia kazi, nimehangaika kiguu na njia kutaka dawa zangu zitambulikane, zipate haki miliki, lakini ....usinikumbushe mbali...na nimechoka,...nia yangu ni kutafuta njia nyingine ya kupata pesa, walinifunga wakidai nauza madawa ya kulevya, achana na mimi kabisa...’akasema

‘Wewe hujasema ukweli kuhusu madawa yako, ....walijua wewe unachanganya a madawa ya kulevya,....ilitakiwa upate mtu wa uhakika wa kukusaidia...mimi naweza kuifanya hiyo kazi, tukishirikiana...’akasema

‘Nikuambie ukweli mimi sihitaji tena kujisumbua kwa mambo ya madawa,....mipango yangu ni kutafuta njia nyingine ya kupata pesa, basi.....’akasema profesa.

‘Njia gani nyingine profesa,....umekata tamaa mapema, unasikia, wewe hukupata mtu sahihi wa kukusaidia, sio kila mtu ni mwema, wengine wanapenda kutumia wenzao kwa hadaa, na jingine ni wewe mwenyewe tu...wewe kinachokupoza ni kuwa unataka upate pesa nyingi kwa haraka, ...ndio maana hufanikiwi....sikiliza ,mimi ninaweza kukusaidia,...’akasema

‘Kunisaidia wewe...kunisaidia mimi, ....?....niambie kwa vipi.....?’ akauliza

‘Eheee, sasa unaanza kunielewa, ...muhimu kwanza nifahamu kama upo tayari, na ukinisikiliza ukanielezea hatua uliyofikia, tunaweza kufika mahali,...najua awali tatizo ilikuwa ni pesa ya kuanzia,....sasa najua pesa za mtaji sio tatizo....hilo tutalipanga...’akasema

‘Mhh, tutapatia wapi mtaji, wakati...wewe mwenyewe hapo unatafuta pesa, mtaji ni pesa, na pesa ndio hizo ngumu,...usinipotezee muda wangu...’akasema

‘Pesa ya mtaji itapatikana,...ni wewe tu,..’akasema

‘Kwa vipi...?’ akauliza

‘Kwanza niambie ukweli....unajua ,mimi ni askari, nilikuwa askari, sasa mimi ni mtu binafsi,na naweza kusikia jambo, nikalipima kwanza, nikamshauri mteja, kuwa hilo ni tatizo, achana nalo, au endelea nalo...’akasema

‘Unajua tofauti yangu na askari hao wengine ndio hiyo,....sifanyi kumfunga mtu, nafanya kutoa ushauri,....unaona, sasa ugumu wa hizi kazi unatokana a kupata ukweli sahihi,....jinsi gani mtu atakavyofunguka, au kuficha jambo...sasa wewe ukiniambia ukweli, itakuwa ni vyema zaidi...’akasema

‘Ukweli, ukweli, ukweli kuhusu nini....?’ akauliza profesa akipaza sauti.

‘Profesa, mimi mpaka nakuja kwako, ujue nimeshafanya kazi ya kutosha najua ni jambo gani unalolifanya hadi sasa...najua kuwa mpo kwenye dili ya pesa nyingi, na ujue pesa nyingi ni hatari....najua yote hayo, ila ....napenda wewe uwe mkweli ili tusaidiane....’akasema

‘Kwahiyo shida yako ni pesa, na kwa vile umesikia tetesi kuwa nipo kwenye dili ya pesa nyingi unataka na wewe uzipate, au sio...kama ni hivyo umedanganyika...hakuna kitu kama hicho...ni nani huyo kakudanganya?’ akawa kama anauliza

‘Sikiliza profesa, mimi nimeshakuambia kuwa sipendi kuja kuwaumiza watu kwa kufichua siri zako ambazo nina uhakika zitawafunga, huwa napenda kuwa muwazi, ili na wao ...watu hao waliojiingiza kwenye ubaya wajijue, na wajirudi, waone kosa lao,...unajua wengine wanaona wanachofanya ni sahihi ,, kwa vile tu wanapata pesa,...lakini mtu kama huyo unaweza kumsaidia akabadilika, na kuwa raia mwema,...unaona hilo...’akasema

‘Kwahiyo wewe umeona kuwa mimi ni raia mbaya, unataka niachane na hizo hisia zako kuwa mimi nafanya biashara haramu, kuwa natumia madawa kuwapumbaza watu waishiwe kujitambua ....na kutenda yasiyo faa...ndivyo unavyonibambikizia makosa au sio..sasa sikiliza, wewe kama una ushaidi peleka huo ushahidi mahamani tutakutana huko.....’akafungua mlango.

‘Sio mimi wa kufanya hivyo, mimi hiyo sio kazi yangu, nielewe hapo, kama ningekuwa nafanya hivyo, kesi ya mama mtemi si ungelishakamatwa na kushitakiwa...’ akasema

‘Kuna watu wengi wanakutafuta tu, wana visasi na wewe kwa uliyowafanyia, wanatafuta sababu, na ushahidi,....na mimi nikitaka naweza kuwasaidia,....lakini wewe ni rafiki yangu, au sio, ...’akasema

‘Rafiki yangu!...wewe,...?! Na nikuulize ni akina nani hao...?’ akauliza

‘Wapo wengi tu , na sasa kaongezeka, yule raia kutoka India...na yeye hajakutambua tu kuwa wewe upo nyuma ya hayo mambo, lakini yupo mbioni, atakutambua tu...unaona hali ilivyo, ni kwamba kwa vyovyote unanihitajia mimi, ndio nikaona nije tuongee,.....sasa uamuzi ni wako, kama unakaidi, sawa, mimi nitafanya kazi yangu, lakini usije kunilaumu...’akasema

‘Una maana huyo raia kutoka India, ndiye kakupa kazi ya kunichunguza..?’ akauliza kwa mshangao, sasa akiwa kashusha mguu mmoja nje...na kabla hajajibiwa, mara simu yake ikaita, na alipotizama aliona ni tajiri wake...

‘Kesho nataka kuonana na wewe....’akaambiwa

‘Kesho.....mmmh tutawasiliana nipo sehemu mbaya....’akasema

‘Ni muhimu, sana..nataka tuongee, kama unaweza kunisaidia....’akaambiwa kwenye simu

‘Kuhusu nini.....?’ akauliza

‘Ukija nyumbani tutaongea,...kuja asubuhi, halafu tutakwenda benki, kazi moja utafanya,.....mengine nitakujulisha ukifika, ....usikose....’akaambiwa na simu ikakatika.

Profesa akili ikampaa, ina maana jamaa anataka kumkabidhi yeye hizo pesa, azipeleke mahali ambapo alishapangiwa huyo mtu kuzifikisha, na hapo hapo yeye ndiye anatakiwa kuzichukua ili wakutane na mtaalamu, kugawana.....,alipowaza hivyo, kwa haraka akafungua mlango wa gari kushusha miguu yote nje kutaka kuondoka.

‘Jamaa aliniambia wewe na mimi tutashirikiana kuupeleka mzigo mahali, ili kumnasa mbaya wake...’akaambiwa na mpelelezi, na wakati huo profesa alikuwa keshatoka nje ya gari, tayari kufunga mlango wa gari, lakini kwa kauli hiyo akasita....

NB: Ni nini kitaendelea


WAZO LA LEO: Nafsi ina nguvu sana, nafsi ina tabia ya kukutuma hata kule kusipofaa, na ikashawishi akili kukubali jambo, ambalo kiukweli halifai, ni kwa vile kuna masilahi tu,...na ili kufanikiwa hilo nafsi italipamba hilo jambo, na ikatuma akili ikajenga hoja za kujirizisha. Ni kazi kubwa kupambana na nafsi, ukiwa hua msimamo, lakini kama una msimamo, na tabia yako ikawa kwenye kutenda yaliyo haki, na ukweli, ni rahisi sana kuishinda nafsi. Tujitahidi kuwa wakweli na kutenda yaliyo haki.IJUMAA KAREEM.
Ni mimi: emu-three

No comments :